Kwa mara nyingine tena, Serikali imevurunda!

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,013
Date::8/13/2009
Fidia ya walioathirika na mabomu Dar yagubikwa na kasoro tele
Geofrey Nyang'oro na Hawa Lukindo
Mwananchi



MAANDALIZI ya kuwalipa fidia wakazi wa Mbagala walioathiriwa na mabomu yameingia dosari baada ya baadhi ya majina ya watu kukosekana kwenye orodha ya malipo, huku majina mengine yakitofautiana na namba za nyumba zilizoathiriwa.

Jumla ya Sh8.5 bilioni zimetengwa kwa ajili ya malipo ya fidia kwa wakazi ambao nyumba zao ziliathiriwa na milipuko ya mabomu iliyotokea Aprili 29 kwenye ghala la silaha la kambi ya Jeshi la Wananchi (JWTZ) iliyo Mbagala na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 29.

Fedha hizo zitatumika kulipa fidia nyumba 9,259 zilizoharibiwa na mabomu hayo na ambazo zilihakikiwa na serikali.

Lakini uchunguzi wa gazeti hili jana umebaini kuwa mchakato wa malipo hayo umeanza kuingia dosari baada ya watu kadhaa waliofika ofisi ya afisa mtendaji kata ya Mbagala Kuu, kugundua kuwa majina yao hayapo kwenye orodha iliyobandikwa ukutani na wengine kukuta tofauti ya majina na namba za nyumba.

Afisa mtendaji wa kata hiyo, Basil David alisema kuwa zaidi ya watu 50 waliofika ofisini kwake kuangalia majina yao, walikuta aidha yamekosewa au hayaendani na namba za nyumba zao.

"Ni kweli zimejitokeza kasoro kwenye mchakato huu. Zipo namba za nyumba zilizokosewa na majina mengine yanatofautiana na namba za nyumba hizo," alisema.

"Kutokana na hali hii tumeziagiza ofisi za serikali za mitaa kuorodhesha majina ya watu ambao majina yao au namba zao zimekosewa, ili ayapeleke kwa mkuu wa mkoa kwa ajili ya kufanyiwa marekebisho kabla ya kuandaliwa kwa hundi za malipo," alisema.

Mmoja wa wakazi wa eneo hilo aliyekosa jina lake kwenye orodha hiyo, Zaituni Zuberi alisema: "Nyumba yangu ilikuwa namba MA/1/1797 na baada ya kuthaminiwa nilipatiwa namba 1048, lakini cha ajabu nimekuta hakuna namba ya nyumba wala jina langu kwenye orodha ya majina yaliyobandikwa hapa ofisini."
Alisema kitendo hicho kimemshtua kwa kuwa tangu kutokea kwa milipuko ya Aprili 29 mwaka huu, anaishi kwenye mahema akisubiri fidia na hivyo kukosekana kwa jina lake kumemchanganya zaidi.
"Nimeambiwa niandike barua ya malalamiko na kuipeleka ofisi ya serikali za mtaa ambako watasaidia kufuatilia suala hili," alisema kwa huzuni.
Hemedi Bakari, 62, alisema orodha hiyo imekosea namba ya nyumba yake moja kati ya mbili zilizobomoka.
Alisema milipuko ya mabomu ilibomoa nyumba zake mbili alizokuwa akimiliki, moja ikiwa na vyumba vitatu na ya pili ikiwa na vyumba sita na kwamba zote mbili ziliathiliwa na milipuko ya mabomu hayo na kuthaminiwa.
Alifafanua kuwa wataalamu hao walifika kwenye eneo la nyumba alizokuwa akimiliki na kuzifanyia uthamini, ikiwa ni pamoja na kuzipiga picha nyumba zote mbili na kumpa namba 330A na 330B, lakini iliyorudi ni moja tu ya 330A.
Alisema namba aliyopata haieleweki kama ni ya nyumba ya kwanza au ya pili na kusema kitendo hicho kimemshtua kwa kuwa, hadi sasa haeliwi ni nyumba gani imekusudiwa na pia kama itakuwa hivyo itampotezea haki zake za msingi.
Mbali na kasoro hizo, zaidi ya watu 700 wanadai hawakujumuishwa kwenye mchakato wa malipo hayo.

Lukuvi alisema juzi kuwa baadhi ya waathirika hao ambao wameishi katika mahema kwa zaidi ya miezi minne, sasa watalipwa fidia hiyo katika ofisi za Halmashauri ya Manispaa ya Temeke.

Kwa mujibu wa Lukuvi, nyumba 235 zilizobomolewa kabisa na milipuko hiyo na nyumba 54 zilizoharibika na 54 ambazo hazifai tena kwa makazi, zimetengewa Sh906,484,000.

Alisema nyumba 8,970 zinahitaji ukarabati mdogo na hivyo zimetengewa kiasi cha Sh4,627,266,000 huku mali zilizoharibika kutokana na milipuko hiyo zikitengewa kiasi cha Sh51, 242,000.

Alisema hundi kwa ajili ya malipo hayo zitaanza kuandaliwa katika ofisi yake Agosti 17 mwaka huu. Milipuko hiyo ambayo mpaka sasa serikali haijatangaza chanzo chake, ilitokea katika ghala la kikosi cha 671 Mbagala Kizuiani.
 
Wabunge ndiyo walitakiwa wapige kura kuhusu hizo hela ndiyo zitolewe; sheria mbovu za Tanzania. Nani aliyeidhinisha utolewaji wa hizo hela?
 
Mafisadi wa CCm wakina Lukuvi wamekwisha zifanyia hesabu fedha hizo za wahanga wa mabomu; humo lazima kuna majina kibao ya watu feki; madai hewa mengi tu!! Ukiona wanakwenda kusimamia malipo ujue wanakwenda kuangalia kama mgao wao unatunzwa!! Mambo ya bongo hayo.
 
Hii siyo bongo tu mkuu, kwenye ugaidi wa Mumbai watu waliandikisha kupoteza ndugu bandia ili walipwe.
 
Yani hizo hela za waathirika wa mabomu nahisi zimewafurahisha sana viongozi wanaohusika nazo.Macho yao yote yamewatoka kusubiri ugawaji uanze...Majina na namba za nyumba hazijakosewa bahati mbaya ni makusudi tu ili wapate na wao kupitia pesa hizo hizo...
Hivi kitu kama hicho cha kuwafidia watu walioathirika na mabomu kwanini wasikifanye kwa umakini sana?!
Serikali yetu ina mambo ya ajabu sana.
Huyo Lukuvi asipoangalia hizo pesa zitamtokea puani tena tundu la kushoto...!
 
Hili swala jamani tulichukulie taratibu maana waliofanya hivyo ni binadamu na wanamapungufu sasa takianza tu lawama na kulihusisha na ufisadi tunakosea jamani.
Lenner
 
Hili swala jamani tulichukulie taratibu maana waliofanya hivyo ni binadamu na wanamapungufu sasa takianza tu lawama na kulihusisha na ufisadi tunakosea jamani.
Lenner

Dah! Kumbe watu kama nyie mpo!
This is Tanzania bwana,mbuzi wengi wanakula kwa urefu wa kamba zao!
 
Back
Top Bottom