JE, UNAJUA SABABU ZA SHEIKH MWAIPOPO KUTAKA 'KUWATAHIRI WATU BILA GANZI'?
Wiki hii kaibuka Sheikh Mwaipopo, kaita press na kutamka maneno mazito. Baadhi ya maneno hayo ni 'kutairi waandamanaji bila ganzi', kuwa na 'kikosi cha mbwa mwitu', nk. Kauli hizo pia zinafuatia kauli zake za nyuma kuwashambulia maaskofu baada ya mauaji ya 29 Oktoba 2025 ambapo yeye alikuwa akiitetea serikali.
Kauli zake zimeibua hamasa za watu wengi za kutaka kumjua Sheikh Mwaipopo ni nani hasa! Hilda Newton Chadema amejitahidi kumueleza jinsi alivyochimba historia yake. Lakini katika maelezo ya Hilda, ameonyesha kuwa alikuwa ni Mkristo wa Kanisa la Roman Catholic kabla ya kusilimu.
Lakini kutokana na ufahamu wangu, Sheikh Mwaipopo hakuwahi kuwa Roman Catholic. Na huu ndio uelewa wangu kuhusu yeye pamoja na sababu zilizompelekea yeye abadili dini na kuwa Muislamu.
Sheikh Mwaipopo alipewa jina la Thomas, hilo lilikuwa jina la babu yake. Elimu yake ni Shule ya Msingi. Kwa wanaomjua wanasema kuwa alibadili dini mwaka 1997.
Mwaipopo alikuwa muumini wa Kanisa la Moravian Mbeya ingawa alipatia Kipaimara katika Kanisa la Moravian Jimbo la Tabora kwa kuwa alikuwa akiishi kule. Lakini Thomas au Thom kama walivyokuwa wakimuita wenzake kule Mbeya, alikuwa akikaa kwa shangazi yake.
Taarifa zake zote za mwaka 1994 ziko Mbata eneo la Nyamagana kule Mbeya ambako pia alikuwa muumini wa Kanisa la Moravian. Picha nyingi za ujana alizopiga na vijana wenzie wa Kanisa la Moravian kule zinapatikana.
Ndugu yake wa damu kwa Dar es Salaam ni Mhandisi na mhadhiri ambaye pia alikuwa akifundisha katika Chuo cha Usafirishaji (NIT) na muumini wa Kanisa la Moravian Usharika wa Mabibo. Jina lake ni Hance Mwaipopo.
Taarifa zinaeleza kuwa katika harakati zake za maisha, Thomas Mwaipopo (ndiye Sheikh Mwaipopo) aliwahi kufungwa jela Segerea. Akiwa Segerea ndipo alikutana na wahadhiri wanaharakati wa Kiislamu kutoka Msikiti wa Mtoro ambao walichanga pesa na kumtoa jela.
Baada ya Waislamu kumtoa jela walimsilimisha na kisha wakamuozesha mke wa Tanga. Lakini kipindi kile (miaka ya 1990s) mihadhara ya dini ilikuwa imeshamiri sana huku Wakristo kama akina Simbaulanga, Ndimbo na wenzao wakiwa moto sana.
Taarifa zinaeleza kuwa kwa kuwa alikuwa na kipawa cha kuongea, Rais mstaafu Mwinyi alimpeleka kusoma dini ya Kiislamu. Lakini pia haijulikani Mzee Mwinyi alimpelekaje kusoma na kwa makubaliano gani. Lakini pia mwanzoni mwa miaka ya 2000, alijiunga na Chama cha Wananchi (CUF). Akiwa na CUF, pia aliisumbua sana serikali akiwa anatekeleza kwa vitendo ile kauli mbiu ya CUF ya Jino kwa Jino. Harakati zile pia zilipelekea Mwaipopo afungwe jela au awekwe ndani na serikali.
Akiwa na CUF, Sheikh Mwaipopo alifanyakazi kwa karibu na Msolopa (Sheikh au Dkt. Majini). Lakini kuna taarifa zinaeleza ya kuwa baadaye serikali iliamua kumtumia [sasa haijulikani pia kama ni serikali yenyewe [TISS), CCM au hata kikundi cha watu ndani ya serikali au CCM ndio hasa waliokuwa wakimtumia].
Miaka ya baadaye kulitokea mgomo mkubwa wa madaktari Muhimbili wakiongozwa na Dkt. Ulimboka. Wanaokumbuka, Dkt. Ulimboka pia alitekwa na kuokotwa akiwa pia ameng'olewa meno [bila ganzi]. Pigai mstari neno bila ganzi!
Watoa taarifa wanaeleza kuwa wakati huo wa mgomo wa madaktari, Sheikh Mwaipopo sasa alikuwa tayari upande wa serikali akiwasema na kuwashambulia madaktari.
Taarifa kutoka ndani ya familia yake zinasema kuwa baadaye Sheikh Mwaipopo aliumwa sana na kulazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili. Inaelezwa kuwa madaktari walimtambua kuwa ndiye Sheikh aliyekuwa akiwashambulia sana. Ila wakati minong'ono ya kulazwa kwake pale Muhimbili ikiendelea, daktari mmoja ambaye alikuwa Mnyakyusa aliwanong'oneza nduguze kuwa wamuondoe Muhimbili kwani hali yake ya usalama mikononi mwa madaktari inaweza pia isiwe ya uhakika. Ndipo ndugu wakamuondoa pale na kumpeleka hospitali nyingine.
Lakini ni kwa ielezwe kuwa Sheikh Mwaipopo alikuwa muumini wa Roman Catholic Church wakati hajawahi kuwa? Inawezekana pia taarifa hizo zimetoka kwa Waislamu wenyewe. Labda yeye aliwaambia hivyo kwani kwa yeye kusema kuwa alikuwa muumini wa Roman Katoliki, basi ingekuwa inamuongezea uhalali fulani hasa kwa sababu pia wanaharakati wa Kiislamu nao wanalifahamu sana Kanisa hilo [hii pia ni hoja nyingine mtambuka].
Kama maelezo hayo ni ya kweli, basi ni wazi kuwa serikali imeamua tena kumtumia Sheikh Mwaipopo kama ilivyomtumia wakati ule wa migomo ya madaktari. Baada ya kuzidiwa hoja na madaktari, serikali iliamua kuwatumia pia wanaharakati wa dini ya Kiislamu kama huyo Sheikh Mwaipopo ili kupambana na madaktari.
Hata sasa kuna dalili kuwa serikali imezidiwa hoja na wanaharakati, watetezi wa haki na hata baadhi ya viongozi wa dini ndio maana sasa imeamua tena kuwatumia wanaharakati wa dini ya Kiislamu kama Sheikh Mwaipopo. Lakini ni wazi kuwa kufuatna na historia na udhoefu wake kama ilivyoelezwa hapo juu, huyu Sheikh hawezi kushindwa 'kutahiri watu bila ganzi'!
Je, unamjua Sheikh Mwaipopo? Je, uliwahi kusoma naye au kuishi naye wapi? Je, mambo yaliyoelezwa hapo yana ukweli gani kutokana na uelewa wako kuhusu yeye? Uliwahi kusali naye wapi? Je, Moravian au Roman Catholic?
Je, ni kwa nini serikali imenyamaza baada ya yeye kutoa kauli tata za kumiliki 'mbwa mwitu' ambao atawatumia 'kutahiri watu bila ganzi'?
Je, ni sheria ipi inayomruhusu Sheikh kumiliki 'mbwa mwitu' na kuwatumia hao kuwakamata wapinzani wa serikali na kuwatairi bila ganzi? Je, ni sheria ipi inayompa mamlaka Sheikh ya kuita vyombo vya habari kwa ajili ya kuwatisha wapinzani wa serikali?
Sisi Askofu Mwamakula tunatoa wito kwa mamlaka kutoa kauli imechukua hatua gani kwa Sheikh Mwaipopo kufuatia kauli zake.
Je, nini kimekushangaza? Je, nini maoni yako?
Mwana Kondoo Ameshinda! Tumfuate!
Askofu Emmaus Bandekile Mwamakula
Itunge, Dar es Salaam; 23 Juni 2026; Saa 4:50 asubuhi