Madame S
JF-Expert Member
- Mar 4, 2015
- 17,190
- 34,526
- Thread starter
- #21
RIWAYA: KONSTEBO NGUZU
MAANDISHI YA: George Iron Mosenya
"Zungumza machache kati ya mengi uyajuayo..... ONYESHA vichache kati ya vingi unavyovimiliki. Katika maisha si vyema kila mtu kukujua kwa asilimia 100"
Hii ni SEHEMU YA KUMI NA MBILI.
GIZA lilikuwa ndani ya giza kwa mara nyingine, Konstebo Martin Nguzu alikuwa amempokea mama yake ambaye alikuwa mmoja kati ya wahanga wa ile kamatakamata iliyofanywa kwa masilahi ya watu wachache waliokuwa wamekerwa baada ya mwenzao mmoja kuuwawa kifedhuli.
Ghafla bin vuu mambo yakabadilika, kota zikatishiwa kuchomwa. Wakagwaya na kuwaachia huru wale waliokuwa wamekamatwa katika namna ya uonevu.
Ni giza hilihili sasa lipo ndani ya giza tena, ana kwa ana na mama yake mzazi.
Martin Nguzu alimpa pole mama yake huku akiwa na haraka sana ya kujua ni wapi hasa anapoweza kumpata Majenga waweze kuzungumza na kutambua ama kujitambua upya yeye ni nani na kwa nini haya yote yanatokea.
Hasira zake bado zilikuwa dhidi ya inspekta Kobo aliyeamini kuwa alimchomea ndani ya nyumba kisa mapenzi.
Alipona vipi na nini kinaendelea katika maisha yake haya nd'o makuu aliyojiuliza.
Kuhusu kutafutwa kwa Majenga na watu asiowajua kukapunguza ile hisi yake kuwa chanzo cha kila kitu ni mapenzi.
Akabaini kuwa lipo la nyongeza.
Mama Martin ambaye hakuwa ameimarika sana kiafya safari hii alionyesha ushirikiano wa hali ya juu, usiku uleule alimpeleka Martin hadi nyumba aliyowahi kuishi mzee Majenga ambapo baadaye alipangisha na kuondoka zake kuelekea Shinyanga.
"Ila Shinyanga sijamuona kabisa..." Nguzu alizungumza wakati wanaelekea katika nyumba ile.
"Bado haujabadilika mwanangu, yaani Shinyanga kubwa vile wewe umtafute mtu usiyemjua na ukampata kabisa. Labda muujiza ama maigizo." Mama alimkata juu kwa juu Nguzu, haikuwa mara ya kwanza hali ile. Tangu utoto wake.
Mtoto hakui kwa mama!
Walipewa ushirikiano mkubwa sana walipowasili eneo lile, uzuri mtoto wa mzee Majenga alikuwa anaishi katika chumba kimojawapo, na alikuwa pale kama msimamizi wa nyumba ile.
"Kumpata kwa leo itakuwa ngumu sana, maana leo watu wametoa kodi. Na yule akipata kodi anamalizia katika ulevi wake.” Mtu aliyekuwa anawapa maelekezo alisema kwa masikitiko.
“Unaweza kujua baa ambazo hupenda kuzitembelea?” Nguzu aliuliza kwa udadisi.
“Bora angekuwa anaenda baa, huyu anaingia vilabuni, ana usemi wake unaosema kwamba mia mbili ya baa ni elfu kumi ya kilabuni”
Martin akajikuta anatokwa na tabasamu hafifu kwa kusikia haya.
Ghafla wakamwona yule mwenyeji akiwafanyia ishara ya kusikiliza kwa makini zaidi, wakasikia sauti ya mtu akiimba.
“Ni yeye... looh! leo amewahi kurudi hivi?” alishangaa na kuwashawishi Nguzu na mama yake washangae pia.
“Halafu..... halafu..... mama huyu kamfanana.... aahm! eeeh!” akaanza kujiuma uma. Alikuwa amemtazama Nguzu vizuri.
“Ninafanana naye sana alikuwa binamu yangu....” Nguzu akaiwahi hii kesi na kuisawazisha.
Mtarajiwa akawasili akiwa anaendelea kuimba nyimbo zake, nyimbo zilizomburudisha yeye pekee.
Hakuwa peke yake.....
Alikuwa na chupa kadhaa za pombe.
“Mnataka kuhama.... mnahama hama na hamjalipa kodi yangu.” Alizungumza huku akiwa hana hata uwezo wa kuona mbele vizuri, sembuse kung’amua kuwa kuna mtu anataka kuhama.
Akasogea kwa kunesanesa bila kuvunja chupa hata moja akawafikia.
“Shkamoo mama..... eeeh! mama nawe umehadimika kweli.” Alisalimia baada ya kumtambua mama Martin.
Salamu ilijibiwa, yule mwenyeji akajitoa katika mkutano huu akawaacha watatu hawa wakizungumza.
Walijitahidi hivyohivyo kuelewana japokuwa ilikuwa ngumu kwani yule mlevi kila mara alikuwa anasahau alichozungumza dakika kumi nyuma.
Mlevi huyu hakujua ni kiasi gani alikuwa faida kwa Martin Nguzu.
______
ASKARI aliyetegemewa na kuaminiwa zaidi alikuwa makini na silaha yake, alikuwa amejinyoosha chini na kunyanyuka kidogo sana usawa wa kifua na kuendelea. Bunduki yake kubwa ilikuwa imelazwa vyema katika muinuko huku akiona kila kitu kilichokuwa kikikatiza mbele yake.
Alitulia katika lindo lile kwa dakika nyingi akingoja walilotarajia litokee waimalize vyema siku yao.
Kilikuwa ni kikosi cha watu saba tu cha siri kilichokuwa kikitambua nini kinaendelea katika giza hili.
Majira ya saa nane usiku mchakacho ulisikika kutoka katika kichaka kimojawapo, mlengaji akatulia tuli bila kufanya shambulizi.
Alihitaji kupata uhakika wa kile alichokuwa anakwenda kukishambulia.
Barua kutoka kwa IGP ilielezea kuwa jambazi aliyekuwa anasakwa miaka mingi alikuwa mjini Shinyanga na huko alitarajia kuanzisha kampeni ya kuvamia na kuiba katika taasisi mbalimbali za kifedha.
Huu ukawa wakati wa askari kujitafutia nyongeza ya nyota kwa kumtia mikononi jangili huyo aliyekuwa anasifika kwa hatari yake na roho mbaya.
Simu ya upepo ilikuwa imeshikiliwa na askari mwingine, kazi yake ilikuwa moja tu kumweleza mlengaji nini cha kufanya ikiwa patakuwa na mabadiliko. Mlengaji hakupaswa kutikisika ama kujihusisha na mawasiliano mengine kwa sababu angeweza kuipoteza shabaha yake.
Mchakacho ule ukaongezeka tena, mlengaji akaendelea kutulia.
Na hapo redio ya upepo ikakoroma ikitoa taarifa kutoka upande wa pili.
“ANGUSHA MBUYU KUNA NYOKA! ANGUSHA HUO MBUYU...”
Sauti ile ikamfikia mlengaji, akaanza kutetemeka mikono yake. Ile sauti haikuwa ngeni na lile neno hakuwa akilisikia kwa mara ya kwanza. Ni siku kadhaa nyuma alilisikia katika simu ya upepo kutoka kwa kijana wake wa kazi aliyeuwawa kwa kupigwa risasi.
Mikono ikazidi kutetemeka, sauti ile nayo ikazidi kusisitiza neno lilelile.
‘angusha mbuyu’
Mapigo ya moyo yakaongezeka kasi yake.
Adui akajitokeza kutoka katika kichaka, mlengaji akatakiwa kufyatua na kumwangusha adui.
“Afande Kobo, fyatua!!” mshika simu alimwamrisha Kobo aliyekuwa anatetemeka na silaha yake.
Inspekta Kobo akaachia risasi ya kwanza, ikaenda malikiti.
Haikumkaribia adui badala yake ilimpa taarifa kuwa kuna hatari inawazunguka.
Kobo akamuona adui akirudi mbio kichakani, na baada ya sekunde chache hakutoka peke yake, lilikuwa jopo la maana lenye silaha za maangamizi.
Mpambano ukaanza.
Kobo akajaribu kutupa risasi nyingine, akakosa!
Ile kauli ya angusha mbuyu ilikuwa ikimsumbua kichwa chake.
Anayeitoa sauti ile ni nani? na kwanini alimuua kijana wake? na ni kipi kinamfanya amfuatilie Juma Kihwele kama yeye alivyokuwa anamfuatilia.
Mlolongo huu wa maswali ukazidi kumpoteza, kwa mara ya kwanza katika maisha yake anafyatua risasi tatu na hakuna hata moja iliyomlenga muhusika.
Kitimtimu kikaanza.
Askari saba ambao umri umewatupa mkono dhidi ya jopo la vijana majangili kumi na watano.
Risasi ziliruka hewani kwa fujo, huyu anarusha yule anajibu.
Inspekta Kobo alikuwa kama mpira wa kona, anakimbia huku na kule angali silaha anayo, badala ya kumkabili adui yeye anajiuliza ni nani mwenye ile sauti inayosema ‘angusha mbuyu’
Wasiwasi mara mbili, kwanza dhidi ya hao vijana majangili na pili juu ya adui ambaye wapo naye katika mpango huu kamambe.
Kobo akatamani kumuuliza askari mwenzake ambaye alikuwa anashikilia simu, amuulize yule ni naji alitoa ile amri.
Lakini, licha ya kuamini kuwa ule wakati haukuwa wa kuuliza maswali bali kila mmoja kuutetea uhai wake. Hata nafasi hiyo pia hakuipata kabla ya kukiona kichwa cha yule askari kikisambaratishwa vibaya mno na risasi iliyotoka inapotokea.
Madonge mazito ya damu yakamrukia wakati akijirusha pembeni zaidi asijekukumbwa na balaa la kusambaratishwa.
Inspekta Kobo alikuwa anahema juu juu huku akiomba dua Mungu amtunze asife usiku huo.
Taswira ya mkewe ambaye yu katika kuzimia ilimvamia. Akahisi kuwa kifo chake kitasababisha mkewe akirejewa na fahamu zake naye apoteze maisha kwa mshtuko wa kupoteza mume.
Sasa hofu ya kifo ilimtawala waziwazi......
Akaiweka sawa silaha yake na kujipa maneno ya ujasiri kupindukia ambayo yangeweza kumrejeshea ari yake ya upambanaji.
Aliiweka vyema silaha mkononi, ikawa inateleza.
Kwa mara ya kwanza bunduki yake ikawa inamsaliti. Akairudisha katika bega lake na kujipapasa kiunoni, akaichukua ile bastola yake anayoiamini kupindukia akaiweka sawa mkononi, hii yenyewe ilimuheshimu ikakaa sawa.
“Serenaserena afande Kobo.... Kobo...” Sauti ikamuita kutokea gizani. Ilianza na utambulisho wao wa siri waliokuwa wamepeana.
Inspekta Kobo akabonyea chini kisha akatoka ‘mkuku’ hadi alipoisikia sauti ile.
Alimkuta mwenzake akiwa katika dimbwi la damu akiogelea bila kupenda.
Hali yake ilikuwa mbaya sana, na alionekana muda si mrefu ataikimbia dunia kuelekea popote anapoamini kwa imani yake.
“Kimbia, hatari.... viumbe hawa hatari. Tunateketea wote....” Alizungumza kwa sauti ya chini sana. Akaweka kituo na kuhema kwa nguvu zote.
“Hakikisha unaishi ili kuwa shuhuda.... viumbe hatari sana wana siri zote. Usimuamini mtu jiamini wewe mwenyewe kuanzia sasa..... kuna wasaliti kati yetu.” alizidi kusihi.
“Na... naku.. nakuf... nakufa afande.” Alizungumza huku akizidi kukauka koo lake na sauti kufifia.
Ikawa kama alivyojitabiria!
Inspekta akazidisha umakini, akabaki na maswali lukuki, ni kwanini bwana yule anamweleza kuhusu wasaliti ndani yao, kwanini amemchagua yeye na amemuamini vipi kuwa yeye sio msaliti?
Mwenzao huyu!! alijisemea huku akiondoka kutoka eneo lile.
Sasa kila upande ulikuwa umetulia, ilikuwa ni vita ya kuviziana baina ya pande hizi mbili. Inspekta hakutaka kumuamini mtu yeyote zaidi.
Alitilia maanani uhai wake pekee.
Akakimbia hadi alipolifikia shimo asilojua matumizi yake, akatumbukia na kutulia ndani yake.
Alikuwa macho kabisa kisije kumdhuru chochote kitu.
Aliendelea kutulia hadi palipokucha akauona mwanga.
Lakini mwanga huu ulikuwa ukingojewa na watu wengi.
Ile Inspekta anatoa kichwa chake nje akakutana na sauti kali zikimkaripia asithubutu kufanya jambo lolote lile atue silaha zake chini na kisha kunyanyua mikono yake juu.
Alijitahidi kujitambulisha lakini hakuna ambaye alimsikiliza.
Akatii, kwa umakini wa hali ya juu askari wenye sare wakamkaribia na kumtia pingu mikononi na miguuni.
Ajabu!
Alistaajabu ni kipi kimejiri hadi kujikuta katika balaa kubwa kiasi kile tena ghafla.
Alionywa asithubutu kusema jambo lolote lile. Akaingizwa katika gari lenye ulinzi mkali kupindukia.
Hawakutaka kulala tena Shinyanga.
Amri ikatolewa kuwa iwe isiwe lazima inspekta Kobo afikishwe jijini Dar es salaam, na hiyo ilikuwa ni amri na sio ombi.
Inspekta Kobo hakuamini, vijana walio chini yake ki-cheo walikuwa wanamlinda huku wakimkaripia mara kwa mara.
Alifedheheka ila hakuwa na la kufanya.
Huu ukawa mwanzo wa safari mbaya na ya kutisha.
Wakati anaiacha ardhi ya Shinyanga, katika ardhi hiyohiyo harakati mpya ilianza kusukwa.
______
MAANDISHI YA: George Iron Mosenya
"Zungumza machache kati ya mengi uyajuayo..... ONYESHA vichache kati ya vingi unavyovimiliki. Katika maisha si vyema kila mtu kukujua kwa asilimia 100"
Hii ni SEHEMU YA KUMI NA MBILI.
GIZA lilikuwa ndani ya giza kwa mara nyingine, Konstebo Martin Nguzu alikuwa amempokea mama yake ambaye alikuwa mmoja kati ya wahanga wa ile kamatakamata iliyofanywa kwa masilahi ya watu wachache waliokuwa wamekerwa baada ya mwenzao mmoja kuuwawa kifedhuli.
Ghafla bin vuu mambo yakabadilika, kota zikatishiwa kuchomwa. Wakagwaya na kuwaachia huru wale waliokuwa wamekamatwa katika namna ya uonevu.
Ni giza hilihili sasa lipo ndani ya giza tena, ana kwa ana na mama yake mzazi.
Martin Nguzu alimpa pole mama yake huku akiwa na haraka sana ya kujua ni wapi hasa anapoweza kumpata Majenga waweze kuzungumza na kutambua ama kujitambua upya yeye ni nani na kwa nini haya yote yanatokea.
Hasira zake bado zilikuwa dhidi ya inspekta Kobo aliyeamini kuwa alimchomea ndani ya nyumba kisa mapenzi.
Alipona vipi na nini kinaendelea katika maisha yake haya nd'o makuu aliyojiuliza.
Kuhusu kutafutwa kwa Majenga na watu asiowajua kukapunguza ile hisi yake kuwa chanzo cha kila kitu ni mapenzi.
Akabaini kuwa lipo la nyongeza.
Mama Martin ambaye hakuwa ameimarika sana kiafya safari hii alionyesha ushirikiano wa hali ya juu, usiku uleule alimpeleka Martin hadi nyumba aliyowahi kuishi mzee Majenga ambapo baadaye alipangisha na kuondoka zake kuelekea Shinyanga.
"Ila Shinyanga sijamuona kabisa..." Nguzu alizungumza wakati wanaelekea katika nyumba ile.
"Bado haujabadilika mwanangu, yaani Shinyanga kubwa vile wewe umtafute mtu usiyemjua na ukampata kabisa. Labda muujiza ama maigizo." Mama alimkata juu kwa juu Nguzu, haikuwa mara ya kwanza hali ile. Tangu utoto wake.
Mtoto hakui kwa mama!
Walipewa ushirikiano mkubwa sana walipowasili eneo lile, uzuri mtoto wa mzee Majenga alikuwa anaishi katika chumba kimojawapo, na alikuwa pale kama msimamizi wa nyumba ile.
"Kumpata kwa leo itakuwa ngumu sana, maana leo watu wametoa kodi. Na yule akipata kodi anamalizia katika ulevi wake.” Mtu aliyekuwa anawapa maelekezo alisema kwa masikitiko.
“Unaweza kujua baa ambazo hupenda kuzitembelea?” Nguzu aliuliza kwa udadisi.
“Bora angekuwa anaenda baa, huyu anaingia vilabuni, ana usemi wake unaosema kwamba mia mbili ya baa ni elfu kumi ya kilabuni”
Martin akajikuta anatokwa na tabasamu hafifu kwa kusikia haya.
Ghafla wakamwona yule mwenyeji akiwafanyia ishara ya kusikiliza kwa makini zaidi, wakasikia sauti ya mtu akiimba.
“Ni yeye... looh! leo amewahi kurudi hivi?” alishangaa na kuwashawishi Nguzu na mama yake washangae pia.
“Halafu..... halafu..... mama huyu kamfanana.... aahm! eeeh!” akaanza kujiuma uma. Alikuwa amemtazama Nguzu vizuri.
“Ninafanana naye sana alikuwa binamu yangu....” Nguzu akaiwahi hii kesi na kuisawazisha.
Mtarajiwa akawasili akiwa anaendelea kuimba nyimbo zake, nyimbo zilizomburudisha yeye pekee.
Hakuwa peke yake.....
Alikuwa na chupa kadhaa za pombe.
“Mnataka kuhama.... mnahama hama na hamjalipa kodi yangu.” Alizungumza huku akiwa hana hata uwezo wa kuona mbele vizuri, sembuse kung’amua kuwa kuna mtu anataka kuhama.
Akasogea kwa kunesanesa bila kuvunja chupa hata moja akawafikia.
“Shkamoo mama..... eeeh! mama nawe umehadimika kweli.” Alisalimia baada ya kumtambua mama Martin.
Salamu ilijibiwa, yule mwenyeji akajitoa katika mkutano huu akawaacha watatu hawa wakizungumza.
Walijitahidi hivyohivyo kuelewana japokuwa ilikuwa ngumu kwani yule mlevi kila mara alikuwa anasahau alichozungumza dakika kumi nyuma.
Mlevi huyu hakujua ni kiasi gani alikuwa faida kwa Martin Nguzu.
______
ASKARI aliyetegemewa na kuaminiwa zaidi alikuwa makini na silaha yake, alikuwa amejinyoosha chini na kunyanyuka kidogo sana usawa wa kifua na kuendelea. Bunduki yake kubwa ilikuwa imelazwa vyema katika muinuko huku akiona kila kitu kilichokuwa kikikatiza mbele yake.
Alitulia katika lindo lile kwa dakika nyingi akingoja walilotarajia litokee waimalize vyema siku yao.
Kilikuwa ni kikosi cha watu saba tu cha siri kilichokuwa kikitambua nini kinaendelea katika giza hili.
Majira ya saa nane usiku mchakacho ulisikika kutoka katika kichaka kimojawapo, mlengaji akatulia tuli bila kufanya shambulizi.
Alihitaji kupata uhakika wa kile alichokuwa anakwenda kukishambulia.
Barua kutoka kwa IGP ilielezea kuwa jambazi aliyekuwa anasakwa miaka mingi alikuwa mjini Shinyanga na huko alitarajia kuanzisha kampeni ya kuvamia na kuiba katika taasisi mbalimbali za kifedha.
Huu ukawa wakati wa askari kujitafutia nyongeza ya nyota kwa kumtia mikononi jangili huyo aliyekuwa anasifika kwa hatari yake na roho mbaya.
Simu ya upepo ilikuwa imeshikiliwa na askari mwingine, kazi yake ilikuwa moja tu kumweleza mlengaji nini cha kufanya ikiwa patakuwa na mabadiliko. Mlengaji hakupaswa kutikisika ama kujihusisha na mawasiliano mengine kwa sababu angeweza kuipoteza shabaha yake.
Mchakacho ule ukaongezeka tena, mlengaji akaendelea kutulia.
Na hapo redio ya upepo ikakoroma ikitoa taarifa kutoka upande wa pili.
“ANGUSHA MBUYU KUNA NYOKA! ANGUSHA HUO MBUYU...”
Sauti ile ikamfikia mlengaji, akaanza kutetemeka mikono yake. Ile sauti haikuwa ngeni na lile neno hakuwa akilisikia kwa mara ya kwanza. Ni siku kadhaa nyuma alilisikia katika simu ya upepo kutoka kwa kijana wake wa kazi aliyeuwawa kwa kupigwa risasi.
Mikono ikazidi kutetemeka, sauti ile nayo ikazidi kusisitiza neno lilelile.
‘angusha mbuyu’
Mapigo ya moyo yakaongezeka kasi yake.
Adui akajitokeza kutoka katika kichaka, mlengaji akatakiwa kufyatua na kumwangusha adui.
“Afande Kobo, fyatua!!” mshika simu alimwamrisha Kobo aliyekuwa anatetemeka na silaha yake.
Inspekta Kobo akaachia risasi ya kwanza, ikaenda malikiti.
Haikumkaribia adui badala yake ilimpa taarifa kuwa kuna hatari inawazunguka.
Kobo akamuona adui akirudi mbio kichakani, na baada ya sekunde chache hakutoka peke yake, lilikuwa jopo la maana lenye silaha za maangamizi.
Mpambano ukaanza.
Kobo akajaribu kutupa risasi nyingine, akakosa!
Ile kauli ya angusha mbuyu ilikuwa ikimsumbua kichwa chake.
Anayeitoa sauti ile ni nani? na kwanini alimuua kijana wake? na ni kipi kinamfanya amfuatilie Juma Kihwele kama yeye alivyokuwa anamfuatilia.
Mlolongo huu wa maswali ukazidi kumpoteza, kwa mara ya kwanza katika maisha yake anafyatua risasi tatu na hakuna hata moja iliyomlenga muhusika.
Kitimtimu kikaanza.
Askari saba ambao umri umewatupa mkono dhidi ya jopo la vijana majangili kumi na watano.
Risasi ziliruka hewani kwa fujo, huyu anarusha yule anajibu.
Inspekta Kobo alikuwa kama mpira wa kona, anakimbia huku na kule angali silaha anayo, badala ya kumkabili adui yeye anajiuliza ni nani mwenye ile sauti inayosema ‘angusha mbuyu’
Wasiwasi mara mbili, kwanza dhidi ya hao vijana majangili na pili juu ya adui ambaye wapo naye katika mpango huu kamambe.
Kobo akatamani kumuuliza askari mwenzake ambaye alikuwa anashikilia simu, amuulize yule ni naji alitoa ile amri.
Lakini, licha ya kuamini kuwa ule wakati haukuwa wa kuuliza maswali bali kila mmoja kuutetea uhai wake. Hata nafasi hiyo pia hakuipata kabla ya kukiona kichwa cha yule askari kikisambaratishwa vibaya mno na risasi iliyotoka inapotokea.
Madonge mazito ya damu yakamrukia wakati akijirusha pembeni zaidi asijekukumbwa na balaa la kusambaratishwa.
Inspekta Kobo alikuwa anahema juu juu huku akiomba dua Mungu amtunze asife usiku huo.
Taswira ya mkewe ambaye yu katika kuzimia ilimvamia. Akahisi kuwa kifo chake kitasababisha mkewe akirejewa na fahamu zake naye apoteze maisha kwa mshtuko wa kupoteza mume.
Sasa hofu ya kifo ilimtawala waziwazi......
Akaiweka sawa silaha yake na kujipa maneno ya ujasiri kupindukia ambayo yangeweza kumrejeshea ari yake ya upambanaji.
Aliiweka vyema silaha mkononi, ikawa inateleza.
Kwa mara ya kwanza bunduki yake ikawa inamsaliti. Akairudisha katika bega lake na kujipapasa kiunoni, akaichukua ile bastola yake anayoiamini kupindukia akaiweka sawa mkononi, hii yenyewe ilimuheshimu ikakaa sawa.
“Serenaserena afande Kobo.... Kobo...” Sauti ikamuita kutokea gizani. Ilianza na utambulisho wao wa siri waliokuwa wamepeana.
Inspekta Kobo akabonyea chini kisha akatoka ‘mkuku’ hadi alipoisikia sauti ile.
Alimkuta mwenzake akiwa katika dimbwi la damu akiogelea bila kupenda.
Hali yake ilikuwa mbaya sana, na alionekana muda si mrefu ataikimbia dunia kuelekea popote anapoamini kwa imani yake.
“Kimbia, hatari.... viumbe hawa hatari. Tunateketea wote....” Alizungumza kwa sauti ya chini sana. Akaweka kituo na kuhema kwa nguvu zote.
“Hakikisha unaishi ili kuwa shuhuda.... viumbe hatari sana wana siri zote. Usimuamini mtu jiamini wewe mwenyewe kuanzia sasa..... kuna wasaliti kati yetu.” alizidi kusihi.
“Na... naku.. nakuf... nakufa afande.” Alizungumza huku akizidi kukauka koo lake na sauti kufifia.
Ikawa kama alivyojitabiria!
Inspekta akazidisha umakini, akabaki na maswali lukuki, ni kwanini bwana yule anamweleza kuhusu wasaliti ndani yao, kwanini amemchagua yeye na amemuamini vipi kuwa yeye sio msaliti?
Mwenzao huyu!! alijisemea huku akiondoka kutoka eneo lile.
Sasa kila upande ulikuwa umetulia, ilikuwa ni vita ya kuviziana baina ya pande hizi mbili. Inspekta hakutaka kumuamini mtu yeyote zaidi.
Alitilia maanani uhai wake pekee.
Akakimbia hadi alipolifikia shimo asilojua matumizi yake, akatumbukia na kutulia ndani yake.
Alikuwa macho kabisa kisije kumdhuru chochote kitu.
Aliendelea kutulia hadi palipokucha akauona mwanga.
Lakini mwanga huu ulikuwa ukingojewa na watu wengi.
Ile Inspekta anatoa kichwa chake nje akakutana na sauti kali zikimkaripia asithubutu kufanya jambo lolote lile atue silaha zake chini na kisha kunyanyua mikono yake juu.
Alijitahidi kujitambulisha lakini hakuna ambaye alimsikiliza.
Akatii, kwa umakini wa hali ya juu askari wenye sare wakamkaribia na kumtia pingu mikononi na miguuni.
Ajabu!
Alistaajabu ni kipi kimejiri hadi kujikuta katika balaa kubwa kiasi kile tena ghafla.
Alionywa asithubutu kusema jambo lolote lile. Akaingizwa katika gari lenye ulinzi mkali kupindukia.
Hawakutaka kulala tena Shinyanga.
Amri ikatolewa kuwa iwe isiwe lazima inspekta Kobo afikishwe jijini Dar es salaam, na hiyo ilikuwa ni amri na sio ombi.
Inspekta Kobo hakuamini, vijana walio chini yake ki-cheo walikuwa wanamlinda huku wakimkaripia mara kwa mara.
Alifedheheka ila hakuwa na la kufanya.
Huu ukawa mwanzo wa safari mbaya na ya kutisha.
Wakati anaiacha ardhi ya Shinyanga, katika ardhi hiyohiyo harakati mpya ilianza kusukwa.
______