Kituo cha Oil Link Afrika Sana huwaibia wateja. EWURA Wamulikeni!

Ngareni3

Member
Dec 4, 2006
31
2
Tukio lilitokea siku ya Jumapili tarehe 11 mwezi Julai, 2010 katika kituo cha mafuta cha Oil link Afrika Sana Mwenge, bado linaniachia maswali mengi. Swali kubwa ni kuwa: EWURA inamlinda vema mlaji wa mafuta nchini? Je, suala zima la kumlinda mlaji katika nchi yetu linapewa kipaumbele cha kutosha? Ni dhahiri kuwa Mlaji katika Nyanja zote bado hana wa kumtetea kwa udhati na umakini unaotakiwa. Zipo juhudi katika maeneo mbali mbali, lakini pamoja na juhudi hizi mamlaka husika bado hazijaweza kuwafikia walaji katika sekta zote. Leo nizungumzie haki za mlaji wa mafuta ya petrol na dizeli.
Lipo suala kubwa la kuchakachua mafuta ambalo pamoja na juhudi mbali mbali, bado mlaji wa kawaida mwenye gari lake ndiye anayebeba hasara pale gari linapoharibika. Hata linapoharibika gari la serikali au kampuni nyingine ya umma, gharama hizi mwisho wa yote zitamwendea mlaji wa kawaida kama wewe na mimi kwa namna ya kodi zaidi au bei zaidi kwa bidhaa husika!
Suala lililonikuta mimi ni kununua mafuta hewa na kulipa pesa taslimu na hata kushawishiwa kulipa zaidi. Nilipita katika kituo cha mafuta cha Oil Link Afrika Sana makutano ya barabara ya Shekilango na Mwenge, karibu na klabu maarufu ya Ambiance. Kituo hiki cha mafuta kwa muda mrefu kimekuwa na bei ndogo ya mafuta ukilinganisha na vituo vingine vya mafuta na jambo hili limekuwa likivutia sana watu wengi kwani bei zao zimekuwa chini kwa zaidi kidogo ya shilingi mia moja kwa lita moja ya mafuta ya petrol ukilinganisha na vituo vingine. Jambo hili limekuwa kama chambo na watu wengi wamekuwa wakikimbilia pale.
Kama waswahili wasemavyo kuwa rahisi ni aghali, usemi huo umenikuta bayana. Nilipofika katika kituo husika, tenki langu lipo upande wa kushoto na kwa bahati mbaya nikavuta gari mbele kidogo na sikuwa naiona mashine, ila abiria wangu aliyekuwa upandewa kushoto nikamwambia kuwa aangalie pampu inavyosoma. Kijana yule aliyekuwa katika pampu ya kwanza kushoto katika kituo hiki ukitoka njia panda ielekeayo Mwenge, alianza kuweka mafuta bila kurekebisha pampu kwa kuwa alikuwa amemaliza kuweka mafuta katika gari lililokuwa mbele yangu. Alifanya hivyo kwa wepesi wa ajabu, nami nikashtuka kidogo kwa kuwa si kawaida, pampu hizi mara nyingi wanazirudisha katika kusoma sifuri ndipo wanamwekea mteja mwingine. Jambo la pili ni muda aliotumia kuniwekea mafuta ulikuwa mfupi sana. Mimi nilipia mafuta ya shilingi elfu ishirini. Kijana huyu kwa muda mfupi sana akasema tayari. Kengele ya pili ikagonja kichwani!
Jambo la tatu katika sinema hii, kijana aliyeweka mafuta alinifuata na kusema kuwa pampu imepitiliza na kaweka mafuta ya shilingi elfu ishirini na nne na mia tano na sabini hivi, hivyo nimwongezee pesa. Ule mshituko wa matukio yaliyojitokeza haraka haraka nikamweleza kuwa nilitaka mafuta ya shilingi elfu ishirini na sina fedha zaidi. Kijana akasisitiza kuwa basi walao nimtulize na shilingi elfu mbili. Nikamjibu na hata hiyo sina. Mwisho akasema basi nimpe elfu moja ili kupunguza hasara, basi kiungwana nikasema nitakapopita tena pale nitampa bila shaka. Kuanza safari nikapata mshtuko mbona mshale wa mafuta hauna mabadiliko. Upo pale pale! Ndipo matukio yote yaliyotangulia yakapata majibu yake. Sikuwekewa mafuta yoyote katika kituo kile!
Nilirudi katika kituo hicho cha Oil Link kupambana na kijana aliyehusika, kwamba hakuniwekea mafuta hata kidogo na zaidi sana alitaka nimpe pesa za ziada. Kijana alisisitiza kuwa kaweka mafuta na hata zaidi na hata kudiriki kusema watu wengine hatuna shukrani nimepewa mafuta zaidi na sitoi shukrani. Hoja ikawa mbona mshale wa mafuta hauna mabadiliko na unafanya kazi vizuri. Akawa hana jibu. Hata wafanyakazi wenzake waliokuwa katika pampu nyingine walionyesha kuwa mwenzao kuna kamchezo katuchezea pale; kwa kuwa walisisitiza kuwa nimbane mwenzao! Bahati mbaya meneja wa kituo hakuwa pale jioni hiyo. Ilibidi kuondoka na kwenda kituo kingine na kuweka mafuta ya elfu kumi na mshale ukapanda inavyotakiwa. Hivyo ni wazi kuwa kijana wa Oil link hakuniwekea mafuta hata kidogo, na pengine aliweka kidogo sana. Alichofanya ni kuendeleza pampu ilipofikia kwa gari lilowekewa mafuta kabla yangu, na kwa kuwa mimi sikuona pampu aliweka pengine mafuta ya elfu nne peke yake.
Siku iliyofuatia nilifanya juhudi kuonana na Meneja wa Oil Link naye japokuwa alisikiliza shauri hilo hakuwa na suluhisho kwa jambo hili la wizi lililofanywa na mfanyakazi wake halali. Hoja yangu kubwa ilikuwa endapo kweli kijana yule alizidisha mafuta ya elfu nne hivi, basi mahesabu yake aliyokabidhi lazima yaonyeshe nakisi hiyo. Alichosema meneja huyo ni kuwa vijana hao wanaajiriwa kwa siku tatu kisha wanapumzika na aliahidi kufuatilia kwa wakubwa wake.
Ni wazi kuwa mlaji wa mafuta ya magari, bado ana maswahibu mengi. Pamoja na janga la kuchakachua tatizo hili la wizi wa wazi wazi lazima EWURA nao watupe ufumbuzi. Mteja anapokwenda katika kituo cha mafuta anayo bajeti yake. Angependa kupata bidhaa hiyo ya mafuta kadiri ya bajeti yake. Mlaji yeyote angependa kupata bidhaa kadiri ya fedha anayotoa. Haiwezekani watu wote sasa twende katika vituo vya mafuta na vidumu ili wapimao wasitudhulumu. Angalia vijana wa daladala, taxi pamoja na bajaji wao walishashtuka siku nyingi. Anakwenda kituo cha mafuta na galoni na pale inakuwa ngumu kumpa kipimo pungufu. Hilo haliwezi kufanywa na kila mtu anayetaka bidhaa ya mafuta. Itakuwa kero na upotezaji mkubwa wa muda wa kufanya shughuli za maendeleo. Hii ni kazi ya EWURA! Tunawalipa kwa ajili hiyo, wapo kwa ajili hiyo, watekeleze wajibu huu!
EWURA pamoja na kusimamia wimbi hili la kuchakachua mafuta ni lazima pia kumlinda mlaji wa mafuta haya kwa kuhakikisha kuwa vipimo vipo sahihi mara zote. Matatizo ya kiuchumi yapo kwa kila mtu, na si vyema kumbebesha mwananchi uzito kwa sababu tu ya tamaa na hulka ya wizi kwa baadhi ya wafanyakazi wa pampu za mafuta hapa nchini. Kijana aliyenifanyia uhuni huu ni mwizi na anapaswa kuhukumiwa kama mwizi mwingine yoyote. Na waliomwajiri nao wanaacha maswali yasiyo na majibu. Ni wangapi amewahi kuwafanyia jambo hili! Inakuwaje wenye vituo waachie hali hii kuendelea kama vile kila mtu kaachie shamba la bibi avune! Meneja wa kituo hakuonyesha ushirikiano. Pengine ni sehemu ya mchezo huu mchafu. Kwa nini tumuache mlaji ajihangaikie kama kuku wa kienyeji kama vile nchi yetu haina sera yoyote ya kumlinda mlaji?
EWURA tusaidieni katika hili. Ndilo jukumu lenu. Mlindeni mteja wenu katika eneo hili. Ndiyo maana kila mteja anaponunua bidhaa mnazosimamia, asilimia ile moja mnayopata ni kwa ajili ya kuhakikisha kuwa mteja husika anapata bidhaa inayolingana na fedha anayotoa. Msitumie fedha hizi mnazokusanya kwa warsha, semina na makongomano. Tumeni vijana kupita katika pampu hizi na kutoa adhabu kali kwa wezi hawa. Anzeni kwa kukimulika kituo hiki cha Oil Link! Mnao uwezo wa kutoa mchango mzito na wa dhati katika azma ile ya kumpa maisha bora kwa kila mtanzania. Hili mnaliweza, tekelezeni wajibu wenu. Katika kufanya hilo mtakuwa mmetoa mchango muhimu kwa fedha tunazowapa kila tununuapo bidhaa mnazozisimamia. Tusimwache mlaji wa bidhaa ya mafuta katika mikono ya hawa wanyang’anyi wa mchana kweupe. Pamoja na taarifa mnazotoa, daima toeni si tu vituo vinavyochakachua mafuta, bali pia na taarifa ya vituo vyenye pampu zinazompunja mlaji, ili MLAJI atoe hukumu yake. Na kwa walaji wenzangu, narudia kusema kuwa: RAHISI ni gharama. Kiangalieni vyema kituo hiki cha mafuta cha Oil Link!
Stephen Kirama; Mhadhiri Msaidizi, Idara ya Uchumi, UDSM.
ngareni3@yahoo.co.uk, 0767250573
 
aaah bana hii kitu ndefu sana bana

Msiwe wavivu wa kusoma, mwandishi ameandika kwa kirefu ili muweze kuelewa tatizo na nani anawajibika kutatua matatizo husika. Amefanya hivyo ili msomaji ajitosheleze na asiwe na maswali mepesi ya kuuliza!! Suala la regulatory role na effciency ya EWURA ni muhimu sana katika uchumi wa soko huria . EWURA wasipofanya kazi yao vyema nchi inaweza kuingia katika machafuko makubwa kwa sababu ya precipitated economic crisis!!
 
Hicho kituo hilo ni tatizo kubwa saana. Mwanzoni niliwahi kuwauliza kwanini wao wanauza mafuta bei rahisi kuliko vituo vingine? wakasema hawajainvest saana kwenye infrastructure km BP nk kwahiyo wakitoza bei kubwa kutakuwa hakuna incentive ya wateja kwenda pale. Ukweli hili lilikuwa ni jibu la Kisayansi.
Na mimi nikaingia katika wale wa kupita kuweka mafuta pale. Lakini nikawa ninawasi huenda yanachanganywa, (ila hili halikuwahi kutokea). Baada ya muda nikagundua kuwa meter reading zao zina tatizo maana ukiweka mafuta yanawahi kwisha mapema kuliko uzoefu wangu wa BP. Baada ya kugundua hilo ndio nikahama kabisa sasa hivi nipo BP.
 
Back
Top Bottom