KISA CHA SINDBAD BAHARIA
SEHEMU 10
"Bwana wangu" nikamjibu "usiwe na khofu mimi si sheitwaan wala si jinni, wala si pepo mbaya, bali ni mwanadamu kama wewe tena mfanyabiashara, kisa changu kilichonifanya nifike hapa ni cha ajabu kishindacho kisa chengine chochote kilichowahi kumpata mtu, kwanza tafadhali hebu pokea almasi hizi ambazo mimi mwenyewe nimezikusanya kutoka katika lile bonde la kutisha.
Hapo nikachagua almasi chache nzuri kutoka mfukoni mwangu nikamkabidhi yule mtu, nikisema: "almasi hizi zitakuletea utajiri wowote unaoutaka."
Yule bwana alipozipokea na alipoona uzuri wake alifurahi sana; akanishukuru na kuniombea dua njema.
Wakati tulipokua tukiongea vile wakatokea wafanya biashara wengine kutoka pande nyengine za ule mlima. Wakatuzunguka wakisikiliza kwa mastaajabu makubwa yale yalionipata. Wakanipongeza wakisema, "hakika kuokoka kwako ni kwa ajabu sana, kwani hakuna mtu yeyote aliewahi kukanyaga bonde lile akarejea hai, mwenyezi mungu ashukuriwe kwa kuokoka"
Basi wale wafanya biashara wakanichukua mpaka kwenye kambi yao wakanipa chakula na kinywaji, halafu nikalala kama mfu, mapema asubuhi ya pili tukang'oa kambi na baada ya kusafiri kwa muda mrefu kupitia milima mirefu, tukafika kwenye ukingo wa bahari, huko tukapanda merkebu tukasafiri mpaka tukafika kwenye kisiwa kimoja kilichojaa miti yenye mashina manene.
Watu mia wangeweza kukaa kwenye kivuli cha mti mmoja, ni kutoka katika mashina ya miti hii ndiko kafuri inayotoa harufu nzuri baada ya watu kichimba mashina ya miti hiyo. Utomvu utokao huangukia kwenye vyombo maalum vilivyotegwa chini yake. Utomvu huo unapoganda hua kafuri.
Kwenye kisiwa hicho niliona pia wanyama wakubwa waitwao karkadan waliofanana na vifaru, wanyama hawa wamefanana na ng'ombe au nyati lakini warefu kuliko hata twiga, karkadan wanapembe katikati ya paji la uso na huwashambulia tembo kwa pembe yao hio na kuwakita nayo na kuwabeba kila waendako mpaka tembo hufa.
Baada ya muda mafuta ya tembo humyenyukia machoni na kumpofoa nakumuuwa yule karkadan. Hapo madege Rok kushuka kwa kasi na kuwabeba wote wawili tembo na karkadan mpaka kwenye vilele vya mlima kwenye viota vyao.
Basi hapo kisiwani nikawauzia wafanya biashara sehemu ya almasi zangu na nyengine nilibadilishana nao kwa bidhaa nyengine nyingi. Baada ya muda tulitweka matanga tukaendelea kufanya biashara kutoka bandari hadi bandari, na kutoka kisiwa kimoja hadi kingine mpaka tukawasili basrah, baada ya kupumzika basrah kwa muda wa siku chache nilielekea Baghdad jiji la amani, huku nimejaa kila namna ya vitu vya tunu na almasi nyungi.
Bila kukawia nilielekea nyumbani kwangu nilipokelewa mikono miwili na ndugu, jamaa na marafiki zangu na majirani. Wote nikawapa zawadi halafu nikatoa sadaka kwa maskini, yatima na wajane.
Baada ya muda nilisahau kabisa yale masaibu yote yalionipata katika safari yangu ya pili, nikaishi kwa raha, furaha na starehe zisizo na kifani nikawa nawaalika ndugu na marafiki kuja kwangu kila siku kushiriki maakuli mbali Mali.
Ikiwa navaa lebasi ghali za thamani mpaka sifa zangu zikaenea kote. Watu wakawa waja kusikiliza visa vya safari zangu zilizonifikisha nchi za mbali. Wote wakawa wanastaajabu kwa hatari nilizozikabili na kuokoka kwangu.
"Na hiyo waungwana ndio ilikua safari yangu ya pili" alimalizia kusimulia Sindbad Baharia. "Kesho in sha Allah nitawasimulia yaliyonipata safari yangu ya tatu."
Itaendelea...