SEHEMU SITA
Baada ya kuuza bidhaa zangu zote kwa bei ya faida kubwa, nilinunua bidhaa za nchi ile ambazo ni adimu kwetu, zikiwemo vipande vya sandali, udi, karafuu maiti, kungu manga, hiliki, pilipili manga, bizari nzima, giligilani na tangawizi.
Mambo yalipokua tayari nilimwendea mfalme Maharjan nikamshukuru kwa wema na ukarimu wake wote, nikamuomba anipe ruhusa ya kurejea kwetu, bila kusita sita alikubali.
Basi tuling'oa nanga tukatweka matanga tukaelekea baharini.
Baada ya safari ya usiku na mchana kwa muda siku kadhaa tuliwasili Basrah Salama salmini, na baada ya kupumzika siku chache, nikaelekea kwetu Baghdad.
Kusema kweli nilifurahi sana kurudi kwetu! Bila kuchelewa nilielekea mtaa wa barabara nilikotoka, huko nilinunua nyumba, mashamba makubwa, watumwa na wajakazi wengi, nikawa tajiri kuliko nilivyokua awali wakati baba yangu alipofariki.
Nikakaa raha mustarehe, walakin baada ya muda nilisahau tabu na mashaka yote yalionipata baharini: nikachoshwa na yale maisha ya kula, kunywa na kukaa tu nyumbani, basi nilianza tena kujitayarisha kwa safari nyengine tena ya baharini.
"Hiki waungwana ndicho kisa cha safari yangu ya kwanza baharini" alisema Sindbad Baharia. Kesho in sha Allah nitawaeleza yalionipata katika safari yangu ya pili."
Kulipokuchwa Sindbad Baharia alimkaribisha Hindbad Hamali ashirikiane nao kesho katika maakuli ya mshana.
Karamu ya siku ile ilipokwishwa Sindbad Baharia alimpa Mgeni wake reale mia moja za dhahabu, akimwambia: "Leo tumefurahishwa na ugeni wako; tunataraji kukuona tena kesho."
Hindbad Hamali akamshukuru mwenyeji wake akienda zake huku amejaa furaha ya kupewa zile fedha nyingi na akistaajabia yale yaliompata Sindbad Baharia.
...
ITAENDELEA