1. Shughuli nzima ya jana Ngerengere, tumeiangalia kumuona CDF Mwamunyange na sasa tunatupiana matusi ya nani alizusha kapewa sumu, na ----- mwingine wote. Kikubwa katika habari nzima ya Ngerengere ni CDF, si alichosema Kikwete, alichosema Mwinyi, alichosema Mwamunyange (tulithibitisha sauti yake haionyeshi kuwa ni mgonjwa) au kuliona kundi kubwa la maafisa wa kijeshi wa Kichina na alichosema Msemaji wa jeshi la China. Hapa inaonekana wazi tabia na mazoea yetu yalikuwa ni ushahidi wa kuonekana Mwamunyange na mengine yote hayakuwa na maana.
2. Sikuhoji uhusiano wetu na China, la hasha. Kwa wanaonifahamu maandiko yangu, miaka 10-15 niliwahi kuuliza kwa nini Tanzania hatujifunzi kutoka kwa Wachina wanavyojijenga kiuchumi. Hovyo kwa wanaodhania nina upofu wa udugu na urafiki wetu na China au kuwa na tatizo na China wamekosea sana.
3. Swali kuu liko kwenye kuhoji kama Tanzania haina fedha zilizotangazwa kuwa ni gharama ya ujenzi wa kiwanja hiki cha ndege cha kijeshi. Kwenye hotuba na taarifa za tukio hili, tumeambiwa kuwa gharama yote ni Dola za Marekani karibu Milioni 70 ($70 Mil), Je Tanzania haina fedha hizi au hazikuwekwa kwenye bajeti mpaka China ije kutufadhili?
4. Utegemezi: Tanzania na hasa awamu ya nne, kumejengeka mazoea ya kuomba misaada (kutembeza Bakuli-Bakulism) hata kwa vitu ambavyo tuna uwezo mkubwa wa kifedha na tunaweza kutumia fedha za mapato yetu wenyewe. Hili ni jambo ambalo sikuwa na ulazima kulifafanua awali, lakini sasa inaeleka ama watu hawaelewi tofauti ya mkopo na misaada. Katika magazeti ya leo, kuna taarifa kuwa tumepokea dola Milioni 5 kwa ajili ya mradi wa umeme kama msaada kutoka kwa wahisani. Nikifikiria capacity charges tunazowalipa IPTL, Symbion na wengine kila siku, ni karibu dola laki 3 zinalipwa kwa makampuni haya badala ya fedha hizi zingeweza kuwekwezwa Tanesco na kuboresha mitambo yetu. Hivyo suala kubwa hapa ni tabia ya utegemezi. Aidha nimeuliza, kama tunafedha zilikaa Benki Kuu na Hazina na zikatolewa kinyemela kiuhalifu kuneemesha watu (EPA, Escrow) kwa nini hatutumii fedha hizi kujikopa na kujitutumua na si kutegemea misaada? Ikiwa 40% ya bajeti ni misaada na mikopo na masharti yake mara nyingine yanatutoa kamasi, ni lini tutaacha kutegemea misaada?
5. Kama tungesema Serikali imetoa ukandarasi wa uwanja wa ndege za kijeshi kwa Jesho la China na tutailipa Serikali ya China, hapo si kitu cha kushangaza. Mlioleta mifano ya ujenzi wa kituo cha nyuklia Uingereza na kufananisha na hili la Ngerengere, au hata jinsi Marekani na nchi nyingine zinavyokopeshwa na china mmesahau kuwa kuna tofauti ya mkopo, mkataba wa kumlipa mkandarasi na msaada.
6. Tumeingia mikataba na kukopa kutoka wachina, fedha nyingi sana ambazo ni mara 4 ya bajeti yetu ya mwaka tangu mwaka 2012. TUna madeni mengi na nchi nyingine, tunaahidi tutayalipa. Lakini ikiwa tunakopa na kutegemea kila kitu tufanyiwe zaidi ya mkopo na kuwa msaada (walishatupa merikebu mbili za kijeshi mwaka jana kama zwadi) hatujiulizi utaifa na ufungamano wetu kujitegemea unatoka wapi? Je deni hili na fadhila hizi tunazilipa vipi ikiwa uzalishaji wetu, mapato ya serikali na hata bajeti yetu inaonyesha hatuna hata uwezo wa kujihudumia kwa 50%?
Leo akiingia madarakani mtu ambaye si Kikwete, lakini akasema sasa tunaruhusu Wamarekani na Warusi watujengee kambi pori lililoko mpakani wa Kigoma/Rukwa na Katavi na kituo cha majini Pangani, kisiasa kuzingatia historia ya mvutano wa kiutawala, kijeshi na kura za veto UN, hatuoni kuna haja ya kuanza kuulizana maswali ya msimamo wetu kama nchi isiyofungamana? au kwa kuwa tunapenda misaada basi kila mtu ni rafiki atatusaidia na kutukopesha?
Kuhitimisha, lengo langu lilikuwa ni kuhoji utegemezi wetu kwa kila kitu hata kwa vitu ambavyo tuna uwezo navyo. Tanzania tumekwama hapa kwenye tope la utegemezi kwa ajili ya ama makusudi ya viongozi kukosa utashi kusema tujitegemee, au ni unyonge wa kutokujiamini kuwa tuna vyanzo vya mapato ya kutosha, tuna fedha za kutosha, tutaweka mipango mizuri kupunguza utegemezi, misaada na mikopo tujitosheleze.
Si suala la kusema tusiwe na Jeshi imara lenye vyombo vya kisasa kutulinda. Wala hilo si suala lililoko kwenye maudhui yangu. Bali ni kulijenga jeshi wa nyenzo na uwezo wetu wenyewe tulionao.
Si suala la UCCM, Upinzani bali ni sisi kama Taifa kujiuliza, leo rafiki yako (ashakum) akimnunulia mmkeo zawadi ya chupi, sidiria na gagulo, bado tutaendelea kufurahia huku unauwezo wa kufanya hivyo ila umekuwa na utegemezi wa kupita kiasi kuwa huoni mambo mengine hayahitaji kusaidiwa?
Maana hii tabia ya kuombaomba si Serikali pekee, imekuwa ni kidonda na ugonjwa sugu kwa Taifa. KIla mtu anaomba asaidiwe japo chai, soda, sukari kwa watoto na si kweli kuwa kila mtu hawezi kuchacharika na kujitutumua na kuwa na kipato.
Ni unyonge huu wa kupenda misaada ambao umetuletea unyonyaji na ufisadi maana hatutoki jasho na kupangia ndururu tuliyonayo itutoshe mpaka masika ijayo.
Ni swaga letu la Ponda Mali, kufa kwaja!