Kikwete si Tatizo la Tanzania!

Rev. Kishoka

JF-Expert Member
Mar 7, 2006
4,526
1,529
Naam, nimeandika mara nyingi sana kumchambua Jakaya Kikwete, lakini safari hii, naandika si kumtetea wala kumkingia kifua bali ni kudhihiri upofu wetu wa kumng'ang'ania mtu mmoja na kumsiliba matatizo yetu.

Ndiyo, Kikwete ni Rais aliyeonyesha Udhaifu wa hali ya juu. Binafsi nimeandika mengi kuhusu udhaifu wake kama Kiongozi, na matokeo yake tumeyaona! Mengi niliandika hata kabla hajaapishwa mwaka 2005, na kila nilichoandika kimetimilika.

Lakini hakuna maana kuendelea kumshambulia Kikwete kwa kila linaloendelea Tanzania!

Tatizo la Tanzania si udhaifu wa Kikwete, bali ni uozo, uzembe na udhaifu wa Chama Cha Mapinduzi!

Wala si Kikwete pekee, rudi nyuma kwa Mpaka hata mpaka kwa Mwalimu Nyerere. CCM chama ambacho kilijijenga kuwa ni chama cha Wakulima na Wafanyakazi, kimejijenga katika mfumo butu ambao umekosa uwajibikaji wa ndani na hata kuiwajibisha Serikali yake yenyewe!

Hebu tujiulize, madakatari walipogoma juzi kutokana na kulalamikia maslahi yao, CCM kama chama Tawala, kilichukua hatua gani kuipigia kelele Serikali yake au kuidhibisha Serikali yake kwa kushindwa kufanya usimamizi makini kuhakikisha maisha ya Watanzania yanalindwa?

Je CCM hii, ilikuwa wapi wakati ubadhirifu na dhuluma za Rada, EPA, Ndege, Richmond, Meremeta na miradi mingine mingi na hata mikataba mibovu ikasainiwa na kuingizwa kati ya Jamhuri ya Tanzania na Wawekezaji walioishia kutunyonya na kutunyausha na kutuacha kavukavu?

CCM kama chama, kilikuwa wapi kuihoji kwa nguvu zote Serikali na hata kuichukulia hatua Serikali au watendaji wa Serikali ambao ni sehemu ya Chama na wamepata madaraka ya Kiserikali kwa kupitia Chama Cha Mapinduzi?

Je leo hii pale Arumeru tunapoingia upofu na kumshambulia Mkapa na Kikwete kama marais wabovu, iweje tukifumbie macho CCM kama chama ambacho wote Mkapa na Kikwete waliweza kufanya maamuzi mabovu na hawakuchukuliwa nidhamu za kichama hata kuondolewa madarakani kama vile Abdu Jumbe na Seif Hamad walivyofanyiwa?

Yaelekea sana kuwa sisi kama Taifa, bado tuna imani na CCM na tunatumaini kuwa kiongozi bora na utawala bora utakuja pale pindi CCM itakapopata mgombea nafuu! Ndio maana tunahangaika mara Magufuli, sijui Mwakyembe, Asha Migiro, Mwandosya, Bilali, Tibaijuka na hata Lowassa na January Makamba kwa mbali kuwa tunaridhika nao!

Lakini tunasahau kuwa Mkapa alitufutia madeni tukashangilia lakini akatuachia mfumo wa kutokuwajibika uliojaa uroho, ulafi na uchu wa mali na ndio uliopanda mbegu nono ya Uhujumu na Ufisadi! Je tushajiuliza iweje tumekuwa na ukubuhu wa Uhujumu na Ufisadi na hata ubabe wa viongozi wa Serikali kama kina Adama Malima kuvunja sheria ya nchi au Andrew Chenge kujisemea kuwa ni vijisenti na kufanya atakalo bila kuhoji CCM?

Ni upofu na upotofu tukiamini kuwa CCM itajirudi au iko siku atatokea mgombea makini kutoka CCM.

CCM ni chama Mufilisi! Kimeoza kinanuka shombo na ndio maana hata magamba imekuwa ni vigumu kujivua wamebakia kusukumiana mipira ya lawama na kuchagua jina moja au mawili kuyabebesha lawama.

Na sisi kama Taifa, tumeingia mtego wa Panya na kuamini tukilenga nguvu zetu kudai Mkapa na Kikwete ni Maraisi wadhaifu, basi tuishie hapo, huku tunasahau kuwa kweney kata, halmashauri, wilaya na mikoa, mfumo mzima wa uongozi uko chini ya CCM na kushindwa kwa Watanzania kupiga hatua za maendeleo kujinasua kutoka umasikini ni kutokana na sisi kuamini kuwa iko siku CCM itatuletea maendeleo.

Ni heri kucheza kamari na kuchagua chama kinginecho, kiwe na mamlaka ya kiutendaji katika mtaa, kata, tarafa, wilaya, mkoa na hata Taifa. Haijali iwe ni NCCR, CUF, Chadema, TLP au DP, lakini si CCM.

CCM kimekuwa madarakani kwa miaka yote 50 ya Uhuru wetu, tangu kikiitwa TANU na pamoja na kuwa kilikuwa na viongozi shupavu na wenye kutetea Utaifa na Uzalendo wa Tanzania, lakini sehemu kubwa ya Uongozi na maamuzi ya CCM yameendelea kushikiliwa wa na wale wengi ambao wameoza!

Ndio maana utendaji wa Mkapa na Kikwete, ni safi na kwa ridhaa kubwa, wote wawili, walipewa dhamana ya kuwa wagombea wa CCM kwa miaka 10!

Jiulize tena, hasira zako kwa nini ziendelee kuwa kwa Kikwete kwa kutuletea giza tororo la kukosa umeme, migomo ya madaktari, posho za kibwanyenye za Wabunge na adha nyingine nyingi ambazo tumezielekeza kwenye Serikali Kuu, huku yenyewe inachofanya ni kutekeleza Ilani za Chama chake, Chama cha Mapinduzi!

Kidumu Chama Cha Mapinduzi!
 
Huku kunaitwa "Kumkoma nyangi giledi JF style"... so what ur saying Your Eminence ni kwamba TATIZO NI CCM? Kwa hiyo kuangalia CCM kutafuta suluhisho ni sawa na kujaribu kutafuta usafi kwenye matope?
 
Nakubaliana wewe kikwete si tatizo,tatzo ni woga wetu.Tungekuwa kama tunisia au misri huyu jamaa angekimbia mwenyewe
 
Hapa ni sawa na kukaa chini na kuchagua kwa ungalifu mkubwa mbegu nzuri zenye umbile zuri na afya miongoni mwa mbegu katika gunia la mbegu za BANGI tukiamini kwamba tukichagua mbegu bora ya BANGI tukaipanda kitaalamu na kuihudumia vizuri tatizo letu sugu la uhaba wa mchicha litakwisha.

Tuonaonekana wazi kusahau kwamba mchicha shambani hautokani na mbegu nzuri na bora za bangi.Tukitaka kumaliza tatizo la uhaba wa mchicha ni lazima tuchague mbegu bora kutoka katika gunia la mbegu bora nzuri za mchicha.

Tunasubiri kuku watoe maziwa na ng'ombe watage mayai.
 
katiba katiba katiba

hata tukiwa na katiba mpya kutokana na tabia zetu hakutakuwa na mabadiliko sana mbona kuna sheria nyingi nzuri na hazifuatwi, inabidi na sisi tubadiike tuwe watu wa kujua na kudai haki yetu panapostahili
 
katiba nzuri ni ile itakayotoa fursa nyingi za kudai haki!!!

hata
tukiwa na katiba mpya kutokana na tabia zetu hakutakuwa na mabadiliko
sana mbona kuna sheria nyingi nzuri na hazifuatwi, inabidi na sisi
tubadiike tuwe watu wa kujua na kudai haki yetu panapostahili
 
Msemayo sawa lakin tatizo kubwa ni sisi watanzania. Kwanini tunaendelea kukumbatia maozo pindi za chaguzi kuu? Au mwataka nani awachagulie kiongozi wa kutetea masilahi yenu?.Yanini kuchagua msosi uliochacha wakati kuna chakula kizuri kwa pembeni?Kukosa uelewa kwa Watanzania kutatufanya tuwe watumwa wa nchi yetu hadi lini?MWENYE BUSARA NA AFUMBUE MACHO.
 
Back
Top Bottom