Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,349
- 33,186
Rais Jakaya Kikwete (kulia) akirudisha fomu za kuwania urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi CCM kwa katibu wa CCM Yusuf Makamba katika ofisi za makao Makuu ya CCM mjini Dodoma jana.
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete, amesema uamuzi wa kumtuma mwanaye, Ridhwani, kutembeza fomu yake mikoani kutafuta wadhamini ni sahihi kwa vile suala la kugombea urais ni lake binafsi na si la chama.
Rais Kikwete alisema hayo jana alipokuwa akihutubia maelfu ya wanaCCM waliohudhuria hafla ya kurejesha fomu yake ya kukiomba chama ridhaa ya kutetea kiti hicho, baada ya zoezi la kupata wadhamini mikoani kukamilika.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Uchaguzi wa CCM, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Chama hicho, Yusufu Makamba, jumla ya wanaCCM waliomdhamini Rais Kikwete, ambaye ni mwanaCCM pekee aliyechukua na kurejesha fomu hiyo, ni 14,069 kati wadhamini 2,800 waliokuwa wakihitajika.
Hafla hiyo ilifanyika katika viwanja vya Makao Makuu ya CCM mjini hapa na kutawaliwa na mbwembwe nyingi, zikiongozwa na wasanii wa ngoma za asili, muziki wa dansi, kizazi kipya, sarakasi kwa vijana na kwaya kutoka kikundi cha uhamasishaji cha chama hicho cha Tanzania One Theatre (TOT) chini ya kiongozi wake, ambaye pia ni Mbunge wa Mbinga Mashariki, John Komba (CCM). Rais Kikwete alisema mara baada ya kuamua kumtuma Ridhiwani kutembeza fomu yake mikoani kutafuta wadhamini, yalizuka maswali mengi, moja likihoji kwa nini atumwe Ridhiwani na wengine kudiriki kutamka kwamba, kwa kumtuma mwanaye, amewadharau viongozi wa wilaya na mikoa wa chama.
Yameulizwa maswali mengi, kwa nini Ridhiwani? Na mimi nikawauliza kwa nini si Ridhiwani? Mimi kugombea urais, si jambo la chama. Ni langu miye. Linapokuwa langu miye, wa kumtuma wa kwanza si mwingine isipokuwa mwanangu na marafiki zake na wenzake, alisema na kuongeza:
Na wapo waliosema kwa kumtuma Ridhiwani, amewadharau viongozi wa wilaya. Sivyo.Viongozi wa wilaya na mikoa wajibu wao katika zoezi hili ni kuandaa wanachama wa kuwadhamini wagombea.
Zoezi la kutembeza fomu kutafuta wadhamini ni la mgombea mwenyewe. Kazi yake yeye, anaigharimia yeye, anahangaikia yeye. Yakimshinda, yamemshinda. Akiweza kwenda, Katibu Mkuu yeye ni kungojea tu. Viongozi wa wilaya na mkoa kule wanangojea kwenye ofisi za chama. Mgombea amepita, hakupita shauri yake.
Alimshukuru Ridhiwani, Kaimu Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Benno Malisa, Katibu Mkuu wa Umoja huo, Martin Shigela, pamoja na marafiki zao, kwa kazi nzuri waliyoifanya ya kutembeza fomu yake kutafuta wadhamini mikoani.
Pia alimshukuru Yusufu Makamba kwa kupokea fomu yake bila mizengwe.
Vilevile, aliwashukuru wote waliomchangia kwa hali na mali na kudhamini fomu yake na kusema hana cha kuwalipa, isipokuwa watalipwa na Mwenyezi Mungu.
Rais Kikwete alisema wanaCCM wenye sifa ya kuwa Rais ni wengi sana kwenye chama hicho, lakini hakuna hata mmoja aliyejitokeza baada ya yeye kuchukua fomu.
Alisema jambo hilo ni kielelezo cha imani kubwa waliyonayo kwake, wamempa heshima kubwa, hivyo hana budi kuwashukuru.
Pia, alimshukuru Mbunge wa Maswa, John Shibuda (CCM), kwa uamuzi wake wa kuondoa nia ya kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia CCM na kumchangia Sh. 200,000 taslimu kwa ajili ya kusaidia kampeni zake katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu. Fedha hizo alikabidhiwa na Shibuda katika hafla hiyo jana.
Matumaini yangu ni kwamba Halmashauri Kuu itapitisha na kupendekeza jina langu kwa Mkutano Mkuu na Mkutano Mkuu utaniteua na baada ya uteuzi, ni matumaini pia wananchi watanichagua tena kwa kishindo kikubwa wanipe ridhaa na fursa ya kuendelea kuwahudumia na kuwatumikia Watanzania wenzangu kwa nafasi ya Rais, alisema Rais Kikwete.
Alisema iwapo atachaguliwa tena, atafanya vizuri zaidi kuliko alivyofanya katika kipindi cha uongozi wake wa miaka mitano iliyopita, kwa vile kazi ya urais haina shule ya kusomea, bali mtu anajitokeza na wenzake wanamuamini na yeye kujiamini, wanamchagua na kuanza kazi.
Ukiwa na bahati ya kumkuta mwenzako aliyekutangulia, akakuelekeza jinsi mambo yanavyofanywa kama alivyonisaidia mzee Mkapa (Rais Mstaafu wa awamu ya tatu), unajua namna ya kuanza, alisema Rais Kikwete na kuongeza:
Lakini hata hivyo, kuna mwaka mmoja mpaka miwili ya kwanza bado unajifunza. Unajaribu hili liko hivi, unajaribu hili haliendi sawa sawa, unajaribu lile.
Hatimaye kwenye mwaka wa tatu, wa nne na wa tano ndio unakuwa umezoea, unapata kasi nzuri na mambo unaelewa vizuri, alisema.
Kutokana na hali hiyo, alisema katika miaka mitano ya kwanza ya uongozi wake, kulikuwa na miaka karibu miwili ya kujifunza, ambayo serikali yake imeweza kufanikiwa kwa kiasi kikubwa, miaka mitano ijayo, ambayo haina tena la kujifunza, ana uhakika itafanya makubwa na vizuri zaidi.
Ninachoomba wanaCCM wenzangu mkiunge mkono, mkipigie kampeni chama chetu kipate ushindi mkubwa, wananchi waendelee kuunga mkono serikali ya Chama Cha Mapinduzi tutakayoiunda iwapo tutachaguliwa. Kwa hiyo, tunakwenda kwenye uchaguzi kwa msimamo wetu uleule, mafiga matatu, alisema Rais Kikwete.
Alimshukuru mkewe, Salma, kwa ushirikiano mkubwa alioutoa kwake pamoja na wanawe na kusema: Sina sharti la Askofu (la kuoa mke mmoja tu) maana mimi ni Muislamu, (wake) wanne. Ninaye mmoja, nina nafasi tatu, lakini sikusudii kuzijaza, maana umri nao unakwenda.
Kauli hiyo ilitolewa na Rais Kikwete, baada ya Makamba, ambaye alitumia muda mwingi kunukuu vifungu mbalimbali vya Kurani Tukufu na Biblia Takatifu kueleza kuwa Rais Kikwete anazo sifa za Uaskofu zilizotajwa katika Waraka wa Paulo Mtume kwa Timotheo na kusema: Kwa hiyo, wewe Mheshimiwa Rais ni mtumishi wa Mungu. Sifa zote unazo, lakini sina hakika ile moja ya kuwa na mke mmoja kama unayo.
Awali, Makamba alisema utabiri alioutoa wakati Rais Kikwete anachukua fomu kwamba, dalili zinaonyesha kuwa atakuwa ni mgombea pekee wa urais, umethibitika jana kwa vile hadi mchakato huo unahitimishwa jana, hakuna mwanachama mwingine aliyejitokeza kuchukua fomu. Makamba alisema hali hiyo inaonyesha jinsi gani wanaCCM walivyo na imani na Rais Kikwete kwa vile ndiye mtaji mkubwa kwa chama na kwa hiyo, anaamini kuwa atakivusha chama katika uchaguzi wa Oktoba.
Tunamuomba Mungu atuchagulie Rais na huyo Rais asiwe mwingine uwe wewe kwa sababu wewe ni mzuri.
Hata Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere aliwahi kusema Rais anaweza kutoka chama chochote, lakini Rais mzuri atatoka CCM, alisema Makamba.
Hafla hiyo ilianza saa 5:10, mara baada ya Rais Kikwete akifuatana na mkewe pamoja na wanawe, kuwasili katika viwanja hivyo, huku gari lake likisindikizwa na msafara wa magari na pikipiki, zilizokuwa zikiendeshwa na watu waliovalia mavazi rasmi ya CCM.
CHANZO: NIPASHE