Stephano Mgendanyi
JF-Expert Member
- May 16, 2020
- 1,895
- 940
KIHENZILE, SILLO & NAJMA - WENYEVITI WATATU WA BUNGE WALIOCHAGULIWA
Bunge limewachagua Wenyeviti watatu wa Bunge ambao watasaidia katika kuongoza vikao vya Bunge kwa maelekezo ya Spika wa Bunge au Naibu Spika kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge.
Waliothibitishwa na Waheshimiwa Wabunge kuwa Wenyeviti wa Bunge mara baada ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uongozi kupendekeza majina yao ni pamoja na Mheshimiwa Najma Murtaza Giga ambaye ni Mbunge wa Viti Maalum na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, Mheshimiwa Daniel Baran Sillo ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti na Mheshimiwa David Mwakiposa Kihenzile, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo
Akizunguza Bungeni, Spika wa Bunge Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson amesema utaratibu wa kuwapata Wenyeviti wa Bunge umewekwa katika Kanuni ya 13 ya Kanuni za Kudumu za Bunge.
Aidha alisema kuwa katika chaguzi zinazofanyika Bungeni iwapo idadi ya wagombea inalingana na nafasi zilizopo na vigezo vinavyohitajika vimetimizwa basi wagombea hao wanapita bila kupigwa.
Aliongeza kuwa utaratibu kama huo ulitumika kwenye uchaguzi wa Wenyeviti wa Bunge katika Bunge la Kumi, Bunge la Kumi na Moja na katika Bunge hili la Kumi na Mbili ambapo; Kamati ya Uongozi ilipendekeza majina matatu na baadaye majina hayo yalithibitishwa na Waheshimiwa Wabunge.
Hivyo kwa muktadha huo, Mheshimiwa Spika aliwahoji Waheshimiwa Wabunge ili kuthibitisha Waheshimiwa hao waweze kuwa Wenyeviti wa Bunge.