Kifo siku ya harusi yangu

Kifo siku ya harusi yangu

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Joined
Apr 29, 2016
Posts
20,746
Reaction score
25,639
HADITHI: KIFO SIKU YA HARUSI YANGU
MTUNZI : ERIC J SHIGONGO



MWANZO

Mamia ya watu walikuwa wamefurika ndani ya ukumbi wa Pundamilia ulio ndani ya hoteli ya maarufu ya Atrium, karibu kila mtu maarufu nchini Tanzania alikuwa ndani ya ukumbi huu. Kuanzia Rais, Mawaziri, Makatibu Wakuu, wanamichezo, wasanii na wafanyabiashara wakubwa wa Kiasia na Afrika. Hakika ilionekana siku ya furaha, watu wakiwa wameketi kwenye meza zao wakiendelea kunywa vinywaji taratibu.

Wanaume wakiwa wamevalia suti nyeusi na wanawake magauni ya rangi nyeupe na zambarau, hakika walipendeza. Kila nilipozungusha macho yangu huku na kule ndani ya ukumbi nilionekana kutoamini kilichokuwa kinatendeka, hatimaye baada ya safari ndefu ya kupanda na kushuka milima, nilikuwa namuoa Bianca Rwegoshora, mtoto wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Wazazi na ndugu wa pande zote mbili walionekana kufurahia kila kitu kilichokuwa kikitokea ukumbini, kwao hakika ulikuwa ushindi, walikuwa wamefanikisha kutokea kwa jambo ambalo kwa muda mrefu walilihangaikia sana, kuhakikisha kwamba namuoa Bianca badala ya Farida Mbaraka, kisa tu alikuwa ni mtoto aliyetokea familia duni, wazazi wake wakiwa hawana elimu hata ya darasa la saba. Hicho ndicho kilikuwa kikwazo, hakuna aliyeuangalia uzuri wake, wala ukarimu wa moyo wake, alihukumiwa sababu ya umasikini wake, hakika iliuma.

Asilimia kubwa ya ndugu zangu waliokuwa ukumbini, macho yangu yalivyowapitia, sikumpata hata mmoja ambaye hakuwa na digrii! Wengi walikuwa ni madaktari, maprofesa, wenye elimu ya chini kabisa walikuwa ni wenye digrii moja pamoja na wanafunzi waliokuwa vyuoni na sekondari ambao pia walitegemea kuingia kaburini wakiwa na digrii si chini ya tatu.

Hiyo ndiyo ilikuwa familia yangu, familia ya wasomi, walioheshimu watu kwa alama zilizotangulia majina yao, mfano Dk., Injinia, Mchumi, Mwanasheria, n.k. Mtu yeyote ambaye hakuwa na vitangulizi vya taaluma yake, hakuheshimiwa na familia yangu. Hicho ndicho kilichompata Farida Mbaraka, kwa sababu ya familia yake kutokuwa na elimu, alionekana kama kinyaa, ingawa nilimpenda mno, baadhi ya ndugu zangu waliomo ukumbini wakishangilia, walimkashfu na kusema kwamba kumuoa ingekuwa ni kutumia sheria iitwayo “The Dilution Law”.

“Mtoto huchukua akili kutoka kwa baba na mama, ukiwa na akili nyingi, halafu ukaoa mwanamke au kuolewa na mwanaume asiyekuwa na akili, mtoto wako atakuwa na akili kidogo, lakini ukioa mwanamke au kuolewa na mwanaume mwenye akili nyingi, lazima watoto wako watakuwa vipanga sana darasani!” Hayo yalikuwa ni maneno ya Joackim, mtoto wa baba yangu mkubwa ambaye yeye katika umri wa miaka thelathini tu alikuwa anasomea digrii ya tatu nchini Marekani. Alikuwepo ukumbini akishangilia juhudi zake za kuhakikisha simuoi Farida bali Bianca, ambaye karibu familia yake yote ilikuwa ni ya wanasheria.

“Genesis!” Ilikuwa ni sauti ya Bianca akiniita, nikageuza kichwa changu kumwangalia, ili kumfanya asigundue kwamba nilikuwa na mawazo, niliusogeza mdomo wangu karibu na wake na kumbusu, wapiga picha wakafanya kazi yao.

“Yes sweetie!” (Ndio mpenzi)
“What is going on your mind?”( Nini kinaendelea kichwani mwako?)
“Why?”(Kwanini?)

“You seem to be contemplating too hard!”(Unaonekana kufikiria sana)
“No! I am just thinking about our future, where we have come from, where we are and where we are going!”(Hapana! Nafikiria tu kuhusu maisha yetu ya baadaye, tulikotoka, tulipo na tunakokwenda!)

“Isn’t Farida on your mind?”(Farida hayupo kichwani mwako?)
“Me? No way! That drug dealer? Probably she is dead by now.”(Mimi? Huyo muuza madawa ya kulevya? Labda amekwishakufa tayari) niliongea nikichukua kitambaa na kujifuta machoni.

Si kweli kwamba nilikuwa simpendi Farida, kila jina lake lilipotajwa huzuni iliniingia na machozi kunilengalenga, nilimpenda sana msichana huyo na katika maisha yangu sikuwahi hata mara moja kukutana na msichana wa aina yake. Alikuwa na sifa zote, kuanzia uzuri wa sura na maumbile mpaka tabia na mwenendo wake na hicho ndicho nilichohitaji kutoka kwa mwanamke wa kuishi naye maisha, sifa ambazo wazazi na ndugu zangu katu hawakuziona, kwao kitu cha muhimu kilikuwa ni elimu.

“Then why are you so sad? Are you not happy that we are finally married?”(Sasa kwanini una huzuni siku ya harusi yetu? Haufurahii kwamba hatimaye tumeoana?)

“I am so happy and excited, though I can’t stop myself thinking of Farida.”(Nina furaha sana ingawa siwezi kujizuia kumfikiria Farida)
“But a few minutes ago you said she is not on your mind!”(Lakini dakika zilizopita ulisema hayupo akilini mwako)
“Let me just be brutally honest with you! I can’t stop thinking of Farida.”(Acha tu niwe muaminifu kupita kiasi, siwezi kuacha kumfikiria Farida) niliongea nikimwangalia Bianca, akainamisha kichwa chake chini kuonyesha maelezo yangu yalimwumiza, lakini ilikuwa ni bora aumie akiwa ameambiwa ukweli.

Haikuwa rahisi kumsahau Farida, kila siku alisumbua akili na mawazo yangu, mpaka wakati huo nilikuwa sijaamini kabisa kwamba alikuwa ni mfanyabiashara wa dawa za kulevya, aliyekamatwa na madawa hayo nchini Saudia Arabia siku chache tu kabla ya kumvisha pete ya uchumba na kilichokuwa kikisubiriwa ni kupigwa risasi mbele za kadamnasi, hiyo ndiyo ilikuwa adhabu ya watu waliokamatwa na madawa hayo katika nchi za Uarabuni.

“Lakini aliondoka kwa lengo la kwenda kufanya usaili ili ajiunge na Chuo Kikuu cha Riyadh, naye akitamani awe angalau na digrii na familia yangu iweze kumkubali. Alifanya kila kilichowezekana ili wazazi wangu wampende. Hivi ni kweli Farida alikuwa akifanya biashara ya madawa?” nilijiuliza bila kupata majibu.

Ingawa Bianca alikuwa kando yangu, tena siku ya harusi yetu bado kichwani mwangu alikuwemo Farida, fikra za kwamba angekuwa amekwishapigwa risasi mpaka wakati huo zilinisumbua sana kiasi cha kunifanya nisifurahie kitu chochote kilichokuwa kikiendelea ukumbini ingawa karibu kila mtu alishangilia mimi na Bianca kufunga ndoa. Nilichotaka kufanya wakati huo ni kuondoka ukumbini kwenda chumbani kupumzika.

Ghafla nilisikia mlio wa ujumbe wa simu kwenye simu yangu, nikijua ni kutoka kwa baadhi ya rafiki zangu waliokuwa wakinitumia ujumbe wa pongezi. Nilinyoosha mkono na kuichukua simu yangu mezani, kisha kufungua sehemu ya ujumbe na kuanza kusoma, moyo wangu ulishtuka nilipoona maneno “Siri kubwa”. Nikazidi kusogea chini ambako kulikuwa na anuani ya barua pepe ya Bianca, pia ikiwa na alama yake ya siri ya kufungulia kama kuna mtu alitaka kusoma. Chini yake kukiwa na maandishi “Tumekuletea hii, ili uingie kwenye sanduku la barua pepe la mkeo, ili upate kumwelewa vizuri na unyama aliomfanyia Farida.”

Moyo wangu ukaruka mapigo kadhaa, jasho likaanza kunitoka, huku nikihisi kama vile shinikizo langu la damu lilikuwa likishuka kwa kasi. Sikutaka tena kukaa ukumbini, ujumbe huo wa simu ndio ulichochea kabisa hamu yangu ya kuondoka kwenda chumbani kupumzika ambako lengo langu lilikuwa ni kwenda moja kwa moja kwenye kompyuta na kufungua anuani ya barua pepe ya Bianca na kujionea kilichokuwemo ndani. Moyoni nilijawa na hofu, nikiogopa ambacho ningekikuta lakini bado nilitamani kujua.

“Sijisikii vizuri!” nilimgeukia Bianca na kumweleza.
“Nini tena?”
“Nataka kwenda kupumzika, ni vizuri tukaondoka.”

“Genesis, tuondoke mapema kiasi hiki? Kabla wazazi hawajaondoka?”
“Naumwa!” nilitoa kisingizio huku nikigeuza kichwa kuongea na Kelvin, mpambe wangu wa siku hiyo. Mimi na Kelvin tulisoma pamoja Chuo Kikuu cha St. Augustine kilichopo mjini Mwanza, alikuwa rafiki yangu mkubwa na tulishirikiana mambo mengi.

“Vipi tena?” aliniuliza.
“Aisee mwambie MC atangaze kuwa tunaondoka kwenda chumbani kupumzika.”
“Eti shemeji?” Kelvin alimuuliza Bianca.

“Kama yeye ameamua mimi sina kizuizi”
Bila kipingamizi Kelvin alifanya kama alivyoombwa, MC akatangaza juu ya kuondoka kwetu na watu wote wakasimama huku wakishangilia, tukitembea kwa madaha tukiwa tumeshikana mikono kuelekea nje ya ukumbi ambako tuliingia kwenye lifti na kwenda moja kwa moja ghorofa ya tatu, kilipokuwa chumba chetu, Kelvin na mke wake Martina walikuwa pamoja na sisi mpaka ndani ambako bila kuchelewa walituaga na kuondoka.

Kitu cha kwanza nilichofanya ni kwenda kwenye kompyuta yenye mtandao wa Internet, haraka nikaiwasha na kuingia kwenye tovuti ya G-mail nikaandika Bianca10@Gmail.com, kisha kwenye alama ya siri nikaandika neno Hadohado, hiyo ndiyo ilikuwa alama ya siri ya Bianca. Niliyafanya yote hayo akiwa amejilaza kitandani, bila kunisogelea. Nikabonyeza sehemu iliyoandikwa Sign in, muda mfupi tu baadaye sanduku lake la barua pepe likafunguka, iliyokuwa juu kabisa iliandikwa “The truth about innocent Farida Mbaraka”

Maneno yaliyomaanisha ukweli kuhusu Farida Mbaraka asiye na hatia. Moyo wangu ukapiga kwa kasi, jasho likinitoka huku nikisubiri ifunguke, sekunde chache baadaye kila kitu kilikuwa wazi nikaanza kusoma huku nikibubujikwa na machozi, mara kadhaa niligeuza shingo yangu kumwangalia Bianca aliyekuwa amejilaza kitandani, hasira ikazidi kunipanda zaidi na zaidi, nilimwonea Farida huruma kiasi cha kutamani kuua, hakustahili unyama aliotendewa kwa sababu yangu. Sikumchukia Bianca peke yake bali pia familia yangu.

Hatimaye nikafikia uamuzi wa kufanya nilichoona kinafaa, kama Farida alikuwa ameshapigwa risasi sababu ya madawa ya kulevya ambayo hakuyamiliki, basi waliofanya mpango huo nao hawakustahili kuishi hata kama walikuwa ni ndugu zangu na wa kwanza kufa alitakiwa kuwa Bianca! Nikanyanyuka nilipokuwa nimeketi na kutembea mpaka kwenye meza iliyokuwa pembeni, juu yake kulikuwa na sinia lenye chakula, pia vikiwepo visu na uma.

“Hiki kinatosha!” niliwaza wakati nakichukua kisu na kuanza kutembea taratibu kuelekea kitandani alipolala Bianca akiwa hajui kilichoendelea, nikahesabu moja mpaka tatu kisha kushusha mkono kwa kasi kifuani kwake upande wa moyo, damu nyingi ikaruka na kulowanisha nguo zangu, nikakichomoa tena na kukizamisha mara ya pili kisha kuchukua mto na kumgandamiza nao Bianca mdomoni ili kelele zake zisitoke nje, dakika tano baadaye alitulia, tayari alishakufa.

“Mungu wangu nimefanya nini? Kwanini nimeua? Si ningemwacha tu na kutafuta mwanamke mwingine?” niliwaza nikimwangalia, ilikuwa kama vile niliachiwa na shetani aliyekuwa amenifunika na kuuona ukweli wa ubaya nilioutenda.
Lakini kwanini nimeua siku ya harusi yangu? Nimesoma nini kwenye barua pepe hii?
 
SEHEMU YA 02


Ilionekana kuwa siku ya furaha kubwa, Genesis mtoto wa tajiri alikuwa akimuoa binti mrembo aitwaye Bianca, mtoto wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Watu wote maarufu walikuwa ndani ya ukumbi kushuhudia tukio hilo la kihistoria bila kufahamu kuwa lingeishia kwenye mauaji, Genesis akiwa amemuua kwa kumchoma kisu Bianca wakiwa chumbani, kisha yeye mwenyewe kujirusha kupitia dirishani ili aanguke chini na kufa. Kwanini aliamua kufanya mauaji hayo ya kikatili? Je, alipojirusha dirishani alikufa?

Genesis anasimulia historia ya maisha yake, jinsi alivyozaliwa kwenye familia ya wasomi ambao hata siku moja hawakukubaliana na suala la mtoto wao kuoa au kuolewa na mtu asiyekuwa msomi. Akiwa kidato cha pili katika shule ya kimataifa ya Mtakatifu Thomas mkoani Morogoro, msichana mrembo aitwaye Farida anahamia katika shule hiyo kutoka shule ya Sekondari ya Kilakala.

Kihistoria msichana huyu anatoka familia maskini sana, wazazi wake hawakupata elimu hata kidogo. Pamoja na hayo, Farida alikuwa na akili nyingi kupita kiasi, zilizomfanya ashike namba moja kwenye mtihani wa taifa Tanzania nzima. Tukio hili ndiyo lilimfanya Padri Bathromayo wa Shirika la Kitume la Women Oppotunity Expanded, aamue kumhamisha Farida kutoka Kilakala kwenda shule ya Sekondari ya Mtakatifu Thomas, gharama zote za masomo yake zikichukuliwa na shirika hilo.

Baada ya kutambulishwa darasani, Farida akatokea kuwa rafiki mkubwa wa Genesis pamoja na kijana mwingine aitwaye Chris. Katika mazungumzo yao, Farida ambaye ameitingisha shule hiyo kwa uzuri wake, wavulana wakiwa wamepania kumpata, aligundua Genesis ni mtoto kutoka familia tofauti sana na yake kiuchumi lakini hakuwa na majivuno na alikuwa muungwana.
Je, nini kitaendelea? SONGA NAYO.

Huo ndio ulikuwa mwanzo, sumaku ya mapenzi ilionekana kuwavuta karibu kadri siku zilivyozidi kusonga ingawa wote wawili walipambana nayo. Mpaka umri huo wote walikuwa bikira, kama hivi ndivyo hata wanaume wanaweza kuitwa kama hawajakutana na mwanamke kimwili! Genesis tangu kuzaliwa kwake alikuwa bado hajamjua mwanamke, kwani aliamini kufanya hivyo ilikuwa ni dhambi kubwa ambayo mtu alistahili kuchomwa moto siku ya mwisho, hivyo ndivyo alivyofundishwa na wazazi wake na pia kanisani siku za Jumapili.

Ilikuwa hivyo pia kwa Farida, mtoto wa kiislamu aliyelelewa kwa maadili mema kila siku akiambiwa bikra yake ilikuwa zawadi kwa mume ambaye angemuoa na aliahidi kuitunza zawadi hiyo mpaka siku ya harusi. Alijitahidi kadri ya uwezo wake kupambana na vishawishi vyote vya wanaume aliokutana nao na kumtamani, kuanzia walimu mpaka wanafunzi wenzake.

Sasa amekutana na Genesis ambaye kama ilivyotokea kwa kila msichana aliyemuona, Farida anajikuta moyoni akitamka neno “Whaoo!” kwa mshangao alioupata kutokana na mvuto wa Genesis, hana uhakika kama kweli ataweza kuyatunza maneno ya mama yake, miguu iliishiwa nguvu.

Kwa Genesis pia ulikuwa ni mtafaruku kichwani mwake, hakukumbuka kama aliwahi kukutana na msichana mrembo kama Farida! Hakujali tena maneno ya wazazi wake ya kuangalia alikuwa na uhusiano na msichana kutoka familia gani, cha muhimu kwake ulikuwa ni uzuri na tabia ya msichana. Farida alimbadilisha kabisa, alikuwa na kila kitu ambacho mwanaume alikihitaji kutoka kwa mwanamke, kwamba familia yake ilikuwa maskini ya watu wasioelimika, halikuwa jambo muhimu kwake.

“Haijalishi, cha muhimu kwangu ni uzuri na tabia ya mtu, digrii hazinisaidii kitu, labda akatae mwenyewe, akikubali sitamuacha!” Aliwaza Genesis, ilikuwa ni ghafla mno kufikiria yote hayo kwa sababu ndiyo kwanza walikuwa wamekutana, lakini alijikuta tu akiwaza na kufikia maamuzi hayo.

Mioyo yao iliteseka mno lakini hakuwepo mtu jasiri wa kufungua mdomo kumweleza mwenzake hisia alizokuwa nazo moyoni mwake, waliishia kuahidiana tu “kesho nitamwambia” lakini haikuwa hivyo, Genesis hakuwa na uzoefu hata kidogo wa kutongoza, alichokifanya ni kuhakikisha maisha ya Farida shuleni yanakwenda vizuri, akishirikiana naye kwa kila kitu na hata kumpatia fedha za matumizi, kwa mwamvuli wa urafiki.

Farida alielewa vizuri kilichoendelea moyoni mwa rafiki yake, kwani hicho ndicho pia kilichomsumbua yeye, lakini akiwa mwanamke asingeweza kuanza kumweleza mwanaume hisia zake za kimapenzi, haukuwa utamaduni wa Kiafrika. Akabaki kimya akisubiri siku ambayo Genesis angefungua mdomo na kumweleza, hiyo ndiyo ingekuwa siku ya furaha zaidi maishani mwake.

Haikuwa hivyo, Genesis aliendelea kubaki kimya, yeye pia akitarajia Farida ndiye aanze kama ambavyo wasichana wengine waliwahi kumwita na kumweleza wazi walivyompenda, jambo ambalo kwa Farida lilikuwa haliwezekani, siku zikazidi kusonga hatimaye mwisho wa mwaka ukafika, shule zikafungwa na wote wakarejea jijini Dar es Salaam. Urafiki wao uliendelea, Genesis akimtembelea Farida nyumbani kwao kila mara na wazazi wake kumfurahia.

“Jumatatu nitakuja nikuchukue twende nyumbani, ukawaone wazazi wangu!”
“Sawa! Watafurahi kuniona?”
“Mhhhh! Watafurahi”

“Mbona umeitikia kwa shingo upande? Unanitisha”
“Wala usitishike, Jumatatu nitakuja asubuhi nikuchukue tupite kwanza Kariakoo!”
“Sawa!”

Farida alibaki mwenye kusubiri kwa siku kadhaa mpaka siku hiyo ya Jumatatu ikafika, Genesis akafika akiwa na gari iliyoendeshwa na dereva wao mwanaume wa makamo. Baada ya kuwasalimia wazazi wa Farida, waliaga na kuondoka hadi Kariakoo mtaa wa Kongo, ambako katika hali ambayo hakuitarajia, Farida aliingizwa kwenye duka la nguo na kununuliwa nguo mpya pamoja na viatu. Zoezi hilo lililopokamilika ndipo waliondoka kwenda moja kwa moja hadi nyumbani kwao Genesis, maeneo ya Masaki karibu na hoteli ya GoldenTulip.

Ilikuwa saa tano kamili walipofika, hawakumkuta mtu zaidi ya wafanyakazi, baba na mama tayari walishaondoka kwenda kazini. Farida hakuamini rafiki yake alitoka kwenye familia tajiri kiasi hicho, maishani mwake hakuwahi hata mara moja kuingia ndani ya nyumba iliyopambwa kiasi kile. Alipolinganisha na nyumbani kwao, ilikuwa ni sawa na usiku na mchana.

“Hongera sana Genesis!”
“Kwanini?”
“Umebarikiwa!”
“Kwanini unasema hivyo?”

“Kupata wazazi wa aina yako ni bahati!”
“Hata wewe pia umebarikiwa, hivi vitu ni vya kupita, cha muhimu ni upendo wa wazazi ambao wako tayari kufanya kila kitu kuhakikisha unafanikiwa maishani mwako, wazazi wako si wanakupenda?”

“Sana!”
“Basi hiyo inatosha, hata kama mnalala na njaa!”
“Ahsante sana!”

Walizungumza mengi wakiwa peke yao mpaka saa saba na nusu, miungurumo ya magari ikasikika nje ya nyumba, Genesis akanyanyuka kwenda kuchungulia dirishani na sauti yake ikasikika akisema “Dad and Mom are back!” Akimaanisha baba na mama wamerudi. Moyo wa Farida ukaingiwa na hofu na kuanza kupiga kwa kasi, akiuliza kama kulikuwa na mlango wa nyuma ili apate kutoka nje kisha kuondoka.

“Kwanini?”
“Naogopa!”
“Nini?”

“Wazazi wako!”
“Kwa sababu gani?”
“ Wanaweza wasinipende!”

“Wewe unataka kupendwa na wazazi wangu au mimi?”
“Wewe!”
“Tulia basi!”

Farida akarejea kwenye kiti na kutulia, haukupita muda mrefu sana kengele ikalia na Genesis akaenda kufungua mlango, wazazi wake wote wawili wakaingia wakiongozana na watu wengine wawili walioonekana kuwa mke na mume. Genesis na Farida wakawasalimia kisha wote wakaketi chini na maongezi kuendelea, wazazi wa Genesis wakionekana kama vile hawakumkuta mgeni mwingine sebuleni, hawakujali kabisa uwepo wa Farida.

“Baba!”
“Naam!”
“Huyu hapa ni rafiki yangu, anaitwa Farida!”
“Aaaaah! Karibu sana, anaishi wapi?”

“Mikocheni!”
“Hapana siyo Mikocheni, Mtoni kwa Aziz All…!”Farida alishindwa kumalizia sentensi yake baada ya kumuona Genesis akimkonyeza, alishachelewa.

“Mtoni kwa Aziz Ally?” Baba yake Genesis aliuliza kwa mshangao.
“Ndiyo!” Farida akaitikia, Genesis akiwa kimya.
“Wazazi wako wanafanya kazi gani?”

“Baba ni fundi selemara na mama ni mama lishe!” Aliongea Farida kwa kujiamini, kwake hapakuwa na tatizo lolote kwa sababu ni kazi ya wazazi wake na hakuona aibu, kwani kwake kazi ilikuwa ni heshima hata kama ni ndogo kiasi gani, hivyo ndivyo baba na mama yake walivyomwambia kila siku lililopokuja suala la kufanya kazi.

“Genesis!” Baba yake aliita.
“Naam baba!”
“Hebu nendeni mkaongelee huko nyuma!”
“Kwanini baba?”

“Huyu ni Dk Rwegoshora, rafiki yangu wa siku nyingi, yuko na mke wake, kwa muda mrefu sana wameishi Uswisi lakini wamerejea nchini wiki iliyopita, ameteuliwa kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, huyu ni binti yao anaitwa Bianca! Tupeni nafasi tuzungumze kidogo”

“Sawa baba!” Genesis aliitikia akimnyanyua Farida kitini ili watoke nje, alishaelewa kila kitu kilichotokea, kusikia neno Mtoni kwa Aziz Ally kulimkera baba yake. Laiti kama Farida angeacha tu neno Mikocheni libaki, hakika wasingetolewa nje. Kwa unyonge wakatembea wakiufuata mlango, kisha kufungua na kutoka hadi kwenye nyumba nyingine iliyokuwa kando, wakaingia ndani ambako Farida alianza kulia, bila hata kuelezwa tayari alishajua kilichotokea.

“Nilikuambia niondoke ukakataa, unaona sasa yaliyotokea?” Alisema maneno hayo, Genesis akimkumbatia.
“Nisamehe!”
Je, nini kitafuata?
 
SEHEMU YA 03


Kwa usoni, Genesis Greyson Mshana, bwana harusi ambaye alikuwa anamuoa mtoto wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali aitwaye Bianca, alionekana mwenye furaha sana, lakini ndani yake alikuwa na mawazo mengi sana. Pamoja na kwamba alikuwa ndani ya suti na Bianca akimeremeta na shela, bado akili yake ilikuwa juu ya mpenzi wake Farida.

Lakini akiwa katika mawazo ya machozi, ambayo tayari alishamweleza ukweli mkewe kuwa alikuwa anamuwaza sana Farida, simu yake ikaingiza ujumbe mfupi wa anuwani pepe na neno la siri ili akafungue, ambapo atakutana na siri nzito.

Akamuomba mpambe wake Kelvin amwambie MC atangaze kwamba wanataka kwenda kupumzika, hilo likafanyika na wakatoka ukumbini. Kelvin na Martina wakawaacha chumbani, hapo ndipo alipoona kitu cha ajabu sana kwenye anuwani pepe ile.

Uamuzi wake ulikuwa mmoja tu; kumuua Bianca kisha yeye mwenyewe kujiua. Hilo lilifanyika, akamchoma kisu Bianca na kuhakikisha kuwa kweli alikufa, kisha naye kupanda dirishani na kujirusha hadi chini, ili apasuke vipande vipande na kufariki!

Kwanini aliamua kufanya mauaji hayo ya kikatili? Je, alipojirusha dirishani alikufa?
Upande wa pili, Genesis anasimulia historia ya maisha yake, jinsi alivyokutana na Farida shuleni. Farida anatoka katika familia ya kimasikini sana, lakini ukaribu wao unaibua hisia nzito ambazo hakuna mmoja aliyekuwa tayari kufungua mdomo na kusema kinachoendelea moyoni mwake.

Wakati wa likizo, Genesis alikuwa anakwenda kumtembelea Farida nyumbani kwao mara kwa mara, lakini siku Farida aliyokwenda nyumbani kwao na kujitambulisha kuwa anatoka Mtoni Kwa Aziz Ally, tena kwenye familia ya baba Fundi Seremala na mama Mama Ntilie, baba yake na Genesis akawaambia watoke nje, kwa kuwa walikuwa na mazungumzo muhimu na Bwana na Bibi Rwegoshora!

Hiyo ilikuwa ishara ya kukataliwa! Genesis na Farida wakatoka kwa unyonge, huku Farida akilia kwa uchungu.
Je, nini kitatokea? SONGA NAYO...

HUZUNI ilikuwa ndani ya mioyo yao wote, Genesis alijua wazi kilichotokea. Ni kweli kwamba wazazi wake hawakuwa tayari kuona anakuwa na uhusiano na mtoto anayetoka kwenye familia ya kimasikini kama Farida! Aliwajua vizuri sana wazazi wake, siku zote walipenda kuwaheshimu na kuwathamini zaidi watu wenye majina yenye heshima!

Neno ‘Mama Lishe’ na Fundi Seremala’ yalitosha kabisa kumkosesha sifa Farida za kuingia katika nyumba ile ya thamani, iliyokuwa pembeni kabisa mwa Hoteli kubwa ya kifahari Golden Tulip.

Moyo wa Farida ulisononeka sana, alikuwa katika mateso makubwa ambayo ni kama aliyatarajia awali. Alitembea kwa huzuni huku Genesis akiwa nyuma yake, akizidi kumuonea huruma rafiki yake.

“Sio sababu lakini, siwezi kuishi bila Farida wangu!” Akawaza kichwani.
“Nampenda sasa nifanyeje?” Akazidi kuwaza.
Wakatoka hadi nje na kwenda kukaa kwenye viti vilivyokuwa kwenye bustani nzuri ya kupendeza. Uso wa Farida ulikuwa umechafuliwa kwa machozi.

“I need to go back home!” (Nataka kurudi nyumbani!) Farida alisema akitetemeka kwa woga.
“No! Farida...no...” (Hapana Farida...hapana...) Akajibu Genesis bila kuwa na maneno mengine ya kuendeleza mbele.

“I don’t have a reason to be here Genesis, remember your family is so reach and my family is poor, can you imagine that different?” (Sina sababu ya kuendelea kukaa hapa, kumbuka familia yako ni tajiri na sisi ni masikini, unaweza kuona hiyo tofauti?)

“It is not the reason, let me ask you a question!” (Siyo sababu, hebu nikuulize swali).
“Go on!” (Uliza!)
“Do you know what is inside my heart?” (Hivi unajua kilicho ndani ya moyo wangu).
“About what?” (Kuhusu?)

“Our relation!” (Uhusiano wetu)
“Yes, I know!” (Ndiyo, najua)
“You know what?” (Unajua nini?)
“We are friends!” (Sisi ni marafiki!)

“Only that?” (Hivyo tu!)
“Genesis mbona unanishangaza, kwani kuna nini kingine?” Farida akasema akiwa amemkazia macho, tena sasa akaamua kuzungumza kwa Kiswahili.

Walikuwa wanafunzi wa kidato cha pili, lakini tayari walikuwa na uwezo mzuri wa kuzungumza Kiingereza. Kwa viwango vya shule walizosoma, ilikuwa ni sahihi kabisa.

Farida alikuwa akijaribu kuuliza swali ambalo alikuwa na jibu lake kichwani, alijua ni kwa nini Genesis alimwuliza swali lile, jibu alikuwa nalo ndani ya moyo wake, kwamba wanapendana, lakini hakutaka kabisa kuonesha kwamba anajua jambo hilo.

Mila na desturi za Kiafrika zilimwongoza vizuri sana Farida, hakutaka kuonekana kama mwanamke ambaye kwao hakufunzwa vizuri.
“Farida, please, forgive me!” (Farida tafadhali naomba unisamehe) Baadaye Genesis akasema kwa sauti ya upole sana.

“For what?” (Kwanini?)
“For what happened, but I have a good message for you today!” (Kwa yaliyotokea, lakini nina ujumbe wako mzuri sana leo!)
“Just tell me!” (Niambie!)
“Farida, I love you!” (Nakupenda Farida!)

“Najua lakini tatizo ni kwamba familia yako hanikubali.”
“Usiseme hivyo tafadhali, unauumiza moyo wangu Farida, najua unafahamu kwamba nimetunza hili penzi kwa muda mrefu sana moyoni mwangu, leo ilikuwa siku ya kukuambia habari hizi, nataka kukuhakikishia kwamba, nakupenda sana na nitahakikisha nafanya kitu chochote kile ili niweze kuwa na wewe.

“Achana na wazazi wangu, hata wao hawakuchaguliwa wake wa kuwaoa, walikutana wenyewe na kuchaguana wenyewe, kwa hiyo hata sisi tunahaki zetu. Kama wana itikadi zao, hizo hazituhusu, tunatakiwa kuangalia mapenzi yetu,” Genesis alisema kwa utulivu akionekana kumaanisha kabisa alichokisema.

Tayari moyo wake ulikuwa umetapika nyongo ya mapenzi mazito aliyokuwa nayo dhidi ya Farida. Katika maisha yake yote hakuwahi kupenda kama alivyompenda msichana huyu ambaye mvuto wake haukuwa na mfano.

“Nimeshakuambia Genesis, naamini hata wewe unatambua kwamba nakupenda, lakini hapa tatizo ni wazazi. Hebu fikiria, kuniona tu, bila hata kujua kama tuna uhusiano au lah wamenichukia na kutuambia tutoke nje, vipi siku wakijua kwamba tuna uhusiano, si itakuwa balaa?”

“Hapana...nashukuru kwanza kwa kuniambia unanipenda, hilo ni jambo nililotarajia kutoka kwako. Kwa sasa tuishie kuwa tunapendana, hayo mambo mengine yatafuata baadaye.”
“Tutaona!”
“Jiamini mpenzi wangu!”

“Najiamini lakini tatizo...” Farida alitaka kuzungumza kitu lakini Genesis alishajua jambo alilotaka kuzungumza kwa hiyo akamkatisha mara moja.
“Sahau kuhusu wazazi wangu Farida, tuangalie mapenzi yetu!”
“Sawa, lakini naomba uniruhusu jambo moja.”

“Ni nini?”
“Naomba niondoke.”
“Subiri kidogo nakuja,” alisema Genesis na kuondoka bustanini.

Ilikuwa safari ya kumfuata dereva wao, baada ya kumuagiza awashe gari, alirudi haraka bustanini na kumuambia Farida asimame kwani muda wa kuondoka ulikuwa umefika. Wakaongozana moja kwa moja hadi kwenye gari, walipolifikia Genesis akafungua mlango wa nyuma.

“Hapana Genesis, nitatumia daladala usijali. Nitapanda hapa mpaka Posta, halafu huko nitachukua gari la Mbagala nitashuka nyumbani!”
“Hapana, twende na gari la nyumbani.”
“Hapana Genesis!”

“Kwanini? Kwanza ukumbuke kwamba ni gari hilihili ndilo lililokufuata nyumbani na kukuleta hapa, isitoshe, wewe ni mgeni wangu, natakiwa kuhakikisha umerudi nyumbani salama!”
“Hata daladala nitafika!”
“Sawa, lakini ujue kuwa sijafurahi!” Sauti ya Genesis ilisikika kavu, akiongea kwa upole kuliko kawaida.

Hiyo ilitosha kabisa kumfanya Farida agundue kwamba mpenzi wake alikuwa amekasirika. Ni jambo ambalo siku zote hakutaka kabisa litokee. Kwake ilikuwa bora Genesis akasirishwe na mtu mwingine, yeye awe mfariji wake. Akaingia kwenye gari.

“Ahsante sana!”
“Usijali mpenzi!”
Safari ikaanza. Tofauti na matarajio ya Farida, safari yao ilianzia Kariakoo, ambapo kwa mara nyingine tena Genesis alimwingiza madukani na kumchagulia nguo na viatu.

Farida akafurahi sana, baada ya hapo wakapanda kwenye gari na kwenda zao Mtoni Kwa Azizi Ally.
“Nashukuru sana Genesis, ahsante kwa kunijali na kunipa moyo!”

“Usijali mpenzi, ni jukumu langu kabisa kukufanya mwenye furaha, nawajua wazazi wangu, nitakuambia kitu cha wakati mwingine ili wakukubali!”
“Nitafurahi sana, maana najaribu kuyatafakari maisha bila wewe, nashindwa kabisa kuelewa yatakavyokuwa!”

“Bila shaka, hakuna kinachoshindikana mbele za Mungu, yeye anayejua vilivyomo mioyoni mwetu atatenda!”
“Amina.”
Wakaagana, Farida akaingia ndani kwao, Genesis akarudi kwenye gari. Dereva akawasha na kuondoka zao.
****
Muda wote walikuwa wakizungumza huku wakicheka, Dk. Rwegoshora alikuwa amepotezana kwa muda mrefu sana na Profesa Mshana. Furaha ikatawala katika sebule ile ya kisasa inayovutia.
“Hongera sana!” Dk. Rwegoshora hatimaye akasema.

“Ya nini?”
“Umejitahidi sana mzee mwenzangu. Unajua lazima uishi kwenye mazingira yanayofanana na hadhi yako! Kuna wenzetu wengine hawajui hilo, wanakuwa wagumu wa kufaidi maisha ipasavyo wakisahau hadhi zao! Hapa ni sehemu sahihi zaidi ya kuishi mtu kama wewe!”
“Ahsante sana Dokta, halafu tunaweza kuzungumza pembeni kidogo?” Profesa Mshana akasema.

“Bila shaka!”
“Jamani samahanini, nipo na mzee mwenzangu kule meeting room, tutarudi baadaye, lakini mama Genesis tafadhali mwambie msichana atuletee maji ya matunda!” Profesa Mshana alimwambia mkewe.

“Sawa darling!”
Muda huo huo wakasimama pamoja na kuanza kuongozana kwenda kwenye chumba cha mkutano. Macho yao yakapokelewa na chumba kizuri kilichopangwa masofa mazuri, chini kukiwa na zulia lenye manyoya laini kabisa. Wakaketi kwenye viti wakiendelea kuzungumza...

“Sasa umeshajipanga kuhusu shule atakayoendelea nayo mwanao?” Profesa Mshana akamwambia Dk. Rwegoshora.
“Hapana, vipi kuna shule nzuri unataka kunionesha nini?”
“Ndiyo, kama unavyojua mimi elimu kwanza, ndiyo msingi wa maisha ya wanangu. Kwanini usimpeleke St. Thomas?”

“Ipo wapi?”
“Morogoro, anasoma Genesis huko. Ni shule nzuri yenye maadili ya kidini, mtoto atakuwa kiakili na kiroho pia, patamfaa sana pale!”
“Kweli eh?!”

“Nakwambia ukweli, maendeleo ya mwanangu yananishawishi kwa kiasi kikubwa sana kukushauri na wewe umpeleke mwanao huko!”
“Sawa, naomba nilichukue hili wazo kama lilivyo, halafu nitazungumza na mama yake!”
“Hapana mzee mwenzangu, unadhani ni kwanini niliomba kuzungumza na wewe pembeni? Ni kwa sababu nilitaka tumalize hili jambo kama wanaume.”

“Ok! Nimekuelewa ndugu yangu, ushauri wako ni mzuri na wa maana sana, nitaufanyia kazi!”
“Tena kwa mafanikio makubwa!”
Wote wakacheka, muda mfupi baadaye wakasimama na kurejea sebuleni.

Ndani ya moyo wa Profesa Mshana kulikuwa na kitu kingine zaidi, alitamani sana kuunganisha familia yake na ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali! Alipenda sana watu wenye heshima kubwa!

Kikubwa alichowaza ni Genesis siku moja amuoe Bianca! Kuwasogeza shule ulikuwa mpango wa kwanza, ambao kwake yeye aliamini kuwa ungeweza kuwasogeza vijana hao na kuwa kitu kimoja. Wakiwa wanaingia sebuleni, Genesis akatokea mlangoni akiingia ndani, uso wake ukiwa umejaa makunyanzi!
Hasira yake ilisomeka wazi kabisa!
****
“Hizi nguo mpya umepata wapi? Na hiyo tabia umeanza lini? Kwanini unataka kutuingiza kwenye matatizo wewe mtoto?” Alikuwa ni mama yake Farida, akimwuliza mwanaye alipoingia ndani, muda mfupi baada ya kuachana na Genesis.

Farida hakuwa na jibu, alinyamaza kimya akiwa anatetemeka.
Je, nini kitatokea?
 
SEHEMU YA 04


Farida msichana mrembo anayetoka katika familia ya kimasikini, anajikuta akiwa
katika penzi zito kwa Genesis ambaye alikuwa mtoto kutoka katika familia ya
kitajiri ya Profesa Mshana lakini siku zote alikuwa anaogopa sana kumweleza
ukweli wa hisia zake.

Kama ilivyokuwa kwa Farida, Genesis naye alikuwa anampenda sana lakini naye pia
akawaza anashindwa kueleza kinachoendelea moyoni mwake. Kilichotokea ni kwamba wote wakawa na ukaribu ambao waliuita ‘urafiki wa kawaida’, huku ndani ya mioyo yao ikiendelea kuungua kwa mapenzi mazito.

Vijana hawa walikutana pamoja katika Shule ya Sekondari Mt. Thomas, iliyopo
kilometa hamsini, kutoka Morogoro Mjini. Ilikuwa shule ya watoto wenye uwezo
kifedha, lakini Farida aliweza kwenda kusoma katika shule hiyo kwa msaada wa
Padre Bathromayo kupitia Shirika la Kitume la Women Opportunity Expanded ambalo
lilikuwa na mpango wa kusaidia wasichana wenye uwezo mzuri kupata elimu.

Farida aliweza kusaidiwa na shirika hilo, baada ya kufanya vizuri katika mtihani
wake wa darasa la saba na kuchaguliwa kujiunga na Shule ya Vipaji Malalum ya
Wasichana ya Kilakala, iliyopo mjini Morogoro.

Hisia za mapenzi kati ya vijana hawa, zinazidi kuwatesa mioyoni mwao, lakini
wote wakiendelea kutambuana kama marafiki tu! Wakati wa likizo, Genesis alikuwa
anakwenda kumtembelea Farida nyumbani kwao mara kwa mara, lakini siku Farida
aliyokwenda nyumbani kwao na kujitambulisha kuwa anatoka Mtoni Kwa Aziz Ally,
tena kwenye familia ya baba fundi seremala na mama mama ntilie, baba yake na
Genesis akawaambia watoke nje, kwa kuwa walikuwa na mazungumzo muhimu na Bwana na Bibi Rwegoshora!

Jambo hilo lilimuumiza sana Farida, lakini ukawa mwanzo wa kueleza hisia zao za
ukweli kuwa wanapendana, lakini mjadala mkubwa ulioibuka ni vipi familia hizo
zingeweza kuungana kutokana na tofauti za kimaisha walizokuwa nazo.

Genesis anajaribu kumtuliza, baadaye anaondoka naye na kwenda Kariakoo kwa mara nyingine, ambapo waliingia madukani na kumchagulia nguo zaidi. Mwisho kabisa akamrudisha nyumbani kwao Mtoni kwa Azizi Ally. Kazi kubwa huko ikabaki kwa
Farida, ambaye mama yake alitaka kujua mahali alipopata nguo mpya!

Nyumbani kwa Profesa Mshana, mazungumzo yanaendelea lakini baadaye baba Genesis anamuomba Dk. Rwegoshera wazungumze kidogo kwenye chumba cha mkutano, huko akamweleza wazo lake la kumhamishia mwanaye Bianca katika shule anayosoma Genesis, akieleza kwamba wanatoa elimu bora.

Ukweli haukuwa huo, alipanga hivyo ili kuwasogeza vijana hao, ambao aliamini
mwisho wa siku wangeweza kuwa wapenzi. Baada ya mazungumzo yao, wanarudi
sebuleni. Macho yao kwa pamoja yanakutana na Genesis akiingia kupitia mlango
mkubwa. Uso wake haufichi hisia zake, anaonekana kutokuwa na furaha kabisa.

Je, nini kitatokea? SONGA NAYO…

“Karibu mwanangu, mwenzako yupo wapi?” Profesa Mshana akamwambia Genesis
akionekana kama anampima.

“Nani?” Genesis akamwuliza.
“Ulikuwa na rafiki yako muda mfupi uliopita siyo?”
“Ni kweli baba, nimeshamrudisha kwao.”
“Ok! Vizuri sana. Keti, nataka kukutambulisha kwa watu hawa muhimu kwa familia
yetu.”

Genesis akaketi kwenye kiti akimwangalia baba yake, lakini kichwani mwake
akionekana kuwa na mawazo mengi sana. Hakukubaliana kabisa na baba yake kumtenga Farida, rafiki yake ambaye hisia zake za mapenzi zilianza kumsumbua tangu siku ya kwanza walipokutana shuleni.

“Kutana na Bw. & Bi. Dk. Rwegoshora, hawa walikuwa wakiishi Uswisi kwa muda
mrefu sasa, lakini sasa watakuwa hapa nchini. Dk. Rwegoshora ameteuliwa kuwa
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, kwa hiyo watakuwa wakiishi hapa!” akamaliza Profesa
Mshana na kukaa kimya.

“Nimefurahi kuwafahamu, karibuni sana!”
“Ahsante!” wakaitika kwa pamoja.
“Yule pale anaitwa Bianca, ni binti yao!” Profesa Mshana akasema akimtazama
Bianca.

Bianca alipokutanisha macho yake na Genesis akaachia tabasamu mwanana kabisa.
Hali ilikuwa tofauti kwa Genesis, usoni mwake alionekana anatabasamu, lakini
ndani ya moyo wake kulikuwa na kitu tofauti kabisa, picha ya mpenzi wake Farida
iliendelea kuutesa ubongo wake.

“Karibu nyumbani Bianca, hawa ni wazazi wangu na hapa ndiyo kwetu, jisikie huru
tafadhali,” Genesis akasema akiendelea kuteseka katika tabasamu lile la
kutengeneza.
“Ahsante sana Genesis!”

Mazungumzo yaliendelea hadi jioni kabisa, wakila, kunywa na kuufurahia
muunganiko wa familia hizi mbili. Baadaye usiku wa saa tatu, Dk. Rwegoshora,
mkewe na mwanao Bianca waliondoka kurudi kwao. Huku nyuma ukabaki mjadala mpya!

“Yule binti ni nani?” Profesa Mshana akamwuliza mwanaye.
“Baba nilishasema ni rafiki yangu!”
“Nakumbuka kama alisema anaishi Kwa Azizi Ally, ni kweli?”
“Ndiyo baba.”

“Sasa mwanangu, nataka kukushauri na unatakiwa kutusikiliza vizuri sana sisi wazazi wako, Yule msichana hana hadhi ya kuwa na wewe. Kwanza hafanani kabisa
na hii familia yetu, kwanini usiwe na marafiki wanaofanana na hadhi yako mwanangu? Au unataka kutudhalilisha?” Profesa Mshana alizungumza kwa sauti ya
taratibu sana, akionekana kutoridhishwa kabisa na kitendo cha mtoto wake kuwa
karibu na Farida.

“Kwani baba yule binti ana nini?”
“Masikini, huwezi kuchanganya mchanga kwenye chakula mwanangu!”
“Unamaanisha nini?”

“Yule anatakiwa kuwa na watu wenye hadhi kama yake, wewe hufanani naye kabisa.”
“Lakini baba, sidhani kama Mungu aliumba watu kwa matabaka, wote tupo sawa mbele zake. Mali na vitu vingine ni vya hapa duniani baba na mwisho wa uhai wetu
tutaacha kila kitu na tutakuwa sawa kwa Mungu.

“Farida ni rafiki yangu, tena rafiki mwema sana baba, nasoma naye, ana uwezo
mzuri darasani kwa hiyo huwa tunasaidiana mambo mengi kwenye masomo. Ni vigumu sana baba kunitenganisha naye, naomba uniruhusu aendelee kuwa rafiki yangu!”

“Kama una baba mwingine endelea kuwa na msimamo wako wa kipumbavu, lakini kama mimi ni baba yako, zingatia hayo maamuzi niliyoyatoa!” Profesa Mshana akasema na kuodoka zake, kuingia chumbani mwake.

*******
Uso wa mama Farida ulikuwa umekunjamana, siku zote hakupenda kuona mwanaye
anaharibikiwa, alishtushwa na mavazi aliyokuja nayo nyumbani. Yalikuwa mavazi ya
gharama sana, tofauti na uwezo wao, kwa hiyo ilikuwa lazima ambane ili amweleze
ukweli.
Kilichokuwa kichwani mwake ilikuwa ni kwamba, mwanaye alikuwa ameshaanza tabia
mbaya na kununuliwa nguo na mwanaume. Hilo hakutaka kabisa kuliruhusu litokee.

“Naongea na wewe Farida!” Mama yake akamwambia Farida.
“Mama naye, mbona hivyo?”
“Nataka kujua ulipopata hizi nguo!”

“Ni Genesis mama!” Farida akasema kwa sauti ya taratibu sana.
“Ndiye aliyekununulia?” Mama yake akauliza.
“Genesis huyu huyu?”

“Ndiyo mama!”
“Isije kuwa mmeshaanza…” mama Farida akasema akionekana kuanza kuwa na wasiwasi.
“Hapana mama, nadhani unanijua vizuri mama, nazingatia masomo zaidi kwa sasa,

maana najua ndiyo msingi wa maisha yangu. Siwezi kukuangusha mama, najua nina
deni la kuja kuwakwamua katika huu umasikini. Genesis ni rafiki yangu, atabaki
kuwa hivyo, tofauti yetu ni vipato, nahisi naye kwa kutambua hilo, ameamua
kunisaidia.

“Sioni ubaya katika hilo mama, niseme ukweli kwamba hata shuleni amekuwa
akinisaidia mambo mengi sana. Genesis ni rafiki mwema kwangu mama, naomba
uniamini!” akasema Farida kwa utulivu sana.

Nje alionekana anayoongea ni dhahiri kabisa, lakini ndani ya moyo wake alikuwa
na siri nzito ambayo hakutaka kuitoa hadharani, alikuwa katika mapenzi na
Genesis, penzi ambalo lilitambulishwa rasmi kwa mara ya kwanza siku hiyo, ingawa
pia alijeruhiwa moyo wake!

*****
Likizo ya Genesis iliisha, hapo sasa alitakiwa kurudi shuleni, alifanya mbinu
zote akahakikisha haongozani na mtu yeyote shule zaidi ya dereva wao tu. Hilo
aliweza kulitimiza, akapewa mahitaji yote na kuingia kwenye gari kwa safari ya
kwenda shuleni Morogoro.

Kikubwa alichokuwa akitarajia kilikuwa ni kusafiri na Farida kwenye gari lao!
Gari lilivyoondoka tu, nyumbani kwao Masaki, Genesis akatoa noti tano za elfu
kumi kumi, ambazo zilikuwa ni jumla ya shilingi elfu hamsini na kumkabidhi
dereva.

“Za nini?”
“Chukua tu!”
“Hapana hizo ni kwa ajili yako shuleni.”

“Najua, lakini chukua, mimi ninazo nyingi.”
“Sawa, lakini kwanini ulikuwa hutaki kuongozana na dada yako kwenda shuleni?”
“Unapakumbuka kule kwa Kwa Azizi Ally?”

“Ndiyo!”
“Twende tukamchukue yule msichana, nakwenda naye shuleni, sikutaka kwenda na
dada, maana asingekubali tumbebe Farida!”

“Mh! Haya bwana,” dereva akaitika akiendesha gari kwenda Kwa Azizi Ally, elfu
hamsini zilitosha kabisa kumlainisha!”

Baada ya mwendo wa nusu saa walikuwa wameshafika Kwa Azizi Ally, wakamkuta
Farida akiwa tayari ameshajiandaa. Akaingia kwenye gari na safari ya kwenda
Morogoro ikaanza. Walizungumza mengi njiani, lakini wote walionekana kupendana
sana, walifurahia safari yao.

******
Ilikuwa ni Januari, wanafunzi wakiwa ndiyo kwanza wamemaliza likizo na kuingia
vidato vipya! Katika darasa la akina Genesis, walikuwa ndiyo wameingia kidato
cha tatu! Mbele ya darasa alisimama Sister Immaculate, ambaye alikuwa
akifundisha somo la Kemia.

Mara akaingia mwalimu wa darasa, akiwa ameongozana na msichana mrembo sana
aliyevalia sare za shule hiyo. Akamwomba radhi Sister Immaculate na kumsogeza
yule mwanafunzi karibu na yeye.

“Jamani huyu ni mwanafunzi mgeni, ambaye amejiunga na shule yetu kuanzia leo,
anaitwa Bianca Rwegoshora, mtakuwa naye hapa darasani. Ni Mtanzania, lakini kwa
muda mrefu amekuwa akiishi nchini Uswisi, naomba mumpe kila aina ya
ushirikiano!” Mwalimu akasema na wanafunzi wote wakapiga makofi.

“Genesis…” mwalimu akaita.
“Ndiyo mwalimu!”
‘Utakaa na Bianca umchangamshe kidogo! Nawatakieni masomo mema. Nashukuru sana mwalimu!” Akasema mwalimu wa darasa na kumwelekeza Bianca akaketi dawati moja na Genesis.

Bianca alikuwa anatabasamu na alifurahi sana kuwa karibu na Genesis, maana alikuwa akimfahamu kabla walipokwenda nyumbani kwao akiwa na wazazi wake.
Genesis akampokea akitabasamu, lakini alipogeuza macho yake kumuangalia Farida,
ALIKUTANA NA MACHOZI!
Genesis akashtuka sana!

Je, nini kitatokea?
 
SEHEMU YA 05


Penzi la dhati linachipuka ndani ya mioyo ya vijana wawili, Farida na Genesis! Hawa wapo katika rika moja, lakini wanatofautiana uwezo wa kifedha katika familia zao. Wakati Genesis akiwa na wazazi wasomi wenye fedha na wamiliki wa Chuo, Farida yeye alitoka katika familia masikini kabisa ya baba Fundi Seremala na Mama Ntilie!

Walikuwa na tofauti kubwa, lakini mioyo yao ilikuwa na hisia sawa! Wote wananyamaza kueleza hisia zao, hadi siku moja wakati wa likizo, Farida alipokwenda nyumbani kwa akina Genesis wakati wa likizo na wazazi wake kuwatoa nje, wakisema kwamba wana mazungumzo muhimu na Bwana na Bi Rwegoshora.

Hiyo ndiyo siku mapenzi yao yalipochipuka! Ahadi yao inakuwa kuishi pamoja mara baada ya kumaliza elimu yao ya chuo.
Likizo ilipoisha na kurudi shuleni, waliingia kidato cha tatu, hapo ndipo msichana Bianca, mtoto wa Dk. Rwegoshora, ambaye alikuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, alipojiunga na shule hiyo.

Mwiba ulikuwa kupangiwa kukaa dawati moja na Geneses. Kwa Farida ilikuwa ni huzuni kubwa, wakati Bianca anakwenda kukaa akitabasamu, macho ya Genesis yalikutana na Farida, alikutana na machozi!
Je, nini kitatokea? SONGA NAYO...

MOYO wa Farida ulishtuka sana, alianza kuogopa moyoni mwake akihisi kunyang’anywa mpenzi wake. Alimkumbuka vizuri sana Bianca. Alimuona siku ambayo alikwenda nyumbani kwa akina Genesis, halafu yeye akafuzwa nje ili awapishe wazazi wake na Bianca wazungumze.

Dharau aliyooneshwa ni wazi kwamba alikuwa hahitajiki kabisa na ile familia. Alionekana hana thamani hata kidogo kutokana na kipato cha wazazi wake kuwa kidogo.

Kumwona Bianca shuleni pale, kulimaanisha ukaribu wake na Genesis ambao aliona kabisa kwamba ungeweza kuzaa mapenzi, na kwa sababu familia zao zinaelewana basi, ingekuwa rahisi kwake kuachwa na Bianca kuolewa jambo ambalo hakuwa tayari kuona linatokea.

Genesis aliendelea kumwangalia akishindwa kuelewa kabisa kilichotokea. Genesis akataka kusimama na kwenda kwenye dawati lake, Sister Immaculate akagundua kilichotokea. Aliyaona macho ya Farida yalivyojaa machozi.
“Farida!” Mwalimu akaita.

“Abee...” Farida akaitikia akitoa kitambaa na kufuta machozi machoni mwake.
“Hebu simama!”
Farida akasimama.

“Una tatizo gani?”
“Sina Mwalimu!”
“Hapana, una tatizo.”

“Sina!”
“Hayo machozi vipi?”
“Macho yananisumbua, halafu nahisi mafua yamenibana sana!”
“Kweli?”

“Ndiyo mwalimu!”
“Huna sababu ya kunificha kama una tatizo Farida!”
“Sina mwalimu ni mafua na macho!”

“Ok! Baada ya kipindi nenda zahanati ukaonane na daktari!”
“Sawa mwalimu.”
Farida alikuwa anadanganya, hakuwa anaumwa macho kama alivyosema na wala hakuwa na ugonjwa wa mafua kama alivyokuwa akijaribu kudanganya.

Tatizo lililokuwa linamsumbua ni wivu, hakufurahi kumuona Bianca akipangiwa kukaa kwenye dawati moja na Bianca.
Kipindi kikaendelea, lakini moyoni Farida hakuwa na amani kabisa. Alikuwa akimwaza Genesis! Siku yake ilianza vibaya, hadi kipindi kinaisha, hakuwa ameelewa kitu chochote.

*****
Wakati wa mapumziko, wanafunzi karibu wote walikwenda kwenye mgahawa wa shule kwa ajili ya kupata soda na vitafunwa, lakini Farida siku hiyo hakwenda, alitafuta sehemu ya peke yake, akajiinamia na kuendelea kulia.

Dalili za kumpoteza mpenzi wake zilikuwa wazi kabisa, dawa pekee ya kutuliza machungu yake ilikuwa ni kulia tu. Akiwa katika eneo hilo, Chris, rafiki wa karibu na Genesis akapita. Huo ukawa ukombozi wake, haraka akamwita.
“Vipi Farida?” Chris akauliza akisogea taratibu sehemu aliyokuwa amekaa.

“Sipo sawa kabisa Chris!”
“Nini tatizo?”
“Tatizo ni Genesis!”
“Genesis?”

“Ndiyo Genesis!”
“Enhee amefanyaje?”
“Naamini unajua kinachoendelea kati yangu na yeye!”
“Ndiyo nafahamu!”

“Sasa sijafurahishwa kabisa na yeye kupangwa dawati moja na Bianca!”
“Bianca ni nani?”

“Yule mwanafunzi mgeni ambaye ameletwa leo darasani kwetu!”
“Usiwe na wasiwasi Farida, najua Genesis anakupenda, hawezi kufanya hivyo, lakini hata hivyo ukumbuke kwamba, si yeye aliyepanga kukaa na yule msichana bali ni mwalimu amempangia. Ondoa wasiwasi wako bwana!”
“Kweli?”

“Niamini mimi!”
“Lakini sijui ni kwanini inakuwa vigumu kuamini, unajua nampenda sana Genesis na moyo wangu hauna amani kabisa na Bianca!”

“Achana na hisia hizo kabisa.”
“Basi nimekuelewa Chris!”
Baada ya mazungumzo yale, Chris alimfuata Genesis na kumweleza jinsi Farida asivyo na imani na Bianca. Alimkuta akiwa na Bianca, akaomba kuzungumza naye pembeni, ndipo alipomweleza malalamiko ya mpenzi wake Farida.

“Hilo nililijua na kusema kweli nilipanga kuzungumza naye, lakini kwa kuwa umekuja kunieleza, nadhani ni bora kama nitazungumza na yeye akiwepo!”
“Nikamwite?”

“Ndiyo, tena haraka sana!”
Chris akatoka mbio kumfuata Farida, muda mfupi baadaye akarudi akiwa ameongozana naye. Genesis akawa kimya kumsikiliza kwanza Chris.

“Nadhani nimeshakueleza nini anacholalamikia mwenzako!” Chris akasema.
“Ni kweli kabisa... Farida!” Genesis akaitika na kumwita Farida.
“Bee!”

“Hebu nieleze kwa uwazi mpenzi wangu, wasiwasi wako ni nini hasa?”
“Genesis unadhani nimemsahau yule msichana?”
“Najua unamkumbuka vizuri!”

“Sasa huoni kama ni hatari kwangu!”
“Hatari ya vipi tena?”
“Kumbuka tukio la siku ile, kumbuka nilifukuzwa sebuleni kwenu kwa sababu wazazi wa Bianca, wakiwa wameongozana naye waliingia. Huoni kwamba yeye ndiye anakubalika zaidi kwenu!”

“Hata kama, lakini hiyo ndiyo sababu ya mimi kutokuwa na wewe!”
“Lakini wazazi wako watakuwa wanamkubali, kumbuka kwamba sisi kwetu hatuna uwezo na nyie kwenu familia yenu inajiweza, mbaya zaidi baba yako alionesha kabisa kwamba hajanikubali katika familia yenu na wala sikuwa na hadhi ya kukaa katika sebule yenu, sasa unadhani kwanini nisiwe na wasiwasi na ukaribu wenu?”

“Mapenzi yangu yanatoka moyoni, sihitaji shinikizo kutoka kwa mtu yeyote. Nimekupenda mwenyewe na nitahakikisha nalinda na kutunza penzi langu la kweli kwako. Niamini Farida nakupenda na nitakuwa wako siku zote!” Genesis alisema kwa utulivu sana akiyaangalia macho ya Farida kama anaelewa alichokuwa akisema.

“Sawa, nimekuelewa vizuri sana Genesis, lakini vipi kuhusu dini zetu?”
“Nimekupenda wewe kama ulivyo Farida, nimependa jinsi wewe mwenyewe ulivyo mzuri kama moyo wako, achana na hivyo vitu vingine mpenzi, amini mimi ni wako wa siku zote!”

“Ahsante, nashukuru kusikia hivyo!”
Haukupita muda mrefu sana, kengele ya kurudi darasani ikapigwa, wote wakakimbia kurudi darasani.

****
Siku zikazidi kwenda huku mapenzi ya Genesis kwa Farida yakizidi kupamba moto, alizidi kumpenda sana Farida, kwake alikuwa mwanamke anayemfaa kwa kila hali, alimpa nafasi ya kwanza kabisa katika maisha yake.

Matokeo ya mtihani ya mwisho ya kidato cha nne yalipotoka, wote walikuwa wamefanya vizuri. Wakaendelea na masomo ya kidato cha tano na sita katika shule ileile. Tayari walikuwa wameshaanza kuwa wakubwa! Katika kipindi chote hicho, Genesis alikuwa karibu na Farida na Bianca kwa wakati mmoja, lakini Bianca alikuwa na mzigo mzito wa mapenzi ndani ya moyo wake.

Kwa kumwangalia tu, Genesis aliweza kugundua kwamba Bianca alikuwa akimpenda sana, lakini alikuwa anashindwa kueleza ukweli moja kwa moja. Macho yake yalisomeka wazi kabisa kwamba, anampenda sana Genesis.

Siku zikazidi kwenda, lakini siku moja Bianca akashindwa kuvumilia zaidi, hiyo ni baada ya kuitunza siri hiyo ya mapenzi moyoni mwake kwa muda mrefu sana.

“Genesis nimekuwa rafiki yako kwa muda mrefu sasa, tangu kidato cha tatu. Kwa muda wote huo nimekuwa nikiteseka sana kimapenzi juu yako, lakini leo nimeshindwa kuvumilia kabisa, lazima nikueleze ukweli kwamba nakupenda sana.

“Tafadhali naomba unipe nafasi moyoni mwako, nataka unioe niwe mke wako, tafadhali sana nakuomba!” Bianca akamwambia Genesis kwa hisia kali sana za kimapenzi.

“Nashukuru kwa kunipenda Bianca!” Genesis akasema baada ya kufikiria kwa muda kidogo.
“Kwa hiyo umekubali?”
“HAPANA!” Genesis akajibu kwa kujiamini sana.

Lilikuwa jibu baya sana kwa Bianca, hakutarajia kabisa kusikia Genesis akimjibu vile, maana kuna wakati alikuwa anaamini kwamba Genesis naye alikuwa anampenda.

BIANCA hakuamini kama maneno yale yalitoka kinywani mwa Genesis, mwanaume
anayeunyanyasa moyo wake. Alikuwa tayari kwa kila kitu ili aweze kumpata. Jibu
la Genesis lilimchoma sana moyo wake.

Hakuamini kama ni kweli Genesis alisema kwa kudhamiria au alikuwa anatania! Bado
moyo wake haukutaka kuamini moja kwa moja maneno ya Genesis. Alikuwa kama
anaungua ndani kwa ndani kwa maumivu makali yanayochoma.

“Genesis!” Bianca akaita.
“Nakusikia.”
“Unayosema yana ukweli au nimesikia vibaya?”

“Wewe unaonaje?”
“Ndiyo maana nimekuuliza, maana sijaelewa kama ni kweli ni wewe unazungumza au
unafanya utani!”

“Sina utani na wewe Bianca, tena katika mambo muhimu kama haya. Sidhani kama
nakutania, ninachokisema kinatoka ndani ya moyo wangu!”
“Kwahiyo ni kweli hunipendi?
“Nahisi utakuwa umenisikia vibaya!”

“Wewe si umesema kwamba hutaki kuwa na mimi...?”
“Ndiyo!”
“Sasa ina maana gani?”

“Kutokuwa na wewe kimapenzi, hakumaanishi kuwa sikupendi. Mimi nakupenda tena
sana, kutoka ndani ya moyo wangu, lakini sitaki kuwa na uhusiano wa mapenzi na
wewe.”

“Kwanini?”
“Hata wewe unajua sababu!”
“Kama ningekuwa najua, unadhani ningekuwa na sababu gani ya kukuuliza?”

“Hebu nikuulize swali moja.”
“Uliza.”
“Wewe hujui kinachoendelea kati yangu na Farida!”

“Farida?”
“Ndiyo, Farida!”
“Najua.”
“Sasa kwanini unataka tena niwe mpenzi wako?”

“Lakini lazima ufikirie mara mbili, kumbuka familia zetu ni marafiki, tena wa
karibu sana, naamini watafurahi sana kusikia kwamba tuna uhusiano ambao baadaye
unaweza kuzaa ndoa. Achana na huyu Farida, kwanza hafanani na wewe. Hata kama ni
mzuri, lakini hana hadhi ya kuwa na wewe. Anatoka familia duni, hana maisha mazuri,
kwanini unataka kuruhusu aingie kwenye familia yenu kuchafua?”

“Achana na hayo mambo Bianca tafadhali, Farida ni mpenzi wangu, tena
ninayempenda kwa dhati kabisa kutoka ndani ya moyo wangu. Unawezaje
kunitenganisha naye?”

“Angalia jinsi ninavyofanana na wewe, achana na yule masikini!”
“Hebu acha kuendelea kuongea huo upuuzi wako, mimi mwenyewe ndiye ninayejua
ninachokipata kwa Farida. Mapenzi ya dhati hayapimwi kwa mali, wadhifa wala
nafasi. Niache na Farida wangu,” Genesis akasema kwa hasira kisha akaondoka na
kumuacha Bianca peke yake.

Bianca alijaribu kumkimbilia akimwita jina lake, lakini Genesis hakugeuka nyuma.
Bianca hakuwa na kitu kingine cha kufanya zaidi ya kwenda zake bwenini akiwa
mwenye huzuni na mawazo tele kichwani. Ndoto za kumpata Genesis bado zilikuwa
palepale!

Hakujali angechelewa kiasi gani, hata kama ingemchukua zaidi ya miaka ishirini,
lakini nia yake ilikuwa kumpata Genesis, baaasi!

“Mimi ndiye Bianca, naweza kufanya mambo yangu kwa uhakika na usahihi kabisa.
Ninachojua ndani ya moyo wangu ni kwamba nampenda sana Genesis, sidhani kama
kuna kitu cha kunitengenisha naye, sidhani kama kitatokea. Genesis atakuwa wangu
siku moja. Najiamini na nitahakikisha hilo linatokea!”akawaza kichwani mwake
akiwa amejilaza kitandani kwake.

****
Macho yake yametulia usoni mwa kijana huyu anayemsikiliza kwa makini. Hasira
aliyokuwa nayo ndani ya moyo wake inaonekana wazi kabisa kupitia makunyanzi
yanayoonekana usoni mwake. Ni wazi kwamba alikuwa amekasirika sana!

Huyu ni Bianca akiwa kwenye kikao muhimu na Chris, rafiki wa karibu na Genesis,
agenda kubwa ikiwa ni jinsi gani angeweza kuwaachanisha Genesis na Farida ili
yeye aweze kuwa mpenzi wake.

Chris alikuwa makini sana kumsikiliza wakati wote aliokuwa akizungumza. Ni kama
alikuwa akijiandaa kikamilifu kuifanya kazi hiyo ambayo Bianca alionekana
kuipania sana. Kazi kubwa aliyokuwa akimpa Chris ni kuhakikisha anafanikisha
zoezi la kuwaachanisha Faida na Genesis.
“Umemaliza Bianca?” Chris akasema baada ya kuona Bianca amemaliza, akisubiri
kumsikiliza.

“Ndiyo nimemaliza, nahitaji msaada wako!”
“Kwanini unataka kufanya hivyo lakini?” Chris akamwuliza Bianca kwa sauti
iliyojaa utulivu sana.

“Mapenzi, Chris, hakuna kingine.”
“Unampenda sana Genesis?”
“Sana!”

“Naomba nikuulize kitu kingine.”
“Uliza.”
“Hufahamu kwamba Farida naye anampenda?”

“Najua, ndiyo maana nataka kuwaachanisha ili mimi niwe naye?”
“Kwani wewe na Farida ni nani wa kwanza kukutana na Genesis?”
“Jibu lipo wazi kabisa, ni Farida.”

“Unadhani hakumpenda au hampendi?”
“Hebu achana na mahubiri yako bwana, sema kama utaweza kunisaidia au lah!”
Bianca akasema akionekana mwenye hasira kidogo.

“Siwezi!” Chris akajibu kwa kifupi sana.
“Sikiliza Chris, mimi nitakuwa tayari kukupatia hata fedha yoyote unayoitaka,
lakini niwe na Genesis, sema unataka kiasi gani unisaidie?”

“Acha ujinga, sitaki kuamini kama unadhani mimi nina shida ya fedha kiasi hicho.
Pamoja na kwamba nipo shuleni nasoma, baba yangu amenipa moja ya kampuni zake
nasimamia kama mkurugenzi, sina shida na pesa kabisa.”
“Najua, lakini naomba unisaidie Chris.”

“Nimesema sitaki!” Chris akasema akionekana kudhamiria sana alichokisema.
“Sawa, nimekuelewa Chris lakini naomba haya mambo yabaki kuwa siri yetu. Acha
mimi nitajua nitatumia njia gani nyingine!”

“Siri nitaitunza, lakini sijui kama utafanikiwa. Kwa ninavyowajua Farida na
Genesis, sijui kama utafanikiwa. Nashauri utafute mwanaume mwingine.”

“Hilo sasa ni juu yangu!”
Chris akaondoka zake, akamuacha Bianca akiwa mwenye mawazo mengi sana. Alihisi
kumkosa Genesis, ingawa kwake lingekuwa pigo kubwa sana.

****
Bianca alibadilika kabisa, kichwani mwake kulikuwa na mtu mmoja tu anayemsumbua,
ni Genesis tu ndiye alikuwa chaguo lake. Hakuwaza kabisa juu ya Farida,
alitamani hata ikiwezekana afe ili yeye aweze kuwa Genesis.

Kipindi hiki cha likizo, ambacho alikuwa nyumbani muda wote, wiki mbili tu za
mwanzoni, mama yake aliweza kugundua kwamba mwanaye hayupo katika hali ya
kawaida, alihisi alikuwa na kitu kinachomchanganya kichwani mwake.

Si mama yake pekee, hata baba yake Dk. Rwegoshera aligundua tofauti aliyorudi
nayo mwanaye kipindi hiki. Alichokifanya ni kumwambia mkewe atafute muda wa
kuzungumza na mwanaye ili amweleze kinachomsumbua.

Wapo sebuleni wawili tu, Dk. Rwegoshora akiwa kazini, mama yake Bianca anataka
kujua kinachomsumbua mwanaye. Anamwangalia machoni kwa makini na kuzungumza kwa sauti ya upole sana.
“Bianca!”
“Abee mama!”

“Unafahamu kwamba sisi wazazi wako tunakupenda sana?”
“Nafahamu mama.”
“Hebu niambie, una nini kinachokusumbua?”
“Sina mama, kwani umeonaje?”

“Haupo sawa, na mimi nakufahamu vizuri sana mwanangu. Sema una nini
kinakutatiza?”
Bianca hakuweza kujibu kitu zaidi ya kulia. Alikuwa akilia kwa sababu ya uchungu
uliokuwa moyoni mwake.

“Machozi hayatasaidia kitu, niambie una nini kinachokusumbua?”
“Acha niwe mkweli mama, tatizo ni GENESIS!” Bianca akasema akilia.
“Genesis?”

“Ndiyo mama, nampenda sana Genesis, lakini haonekani kuwa na wazo la kunipenda,
naumia sana mama, nateseka!” Bianca akasema, lakini machozi yakizidi kumiminika
machoni mwake.

Je, nini kitatokea?
 
SEHEMU YA 06



Wakati Farida akiwa na wasiwasi kwamba mpenzi wake Genesis ameanzisha uhusiano wa kimapenzi na Bianca, mtoto wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Genesis hana wazo kabisa la kuwa na Bianca. Hilo limethibitika hata katika mazungumzo yao ya ana kwa ana, ambapo Genesis ameeleza msimamo wake.

Pamoja na msimamo wake huo, Bianca anaonekana kutumia nguvu nyingi sana kuhakikisha anamnasa Genesis.

Alivyoshindwa katika mazungumzo naye, akaamua kuzungumza na rafiki wa karibu na Genesis aitwaye Chris, ambaye hakuonekana kumuunga mkono wazo lake hilo.

Upendo wake kwa Genesis ukaanza kumuumiza ndani kwa ndani. Walipofunga shule, alirudi nyumbani akiwa na mawazo sana, akili yake yote ilikuwa kwa Genesis, muda mwingi alikuwa na mawazo sana, jambo ambalo wazazi wake waliligundua na mama yake akaamua kuzungumza naye ili kugundua kilichokuwa kinamsumbua!

Katika mazungumzo yao, Bianca akaamua kuwa mkweli, akamweleza mama yake kwamba kilichokuwa kikimsumbua na kumtesa ni Genesis!
Je, nini kitatokea? SONGA NAYO...

MSHTUKO mkubwa uliingia moyoni mwa mama yake Bianca, akamwangalia mwanaye akiwa haamini kabisa kama angeweza kutamka maneno yale. Hakuamini kama mwanaye tayari alikuwa ameshaingia kwenye mambo ya mapenzi, zilikuwa habari mpya kabisa kwake.

Macho yake yaliweza kuonesha kabisa kilichokuwa ndani yake, kwamba haamini au hakubaliani na alichosikia kutoka kwa Biaca, lakini mwanaye alizidi kumwangalia mama yake akionekana kutaka usaidizi, lakini macho yake yalikuwa yamejaa machozi.
“Bianca!”

“Abee mama,” akaitika Bianca akishindwa kuzuia hisia zake za ndani.
“Nilichokisikia ni sahihi?” mama yake akauliza.
“Ndiyo mama, kwanini nikufiche, kwanini niendelee kuteseka? Ni kweli kabisa nampenda sana Genesis, nahitaji awe mume wangu wa baadaye, lakini ndiyo hanitaki, kisa eti Farida!”

“Farida ndiyo nani?”
“Yule msichana aliyekuwa naye siku ya kwanza tunaenda kwao. Naye anasoma kule St. Thomas!”

Mama yake akakaa kimya akitafakari vizuri maneno ya mwanaye, kwa namna fulani yalikuwa yakimuingia, kwa umri wa miaka miaka kumi na tisa aliokuwa nao, hisia zake za mapenzi zilikuwa sahihi kuwa vile, ila hakupenda mwanaye ajiingize kwenye mapenzi mapema kiasi kile.

“Lakini Bianca binti yangu, kama tayari mapenzi yameanza kukuchanganya kiasi hiki, utaweza kusoma kweli?”
“Naweza mama, tayari mimi ni mtu mzima, ninayejua kila baya na jema, siwezi kuharibu masomo yangu kwa sababu ya mapenzi mama!”

“Lakini umerudi ukiwa na mawazo kwa muda wote uliokuwa hapa nyumbani na wewe mwenyewe umekiri kwamba, tatizo ni Genesis, sasa huoni kwamba utachanganya mambo!”
“Hapana mama!”

“Kwani kabla ya kukutana na Genesis ulikuwa na nani?” Mama yake akamuuliza swali lile kwa nia ya kutaka kujua ukweli.
“Mpenzi mwingine mama? Hapana...sijawahi kabisa mama!”
“Kwa hiyo ndiyo unaanza kupenda?”
“Ndiyo mama!”

“Unataka kuniambia kwamba bado mzima kabisa?”
“Nadhani sijakuelewa vizuri mama!”
“Namaanisha kwamba, bikira yako bado unayo?”

“Sijawahi kukutana na mwanaume yeyote tangu nizaliwe, sidhani kama nitafanya hivyo kabla ya ndoa. Hata huyo Genesis mwenyewe akinikubali leo, hataweza kuuona mwili wangu hadi siku ya ndoa yetu, lakini mama, kikubwa ni kwamba nampenda!”

“Hilo suala niachie!”
“Utanisaidia mama?”
“Nipe muda, nitajua cha kufanya.”
“Nashukuru sana mama yangu!”

“Usijali, lakini kwa sasa nataka ubadilike, rudisha moyo wako. Fanya kazi zako kama kawaida, jisomee, nenda tuition ili ujiandae vyema kwa mtihani wako wa mwisho ukirudi shuleni.”
“Nimekuelewa vizuri sana mama.”
“Nakupenda sana mwanangu!”

“Hata mimi pia mama, najivunia sana kuwa na mzazi kama wewe mama’ngu!”
“Usijali!”

Baada ya hapo, Bianca akaendelea na kazi zake ndogo ndogo, mama yake akaingia kwenye gari na kwenda zake mjini kufanya manunuzi ya mahitaji ya ndani.

***
Dk. Rwegoshora alikuwa ndiyo kwanza amepanda kitandani baada ya kumaliza kuangalia taarifa ya habari ya saa tano usiku katika Kituo cha ITV. Alionekana kuwa mchovu sana. Alipopanda tu kitandani, aligeukia upande wa pili na kuvuta shuka.

Mkewe alikuwa amejilaza muda mrefu kwenye ubao wa kitanda, hakuwa kwenye usingizi, muda wote alikuwa akisoma kitabu cha riwaya ya “Rais Anapenda Mke Wangu”. Kwa mtazamo ni kama alikuwa akimsubiri mume wake amweleze jambo fulani.

Aliyaondoa macho yake kwenye maandishi ya kitabu kile, kisha akamwangalia mumewe ambaye alionekana kuchoka pengine kuliko siku nyingine yeyote.

Alikuwa amegeukia upande wa pili, alama ile ilitosha kabisa kumfanya afahamu kwamba, mume wake alikuwa amechoka na hakutaka usumbufu kabisa.

Akainua mkono wake taratibu na kumgusa bega moja, Dk. Rwegoshora, ambaye alishtuka na kugeuka upande wa pili kumwangalia mkewe.
“Vipi mke wangu, nimechoka sana. Nahitaji kupata muda mwingi wa kupumzika!”

“Najua, lakini umesahau asubuhi uliniachia kazi gani?”
“Mambo mengi mke wangu, hebu nikumbushe!”
“Ni kuhusu binti yetu!”

“Enhee, amesemaje? Ana nini?” Dk. Rwegoshora akatamka kwa sauti yenye nguvu kidogo baada ya kusikia binti yake akitajwa.

Bianca alikuwa kila kitu kwake, alimpenda sana mwanaye huyo wa pekee, hakuwa tayari kuona anapata matatizo katika maisha yake.

Kitu chochote ambacho kingehusu pesa, alikuwa tayari kutumia gharama yoyote ili kumsaidia mwanaye. Alikaa kwa utulivu kumsikiliza mkewe.
“Binti yetu amekua!”
“Kivipi?”
“Genesis!”

“Kafanyaje?”
“Ndiyo chanzo cha matatizo yake.”
“Mama Bianca, hebu nieleze vizuri!”
“Anasema anampenda sana, kiasi kwamba anachanganyikiwa, lakini alijaribu kuzungumza naye, akamkataa kwa sababu ana mpenzi wake mwingine!”

“Unadhani ni sahihi kwake kwa kipindi hiki?”
“Kwa kweli si sahihi mume wangu mpenzi, lakini kwa upande mwingine naona kama ni sahihi.”
“Kwa nini unasema hivyo?”

“Umri wake unamruhusu mume wangu, tena imekuwa afadhali tumegundua hilo mapema, tofauti na kama angeanza kuparamia wanaume wenyewe.

Kwa mtazamo wangu, naona kama tukiweza kuwaunganisha hawa watoto, hasa kwa kuwa wazazi wa Genesis ni marafiki zetu, nahisi kama itakuwa ni vizuri zaidi, maana hatuna wasiwasi na malezi ya Genesis, lakini pia familia yao ni nzuri, inayoendana na sisi, kwa nini tusimsaidie?” Mama Bianca akazungumza kwa sauti ya taratibu sana.

Dk. Rwegoshora alimsikiliza mkewe kwa makini sana, akaonekana kutumia muda mwingi kufikiria, lakini baadaye alionekena kupata jibu.

“Ok! nadhani tufanye hivyo, tukutane na wenzetu tujadiliane, naamini matokeo yatakuwa mazuri kabisa!”
“Sawa, tufanye hivyo!”

“Ok! tulale sasa mama Bianca, nimechoka sana, halafu kesho nina vikao vitatu na vyote mimi ndiye mwenyekiti, kwa hiyo natakiwa kuwahi ofisini kuliko siku zote!”

“Pole mume wangu, ndiyo msingi wa maisha yetu mume wangu,” akasema mama Bianca akiweka kitabu chake pembeni, akazima taa ya mezani kisha akavuta shuka na kulala.
***
Mapenzi ya Farida na Genesis yalipamba moto, kila mahali walikuwa pamoja, ingawa Farida alikuwa hakubaliki nyumbani kwa akina Genesis, alikuwa anakwenda na kuishia bustanini ambapo alizungumza na mpenzi wake kwa muda mrefu wakinywa juisi.

Siku zote Genesis alipoulizwa kuhusu ukaribu wao, alisema kwamba walikuwa marafiki wa kawaida. Jambo hilo liliwashangaza sana wazazi wake, walijua wazi kulikuwa na kitu kingine kilichojificha nyuma ya urafiki ambao Genesis hakutaka kijulikane.

Walikwenda tuition pamoja, wakipeana moyo na kuelekezana mambo mengi ya masomo yao. Uhusiano wao, haukuwafanya washindwe kufanya vyema kwenye masomo yao, siku zote walibaki kama marafiki, wakiwa hawajawahi kukutana kimwili hata mara moja tangu walipokutana!
“Nakupenda sana Farida,” Genesis alimwambia Farida siku moja wakiwa wanapunga upepo baharini.

“Najua mpenzi wangu, natambua hilo vizuri sana, lakini tatizo bado lipo kwa wazazi wako ambao hawanipendi!”
“Usiseme hivyo Farida wangu, huolewi na wazazi wangu wewe, ni mimi ndiye nitakayekuoa!”

“Sasa kama wao hawanitaki?”
“Lakini mimi sijasema kwamba sikutaki, zingatia maneno yangu, sikiliza moyo wangu, tupo kwenye dunia mpya sasa hivi Farida, hakuna atakayeweza kunichagulia mke wa kuishi naye!”
“Acha nikuamini mpenzi wangu, lakini moyo wangu hauna amani kabisa.”
“Niamini mimi!”
“Sawa.”

***
Profesa Mshana Jr alikuwa amekunja uso wake kwa hasira akimwangalia mwanaye Genesis aliyekuwa anaingia sebuleni taratibu. Ilikuwa ni usiku wa saa 4:30, baada ya kuondoka tangu asubuhi akisema anakwenda kumtembelea rafiki yake Mbezi Beach.

“Hebu angalia saa pale ukutani ni saa ngapi?” Profesa Mshana alisema kwa sauti ya ukali sana.
“Samahani baba, nilipata dharura nyingine, ndiyo maana nimechelewa kurudi. Tafadhali naomba unisamehe.”
“Dharura gani?”

“Nilivyotoka Mbezi, Farida alinipigia simu, nikamfuata kwao na kwenda naye Bagamoyo, sasa wakati wa kurudi kukawa na foleni ndefu sana tangu Tegeta hadi kwao!”
“Umesema nani?”
“Farida baba!”

“Nilikuambia nini kuhusu huyo Farida wako? Sasa hebu amua moja, unataka kuendelea kuishi hapa nyumbani kwangu au uende kwa huyo Farida wako ukaishi kwao? Amua moja na unipe jibu sasa hivi!” Maneno hayo yalitoka kinywani mwa Profesa Mshana akionekana kufura sana kwa hasira.

Hakuwa na masihara hata kidogo na kauli, kwa Genesis ulikuwa mtihani mgumu sana, moyoni mwake alimhifadhi Farida na nyumbani kwao alitaka kuendelea kuishi.

Je, nini kitatokea?
 
SEHEMU YA 07


Bianca binti wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Dk. Rwegoshora amezama mapenzini kwa mtoto wa Profesa Mshana aitwaye Genesis. Familia zao ni marafiki wakubwa, wote wakiwa na uwezo mkubwa kifedha.

Tatizo ni kwa Genesis ambaye anampenda sana Farida, binti kutoka familia duni ya baba Fundi Seremala na Mama Ntilie. Upinzani mkubwa unaibuka kati ya Genesis na wazazi wake, lakini Genesis hakubali kuachana na Farida.

Bianca aliporudi likizo, akaamua kumweleza mama yake ukweli kwamba anampenda Genesis lakini yeye hampendi. Inapangwa mipango ya kwenda kuzungumza na wazazi wa Genesis ili kuweka mambo sawa.

Genesis anarudi nyumbani usiku, anamkuta baba yake akiwa anamsubiri sebuleni kwa hasira. Alipoulizwa alipotokea, akasema ametoka kwa akina Farida. Hapo ndipo alipoiibua hasira ya baba yake ambaye limtaka achague kitu kimoja kati ya viwili; Ahamie kwa akina Farida ili aendelee kuwa naye au aachane naye aendelee
kuishi pale nyumbani!
Je, nini kitatokea? SONGA NAYO....


GENESIS hakutakiwa kujibu haraka, ilikuwa lazima atulize kichwa chake kabla ya kufungua mdomo waake kuongea chochote! Alipomwangalia vizuri baba yake usoni, hakuonekana kuwa na masihara kabisa na alichokuwa akikizungumza. Profesa Mshana alikuwa amevimba kwa hasira!

Aliangalia kwa macho ya huruma akihitaji msamaha wa baba yake, lakini Profesa Mshana hakuonekana kujali kabisa alichokiona machoni mwa mwanaye.

“Nahitaji unipe jibu moja,” akasema kwa hasira sana.
“Jibu la nini baba?”
“Utaishi hapa nyumbani kwangu au kwa kina Farida?”
“Baba, kwanini unasema hivyo?”

“Wewe si huwezi kuachana na huyo Farida wako?”
“Lakini baba ni rafiki yangu, sasa kwanini un....” Profesa Mshana hakumpa nafasi ya kumalizia kauli yake, akamkatisha.

“Sikiliza wewe mpumbavu, kama mimi ningechagua mwanamke masikini, asiye na elimu, familia duni, nisingekuwa na maisha haya. Nilimchagua mama yako kwa kuzingatia haya ninayokuambia, kwanini wewe unakuwa kichwa ngumu? Kwanini
huelewi?”

“Baba, acha niwe mkweli...nampenda Farida na siwezi kumuacha. Nipo tayari kwa lolote lakini si kumuacha Farida wangu. Yeye ndiye chaguo langu na atakuwa mke wangu hapo baadaye. Wewe una vigezo vyako na mimi pia.

“Kwa bahati mbaya, siamini kama mtu anakuja na mali duniani, lakini upendo wa kweli wa Farida ndiyo hasa ulionifanya nizidi kumpenda kila siku. Siwezi kuachana naye baba!”
“Unasemaje?”

“Nampenda Farida baba!”
“Unampenda eeeh?!”
“Ndiyo!”
“Haya nenda chumbani kwako ukalale!”

Genesis hakujibu kitu zaidi ya kwenda zake chumbani kulala. Moyoni alikuwa na hasira sana, hakupenda kabisa tabia ya baba yake umkataa Farida. Siku zote alikuwa na heshima sana kwa wazazi wake, lakini siku hiyo alijikuta akitoa majibu mabaya kwa baba yake.

Mapenzi yake kwa Farida ndiyo chanzo cha yote hayo, hakutaka kusikia mwanamke yeyote zaidi ya Farida, akili yake ilikuwa kwa Farida tu. Alishaingia ndani ya moyo
wake na ilikuwa vigumu sana kumtoa kwa sababu tu, wazazi wake hawamtaki.

Msimamo wake ndani ya moyo wake ulikuwa ni kumpenda Farida milele, hata kama angechukiwa na ulimwengu mzima. Mzigo wa mapenzi ndiyo uliomfanya awe kipofu kwa kila kitu mbele yake, isipokuwa kwa Farida tu.

Baba yake akabaki amesimama pale sebuleni akiwa amekasirika sana, alipotaka kupiga hatua kwenda chumbani ili akazungumze na mke wake, akashangaa anamuonam amesimama kwenye mlango mkubwa wa kuingia kwenye korido za kuelekea vyumbani.
“Vipi darling, nilisikia unakwaruzana na mwanao, kuna nini?” Mama Genesis
akamwuliza mumewe.

“Acha tu mke wangu, yaani hapa tuna hasara!”
“Kwanini?”
“Eti kuchelewa kote huku, alikuwa na Farida, hivi amempa nini mwanangu?”

“Usiwe na imani hiyo mume wangu, twende ndani tukalale!”
“Hapana huyu mtoto inabidi ashughulikiwe!”
“Sawa basi, twende ndani tukazungumze vizuri!”
“Ok!”

Profesa Mshana alikuwa hapendi kusikia kabisa umasikini, ndiyo malezi aliyolelewa na wazazi wake, siku zote alipenda watu wenye pesa, elimu na heshima mbele ya jamii. Ndoto yake kubwa ilikuwa mwanaye aoe katika familia ya wasomi, wenye fedha na heshima kubwa kama yao.

Msimamo wa Genesis ukamkosesha raha kabisa, lakini kichwani mwake alikuwa anajaribu kupanga namna ya kumdhibiti mwanaye.

“Nitajua nitakavyoshughulika naye, labda kama mimi si baba yake niliyemzaa
mwenyewe!” akawaza Profesa Mshana na kujifunika shuka na kulala.

****
Ulikuwa ugeni wa ghafla sana nyumbani kwa Profesa Mshana. Hawakusema kama
wangekwenda kwao siku hiyo, hata hivyo walijua lazima wangewakuta maana ilikuwa siku ya Jumapili, ambayo wote walikuwa hawaendi kazini.

Walikuwa ni Dk. Rwegoshora, mkewe pamoja na binti yao Bianca. Kwa kuwatazama machoni, walionekana kuwa na jambo muhimu lililowaleta nyumbani kwa akina Profesa Mshana.
“Mzee mwenzangu, mbona ghafla sana?”
“Hamjapenda nini?”

“Hapana, nimezoea kupokea simu yako kabla ya ujio wako!”
“Ni kweli, lakini leo tumeona tuwashtukize, lakini pia tulikuwa na uhakikakabisa kwamba, leo hamuendi kazini!”

“Karibuni!”
“Tunashukuru sana.”
“Enhee za nyumbani?”

“Sisi ni wazima kabisa!”
Muda huohuo akatokea Genesis, akawasalimia na kutaka kutoka nje, baba yake
akamzuia.
“Hebu keti hapo kwanza Genesis!”

“Sawa baba,” Genesis akajibu na kuketi.
Bianca akapata wakati mgumu sana, kila alipogonganisha macho yake na Genesisalikuwa akisisimkwa sana, moyo wake ulikuwa umeshampenda Genesis sana, hakutaka kusikia juu ya mwanaume mwingine zaidi yake, lakini Genesis hakuwa na habari naye kabisa.

“Mzee mwenzangu, lililotuleta ni muhimu sana, sijui kama tunaweza kuzungumza kwenye chumba cha mkutano?”
“Bila shaka!”

“Sawa, nadhani ni vyema kama na mama naye angekuwepo!”
“Hakuna tabu katika hilo...Genesis hebu mwite mama yako, mwambie aje meetingroom, wewe utabaki na mwenzako hapa sebuleni. Kabla hujaondoka, nahitaji kuongea
na wewe kwanza!”

“Nimekuelewa baba!”
Dk. Rwegoshora na mkewe wakaongozana na Profesa Mshana hadi kwenye chumba cha mkutano, muda mfupi baadaye mama yake Genesis akaingia, akionekana kushangazwakidogo na ugeni ule wa ghafla.
“Mmetuvamia?!” akasema akicheka.

“Hapana, hapa ni kwetu, tuna uhuru wa kuja muda wowote, kwa taarifa au bila taarifa...karibu ukae...” Dk. Rwegoshora akasema, wote wakaangua vicheko.
Tayari alishakuwa kama mwenyeji na yeye ndiye aliyemkaribisha mama Genesis kiti.

“Bila kupoteza muda, sisi tumekuja na jambo moja la msingi sana, ambalo tunataka
tujadiliane kama wazazi!” akaanza kusema Dk. Rwegoshora.
“Ndiyo, tunakusikiliza!”

“Sisi ni marafiki wakubwa, familia hizi sasa tumeshakuwa ndugu kabisa, tunaona
ni vyema tutazingunisha kwa ukaribu zaidi!”

“Una maana gani kusema hivyo?”
“Tutakachokiongea baadaye, kinaweza kuwashangaza kidogo, lakini kwa sababu sisi
ni wasomi, najua halitawapa mshtuko mkubwa sana. Bianca amerudi shuleni safari
hii akiwa hana amani kabisa.
“Hana raha na anaonekana mwenye mawazo sana, sisi kama wazazi wake, tukagundua
tofauti ya mwanetu, nikamwambia mama yake azungumze naye. Kweli akaongea naye,

kitu ambacho amemwambia kimetushtua sana, lakini baada ya kutafakari kwa muda,
tukagundua kwamba hakina mshtuko, bali kinahitaji kufanyiwa kazi!” akasema Dk.
Rwegoshora.

“Dokta, maneno yako yamejaa mafumbo sana, kwanini hutaki kwenda moja kwa moja
kwenye hoja ya msingi?”
“Mama Bianca, hebu waeleze!” Dk. Rwegoshora akashindwa kusema na kumtupia mkewe
mpira.

“Waambie wewe!”
“Hapana waeleze tu usiogope mke wangu, hawa ni ndugu zetu, hakuna
kitakachoharibika, waeleze tu!” Dk. Rwegoshora akazidi kusisitiza mkewe ndiyo
azungumze.

Profesa Mshana na mkewe wakabaki na maswali kichwani ambayo hayakuwa na majibu
hakika. Dk. Rwegoshora alikuwa anazunguka sana katika kauli zake. Haikujulikana
alikuwa anataka kusema nini hasa.

Alipoanza kumtupia mpira mkewe wakahisi kuna jambo kubwa zaidi. Mioyo yao ikawa
juu kwa hofu, lakini baadaye Profesa Mshana akaamua kuingilia.
“Kwani ni kitu gani hicho mnashindwa kuongea hadi mnatupiana mpira jamani?”
Profesa Mshana akasema.

“Ngoja niwaeleze ukweli jamani, binti yetu ametokea kumpenda sana kijana wenu
Genesis, kwa hiyo sisi kama wazazi tumeona tukutane na kujadiliana juu ya hili
vizuri!” akasema mama yake Bianca.

“What?” Profesa Mshana akaruka kwa furaha.
“Kweli?” Mama Genesis akauliza.
“Ndiyo ni kweli kabisa!”
“Unaona mama Genesis, mwanao sasa ameshapata mtu anayemfaa siyo hilo li-Farida

lake!”
“Lakini kuna tatizo kidogo, ndiyo maana tumekuja hapa tujaliane!” akasema mama
Bianca kwa sauti ya unyonge kidogo.
“Tatizo gani?” Mama Genesis akadakia.

“Genesis hamtaki kabisa Bianca!”
“Nini?” Profesa Mshana akauliza, akisimama haraka kuelekea sebuleni alipo
Genesis na Bianca.

Je, nini kitatokea? Genesis atamkubali Bianca?
 
SEHEMU YA 08


Farida Mbaraka, mtoto wa Fundi Seremala na Mama Ntilie, anapata bahati ya kusomeshwa katika Shule ya Sekondari ya Mt. Thomas iliyopo Morogoro kwa msaada wa Padri Bartholomayo kupitia Shirika la kusaidia wanawake linalojulikana kwa jina la Women Opportunity Expanded la nchini Italia.

Anahamishwa katika shule aliyokuwa akisoma awali ya Kilakala na kujiunga na shule hiyo. Uzuri wake unakuwa tishio, vijana wengi wanachanganyikiwa, lakini baadaye akanasa kwa kijana Genesis Mshana, mtoto wa Profesa Mshana ambaye alikuwa mmiliki wa Chuo Kikuu cha Global Engineering.

Mapezi yao yanazidi kukua kadri siku zilivyozidi kwenda, lakini baba yake na Genesis hakupenda kabisa mwanaye awe na uhusiano na Farida kwa sababu anatoka familia masikini.

Bianca Rwegoshora binti wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, anahamia katika shule ileile akitokea Uswis alipokuwa akiishi na wazazi wake kikazi. Ghafla anajikuta anampenda sana Genesis, lakini kijana huyo anakataa na anampa sababu kwamba anaye mpenzi wake Farida.

Baada ya kutumia kila mbinu bila mafanikio, Bianca amerudi nyumbani kwao kwa likizo akionekana ana mawazo sana, jambo lililowafanya wazazi wake wamdadisi, akawaeleza ukweli kuwa sababu kubwa ni Genesis.

Kwa kuwa familia hizi mbili ni marafiki, wazazi wa Bianca wanafunga safari hadi nyumbani kwao na Genesis na wanawaeleza ukweli kuhusu binti yao kumpenda kijana wao, lakini pia Genesis haoneshi ushirikiano.

Zilikuwa habari njema sana kwa Profesa Greyson Mshana, baba wa Genesis, lakini alichukia sana kusikia kwamba, Genesis alikuwa hataki kuwa na Bianca. Haraka akaamka kitini akitaka kutoka kwenye chumba cha mazungumzo ili akazungumze na Genesis!
Je, nini kitatokea? Wazazi watafanikiwa kuwaunganisha vijana wao? SONGA NAYO...

KWA Profesa Mshana ulikuwa ushindi mkubwa, siku zote alipinga kabisa mwanaye kuwa na uhusiano na Farida, ambaye kwake hakuwa na thamani kabisa. Alimchukia Farida kutokana na familia yake kuwa duni.

Siku zote alitamani mtoto wake aoe msichana ambaye kwao wana uwezo mkubwa kifedha na wasomi, wenye majina makubwa nchini. Dk. Rwegoshora na mkewe walikuwa na ujumbe mzuri sana kwake.

Hakutaka kusikia suala la kipingamizi kutoka kwa Genesis, hoja ya kumkataa aliitupilia mbali na hakutaka kabisa kuelewa.
Tayari alikuwa ameshasimama na kuanza kutoka chumba cha mkutano kwa ajili ya kumfuata Genesis sebuleni.

Hasira yake ilikuwa haipimiki hakika. Dk. Rwegoshora aliweza kuona tofauti aliyokuwa nayo mzee mwenzake, hakutaka jambo hilo litumiwe nguvu nyingi kiasi kile, akasimama haraka na kumfuata Profesa Mshana, kabla hajafika kwenye mlango mkubwa wa kuingilia sebuleni akamshika bega.

“Vipi?”
“Hebu rudi kwanza!”
“Kwanini?”
“Njoo kwanza tuzungumze!”

“Hapana, nataka kwenda kumuita Genesis ili tuone kama anaweza kukataa mbele yetu wote!”
“Mzee mwenzangu, sisi ni wasomi, mambo mengine tunatakiwa kutumia akili za kawaida tu. Hebu twende tukashauriane kwanza!”
“Sawa!” Profesa Mshana akaitika na kukubali kurudi tena kwenye chumba cha mkutano.

“Keti kwanza mume wangu, tusikilize mawazo yao!” Mke wa Profesa Mshana akasema.
“Ndiyo maana nimekuja mke wangu.”

Profesa Mshana akaketi kwenye kiti kimya, macho yake yakiwa kwa Dk. Rwegoshora na mkewe, ambao walishangaa kuona jinsi alivyopokea taarifa zile kwa shangwe kubwa.

“Sikilizeni wazee wenzangu, hapa tunazungumzia jambo jema na lenye manufaa kwa wanetu na hata familia kwa ujumla wake!” akasema Dk. Rwegoshora.
“Hujakosea kitu,” akajibu Profesa Mshana.

“Sasa hatutakiwi kufanya mambo kwa haraka au kutumia nguvu!”
“Ni kweli, lakini wakati mwingine mambo yaliyo ndani ya uwezo wetu yakionekana yanakuwa magumu, tunapaswa kutumia hata nguvu!”
“Hapana sisi ni wasomi bwana, tunapaswa kutumia zaidi hekima kuliko nguvu!”

“Wewe ulipanga kufanya nini?”
“Hilo sasa ndiyo jambo la kujadiliana. Huyo Farida mnayemsema hata Bianca ametueleza, lakini ipo dawa nzuri sana ya kuwaachanisha hawa watoto!”

“Enhee!” akadakia mama Genesis.
“Kwanza kabisa, Genesis anatakiwa kushauriwa na ninyi wazazi wake kuhusu ubaya wa kuwa na Farida na umuhimu wa kuwa na Bianca, kama ataonekana kukubali kuwa na Bianca, kama akikataa ipo njia nyingine!”

“Njia gani?” Profesa Mshana akauliza.
“Mkubalieni aendelee naye!”
“Aendelee naye?”
“Ndiyo!”

“Hapana, siwezi kuruhusu yule karagosi aje kuharibu familia yangu, sitaki kuchafua sifa ya familia yangu!”
“Hawezi kufanya hivyo, kuna kitu cha kufanya baada ya hapo!”
“Ni nini?”

”Hapo tutapanga mipango yenye akili, kwanza tutamwambia Bianca awe naye karibu sana, lakini kama rafiki yake wa kawaida, halafu Genesis apewe sharti moja; ili aweze kumuoa huyo Farida, lazima afaulu vizuri mitihani yake ya mwisho akiwa na alama za kuendelea na Elimu ya Chuo Kikuu!”

“Akifaulu sasa itakuwaje?”
“Hawezi kufaulu kama Bianca atakuwa karibu na Genesis, kinachofanyika hapo ni Bianca kumsumbua Farida kiakili, hawezi kufurahishwa na ukaribu wao na hata kama akimuuliza Genesis bado atamwambia kwamba hana uhusiano naye.

“Jambo lingine, Bianca anatakiwa kupandikiza watu ambao watakuwa wanamtumia ujumbe Farida na kumdanganya kwamba Genesis na Bianca wana uhusiano, hayo yanatosha kabisa kumchanganya akili Farida na hivyo kufanya vibaya kwenye mitihani yake ya mwisho. Kuna nini tena baada ya hapo?” akauliza Dk. Rwegoshora.

Wakati akianza mazungumzo yake, wote walionekana kuwa na wasiwasi na mpango wake, lakini alipomaliza kuzungumza, kila mmoja alikuwa akitoa tabasamu mwanana usoni mwake, wakimaanisha kwamba wamekubaliana na wazo lake.

“Wazo zuri kabisa shemeji,” akasema mama Genesis.
“Safi sana,” Profesa Mshana akasema.
Wote wakakubaliana kwa kauli moja. Kilichondelea hapo ikawa ni kuburudika na vinywaji kabla ya baabaye kuhamia sebuleni. Walishinda pamoja siku hiyo, hadi saa 10:30 za jioni ndipo walipoondoka kurudi nyumbani kwao.

****
Siku hiyo Genesis hakutoka kabisa, pamoja na kwamba alikuwa na safari zake, lakini alilazimika kuzikatisha baada ya baba yake kumwambia kuwa alikuwa anahitaji kuzungumza naye.

Wakiwa sebuleni, Genesis akamkumbusha baba yake. Alitamani sana kujua sababu ya kuzuiwa kuondoka kabla hajazungumza naye. Ni kweli alijua jambo alilotaka kuzungumza baba yake halikuwa zuri, hilo aliweza kugundua kutokana na ukweli kwamba wakati baba yake akimzuia kuondoka, sura yake ilikuwa imejaa makunyanzi, hilo lilitosha kabisa kudhibitisha kwamba hakukuwa na amani!

“Baba ulisema unataka kuzungumza na mimi!”
“Ni kweli mwanangu,” tofauti na matarajio yake, baba yake akajibu kwa sauti ya upole sana.
“Sawa baba, nakusikiliza.”
“Unaamini kuwa mimi ndiye baba yako?”

“Naamini baba.”
“Kweli?”
“Ndiyo, kwani vipi?”
“Kwanini hutaki kunisikiliza?”
“Unazungumzia juu ya Farida?”

”Ndiyo!”
“Kwa nini lakini baba humpendi Farida?”
“Sababu zipo nyingi, hata wewe unazifahamu!”
“Lakini baba, siamini kama vigezo vya fedha na mali ni muhimu katika uchaguzi wa mke.”

“Unaweza usione umuhimu leo, lakini kesho ukaona, muda ambao tayari utakuwa umeshachelewa, sikiliza nikuambie...unaonaje kama ukiwa na msichana mzuri, mwenye tabia njema na anayetoka kwenye familia bora kama wewe?”
“Ndiyo nani huyo?”

“Bianca naona anaweza kukufaa zaidi kuliko huyo Farida.”
“Hapana baba, nakupenda sana na ninakuheshimu sana mzazi wangu, lakini naomba sana ukubali kusikiliza hisia zangu. Nipe nafasi ya kuamua baba, unajua suala la mke ni la milele, si la kufanyia majaribio, kwangu mimi Farida si mwanamke wa majaribio, natamani awe mke wangu kwa sababu nampenda.”

“Kweli unampenda Farida?”
“Sana baba.”
“Una uhakika na unachoongea?”
“Kwa asilimia mia moja!”

“Sawa, vizuri. Mimi sitaweza kutumia kofia yangu ya u-baba kukulazimisha uachane na Farida, nimetumia nafasi yangu kukushauri kama mwanangu, lakini mwamuzi wa mwisho ni wewe.”
“Ni kweli baba, naomba niruhusu niendelee na Farida.”
“Ok! sawa, hilo nimekubaliana nalo.”
“Ahsante sana baba kwa kukubaliana na mimi.”

“Lakini kuna kitu kimoja unatakiwa kufahamu Genesis, bado sijadhirika moja kwa moja na huyo Farida, sasa ili angalau aweze kuwa na sifa ya kuingia katika familia yangu, lazima afaulu vizuri mitihani yake ya mwisho na apate pointi zitakazomwezesha kuingia Chuo Kikuu,” akasema Profesa Mshana akimwangalia mwanaye usoni.

“Hiyo rahisi sana baba, nakuahidi itakuwa hivyo na kama akifeli, basi nitakubali kwa moyo mmoja kuachana naye,” Genesis akasema kwa kujiamini.

Aliujua vizuri sana uwezo wa Farida hakuwa na mashaka kuhusu kupata daraja la kwanza, lilikuwa sharti jepesi sana kwake. Hakujua kichwani mwa baba yake kulikuwa na nini. Mpango uliokuwa umepangwa kwa kushirikiana na wazazi wa Bianca hakufahamu kabisa.

Genesis akafurahishwa sana na uamuzi wa baba yake, alichokifanya ilikuwa ni kukimbia chumbani kwake haraka kisha akachukua simu yake na kumpigia Farida.

“Vipi mpenzi wangu, mbona unahema sana?” Farida akamwuliza Genesis mara baada ya kupokea simu.
“Nina habari njema!”
“Umeokota pesa?”

“Bwana acha utani wako, sijaokota pesa, ila ninazo habari njema sana!”
“Ni nini?”
“Kwani huwezi kupata Division One katika mtihani wako wa mwisho?”
“Swali gani hilo Genesis?”

“Jibu kwanza, nina maana yangu.”
“Sijaona kikwazo cha kunikosesha Div One!”
“Basi huo ndiyo mtihani wako wa mwisho wa kuwa na mimi, baba amesema hana tatizo tena na uhusiano wetu, lakini lazima upate One ili uingie Chuo Kikuu, si unajua tena wazee wangu wanavyopenda wasomi?”

“Mtihani mdogo sana huo.”
“Kweli mpenzi wangu?”
“Genesis unajua uwezo wangu darasani, katika hilo sitakuangusha kabisa, usijali mpenzi wangu!”

Walikuwa na furaha sana, wakiamini baada ya matokeo ya mtihani wa mwisho wangepewa baraka zote na wazazi wa Genesis. Wakati hayo yakiwa vichwani mwao, hawakujua kwamba kulikuwa na mkakati mwingine mzito wa kuzima mipango yao. Hilo hawakulijua kabisa.

Je,nini kitatokea? Mipango ya wazazi wa Genesis na Bianca itazaa matunda?
 
Nifah Divine... glory to yhwh BansenBurner Alisen Papushikashi Magazine Fire miss chagga SANCTUS ANACLETUS mngony Excel Mussolin5 Jimena Inferiority Complex gwijimimi wambura marwa Hoshea shareef conscious wambeke The Boss Deejay nasmile gkileo Juma chief Mangi flani hivi Ngongo makaveli10 KENZY kadada wa pili Root aretasludovick jonnie_vincy Clkey KAFA.cOm mbewe makedonia Afande Nyati peterchoka Leonard Robert Nchi Kavu STUNTER Chrizo jully Van persie Khalidoun Tetramelyz punje haradari Mazigazi @Alybaba babu na mjukuu platozoom jimmyfoxxgongo Nicodemas Tambo Mwikozi @Ls man Heaven Sent sifongo Infantry Soldier haa mym 20acres MTS MarkHilary compos Tembo2 Erick the future nancy1983 Bulah binsaad @Fazzaly the wolf everhurt Melvine Mgibeon kijana wa leo samsun Coolant Jagood pacesetter apologize payton George Betram kisengeli Kiranga Jiwe Linaloishi Madame B jay john Guasa Amboni Dinazarde Analyse Diva Beyonce snowhite Mmanu Expected Value onechromosome Missy rose Innocenthezron Immortal_MH Ficus sunola Robot la Matope mamaafacebook II JEKI likikima Compact scorpio me G'taxi YNWA adna yuzo ntamaholo Otorong'ong'o naan ngik-kundie kandukamo1 AFRICA101 mwalidebe Kobe Blaki Womani kalendi savius The Great Emanuel r2ga Ntaluke.N. Transcend Msemachochote Mchumiajuone mwampepec MTOTO WA KUKU Fukara proto cute kawombe zinginary MLALUKO JR Vupu barafu BlackPanther Ntuzu Matola impongo ntamaholo Mkoroshokigoli Deadbody KING easy mahoza Msolo kkenzki deborah1 KIDUDU buffalo44 winlicious riziki Allys MUHUNZI Moses2015 nacktary Liuumi dochivele Renzo @barbers hmjamii mbere TATIANA famicho LUCKDUBE mwanadome Straton memphis ghazar Graph Theory Honey Faith Shunie Slave ddcmanesto zinginary pacesetter Nkanaga KOMUGISHA mikatabafeki johnsonmgaya lee empire wigo MJINI CHAI Asprin mtzmweusi Erasto kalinga Chrizo kichakaa man LULU bike FORTALEZA poleni shibumi ZE DONE umande Edger Sr sir joshua sammoo Roram Password Bavaria hambiliki mwanangu Asili100 Evarist Massawe nice1 Jumong S Rogie 1babake nasreen uberito baest dustless Kilemachocho Tumosa mtembea kwa miguu debbs Joe scorpnose musacha shibumi seeker of knowledge Simuchi Veni Vidi Vici TUJITEGEMEE abuu garcia Hon Nkundwe Festo Festo marion09 mike2k The dream bro kay vandelintz kirikou1 POINT LOAD lusaka city Dirham Rodcones bato MANCNOO @multiphill90 GEORGE Dalali mwanamalundi90 MwaFreeca Roram Ta-kibombo troublemaker mambo KOMUGISHA calabocatz Papaa Azonto Msemachochote Mdomo bakuli tizo1 option dikembe iL Buono fakalava ABDUL KAREEM @Gobe Justine Marack Goodluck Mchika MR UNINFORMED darcity nkasoukumu nG'aMBu thatonegAl kabanga MPARE KIBOGOYO Edward Sambai Rassa mnonje srinavas last king of uscoch proto cute Kennedy krava Rais2020 kbosho Mzee wa BsN sam2000 fuma 999 Bableee dawa yenu The Certified DON SINYORI mij adden
bwii ONTARIO Kobe The Vein @Mondray jaxonjaxon successor mzee wa liver sawariya SITAKI ukuda Domhome Mpatanishi MKANDAHARI mtugani wa wapi huyo wealthier cluecell Toyota escudo mgumu2 troublemaker Linamo @shedede kamtu33 SteveMollel Ngushi DONALD stewart Mshuza2 Glycel mnonje Ochuanilove SingleFather Santi DEOD 360 Ngushi anatory antony ukhuty chris van chicha auxillius Goma Son Hubeb pes KING DUBU VILLAIN mwayena donbeny Aleppo JipuKubwa shoo61 BOMBAY John mungo Nyakageni bato Dogo 1 sufra chamlungu painscott wegman Bravo Engliash MOSELBAY wa stendi FaizaFoxy bigmind cadabraa Internal Kelvin mwalukas mnonje Kelvin X Somoche Wgr30 Miiku Poise Jabman kalamuyamwalimu BOMBAY the say juxhb witnessj Gide MK Mmanyema mgogoone Mnongane Mandingo koncho77 afsa ngaboru Paradoxer Heavy Metal KIMBURU 06 Raaj kichekoh ngumba njeche kikale DullahTza Goodluck Mshana julius Darcy Denis Kasekenya mashonga kitalembwa Khaleed Shaban middle east SirChief jiwe jeusi Mkambarani mansakankanmusa gambada ynwa ney kush
 
SEHEMU YA 09


Uwezo duni wa familia ya Farida ndiyo unaotaka kumnyima mwenzi wa kweli wa maisha yake. Farida anapata wakati mgumui sana kuwa na Genesis mtoto wa Profesa Mshana ambaye aliamini fedha, mali na elimu ni msingi imara wa maisha ya binadamu.

Maisha mazuri aliyonayo pamoja na fedha ndivyo vilivyompa kiburi cha kuwaza hayo yote. Familia mbili zenye uwezo mkubwa kimaisha, Bwana na Bibi Rwegoshora na Bwana na Bibi Mshana wanakutana katika kikao kupanga namna watakavyowakutanisha watoto wao.

Sharti kubwa limewekwa: iwapo Genesis anataka kumuoa Farida basi lazima afaulu vizuri mitihani yake ya mwisho ya kidato cha sita na kupata nafasi ya kwenda chuo kikuu, jambo ambalo Genesis hakuwa na wasiwasi nalo kabisa.

Tayari ameshamwambia Farida ambaye ameahidi kwamba ataweza kufanya vizuri ili waoane.
Je, itawezekana? Nini kitatokea katika njama walizopanga familia hizo mbili? SONGA NAYO...

FURAHA ilitawala mioyoni mwao, wakiwa na uhakika wa asimilia mia moja kwamba walikuwa wanaelekea kukamilisha malengo yao ya kuishi pamoja katika ndoa takatifu. Suala la Farida kufaulu halikupewa nafasi kabisa katika akili zao, Genesis aliufahamu vizuri sana uwezo wa Farida, kwa hiyo ilikuwa tiketi ya moja kwa moja!
“Umenifurahisha sana mpenzi wangu!”
“Au huamini?” Farida akamwuliza.

“Huenda kuna maeneo mengine naweza nisikuamini, lakini si katika masomo, natambua uwezo wako mpenzi wangu, ila nakuomba usibweteke na usiniangushe tafadhali, unajua huo ndiyo utakuwa mtihani wetu wa mwisho.

“Wewe ndiye mwamumuzi wa kuniangusha au kunifanya niwe nawe milele,” akasema Genesis kwa sauti ya utulivu.
“Kwani Genesis, hatuna mambo mengine ya kujadiliana?”
“Kwa nini umesema hivyo?”

“Maana naona tunajadili kitu ambacho tayari kina ufumbuzi wake, kama ni bajeti ni kama imeshapitishwa, sasa wasiwasi wa nini?”
“Sawa basi kama ndivyo, kesho vipi tunaonana?”
“Kama kawaida tukutane tution.”

“Centre gani?”
“Mapambano.”
“Sawa, unajua bado sijawa sawa kwenye namba, kwa hiyo lazima nikaze zaidi,” akasema Genesis.

“Sawa, kesho basi!”
“Poa, wasalimie wazee huko.”
“Nawe pia.”

Genesis alifurahi sana ndani ya nafsi yake, lakini alikuwa hana hata ndoto ya mipango ambayo ilikuwa jikoni. Mipango ambayo kama ingetimia, basi yeye na Farida wangebaki na historia tu kwamba waliwahi kuwa wapenzi lakini si kwa kuingia kwenye ndoa.

***
Ni saa kumi na moja na dakika kadhaa za jioni, Bianca alikuwa anaingia kutoka katika mizunguko yake, mama yake alikuwa amekaa sebuleni akiangalia filamu mpya iliyotoka wiki hiyo.

Bianca alipita kimya, maana hakugeuza macho yake kumuona mama yake aliyekuwa amekaa kwenye sofa dogo kwenye moja ya kuta katika sebule ile ya kifahari.

“Bianca, huna macho kabisa mwanangu!” mama yake akasema akicheka.
“Samahani mama sijakuona kabisa!”
“Vipi za tution?”
“Nzuri mama, shikamoo!”

“Marhaba mwanangu, enhee vipi mambo yako mengine?”
“Ninayo mama, kwanza naona huku uraiani kumenichosha sasa, natamani sana kurudi zangu shule!”

“Tena umenikumbusha, hebu keti hapo nizungumze na wewe kidogo!”
Bianca hakupoteza muda, akaweka begi lake pembeni na kuketi kwenye kiti kimya tayari kwa kumsikiliza mama yake.

“Wiki ijayo unarudi shule, si ndivyo?”
“Ndiyo mama.”

“Kwanza kabisa nakupongeza kwa ujasiri wako wa kuwa mkweli kwangu kama mama yako, lakini pia napenda kukufahamisha kwamba, mimi na baba yako tunaunga mkono kwa asilimia mia moja uhusiano wenu wewe na Genesis.

“Kikubwa ambacho tumeshawishika nacho ni namna familia yao ilivyo bora, yenye malezi mazuri na hata historia yao pia inaridhisha. Tusingependa kuona unakuwa na watu wa uchochoroni, wahuni na wasio na mbele wala nyuma, kwa hiyo sisi tunakubaliana moja kwa moja na uchaguzi wako.”

“Ahsante sana mama, nimefurahi sana kusikia hivyo, lakini mama unadhani itaweza kuwa rahisi kama mtu mwenyewe ndiyo huyo hanitaki?”

“Kwa nini isiwezekane mwanangu? Tayari hatua ya kwanza imeshapita, sisi kama wazazi tumekaa na kukubaliana kwa pamoja, kwa hiyo wote lengo letu ni kuwaona mkiwa pamoja.

“Hatua ya pili ndiyo ya wewe kuhakikisha Genesis na huyo msichana wake hawana maelewano, mbona kazi ndogo sana mwanangu, ambayo ndiyo iliyobakia mikononi mwako? Sisi tutakuwa tayari kutoa chochote unachohitaji ili kukamilisha hili zoezi. Tunachohitaji kusikia ni Genesis amekubali kuwa na wewe baasi!”

“Sawa mama, nakuahidi!”
“Vizuri sana, unaweza kwenda chumbani kwako sasa!”

“Ahsante mama, leo nini?”
”Nini zaidi ya wali? Si unajua dada anavyopenda kutupikia wali kila siku, lakini hajapika nyama za mchuzi, amekaanga!”

“Afadhali, ngoja nikabadili nile halafu niangalie ratiba nyingine.”
“Sawa mwanangu.”
Bianca akapiga hatua za taratibu kuelekea chumbani kwake, mama yake akamsindikiza kwa macho akitabasamu.

***
Mawimbi yalikuwa yanapiga kwa kasi sana katika ufukwe wa Bahari ya Hindi. Macho yao yalikuwa baharini, wakiwa wameshikana mikono huku wakitembea taratibu kabisa.

Zilibaki siku tatu tu kabla ya kurejea tena shuleni, ambapo walikuwa wanakwenda kuingia kidato cha sita. Wapo katika Hoteli ya Chadibwa iliyopo nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam, eneo la Kigamboni. Wote wana furaha sana ya kuwa pamoja.
“Bado siku tatu turudi shule mpenzi wangu,” Genesis akamwambia Farida.

“Nafahamu hilo mpenzi wangu.”
“Unatakiwa kufahamu kwamba ni kipindi chako cha mwisho cha kuonesha uwezo wako wote ili ufanye vizuri.”
“Nalitambua hilo!”

“Kama ndivyo nimefurahi mpenzi wangu, lakini samahani kwa hili nitakalokuambia.”
“Nini?”

“Hatutekwenda pamoja shuleni kipindi hiki!”
“Kwanini?”
“Baba amesema niongozane na Bianca.”

“Kwa nini?”
“Si unajua wale ni rafiki wa baba yangu, kwa hiyo inawezekana wameamua kukwepa gharama kama wazazi!”

“Lakini nina mashaka sana mpenzi wangu, sina amani kabisa na wewe.”
“Farida unaweza kukosa imani na mimi kweli mpenzi wangu? Sasa kama utashindwa kuniamini mimi utamuamini nani mwingine?”

“Nimeona nieleze hisia zangu, sipendi kulalamika ndani kwa ndani wakati naweza kukuambia Genesis, jambo la msingi ni kuhakikisha unakuwa salama, sitaki unitese mpenzi wangu, sitaki kusalitiwa Genesis, unajua ndani ya moyo wangu ninavyokupenda, sitapenda kukupoteza,” Farida alizungumza kwa hisia kali sana za mapenzi akiwa anamaanisha alichokuwa akizungumza.

“Niamini mimi mpenzi wangu.”
“Nakuamini dear.”
Kilichofuata hapo ilikuwa ni kuingia kwenye maji na kuanza kuogolea, penzi lao lilikuwa la dhati kabisa, likitoka katikati ya mioyo yao!

“Genesis nakupenda sana.”
“Najua mpenzi, nakupenda pia.”
Jioni, Genesis alimrudisha Farida nyumbani kwao Kwa-Azizi Ally kisha akarudi nyumbani kwa Masaki.

***
Gari aina ya Toyota VX, jeupe liliegesha katika nyumba ya Profesa Mshana, Masaki. Dereva hakushuka, alipiga honi tu, Genesis akajua alichotakiwa kufanya. Akaburuza begi lake hadi kwenye gari akisindikizwa na dada yake.
“Masomo mema na safari njema,” akamwambia.
“Ahsante dada, mbaki salama!”

“Usijali...Bianca mambo?”
“Poa,shikamoo dada!”
“Marhaba, mnatakiwa kusoma kwa bidii, sawa wadogo zangu?”
“Sawa.”

Genesis akaingia kwenye gari na kuketi siti ya nyuma aliyokuwa amekaa Bianca. Hakumsemesha neno lolote baada ya kuingia kwenye gari zaidi ya kuegemea kiti kimya kabisa.

Mawazo yake yalikuwa kwa mpenzi wake Farida, ambaye alikuwa ana uhakika kabisa kwamba alikuwa amepanda basi. Hakutaka Farida ateseke wakati yeye alipanda gari binafsi tena la thamani kubwa.

Mpaka wanafika Ruvu hakuna aliyefungua mdomo wake kusema chochote, muda wote Genesis alijifanya anasinzia. Bianca alivumilia lakini alishindwa, akaona ni vyema aanzishe mazungumzo.

“Genesis, mbona upo kimya sana?” Bianca akauliza.
“Hapana, mambo mengi!”
“Una mambo gani wakati unakula, kulala na kila kitu unapata bure kutoka kwa wazazi wako?”

“Hata kama ni hivyo Bianca, lazima utambue kwamba hakuna binadamu ambaye hawazi, hata kichaa naye huwaza. Kwanini mimi nisiwe na mawazo yangu kichwani?”

“Basi umeshinda!”
“Kwani tulikuwa kwenye mashindano?”
“Mh! Mbona umekuwa mkali? Samahani kama nimekuudhi, lakini haikuwa nia yangu!”

“Ok!”
Walikuwa wanazungumza taratibu sana, ingawa walitofautiana. Hawakutaka dereva ajue kwamba walikuwa wana tofauti, walitaka hilo libaki kuwa siri yao wenyewe.

Kwa mwendo wa dereva yule, waliweza kuingia Morogoro, saa mbili na nusu baadaye, kisha wakaanza safari ya kwenda nje kidogo ya mji wa Morogoro ilipo shule ya Sekondari ya Mtakatifu Thomas ambapo iliwachukua robo saa tu kufika.

Wakashusha mizigo yao na kuondoka,dereva akawasha gari na kurudi Dar es Salaam, kila mmoja akaendelekea bwenini kwake.

***
Genesis hakutegemea kukutanisha macho yake na Farida darasani asubuhi hiyo,mpaka jana yake usiku wa saa tatu, Farida alikuwa hajaingia shuleni, hata alipojaribu kumpigia simu yake hakupatikana.

Hakutegemea kabisa kumuona Farida, alishindwa kuelewa Farida alikuwa ameingia shuleni muda gani. Kitu cha kushangaza ambacho hakutarajia kabisa ni kwamba, kila alipokuwa akikutanisha uso wake na Farida, alionekana kuwa na hasira.

Matuta yalikuwa yanaonekana usoni mwake, kuashiria kwamba kulikuwa na tatizo. Hakuna kitu kilichoingia kichwani mwa Genesis hadi kipindi kinaisha, alikuwa anatamani kujua mpenzi wake alikuwa na tatizo gani. Haikuwa kawaida ya Farida kuwa katika hali ile.

Kipindi cha pili kikaanza na cha tatu, kisha kengele ya mapumziko ikalia. Kama kawaida wanafunzi wakatoka na kwenda kwenye mgahawa wa shule kwa ajili ya kupata soda. Genesis hakuwa na muda huo, alitamani sana kujua kilichompata mpenzi wake.

Alivyotoka tu, nje kazi yake kubwa ilikuwa kumtafuta Farida, alitamani sana kujua kilichokuwa kikimsumbua. Baada ya kumtafuta kwa muda mrefu bila mafanikio na kuwauliza baadhi ya wanafunzi, aliweza kumuona akiwa amejibanza kwenye mjohoro akionekana kuwa na huzuni sana.

Genesis akapiga hatua za haraka hadi alipokuwa, akamshika mkono kwa upendo na kuanza kumhoji ili ajue kilichokuwa kikimsumbua.

“Farida una nini, mbona unaonekana hauko sawa?” Genenesis akauliza.
Tofauti na matarajio yake, Farida hakumjibu kitu, zaidi alimsukuma pembeni, akionekana kuwa na hasira.
“Kuna nini tena Farida?” Genesis akauliza akiwa ameyatoa macho kwa mshangao.

“Najua kila kitu, hakuna utakachonidanganya. Nenda kaendelee na Bianca wako!”
“Nani?”
“Hujasikia au?”

Genesis akiwa bado yupo katika hali ya mshangao sana, akamuona Bianca akielekea eneo lile, akitembea kwa maringo, sura yake ikiwa imepambwa na tabasamu mwanana. Alipowafikia, alionekana kumfuata Farida aliyekuwa amesimama kwa hasira, lakini cha ajabu Bianca alikuwa na tabasamu pana usoni. Wote wakatahayari!

Je, nini kitatokea? Bianca anataka kumfanya nini Farida? Nini mwisho wa ugomvi huu?

NISINGE PENDA KUWAONA WANYONGE LEO WACHA NIWAONGEZE KIDOGO ENDELEA NAYO


TABASAMU la Bianca liliongezeka, akaendelea kupiga hatua za taratibu kumfuata Farida. Alipomfikia akashika mkono wake mmoja na kumgeuza ili waangaliane.

“Habari yako Farida?” Bianca akasalimia akibenua midomo yake kwa dharau za wazi kabisa.

Farida alikuwa kimya akimsikiliza, hakutaka kufunua kinywa chake kuzungumza chochote, ndani ya nafsi yake aliweza kugundua kabisa kilichoendelea. Hakutaka ushahidi zaidi ya ule, alikuwa na uhakika kabisa kwamba Bianca alikuwa akitoka na Genesis.

Genesis alikuwa kimya akiwaangalia bila kupata majibu. Ni muda mfupi tu uliopita, Farida alimsukuma akidai kwamba ana uhusiano na Bianca, halafu muda mfupi baadaye Bianca anatokea, kidogo lilimpa mashaka.

“Nakusalimia shoga yangu Farida,” Bianca akasema tena, safari hii akimtingisha.
Hapo akazidi kupandisha hasira za Farida, lakini hakutaka vurugu, alijua ni kiasi gani kama angefungua kinywa chake kusema chochote ugomvi mkubwa ungeibuka kitu ambacho hakutaka kabisa kitokee.

“Miss St. Thomas, unasalimiwa jamani, kwa nini hutaki kuniitikia, kwani nina kosa gani kwako jamani?” Bianca akasema akizidisha kejeli.

“Nilisema nini Genesis, nilikuambia nini? Sasa naanza kufanyiwa fujo na wewe upo kimya, unanithibitishia upuuzi wako mbele yangu!” akasema Farida kwa hasira machozi yakianza kumwagika machoni mwake.
Genesis ni kama alinasuliwa kutoka kwenye shoti ya umeme, maana baada ya hapo akaonekana kusogea haraka na kuwafuata walipokuwa wamesimama, akamshika Bianca.

“Nini kinaendelea Biaca?” Genesis akauliza.
“Acha ujinga bwana, yaani hujui kinachoendelea?”
“Nini?”
“Hujui?”

“Bianca, mimi sihitaji matatizo na watu na wewe unatambua hilo na nilishakueleza kabisa kuwa sipendi matatizo na watu, sasa kwa nini wewe unataka kunitibua?” Genesis akasema akionekana kuwa na hasira.

Farida hakumwelewa, alihisi kama alikuwa anaongea kwa kumridhisha, muda ule ule akatoka mbio na kuwaacha Genesis na Bianca wakiwa wamesimama pale.

“Faridaaaa....” Genesis akaita lakini Farida hakugeuka nyuma.
“Umefanya nini?” Genesis akamwuliza Bianca.
“Kwani nimefanya nini jamani Genesis, kuna kitu umeona nimefanya hapa kwa muda wote huo uliokuwa hapa?”

“Mbona Farida amekimbia?”
“Labda nikuulize wewe!”
“Kwani ulivyokuja hapa umemwambia nini hasa?”
“Nini tena zaidi ya kumsalimia?”

“Lakini analalamika kwamba eti anasikia mimi natembea na wewe. Nani ambaye anasambaza hizi habari za kizushi?”
“Kwani ni kweli tuna uhusiano?”

“Hatuna.”
“Unadhani mimi naweza kutangaza uhusiano hewa na wewe?”
“Nashindwa kuelewa hapo sasa Bianca.”

“Kwa nini Farida hajaitikia salamu yangu?”
“Nikuulize wewe!”
“Mbona unashangaza sana, mimi nimekukuta naye, kwa kuzingatia ustaarabu nimekwenda kumsalimia, tena wewe ukisikia. Sasa kosa langu hapo ni nini?”

Genesis akashindwa kuelewa kabisa, kwa kumtazama Bianca usoni, aliweza kugundua kwamba huenda kulikuwa na mchezo uliokuwa ukichezwa bila yeye kujua, lakini akashindwa kuufahamu na kumhusisha moja kwa moja!

“Kuna nini lakini? Mbona sielewi?” akajisemea mwenyewe moyoni mwake na kuondoka bila kumuaga Bianca.
“Kuna nini Genesis?” Bianca akauliza.
Genesis hakujibu zaidi ya kuendelea kutembea kwa kasi kurudi zake darasani.

***
Baada ya Bianca kuachana na Genesis waliposhuka kwenye gari wakitokea nyumbani, Bianca alipeleka mabegi yake bwenini kisha akaitisha kikao kifupi na marafiki zake watatu.

Hakuna aliyekuwa akijua sababu ya kuitwa, lakini wote waliitikia wito kwa sababu Bianca alikuwa rafiki yao mkubwa. Hakikuwa kikao rasmi sana, maana walitafuta sehemu moja bwenini kwao na kujikusanya!

“Hakuna asiyefahamu kwamba ni kwa kiasi gani natafuta mbinu za kuwa na Genesis,” ndivyo alivyoanza Bianca.
“Ni kweli!” Latifa akasema.
“Pia wote mnatambua kwamba, anayemzuzua ni Farida.”

“Ni kweli kabisa,” Grace naye akaitikia.
“Josephine...” Bianca akaita.
“Wewe ndiye unayefahamu vizuri zaidi jinsi ninavyokulalamikia kuhusu Genesis.”

“Ni kweli Bianca,” Josephine akajibu.
“Sasa ni kwamba nimeshapata kitu cha kufanya, lakini sitaweza kufanya mwenyewe, nahitaji sana msaada wenu. Mpaka sasa hivi Farida hajaja shuleni, ninavyojua atakuja hata kama atachelewa, lakini lazima atakuja.

“Anatakiwa akute hali ya hewa imechafuka kabisa. Akutane na tetesi kwamba mimi na Genesis ni wapenzi. Watu wa kusambaza huu uvumi ni nyie na mnatakiwa pia akija, kila mmoja kwa wakati wake anamzonga na kumpa habari hizi za uongo ambazo hatazipenda na atagombana na Genesis, wakati yeye akigombana na Genesis, mimi najisogeza karibu na Genesis na kujifanya rafiki mwema kwake, hiyo ni nafasi yangu ya kuwa naye.

“Kingine mnatakiwa muanze kunifuatilia, nikiwa nazungumza na Genesis mnipige picha, tena mimi nitajitahidi sana kuwa naye karibu na kufanya mambo yanayoashiria mapenzi. Sasa akija mkizungumza naye, akawa haelewi au hataki kukubali mtakachomwambia, mnampa ushahidi wa picha. Naamini nimeeleweka vizuri rafiki zangu,” Bianca aliwaambia rafiki zake ambao walionekana kumsikiliza kwa makini sana.

“Tumekupata vizuri sana Bianca, kwa upande wangu mimi naona nimekuelewa vizuri sana, sijui kwa wenzangu!” Josephine akasema.
“Nimekuelewa pia,” Latifa akasema.
“Grace?” Bianca akamwuliza.

“Nimekupata.”
“Basi, kazi ianze.”
“Poa,” wote wakaitikia na kugongeana mikono kwa ishara ya kukubaliana na kila walichojadiliana katika kikao kile.

***
“Lakini kwa nini unanichukia kiasi hicho Genesis?” Bianca alikuwa akimwambia Genesis usiku wa siku waliyoingia shuleni wakitoka likizo.
“Sijawahi kukuambia nakuchukia, nilikuambia sitaweza kuwa na wewe kwa sababu tayari nina mpenzi wangu, mbona jibu jepesi sana na lipo wazi kabisa.”

“Sawa lakini picha uliyoionesha wakati tukiwa njiani, sikuipenda kabisa.”
“Picha gani?”
“Ulikuwa kimya muda wote na hata ulipoongea, ulinisema kwa kifupi sana, sijui ni kwa nini hunipendi Genesis.”

“Unaniwazia tofauti sana na nilivyo, lakini kwa suala la mapenzi ni kweli kwamba sitaweza kuwa na wewe!”
“Urafiki wa kawaidia je?”

“Bila hata kusema, tayari sisi ni marafiki au wewe unaonaje?”
“Sawa kama ni hivyo, maana nilikuwa roho juu mwenzio!” Bianca akasema kwa sauti iliyojaa mahaba huku akizidi kujisogeza karibu na Genesis.

Aliendelea kufanya hivyo mpaka walivyokaribiana kabisa, Genesis akashtuka sana. Alihisi mwili wake kulipuka ghafla kwa hisia kali za mapenzi, hakuzoea kabisa kusogeleana na mwanamke kwa ukaribu kiasi kile.

Alihisi chuchu za Bianca zikimchoma kama msumari mwilini mwake, akasisimka kupita kiasi. Akamsogeza pembeni haraka.
“Vipi Genesis?”
“No! Sitaki!”

“Hutaki nini?”
“We kwani unataka kufanya nini?”
“Nataka nikupe zawadi Genesis!”
“Zawadi ya nini?”
“Sogea kidogo!”

Bianca alimdanganya Genesis kwa maneno matamu, mpaka akajikuta amelainika na kumsogelea. Bianca akampiga busu kwenye mashavu yake yote mawili, akahisi mwili wake kusisimka katika msisimko wa ajabu kabisa ambao hakuwahi kuupata katika maisha yake.

Lakini kuna tukio la ghafla sana lililomshtua! Bianca akiwa anaendelea na zoezi lake la kummiminia mabusu mashavuni mwake, akaona mwanga wa flash ukiwapiga! Hakuwa na haja ya kuuliza ulikuwa mwanga wa nini. Ilikuwa ni kamera, tena mpigaji alionekana kuwa makini sana, maana picha tatu zilipigwa haraka haraka.

“Ni nani anatupiga picha?” Bianca ndiyo akawa wa kwanza kuuliza akiwa ameyatoa macho yake kwa hasira.

Yote ile ilikuwa ni janja ya kuzima hisia kwamba anahusika, lakini ukweli ni kwamba waliopiga zile picha ni kundi lake ambalo lilijipanga vyema kuhakikisha Farida anaachana na Genesis.
“Sijui!”

“Siyo kiranja?”
“Sijui!”
“Tumekwisha Bianca, kama ni viongozi wa shule, Mkuu wa Shule akipewa hizo picha utakuwa mwisho wetu wa kuwa hapa shuleni, sijui nitamwambia nini Profesa Mshana?” akasema Genesis akionekana kuwa na hofu sana moyoni mwake.

Kwa upande wa Bianca ilikuwa tofauti sana, hakuonekana kuogopa, badala yake alikuwa akimtuliza Genesis. Alijua kila kitu juu ya nani aliyepiga zile picha, wasiwasi wa nini?

Je, nini kitatokea?
 
SEHEMU YA 10

Penzi la Genesis na Farida linaingia kwenye mgogoro mkubwa, baada ya wazazi wake kumkataa kwa sababu alitoka katika familia masikini, baba akiwa Fundi Seremala na Mama Ntilie, wakati wao walikuwa wahadhiri tena wa chuo chao wenyewe!

Baada ya mgogoro mkubwa, huku Genesis akiendelea kushikilia msimamo wake, akakubaliwa kuendelea na Farida lakini anapewa sharti kwamba lazima Farida afaulu vizuri mitihani yake ya kidato cha sita na apate nafasi ya kuendelea na Elimu ya Chuo Kikuu, jambo linalopokewa na Genesis na Farida kwa shangwe maana walikuwa na uhakika na sharti hilo.

Likizo ilipoisha Genesis na Bianca wanarudi shuleni kwa kutumia gari moja, njia nzima walikuwa hawaongei.

Siku ya kwanza ya masomo, Genesis anakutanisha macho yake na Farida anashangaa kusoma huzuni, wakati wa mapumziko akamfuata na kumuuliza, akamjibu asiendelee kumfuatilia na badala yake aendelee na Bianca.

Akiwa bado yupo kwenye mshangao, Bianca anatokea akionekana kuwa na sura ya tabasamu. Akawa anatembea kuelekea sehemu aliyokuwa amesimama Farida ambaye uso wake ulionesha wazi hasira iliyopo ndani yake, lakini cha ajabu Bianca aliendelea kutabasamu!
Bianca alijifanya kumsamilimia, lakini Farida akachukia na kuondoka zake. Genesis naye akaondoka kwa hasira.

Usiku wa siku walioingia shuleni, Bianca alikuwa katika mazungumzo na Genesis, lakini baadaye akamuomba ampe zawadi, ingawa Genesis alikuwa mgumu kukubali, lakini alipomkubalia, Bianca alimsogelea na kumbusu!

Ghafla mwanga wa flash ya kamera ukaonekana. Ni wazi kwamba walikuwa wamepigwa picha. Kitu pekee ambacho kilivamia kichwani mwa Genesis ni kwamba, aliyepiga picha ile alikuwa kiongozi wa shule na kama zingepelekwa kwa Mkuu wa Shule, basi wangeishia kutimuliwa shule!
Je, nini kitatokea? SONGA NAYO...

UBONGO wa Genesis ulisafiri maili nyingi sana akiwaza namna ambavyo baba yake angemuadhibu kwa kosa kubwa kama lile. Siku zote baba yake alikuwa akimuamini sana mwanaye kama mwanafunzi anayejituma sana kwenye masomo, kupatikana kwa tuhuma za kujihusisha na mapenzi kungemchafua sana!

Hakuwaza kuhusu Bianca ambaye alionekana kuwa chaguo hasa la familia, maana hata kama ingekuwa hivyo, bado hawakupewa nafasi ya kufanya mambo machafu shuleni. Kichwa kilimuuma na akakosa amani kabisa.

Kitu kingine kilichokuwa kikimuumiza zaidi ni kwamba, ile ilikuwa shule ya seminari, ambayo mwanafunzi akihusishwa na tuhuma za mapenzi, kinachofuata ilikuwa ni kufukuzwa tu!

“Mungu wangu, napoteza masomo sasa!” akasema kwa sauti kubwa Genesis.
“Kwa nini?”
“Nani amepiga picha?”

“Sijui!”
“Sasa kwa nini huna wasiwasi Bianca, hudhani kwamba wanaweza kuwa watu wabaya ambao wanaweza kutuchomea kwa uongozi?”
“Sidhani?”

“Na wewe kwa nini uling’ang’ania kunikumbatia?”
“Niliamua tu, wewe ni rafiki yangu, kukumbatiana ni ishara ya upendo, sasa kuna tatizo gani?”

“Lakini kumbuka hii shule ni ya seminari!”
“Najua.”
“Sasa hujui adhabu ya mwanafunzi anayekutwa na tuhuma za mapenzi?”
“Najua!”

“Ni nini?”
“Kufukuzwa shule!”
“Sasa wewe upo tayari kupoteza shule?”

“Hapana.”
“Halafu kumbuka huu ni mwaka wa mwisho wa masomo yetu, hii ndiyo njia ya kwenda chuo kikuu, unadhani kama tutaiharibu nini kitafuata?”

“Kwa nini iharibike?”
“Halafu majibu yako siyaelewi kabisa...” Genesis akasema na kumsukuma pembeni Bianca kisha akaenda zake bwenini.

Majibu ya Bianca hayakufanana kabisa na mtu anayejutia kosa alilolifanya ambalo linaweza kugharimu kitu muhimu katika maisha yake. Hakuonekana kujali kabisa.

Ni kama walikuwa wamefanya kitu cha kawaida kabisa, jambo ambalo halikuwa na ukweli, lilikuwa tukio kubwa ambalo lingesababisha wote wawili kufukuzwa shule haraka sana bila maelezo yoyote. Genesis akalala akiwa na mawazo tele kichwani.

Pamoja na kuwaza kufukuzwa Shule, lakini pia aliwaza sana juu ya Farida wake. Kama Farida angesikia habari za yeye kupigwa picha ni wazi kwamba mapenzi yao yangefikia mwisho, jambo ambalo hakutaka kabisa litokee. Kichwa chake kilikuwa kizito sana, akalala akiwa na mawazo mengi sana kichwani mwake.

Maswali mengi sana, ambayo hata moja hakuwa amepata jibu lake.
“Sijui ni balaa gani hili?” akawaza kichwani mwake akijifunika shuka vizuri kitandani.
Hapo akaanza kuubembeleza usingizi, ambao ulikuwa mgumu sana kupatikana.

****
“Kazi nzuri!” Bianca akasema akiangalia picha kwenye kamera aliyokuwa ameishika Josephine.
“Na wewe uko fasta sana, kama si hivyo huenda tungechemka.”
“Kwa nini?”

“Hukumkawiza, yaani ulikuwa unajua cha kufanya,” Grace naye akasema.

“Ok! Vizuri, sasa mnajua kinachofuata?” Bianca akauliza.
“Yeah!” Grace akajibu.
“Basi poa, kamilisheni hilo zoezi haraka!”

“Sawa, hivi na akiwa haamini tunaweza kumuonesha hizi picha?”
“Itakuwa bado mapema sana kwa sasa, nawashauri mwageni maneno kadri mnavyoweza lakini kwa suala la picha acheni kwanza.”
“Sawa.”

Wakatawanyika wakiwa na kazi moja tu, mbele yao. Walikuwa wanamsubiri Farida aingie shuleni na kukamilisha zoezi lao, tayari walikuwa na ratiba nzima, kwamba ilikuwa lazima Farida afike shuleni siku hiyo hata kama ni usiku sana.

****
Farida aliingia shuleni akiwa amechelewa sana, hii ilisababishwa na kutoka kwao jioni, lakini mbaya zaidi gari alilokuwa akisafiri nalo kuharibika njiani, eneo la Bwawani.

Tatizo hilo lilisababisha abiria wote washuke, na kusubiri gari lingine liliagizwa kutoka Dar es Salaam, maana Morogoro hapakuwa na magari mengine. Kwa wenye fedha zao, walipanda mabasi mengine yaliyopita.

Farida hakuwa na fedha za kutosha, kwa hiyo alilazimika kusubiri mpaka gari lile lilipokuja, muda ukiwa umekwenda sana. Alifika Morogoro usiku na kukodisha teksi iliyompeleka mpaka shuleni.

Aliburuza begi lake kichovu sana, akiwa anatembea kuelekea bwenini kwake. Akashangaa Grace anamkimbilia na kumpokea begi lake. Ni kweli alikuwa naye karibu, lakini si kwa kiwango kile.
Alisoma naye darasa moja, lakini walilala mabweni tofauti.

Ukaribu ule wa ghafla ukampa mashaka kidogo, lakini hakuwa na namna zaidi ya kukubalia kampani yake, ambayo kwake ilikuwa na maswali mengi sana.
“Pole mwaya, Farida.”
“Ahsante, vipi?”

“Shwari...jamani mbona umechelewa sana?”
“Mwenzangu gari liliharibika Bwawani!”
“Si ungepanda lingine?”
“Mh!”

“Vipi mbona unaguna?”
“Hiyo pesa ya kupanda magari mawili kwa wakati mmoja ningeipata wapi?”
“Pole mwaya, bora umefika salama.”

“Ahsante.”
Akaendelea kuongozana naye huku wakiendelea kuzungumza mpaka walivyofika mlangoni mwa bweni analolala Farida. Grace akasimama na kumgusa Farida begani.

“Mwezangu nina mchapo, tena nilikuwa na hamu sana ya kukuambia ili uelewe ukweli.”

“Juu ya nini?”
“Genesis!”
“Genesis?” Farida akauliza kwa mshangao, hakutarajia kusikia kwamba mchapo wenyewe ulikuwa unamhusu Genesis.
“Ndiyo Genesis, mbona umeshtuka sana?”

“Nimeshangaa!”
“Sikiliza, wewe ni rafiki yangu, mwanamke mwenzangu, lakini nataka kukuambia shoga yangu, huyu bwana anataka kukuharibia maisha yako, hakupendi!”

Yalikuwa maneno mazito sana yalimchanganya sana kichwa Farida, Genesis awe hampendi? Ni maneno ambayo yaligoma kabisa kuingia kichwani mwake.
“Kwa nini umesema hivyo?”

“Unafahamu uhusiano wake na Bianca?”
“Ndiyo!”
“Ni nini?”

“Marafiki, familia ya Bianca na akina Genesis ni marafiki wakubwa!”
“Hivyo tu?”
“Sijui zaidi ya hapo!”

“Genesis na Bianca wanatoka kimapenzi, leo wameonekana mahali wanazungumza kimapenzi, tena wakiwa wamekumbatiana!”
“Leo?”

“Ndiyo usiku huu, tena nasikia wamekuja pamoja kutokea Dar. Nimekuambia kama rafiki yako, wewe ni mwanamke mwenzangu, nimeona nikuambie ukweli. Fanya uchunguzi utagundua, lakini nakuomba sana usinitaje!” akasema Grace na kuondoka zake.

Akamuacha Farida akiwa na mawazo tele kichwani mwake, kwa mbali alianza kuamini maneno ya Grace, lakini alichopanga kufanya ni kuwafuatilia kwa karibu ili kugundua ukweli wa maneno ya Farida.
****

Mwili wa Farida ulikuwa darasani, lakini akili yake haikuwa hapo kabisa. Maneno ya Grace yalianza kumuingia kwa kasi sana kichwani mwake. Aliyomwambia usiku, yalijidhihirisha asubuhi wakati akiwa anazozana na Genesis, na Bianca kuwafuata.

Hilo lilitosha kabisa kumthibitishia kwamba walikuwa na uhusiano. Genesis naye alikuwa kimya kwenye dawati lake, akijilazimisha kumwelewa mwalimu aliyekuwa ubaoni, lakini alishindwa, mawazo yake yote yalihamia katika uhusiano wake na Farida.

Walikuwa wakitazamana kila wakati kwa kuibia, lakini safari hii Genesis akakutana na kitu cha ajabu sana machoni mwa Farida; MACHOZI!

Macho ya Farida yalikuwa yanachuruzisha machozi kama maji. Kwa bahati mbaya sana, mwalimu aliyaona machozi ya Farida.
“Farida unalia nini?” Sister Adventina, aliyekuwa akiwafundisha somo la Kemia alimwuliza.
Farida akabaki ameganda bila kuwa na jibu. Genesis akaogopa sana!

Je, nini kitatokea?
 
SEHEMU YA 11


“FARIDA una nini?” Sister Adventina akauliza tena.
Farida alibaki kimya!
“Farida!” akaita akianza kupiga hatua kumfuata.
Darasa zima lilikuwa kimya, Genesis alijua kabisa sababu ya machozi ya Farida, moyo wake ukamuuma sana, lakini hakuwa na namna ya kufanya. Alibaki kuwa mtazamaji kuona jambo gani lingetokea.

Sister Adventina akatembea haraka hadi kwenye dawati la Farida. Akamwangalia kwa huruma, alishafahamu kwamba lazima alikuwa na tatizo kubwa la kifamilia linalomsumbua.

Hisia za mapenzi ndilo lilikuwa tatizo kubwa kwa Farida, kila alipogeuza uso wake na kukutanisha macho yake na Genesis machozi yalizidisha kasi ya kuchuruzika!

Anayafuta, lakini yanadondoka tena. Tayari Sister Adventina alikuwa ameshamfikia, akamgusa begani na kumwuliza kwa sauti ya taratibu sana.
“Tatizo ni nini Farida?”

“Hakuna!”
“Hakuna?”
“Sina tatizo Sister!”
“Sasa mbona unalia? Mbona machozi yanadondoka machoni mwako?”
“Sister, samahani nina mafua makali sana, yananisumbua tangu juzi, kichwa kinaniuma sana!” Farida akadanganya.

Hakuwa akiumwa na kichwa wala tatizo la mafua. Aliamua kudanganya, maana ukweli haukuwa huo.
“Kweli Farida?”
“Ndiyo Sister!”
“Hakuna kingine?”

“Na kwa nini nisikuambie?”
“Ok! Naona basi uende bwenini ukapumzike.”
“Hapana.”
“Basi nenda zahanati ukachukue dawa!”

“Tayari zipo ninazotumia, kabla sijaja darasani nimekunywa!”
“Lakini kama hujisikii vizuri naona ingekuwa vyema kama ungerudi bwenini kupumzika.”
“Usijali sister nitavumilia, sitaki kupitwa na sehemu hata moja ya hii topic!”

“Sawa.”
Sister Adventina akaendelea kufundisha, Farida akiendelea kuyazuia machozi yake kwa tabu kubwa. Haikuwa kazi nyepesi kuyazuia yasitokee, lakini alijitahidi sana kupambana nayo!

Kosa kubwa ambalo alikuwa akifanya mara kwa mara lilikuwa kumwangalia Genesis, kila alipogeuza macho yake na kukutanisha na Genesis, alijisikia vibaya sana. Alimuona kama msaliti ambaye anaweza kumharibia maisha yake.

Kwa wakati huo Genesis alikuwa kama injini ya gari katika maisha yake. Alikuwa na umuhimu mkubwa sana, maana moyo wake ulimpenda kwa dhati kabisa. Kipindi kiliisha akiwa hana alichombulia. Kipindi kilichofuata kilikuwa kigumu kwake, akaomba ruhusa na kwenda bwenini kupumzika. Tatizo kubwa likiwa ni Genesis!

****
Kichwa chake kilikuwa kizito sana, siku nzima iliisha akiwa hana furaha kabisa, hakupenda Farida wake kuwa katika hali ile, alijua kabisa kwamba yeye ndiye alikuwa chanzo cha kila kitu. Hata hivyo alijiamini kabisa kwamba hana kosa lolote katika fikra za Farida.

Alifahamu kabisa kwamba yeye hana uhusiano wa kimapenzi na Bianca ambaye Farida alisema kwamba ana uhusiano naye. Usafi wake katika eneo hilo, ndiyo uliomwongezea huzuni zaidi ndani ya moyo wake. Farida hakupaswa kukasirika kiasi kile kwa mambo ambayo hakuwa na uhakika kama ameyafanya!

Hata hivyo, hakujua kilichokuwa kinafanyika nyuma ya pazia! Hakujua kundi la Bianca lilikuwa kazini kuhakikisha uhusiano wake na Farida unayumba na kitu kikubwa cha kuzingatia kikiwa ni kuhakikikisha Farida anafanya vibaya katika masomo yake. Hilo ndilo lilikuwa lengo kubwa zaidi.

“Ipo sababu ya kumtafuta Farida, ipo sababu ya kuzungumza naye, sitakiwi kukaa kimya kwa jambo zito kama hili. Naweza kupuuzia, lakini mwisho wake nikampoteza mpenzi wangu,” akawaza Genesis jioni hiyo.

Kitu pekee ambacho alitakiwa kufanya kilikuwa ni kuhakikisha anazungumza na Farida jioni ileile. Kwanza alijaribu kumpigia kwenye simu yake lakini hakupatikana. Ni muda ambao alitakiwa kupatikana, shuleni hawakuruhusiwa kuwa na simu, lakini wanafunzi wengi walikuwa na simu, ila walikuwa wanazitumia kwa kificho, hasa baada ya masomo.

Kwa muda wa saa kumi na mbili za jioni kama hiyo, alitakiwa kupatikana, lakini hakupatikana. Akaenda sehemu zote muhimu ambazo Farida alipendelea kwenda, lakini hakumuona. Hapo akalazimika kwenda karibu na bweni lao, akasimama na kujaribu kumwangalia bila mafanikio.

Wavulana hawakutakiwa kabisa kwenda kwenye mabweni ya wasichana na wasichana nao kadhalika hawakuruhusiwa, hivyo alisimama mita chache akijaribu kutupa macho bila mafanikio. Muda kidogo akapita msichana mmoja ambaye alionekana kuelekea bwenini. Mara moja akamuita.

“Mambo?”
“Poa!”
“Samahani kidogo!”

Yule msichana akasimama kisha akageuka na kumfuata Genesis alipokuwa amesimama. Genesis hakumjua msichana yule, lakini yeye alimfahamu vizuri sana. Genesis alikuwa maarufu sana shuleni pale.

Utambulisho wake wa kwanza ni kwamba alikuwa mvulana mwenye mvuto sana; wenyewe walimuita School Hb wakimaanisha kwamba alikuwa kijana mwenye mvuto shule nzima!
“Vipi?” akauliza msichana yule akiwa katika mshangao.
“Samahani lakini!”

“Bila samahani!”
“Unalala kwenye Bweni la Tanganyika?”
“Ndiyo!”
“Unamfahamu Farida.”

“Ndiyo!”
“Naomba uniitie, tafadhali ni muhimu sana.”
“Nimuambie nani?”
“Genesis!”

“Jina lako nalijua, namaanisha nani wake?”
“Hapana, mwambie tu Genesis.”
Yule msichana akaachia tabasamu pana kisha akaanza kupiga hatua na kuondoka taratibu sana. Genesis akasubiri kwa hamu. Akiwa bado amesimama pale, kwa mbali akatokea Bianca akiwa anacheka.

Genesis akamshangaa kwa kicheko kile, hakujua ni kwa nini hasa alikuwa akicheka na kwa nini alimfuata na pia alijuaje kama yupo mahali pale muda ule.

“Vipi kaka Genesis, mbona unaonekana una mawazo sana,” akauliza Bianca lakini akiwa bado anacheka.
Kwa upande wa Genesis ilikuwa furaha kwake kusikia akiitwa kaka, mara zote Bianca alikuwa akimuita kwa jina lake moja kwa moja na alilazimisha awe mpenzi wake, kwa hiyo kumuita kaka kulimpa matumaini kwamba, tayari Bianca alishaziondoa hisia hizo katika kichwa chake. Akawa tayari kumsikiliza kwa makini.

“Ni kweli kuna kitu kinanisumbua, lakini kwa nini unauliza huku unacheka?”
“Sikucheki wewe kaka yangu, kuna kitu nacheka!”
“Kitu gani?”

“Ah! Ni mambo ya kike, nilikuwa nazungumza na rafiki zangu kule, ndiyo maana nacheka, kuna jambo walinichekesha sana!”
“Ok! poa, kuna kitu kinanichanganya, lakini usijali.”
“Sitakiwi kujua?”

“Hapana, ni binafsi sana!”
“Mbona uko maeneo haya karibu na mabweni ya wasichana?”
“Kuna mtu namsubiri.”
“Bila shaka ni Farida,” akasema Bianca akimsogelea Genesis taratibu.

“Ndiyo,” Genesis akasema, lakini muda huo tayari Bianca alikuwa ameshamkaribia kabisa.
Kwa mbali akamuona Farida akija eneo lile akiwa ameongozana na yule msichana. Alipomuona Bianca amesimama pale, akarudi!
“Farida njoooo,” Genesis akaita kwa sauti kubwa.

Farida hakugeuka nyuma, mara moja akarudi zake bwenini. Muda huo huo Bianca naye akaondoka kwa ghafla sana. Genesis akabaki ameduwaa.
“Haya mambo yataisha lini? Mbona sielewi jamani?” Genesis akapiga kelele akiwa amesimama pale pale akishangaa.

“Kuna nini kinaendelea? Kwa nini Farida anataka kunipa lawama ambazo hazinistahili? Kwa nini anakataa kukutana na mimi kwa hisia ambazo si za kweli? Kuna nini?” alizidi kuwaza mfululizo, lakini hakuweza kupata jibu yakinifu.

Kwa dakika kumi nzima aliendelea kusimama pale akiwa hana hili wala lile, kichwa chake kilivurugika kabisa. Hakuwa na amani kwa sababu ya Farida wake, alikuwa mwanamke muhimu sana katika maisha yake.
Kwake, maisha yake bila Farida ilikuwa ni sawa na kuishi bila kupata maji ya kunywa, jambo ambalo kwa hakika lingeweza kukatisha uhai wake.

Akiwa bado yupo katika butwaa, akamuona yule msichana aliyemuagiza akamuitie Farida akija eneo lile, mkononi mwake akiwa na karatasi. Alipomfikia, akamkabidhi na kuondoka haraka. Hilo la kuondoka ghafla, hakutaka kulipa nafasi katika kichwa chake, alitaka kujua kilichoandikwa katika lile karatasi baaasi!

Haraka akaifungua, mwandiko ulikuwa wa Farida, hilo hakutaka kuambiwa na mtu yeyote; aliufahamu vizuri sana. Akaanza kuyatembeza macho yake katika mwandiko ule mzuri unaosomeka vyema!

Maneno aliyokutana nayo, yalichanganya sana kichwa chake, alitamani kulia. Alihisi kupoteza nguvu. Moyo wake ukabadilisha mapigo na kwenda kasi sana. Hakika yalikuwa maneno mazito sana.
Maneno yale yalisomeka hivi;

Kwa Genesis.
Najua wewe ni mzuri sana, mtanashati unayewavutia wasichana shule nzima. Najua pia unatambua kwamba nakupenda sana na hiyo ndiyo umeifanya fimbo ya kunichapia!

Nimeshakuambia nafahamu kwamba una uhusiano na Bianca lakini unakataa, kumbeuilikuwa unafiki, maana sasa umeamua kunionesha wazi kwamba kweli unatoka na Bianca.

Picha iliyojionesha leo asubuhi na jioni hii inatosha kabisa kuthibitisha kwamba umeamua kunitesa moyo wangu, tena kwa makusudi kabisa, ndiyo maana unafanya mambo kwa kunionesha waziwazi.

Ahsante kwa kila kitu, napenda kukuambia kwamba, nimekubali matokeo. Mungu atanipa mwingine ambaye atailinda furaha yangu. Nakutakia maisha mema na Bianca wako, lakini sikutegemea kama ungenifanyia hivi.
Ahsante.
Farida.

Genesis alihisi kama moyo wake unaingia ubaridi mkali, bila kutegemea machozi yakaanza kutiririka machoni mwake.

“Kwa nini Bianca unaharibu penzi langu?” Genesis akatamka kwa sauti ya chini akipiga ngumi kwenye mti aliokuwa amesimama chini yake.

Je, nini kitatokea katika penzi la misukosuko la vijana hawa?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom