KadaMpinzani
JF-Expert Member
- Jan 31, 2007
- 3,715
- 86
UVCCM yasema maandamano ya wapinzani hayana jipya
*Yawafananisha na kikundi cha uzushi na propaganda
Na Gladness Mboma - Majira
*Yawafananisha na kikundi cha uzushi na propaganda
Na Gladness Mboma - Majira
UMOJA wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) umewataka Watanzania kupuuza maandamano yaliyoandaliwa na vyama vya Upinzani kwa maelezo kuwa hayana jambo jipya lenye manufaa kwa wananchi.
Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM, Bw. Amos Makalla, alitoa mwito huo jana Dar es Salaam, kuhusiana na maandamano yanayotaka kufanywa na wapinzani kwa lengo la kutoa tuhuma mbalimbali dhidi ya serikali.
Bw. Makalla alisema taarifa ya umoja wa Upinzani kutaka kutaja majina ya ufisadi na kufanya maandamano nchi nzima ni propaganda zilizojaa hadaa na upotoshaji mkubwa wenye lengo la kujitafutia umaarufu.
"UVCCM haishangazwi na uongo huu wa wapinzani na Watanzania wasishangae kusikia uzushi wa mambo mengine mengi ya uzushi na uongo mkubwa dhidi ya Serikali na viongozi wake.
"Sisi tunawafananisha wapinzani na bingwa wa propaganda Hitler Joseph Gobells, huyo alikuwa bingwa wa kuzua kashfa na mambo mengi ya uongo kila kukicha, kwa lengo la kuiingiza nchi katika machafuko na hapa Tanzania kumezuka kikundi cha kuzua mambo kwa lengo hilo hilo," alisema Bw. Makalla.
Aliwaomba Watanzania wapenda amani kukwepa hadaa za kisingizo cha maandamano na kuingiza nchi katika umwagaji damu na kusisitiza kuwa maandamano yaliyopangwa ni sehemu ya mkakati wa kuiingiza nchi katika machafuko na uvunjaji wa amani.
Aliwataka Watanzania kuchukua tahadhari dhidi ya viongozi wa aina hiyo ambao baada ya kushindwa uchaguzi wa mwaka 2005, sasa wanataka njia ya mkato ya kuingia Ikulu kwa kuzua mambo kila kukicha na kupotosha mambo kwa lengo la kuiingiza nchi katika machafuko na mgogoro wa kitaifa, kitu ambacho kitaathiri ustawi wa Taifa.
"Lengo la madai kuwa mawaziri wanaishi maisha ya anasa ni kuwatengenezea chuki wananchi na kuwapunguzia kazi ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi kwa kutumia muda mrefu kujibu hoja dhaifu zilizojaa uongo na uzushi," alisisitiza Bw. Makalla.
Alisema UVCCM inajua mkakati mzima wa umoja wa upinzani na kwamba utekelezaji wa Ilani umewashitua wapinzani hivyo uzushi huo wa mambo mapya dhidi ya Serikali ni jitihada za 'kuishika shati', Serikali kwa kuipunguza kasi ya utekelezaji wa Ilani na suala zima la kuwaletea maendeleo Watanzania.
Bw. Makalla alisema umoja unatambua jitihada na dhamira ya Serikali kuwa ni kudumisha amani na kuwaletea Watanzania maendeleo na utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya mwaka 2005 hadi 2010 na kuwataka Watanzania kuwa na imani na Serikali yao na kupuuza uongo na uzushi wa wapinzani.
Pia aliwataka vijana nchini kuwa macho na watu ambao wanataka kuwatumia kama daraja la kufanikisha maandamano, ambayo yatasababisha mgogoro wa kitaifa na kuhatarisha ustawi wa Taifa.