DuaZaMama
JF-Expert Member
- Jun 2, 2025
- 1,882
- 4,129
Mwana siasa nguli na Mwanachama wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia, ametoa wito kwa Watanzania kuenzi misingi ya majadiliano yenye hoja badala ya kuendeleza chuki na mifarakano inayotokana na tofauti za kimtazamo.
Akizungumza na wanahabari leo jijini Dar es Salaam, Mbatia amesema kuwa hali ya sasa ya kisiasa nchini inahitaji hekima na ustaarabu mkubwa wa kisiasa, hasa katika kuyatazama masuala yanayogusa mustakabali wa taifa kwa jicho pana na lenye kujenga.
“Upinzani wa fikra sio uadui. Kuwepo kwa mitazamo tofauti si kosa, bali ni utajiri wa mawazo unaopaswa kutumika kujenga msingi imara wa taifa letu. Tusiruhusu tofauti hizo ziendelee kutugawa,” alisema Mbatia.
Ameongeza kuwa ni muhimu kwa viongozi wa kisiasa, wanahabari na wananchi kwa ujumla kujiepusha na lugha za kejeli, dharau na uchochezi ambazo zinaweza kuibua mivutano isiyo ya lazima.
Kauli hiyo ya Mbatia imekuja katika kipindi ambacho mjadala wa masuala ya kisiasa na kijamii umeendelea kuchukua sura ya migawanyiko miongoni mwa makundi mbalimbali, hasa kwenye mitandao ya kijamii.
Aidha, Mbatia ametumia nafasi hiyo kuwakumbusha viongozi wa vyama vya siasa na serikali kuzingatia misingi ya Katiba, demokrasia na utawala wa sheria, huku akisisitiza kwamba uhuru wa kutoa maoni ni haki ya msingi ambayo haihitaji kulindwa kwa jazba au hofu.
“Tanzania imejengwa juu ya misingi ya umoja, haki na mshikamano. Lazima turejee kwenye mazungumzo ya kistaarabu. Hatuwezi kuijenga Tanzania kwa kutishana, kubezana au kulazimishana,” alisisitiza.
Mbatia ni mmoja wa wanasiasa waliowahi kushika nyadhifa mbalimbali ndani na nje ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na amekuwa mstari wa mbele katika kuhimiza siasa zenye misingi ya hoja, maadili na maridhiano.