Kakke
JF-Expert Member
- Dec 4, 2010
- 1,883
- 1,482
Absalom Kibanda
NIMELAZIMIKA na kulazimishwa kuendelea na mada niliyoiandika wiki mbili zilizopita si kwa sababu nyingine yoyote bali kutokana na makala iliyojaa vimelea vya chuki, uongo, upotoshaji na ubabaishaji usiomithilika iliyoandikwa na mwandishi Nkwazi Nkuzi katika gazeti hili wiki iliyopita.
Ingawa ninao wajibu wa kuheshimu maoni au mawazo ya wengine yawe ni yale yanayounga mkono au kupinga mitazamo yangu katika jambo lolote, ninajiona pia kuwa na dhamana ya kusahihisha upotoshaji, kukemea uzushi au uongo sambamba na kupambana na ubabaishaji wa hoja wa aina ile uliofanywa na Nkuzi.
Katika makala yangu ya kwanza, nilisema bayana namna mashabiki wa hoja za Hamad Rashid watakavyopokea kwa mshangao na pengine upinzani kile nitakachokiandika kuhusu Maalim Seif na nafasi aliyonayo ndani ya CUF na katika siasa za Zanzibar kwa ujumla.
Ni jambo la kufikirisha kwamba, Nkuzi amegeuza wasifu stahili niliompa Maalim Seif kuwa ni ‘sifa za kumpamba' mwanasiasa huyo ambazo kwa mtazamo wake hazipaswi kuelekezwa kwake na kimsingi kama alipata kuwa nazo wakati fulani basi zimebaki katika vitabu vya historia sahaulifu.
Katika sehemu moja ya makala yangu, nilimuelezea Maalim Seif kuwa ni kiongozi aliyejijengea heshima kama kiongozi wa watu na mtu aliye na ushawishi na nguvu kubwa, kwanza katika kisiwa cha Pemba na kisha Unguja. Maelezo haya yalionekana kumkera sana Nkuzi.
Akionyesha kuchukizwa na maneno hayo, pengine kwa sababu za chuki au kwa nia ya kupotosha, Nkuzi alifikia hatua ya kuhoji, kama kweli Maalim Seif ni kiongozi wa watu, "ni kwa kwanini hajawahi kuchaguliwa kuwa rais wa watu hao ambao mimi nilimhusisha nao?
Huku akionekana dhahiri kulijua jibu ambalo linasababisha au limepata kusababisha Maalim Seif ashindwe kutawazwa kuwa Rais wa Zanzibar, haraka haraka, akasema eti tunaweza kudai kwamba aliibiwa ushindi wake!
Ni wazi kwamba swali aliloulia Nkuzi si la kufikirisha kwani majibu yake ni rahisi sana, kwani akiwa ni mchambuzi wa siku nyingi wa siasa za Zanzibar alipaswa awe akijua na kuamini kwa dhati kuhusu kile ambacho kimekuwa kikitokea Zanzibar katika chaguzi za urais za mwaka 1995, 2005 na 2010.
Ili kuhalalisha upotoshaji wake wa wazi na kwa malengo ya kujaribu kuwasahaulisha Wazanzibari historia iliyozaa maafa na miafaka mitatu kati ya mwaka 1995 na 2010, Nkuzi anahoji iwapo kweli Maalim Seif ni mtu wa watu, hao watu wake walikuwa wapi na walifanya nini kila alipoporwa ushindi?
Haishii hapo, anaweka msisitizo katika uzushi na upotoshaji wake kusema kwamba kile ambacho kimekuwa kikidaiwa kuwa ni wizi wa kura Zanzibar si chochote na lolote zaidi ya "sanaa za CCM na (Maalim) Seif mwenyewe".
Kwa vyovyote vile iwavyo, alichokiandika Nkuzi kwa sababu tu ya hasira au chuki zake dhidi ya Maalim Seif au sababu nyingine yoyote aliyonayo ni dhihaka kwa Wazanzibari, jumuiya ya kimataifa na matusi kwa demokrasia ya kweli.
Ni wazi kwamba Nkuzi anajua namna Jumuiya ya Madola ilivyoingilia kati kutafuta ufumbuzi wa mgogoro wa kisiasa Zanzibar kwanza kupitia kwa Katibu Mkuu wake wa zamani, Chifu Emeka Anyauko.
Anaandika hivyo akionyesha dhahiri kusahau kama si kuzipuuza ripoti za waangalizi wa ndani na wa kimataifa wa uchaguzi wa Zanzibar ambao siku zote wamekuwa wakieleza utata katika matokeo ya kura za urais.
Mwandishi huyu haishii hapo kupotosha, bali anakwenda mbele zaidi na kufikia hatua ya kupinga hata wingi wa mambo mema na ya msingi ambayo Maalim Seif amewahi kufanya kwa ajili ya Zanzibar kwa kiwango ambacho hakiwezi kulinganishwa na kiongozi mwingine yeyote.
Pasipo kutoa mfano hata mmoja zaidi ya kuishia katika kutaja majina ya watu, Nkuzi anaandika uzushi mwingine anapodai kwamba, eti Mzee Ali Hassan Mwinyi amefanya mengi kwa Wazanzibari kuliko aliyopata kuyafanya Maalim Seif.
Nauita huu uzushi wa mchana kwa sababu, kwa kipindi cha takriban mwaka mmoja alichoitumikia Zanzibar kama Rais na kabla ya hapo akiwa waziri katika serikali ya muungano kwa nafasi mbalimbali, wingi wa mambo aliyofanya yanaweza kuunganishwa na yule yule anayemponda, Maalim Seif.
Sisi tunaodadisi na kufuatilia historia ya Zanzibar tunatambua kwamba, katika kipindi kifupi alichokuwa rais wa visiwa hivyo umaarufu aliojijengea Mwinyi ulibebwa na ushupavu wa mtu aliyekuwa waziri kiongozi wake, ambaye hakuwa mwingine zaidi ya Maalim Seif huyo huyo.
Ni kwa sababu hiyo basi, ndiyo maana hata ilipofikia hatua CCM ikamlazimisha Mwinyi kuwa Rais wa Tanzania mwaka 1985 akirithi mikoba ya Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, chaguo la kwanza la Wazanzibari walio wengi ndani ya CCM na hata wale walio nje ya chama hicho lilikuwa Maalim Seif.
Katika kuthibitisha kwamba, Maalim Seif ndiye aliyekuwa akitajwa kuwa nyuma ya mabadiliko na mafanikio makubwa ya kisera na kisiasa zama Mwinyi akiwa rais wa Zanzibar, wana CCM wenzake walio wengi walipinga uteuzi wa Idris Abdul Wakil wa kuwa mgombea urais.
Nitashangaa iwapo Nkuzi aliyefikia hatua ya kuhoji kiwango cha usomi wangu wa somo la historia, atakuwa hajui au amesahau namna Mzee Abdul Wakil (Mungu ampumzishe Pema Peponi) alivyoshindwa kupata asilimia 50 ya kura katika uteuzi wake wa urais.
Sijui ni kwa kiwango gani Nkuzi na wapotoshaji mambo wenzake wanajua na kutambua kuwa, katika kujaribu kupooza mambo, CCM ikiongozwa na Mwalimu Julius Nyerere ililazimika kumuangukia Maalim Seif ili akubali tena kuwa waziri kiongozi wake katika serikali ya Abdul Wakil.
Kilichotokea baada ya hapo kila mtu anajua, Maalim Seif akawa ana nguvu na ushawishi mkubwa kuliko rais wake. Mambo yakawa yanaenda mrama ndani ya CCM Zanzibar na katika Baraza la Mapinduzi lililokuwa chini ya Abdul Wakil.
Sitaki kuamini pia kwamba, Nkuzi na wachambuzi wengine wenye makusudi ya kupindisha historia kwa sababu wanazozijua wao, hawajui kwamba, ushawishi aliokuwa nao Maalim Seif dhidi ya rais wake ndiyo uliosababisha ajikute akifukuzwa katika uongozi mwaka 1988.
Ninachojua mimi na kukiamini kwa dhati kwa sababu ya kuisoma na kuijua historia ya mapambano ya kisiasa Zanzibar, Maalim Seif alinyimwa urais mwaka 1985 si kwa sababu nyingine, bali kwa kuwa siasa za uongozi za zama hizo ziliwatazama Wapemba kwa jicho la mashaka na la kuwatenga.
Ikumbukwe kwamba, hadi wakati huo kulikuwa na Wapemba wawili tu maarufu zaidi katika siasa za kitaifa na kimataifa, wa kwanza akiwa ni Dk. Salim Ahmed Salim na nafasi ya pili ilishikiliwa na Maalim Seif. Katika wote hao hakuna hata mmoja ambaye angeweza kuukwaa urais wa Zanzibar enzi hizo.
Nitashangaa zaidi iwapo, Nkuzi na mashabiki wake wataukataa ukweli mwingine kwamba, kama si nguvu na ushawishi wa kihistoria wa Maalim Seif na wa chama chake cha CUF alichotumia muda wake mwingi kukijenga akiwa na wanasiasa wenzake wengine, ndiyo ulioilazimisha CCM kumteua Mpemba mwingine, Dk. Ali Mohamed Shein, kuwa mgombea urais mwaka 2010?
Hivi Nkuzi hafahamu kwamba, aliyefanya kazi kubwa ya kuwajengea Wapemba wenzake heshima na kuanza kujenga aina mpya ya siasa za udugu na usawa miongoni mwa Wazanzibari ni Maalim Seif na chama chake cha CUF. Je ni sahihi kumpuuza leo kama alivyofanya Hamad Rashid?
Nkuzi anajaribu kumpuuza Maalim Seif akisahau kwamba, miezi kadhaa kabla ya kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1995, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere alikutana naye kwa faragha katika kikao ambacho kiliibua maneno mengi ndani ya CCM.
Katika kuonyesha kwamba Mwalimu Nyerere alifikia hatua ya kumuomba radhi Maalim Seif kiutu uzima (Nkuzi analipinga hili) alikuwa ni kiongozi wa juu wa kwanza, kupendekeza kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa Zanzibar mara tu matokeo ya urais yenye utata yaliyompa Dk. Salmin Amour Juma ushindi wa asilimia 50.2 dhidi ya asilimia 49.8 ya Maalim Seif yalipotangazwa mwaka 1995.
Watanzania tumekuwa ni watu wa ajabu sana. Wengi kwa sababu ya kutofikiri sawasawa au kwa sababu tu ya kushabikia mambo kabla ya kufanya utafiti tumejikuta tukiwa majeruhi wa siasa za dhihaka dhidi ya CUF na Maalim Seif.
Tumefikia hatua ya kukiita CUF kuwa ni ‘CCM B' na rafiki yangu Nkuzi akaenda mbele na kudai kwa jeuri kabisa kwamba, eti Maalim Seif amekiuza chama chake kwa sababu ya hadaa ya madaraka. Huu ni mzaha wa hatari.
Tunafanya hivi leo, tukisahau haraka vidonda na makovu ya uhasama yaliyozaa maafa makubwa mwaka 2001 wakati Wazanzibari mashabiki wa CUF na Maalim Seif walipoandamana kupinga ushindi wa CCM na wa Rais Amani Abeid Karume katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2000.
Tumefika hatua ya kumuona Maalim Seif kuwa ni msaliti kwa sababu tu ya uzalendo wake wa kukaa meza moja na Karume na kufikia muafaka uliookoa maisha ya watu ambao yumkini wangejitokeza kupambana tena, kumwaga damu na wengine kurejea ukimbizini Mombassa kama ilivyokuwa mwaka 2001 iwapo kiongozi huyo, angetangaza kutoyatambua matokeo yaliyompa ushindi Dk. Shein mwaka 2010.
Ni jambo la kufedhehesha kwamba, wakati Nelson Mandela alionekana na bado anaendelea kubakia kuwa shujaa wa kihistoria kwa taifa lake na katika jumuiya ya kimataifa kwa sababu tu ya kukubali kukaa meza moja na hata kuunda serikali ya umoja wa kitaifa na Makaburu waliomfunga na kuua maelfu ya weusi nchini Afrika Kusini, Maalim Seif anaonekana kuwa msaliti kwa chama chake na kwa Watanzania wenzake eti kwa kuwa amesalimu amri na kukubaliana na CCM kuunda serikali ile ile ya umoja wa kitaifa.
Wakati tukimng'ong'a Maalim Seif wetu na CUF yake, sijawasikia Wakenya wakimponda Raila Odinga na chama chake cha ODM kwa sababu tu ya uamuzi wao wa kukubali kuunda serikali ya umoja wa kitaifa na Rais Mwai Kibaki ambaye alitangazwa mshindi katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2008 katika mazingira yaliyojaa utata mwingi.
Kama hiyo haitoshi, sijawasikia Wazimbabwe wakimponda, Morgan Tsvangirai sababu ya kukubali kwake kuunda serikali ya umoja wa kitaifa na hasimu wake Rais Robert Mugabe.
Hili tunalomshambulia nalo Maalim Seif sasa limetokea hata nchini Uingereza ambako tumeona chama cha Conservative kikilazimika kuunda serikali ya pamoja na chama cha Liberal. Mbona kelele za usaliti na kuuza vyama hatuzisikii huko? Kulikoni?
Katika mazingira ya namna hiyo, nitakuwa nikijiingiza katika mkumbo wa hovyo iwapo nitaamua kuwa miongoni mwa Watanzania wanaoshabikia matendo kama yale yaliyofanywa na Hamad Rashid na wenzake ambayo natambua wazi kwamba matokeo yake yana athari kubwa hata katika mafanikio madogo ambayo wanaharakati wa demokrasia wameyapata katika siasa za Zanzibar.
Watu tunaofuatilia kwa ukaribu siasa za visiwa hivyo na kudadisi kila siku kile kinachoendelea ndani ya serikali ya umoja wa kitaifa tunatambua maana halisi ya matendo ya kina Hamad Rashid kwa mustakabali wa CUF na siasa za visiwa hivyo sasa na ule wa baada ya mwaka 2015.
Ningemwelewa Nkuzi na mashabiki wengine wa Hamad Rashid iwapo wangekaa chini na kuhoji ni kitu gani kilikuwa kikitokea ndani ya CUF na Zanzibar sasa, hata kuwalazimisha wanasiasa hao waanze kuzungumzia kuhusu kumng'oa Maalim Seif katika nafasi yake ya Katibu Mkuu wa chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa ndani uliopangwa kikatiba kufanyika mwaka 2014?
Ni jambo lisiloingia akilini kwa mwanasiasa mkomavu wa aina ya Hamad Rashid kupanda katika majukwaa ya wazi na kuanza kumshambulia kiongozi wake mkuu na kufikia hatua ya kutangaza hadharani kuhusu kudorora kwa chama chake ilhali yeye si tu kwamba ni mwanachama wa kawaida, bali kiongozi mwenye dhamana kubwa.
Pamoja na ukweli kwamba, mimi si muumini wa siasa za kufukuzana ndani ya vyama vya siasa bado naamini pia kwamba, nidhamu ni jambo la msingi na linalopaswa kuzingatiwa na kuheshimiwa miongoni mwa wanasiasa hususan wale wenye majina makubwa kama walivyo kina Maalim Seif na Hamad Rashid.
Watu wanaoamini katika nadharia na harakati za mabadiliko ya kisera, kiuongozi na kimadaraka ndani ya vyama vya siasa na hata ya kiserikali kupitia katika mifumo ya kidemokrasia, wanapaswa kutambua kwamba ndoto za ushindi huko waendako haziwezi kufikiwa pasipo kutanguliza nidhamu katika kauli na matendo yao.
Chanzo: Tanzania daima