JK mweledi pekee mchakato wa Katiba
Kwa hiyo hapa tunamuona Rais Kikwete kama mtu aliyejitoa mhanga na kujivalisha ujasiri kwa kufanya jambo ambalo halipo katika chama chake na ambalo haliungwi mkono na wanasiasa wenzake katika chama na serikali.
Rais Kikwete anaelekea kuibuka shujaa tena kwa kuacha suala la kura ya maoni likielea. Utabiri wangu ni kuwa katika kipindi cha sasa na Bunge kukaa Novemba, CCM watafanya tafakuri kuangalia mazingira mazuri zaidi kwao ya kupitisha Katiba kupitia kura za wananchi.
Wanasiasa wetu wangekuwa na nia njema na dhamira ya kweli wangerekebisha sheria ya mabadiliko ya Katiba ili kuruhusu mambo mawili.
Mosi, kuruhusu kura ya maoni ifanyike baada ya uchaguzi mkuu tukitarajia kwamba katika kipindi hiki tutapata nafasi ya kutibu majeraha ya kisiasa yaliyojitokeza.
Pili, kuruhusu kuundwa kwa tume ya kitaalamu itakayohusisha wajumbe kutoka ndani na nje ya nchi. Kazi ya tume hii ingekuwa ni kusafisha Katiba inayopendekezwa kwa kupitia kwa makini hoja zilizojitokeza kwenye Rasimu na ambazo zimetupwa na zile zilizojitokeza katika Bunge Maalumu la Katiba.
Tume hii pia ingeweza kukaa na wanasiasa wa pande mbili zinazosigana ili kuwasuluhisha na kufikia mwafaka katika mambo ya msingi bila kuvuruga mchakato.