Mtambuzi
Platinum Member
- Oct 29, 2008
- 8,810
- 15,398
Karibu juma zima lililopita nimekuwa nikitembelea eneo hili la Kimboka by Night hapa Buguruni, Klabu ambayo iko jirani na kituo cha mafuta ambacho wengi huita Buguruni Sheli. Nimekuwa nikitembelea mahali hapa ili kufanya udadisi kwa hivi vibinti vinavyojiuza. Naamini mimi sio mtu wa kwanza kuzungumzia mahali hapa, naamini wapo wengi wameshawahi kusoma habari za eneo hili ambalo limekuwa likijizolea umaarufu kila kukicha. Siku ya kwanza kabisa kwenye majira ya saa tatu za usiku nilikutana na mabinti wengi ambao walionekana dhahiri ni wanafunzi kutokana na umri wao kuonekana mdogo. Mabinti hao walikuwa wamevaa vivazi ambavyo viliacha sehemu kubwa ya miili yao ikiwa wazi au tuseme nusu uchi. Walikuwa wakipita pale niposimama njia panda ya kwenda kwa mnyamani wakiwa katika makundi ya watatu watatu au wanne wakielekea kwenye hiyo klabu iliyoko jirani na kituo hicho Sheli.
Nilijongea karibu na Klabu hiyo na kukaa kwenye kibanda cha muuza Vocha pamoja na vipakiti vya Konyagi maarufu kama Viroba. Nilinunua Vocha kisha nikaanzisha urafiki na huyo muuza vocha ili niweze kufanya udadisi wangu kwa urahisi. Nilianza udadisi kwa kumuuliza muuzaji wa kile kioski juu ya wale mabinti wanaopita pale. Yule muuzaji alinieleza kuwa wale mabinti ni makahaba ambao wanajiuza katika ile klabu ya Kimboka na bei yao inaanzia shilingi elfu tano na chumba ambacho kinapatikana hapo hapo Kimboka kinalipiwa shilingi elfu mbili, kwa hiyo kwa mshindo mmoja inamlazimu mwanaume kutumia shilingi elfu saba lakini inategema zaidi na mwonekano wa mtu, na inaweza kupanda hadi shilingi elfu kumi au kushuka hadi shilingi elfu tano kulingana na hali ya biashara siku hiyo.
Aliendelea kubainisha kwamba baadhi ya mabinti wale hufika pale na mabwana zao ambao huitwa Ving'asti. Vijana hao ambao wengi ni vibaka na watumiaji wa madawa ya kulevya hutumika kama walinzi wa kuwalinda mabinti hao ili wasidhulumiwe na wanaume wakware, lakini mwisho wa siku hugawana kipato. (Kwa wenzetu wa Ughaibuni huitwa Pimp). Lakini pia wapo mabinti wanaokomaa wenyewe na hawa hata wakidhulumiwa hawapati msaada kutokana na kutokuwa na ving'asti. Habari ya mabinti wale ilinifanya nitafakari juu ya mustakabali wao. Katika kutafakari kwangu, nilijiuliza swali moja, Je kwa nini mabinti wale wanaitwa ni makahaba? Au ni kwa nini kuwe na makahaba? Kwa kawaida sisi wanadamu huwa tunapenda kuhukumu matokeo au dalili badala ya kuangalia chanzo. Kwa nini nasema hivyo? Ni kwa sababu wakati nawazungumzia wale mabinti, muuzaji wa kile kioski aliniambia kuwa wale ni makahaba wanaojiuza. Lakini hebu tujiulize, Je wanajiuza kwa nani?
Kama kungekuwa hakuna wanunuzi wa kile kinachouzwa na hao makahaba, ni wazi kusingekuwa na watu hao wanaoitwa makahaba. Kwa bahati mbaya kabisa ni kwamba wanunuzi wa bidhaa hiyo ambao wengi ni sisi wanaume, lakini sisi hatuna jina la kejeli zaidi ya kuonekana vijogoo. Inashangaza kidogo kuona kuwa wanaoshiriki katika tendo hilo ni watu wa jinsia zote mbili lakini sifa na jina baya wanapewa mabinti hao.
Hata hivyo sishangai sana kwani kwa nchi kama Tanzania ambayo hivi sasa inavuma kwa ufisadi, vitendo vya kuvunja sheria na ukahaba ni vya kutarajiwa sana. Kwa nini tusitarajie vitendo vya aina hiyo wakati wananchi wamekata tamaa kutokana na ugumu wa maisha. Kuna baadhi ya watu wamejilimbikizia mali huku wengine wakishindia mlo mmoja kwa siku.Hivi sasa kuna wimbi kubwa la mabinti na vijana wa kiume ambao wamejikuta wakiingia katika vitendo vya uvunjaji wa sheria ikiwemo uvutaji wa bangi, matumizi ya madawa ya kulevya na uporaji wa kutumia silaha za jadi kutokana na hali ngumu ya maisha.Wazazi wa watoto hawa wameshindwa kuwalea watoto wao kwa kufuata maadili kutokana na umasikini.
Hivi ni nani asiyejua kuwa pale kipato kinapokuwa kigumu katika familia, wazazi hutokea kuwa wakorofi, wakali na wasiojali sana kuhusu mahitaji ya watoto wao. Kwa kawaida katika ugumu wa mambo, kunakuwa na kutoelewana hata kwa wazazi. Watoto wanaonekana kwa kiasi cha kutosha kubeba mzigo ambao wazazi wangepaswa kuubeba wenyewe. Hivi sasa kuna wimbi kubwa la watoto, na hasa wenye kati ya umri wa miaka 13 hadi 19 ambao wamebainika kuwa na sononi, ukatili na kukosa adabu kwa sababu ya umasikini wa familia. Hivi mnajua ni kwa nini makahaba wengi wanatokea katika maeneo ya uswahilini kama vile Buguruni, Mwananyamala, Tandale, Kigogo, Tandika na kwingineko, na isiwe ni Masaki, Kawe au Mikocheni?
Ni kwa sababu watu wa maeneo hayo, hali zao kimapato ni nzuri ukilinganisha na wale wa maeneo ya uswahilini. Na msije mkadhani kwamba mabinti hawa wanafanya bishara hii ya ukahaba kwa kupenda? La hasha, sio kweli kabisa, mabinti hawa wamejikuta wakijiingiza katika bishara hiyo kutokana na kukosa namna nzuri ya kujitafutia kipato kwa njia ya halali. Nilipata bahati ya kuzungumza na mabinti wawili ambapo hata hivyo sikupata muda mzuri baada ya kutishiwa na hao vijana wanaoitwa Ving'asti wao wanaowalinda kutokana na kuonekana kama nawapotezea muda au timing kama wenyewe wanavyosema. Lakini kwa kifupi waliniambia kuwa walilazimika kuacha shule na kujiingiza kwenye ile biashara baada ya kushawishiwa na marafiki zao. Wengine walidai kwamba walikuja mjini kama watumishi wa majumbani na baada ya kufukuzwa na waajiri wao walilazimika kujiunga na kazi hiyo ili kujikimu.
Walikiri kuwa hali ya kipato katika familia zao sio nzuri na wanawajibika kujinunulia kila kitu ikiwemo hata chakula. Kwa upande wa kazi hiyo, ya ukahaba walikiri kuwa ni ngumu sana kwani wanaume wengi hupenda kulawiti tena bila kondom, na wakati mwingine huwadhulumu fedha zao walizopatana. Lakini hata hivyo niligundua kuwa mabinti wale ni wavutaji wazuri wa bangi, sigara na ni wanywaji wa Pombe waliobobea. Nilipowadadisi walikiri kuwa wanalazimika kutumia huo ulevi ili kupata kitu walichoita stimu, yaani kuondoa mawazo. Walidai kuwa ingekuwa ni vigumu kwao kufanya kazi ile bila kupata hiyo Stimu. Nilichojifunza kutokana na kile nilichokishuhudia pale Buguruni ni kwamba, kunahitajika mkakati wa kutosha kupunguza pengo kati ya masikini na matajiri. Kuna nguvu kazi nyingi inapotea hivi sasa. Kujenga shule za kata haitoshi kama hakutakuwa na mkakati maalum wa kupunguza umasikini miongoni mwa jamii ya Watanzania.
Ikiwa kama kila mwaka kuna watoto wanakimbia shule na kuingia katika vitendo vya ukahaba na utumiajji wa madawa ya kulevya, je tutarajie jamii gani itakayoujenga uchumi wetu? Kelele za majukwaani peke yake hazitoshi kama mikakati na sera maridhawa hazitawekwa ili kukinusuru kizazi hiki kilichokosa mwelekeo.