Roving Journalist
JF Roving Journalist
- Apr 18, 2017
- 4,809
- 15,034
RAIS SAMIA AKUTANA NA WAGOMBEA URAIS WA TANZANIA BAADA YA UCHAGUZI MKUU WA 2025
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, jana tarehe 31 Machi, 2026, alikutana na wagombea wa nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, akiitikia wito wao wa kufanya majadiliano ya pamoja kuhusu hali ya kisiasa na masuala ya maendeleo ya Taifa kwa ujumla.
Viongozi hao kutoka vyama 16 vya siasa nchini walimtembelea Rais Dkt. Samia na kuwasilisha maoni yao kuhusu namna ya kuimarisha maridhiano ya kisiasa, demokrasia ya vyama, amani na mshikamano wa kitaifa baada ya Uchaguzi Mkuu, pamoja na namna ya kuimarisha ushiriki wa wananchi katika shughuli za maendeleo na kudumisha tunu za umoja wa kitaifa.
Majadiliano hayo pia yaligusia umuhimu wa kuendeleza maadili ya uongozi, uwajibikaji na siasa zenye staha, kama msingi wa kujenga Taifa lenye utulivu wa kisiasa na maendeleo endelevu.
Katika kukuza demokrasia jumuishi, viongozi hao walisisitiza ushirikishwaji wa wadau mbalimbali katika masuala ya kitaifa na mchakato wa maendeleo, sambamba na kulinda utulivu wa kisiasa wakati wa utekelezaji wa mipango ya maendeleo, kwa kutambua kuwa mazingira ya amani na umoja ni msingi wa ukuaji wa uchumi na ustawi wa wananchi.
Sambamba na hilo, walielezea umuhimu wa kuimarisha utamaduni wa uvumilivu wa kisiasa, kuheshimiana na kujenga uaminifu miongoni mwa wadau wa kisiasa, kama njia ya kuendelea kudumisha utulivu wa nchi.
Hali kadhalika, walisisitiza haja ya kuendeleza mazungumzo ya mara kwa mara baina ya viongozi wa kisiasa ili kujenga uelewano wa pamoja na kushughulikia changamoto za kitaifa kwa njia ya mazungumzo na ushirikiano, kwa kutanguliza maslahi ya wananchi na maendeleo ya Taifa.
Mazungumzo hayo yanaakisi dhamira ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuendeleza mawasiliano ya wazi na ya kujenga miongoni mwa viongozi wa kisiasa, kwa lengo la kuimarisha maridhiano na mshikamano wa kitaifa
Shaaban Kissu
K.n.y. Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu