Maalim Seif kuunguruma leo Zbar
Kamati ya Nidhamu yaanza kazi
NCCR kukata mzizi wa fitina leo
Mbunge wa Wawi visiwani Zanzibar, Hamad Rashid Mohamed, amesema iwapo njama za kumngoa katika Chama cha Wananchi (CUF) zitafanikiwa, atakwenda mahakamani au kuanzisha chama kingine cha siasa na si kuhamia katika chama kingine.
Wakati Hamad akisema hayo, Kamati ya Nidhamu na Maadili ya CUF, imeanza kukutana kwa lengo la kukusanya ushahidi wa tuhuma za uasi unaodaiwa na Naibu Katibu Mkuu Tanzania Bara, Julius Mtatiro, kufanywa na Hamad na wafuasi wake, kwa lengo la kukipasua chama hicho.
Hamad ambaye hivi karibuni ameingia katika vita kubwa na Katibu Mkuu, Maalim Seif Sharif Hamad, inayohusisha uongozi katika chama hicho, alitoa kauli hiyo wakati akihojiwa katika kipindi cha Baragumu kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni ya Channel Ten, jijini Dar es Salaam jana.
Kama nilivyowahi kusema hapo awali kuwa mimi si malaya wa kiasiasa, na naendelea kusema mimi si malaya wa kisiasa. Sikuhama CCM (Chama Cha Mapinduzi). Tulifukuzwa mimi na Maalim Seif, Mei 13 mwaka 1988. Nilipata ushawishi mkubwa sana nirudi CCM. Nikawaambia mmenifukuza tumeanzisha chama. Nitakwenda na chama changu hiki hadi last minute (dakika ya mwisho), alisema Hamad.
Alisema kama wanachama kupitia Baraza Kuu la Uongozi wa CUF Taifa wataamua kumfukuza, atakuwa na chaguo la njia mbili za kufanya; ya kwanza itakuwa ni kupinga maamuzi hayo mahakamani na ya pili; kushawishi kuanzisha chama kingine cha siasa na si kujiunga na chama chochote cha siasa.
Kama ni kuunda chama niunde chama kingine na wenzangu. Tukiamua mimi na wenzangu kuwa tunaweza kuunda chama, hatutafanya hivyo. Lakini naamini busara zitatumika kabla ya kufika huko, alisema Hamad. Alisema juzi alipata taarifa kuwa kuna baadhi ya viongozi wa CUF walikwenda jimboni kwake, Wawi, na
kuwauliza wananchi kama wanaweza kutumia utaratibu wa kumuondoa yeye (Hamad) kwa kupitia tawini. Kwa mujibu wa Katiba ya Chama hicho, mwanachama anaweza kufukuzwa kwa kupitia tawini ama Baraza Kuu la Taifa la chama hicho.
Wakasema tayari tumeshakaa katika mkutano wetu na tumeshapitisha azimio letu, lakini jimbo letu na matawi yetu hayaoni kosa la Hamad kama mnataka kumshughulikia Hamad ni huko huko juu (Baraza Kuu la Uongozi Taifa, alisema Hamad. Alisema hiyo inaonyesha kuwa maamuzi yamekwisha kupitishwa kuwa ashughulikiwe, lakini hajapewa nafasi ya kujitetea tuhuma ambazo zimekuwa zikisambazwa katika matawi na majimbo dhidi yake.
Hawa wanaonipandikiza ukorofi kwangu uko wapi? Kesho (leo) muulizeni (Maalim Seif), nyinyi Hamad mmemuandikia barua? Mmemwita katika kikao? Mbona hamshirikishi katika vikao ili wajumbe nao wakapata nafasi ya kuelewa? Kuna tatizo gani la kumuita Hamad? alihoji. Aliongeza: Nawaomba sana Watanzania. Mimi si mkorofi wala sina asili ya ukorofi.
Hoja ni kusimamia principles (misingi). Hilo ni kweli. Misingi nitaisimamia na msingi wa kwanza nasema turudi taasisi. Namuomba sana Katibu Mkuu aniandikie barua aniambie Hamad njoo. Hata anipigie simu njoo ofisini, njoo kwenye kikao, nitakwenda mimi watoe hoja zao.
Alisema alihoji kuhusiana na fedha zilizotumika katika uchaguzi mdogo wa jimbo la Igunga, uliofanyika Oktoba, mwaka huu, lakini hadi sasa hajajibiwa.
Nasikitika sana. Tumetumia Shilingi milioni 307 wakati wa Uchaguzi Mkuu, mimi nilimsaidia mgombea wetu Sh. laki tano. Nimemnunulia t shirt (fulana), uchaguzi umekwisha tumetoka na kura 11,000. Leo wametumia milioni 307 wamekuja na kura 2,000, alisema Hamad.
Aliongeza: Hawaulizi hawa. Hawa ndio mahasibu wa chama. Waulize mmetumiaje helikopta milioni 49 kwa siku tatu? Chenji yetu iko wapi? Mtatiro, hayo ndio maswali ya kuuliza. Milioni 307 zimetumikaje? Ukiuliza hayo unaambiwa ohh una matatizo.
Alisema sasa hivi viongozi wa CUF wamekuwa wakizunguka kila jimbo kwa lengo la kumchafua bila kumshirikisha.
Kwa mujibu wa kituo hicho, Maalim Seif ambaye alikuwa afanye mahojiano ya njia ya simu jana, aliomba kuwa asizungumze kwa kuwa amepanga kukutana na waandishi wa habari kuzungumzia ngogoro huo leo saa 4.00 asubuhi.
KAMATI YA NIDHAMU NA MAADILI YA CUF YAANZA KAZI
Katika hatua nyingine, Kamati ya Nidhamu na Maadili ya CUF, imeanza kukutana kwa lengo la kukusanya ushahidi wa tuhuma za uasi unaodaiwa na Mtatiro, kufanywa na Hamad na wafuasi wake, kwa lengo la kukipasua chama hicho.
Mtatiro alitoa tuhuma hizo Jumanne wiki hii alipozungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
Alitoa kauli hiyo ikiwa ni hatua mpya ya msuguano uliopo kati ya pande mbili za mgogoro ndani ya CUF unaomhusisha Hamad Rashid na Katibu Mkuu, Maalim Seif Sharif Hamad, kuhusu uchaguzi wa viongozi wa chama hicho.
Tayari msuguano huo umekwishasababisha mapigano baina ya makundi ya pande mbili hizo.
Mapigano yalisababisha watu kadhaa, wakiwamo walinzi wa chama hicho, maarufu kama Blue Guard kutoka makao makuu ya chama kujeruhiwa kwa kukatwa mapanga. Akizungumza na NIPASHE jana, Mtatiro alisema baada ya kumaliza kazi ya kukusanya ushahidi huo, kamati hiyo itamwita Hamad Rashid na kundi lake ili kuhojiwa.
Kamati (ya Nidhamu na Maadili) imeshaanza kukutana kwa ajili ya kukusanya ushahidi. Wakimaliza watawaita kuwahoji, alisema Mtatiro. Katika mkutano huo na waandishi wa habari, Mtatiro alisema hatua hiyo itachukuliwa kwa madai kwamba vitendo vinavyofanywa na Hamad Rashid na wafuasi wake ni vya utovu wa nidhamu na pia kinyume cha taratibu halali za chama.
Mbali na kuitwa na kuhojiwa na kamati hiyo, CUF pia iliagiza Blue Guard kumfuatilia Hamad Rashid na wafuasi wake popote watakapofanya mkutano ili kumhoji kama amefuata utaratibu wa kufanya mkutano husika wa chama au la.
Hata hivyo, Mtatiro alisema hajui hatua zitakazochukuliwa dhidi ya Hamad Rashid na wafuasi wake iwapo watakutwa na hatia, lakini akasema kwa mujibu wa Katiba ya chama, wanaweza ama kuonywa, kupewa karipio kali, kusimamishwa au kufukuzwa katika chama.
Chimbuko la hali hiyo linadaiwa ni vuguvugu za ndani kwa ndani za uchaguzi wa viongozi wa chama hicho akidaiwa kutamani kiti cha Katibu Mkuu kitakaachoachwa wazi na Maalim Seif kama ataamua kustaafu. Hamad Rashid analalamika kuwa Maalim Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa ya Zanzibar, ana mwanachama anayemuandaa kwa ajili ya kiti hicho.
Harakati hizo pia zimesababisha viongozi hao wawili kulaumiana juu ya utendaji na ujenzi wa chama Tanzania Bara, huku Hamad Rashid akimlaumu Maalim Seif kwa kutokufanya kazi kubwa ya kisiasa Tanzania Bara.
Miongoni mwa lawama anazobebeshwa Maalim Seif ni kufanya vibaya kwa CUF katika uchaguzi mkuu wa
mwaka jana, ambao chama hicho kilishika nafasi ya tatu huku kikipata idadi ndogo ya wabunge Bara kiasi cha kupoteza nafasi ya kuunda kambi rasmi ya upinzani bungeni nafasi ambayo wameishikilia tangu mwaka 1995.
MAALIM SEIF KUUNGURUMA LEO
Wakati huo huo, Maalim Seif leo atazungumza na waandishi wa habari mjini Unguja. Habari zinasema kuwa kiongozi huyo atazungumzia masuala ya kiserikali, lakini kama yatajitokeza maswali kuhusu chama atayajibu.
NEC NCCR-MAGEUZI KUFANYA KIKAO CHA DHARURA LEO
Naye Katibu Mkuu wa Chama cha NCCR-Mageuzi, Samwel Ruhuza, alisema jana kuwa karibu wajumbe wote wa Halmashauri Kuu (NEC) wamewasili kwa ajili ya kuhudhuria kikao cha dharura kinachofanyika jijini Dar es Salaam leo.
Hata hivyo, Ruhuza alikataa kutaja idadi ya wajumbe wa NEC waliowasili, badala yake alisisitiza kuwa ni wajumbe wachache tu ambao kufikia jana mchana walikuwa hawajawasili.
WAZEE NCCR-MAGEUZI WAPINGA MBATIA KUNGOLEWA
Nao wazee wa NCCR-Mageuzi Mkoa wa Dar es Salaam wamesema vigezo vilivyotolewa na wajumbe 28 wa NEC kutaka Mwenyeketi wa Chama hicho Taifa, James Mbatia, ajiuzulu, havina msingi.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam kwa niaba ya wenzake jana, Katibu wa Kitengo cha Wazee cha NCCR-Mageuzi, Ernest Mwasada, alisema vigezo hivyo mbali ya kuwa havina msingi, vimetolewa kinyume cha taratibu za chama.
Alisema hata kama Mbatia ana makosa kuna vikao vya chama ambavyo vinapaswa kutumika tofauti na inavyofanyika hivi sasa kwa baadhi ya watu kutangaza kupitia vyombo vya habari.
Maswada alisema wanaofanya hivyo, wanafanya kwa maslahi binafsi na si kwa mapenzi ya chama.
Alisema Mbatia amekuwa msaada mkubwa kwa chama na kwamba, tuhuma zote zinazoelekezwa kwake ni uzushi na wanaomtuhunu wanafanya hivyo kwa lengo la kujitafutia umaarufu.
Maswada alisema umaarufu huo wameshindwa kuupata ndani ya chama kwa njia za demokrasia na pia ni waroho wa madaraka. Alisema kwa mfano kigezo kwamba, Mbatia amekuwa akishidwa katika chaguzi anazogombea, hivyo ni halali kungolewa hakina msingi, kwa vile kuna viongozi pia wameshindwa zaidi ya mara mbili, lakini bado wapo madarakani.
Kuhusu Mbatia si mwaminifu kwa madai kwamba, ameonekana kukitetea Chama Cha Mapinduzi (CCM), alisema hawawezi kumsemea hilo kiongozi huyo na kwamba, tuhuma ana nafasi kuzijibu mwenyewe. Hata hivyo, alisema wanachokitaka wao, ni kuona haki ikitendeka na watu kutokuwatumia wengine kwa maslahi binafsi. Alisema tuhuma dhidi ya Mbatia, zimekuwa zikitolewa hasa na watu wenye asili ya Mkoa wa Kigoma, hali inayoonyesha dalili zote za kutaka kutengenezwa ukabila ndani ya chama.
Walipendekeza watu hao kufikishwa kwenye Kamati ya Nidhamu na Usuluhishi mara moja ili wakajibu hoja zilizopo kwenye kanuni na baadaye Sekretarieti ya chama iwaandakie barua ya kujieleza mbele ya NEC. Pia chama kipate muda wa kujiandaa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, ikiwa ni pamoja na watu hao kuvuliwa uanachama.
TENDWA: CUF, NCCR-MAGEUZI ACHENI MALUMBANO
Msajili wa Vyama Vya Siasa nchini, John Tendwa, ameitaka CUF na NCCR-Mageuzi, kutumia njia ya mazungumzo kutatua malumbano ya viongozi yanayoendelea ili kustawisha na kudumisha demokrasia ndani ya vyama hivyo.
Tendwa alisema hayo jana jijini Dar es Salaam kwenye Mkutano wa 18 wa Hali ya Siasa Tanzania ulioandaliwa na Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, chini ya Mpango wa Utafiti na Elimu ya Demokrasia Tanzania (Redet).
Alisema hayo kujibu swali aliloulizwa na waandishi wa habari waliotaka kujua sababu za yeye kutoingilia kati malumbano yanayoendelea ndani ya vyama hivyo kwa minajili ya kuyatatua.
Ninachoweza kusema sijaingilia kutatua yanayoendelea CUF na NCCR kwa sababu sijaombwa kufanya hivyo na vyama vyenyewe pamoja na ukweli kuwa mimi ni mlezi wa vyama vya siasa kama msajili nchini, alisema Tendwa.
Imeandaliwa na Sharon Sauwa (Dodoma) na Muhibu Said, Loveness Massero na Raphael Kibiriti (Dar).
CHANZO: NIPASHE