Hadithi ya kusisimua: Mkataba wa siri - 2

Hadithi ya kusisimua: Mkataba wa siri - 2

Joined
Feb 9, 2014
Posts
20
Reaction score
6

MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
ILIPOISHIA...
“Lazima niwapitie wenzangu kwanza.”
“Wako wapi?”
“Si mbali, ni hapo Tangibovu.”
“Kwa hiyo?”
“Twende, we fuata maelekezo yangu tu.”
“Sawa.”
SASA ENDELEA...

GARI lilipofunga breki tu, tayari wale watu walishafungua milango na kuingia ndani ya gari. Tayari walishaelezwa dharura iliyotokea nyumbani kwa hiyo walifanya haraka haraka bila kupoteza muda.
Hapakuwa na mazungumzo ndani ya gari, Suma alikimbiza kama limeibiwa, robo saa tu baadaye alikuwa anaegesha nje ya geti lake. Aliogopa hata kuingiza ndani ya geti kwa kuhofia moto.
Walishuka wote watano, Suma, Ustaadhi Alii na wenzake watatu.
“Fungua mlango Suma,” Ustaadhi Alii akamwambia.
“Naogopa.”
“Huna haja ya kuogopa, fungua tu.”
Suma akasukuma mlango mdogo wa geti. Wakaingia kwa pamoja. Suma alikuwa akitembea taratibu huku akiogopa sana. Mazingira yalimshangaza sana. Nyumba ilikuwa kimya kabisa kama vile hapakuwa na kitu kilichokuwa kikitokea ndani.
Kwa moto aliouacha alitegemea kukuta tayari moto umeshasambaa nyumba nzima. Haikuwa hivyo. Kwa mwendo wa taratibu, Suma akatembea hadi barazani kwake na kusimama hapo kisha akamwangalia Ustaadhi Alii akionekana dhahiri alitaka kusikia maelekezo kutoka kwake.
“Simama.”
Suma akasimama. Ustaadhi Alii akawaonyesha wenzake ishara akimaanisha kwamba wazungushe duara dogo kwa kushikana mikono. Wakafanya hivyo. Mara wakaanza kusoma dua kila mmoja kwa wakati wake. Zoezi hilo liliendelea kwa dakika tano kisha baadaye wakaanza kusoma kwa kuelekezana...
Suma alibaki amesimama palepale barazani akiwa ameiinua mikono yake juu akimuomba Mungu akubali dua ile ili mabalaa yamuondoke. Alikuwa kwenye wakati mgumu sana.
Baada ya muda, dua ikamalizika. Suma akawakazia macho kusikiliza maelekezo mengine.
“Iingia ndani Suma,” Ustaadhi Alii akamwambia.
“Naogopa moto.”
“Hakuna moto.”
Suma akafungua mlango na kuingia sebule, wale watu wakiongozwa na Ustaadhi Alii nao wakaingia. Wote kwa pamoja wakaketi kwenye viti vilivyokuwa pale sebuleni.
“Vipi, moto uko wapi sasa?”
“Ulikuwa unatokea chumbani.”
“Haya fungua huo mlango wa chumbani.”
“Hapana hapana, hilo siwezi kufanya.”
“Suma.”
“Naam Ustaadhi.”
“Fungua mlango wa chumbani.”
Suma kwa woga sana akausogelea na kuufungua ule mlango, akaangalia ndani...hapakuwa na moto na kila kitu kilikuwa vilevile. Alijikuta akipiga kelele kwa hofu. Ustaadhi Alii akamfuata nyuma na kuingia kule chumbani.
“Usiogope tumeshasoma dua, hakuna madhara yoyote humu ndani,” akasema Ustaadhi Alii.
“Hata mimi nimeamini.”
“Hebu sasa turudi sebuleni.”
“Sawa.”
Wakaongozana hadi sebuleni, wakaketi kwenye viti. Utulivu wa muda ukapita wote wakiwa hawazungumzi chochote. Ustaadhi Alii alionekana kuwa na mawazo sana, alikuwa kwenye fikra nyingi sana akijaribu kuwaza juu ya tukio lile.
“Ni kweli umedhamiria kubadilisha mfumo wa maisha yako?” Ustaadhi Alii akamwuliza Suma.
“Ndiyo Ustaadhi.”
Akatulia tena kwa muda. Alimeza funda kubwa la mate, kisha midomo yake ikaanza kutingishika. Ni dhahiri sasa alidhamiria kuanza kuzungumza tena. Kweli, Ustaadhi Alii alikuwa akizungumza...
“Si umesema mkeo ndiye aliyekuwa akikutokea na kupiga makelele kuwa umemtesa na kumsababishia maumivu?”
“Ndiyo.”
“Una uhakika ni yeye?”
“Kabisa.”
“Kuna kitu nahisi, lakini kabla sijafika huko nataka kuuliza jambo moja la msingi sana.”
“Ndiyo niulize tu.”
“Huyo mkeo ulimchunguza vizuri kabla ya kuoana?”
“Sana Ustaadhi, sana.”
“Ulifunga naye ndoa?”
“Tena nyumbani kwao, mbele ya wazazi wake.”
“Sawa, hebu turudi katika upande wa pili...mambo yote haya yanayotokea yana sababu zake bila shaka. Unaweza kutusimulia vizuri ili tuweze kupata mwanga zaidi wa kumaliza tatizo lako?”
“Bila shaka yoyote Ustaadhi.”
“Enhee...unaweza kuanza basi, sisi tunakusikiliza,” akasema Ustaadhi Alii.
Wote walikuwa kimya wakijiandaa kumsikiliza Suma. Ni kweli alionekana kuwa na kitu kikubwa sana katika maisha yake. Suma alidhamiria kueleza ukweli wa ndani kabisa. Hakuwa na haja ya kuficha kitu chochote.
“Ni kweli ni stori ambayo huwa sipendi kabisa kuikumbuka, lakini kwa sababu nimeshaamua kubadilika na kuanza maisha mapya, inanipasa sasa nieleze kilichotokea...” akasema Suma.
“Sawa.”
“Lakini naamini kuna sehemu zinaweza kuwachukiza, naomba unisamehe maana nitawaeleza ukweli wa kila kitu kilichopata kutokea katika maisha yangu ya nyuma.”
“Usiwe na wasiwasi juu ya hilo Suma.”
Suma aliangalia juu, kisha akarudisha macho yake tena chini akitafakari mahali pa kuanza kueleza historia yake. Alifikiria kwa muda, hatimaye alipata mahali pa kuanzia.
“Nakumbuka vizuri sana...ilikuwa ni Moshi...” Suma akaanza kusimulia.
***
MOSHI - KILIMNJARO
Suma aliendelea kukaza macho kwenye ubao wa matangazo ya sinema nje ya kibanda cha kuonyesha muvi cha Baba Lau Cinema. Aliendelea kukaza macho yake kwa umakini mkubwa kama vile alikuwa akitafuta kitu muhimu.
Ni kama mwanafunzi aliyekuwa akiangalia majina ya watu waliochaguliwa kujiunga na chuo fulani wanavyofanya. Haikuwa hivyo, alikuwa akiangalia ratiba ya filamu zitakazoonyeshwa hapo kwa Baba Lau.
“Mh!” akaguna Suma baada ya kuangalia sinema itakayooneshwa saa 8:00 mchana.
Ilikuwa ni sinema ya Jack Chun. Akashuka chini kukaza macho tena. Akaangalia kwa umakini zaidi...
Saa 10:00 – Delta Force
Saa 1:00 Anold Schwarzenegger
Saa 3:00 Amitha Batchan
“Aaaah! Huyu jamaa bwana sijui vipi?” akasema kwa sauti kubwa kiasi kisha akasonya kwa hasira.
Suma hakuzipenda kabisa hizo sinema. Ilikuwa tofauti sana na wenzake waliokuwepo pale, walionekana kufurahishwa sana na ratiba hiyo.
“Daaah! Siwezi kukosa kumwangalia Amitha, lazima nije...” mmoja wa vijana waliokuwa pale akasema huku akimwangalia mwenzake.
“Tatizo ni ndefu sana, kwanza angalia muda wenyewe,inaanza saa tatu usiku, kuisha kwake ni hadi saa sita!”
“Hata kama ni mpaka asubuhi, mimi lazima nije. Huyu jamaa ananikosha sana. Kwanza sinema zao hazichoshi...kidogo wanapiga na wimbo kabisa. Yaani safi sana!”
“Kuchukuchu hotahe....ha ha ha ha...acha kunichekesha wewe!”
“Nyie mnazungumza nini?” Suma akapaza sauti.
“Kwani vipi Suma?”
“Mimi sijaona sinema ya maana hata moja hapo.”
“Unataka filamu gani sasa?”
“Mambo yangu huyajui?”
“Nini?”
“Vampire!” (Majini)
“Aaaah! Mimi naogopa sana kuangalia filamu za majini.”
“Sasa mimi ndiyo huniambii kitu kuhusu hizo filamu, yaani hapa sina raha kabisa, ngoja niondoke zangu,” akasema Suma huku akianza kupiga hatua za taratibu kuondoka mahali pale.
Kabla hajageuka, Baba Lawrance ambaye alifupishiwa jina na kuitwa Baba Lau alitokea...
“Afadhali nimekuona Baba Lau.”
“Suma hata salamu?”
“Nilijua ningekusalimia tu....shikamoo mzee.”
“Marhaba, vipi kuna tatizo?”
“Tena kubwa sana.”
Baba Lau akashtuka sana. Alitumia dakika nzima kutafakari hilo tatizo kubwa. Mawazoni mwake aliamini Suma alikuwa ameibiwa ndani ya banda lake la video. Akamkazia macho sawasawa.
Sauti yake ilikuwa kavu iliyotoka kikakamavu wakati akimwuliza Suma kwa mara ya pili...
“Lipi hilo?”
“Kwa nini hamna usawa?”
“Kivipi?”
“Mimi ni mteja wenu wa siku nyingi sana, lakini mbona mnaweka filamu za aina moja tu?”
“Kwani wewe unataka filamu gani?” akauliza Baba Lau ingawa alishajua kuwa alihitaji nini.
“Nataka sinema za majini, unajua zile zinafundisha mambo mengi ndiyo maana napenda kuangalia, halafu sipo mwenyewe, wengi tu wanapenda filamu za hivyo.”
“Sawa nimekuelewa vizuri Suma, kesho nitaweka.”
“Haya ahsante sana,” akasema Suma huku akiaga.
***
Ilikuwa ghafla tu, hata leo hii ukimwuliza Suma ni kwa nini anapenda kufahamu kuhusu majini, hajui. Kuna tukio moja ambalo halikumbuki. Ni siku aliyoangalia filamu ya majini yenye hadithi ya mapenzi iitwayo Even Devils Loves (Hata Majini Wanapenda).
Ni filamu hiyo ndiyo iliyobadilisha mtazamo wake kuhusu mapenzi. Ilikuwa na hadithi inayoonesha namna ambavyo majini wanaweza kupenda, kujali na kumthamini mwanadamu bila kumdhuru.
Mapenzi ya majini katika sinema hiyo, yalikwenda mbali zaidi na kuonesha namna ambavyo yanaweza kubadilisha maisha ya mtu ambaye ameingia naye kwenye mapenzi. Akajikuta akitamani kuwa yeye!
Msisimko alioupata ulikuwa mkubwa sana. Pamoja na kufikisha umri wa miaka 22, akiwa tayari ameshamaliza elimu yake ya kidato cha nne, hakufikiria kabisa suala la kuoa binadamu. Alitamani kuoa jini.
ITAENDELEA KESHO, HAPAHAPA…
 
MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
ILIPOISHIA...
Msisimko alioupata ulikuwa mkubwa sana. Pamoja na kufikisha umri wa miaka 22, akiwa tayari ameshamaliza elimu yake ya kidato cha nne, hakufikiria kabisa suala la kuoa binadamu. Alitamani kuoa jini.
SASA ENDELEA...

Aliamini hao ndiyo wangeweza kuwa na upendo wa dhati, wasingemtesa wala kumnyanyasa. Hapo ndipo kulipokuwa na tatizo. Kwa Mkoa wa Kilimanjaro, tena akiwa anaishi katika Manispaa ya Moshi Mjini, katika kitongoji maarufu cha Njoro, stori za majini hazikuchukua nafasi kubwa sana kwa wakazi wa eneo hilo.
Alikulia mikononi mwa wazazi wake wenye kipato cha kawaida kabisa, tena wakiwa wanaishi nyumba ya kupanga hapo Njoro. Walichoweza kufanya kwake, ilikuwa ni kumsomesha kwa uwezo wao wote. Kwa fedha za kuokoteza kwa kufanya biashara ndogondogo na vijibarua visivyo na uhakika!
Alisoma Shule ya Msingi Njoro na baadaye akachaguliwa kujiunga na Shule ya Sekondari JK Nyerere ambapo kwa bahati mbaya hakufanikiwa kuchaguliwa na elimu ya juu zaidi kwa sababu alipata dalaja la nne!
Kwa namna alivyofundishwa na wazazi wake, kwa Suma maisha hayakuwa magumu sana, kwani aliamua kufanya vibarua mbalimbali ili aweze kujikimu. Hakutaka kujihusisha kabisa na mambo ya wasichana.
Alikuwa na msimamo mkali sana kuhusu mambo ya wasichana. Jambo hilo liliwashangaza wengi wakiwemo wazazi wake, maana hata siku moja, hawakuwahi kusikia Suma alikutwa amesimama na msichana mahali.
Miaka mitatu ilipita baada ya kumaliza kidato cha nne, kwa kudunduliza fedha zake, aliweza kupanga chumba chake na kununua vitu vyake vya ndani kisha akahamia Kitongoji cha Majengo. Wengi waliamini Suma alihama kwa lengo la kukwepa maneno ya watu.
Hilo hakujali.
Aliangalia sana maisha yake na namna alivyotamani yawe. Siri kubwa ilikuwa ndani ya moyo wake. Ni kweli alitamani sana kuoa, lakini si binadamu. Alitaka jini! Angempataje? Hilo lilibaki kuwa swali gumu lililomtesa kichwa chake.
“Yes...even devils loves,” (Ndiyo...hata majini wanaweza kupenda) aliwaza Suma akikumbuka sehemu ya jina la ile sinema aliyoiangalia.
“Kwa nini nisioe jini? Mimi sitaki usumbufu na hawa binadamu wenzangu,” akawaza Suma.
“Halafu maisha magumu niliyonayo, nitawezaje kuogeza mtu mwingine wa kunitegemea ambaye naye atazaa wengine na kunizidishia machungu katika hii dunia yenye ubaguzi?
“Ona wenzangu...mbona wanaishi vizuri. Wana majumba ya kifahari, magari na biashara za uhakika...mimi nitawezaje? Nahitaji msaada hakika na mahali pekee nitakapoweza kupata ni kwa majini. Lazima nitampata tu,” akazidi kuwaza Suma.
Ni mawazo yaliyomtesa sana kichwa chake. Hakutaka mateso wala shida maishani mwake. Alihitaji kustarehe na kutulia. Alihitaji faraja ya moyo hakika. Kwake, hapakuwa na binadamu ambaye angekuwa na uvumilivu kama majini aliowaona kwenye sinema za majini.
“Lazima hilo litimie,” akazidi kuwaza.
***
Walikuwa wanawake wawili tu barabarani, wakitembea kwa miguu, vikapu vikiwa juu ya vichwa vyao. Walitokea kununua mahitaji katika soko maarufu la vyakula mjini Moshi – Mbuyuni. Walishavuka kwenye mto mdogo unaopitisha majitaka maarufu kwa jina la Maji Machafu, wakishika njia pembeni ya kiwanda cha zamani cha Pepsi.
Hawa ni mama Suma na mama Mwaija. Kama kawaida ya wanawake, walizungumza mengi sana. Waliongelea ndoa, wakajadili kuhusu maisha na baadaye wakaanza kuwateta watu. Stori zilipoisha, mama Mwaija akaanza mpya...
“Halafu mwenzangu kuna jambo nimelisikia mitaani limeniuma sana, nimelivumilia sana lakini naona limenifika hapa, siwezi kuacha kukuambia, wewe ni shoga yangu.”
“Nini hicho mama Mwaija?” akauliza mama Suma.
“Ni kuhusu mwanao.”
“Yupi sasa? Mwenyewe unajua nina watoto wanne.”
“Suma.”
“Nini tena?”
“Hivi mtoto wenu mzima kweli?”
“Kivipi yaani?”
“Maneno niliyoyasikia, mbona yanatisha? Inasekana eti hawezi kitu!”
Mshtuko mkubwa ukaingia moyoni mwa mama Suma. Zaidi ya mara tatu neno lile likajirudia kichwani mwake; ‘Hivi mtoto wenu mzima kweli?’. Maumivu yasiyoelezeka yakauvamia moyo wake. Hata hivyo hakujua uzima uliozungumziwa.
Alitaka kufungua kinywa chake aulize, akahisi kama kuna kitu kinamkaba na kumzuia kufanya hivyo.
“Mwanangu anaumwa nini?” akajiuliza mwenyewe.
“Lakini haina maana kuumiza kichwa wakati naweza kuuliza,” akajisemea moyoni.
Ukweli ni kwamba siyo hakuweza kuuliza ila aliogopa na hakuwa tayari kusikia tatizo la mwanaye mpendwa. Ya nini ajitese? Kwa nini abaki na maswali? Akaamua kuvunja ukimya...
“Kivipi yaani?”
“Maneno niliyoyasikia, mbona yanatisha? Inasekana eti hawezi kitu!” mama Mwaija akagongelea msumari.
“Mh!”
“Unaguna nini mwenzangu, ndiyo mambo yanayosemwa huko mitaani.”
“Unadhani ni kwa nini wanasema hivyo?”
“Haya mambo yameanzia mbali, inasemekana kwanza hajawahi kuonekana na mwanamke yeyote wa mtaani, halafu kingine ilifikia hatua Tatu akamwambia wazi kuwa anampenda, mwanao akamtukana sana nusu ampige kwa sababu eti alimwambia mambo ya kijinga!”
Mama Mwaija alikuwa anamzunguzia Tatu, mtoto wa mzee Mvungi ambaye anasifika kwa uzuri mtaa mzima. Watu wenye fedha zao waligongana vikumbo kumgombea msichana huyo bila mafanikio. Leo hii eti Suma anatamkiwa na malkia huyo kuwa anampenda halafu anamkataa!
Lazima ushangae!
“Mh! Lakini labda hajamtaka!” akajibu mama Suma kwa lengo la kujiondolea aibu.
“Sawa ila sasa hata akiwa na wenzake, wakianza kuzungumzia mambo ya wasichana huonekana anakasirika na kuondoka zake.”
“Sina uhakika na hili jambo.”
“Usinitaje, mimi nimekuambia tu kama shoga yangu. Sisi wote ni wazazi.”
“Sawa.”
“Lakini jambo lingine linalowashtua zaidi watu ni tabia yake ya kujipenda kupita kiasi. Muda wote msafi, ananukia marashi, ananyoa vizuri, anavaa nguo nzuri...kwanini ajipende hivyo kama mtoto wa kike? Mchunguze mwanao shoga yangu!”

ITAENDELEA KESHO...
 
MKATABA WA SIRI
SEHEMU YA NNE


MTUNZI: JOSEPH SHALUWA
ILIPOISHIA...
“Lakini jambo lingine linalowashtua zaidi watu ni tabia yake ya kujipenda kupita kiasi. Muda wote msafi, ananukia marashi, ananyoa vizuri, anavaa nguo nzuri...kwanini ajipende hivyo kama mtoto wa kike? Mchunguze mwanao shoga yangu!”
SASA ENDELEA...

Mama Suma alikuwa kimya kabisa, hakuwa na la kujibu, tayari walikuwa wameshaingia mtaani kwao. Mama Mwaija akaagana na mama Suma ambaye nyumbani kwake ilikuwa mtaa wa pili.
***
Siku nzima mama Suma alishinda na mawazo. Maneno aliyoambiwa na mama Mwaija yalimuumiza sana. Hayakuwa mambo mapya kwake, ila alishtuka baada ya kugundua kwamba kumbe yanajulikana na watu walishaanza kuyajadili!
Hata yeye mwenyewe alikuwa na mawazo sana juu ya tabia ya mwanaye kujipenda kupita kiasi. Jambo lingine lililomtesa ni kutokana na tabia yake ya kutopenda kabisa kuwa karibu na wanawake.
“Mwanangu jamani, hivi inawezekana ni kweli anafanya huo mchezo?” akawaza mama Suma.
“Lakini ngoja nitazungumza na baba yake, lazima nitafute ukweli wa hili jambo, ni aibu sana kwa familia yangu,” akaendelea kuwaza.
Jioni mumewe alivyorejea kutoka kazini, jambo la kwanza kuzungumza naye lilikuwa ni juu ya Suma.
“Kuna nini tena mke wangu?”
“Zungumza na mtoto, Suma anapotea.”
“Kivipi? Bado una yale mambo tu?”
“Siyo ninayo? Hata mtaani sasa wameanza kuyazungumza.”
“Mtaani?”
“Ndiyo.”
“Kivipi?”
Mama Suma akamsimulia mumewe kila kitu jinsi alivyozungumza na mama Mwaija. Baba Suma alishtuka sana, hakutegemea kama mwanaye angekuwa akisemwa hivyo mitaani.
“Ngoja nitakwenda kuzungumza naye.”
“Ndiyo maana alivyoamua kujitegemea amekwenda kupanga Majengo, hataki kukaa hapa mtaani kwa sababu wameshajua tabia yake.”
“Mke wangu acha kumhukumu mtoto kabla hujawa na uhakika, Jumapili nitakwenda kwake, nitajua huko huko.”
“Rajabu ameshaoa, Elibariki ana mchumba, Meshack ndoa yake ilikuwa Jumamosi iliyopita, wote hawa amemaliza nao shule, mbona yeye hana hata mtoto wa kusingiziwa mitaani? Lazima kuna kitu,” akasisitiza mama Suma.
“Nimesema nipe muda nikazungumze naye, ukweli utajulikana mke wangu,” akasema baba Suma.
“Sawa.”
***
Alichelewa sana kutoka kazini siku hiyo, tayari ilikuwa imeshatimu saa moja na dakika zake za jioni. Alikuwa amechoka sana lakini pia alikuwa na hamu ya kujua mengi zaidi kuhusu majini.
Alikuwa amesimama kwenye duka maarufu la viatu mjini Moshi liitwalo Bora, akakumbuka kwamba katika jengo lilelile kuna ukumbi wa sinema wa Plaza. Asingeweza kwenda hadi Majengo akawahi kuangalia kwenye vibanda vya mitaani wakati ukumbi ulikuwa pale pale.
“Tatizo watakuwa na hiyo filamu?” akawaza.
“Ngoja nijaribu,” akajisemea.
Akapandisha juu haraka, ambapo alipita mbele ya duka la vifaa vya ujenzi la Njiwa Hardware, akapanda hadi kwenye ubao wa matangazo ya filamu katika Ukumbi wa Plaza Cinema.
Saa 12:00 jioni – Game in Forest (Billy Blanks)
Saa 2:00 usiku – Vampire’s With True Love (Sarafina Hollins)
Saa 4:00 – Shamba Kubwa - Kiswahili (Mzimuni Theatre Group)
Wengi walikuwa wakifurahia sana kuona kwamba kuna Filamu ya Shamba Kubwa ambayo ni ya Kiswahili. Ilikuwa filamu ya kwanza ya Kiswahili kuoneshwa katika ukumbi huo. Ingawa ratiba ilionesha kwamba ingeoneshwa saa 4:00 usiku, walikuwa tayari kusubiri!
Kwa Suma ilikuwa tofauti kabisa, alirukaruka juu kwa furaha alipoona Filamu ya Saa 2:00 usiku – Vampire’s With True Love, pamoja na elimu yake ya kawaida ya kidato cha nne, aliweza kupata tafsiri rahisi kuwa, sinema ile ilikuwa juu ya majini wenye upendo wa kweli.
“Haya ndiyo mambo ninayoyataka sasa,” akasema moyoni mwake kisha akatoka na kuvuka barabara.
Moja kwa moja aliingia kwenye Mgahawa wa Shaonaro kwa lengo la kupata chakula ili kuvuta muda wa kuingia kwenye sinema. Alikula kijeshi, robo saa kabla ya sinema kuanza tayari alikuwa dirishani akikata tiketi – alichosubiri ilikuwa ni muda tu!
Dakika zilikwenda taratibu sana, lakini hatimaye akaona watu walioingia saa 12 wakitoka, haraka akatupa macho yake kwenye saa yake ya mkononi, zilibaki dakika tano tu. Watu walipoisha, akaingia zake ukumbini na kukaa siti za mbele kabisa akisubiri muda ufike.
Saa 2:00!
Sinema ikaanza!
***
“Majengo Polisi....” sauti ya konda ilisikika akiuliza abiria wake.
“Shusha!” Suma akasema kwa sauti kubwa kwa kuwa alikuwa amekaa siti ya nyuma.
“Polisi?!!!”akauliza tena.
“Amesema shusha....tatizo nyie makonda huwa mnauliza abiria halafu mnatoa vichwa nje, mtasikiaje?” abiria mmoja akadakia.
“Tuliza mzuka, nimesikia.”
Daladala ile iliyotokea Mbuyuni kuelekea Kiboriloni ilisimama kwenye makutano ya barabara ya kuelekea Kituo cha Polisi Majengo. Suma akalipa nauli na kushuka zake, akavuka barabara na kuanza kutembea taratibu.
Akiwa anakaribia kufika Posta, akakutana na msichana mrembo sana. Alikuwa mweupe, mrefu, mwenye tabasamu pana, aliyevalia gauni aina ya dira. Suma alivutiwa naye sana, akamwangalia kwa muda mrefu sana bila kupepesa macho. Alivyokutana naye kabisa, akajifanya kuangalia pembeni.
Walivyopishana, Suma akageuza shingo; akakutana uso kwa uso na yule msichana. Alikuwa na tabasamu pana sana. Wote wakasimama.
“Si vibaya tukisalimiana,” yule msichana akasema akitabasamu.
Suma hakuwahi kupata mshtuko wa moyo kama wakati huo. Alihisi moyo wake kama umepigwa shoti ya umeme baada ya kusikia sauti tamu ya yule dada. Hakukumbuka kama hakumjibu ila naye aliendelea kutabasamu.
“Mambo vipi?” yule dada akasalimia.
“Poa, mzima?” akaitikia Suma.
“Wa afya.”
Wakapeana mikono.
“Mimi naitwa Zakhia, sijui mwenzangu?”
“Suma.”
“Unaishi mitaa gani?”
“Hapo chini, jirani na Makando Bar.”
“Sawa.”
“Wewe je?”
“Nakaa nyuma ya nyumba ya Kishamba Dispensary.”
“Ahsante, nimefurahi kukutana na wewe.”
“Hata mimi pia, ingawa nataka kukuambia jambo litakalokushangaza kidogo,” akasema Zakhia.
“Jambo gani hilo la kushangaza?”
“Samahani lakini, usinielewe vibaya.”
“Niambie.”
“Suma mimi ni mwanamke, najua sina haki ya kueleza hisia zangu kwa mwanaume kwa sababu wengi wanachukulia kama ni tabia mbaya, lakini naogopa kuacha kufanya hivi kwa muda huu maana sina uhakika wa kukutana tena na wewe...” akasema Zakhia kisha akatulia kwa muda.
Pumzi ndefu zilivutwa puani mwa Zakhia, kisha akaanza kuzishusha taratibu kabisa. Suma alikuwa kimya akimsikiliza. Alishahisi jambo lililokuwa njiani kumfikia...
“Hisia? Hisia gani hizo Zakhia?”
“Nakupenda sana!”
Suma akakunja uso.
“Samahani Suma, usinielewe vibaya tafadhali, ni hisia za moyo wangu. Nilijua ungenifikiria vibaya, lakini sina namna ya kuficha hisia hizi wakati ni kweli ninakupenda kutoka ndani ya moyo wangu.”
“Samahani sana Zakhia.”
“Niambie tu!”
“Wewe ni mwanamke mrembo sana, lakini hatuwezi kuwa wapenzi.”
“Kwanini?”
“Basi tu!”
“Au una mtu wako?”
“Sina.”
“Hujanipenda?”
“Hapana.”
“Bali tatizo ni nini sasa?”
“Tatizo ni msimamo wa maisha.”
“Unamaanisha nini?”
“Katika maisha yangu sijapanga kumuoa mwanamke na kumuoa.”
“Kwanini?”
“Ni utaratibu tu.”
“Kwahiyo hutaoa?”
“Hapana...natarajia kuoa lakini siyo bi....” Suma akakatiza sentesi yake baada ya kujisahau na kutoka kumponyoka neno ambalo hakutaka lisikike.
Zakhia akashtuka sana. Hakuelewa alichokuwa akimaanisha Suma. Haraka neno likamponyoka: “Sijakuelewa.”
“Samahani, kwaheri,” akasema Suma kwa sauti ya ukali kidogo kisha akaondoka zake.
“Watu wengine kwa kuingilia maisha ya wenzao bwana...sijui balaa gani hili?” akawaza kichwani mwake Suma.
Zakhia alibaki amesimama kwa mshangao akimsindikiza Suma kwa macho hadi alivyoishilia. Hakuwa na jibu sahihi juu ya yale yaliyotokea.
***
Mtu aliyekuwa akigonga mlangoni asubuhi hiyo ndiye aliyemshtua Suma usingizi. Ilikuwa Jumapili, saa 2:30 za asubuhi. Muda ambao kwa siku ya mapumziko kama hiyo huwa yupo kitandani hadi saa 4. Akatoka kitandani na kusogea hadi mlangoni, akafungua.
Alikuwa ni baba yake mzazi.
“Kumbe baba, karibu sana baba...” akasema Suma kwa furaha.
“Ahsante.”
“Shikamoo mzee.”
“Marhaba,” akaitikia akionekana hana furaha kabisa usoni mwake.
“Vipi baba, mbona kama haupo sawa? Kuna tatizo gani?”
“Tatizo lipo Suma mwanangu, tena tatizo kubwa sana lakini leo nahitaji hili tatizo liishe.”
“Ni nini baba?”
“Matusi tunayotukanwa sasa yanatosha. Njoro nzima inatutusi kwa sababu yako. Umetuvua nguo mwanetu.”
“Ni juu ya nini baba?”
“Wewe una tatizo gani?”
“Kuhusu nini baba?”
“Kwanini hutaki kuoa?”

ITAENDELEA KESHO...
 
MKATABA WA SIRI – 5

MTUNZI: JOSEPH SHALUWA

ILIPOISHIA...
"Matusi tunayotukanwa sasa yanatosha. Njoro nzima inatutusi kwa sababu yako. Umetuvua nguo mwanetu."
"Ni juu ya nini baba?"
"Wewe una tatizo gani?"
"Kuhusu nini baba?"
"Kwanini hutaki kuoa?"
SASA ENDELEA...

"Ni hilo tu baba?"
"Kwani dogo?"
"Hapana mzazi wangu, nipe muda nijipange baba. Tatizo ni maisha hakuna kingine."
"Unataka maisha gani zaidi ya haya?"
"Baba sina fedha, nitamtunza vipi mwanamke?"
"Mwanangu kila mtu huja na riziki yake. Kuoa ni faradhi, utajiwekea riziki mwenyewe mpaka utashangaa. Tafadhali nisikilize baba yako, mambo yanayozungumzwa kuhusu wewe ni makubwa sana, kikubwa ninachokuomba oa mwanangu. Kama huna mwanamke sema nikutafutie mimi mwenyewe, nimechoka na haya matusi ya mtaani."
Suma alitulia kwa muda, akatafakari sana kisha akamwangalia baba yake...
"Nimekuelewa baba, nipe muda nitakuwa nimekamilisha hili suala."
"Muda gani?"
"Miezi sita inatosha."
"Mingi sana."
"Baba ulichoniambia siyo chepesi kiasi hicho, ndiyo maana nimekuomba unipe miezi sita nitakuwa nimeshapata mtu sahihi."
Baba yake akatingisha kichwa kukubaliana na jibu la mwanaye.
"Tafadhali na iwe hivyo."
"Nakuahidi baba."
"Sawa, ngoja mimi nikuache sasa."
Suma akafungua droo la kabati la nguo, akatoa fedha kidogo na kumpatia baba yake. Hawakuwa na mazungumzo zaidi, mzee huyo akaondoka.
Kichwani mwa Suma kulikuwa na mwanamke mmoja tu; Zakhia! Ingawa hakutaka kuharibu mipango ya maisha yake, lakini aliona si vyema kuwaudhi wazazi wake, Zakhia ndiye mwanamke pekee ambaye angekidhi kuwa mke wake!
"Alisema anakaa kwa Kishamba....nitamfuatilia, tena leo hiihii!" akajisemea kwa sauti ya chini.
"Lakini pia sitakiwi kuacha wazo langu lipotee. Nitamfuatilia lakini wakati huo huo nitandelea kufikiria namna ya kupata jini wangu wa kuoa. Nimeshasikia maneno eti natakiwa kupuliza manukato makali chumbani, ngoja nitajaribu kufanya hivyo.
"Hapa inabidi nitumie mbinu mbili kwa wakati mmoja. Najua nitafanikiwa tu. Hawa wazee nao wananiingilia sana kwenye mambo yangu. Ngoja nitaona mwisho wake," Suma akawaza.
Akajirudisha kitandani.
***

Aprili 14, 1996
Majengo, Moshi – Kilimanjaro


MOSHI nzima ilikuwa kimya kabisa, ni siku ambayo ilitawaliwa na mvua za rasharasha karibu siku nzima. Usiku wa kuamkia siku hiyo, mvua kubwa ilikesha, ilikatika alfajiri kabisa na kusababisha hali ya hewa kuwa tulivu sana.
Kwa namna udongo wa mji huo ulivyo, kila mahali kulikuwa na tope jingi kwenye barabara za mitaani. Ni kama vile mvua hiyo iliamua kuacha kunyesha ili kuwapisha waumini wa dini ya Kikristo waende kanisani.
Ilikuwa Jumapili ya Matawi, katikati ya Kipindi cha Kwaresma ikiwa ni wiki moja kabla ya Sikukuu ya Pasaka. Kuanzia saa nane mchana, mvua ikaanza tena kunyesha. Ilinyesha kwa saa moja kwa kasi ya ajabu, halafu ikakatika kisha ikafuata rasharasha.
Suma alikuwa ametulia kimya chumbani mwake. Alikuwa na mawazo mengi sana; kwanza alimfikiria baba yake na uamuzi wake wa kumtaka aoe haraka, halafu pili alikuwa akimfikiria msichana ambaye angalau anaonekana kufaa kuwa mkewe – Zakhia. Juu ya yote hayo, aliwaza zaidi namna ambavyo anakwenda kubadilisha nadhiri aliyojiwekea kwa muda mrefu sasa.
Alitamani sana kuoa jini na si binadamu. Kichwani mwake aliamini ni jini pekee ndiye ambaye angeweza kumfanya akaishi maisha ya raha mustarehe. Katika ubongo wake kulijengeka taswira ya kwamba majini ni viumbe wenye mapenzi, wasiotesa na wanaojali kuliko binadamu ambao wamekuwa wasaliti mara kwa mara kwa wenzi wao.
"Tatizo ni hilo..." akawaza.
"Lakini nitawezaje kujipinga mwenyewe?"
Alipata tabu sana ya kuwaza na kuwazua kichwani mwake. Akiwa mwenye kujiuliza maswali lukuki na kujijibu mwenyewe: "Mimi sina pesa, sasa msichana mzuri kama Zakhia, nitawezaje kumtunza na akaishi vizuri kama wanawake wengine? Jamani si nitadhalilika mimi? Au nikubali tu? Baba alisema kwamba kuoa ni jambo jema na mwanamke huja na riziki yake...
"Sasa kama aliniongopea nitajuaje? Nitawezaje kufanya majaribio katika jambo makini na linalohusu maisha yangu kama hili? Nitaweza kweli? Lazima nipate jibu la swali hili kwanza. Sitakiwi kukurupuka tu....sitakiwi kabisa...mimi ni mwanaume mwenye akili timamu na kichwa changu kinafanya kazi vizuri.
"Mwanamke anahitaji matunzo. Nitayatoa wapi? Baba ananidanganya na maneno yake ya uongo mtupu...kama mwanamke huja na riziki yake, mbona yeye amemuoa mama na wametuzaa sisi hadi tunakuwa wakubwa, bado wanaishi maisha duni? Wanaishi nyumba ya kupanga? Au mama hana riziki? Sisi watoto wao je? Uongo mtupu!" aliwaza Suma.
Kwa kiasi kikubwa alipingana na mawazo ya baba yake, alijua ni ya kumshawishi tu! Hata hivyo, kuna jambo liliingia kichwani mwake kwa kasi ya ajabu sana. Alitakiwa kuheshimu na kusikiliza mawazo ya baba yake, lakini akiendelea kufanyia kazi ndoto zake.
"Acha nikazungumze na Zakhia, muda ambao nipo naye nitaendelea kufikiria namna ya kumpata jini wangu," akawaza Suma.
Wazo hilo lilipita, tena aliamua kwenda kumfuatilia siku hiyohiyo. Tatizo likawa ni mvua. Aliendelea kusubiri sana mvua ipungue lakini haikukatika. Rasharasha ziliendelea. Hadi saa kumi mvua ilikuwa haijakatika. Alichoamua ilikuwa ni kutoka kwa kutumia mwavuli wake. Alipita njia za mkato.
Muda mfupi baadaye alikuwa anapita kwenye makutano ya barabara inayoelekea Faya na ile inayopandisha kwenda sokoni kupitia kwenye Baa ya Kipanga. Alikazana hadi alipokutana na Barabara ya Tunisia inayoelekea Mbuyuni kupitia Kiwanda cha Kahawa cha Coffee Quring na ile inayopandisha kwenda Kwa Kishamba.

Akashika ya kulia kwake. Hakuuachia mwavuli wake ambao ulimsaidia sana kuzuia mvua iliyoendelea kunyesha. Dakika tatu baadaye alikuwa ameshafika Kwa Kishamba. Kama alivyoelekezwa na Zakhia, alizunguka nyuma ya Zahanati hiyo na kwenda kusimama kwenye duka moja mbele ya nyumba hiyo.
"Habari yako ndugu yangu?" Suma akamsalimia mhudumu aliyekuwa pale dukani.
"Salama, karibu."
"Ahsante...sihitaji bidhaa yoyote dukani kwako ila naomba kuuliza."
"Uliza tu ndugu yangu."
"Kuna msichana namwulizia, alinielekeza anaishi humu ndani."
"Anaitwa?"
"Zakhia."
"Zakhia?" akamwuliza kwa mshangao kidogo.
"Vipi mbona umeshtuka ndugu yangu?"
"Ni ndugu yako?"
"Hapana ni rafiki yangu."
"Dah!"
"Vipi kwani?"
"Yule matawi ya juu sana, nimeshangaa kuona mnafahamiana tena mna ukaribu."
"Kawaida tu, yupo lakini?"
"Kwani yeye amekuelekeza lini hapa?"
"Muda kidogo, ni kama miezi minne hivi imepita."
"Ni kweli alikuwa anaishi hapa..."
"Na sasa?"
"Amehama."
"Amehamia wapi?"
"Soweto."
"Dah....sijui itakuwaje sasa?" akasema kwa sauti Suma.
"Vipi ni muhimu sana kuonana naye?"
"Sana tena sana yaani."
"Pole sana, unajua anapofanyia kazi?"
"Hapana."
"Nitakusaidia, labda hapo unaweza kumpata."
"Nitashukuru sana ndugu yangu."
"Anafanya kazi Benki ya CRDB."
"Wapi?"
"Hapa Moshi zipo ngapi? Si pale Kahawa House?"
"Ahsante sana kaka, utakuwa umenisaidia sana. Ngoja nitajaribu kwenda kumwulizia pale."
"Poa bwana."
Suma akaondoka zake.
***
Hakwenda kazini. Alitaka kumpata kwanza Zakhia. Alichojua yeye ni kwamba Zakhia anafanya kazi Benki ya CRDB tu. Si zaidi ya hapo. Mawazo tele yalikuwa kichwani mwake wakati akifikiria namna ya kumpata huyo Zakhia.
Alijua wazi kwamba benki hiyo ni kubwa na kuna idara nyingi, hivyo isingekuwa rahisi kwake kufahamu moja kwa moja yupo idara gani, jambo ambalo kwa kiasi fulani lilimkatisha tamaa.
"Lakini nikiulizia watakuwa wanamjua tu.....tatizo ni kama kuna Zakhia mwingine hapo...hata akiwepo ni rahisi kumwelezea huyu ninayejua jinsi alivyo. Watakuwa wanamfahamu tu.
"Nitajua la kufanya. Mimi si mgeni hapa mjini na sidhani kama nitashindwa kujieleza kwa kiwango hicho. Nitampata tu Zakhia," aliwaza kichwani mwake akiwa ndani ya daladala asubuhi hiyo wakati likishusha abiria katika kituo cha YMCA.
Alishukia KNCU, kisha akatembea kwa miguu taratibu jirani na Benki ya NBC, akapita katikati ya mzunguko wa mnara wa saa kisha akachepuka kidogo na kurudi kwenye Jengo la Kahawa House. Alipita getini kulipokuwa na askari wawili wenye bunduki mikononi mwao.
Akaingia moja kwa moja ndani ya Benki ya CRDB. Pamoja na kwamba ilikuwa ndiyo kwanza saa 3 asubuhi, alikuta ndani ya benki hiyo kumefurika watu wengi. Wengine wakiwa wamekwenda kuhifadhi fedha huku wakiwemo waliokwenda kuchukua.
"Customer Care..." Suma alisoma maneno hayo kwenye bango dogo juu ya meza iliyokuwa na wahudumu watatu; mmoja kati yao mwanaume.
"Huyu mwanaume hawezi kunisaidia, huenda labda naye anamtaka akanikosesha bure,"akawaza Suma huku akimsogelea mhudumu mmoja wa kike, akiwa amepamba uso wake kwa tabasamu mwanana kabisa.
"Habari yako sister?" Suma akasalimia.
"Njema kabisa kaka, karibu sana."
"Ahsante."
"Tafadhali naomba nikusaidie."
"Ahsante sana...samahani sana, nina shida muhimu nje ya kazi."
"Unaweza kunieleza tafadhali."
"Mimi naitwa Suma, ni ndugu yake na Zakhia. Najua anafanya kazi hapa, lakini sifahamu ni kitengo gani. Tafadhali dada naomba unisaidie nionane naye kama unamfahamu!"
"Zakhia?"
"Ndiyo."
"Pole sana!"

ITAENDELEA...
 
Hadithi nzuri ila sidhani kama tafsiri sahihi ya vampires ni majini. Sina hakika sana ila fuatilia, kuna uwezekano mkubwa hakuna tafsiri sanifu ya kiswahili ya "vampire" kwa kuwa hili suala halipo katika jamii za kiswahili. Kiufupi tafsiri ya watu wa Ulaya ya "vampire" haisadifu kabisa tafsiri ya kiswahili ya majini. Kwa maneno mengine vampires na majini ni vitu viwili tofauti kabisa.
 
Back
Top Bottom