Hadithi : Wakili Wa Moyo

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Apr 29, 2016
20,744
25,446
Image may contain: text

Hadithi: WAKILI WA MOYO
SEHEMU: 01
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500..
WAKILI WA MOYO
Maumivu ya moyo hayana msaidizi na moyo wa kupenda hauna subira, kilichojificha moyoni huwa sawa na mfungwa asiye na kosa lakini hajui kujitetea. Siku zote anayependa kama mhusika hajui kama anapendwa huwa mateso ya kujitakia. Cecilia msichana alinayetoka katika familia ya maskini anampenda Colin mvulana aliye katika familia ya kitajiri mwenye mchumba anayetaka kufunga naye ndoa. Anajikuta akiumia kila akimuona, pamoja na kuonekana jambo hilo kama maji kupanda mlima lakini msichana Cecy anauapia moyo wake kuwa atauwekea wakili na kuweza kushinda kesi ya maumivu ya mapenzi.
Je, atafanikiwa? Kuyajua yote ungana tena na mtunzi mahiri katika hadithi tamu ya mapenzi ili upate uhondo mwanzo mwisho.
TWENDE KAZI.....
Mama Cecy alishangaa kumuona mwanaye amerudi mapema huku sinia likiwa limejaa ndizi, alimalizia kupuliza moto wa kuni kisha alitoka jikoni huku akifuta machozi kwa upande wa khanga kutokana na moshi wa kuni kumuingia machoni. Alimtazama binti yake aliyekuwa amekaa chini huku ameshika tamaa na machozi kumtoka.
“Cecy nini tena mama?” alimuuliza huku akimsogelea.
“Mama hata nashindwa kujielewa sijui ni kwa nini inakuwa hivi?” alisema huku akiondoka mkono shavuni bila kufuta machozi.
“Una lingine au ni lilelile za siku zote?”
“Kuna lingine lipi mama yangu! Hata sijui kwa nini nimejiingiza kwenye mateso ya kumpenda Colin mtu ambaye hayajui mapenzi yangu kwake.”
“Lakini kwa nini mwanangu unapenda kuota ndoto za mchana, wewe na Colin wapi na wapi kama mbigu na ardhi.”
“Najua mama utasema hivyo lakini katika mapenzi hakuna kitu kama hivyo, nakuapia kwa Mungu Colin atakuwa mume wangu wa ndoa.”
“Cecy mwanangu hebu achana na kujishugulisha na masuala ya mapenzi, hebu jiangalie ulivyo na alivyo Colin. Kwanza mwenzako hand same.”
“Hata mimi beutiful girl,” Cecy alijibu kwa kujiamini huku akinyanyuka na kujishika mkono kiunoni kujionesha kuwa ni mrembo.
“Mwenzio ana elimu ya chuo kikuu wewe darasa la saba la kufeli, mwenzako anatoka kwenye familia ya kitajiri wewe pangu pakavu tia mchuzi. Kingine ambacho kinafanya usiweze kabisa kumpa ni kuwa Colin ana mchumba na mipango ya harusi ipo karibuni sasa huyo Colin yupi wa kukuona?”
“Mama nina uhakika kwa asilimia mia Colin kunioa,” Cecy alisema kwa kujiamini.
“Wee mtoto una wazimu? Au kuna mganga kakudanganya, maana siku hizi ushirikina hauna mtoto wala mzee.”
“Mama katu mapenzi sitayaendelea kwa mganga, ila nitayapigania kwa nguvu zote.”
“Kipi hasa kinakupa jeuri ya kusema hivyo?”
“Ipo siku nitakwambia lakini amini ndoa ya Colin na Mage haipo ila mimi ndiye mke wake.”
“He he he heee, usinichekeshe miye, kwa nini unasema hivyo?” mama Cecy alicheka mpaka machozi yakamtoka.
“Mage hampenzi Colin.”
“We umejuaje?”
“Ni historia ndefu mama.”
Cecy alianza kumhadithia mama yake sababu ya kuamini siku moja Colin atakuwa mpenzi japokuwa hajawahi kumtamkia kitu kama hicho hata siku moja.
Alianza toka siku ya kwanza kumuona Colin, Mage msichana aliyetoka katika familia ya kimaskini elimu yake ya darasa la saba shuleni alikuwa mmoja wa wasichana waburuza mkia.
Baada ya kufeli kwenye mtihani wa mwisho aliamua kufanya biashara ya ndizi kwa kupita mtaani kuuza. Japokuwa alikuwa maskini lakini alijipenda sana.
Baada ya kuuza ndizi siku za mwanzo alinunua nguo nzuri ambazo alizivaa kila alipozunguka mkaani kuuza ndizi zake.
Kitu kilichopelekea apendwe na wateja wengi kutokana na umaridadi wake na heshima kwa wote akiwemo mama Colin ambaye alikuwa mnunuzi wake mkubwa.
Nyumba ya mama Colin ilikuwa ndiyo iliyokuwa ikinunua ndizi nyingi kitu kilichomfanya Cecy aongeze mtaji. Mama Colin alitokea kumpenda sana na kumwita mkwe.
Siku moja alipitisha ndizi kama kawaida bila kujua kama nyumba ile ina kijana mzuri aliyekuwa nje amerudi baada ya kumaliza masomo yake. Baada ya kufika nje ya geti alibonyeza kengele na mlinzi alimfungulia mlango na kuingia ndani.
“Mwambie mama mkwe leo nimeleta ndizi za ukweli,” alimwambia mlinzi aliyekuwa amemzoea sana.
“Mamkweee,” Cecy alipaza sauti kama kawaida yake kila alipofika.
Mara alitoka mama Colin akiwa katika muonekano wa mtoko.
“Ha! Ma mkwe safari ya wapi tena?”
“Nampeleka mchumba wako mjini.”
“Muongo, yupo wapi?”
“Yupo ndani anakuja.”
“Amekuja lini?”
Siku zote Cecy alipokuwa akipeleka ndizi alitaniwa na mama Colin kwa kuitwa mkwe japokuwa hakuwahi kumuona huyo mwanaume. Kila siku alikuwa na hamu ya kumuona japokuwa alikuwa akitaniwa.
“Jana usiku na ndege.”
“Waawooo,” Cecy aliruka juu kama anamfahamu.
Ghafla alinyamaza baada ya kumuona mvulana mzuri tena mtanashati akitoka ndani. Alibakia kama kapigwa shoti ya umeme kwa jinsi alivyosimama kwa mshangao kidole mdomoni.
“Colin umemuona mchumba wako niliyekuandalia?” mama Colin alitania.
“Nimemuona mzuri tena mrembo,” Colin alisema huku akimtazama Cecy aliyekuwa bado amesimama.
“Cecy umemuona Colin?”
“Ndi..ndi..yo,” Cecy alipatwa na aibu na kushindwa kuzungumza.
“Sasa mkwe, msichana wa kazi atachukua ndizi sisi tuna safari ya mjini.”
“Sawa mkwe.”
Mama Colin alifungua pochi na kutoa noti ya elfu tano na kumpatia Cecy, wakati huo Colin alikuwa akilisimamisha gari pembeni ya mama yake. Mama Colin alifungua mlango wa gari wa nyuma na kuingia.
“Bai mchumba,” Colin alimuaga Cecy aliyekuwa ameingiwa aibu.
“Bai,” Cecy alisema huku akiangalia pembeni kwa aibu.
Geti lilifunguliwa na gari lilitoka nje kuelekea mjini na kumuacha Cecy akitoa ndizi kwa msichana wa kazi kisha alitoka na kuendelea kufanya biashara kama kawaida.
****
Safari ya mama Colin na mwanaye ilikuwa kwenda nyumbani kwao Mage msichana aliyemchagua kuwa mke wa mwanaye. Alimuona siku moja alipokuwa na mama yake walipokutana na shoga yake Super Market, wakati akiwa katika manunuzi ya bidhaa muhimu.
“Ha! Shoga za siku?” Mama Colin alimsemesha mama Mage.
“Nzuri shoga, za kupotezana?”
“Mmh! Nzuri, vipi Colin bado hajarudi?”
“Anarudi mwezi kesho mwishoni.”
“Shikamoo,” Mage alimwamkia mama Colin.
“Marahaba, hujambo mama?”
“Sijambo.”
“Monika, binti yako?” mama Colin alimuuliza shoga yake.
“Ndiyo amemaliza chuo kikuu Mlimani anasubiri ajira.”
“Nimempenda sana, unafaa kuwa mke wa Colin.”
“Tena wataendana wasomi kwa wasomi,” mama Mage aliunga mkono.
“Anaitwa nani?”
“Mage,” Mage alijibu mwenyewe.
Tokea siku ile wakawa wakiwasiliana hata kutembelea huku wakisubiri muda wa Colin kurudi toka masomoni ili wapange mipango ya ndoa. Mama Colin alimpenda sana Mage kwa umbile lake nzuri na heshima aliyoionesha siku zote kwake. Naye mama Mage alifurahi mwanaye kuolewa na Colin kutokana na kumfahamu vizuri.
Siku Colin aliyofika hakutaka kuwajulisha, kesho yake alimpeleka nyumbani kwao Mage bila taarifa ili wafanye surprise. Familia ya kina Mage ilikuwa ikikaa Kigamboni walikwenda hadi kwao na kupiga honi nje ya geti. Wakati wote huo Colin alikuwa hajui anakwenda wapi.
Baada ya geti kufunguliwa Colin aliliingiza gari ndani na kwenda kulipaki kwenye maegesho. Mama Mage alitoka nje baada ya kusikia gari likingia ndani na kujiuliza nani amekwenda kwake bila taarifa. Alishtuka kumuona mama Colin akiteremka kwenye gari.
“Waawooo jamani, ha! Colin siamini jamani karibu mwanangu,” alikuwa akimfuata mama Colin kumkumbatia lakini aligeuza baada ya kumuona Colin na kwenda kumkumbatia.
Colin alijikuta akishangaa baada ya kuteremka kwenye gari na kujiuliza pale ni wapi na yule aliye mfurahia na kumkumatia ni nani.
“Asante, shikamoo.”
“ Marahaba karibu sana mwanangu,” mama Mage alisema kwa furaha huku amemshika mabegani Colin na kumtazama.
Aliwapokea wageni na kuingia nao ndani kwenye sebuleni, baada ya kukaa alimwita Mage kwa sauti kubwa.
“Mageee.”
“Abee mama,” sauti ya Mage ilitoka chumbani.
“ Njoo mara moja.”
“Nakuja.”
Mage alikuja mbio bila kujua anaitiwa nini, alipofika alishtuka kumuona mama Colin.
“Ha! Mama mkwe.”
“Nimejaa tele,” mama Colin alijibu kwa tabasamu pana.
“Shikamoo.”
“Marahaba.”
“Mambo?” Mage alimsabahi Colin bila kumjua.
“Poa za hapa?”
“Nzuri,” Mage alijibu huku akishtuka na kujiuliza yule kama ndiye Colin, ili kupata uhakika aliomba msamaha na kutoka mara moja.
“Jamani samahanini nakuja mara moja.”
“Bila samahani,” alijibu mama Colin.
Alichepua mwendo na kwenda upande wa vyumba huku akimwambia mama yake.
“Mama njoo mara moja.”
“Jamani samahanini nakuja mara moja.”
“Hakuna tatizo,” mama Colin alijibu.
Baada ya mama Mage kuondoka kumufuata mwanaye, mama Colin alimsemesha mwanaye kwa sauti ya chini.
“Mchumba unamuonaje?”
“Yupo vizuri.”
“Umempenda?”
“Sana.”
“Nimefurahi kuona chaguo langu amelikubali.”
“Mama wee kiboko unajua kuchagua.”
Mama Mage baada ya kufika kwa mwanaye aliyekuwa amesimama upande wa vyumba.
“Vipi?” alimuuliza mwanaye.
“Safi, eti mama yule si Colin?”
“Ndiyo.”
“Mamaaa! Kwa nini hukuniambia mapema nijiandae anaweza kuniona sijipendi.”
“Walaa mbona umependeza, vipi umempenda?”
“Ndiyo,” Mage alikubali huku akinyanyua kichwa.
“Basi turudi.”
“Naona aibu ngoja nikaoge na kubadili nguo.”
Mama Mage aliwarudia wageni wake ili kuwapatia kinywaji kabla ya kuanza mazungumzo.

Itaendelea Jumatatu
 
HADITHI: WAKILI WA MOYO
SEHEMU: 02
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500..
ILIPOISHIA:
“Walaa mbona umependeza, vipi umempenda?”
“Ndiyo,” Mage alikubali huku akinyanyua kichwa.
“Basi turudi.”
“Naona aibu ngoja nikaoge na kubadili nguo.”
Mama Mage aliwarudia wageni wake ili kuwapatia kinywaji kabla ya kuanza mazungumzo.
SASA ENDELEA...
***
Mage msichana mwenye elimu ya chuo aliyekuwa na shahada ya Uhusiano, baada ya kuachana na mama yake alikwenda chumbani kwake ili kujiandaa kuonana na wageni. Kwanza alikwenda kuoga kisha alibadili nguo ambayo aliamini ni sahihi kwa ajili ya kumpokea mgeni wake.
Alijipulizia manukato ya bei mbaya aliyonunuliwa na baba yake alipokwenda Ufaransa kikazi. Alisimama mbele ya kioo kikubwa cha ndani na kujitazama kisha kujigeuza kila pembe. Baada ya kuridhika na gauni alilovaa alikisogelea kioo na kujitazama jinsi Mungu alivyomuumba kwa uzani unaolingana, alijikuta akitokwa machozi ( siri ya machozi yake soma katika muendelezo wa hadithi hii.)
Aligundua kuna mapungufu kichwani mwake, alikwenda mpaka kwenye dresing table na kukaa kwenye kiti kidogo kisha alivuta droo na kutoa wanja. Alipaka wanja mwembamba ulioongeza uzuri wa sura yake.
Alichukua heleni ndogo na kuvaa kisha alichukua cheni yake ndogo ya dhahabu na kuivaa, kidani chenye jila lake kilikaa kwenye mfereji ya matiti yaliyojaa na kumfanya apendeze zaidi.
Mage aliamini mpaka pale alikuwa amekamilika kwenda mbele ya wageni wake ambao walikuja mahususi kwa ajili yake. Alikwenda kwenye kabati na kutoa kiatu cha kisigino kifupi cha rangi ya machungwa kilichoendana na linda la chini la gauni lake alilovaa lenye mchanganyiko wa rangi nyeusi na weupe kwa mbali.
Hakika Mage alikuwa amependeza kama malkia aliyekuwa tayari kuonana na mfalme. Alitembea kwa madaha toka chumbani kwake kuelekea sebuleni palipokuwa na wageni.
Harufu ya manukato yake yalitangulia kabla yake. Colin na mama yake waligeuza macho kuangalia upande wa chumba na kukutana na Mage aliyetokeza akiwa amependeza mara dufu na awali alivyokuwa.
Moyo wa Colin alipasuka vipande na kuwa hoi taabani kwa uzuri wa Mage msichana chaguo la mama yake. Alijikuta akijiuliza hali ile mama yake ni mwanamke amejua kuchagua binti mrembo kama yule, je, angekuwa mwanaume angekuwa na uwezo gani wa kuchangua wanawake warembo.
Mama Colin alitulia kama mtu aliyepigwa na shoti ya umeme hata kukapua macho alishindwa kutokana na uzuri wa Mage mkwewe mtalajiwa.
“Wageni karibu sana huyu mnayemuona ndiye Magreth halisi.”
“Asante, tunashukuru kukutambua,” Colin alijitahidi kuitikia japo mwili ulipoteza ujasiri wa kiume baada ya kuingiwa baridi la mshtuko.
“Mama zangu samahanini namuomba mgeni wangu,” Mage alisema huku akisogea kwa Colin na kumshika mkono.
Colin alinyanyuka na kukiacha kinywaji chake juu ya meza ndogo, lakini Mage alikichukua na kukishika mkono wa kushoto huku wa kulia akimshika mkono Colin na kuondoka naye kuelekea nyuma ya nyumba kwenye bustani.
Walivyokuwa wakitembea wazazi wao waliwasindikiza kwa macho mpaka walivyopotea kwenye macho yao. Waligeuka na kutazamana kisha walitabasamu.
“Yaani walivyopendeza nilitamani leo ndiyo iwe siku ya sendoff ya mwanangu,” mama Mage alisema kwa hisia kali.
“Kila kitu kina wakati wake, kilichonifurahisha mimi jinsi walivyoonekana kupenda. Wasiwasi wangu huenda Mage asingempenda Colin.”
“Isingekuwa rahisi, Colin ni mmoja wa vijana wazuri ambao Mungu kawajalia. Nitajivunia kuwa na mkwe kama yeye, nitatembea kifua mbele.”
Upande wa pili Mage alimpeleka Colin mpaka kwenye bustani.
“Karibu kwenye kiti mgeni wangu,” Mage alimkaribisha kwenye kiti cha uvivu na meza ndogo katikati ya kuwekea vinywaji. Mage kabla ya kukaa alikumbuka amesahau kinywaji chake.
“Sorry Colin nakuja nimesahau kinywaji changu,” Mage alisema huku akigeuka ili arudi ndani.
“Mage,” Colin alimwita Mage aliyeanza kwenda ndani.
“Abee,” Mage alitikia huku akigeuka kumsikiliza Colin.
“Kinywaji hiki kinatutosha.”
“Mbona kidogo hakitutoshi.”
“Kinatutosha, kwangu wewe ni zaidi ya kinywaji.”
“Colin nimefurahi kufahamu hilo.”
Mage alirudi na kukaa pembeni ya Colin, baada ya kukaa Colin alibeba glasi iliyokuwa na kinywaji na kumnywesha Mage ambaye alisogeza mdomo kuipokea.
Baada ya kumeza funda ya juisi alimumunya midomo yake mipana na kusema:
“Colin, leo ni siku yetu ya kwanza kuonana lakini umenifanya nikuone mwenyeji katika moyo wangu. Nasikia fahari kuwa mkeo,” Mage huku akimtazama kwa macho yake makubwa kidogo yaliongezwa uzuri na wanja aliojipaka.
“Nashukuru kwa hilo,” Colin alijibu huku akiachia tabasamu pana.
“Lakini nina wasiwasi mmoja ambao umekuwa ikisumbua mawazo yangu na kuukosesha amani moyo wangu,” Mage alisema huku uso wake ukionesha uzuni.
“Wasiwasi wa nini Mage?”
Colin aliuliza huku akijiweka vizuri kitini na kuiweka glasi ya juisi juu meza kisha alipeleka mkono kwenye nywele fupi za kipilipili na kuzichezea kitu kilichofanya Mage mwili umsisimke.
“Najua ndiyo siku yako ya kwanza kuniona, siamini kama Colin unanipenda kama ninavyokupenda?”
“Mage toka nilipoelezwa nimepatiwa mchumba moyo wangu ulikuwa taabuni kutaka kukuona. Nilikuumba akilini kwa kila umbile na kukupamba kwa rangi nyingi.
“Amini Mage kila nilichokiwaza moyoni mwangu kilikuwa uongo. Nilichokiona ni zaidi ya vyote nilivyoviwaza,” Colin alisema huku amemshika mabegani Mage na kumtazama usoni kwa jicho la huruma.
“Vitu gani hivyo Colin?” Mage aliuliza huku akijitahidi kuyatoa macho nje kama anaweza kuyaona maneno kwa macho.
“Kila umbile na sura niliyoiwaza ambayo niliamini huenda moja wapo litakuwa yako imekuwa kinyume kabisa.”
“Mmh! Colin, kwa nini?”
“ Mage we ni mzuri wa wazuri mrembo wa warembo. Najiona kiumbe mwenye bahati kama nitakuwa mume wako,” Colin alisema akiwa ameyakaza macho kuonesha anachokizungumza hatanii.
“Siamini, Colin siamini,” Mage alisema mikono ameshika kifuani huku machozi yalinitoka.
“Mage huamini nini?”
“Inawezekana Colin unalitamani umbile langu lakini si mapenzi ya dhati toka moyoni mwako,” Mage alisema huku machozi yakimtoka na kuweka michirizi kwenye mashavu.
“Mage amini nakupenda kama ugonjwa wa shinikizo la damu linavyochukuwa uhai wa mtu ghafla.”
“Colin sijui wewe ni mwanaume wa aina gani,” Mage alijisema huku akijitahidi kutengeneza tabasamu ndani ya machozi.
“Kwa nini mpenzi?”
“Maneno yako yamekuwa na sumaku yenye nguvu ya ajabu kuweza kunasa chuma kilichomo moyoni mwangu.”
“Sijakuelewa mpenzi.”
“Ameweza kuuteka moyo wangu na kukubali kuwa mateka wako. Colin nakuamini, usiniache katikati ya bahari nitakufa maji boya langu ni wewe. Maumivu ya mapenzi ni zaidi ya kung’olewa jino bila ganzi.”
“Amini Mage nakuahidi kuwa mume mwema.”
“Nami nakuahidi kuwa mke mwema.”
Baada ya hapo mazungumzo yaliendelea kila mmoja kuitaka kumjua mwenzake kiundani mpaka muda ulipofika wa kuondoka.
Colin akiwa mtu mwenye furaha na mama yake waliondoka na kuwaacha Mage na mama yake nje baada ya kuwasindikiza wageni. Walirudi ndani mtu na mama yake wakishikana mikono.
Walipoingia ndani Mage alimuuza swali mama yake.
“Mama, kweli Colin atanioa?” alimuuliza huku akimkazia macho.
“Mbona umeniuliza hivyo, kwani mmezungumza nini?”
“Amenihakikishia atanioa.”
“Sasa wasiwasi wako nini?”
“Mama anaweza kuwa na mwanamke mwingine na kuniacha njia panda kama alivyofanya Hans. Najiona nimefanya haraka sana kumkubali Colin bila kujua historia yake. Safari hii sitakubali kuumizwa mara mbili lazima nitanyongwa tu,” Mage alisema kwa hisia kali.
“Kwa hiyo ukigundua Colin ana mwanamke mwingine utamuua?”
“Siwezi kumuua Colin bali mwanamke wake.”
“Lakini Hans alikuwa akikupenda tatizo wazazi wake ndiyo waliomchagulia mwanamke mwingine.”
“Mama, Hans hakuwa ananipenda ni muongo mkubwa.”
“Kwa nini?”
“Alisema anamuoa yule mwanamke hatakaanaye atamuacha, mwezi jana nilimekutana na yule mwanamke akiwa mjamzito.”
“Ndiyo basi tena, nawe umepata wako tena kijana mzuri msomi mwenzako.”
“Mama bado inaniuma sana, niliutoa mwili wangu kwa Hans kwa kujua ndiye atakaye kuwa mume wangu. Mama sijui mwanaume yeyote zaidi ya Hans, nilijitunza kwa ajili yake matokeo yake alinidanganya ataachana na yule mwanamke aliyelazimishwa kuoa.
“Nilimuamini lakini mwezi ulioisha nilijikuta nikimchukia Hans baada ya kumuona yule mwanamke mjamzito. Imeniuma sana mama nakuahidi sitamsamehe Hans na sitakubali kuchezewa tena na Colin nitakufa mimi au yeye,” Mage alibadili uzuri wake wote ulipotea alikuwa kama akipigana na mtu.
“Mage mwanangu, ya Hans tuliyazungumza tukayamaliza.”
“Mama hujui kiasi gani nilivyoumizwa na Hans kuoa, lakini alinituliza na kusema kuwa ataachana na mpenzi wake ili anioe. Lakini nilichokiona niliwaza mbali sana mama.
“Leo nakupa siri niliyoificha moyoni, siku niliyokutana na mke wa Hans mjamzito, nilinunua vidonge na pombe kali ambavyo nilipanga kunywa usiku ili asubuhi ukiamka ukute mzoga.
“Usiku ulipoingia niliandaa vitu vyote kwa ajili ya kuutoa uhai wangu, kabla ya kufanya tendo lile nilikumbuka kauli ya profesa mmoja wakati tupo chuoni, kuwa thamani yangu haipo kwa mtu mmoja bali ya ulimwengu mzima kwa hiyo nisipoteze uhai wangu kwa kosa la makusudi bali niitazame thamani yangu mbele ya jamii.
“Mama nililia sana na kuchukua vitu vyote na kwenda kuvitupa. Huwezi kuamini nimchukia Hans kama kifo. Ujio wa Colin umenishtua na kuona kama maumivu mengine yanakuja.”
“Mage mwanangu naiamini familia ya kina Colin, uzuri mama yake kakuchagua.”
“Mamaa! Ngoja tuone.”
Mage alisema huku akielekea chumbani kwake.
***
Cecy baada ya kufanya biashara yake ambayo iliisha mapema na kurudi nyumbani akiwa mwenye furaha. Mama yake alijua furaha ile ni kwa ajili kumaliza bishara mapema kumbe sivyo. Usiku ulipoingia aliwahi kula, baada ya kuoga alipanda kitandani mapema.
Kitendo kile kilimshtua mama yake na kuamini mwanaye labda anaumwa. Mama Cecy baada ya kumaliza kazi zake alimfuata mwanaye chumbani aliyekuwa amejilaza chali mikono ameilalia kwa nyuma.
Mpaka anaingia chumbani Cecy alikuwa ametulia macho kayaelekeza juu. Mama yake alitulia akimuangalia na kumuona mwanaye yupo katika lindi la mawazo jambo ambalo halikuwa kawaida kuliona kwa mwanaye.
Baada ya muda alimuona akitabasamu na kujikuta akitazama juu labda kuna kitu mwanaye anakitazama na kumfurahisha, lakini hakuona kitu. Alijiuliza kipi kilichomfanya mwanaye awahi kitandani kisha kutulia akitazama juu na kutabasamu.
Baada ya kutabasamu alimuona alishika mikono kifuani na kusema kwa sauti ya chini ambayo mama yake aliisikia.
“Cecy mimi,mmh! Sijui?”
Baada ya kusema vile aligeukia ukutani na kumpa mgongo mama yake aliyekuwa amesimama mlangoni bila kumuona.
“Cecy..Cecy,” mama yake alimwita.
“A..a..bee,” Cecy aliitikia huku akigeuka kumtazama mama yake na kumshangaa kumuona amesimama mlangoni.
“Vipi mama?” alimuuliza bila kunyanyuka zaidi ya kujigeuza.
“Unajua leo sikuelewi kabisa.”
“Kivipi?” Cecy alijibu huku akikaa kitako.
“Umewahi kupanda kitandani si kawaida yako, nimefika muda nimekuona akitazama juu na kutabasamu peke yako. Kisha unazungumza peke yako una nini leo mwanangu?”
“Mama nipo kawaida, siku azilingani.”
“Kipi kilichokupa furaha leo.”
“Mama nawaza kama siku moja nitaolewa na mwanaume mzuuuri mwenye uwezo tena mwenye mapenzi ya dhati nitafurahi sana.”
“Utapata tu mwanangu, Mungu nawezi kutunyima vyote.”
“Asante mama yangu kunipa moyo.”
“Lakini huna tatizo lolote?”
“Sina mama yangu.”
“Haya mwanangu usiku mwema.”
“Na wewe pia mama yangu.”
Mama Cecy aliondoka na kurudi chumbani kwake kulala na kumuacha mwanaye akirudi kujilaza kama mwanzo macho yake yakiangalia juu.
Alijikuta akikumbuka kauli ya mama Colin baada ya kutoka ndani, mwanaume mzuri ambaye alikuwa na kila sababu ya kujivunia kama akiwa mumewe au mpenzi wake.
Alikumbuka jinsi alivyoshtuka baada ya kumuona Colin. Kauli ya mama Colin ilijirudia kichwani mwake.
“Colin umemuona mchumba wako niliyekuandalia?”
“Nimemuona mzuri.”
“Cecy umemuona Colin?”
“Ndi..ndi..yo,” Cecy alikumbuka alipipata kigugumizi na kuugua ugonjwa wa mapenzi ghafla.
“Sasa mkwe, msichana wa kazi atachukua ndizi sisi tuna safari ya mjini.”
“Sawa mkwe.”
Cecy alijiuliza kauli ile ya mama Colin ilikuwa na ukweli gani kutokana na kuona kuolewa na Colin sawa na ngamia kupita kwenye tundu la sindano.
“Mbona sielewi, kweli Colin atanioa au ananitania, mbona hakukataa mbele ya mama yake, na kwa nini mama yake aendelee kuniita mkwe?”
Cecy alijiuliza bila kupata jibu la moja kwa moja. Lakini wasiwasi wake ikawa kwenye hali zao yeye muuza ndizi anazurura mitaani na mwenzake mtoto wa kitajiri.
“Watakuwa wananitania,” alisema kwa sauti ya kakata tamaa na kugeukia ukutani kuutafuta usingizi.
ITAENDELEA
 
HADITHI: WAKILI WA MOYO
SEHEMU: 03
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500..
ILIPOISHIA:
Cecy alijiuliza kauli ile ya mama Colin ilikuwa na ukweli gani kutokana na kuona kuolewa na Colin sawa na ngamia kupita kwenye tundu la sindano.
“Mbona sielewi, kweli Colin atanioa au ananitania, mbona hakukataa mbele ya mama yake, na kwa nini mama yake aendelee kuniita mkwe?”
Cecy alijiuliza bila kupata jibu la moja kwa moja. Lakini wasiwasi wake ikawa kwenye hali zao yeye muuza ndizi anazurura mitaani na mwenzake mtoto wa kitajiri.
“Watakuwa wananitania,” alisema kwa sauti ya kakata tamaa na kugeukia ukutani kuutafuta usingizi.
SASA ENDELEA...

Usiku ulikuwa mrefu kwake baada ya kushtuka katikati ya usiku kutokana na ndoto aliyoota akiwa na Colin ndani ya gari yeye akiwa anafundishwa na baada ya hapo walikwenda ufukweni kupumzika. Wakiwa wamejilaza ufukweni Cecy alitembeza mikono yake kwenye kifua cha Colin kilichojaa kimazoezi na vinyweleo vingi ‘garden love.’ Upepo mwanana wa bahari uliwapepea.
Aliposhtuka alijikuta yupo kitandani peke yake, mapigo ya moyo yalimwenda mbio na kijacho chembamba kilimtoka. Alikaa kitandani na kujiuliza ndoto ile ina maana gani.
Aliwasha taa na kukaa kitandani mkono shavuni akijitahidi kujua ndoto ile ilikuwa na maana gani. Mama yake aliyeshtuka usingizi alishtuka kuona taa inawaka, alijiuliza usiku ule Cecy alikuwa akifanya nini.
Alinyanyuka taratibu na kwenda chumbani kwa mwanaye. Kwa vile chumbani hakikuwa na mlango zaidi ya pazia la kitenge kichakavu. Alipofika alifunua taratibu na kuangalia ndani.
Alimkuta mwanaye amekaa kitandani mkono shavuni. Alitulia kwa muda bila kumsemesha na kutaka kujua mwisho wake nini. Baada ya muda kidogo Cecy alizima taa na kujilaza kitandani.
Mama yake aliendelea kusimama mlangoni kwa muda huku akiwa na maswahi na hali ya mwanaye toka jana yake. Aliamua kurudi chumbani kwake na kupanga kumuuliza siku ya pili kwa kumbana sana ili ajue sababu ya mwanaye kuwa katika hali ile ambayo kwake ilikuwa ngeni.
***
Colin akiwa chumbani kwake amejilaza kitandani aliukumbuka uzuri wa Mage msichana aliyeonekana mwelewa lakini mwenye jeraha la mapenzi. Sifa zake za elimu ya juu pia urembo na ucheshi ni vitu vilivyomteka kimwili na kiamili.
Moyoni alijiapiza kumpenda Mage kwa moyo wake wote, aliiona familia bora mbele yake yeye akiwa baba, Mage mama na watoto wao wawili wa kike na kiume.
Siku zote alipanga kuzaa watoto wachache ambao angewamudu kuwahudumia kimalazi na elimu. Hakupenda kuwa na familia kubwa japokuwa wao walizaliwa sita, lakini yeye alitaka watoto wawili wakizidi basi wanne.
Alitaka ndoa yake ifanyike haraka ili kujipanga kwa maisha mapya. Wazo lake la kuanzisha kampuni aliliona litakwenda zuri kama Mage mwanamke mwenye Shahada ya uhusiano akiwa mkewe ambaye ingesaidia kampuni yao kukua na kutanuka.
Moyoni alimshukuru mama yake kuwa na jicho la tatu kumtafutia mwanamke ambaye hakuwa tofauti na samaki anayekaa kwenye maji marefu bila kuwa na chombo madhubuti huwezi kumpata.
Alijikuta akiyakumbuka maneno mawili ya Mage ambayo yaliuumiza moyo wake na kuamini ana deni kubwa kwa msichana yule:
“Inawezekana Colin unalitamani umbile langu lakini si mapenzi ya dhati toka moyoni mwako,” Mage alisema huku machozi yakimtoka na kuweka michirizi kwenye mashavu.
Baada ya kumuhakikishia anampenda mapenzi ya dhati alimpa mtihani ambao Colin aliamini anauweza kwa vile hakuwa mwanaume kigeugeu.
“ Colin umeweza kuuteka moyo wangu na kukubali kuwa mateka wako. Colin nakuamini, usiniache katikati ya bahari nitakufa maji boya langu ni wewe. Maumivu ya mapenzi ni zaidi ya kung’olewa jino bila ganzi.”
Baada ya kuyakumbuka maneno ya Mage, Colin alijiapiza kuwa tiba ya maumivu aliyoyapata siku za nyuma. Aliamini maumivu yale yalikuwa na sababu ya kuwakutanisha ili wajenge familia bora. Usingizi mororo ulimpitia Colin huku akitabasamu.
***
Asubuhi Cecy aliamka kama kawaida na kwenda kwenye gulio kununua ndizi za kuuza. Mama yake aliposhtuka alikuta ameishatoka muda. Baada ya kupata alirudi nyumbani na kuzipanga kwenye beseni kisha alikwenda kuoga na kutafuta nguo nzuri ambayo aliiteua kwa ajili ya kanisani tu.
Hakutoka kama siku nyingine anazokwenda kwenye biashara, alitumia muda mwingi kujipamba zaidi ya siku ya jumapili akienda kanisani. Baada ya kuhakikisha amependeza sana alitoka kwa ajili ya kwenda kuuza ndizi. Mama yake alishtuka kumuona mwanaye kwenye hali ile aliingiwa wasiwasi labda mwanaye ana safari nyingine si kwenda kufanya biashara.
“Cecy safari ya wapi?”
“Kwenye biashara mama.”
“Kwenye biashara! Ndiyo uvae vizuri hivi?”
“Basi tu leo nimeamua.”
“Si kweli toka jana sikuelewi kabisa, sasa nimeanza kupata mwanga.”
“Mwanga gani mama?” Cecy alishtuka.
“Si bure lazima utakuwa umepata mwanaume, Cecy angalia mwanangu, we bado mdogo usijishughulishe na wanaume mwisho wake mbaya.”
“Mamaaa!” Cecy alimshangaa mama yake.
“Unashangaa nini, ndiyo maana eti unatamani kuolewa kumbe una mwanaume,” mama Cecy alizungumza ameshika pua.
“Maama...mama kwa nini unanihukumu bila kosa?” Cecy alimlalamikia mama yake.
“Huna kosa, haya endelea ukiniletea tumbo hapa utatafuta mbereko ya kunibebea.”
“Mama yangu sijawaza kufanya hivyo, japokuwa nami napenda siku moja niolewe na mwanaume mwenye mapenzi ya dhati si kuanza mapenzi kihuni.”
“Haya kipi kilichokufanya nguo ya kanisani kwenda kuuzia ndizi na kujipamba kupita kiasi?”
“Mama nikueleze mara ngapi siku hazilingani.”
“Mmh! Haya biashara njema.”
“Asante mama.”
Cecy alibeba ndizi zake na kuelekea kwenye bishara zake, hakutaka kupita popote mpaka kwa mama Colin ndipo alipopanga kuanzia biashara yake kwa siku ile. Alipofika kama kawaida alibofya kengele na mlinzi alimfungulia.
“Ha! Cecy mbona umependeza hivyo?” mlinzi alimshangaa Cecy.
“Mbona kawaida yangu,” Cecy alisema huku akiingia ndani ya geti, aliweka ndizi chini na kumwita mama Colin kwa sauti ya juu.
“Mamkweee nimeisha fika.”
Colin ndiye aliyetoka kufuata ndizi kutokana na wasichana wa kazi kuwa na majukumu mengine. Macho yake yalishtuka kumuona Cecy.
“Ha! Mchumba ni wewe?”
“Ndiyo mpe...,” Cecy hakumalizia aliingia kigugumizi.
“Karibu sana.”
“Asante.”
Colin alinunua ndizi na kumlipa fedha yake.
“Mama mkwe yupo wapi?”
“Anatoka sasa hivi.”
Mara alitoka mama Colin, Cecy baada ya kumuona alimsalimia kwa kuchuchumaa chini kuonesha heshima.
“Shikamoo mkwe.”
“Marahaba mkwe wangu hujambo?”
“Sijambo.”
“Nyumbani?”
“Wanakusalimia.”
“Mkwe una safari nyingine?” mama Colin aliuliza Cecy.
“Kwa nini mama mkwe?”
“Umependeza sana.”
“Hapana nipo kwenye biashara, mwanamke kujipenda bwana,” Cecy alisema kwa pozi.
“Hongera, nina wasiwasi mwanangu anaweza kuibiwa.”
“Walaa,Colin mpenzi nipo kwa ajili yako na wewe ndiye itakuwa mwanaume wangu wa kwanza.”
“Muongo! Usimdanganye mwanangu,” mama Colin alisema.
“Kweli mamkwe.”
“Mchumba umenifuhisha sana, kesho ukija nitakupa zawadi,”Colin alisema.
“Zawadi gani?”
“Utaiona hiyo kesho.”
“Mmh! Asante.”
“Unakubali tu, hujui zawadi gani?” mama Colin alitania.
“Yoyote atakayonipa, zawadi haipangwi.”
Baada ya manunuzi Cecy aliondoka kuendelea na biashara zake. Colin na mama yake walirudi ndani, baada ya kuweka ndizi jikoni alirudi sebuleni alipokuwa amekaa mama yake.
Alipofika alikaa pembeni ya mama yake aliyekuwa yupo bize na simu. Baada ya kuachana na simu Colin alimuuliza mama yake.
“Mama unajua Cecy ni mzuri?”
“Ni kweli mwanangu, Cecy ni binti yule mzuri sana,” mama yake alimuunga mkono.
“Tena anajipenda, ana tofauti na wasichana wengi wanaofanya biashara kama yake. Hali hii anauza ndizi yupo vile akifanya kazi za ofisini itakuwaje?” Colin alisema huku akitazama mama yake aliyejenga tabasamu kutokana na maneno ya mwanaye.
“Ni kweli, ndicho kitu kilichonifanya nipende kununua biashara yake. Toka nimfahamu sijawahi kumuona mchafu.”
“Sasa kipi kilicho kufanya umwite mkwe?” Colin alimuuliza mama yake akiwa amemkazia macho.
“Nilitokea kumpenda sana binti yule na kutamani awe mkwe wangu lakini alikosa sifa muhimu.”
“Zipi mama?”
“Kwanza elimu yake darasa la saba tena la kuferi, pia anatoka katika familia ya kimaskini.”
“Tabia yake?”
“Kwa kweli binti yule ana tabia nzuri sana, ila tatizo ni hilo. Kama angekuwa na sifa angalau ya elimu ya kidato cha sita au chuo kama Mage basi yeye ndiye alikuwa chaguo langu la kwanza.”
“Kweli mama Cecy ni mzuri, lazima nikusifie unajua kuchagua wasichana wazuri.”
“Nataka mwanangu mwanamke utakaye muoa basi moyo utabasamu kila ukimuona.”
“Nashukuru kwa hilo mzazi wangu.”
***
Kama kawaida Cecy baada ya biashara zake, usiku aliwahi kuoga na kula kisha kuwahi kitandani. Alitaka kupata muda wa kuyatafari yote aliyokutanana nayo mchana. Mama yake hakutaka kupoteza wakati alimfuata na kumwita ili ajibiwe maswali yanayomsumbua mwanaye.
“Cecy.”
“Abee mama.”
“Tabia gani uliyoanzisha akimaliza kula inawahi kitandani?”
“Mama kazi ya kuzurura na ndizi inachosha.”
“Umeanza leo?”
“Mama siku azilingani.”
“Hebu njoo.”
Cecy kwa mara ya kwanza alimuona mama yake anamsumbua kwa kumnyanyua kitandani wakati yeye alitaka kuzama kwenye dunia nyingine ya kufikilika yenye raha zisizo na kikomo.
Alitoka ndani akiwa amekunja uso kitu alichokigundua mama yake na kumuonya:
“ Tabia ya kukasirika nikikuita imeanza lini?”
“Mama nimechoka.”
“Hata ukichoka hujawahi kunikunjia uso, hebu njoo hapa.”
Cecy alikaa kwenye kigoda pembeni ya mama yake huku ajitahidi kuficha hasira alizokuwa nazo.
“Umepata mwanaume?” mama yake alimuuliza kwa sauti kavu.
“Hapana mama.”
“Cecy, mi mtu mzima nimeona jua kabla yako, wasichana wakipata wanaume hujenga kiburi na kujiona wapo sawa hata na wakubwa zao.”
“Haki ya Mungu mama sijapata mwanaume,” Cecy alijiapiza.
Mama yake alimweleza yote aliyoyaona kwa mwanaye usiku wa kuamkia siku ile.
“Haya bisha ninakusingizia?”
“Najua utasema hivyo, lakini mama sina mwanaume ila kuna mtihani moyoni mwangu wenye majibu tata.”
“Mtihani gani?”
Cecy alimwelezea ukaribu wake na mama Colin wa kuwa mteja mzuri wa ndizi zake na tabia ya kumwita mkwe mpaka siku aliporudi Colin kutoka Ulaya na kutambulishwa kama mchumba wake.
“Sasa hapo kipi kinakitatiza?” mama yake alimuuliza baada ya kumsikiliza.
“Mama sielewi kama kweli mama Colin amenichagua niwe mchumba wa mwanaye.”
“Mwanangu kumbe ndicho kinachokuchanganya?”
“Ndiyo mama yangu hakuna kingine, sijawahi kupenda wala simjui mwanaume. Lakini nimetokea kumpenda sana Colin na kutamani awe mume wangu.”
“Umesema ametoka Ulaya kusoma, sasa akuoe wewe mbumbumbu ambaye hata darasa la saba limekushinda?”
“Mama elimu haina mwisho, naweza kujiendeleza najua tatizo labda kuzungumza kingereza.”
“Sasa hicho kingereza utakijualia wapi?”
“Zipo shule nitajifunza nitajua.”
“Nataka nikuambie mwanangu, mama Colin kukuita mkwe ni kukutania tu, siku zote matajiri huwapeleka watoto wao kusoma Ulaya ili wawaoe watoto wa matajiri wenzao tena wasomi. Sasa wewe pangu pakavu wapi na wapi?”
“Sawa mama, lakini naamini ipo siku maji yatapanda mlima.”
“Hizo ni ndoto za mchana.”
“Sawa mama, ipo siku utakubali ndoto za mchana huwa zina ukweli.”
“Mwanangu naomba uachane na mawazo hayo muda ukifika Mungu atakupa mume mzuri mwenye mapezi na wewe.”
“Asante mama yangu.”
“Haya kalale mwanangu.”
“Haya mama usiku mwema.”
“Na kwako pia.”
Cecy aliagana na mama yake na kurudi chumbani kwake kulala, alipofika chumbani alizima taa na kujilaza kitandani. Hakukubaliana na mama yake, akili yake kubwa ilikuwa kwenye zawadi aliyoahidiwa na Colin.
Alijiuliza ni zawadi gani anayotaka kumpa ambayo hakuweza kumpa siku ile mpaka asubiri siku ya pili. Alijikuta akiuona usiku ukienda taratibu sana, hamu yake kukuche upesi ili akaione zawadi aliyoahidiwa na Colin.

Itaendelea Ijumaa
 
HADITHI: WAKILI WA MOYO
SEHEMU: 04
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500..

ILIPOISHIA:
Cecy aliagana na mama yake na kurudi chumbani kwake kulala, alipofika chumbani alizima taa na kujilaza kitandani. Hakukubaliana na mama yake, akili yake kubwa ilikuwa kwenye zawadi aliyoahidiwa na Colin.
Alijiuliza ni zawadi gani anayotaka kumpa ambayo hakuweza kumpa siku ile mpaka asubiri siku ya pili. Alijikuta akiuona usiku ukienda taratibu sana, hamu yake kukuche upesi ili akaione zawadi aliyoahidiwa na Colin.
SASA ENDELEA...

***
Mage pamoja na kukubali kuolewa na Colin bado alikuwa na kovu moyoni mwake la kutendwa na mtu aliyempenda kuliko kitu chochote chini ya jua Hans, mwanaume aliyemuingia kwenye ulimwengu wa mapenzi.
Wasiwasi wake mkubwa kwa Colin kuwa na mpenzi mwingine ambaye ametoka naye mbali na mwisho kuwa kama Hans na kuumizwa kwa mara ya pili kitu ambacho hakutaka kijirudie. Japokuwa hakuwa tayari kuliona lile na alikuwa tayari kulipigania penzi lake kwa nguvu zake zote.
Wazo la peke yake liliisumbua akili yake alihitaji msaada wa mtu
wa karibu. Mtu muhimu katika maisha yake alikuwa shoga yake Brenda ambaye aliamini anaweza kumsaidia juu ya uamuzi wake wa ghafla wa kumkabidhi moyo wake Colin bila kumchunguza.
Akiwa amejilaza kitandani alichukua simu yake na kumpigia Brenda, baada ya kuita kwa muda ilipokelewa upande wa pili.
“Vipi shoga kulikoni mpaka leo kupiga simu, badala ya kutumia njia ya whats up au twiter?”
“Shoga si la kulizungumzia kwenye mtandao, hili ni la uso kwa macho.”
“Mmh! Una nini tena shoga?” Brenda alishtuka.
“Kwanza upo wapi?”
“Nimerudi muda si mrefu natoka kufuatilia ile ishu.”
“Sasa naomba basi nikupitie tukakae ufukweni tuzungumze vizuri.”
“Hakuna tatizo.”
“Basi nakuja sasa hivi.”
“Poa.”
Mage alikata simu na kwenda kubadili nguo, kwa vile alikuwa ametoka kuoga muda si mrefu hakuwa na haja ya kwenda kuoga tena. Baada ya kuchagua nguo nzuri iliyompendeza alitoka kuelekea nje. Mama yake aliyekuwa sebuleni alishangazwa na mwanaye kutoka bila taarifa.
“Mage safari ya wapi?”
“Ufukweni mama.”
“Kufanya nini?”
“Mama akili yangu bado haipo vizuri ngoja nikaipoze kwa kuangalia maji.”
“Brenda mwanangu kumbuka sasa hivi wewe ni mchumba wa mtu, japokuwa hujavalishwa pete. Hiki huwa kipindi kibaya sana kwa msichana kwani anatakiwa kutulia. Unaweza kuharibu kila kitu na matokeo yake useme umerogwa.”
“Mama hujui kiasi gani nilivyo na msogo wa mawazo juu ya uamuzi wangu wa haraka wa kumkubali Colin. Katika mapenzi yangu na Hans sikuwaza kama kuna siku tutakuwa mbalimbali. Hivyo nimekuwa muoga sana mama naona kama nimefanya uamuzi wa ghafla sana.”
“Katika penzi lenu na Hans kuna kosa mlifanya ambalo nina imani kwa Colin limekuwa wazi sana.”
“Kosa gani mama?”
“Penzi lenu lilitawaliwa na usiri na mambo mengi mlifanya kwa siri bila wazazi wa mwenzako kujua.”
“Mamaa! Wadogo zake wote wananitambua.”
“Wazazi wake?”
“Ndiyo tulikuwa katika harakati za kutambulishana likatokea la kupatiwa mchumba,” Mage alisema kwa sauti ya masikitiko.
“Umeona! Pengine kama mngekuwa wawazi yote yasingetokea, sasa hivi ungekuwa mke wa Hans.”
“Mamaa! Usinikumbushe, kutaja ndoa yangu na Hans moyo unaniuma. Nampenda Colin lakini hawezi kumfikia Hans, kwake nilikuwa kama kipofu niliyebahatika kufumbua macho mara moja na kitu cha kwanza na mwisho kukiona kilikuwa ni yeye.”
“Ndiyo hivyo ukificha moto kwa kuufunika na shuka moshi utakuumbueni. Penzi mlilifanya la siri ndoa ya mwanamke mwingine imekuumiza.”
“Basi mama inatosha, niache nikapunguze mawazo ufukweni.”
“Kwa nini usimfuate mwenzio ili mwende pamoja, kufanya hivyo unaonesha jinsi gani unavyo muhitaji kama mumeo.”
“Mama siku za kutoka na Colin zipo, leo nina mazungumzo na Brenda.”
“Haya ila punguza mawazo, Mungu kasikia kilio chako umempata mwanaume wa haja anamzidi kila kitu Hans.”
“Kwa macho ni rahisi kusema hivyo, macho huwa yanaona lakini moyo ndiyo wenye jukumu la kuchagua ulichokipenda. Colin anaweza kuwa na umbile na sura nzuri lakini hakawa hana mapenzi kama Hans.”
“Mmh! Huyu Hans kakuchanganya sana mwanangu, ina maana akiachana na mkewe upo tayari kuolewa?”
“Mkewe angekuwa hajazaa ningekubali, lakini alichonifanyia Mungu anajua. Sasa hivi namchukia Hans kuliko kifo.”
“Basi mwanangu muwahi Brenda.”
“Sawa mama.”
Mage alitoka hadi nje na kuchukua gari aina ya Harrier Lexus na kuelekea Osterbay kwa shoga yake Brenda. Alimkuta akiwa tayari amejiandaa, hakuwa na haja ya kuingiza gari ndani kwani alikuta tayari ameishatoka nje ya geti.
Baada ya Brenda kuingia ndani ya gari Mage aliliondoa bila kusema kitu. Shogaye aligundua mabadiliko kwenye uso wa rafiki yake.
“Shoga kuna usalama?”
“Kiasi.”
Mage alijibu kwa mkato bila kumtazama shoga yake huku akifunga bleki katika foleni ndogo kwenye taa za daraja la Salenda. Baada ya taa kuruhusu aliondoa gari, Brenda hakubandua uso wake kwenye uso wa Mage na kugundua michirizi ya machozi kitu kilichomshtua sana.
“Shoga kulikoni?”
Mage alijikuta akipaki gari pembeni na kuanza kulia kilio cha chinichini. Brenda alishtuka sana na kumsogelea shoga yake aliyekuwa amelalia usukani huku akilia.
“Mage nini tena shoga si umesema tukazungumzie ufukweni?”
“Ni kweli, lakini inauma sana.”
“Sawa, hebu twende huko tutayaongea yote.”
“Papara ya mapenzi itaendelea kunitesa, hata sijui kwa nini nimeshindwa kujikontroo,” Cecy alisema akiwa bado ameinama kwenye usukani.
“Jamani Cecy, nani kakutenda tena?”
“Shoga hebu njoo uendeshe gari naweza kugonga maana kichwa changu hakipo sawa.”
Brenda alizunguka upande wa pili na kuingia kwenye gari na kuliondoa kuelekea Kigamboni. Baada ya kusubiri pantoni Kivukoni kwa robo saa, walivuka upande wa pili.
“Twende ufukwe gani?” Brenda alimuuliza baada ya kutoka nje ya geti.
“Yoyote ile,” Cecy alijibu akiwa amejilaza kwenye kiti ilichokilaza kwa nyuma.
“Mikadi panafaa?” Brenda alimuuliza huku akimtazama.
“Popote utapopaona panafaa.”
Brenda alipaki kwenye maduka na kununua vitu vya kutafuna wakiwa ufukweni kisha aliendesha gari hadi ufukwe wa Mikadi. Waliteremka na kuelekea upande wa bahari.
Hali ya hewa ilikuwa ya kawaida jua lilikuwa limefichwa kwenye mawingu huku upepo wa bahari ukipepea bila kuwa kero kwa mtu aliyekuwa ufukweni.
Kwa vile ilikuwa katikati ya wiki watu walikuwa wa kuhesabu ufukweni. Walitafuta sehemu nzuri na kutandika khanga na kukaa juu yake, kila mmoja kulinyoosha miguu kuelekea baharini.
Baada ya utulivu wa muda huku kimya kikitawala, Brenda alikuwa wa kwanza kuuvunja ukimya ule kwa kumsemesha shoga yake aliyekuwa ametuliza macho akitazama baharini.
“Mage.”
“Abee.”
“Hebu nitoe tongotongo, najiona kama nipo kizani na sauti ya upande wa pili ikiomba msaada bila kumuona mwenye tatizo. Siku zote tumekuwa watu tunaotegemeana kwenye matatizo yetu. Najua umeniita ili tusaidiane mawazo.
“Naomba unieleze tatizo lako, siku zote tunajua machozi si ufumbuzi wa tatizo zaidi ya kupambana nalo na kulitatua. Basi naomba unieleze kinachokusibu,” Brenda alisema kwa sauti ya kubembeleza.
“Brenda, nimekuwa nikikurupuka mara nyingi katika suala la mapenzi kitu ambacho kimekuwa kikinihukumu,” Mage alisema huku akimtazama Brenda.
“Mage mara ngapi umekurupuka? Suala la Hans pale ulikurupuka nini, ikiwa wote mlikuwa mkipendana tatizo wazazi wake.”
“Alichonitenda Hans hukijui?” Mage alimuuliza Brenda huku akimkazia macho.
“Mage nilikueleza toka siku ya kwanza, kitu kama kile hakiwezekanani. Hawawezi kulala pamoja kufanya mapenzi bila kinga ujauzito usipatikane.”
“Hans alinihakikishia hawezi kuzaa na yule mwanamke, kitu ambacho tungekifanya tukioana ili tuanze kutafuta mtoto pamoja.”
“Inawezekana alipanga vile, lakini imetokea bahati mbaya. Lakini nilikueleza mapema kuhusu mategemeo yako kwa Hans baada ya kuoa kuwa usimtegemee kabisa, lakini ulinibishia.”
“Brenda, unajua kiasi gani nilivyokuwa nampenda Hans?”
“Hilo lipo wazi, lakini ndiyo hivyo tena, kitu gani kingine kilichokufanya mpaka ukawa kwenye hali hii tofauti na la Hans?” Brenda alimuuliza Mage huku akimkazia macho.
Mage alimweleza kila kitu toka walipokutana kwa mara ya kwanza na mama Colin na kumwita mkwe kwa kujua anamtania mpaka siku alipomfanyia surprise ya kuletewa mwanaume nyumbani kwao.
“He! Makubwa, mbona kama umegeuzwa mbuzi hata bila ridhaa yako?” Brenda alihoji huku akigeuka kumtazama Mage usoni.
“Si kwamba sikutaarifiwa bali niliona kama utani, lakini kumbe yule mama alikuwa hatanii.”
“Ehe, baada ya kuletwa ikawaje?”
“Yaani hata sijielewi, baada ya kumuona nikawa nimevurugwa mtoto wa kike.”
“Mtume!” Brenda alisema huku akimtazama shoga yake kwa jicho la huruma.
Mage alimweleza chote kilichoendelea baada ya kumuona Colin.
“Mmh! Basi inaonekana Colin ni kitu cha haja?”
“Kwa kitu? Kitu hasa! Colin Mungu kajua kumtengeneza mwanaume yule. Yaani mpole na mstaarabu hadi raha,” Mage alisema huku akijishika kifuani na kufumba macho.
“Sasa tatizo nini?”
“Najiona nimejirahisi mapema sana bila kuijua historia yake.”
“Lakini si amekuhakikishia kuwa yupo tayari kukuoa?”
“Ndiyo, lakini mvulana mzuri kama yule lazima atakuwa na mpenzi tu. Mimi kumkubali nitakuwa naingilia penzi la mtu. Huoni kumkubali Colin ni sawa na kuyatafuta maumivu mengine?”
“Lakini bado hamjavishana pete ya uchumba una nafasi ya kumchunguza, kwani mmeisha du?”
“Bado.”
“Kumbe! Sasa tatizo nini?”
“Hata kama bado, najua nimechelewa kwa vile Colin, maisha ya Tanzania hajaishi sana. Kuna vitu aliniambia vimenichanganya sana.”
“Vitu gani?”
“Nilimweleza jinsi nilivyoumizwa na mapenzi na kumweleza najitupa tena ndani ya dimwi la huba bila kujua kina chake. Kuwa yeye ni boya la kuniokoa bila hivyo nitakufa maji.”
“Ukasemaje?”
“Alinieleza ananipenda zaidi ya kupenda huku akinithibitishia kuwa yeye ndiye tiba sahihi ya maumivu ya moyo wangu. Nilimweleza huenda hanipendi bali ananitamani na baada ya kuufaidi mwili wangu akinimbie.”
“Akajibu nini?”
“Brenda, Colin alizungumza kwa taratibu na kunihakikishia ananipenda sana nakumbuka baadhi ya mazungumzo yetu baada ya kumbana na maswali, nilimwambia:
“Najua ndiyo siku yako ya kwanza kuniona, siamini kama Colin unanipenda kama ninavyokupenda?”
Colin alinijibu: Mage toka nilipoelezwa nimepatiwa mchumba moyo wangu ulikuwa taabuni kutaka kukuona. Nilikuumba akilini kwa kila umbile na kukupamba kwa rangi nyingi.
“Amini Mage kila nilichokiwaza moyoni mwangu kilikuwa uongo. Nilichokiona ni zaidi ya vyote nilivyoviwaza,” Colin alisema huku amemshika mabegani na kunitazama usoni kwa jicho la huruma.
Nilimuuliza: Vitu gani hivyo Colin?” niliuliza huku nikijitahidi kuyatoa macho nje kama naweza kuyaona maneno atakayo niambia kwa macho.
Colin alinijibu: Kila mtu anapenda kuwa na mwenza mwenye sura anayoiwaza ambayo huamini huenda moja wapo, nami niliitengeneza yako niwezavyo. Lakini imekuwa kinyume kabisa,” Colin aliniambia huku akiachia tabasamu ambalo lilivunja nguzo za moyo wangu.
Nilijitahidi kumuuliza: Mmh! Colin, kwa nini?” nilimuuliza nami niliilazimisha tabasamu.
Alinijibu: Mage we ni mzuri wa wazuri mrembo wa warembo. Najiona kiumbe mwenye bahati kama nitakuwa mume wako,” Colin alisema huku akiwa ameyakaza macho kuonesha anachokizungumza hatanii.
Huku moyo wangu akiwa umetawaliwa na tabasamu nilimwambia: Siamini, Colin siamini,” nilisema mikono yangu nikishika kifuani huku machozi yakinitoka.
“Mage huamini nini?” Colin aliniuliza kwa uso wa huruma.
“Inawezekana Colin unalitamani umbile langu lakini si mapenzi ya dhati toka moyoni mwako,” nilisema huku machozi yakinitoka na kuweka michirizi kwenye mashavu yangu.
“Mage amini nakupenda kama ugonjwa wa shinikizo la damu linavyochukuwa uhai wa mtu ghafla,” kila kauli ya Colin ilizidi kuusambalatisha moyo wangu.
“Colin sijui wewe ni mwanaume wa aina gani?” nilijisema huku akijitahidi kutengeneza tabasamu ndani ya machozi.
“Kwa nini mpenzi?” aliniuliza huku akinitazama kwa huruma kitu ambacho sikuwahi kukiona kwa Hans pamoja na kumpenda kote.
“Maneno yako yamekuwa na sumaku yenye nguvu ya ajabu kuweza kunasa chuma kilichomo moyoni mwangu,” nilimweleza nilivyo kuwa radhi kuwa mateka wa penzi lake.
“Sijakuelewa mpenzi?” Colin aliniuliza.
“Ameweza kuuteka moyo wangu na kukubali kuwa mateka wako. Colin nakuamini, usiniache katikati ya bahari nitakufa maji boya langu ni wewe. Maumivu ya mapenzi ni zaidi ya kung’olewa jino bila ganzi,” nilimtaadhalisha Colin.
“Amini Mage nakuahidi kuwa mume mwema,” Colini aliniahidi japokuwa sikujua aliyosema yanatoka moyoni au mdomoni.
“Nami nakuahidi kuwa mke mwema,” nami nilimuahidi ahadi toka moyoni wangu.
Baada ya Brenda kumsikiliza kwa muda shogaye alisema:
“Mmh! Mbona kina kitu kipo wazi tatizo nini?”
“Wasiwasi wangu anaweza kuwa na mtu wake.”
“Anaweza kuwa naye lakini si wa malengo ya kuwa mke na mume, kwani picha yake unayo?”
“Ndiyo, tulipiga siku ile tena alilazimisha yeye.”
Mage alisema huku akifungua simu yake upande wa picha. Baada ya kuijaza kwenye kioo cha simu alimuonesha Brenda. Shoga yake alishtuka kumuona mwanaume mzuri akiwa na Mage katika pozi tofauti za mahaba.
“Mage! Colin ni mwanaume mzuri sana, mlivyokaa kama mke na mume sijui picha za ndoa yenu zitakuwaje?”
“Nina wasiwasi nimekurupuka sana katika kumkubali.”
“Walaa, mapenzi shoga yangu hayana fomula, mnaweza kukutana hivi na penzi lenu likadumu milele, lakini mnaweza kuandaana mwisho mkawa maadui wakubwa kama unavyomuona Hans.”
“Umeona! Yaani sasa hivi sitakiwa kumuona wala kusikia jina lake.”
“Nina imani hili litakwenda vizuri kwa vile hata mzazi wake amekupenda pia familia zenu zinafahamiana na zinapendana.”
Wakiwa katikati ya mazungumzo simu ya Mage iliita, namba ilikuwa mgeni. Aliiangalia kwa muda bila kuipokea.
“Mbona hupokei?” Brenda alihoji.
“Hata sijui nani, inawezekana ni Hans, niliapa sipokei simu yake.”
“Hebu pokea hujui anataka kukuambia nini?”
“Hana chakuniambia.”
Wakati huo simu ilikuwa imekatika, baada ya muda uliingia ujumbe mfupi wa maneno. Mage aliufungua na kuusoma:
Najue upo bize na mambo ya mchana, ushikapo simu naomba unipigie, Moyo wangu u taabuni mpaka sikie sauti yako.
It ‘s me Colin.
Mage baada ya kusoma ujumbe ule alipiga kelele huku akishika kifua.
“Mungu wangu!”
“Nini tena mbona unanitisha?” Brenda alishtuka.
“Mungu wangu! Kumbe alikuwa Colin,” Mage alisema huku akishika kifua.
“Mmh! Ina maana huna namba yake?”
“Sina.”
“Ina maana mlipokutana hamkupeana namba za simu?”
“Hatukupena, wote tulichanganyikiwa.”
“Basi mpigie.”
“Duh! Sijui anielewaje?” Mage aliingia wasiwasi.
“Mage akuelewe kivipi? Brenda alimshangaa rafiki yake.”
“Ataona kama ninalinga au siyo muaminifu!”
“Hawezi kwa vile leo ndiyo siku yake ya kwanza kukupigia.”
“Mmh! Ngoja nijaribu.”
Mage alichukua simu na kumpigia Colin, iliita kwa muda bila kupokelewa. Alirudia zaidi ya mara nne lakini haikupokelewa kitu kilichomnyima raha Mage.
“Brenda lazima Colin atakuwa amekasirika, siwezi kupiga mara nne bila kupokelewa.”

Itaendelea Jumatatu
 
HADITHI: WAKILI WA MOYO
SEHEMU: 05
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500..

ILIPOISHIA:
“Waaawoo! Itafanyikia wapi?”
“Nyumbani saa moja usiku.”
“Kesho nitakuletea zawadi nzuuri.”
“Nitafurahi sana, nikuacheni muendelee na mazungumzo, mengi tutazungumza kesho.”
“Asante mpenzi nimefurahi sana kusikia sauti yako.”
“Unishindi mimi.”
SASA ENDELEA...

****
Usiku ulikuwa mrefu kwa Cecy, alitamani siku ya pili ifike haraka ili akaijue hiyo zawadi aliyoahidiwa na Colin. Alijikuta akipindua kitandani usingizi ulikimbia kabisa. Kutokana na kukosa usingizi akiwazia zawadi alijikuta akichelewa kuamka, kitu kilichofanya akose ndizi nzuri.
Kwa vile shida yake ilikuwa kufika kwa kila Colin akachukue zawadi, ilibidi anunue ndizi nzuri kwa wenzake ambazo kwake hazikuwa na faida kwa vile angekwenda kuuuza kwa bei ileile.
Hakuchukua ndizi nyingi, alirudi hadi nyumbani. Baada ya kuoga na kujipamba na kuhakikisha amependeza alibeba ndizi zake na kuelekea kwa mama Colin huku akijiuliza Colin anataka kumpa zawadi gani.
Kama kawaida alipofika kwenye mlango wa geti alibonyeza kengele, mlinzi alimfungulia na kuingia ndani.
“Mmh! Cecy muuza ndizi unapendeza kuliko mfanyakazi ofisini!” Mlinzi alimshangaa Cecy kila siku kupendeza na kuonesha uzuri wake.
“John acha ushamba nani alikuambia muuza ndizi anatakiwa kuwa mchafu?”
“Pamoja na hayo, wee umezidi.”
“Kwa hiyo ulitakaje?”
“Walaa, nakupongeza tu.”
“Asante.”
“Ila mama ametoka sasa hivi umechelewa kama dakika mbili.”
“Na..na Colin?” Cecy alishtuka.
“Ye yupo.”
“Ooh! Afadhali!”
Cecy alisema huku akishusha pumzi ndefu kitu kilichomshangaza mlinzi.
“Mbona umeshusha pumzi?”
“John, mbona una maswali mengi kama polisi?” Cecy alimjia juu mlinzi.
“Basi Cecy nisamehe.”
Cecy alisogea mlangoni wa kuingilia nyumba kubwa, aliweka beseni la ndizi chini na kuita kwa sauti.
“Ndiziii.”
Colin alitoka mlangoni akiwa amebeba mfuko mkubwa kidogo mkononi, Cecy alipomuona alijikuta akipoteza kujiamini na mapigo ya moyo kwenda mbio.
“Karibu mchumba,” Colin alimkaribisha huku akitabasamu.
“Asante.”
Colin alisogea hadi beseni na kuchagua ndizi.
“Mbona leo ndizi kidogo?”
“Chukua zote, nilichelewa kuamka.”
“Ooh!Pole.”
Baada ya kuchukua ndizi aliingia nazo ndani huku akiacha mfuko wake pembeni ya Cecy. Cecy alimsindikiza kwa macho huku moyo wake ukiendelea kuteseka juu ya Colin.
Aliutazama mfuko ulioonekana una vitu ndani, alijiuliza ni wake na kama wake kuna zawadi gani? Lakini hakujua kama ndiyo wake. Baada ya muda alitokeza tena Colin akiwa kwenye tabasamu.
“Mmh! Mchumba samahani nilisahau kukusifia umependeza sana.”
“Asante,” Cecy alijibu huku akiwa ametawaliwa na aibu.
“Jana nilikuahidi nini?” Colin alimuuliza Cecy.
“Zawadi.”
Colin alichukua mfuko na kumpa, Cecy aliupokea kwa kupiga magoti kwa heshima mpaka chini.
“Asante mpe...M..chumba,” Cecy aliingia kigugumizi.
“Usijali, sasa ni hivi...leo jioni nitakuwa na sherehe ndogo ya kuzaliwa kwangu.”
“Waaaooo, hongera mchumba.”
“Asante, naomba kila kilichomo ndani ya mfuko huu, uvae leo kwenye sherehe yangu sawa mchumba?”
“Sawa.”
Colin alimpa elfu ishirini, Cecy alishtuka kwa vile ilikuwa nyingi tofauti na malipo ya siku zote ya shilingi elfu tano.
“Colin mbona nyingi?”
“Usiwe na wasi chukua zote.”
“Asante, kwa hiyo sherehe inaanza saa ngapi?”
“Saa moja usiku, ukikosa utaniudhi.”
“Jamani si usiku?”
“Kodi gari.”
“Basi nitakuja.”
Cecy aliondoka na kumuacha Colin akimsindikiza kwa macho. Wakati Cecy akiingia getini Colin alikuwa ghorofani akimtazama. Aligundua Cecy ni mzuri kuliko Mage, lakini alikosa vigezo kutokana na hali ya maisha kuwa ya sayansi na tekinolojia inayomtaka kila mtu kuwa na elimu ili kukabiliana na kasi yake bila hivyo lazima ikuache.
Wakati Cecy anatoka alipishana getini na Mage aliyekuwa kwenye gari aina ya Toyota Land Cruiser V8. Colin aliyekuwa ghorofani alishtuka kuona gari la kifahari likiingia nyumbani kwao. Hakuteremka chini haraka, alisubiri kumuona nani anaingia. Baada ya gari kusimama kwenye maegesho alishtuka kumuona Mage akiteremka.
Alijikuta akimsahau Cecy ghafla kutokana na jinsi Mage alivyokuwa amependeza kwa vazi la gauni fupi la rangi nyeusi na weupe lililoishia chini kidogo ya makalio.
Alijikuta akijisemea mwenyewe moyoni.
“Mage ni msichana mrembo sana.”
Aliteremka chini kwenda kumpokea, Mage alipomuona alimkimbilia na kumrukia kwa furaha.
“Waaaoo my husband to be.”
“Waaaooo my wife.”
Walishikana mikono na kuelekea ndani kila mmoja akiwa na furaha tele moyoni. Wakiwa wanaelekea ndani Mage alimwambia Colin.
“Baby, naomba ujitayalishe tuna mtoko mdogo.”
“Wapi baby?”
“Surprise.”
“Mmh! Haya.”
Walikwenda wote chumbani kwa Colin, ili kuokoa muda aliingia bafuni kuoga ili watoke. Akiwa bafuni Mage alimfuata.
“Vipi Mage,” Colin alishtuka huku akigeuka nyuma.
“Nimekuja kukuosha mpenzi wangu, au kuna ubaya?”
Colin hakuwa na jinsi alikubali kuoga na Mage, baada ya kuoga waliondoka kuelekea mjini. Mage alimpeleka kwenye duka la nguo na kumtaka mpenzi wake achague itakayo mpendeza kwenye sherehe yake ya kuzaliwa.
“Colin mpenzi nataka uchague suti nzuuuri, itakayokupendeza jioni ya leo. Nami unichagulie nguo nzuri ambayo tukisimama wakati wa kulishana keki kila mtu moyo umchome.”
“Suti nichagulie wewe, nguo yako nitakuchagulia mimi,” Colin alijibu huku akitabasamu na kufanya Mage auone vizuri uzuri wa mpenzi wake.
“Sawa.”
Walikubaliana kila mmoja kumchagulia mpenzi wake nguo nzuri.
***
Cecy baada ya kutoka kwa kina Colin hakuwa na biashara yoyote alirudi moja kwa moja nyumbani kwao akiwa na shauku ya kuiona zawadi aliyopewa.
Alijikuta akianza kuiamini ndoto yake kuwa Colin naye anampenda kama yeye bila kujali elimu yake ya kata.
Kutokana na kuchanganywa na zawadi, alipofika kwao alisahau kumsalimia hata mama yake aliingia moja kwa moja chumbani kwake na kutoa vilivyokuwemo kwenye mfuko na kuviweka kitandani.
Alikuta gauni zuri la rangi ya zambarau lenye mchanganyiko mweusi kwa mbali. Alishtuka kukuta nguo za ndani mbili moja nyekundu na nyingine nyeupe.
Viatu vilikuwa vya kisigino kirefu kidogo chenye mikanda. Alivaa na kuzunguka chumbani kama miss aliyekuwa akitafuta pointi. Aliufungua mkebe kidogo na kukuta mkufu mdogo ya fedha.
Aliivaa na kuchukua kioo na kujikuta akitabasamu huku akiwa na hamu ya kutoka nje ili walimwengu wamuone alivyopendeza.
“Kumbe na mimi mzuri namna hii, kwa nini Mungu umeninyima elimu?” Cecy alijikuta akianza kulia.
Mama yake alikuwa amesimama mlangoni baada ya kupitwa na mwanaye bila kusemesha na kuacha kazi zake kumfuata ili kujua mwanaye amepatwa na kitu gani.
Alipofika alimuona akitoa vitu kwenye mfuko alitulia mpaka aone mwisho wake. Alishtuka kumuona akitoa nguo za gharama na kuvaa. Alijiuliza amezitoa wapi, lakini hakutaka kumuuliza haraka alisubiri aone mwisho wake.
Kauli ya mwanaye ya kujisifia ilimfanya atabasamu, lakini alipoanza kulia huku akimlaumu Mungu kukosa elimu alimshtua.
“Cecy.”
Cecy alishtuka na kugeuka bila kuitikia huku akifuta machozi, alipomuona mama yake aliitikia.
“Abee mama.”
“Unalia nini?”
“Roho inaniuma kukosa elimu pia nipo njia panda kwa Colin.”
“Kwanza nguo hizi umetoa wapi?” mama yake alikaza sauti.
“Kanipa Colin.”
“Ili?”
“Mama alisema atanipa zawadi, nilipofika kwao leo alinipa na ameniomba leo nihudhulie kwenye sherehe yake ya kuzaliwa.”
“Saa ngapi?”
“Saa moja usiku.”
“Utakwendaje usiku na utarudije?”
“Amenipa hela ya gari.”
“Mmh! Haya, mwisho wako na Colin tutauona.”
“Mama unavyonifikiria sivyo,” Cecy alijitetea.
Mama yake aliachana na mwanaye na kurudi nje kuendelea na kazi zake na kumuacha Cecy akibadili nguo. Aliziweka vizuri nguo zake ambazo alitakiwa kuzivaa jioni ya siku ile.
***
Cecy alitumia zaidi ya nusu saa bafuni kuoga na saa nzima kujipamba kuhakikisha ile inakuwa kete ya kumfanya Colin aamini yeye ni msichana mrembo. Kabla ya kutoka alimwita mama yake aongeze kumremba.
“Mmh! Mwanangu inatosha.”
“Mamaa! Sitaki nionekane tofauti na nitakaowakuta si unajua lazima kutakuwa na wageni wengi.”
Mama yake alimtengeneza mwanaye kwa kumpaka vizuri poda lipsitiki na wanja mwembamba na kumfanya Cecy kuwa kama malkia. Baada ya kujiamini amependeza alitembea taratibu kuelekea barabarani na kukodi gari kuelekea kwa kina Colin.
***
Sherehe ilifanyika kwenye ua wa jengo la nyumba ya kila Colin kwa kupambwa vizuri kuwafanya wageni wafurahie mandhali ile. Wageni walifika kwa wakati kila mmoja alionekana ana maisha mazuri kutokana na magari ya kifahari kupaki kwenye maegesho.
Asilimia kubwa ya wageni walikuwa wamefika na kukaa kwenye nafasi zao huku wakiendelea kutumbuizwa na muziki laini. Kutokana na foleni Cecy alikuwa wa mwisho kuingia, ilikuwa dakika chache kabla ya sherehe haijaanza.
Baada ya kuteremka kwenye teksi, alishika gauni lake kwa kulipandisha juu na kusogea mlangoni. Mlinzi alimfungulia bila kumfahamu kama ni Cecy muuza ndizi kwa jinsi alivyokuwa amependeza kupita kiasi.
Aliingia kwa mwendo wa taratibu kuelekea kwenye kiti kilichokuwa wazi, kila mmoja aligeuka kumuangalia Cecy msichana maskini mwenye elimu duni lakini mwenye urembo wa asili.
Mama Colin aliyekuwa amekaa na mama Mage alishtuka kumuona msichana mrembo lakini mgeni machoni mwake. Alimsindikiza kwa macho mpaka alipokwenda kukaa.
Baada ya Mage kukaa na kupatiwa kinywaji, zilipita dakika tano sherehe ya kuzaliwa Colin ilianza kwa Colin kutokeza akiwa ameongozana na Mage.
Moyo ulimshtuka Cecy lakini hakujua yule msichana aliyetoka naye ndani ni nani yake. Lakini hakutaka kuumiza moyo wake kwa kuamini kabisa huenda yule ni mpambe aliyechaguliwa kwa ajili ya kumsindikiza. Alijikuta akiingia wivu kwa kujiuliza kwa nini hakuchaguliwa yeye ndiye awe mpambe wake.
Lakini kwa upande mwingine aliamini huenda kutojua kingereza kulichangia, kwa vile mambo mengine yanayohitaji kuzungumza kingereza yangemshinda. Wazo lile aliliafiki na kujiona ana deni la kwenda twisheni kujifunza maneno mawili matatu ya Kingereza ili aendane sawa na Colin.
Kila alivyomuangalia Colin alivyokuwa amependeza katika vazi la suti, moyo wake ilizidi kuteketea na kutamani siku ile ndiyo ingekuwa siku ya kuvishwa pete ya uchumba na kila mtu kujua yeye ni mchumba wa Colin angekuwa juu zaidi ya mawingu.
Wakati sherehe ikiendelea Colin alishtuka kutomuona Cecy kwenye sherehe ile, pamoja hakuwa mpenzi wake lakini alitokea kumpenda kumuona kutokana na jinsi alivyojiweka na kuwa tofauti na wasichana wengi wanaotoka familia duni.
Alijikuta akiwa na wasiwasi wa kutomuona kwenye sherehe yake wakati alimualika. Aliondoka kwenye kiti chake na kumfuata mama yake kumuuliza kama amemuona Cecy.
“Vipi Colin?” mama yake aliinama kumsikiliza.
“Eti, hujamuona Cecy?”
“Cecy! Yupi?”
“Mkweo.”
“Mmh! Sikumualika si unajua watu waliokuja hapa mwenye hadhi zao, hivyo angekuwa tofauti na wengine.”
“Mimi nilimualika.”
“Sasa Colin... yule msichana atavaa nini ili alingane na hadhi ya sherehe hii. Inawezekana kabisa John kamzuia getini kutokana na hadhi ya sherehe yako.”
“Kama atakuwa amefanya hivyo atakuwa hakutenda haki kwa vile mimi ndiye niliyemualika.”

Itaendelea Jumatano
 
HADITHI: WAKILI WA MOYO
SEHEMU: 06
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500..

ILIPOISHIA:
“Mmh! Sikumualika si unajua watu waliokuja hapa mwenye hadhi zao, hivyo angekuwa tofauti na wengine.”
“Mimi nilimualika.”
“Sasa Colin... yule msichana atavaa nini ili alingane na hadhi ya sherehe hii. Inawezekana kabisa John kamzuia getini kutokana na hadhi ya sherehe yako.”
“Kama atakuwa amefanya hivyo atakuwa hakutenda haki kwa vile mimi ndiye niliyemualika.”
SASA ENDELEA...

“Achana naye, si muhimu kama sherehe yako,” mama Colin alijibu kwa mkato huku akichukua glasi ya kinywaji na kupeleka mdomoni.
“Hapana,” Colin alisema huku akielekea getini.
Mama yake hakushughulika naye alimuacha aende, alipofika getini alimuuliza John kama amemuona Cecy.
“Sijamuona, sizani kama anaweza kuja kwenye sherehe ya watu wazito kama hii. Kila mmoja kaja na gari la kifahari, msichana mmoja ndiyo kaja na gari la kukodi, muuza ndizi kama Cecy atakaa wapi?” John alisema kwa dharau.
“John au umemkatalia?” Colin alimuuliza huku akimkazia sauti na macho.
“Hapana bosi,”John aliingiwa hofu.
“Sasa kesho aje aseme umemzuia jihesabu huna kazi.”
“Sijamuona kwa kweli, kama akifika nitamruhusu aingie.”
Wakati Colin akirudi ndani, Cecy alikuwa akitoka msalani na kukutana uso kwa uso. Kwa vile Colin alikuwa na hasira alimuona msichana mrembo lakini akili yake haikumtambua.
Baada ya kusalimiana alimchangamkia kama wageni wengine na kutaka kuelekea ukumbini.
“Colin jamani ndiyo nini?” Cecy alimsemesha.
Sauti ya Cecy ilimshtua Colin na kugeuka na kujikuta akitazamana na msichana mrembo.
“Mungu wangu, nini wewe Cecy?” Colin alishtuka.
“Naam, ni mimi,” Cecy alisema kwa sauti ya kike huku akishika mkono mmoja kiunoni na kunesa kwa madaha na macho kuyarembua.
“Yaani huwezi kuamini, natoka nje kukuuliza.”
“John kasemaje?”
“Cecy ulivyopendeza umetuchanganya wengi, kuanzia mama mpaka John getini amekusahau, anasema hajakuona.”
“Jamani! Ndizi ni kazi lakini umbile kazi ya Muumba, ninyimwe kila kitu? Nimemkosea nini Mungu?” Cecy alisema kwa sauti ya kinanda na kumfanya Colin aamini kama si kutangaza uchumba basi yeye angekuwa chaguo lake.
“Basi nimefurahi kukuona pia hongera umependeza sana na karibu sana.”
“Asante.”
“Wacha niwahi sherehe inanisubiri mimi.”
“Hakuna tatizo tupo pamoja.”
“Nilisahau kamsalimie mama ajue upo.”
“Sawa.”
Cecy baada ya kuagana na Colin alikwenda mpaka alipokuwa amekaa mama Colin na kumsemesha.
“Shikamoo ma’ mkwe,” alimsalimia huku akipiga magoti kwa heshima.
“Ha! Cecy mkwe wangu jamani, nisamehe sana nilikusahau nawe umependeza sana.”
“Ni kawaida yangu.”
“Karibu mkwe.”
“Asante, nipo mbele.”
“Hakuna tatizo.”
Mama Colin alimsindikiza mpaka anakaa na kutikisa kichwa na kujisemea moyoni: “Cecy msichana mzuri sana.”
Sherehe iliendelea kila mmoja akiifurahia huku Mc akieleza kila hatua iliyokuwa ikiendelea. Ilifika wakati wa kukata keti, kama kawaida Mage ndiye aliyekata keki na kumlisha kisha Colin kumlisha Mage.
Kisha keki ilikatwa vipande kisha Colin alipita kila meza ya wageni na kumlisha mojamoja huku akipiga naye picha. Baada ya zioezi lile alimwambia mpigapicha ahakikishe anampiga Cecy picha zaidi ya ishirini za mikao tofauti na kumpelekea.
Mpiga picha alifanya kama alivyoelekezwa kwa kumfuata Cecy na kwenda naye kumpiga picha tofauti.
Baada ya zoezi la kulishana keki kumalizika, Colin aliomba kipaza sauti na kuzungumza machache kuhusiana na sherehe yake kwa kuwashukuru wageni waalikwa.
“Kwanza namshukuru wazazi wangu kunizaa kwa mama yangu mzazi kunilea na baba yangu aliyetangulia mbele ya haki. Pia nawashukuru wageni waalikwa kwa kufika katika sherehe ya kuzaliwa kwangu.
“Leo ni siku muhimu na maalumu katika historia ya maisha yangu, kitakacho kifanya ni hatua moja kuelekea katika maisha yangu ya kujitegemea. Wazazi wangu na wageni waalikwa natumia siku ya yangu ya kuzaliwa ili kumtambulisha mchumba wangu kwa kumvisha pete.”
Kauli ile ilifanya moyo wa Cecy ilipuke pa! Na kufanya mapigo ya moyo kwenda kwa kasi. Alijiuliza kauli ile anayoisikia ni ya kweli au anaota ndotoni. Akili yake ilipata jibu la kupewa nguo nzuri na kualikwa kwenye sherehe ile. Aliiona ndoto yake ya mchana kuwa mke wa Colin ilikuwa ikitimia muda si mrefu.
Alitulia akijipa ujasiri ili kunyanyuka kwenda kuvishwa pete mbele ya umati ule akiitwa. Colin aliendelea kuzungumza huku akiingiza mkono mfukoni na kutoa mkebe wenye pete ya uchumba.
“Jamani naomba mpenzi wangu wa moyo ambaye anatarajiwa kuwa mama wa watoto wangu asogee mbele.”
Kauli ilimfanya Cecy atake kunyanyuka akiamini kabisa yeye ndiye mchumba wa Colin. Kabla hajanyanyuka kwenda mbele alishangaa kumuona Mage msichana aliyetoka naye ndani akisogea mbele akiwa ameshika kifuani asiamini kilichosemwa.
Baada ya kufika hapo Mc alichukua kipaza sauti na kuongoza zoezi lile.
Wakati huo Cecy alikuwa ameingiwa ganzi mwilini na kuona kama Colin kumuita kwenye sherehe ile ilikuwa amemtendea unyama. Alijiuliza kitu gani alichomtendea Colin mpaka kumfanyia ukatiri kama ule. Alijitahidi kuzuia hali ile kwa kushika mkono kifuani kuzuia mapigo yaliyokuwa yakienda kasi huku kijasho chembamba kikimtoka.
Wakati wa kuvishwa Mage pete kilikuwa kipindi kigumu kwa Cecy, ilikuwa sawa na kupasuliwa moyo wake kwa kisu butu bila ganzi. Bila kujielewa presha ilimpanda alishindwa kuizuia na kujikuta akiona kiza kizito mbele yake , alipiga kelele. “Mungu wangu.” alijikuta akinguka chini kama mzigo na kuwashtua waliokuwa wamekaa naye karibu.
Tukio lile lilizua taharuki na kusababisha sherehe kusimama, wakati huo zoezi la pete lilikuwa limeisha. Colin na mama yake walishtuka kusikia aliyeanguka ni Cecy.
Walikimbia eneo la tukio na kumkuta amezungukwa na watu.
“Vipi?” waliuliza kwa sauti ya mshtuko.
“Hata sijui, nilimuona akishika kifuani na kuhema kwa kasi kisha kufumba macho. Nilipotaka kumuuliza nilimsikia akisema Mungu wangu na kushangaa kumuona akianguka chini. Nilijitahidi kumuwahi nilichelewa tayari alikuwa ameanguka chini,” alisema dada mmoja aliyekuwa amekaa meza moja na Cecy.
“Labda ana kifafa?” mmoja alichangia.
“Hapana kile si kifafa, kwa jinsi nilivyomuona si kifafa,” alijibu aliyekaa naye meza moja.
“Kifafa gani kisicho na povu,” mwingine aliongezea.
“Jamani tumuwahishe hospitali,” mama Colin alisema.
“Mama we’ baki na wageni acha mimi nimpeleke,” Colin alisema huku akipiga magoti na kushika kichwa cha Cecy aliyekuwa ametulia kama amelala.
“Hapana Colin wewe baki na wageni kumbuka sherehe ni ya kwako pia umemaliza kumvisha mchumba wako pete muda mfupi, hivyo unatakiwa kuwa naye karibu. Endeleeni na sherehe mimi ninatosha.”
Colin alikubaliana na mama yake, yeye alibaki na kuendelea na sherehe na mama aliyemchukua Cecy na kumuwahisha hospitali.
***
Cecy baada ya kufikishwaa hospitali alichukuliwa vipimo na kuoneka hana tatizo kubwa ila presha ilikuwa juu. Lilifanyika zoezi kuishusha mara moja na kurudi katika hali ya kawaida.
“Nafikiri tatizo siyo kubwa sana, baada ya kumaliza drip nitamruhusu,” daktari alisema.
“Itachukua muda gani?”
“Si muda mrefu mtaondoka naye.”
Mama Colin alitoka na kukaa kwenye makochi huku amekasirika na kulaumu kitendo cha mwanaye kumualika msichana yule ambaye hakuwa na hadhi ya sherehe ile na kufikia kuharibu starehe yake kwa kuacha shughuli ya mwanaye kwa ajili ya msichana dhalili kama yule.
Alipanga kupiga marufuku ukaribu wa Cecy na Colin kwa vile aliuona unataka kwenda ndivyo sivyo. Yeye alitengeneza utani ambao ulimtia wasiwasi kwa mwanaye kuamini ni kweli, akiwa katikati ya mawazo daktari alimshtua:
“Mama mgonjwa wapo yupo tayari unaweza kumchukua.”
Alinyanyuka na kwenda wadini alipomkuta Cecy amekaa kitandani.
“Vipi mkwe?”
“Nashukuru sijambo.”
“Tatizo nini?”
“Hata najua! Nimejikuta nikiona kiza ghafla,” Cecy alipindisha ukweli.
“Imeisha wahi kukutokea?”
“Hata siku moja, hata mimi najishangaa, ila samahani mkwe kwa kuharibu sherehe ya mwanao.”
“Ujaharibu kitu sherehe inaendelea kama kawaida.”
“Naomba uniende nyumbani.”
“Hapana nitakupeleka.”
Alimchukua na kumuwahisha kwao ili yeye ageuke awahi sherehe. Alipomfikisha alimpa elfu hamsini kwa ajili ya kujiangalizia hali yake.
“Mkwe ugua pole.”
“Asante ma’ mkwe.”
Cecy aliagana na mama Colin na kwenda kugonga mlango, mama yake aliyekuwa hana amani na moyo wake toka aondoke mwanaye kwenda kwenye sherehe za usiku.
Muda wote alikuwa macho, mwanaye alipogonga aliwahi kufungua.
“Umerudi mwanangu?”
“Ndi..ndi..ndiyo mama.”
Kauli ya Cecy iliyochanganyikana kigugumizi na kilio ilimshtua.
“Cecy nini mama?”
“Ningejua nisingeenda,” alisema sauti ya kilio.
“Kwa nini?”
“Yaani wameniita kuniumiza! Nimewakosea nini?”
“Kukuumiza! Kivipi?”
“Mama yaani sijawahi kuumizwa moyo wangu kama leo, najua unaniona mtoto mdogo lakini nina hisia kama mtu mwingine, mama inaumaa,” Cecy alisema kwa uchungu huku akishika mkono kifuani.
“Kuna nini mbona uniweki wazi?” mama yake alishtuka.
“Mama Colin wa kuniita kunionesha mchumba wake?”
“Kukuonesha kivipi?”
Cecy alimweleza kila kitu kilivyokuwa katika sherehe, mama yake alishtuka na kusema:
“Mwanangu unataka kujiua bure, nilikueleza na mapema tajiri na sisi kina pangu pakavu wapi na wapi?”
“Kwa nini mama yake ananiita mkwe wakati mwanaye ana mwanamke mwingine?” Cecy aliuliza macho yakijaa machozi.
“Kuna siku alikutamkia suala la uhusiano kati yake na wewe?”
“Hapana.”
“Sasa kuumia huko kumetoka wapi?”
“Mama! Nampenda sana Colin.”
“Ulimwambia unampenda?”
“Nilikuwa naona aibu.”
“Siku zote moyo ni mfungwa wa mapenzi hasa kumpenda asiyejua anapendwa mdomo wako ndiyo wakili wa kuutetea moyo wako. Bila hivyo upendo wako utateketea kama mwanga wa mshumaa mchana wa jua kali, hakuna atakayeuona mwanga wake.”
“Mama, Colin alionesha ananipenda.”
“Nilikueleza toka zamani ule ni utani tu wala hakuna ukweli wowote.”
“Kwa kitendo walichonifanyia siendi tena kwao kuuza ndizi.”
“Mwanangu nikueleze mara ngapi kila kitu kinatokana na baraka za Mungu. Muombe yeye ndiye atakayekuchagulia mwanaume wa maisha yako.”
“Asante mama kwa kunitia moyo.”
“Basi badili nguo kisha uoge ule ulale.”
“Mama hata hamu ya kula ninayo, wacha tu nikalale.”
Cecy aliingia chumbani kwake kulala na kumwacha mama yake akiwa amesimama na kuyafikiria yote aliyoelezwa na mwanaye. Alimuonea huruma kwa kujiingiza kwenye mapenzi ya kumpenda mtu mwenye mpenzi mwingine anayempenda.
Kingine kibaya ilikuwa hali yao duni ambayo ilikuwa tofauti na matazamo ya familia yenye fedha kuwaangalia matajiri na wasomi wenzao. Alijiuliza kwa hali iliyomtokea mwanaye iliyopelekea kupatwa na presha kupelekea kukimbizwa hospitali itachukua muda gani kumtoa.
Aliamini ingemtesa mwanaye kwa kipindi kirefu na kumfanya akose amani ya moyo wake. Lakini aliamini atampatia ushauri nasaha utakaomrudisha katika hali ya kawaida. Aliachana na mawazo yale na kwenda chumbani kwake kulala.

ITAENDELEA
 
SEHEMU: 08
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500..

ILIPOISHIA:
“Mama tukiwaacha watatuzoea, nimeacha kwenda kwao bado tu hawajaridhika mama niache akanithibitishie alichokisema. Ni kweli nampenda Colin lakini hatujatamkiana mambo ya mapenzi yeye kayatoa wapi?” Cecy alisema kwa jazba.
“Mwanangu jasho la mnyonge haliendi joshi.”
“Sawa, lakini Mungu yupo.”
Cecy aliweka beseni lake na kwenda chumbani kwake akiwa amefura kwa hasira. Moyoni alijiapia siku akikutana na mama Colin siku hiyo atamkosea adabu kwa dharau aliyoifanya nyumbani kwao.
SASA ENDELEA...

****
Familia mbili zilikutana kupanga tarehe ya harusi ya watoto wao. Kila mmoja alitaka kufanyika harusi ya kifahari kutokana na watoto wao kuwa wa kwanza kuoa na kuolewa katika familia zao.
Baada ya makubaliano ya tarehe ya ndoa, waliwataarifu watoto wao kilichokuwa kikiendelea juu ya ndoa yao. Mara moja zilisambazwa taarifa kwa ndugu na jamaa kwa kupewa kadi na wengine kuhudhulia vikao vya maandalizi ya harusi vilivyoanza mara moja.
Mage alipanga picha zake za harusi kuzisambaza katika mitandao yote ili kumuonesha Hans naye ana watu wanaompenda kwa dhati kuliko yeye aliye upasua moyo wake kwa kisu butu bila ganzi.
Wakiwa katika Mgahawa wa Samakisaki Mlimani City walipokutana Mage na shoga yake kipenzi Brenda kwa ajili ya kula raha. Wakiwa wanakula piza na juisi, baada ya kutafuna kipande cha piza na kusukumia na juisi ya embe, alisema:
“Brenda yaani sijui siku ya harusi yangu itakuwaje?”
“Mage, litakuwa bonge la harusi ambalo halijawahi kutokea jijini. Mama yako alivyopania, sijui!”
“Yaani, baada ya ndoa wakati tupo honey moon nitazisambaza picha za harusi mitandao yote ili kuwakonga wavimba macho walionicheka baada ya Hans kuoa.”
“Najua Hans ataumia sana,”Brenda alisema huku akikata kipande cha piza.
“Aumie nini wakati amefurahia, lakini Mungu yupo, kisasi changu kwake hakijaisha ningekuwa na uwezo ningemmwagia tindi kali,” Mage alisema huku akikunja uso kwa hasira.
“Magee! Tindi kali ya nini ikiwa tayari umepata mtu mwenye mapezi ya kweli?”
“Brenda hujui tu jinsi nilivyoumia kwa kitendo cha Hans kunihalibia ndoto zangu za maisha.”
“Mage bado unampenda Hans!”
“Aah, wapi!”Mage aliruka kimanga.
“Muongo unampenda na akitokea leo haki ya nani ndoa hakuna,” Brenda alimwambia shoga yake akiwa amemkazia macho.
“Haitatokea hata siku moja, labda jua litoke Magharibi kwenda Mashariki.”
“Unajikomba tu, lakini upo na Colin kama bodi lakini injini ni Hans.”
“Mawazo yako, kwanza tuachane na mambo ya Hans tuzungumzia harusi yangu.”
“Kama kweli umedhamilia kuolewa na Colin basi litakuwa bonge la harusi.”
Wakiwa katika ya mazungumzo simu Brenda iliita, alipoangalia alikuta namba ngeni alipokea.
“Haloo.”
“Haloo Brenda.”
“Abee, nani mwenzangu?”
“Yaani nawe umenichukia kama shoga yako, Brenda nimekukosea nini?”
Sauti ile ilimshtua na kugundua anazungumza na Hans.
“Jamani shemu mambo mengi si unajua mitihani ilitukamata.”
“Pamoja na mitihani, lakini umenitenga shemeji yangu!”
“Siwezi kukutenga.”
“Naomba msaada wa kunikutanisha na Mage, kuna tetesi zimeniumiza moyo wangu. Usishangae wakati wowote ukisikia kifo changu.”
“Brenda unazungumza na nani?” Mage aliingilia kati mazungumzo kwa kusimama na kusogea kwa Brenda.
“Mage hebu subiri,”Brenda alimtuliza Mage na kuendelea kuzungumza.
“ Kipi tena kitasababisha kifo chako, unaumwa?”
“Heri ningeumwa kuliko ukatili anaonifanyia shoga yako. Anajua mimi na yeye tumetoka wapi na tuliahidiana nini. Kweli Mage unakubali kuolewa na mwanaume mwingine tofauti na mimi?” Hans alisema kwa sauti ya huzuni.
“Hans utakuwa unakosea kusema hivyo, wewe ndiye uliyesababisha yote. Ulikuwa ukifahamu Mage alikuwa akikupenda kiasi gani na unajua nini kilimpata baada ya wewe kufunga ndoa.”
“Najua, lakini nilimweleza kila kitu.”
“Mbona ulikwenda kinyume?”
“Nilikuwa na sababu yangu ambayo Mage alitakiwa kunisikiliza na kuelewa sababu ya mimi kufanya vile wala asingefikia huko.”
“Hans usimlaumu Mage kwa vile naye kafanya kama wewe.”
“Kivipi?”
“Mume katafutiwa na mama yake.”
“Duh! Haijawahi kutokea.”
“Basi imetokea.”
“Basi naomba anipe nafasi ya kuzungumza naye kwa dakika chache.”
“Sidhani kama anaweza kupata nafasi kwa muda huu wa maandalizi ya harusi.”
“Najua, ila nilikuwa nataka kuzungumza naye hata dakika kumi kabla ya ndoa yake.”
“Hans, hiki si kipindi cha kuzungumza chochote na Mage, unaweza kuivuruga ndoa yake.”
“Siwezi, nataka tu nizungumze naye ili akiolewa ajue mimi si adui yake.”
“Mmh! Nitafikisha ujumbe.”
“Naomba shemeji yangu unikutanishe na Mage nitakupa zawadi yoyote unayotaka.”
“Sawa shemu.”
“Nashukuru kwa kunisikiliza pia wewe ni daraja muhimu kati yangu na Mage.”
“Nimekuelewa.”
Brenda alikata simu na kumgeukia shoga yake aliyekuwa na kumuhemuhe cha kutaka kujua Hans alikuwa akisemaje.
“Vipi mzushi alikuwa akisemaje?”
Brenda alimweleza mazungumzo yote waliyozungumza na Hans.
“Mmh! Anataka kuniambia nini?”
“Sijui, ninyi ndiyo unajua mlizungumza nini katika ahadi ya penzi lenu.”
“Uhuu!” Mage alishusha pumzi na kusema:
“Brenda unanishauri nini?”Mage alionekana kama ametahayari kusikia taarifa za Hans.
“Kwa vile upo katika hatua nzuri ya harusi, huu si muda wa kuzungumza na Hans unaweza kuharibu kila kitu ukakosa bara na pwani,” Brenda alimtaadhalisha rafiki yake.
“Eti eeh, sijui Hans anataka kuniambia nini?”
“Achana naye.”
“Mmh! Sawa.”
Kwa vile muda uliokuwa umekwenda sana, kila mmoja aliingia kwenye gari lake kurudi nyumbani.
***
Brenda alipofika nyumbani kwao alikwenda kuoga na kupata chakula kisha alijifungia chumbani kwake na kuwasha Ipad yake na kuanza kuchati na marafiki zake kwenye Twiter na Skype.
Akiwa anaendelea kuchati simu yake iliita, namba ilikuwa ngeni aliipokea.
“Haloo.”
“Haloo Brenda.”
“Abee, nani?”
“Brenda unaniuliza nani wakati tumetoka kuzungumza muda si mrefu.”
“Hans?” Brenda aliuliza.
“Ndiyo.”
“Unasemaje?”
“Brenda samahani sana.”
“Bila samahani.”
“Naomba unikutanishe leo na Mage.”
“Hans, si tumeisha ongea?”
“Hapana Brenda, kuna kitu cha muhimu sana nataka nizungumza naye kabla siku ya kesho.”
“Samahani Hans, nipo Bagamoyo sitarudi leo.”
“Naomba hata umpigie simu ili anisikilize hata kwa sekunde tano tu.”
“Hans kwanza samahani, hapa nipo na boy friend yangu, ana wivu sana naomba tuzungumze kesho,” Brenda alidanganya.
“Samahani, ila utakacho kisikia kesho usishangae najua Mage atafurahi.”
“Unataka kufanya nini Hans?”
“Nilitakiwa kumweleza Mage mwenyewe, kwa heri.”
Hans alikata simu na kumfanya Brenda abakie na simu mkononi kama anatazama kitu cha kumshangaza, alijikuta akijuliza.
“Hans anataka kufanya nini? Au anataka kujiua? Mmh! Ngoja nimweleze Mage maana sasa imekuwa kazi. Lakini kipi cha ajabu Mage akiolewa? Kwani alitaka akae vile mpaka lini? Hivi Hans anashida na Mage au anataka kumvuruga maisha tu?”
Brenda alijikuta akiwaza peke yake, wakati huo simu aliyopiga ilikuwa ikiita. Ilipokelewa upande wa pili.
“Haloo shoga lete stori,” Mage alipokea.
“Mmh! Mtu wako ananisumbua sana.”
“Nani?”
“Hans.”
“Kakupigia tena?” Mage alishtuka.
“Ndiyo.”
“Brenda achana naye, kwa nini unamsikiliza?”
“Mage siwezi kumkatia simu kwa vile sina ugomvi naye.”
“Yaani hivi najiandaa kwenda kwa Colin, tulikuwa tunachati tukaona haitoshi, tukaongea vilevile tukaona haitoshi, nimeamua kwenda kabisa kuonana uso kwa macho.”
“Duh!”
“Brenda, nimeamini Colin ananipenda sana.”
“Sasa ndiyo utulie.”
“Brenda, lazima nitulie Colin kaniahidi vitu vingi sana baada ya ndoa nina imani ndoto zangu nilizoziota kwa Hans zitakuwa mara kumi.”
“Basi ndiyo hiyo mtu wako wa roho ya Mungu anatapatapa kama mfa maji.”
“Kwani alikuwa akisemaje?”
Brenda alimweleza yote aliyoelezwa na Hans na alivyomdanganya, Mage baada ya kumsikiliza alishusha pumzi na kusema:
“Kwani Hans anataka kuniambia nini?” Mage aliuliza.
“Akwambie nini! Yule muharibifu, huu si muda wa kumsikiliza, ukirogwa kumsikiliza tu ndoa huna.”
“Mmh! Nimekuelewa japo moyo unatamani kumsikiliza ili nijue anataka kusema nini?”
“La kusema hakosi, anaweza kukuvuruga akili na ndoa yako ukaiona chungu. Najua bado unampenda sana Hans, kama utampa nafasi narudia tena ndoa hakuna,” Brenda alimtaadhalisha Mage.
“Hata siku moja, labda siyo Mage mimi, siwezi kuumizwa mara ya tatu mbili zinatosha.”
“Basi ndiyo hivyo kuwa makini na Hans, kwa nini muda wote akae kimya, kusikia unataka kuolewa ndiyo ajifanye anakupenda sana.”
“Nimekuelewa basi wacha niwahi kwa mahabuba wangu.”
“Mambo si hayo.”
Brenda alikata simu na kuendelea kuchati na mashoga zake.
***
Sauti ya simu kuita ilimshtua Brenda aliyekuwa bado amelala, alipoangalia ilikuwa namba ngeni, aliipokea.
“Haloo.”
“Haloo, nazungumza na Brenda?”
“Ndiyo, nani mwenzangu?”
“Naitwa Ndubi rafiki mkubwa wa Hans.”
“Ndiyo Ndubi.”
“Kuna habari siyo nzuri.”
“Habari gani?”
“Hans amepata matatizo makubwa sana, nilijaribu kumpigia Mage simu yake haipatikani nikaona nikupigie wewe ili umjulishe.”
“Mmh! Matatizo gani?”
“Jana usiku wamevamiwa nyumbani kwake na majambazi, mkewe na mwanaye wameuawa na yeye hatujui kama yupo hai.”
“Mungu wangu! Yupo wapi kwa sasa?”
“Yupo hospitali ya muhimbili chumba cha wagonjwa mahututi.”
“Mungu wangu! Ngoja nimjulishe Mage.”
“Itakuwa vizuri.”
Baada ya simu kukatwa Brenda alimpigia simu Mage aliyekuwa bado yupo kwa mchumba wake Colin. Baada ya simu kuita kwa muda ilipokelewa upande wa pili.
“Haloo Brenda mbona unaharibu pozi za watu,” Mage alisema kwa utani.
Brenda hakupoteza muda alimweleza taarifa aliyopokea asubuhi ile, taarifa ile ilimshtua sana Mage.
“Mungu wangu! Yupo wapi?”
“Mihimbili.”
“Nakuja sasa hivi twende.”
“Noo, tutakutana hospitali.”
Mage alinyanyuka kitandani na kupitia nguo zake na kuvaa bila kuoga, hakutaka kumwamsha Colin aliyekuwa bado amepitiwa usingizi. Alitoka hadi kwenye gari lake na kuondoka kuelekea muhimbili kumuona Hans. Njia nzima alijilaumu kukataa kusikiliza wito wa Hans kwa kuamini kuna kitu cha muhimu alitaka kumweleza.
Alijiuliza Hans alitaka kumweleza nini na kwa nini alilazimisha waonane usiku wa jana yake kisha asubuhi asikie habari kama zile za kushtusha.
“Mungu wangu kama Hans atakuwa amekufa atakufa na kinyongo, sikutakiwa kuwa katili kiasi kile. Japokuwa sikuwa tayari kurudiana naye lakini nilitakiwa kumsikiliza.”
Mage alikuwa kwenye lindi la mawazo juu ya Hans kuwa katika hali ile. Alijikuta akitokwa na machozi kumlilia. Alijiuliza kama ndiye yeye angekuwa mke wa Hans na tukio lile likatokea ina maana angekufa yeye.
Kutokana na mawazo mengi alijikuta akiendesha gari pasipo umakini, alifunga breki mbele ya gari lililosimama baada taa nyekundu kuwaka za makutano ya barabara ya Oceon na Upanga. Alikanyaka breki kwa nguvu zote huku akifumba macho na kuuma meno. Gari lilisota na kwenda kujigonga kidogo kwenye Land Cruser la Mwarabu.
Kelele za breki zilifanya watu wote kugeuka kuangalia, askari wa barabarani alifika lakini Mwarabu hakutaka kesi kwa vile gari lake halikuharibika sehemu yoyote. Aliliruhusu na kumfuata Mage kumuuliza:
“Vipi mbona hivyo?”
Mage alishindwa kumjibu kwa vile presha ilikuwa juu na uso ulikuwa umejaa machozi. Askari hakutaka kumuhoji kitu alimruhusu kuondoka. Mage aliondoa gari kuingia barabara ya Upanga kuelekea Muhimbili kumuona Hans.
Njia nzima Mage alikuwa akilia, alikumbuka maisha aliyoishi na Hans, mwanaume akiyempenda kuliko kitu chochote chini ya jua. Waliishi maisha ya mapenzi kama njiwa, kila mmoja alimpenda mwenzake penzi la glasi halikuwa na kificho kila mmoja aliamini anapendwa na mwenzake.
Alikumbuka ahadi ya Hans alipomwambia kumuacha yeye ni sawa na roho kuachana na mwili. Alimuhakikisha yeye ndiye mwanamke wa maisha yake. Baada ya Hans kuozwa kwa shinikizo la wazazi, walikubaliana avumilie ili baadaye amuache mwanamke wa kulazimishwa ikiwa pamoja na kuitozaa naye.
Lakini Hans alionekana kugeuka pale alipopata mtoto ndani ya ndoa yake tofauti na walivyokubaliana kutozaa na yule mwanamke na kwenda kinyume na kumfanya naye akubali kuolewa na Colin.
Alijiuliza nani aliyefanya kitendo kile, alijikuta akitengeneza mawazo ya kijiunga kuwaza labda mpango ule kaufanya Colin kutokana na wasiwasi wa kurudiana na Hans.
“Nikigundua Colin kama ndiye aliyemuua mpenzi wangu, nitamchukia mpaka kufa na nitakuwa shahidi namba moja kuhakikisha na yeye ananyongwa,” Mage aliwaza.
Alipofika Muhumbili alisimamisha gari na kuelekea kwenye wadi ya wagonjwa mahututi. Nje ya wadi aliikuta familia ya Hans, hakuna aliyemjali japokuwa alionekana amevimba macho kutokana kumlilia Hans.
Alipojaribu kuingia wadini alikatazwa na kuamua kusimama pembeni peke yake, baada ya muda shoga yake Brenda alifika na kwenda aliposimama.
“Vipi shoga?”
“Yaani mama Hans kanifukuza kama mbwa!”
“Kwa nini?”
“Hata sijui wakati anafahamu mimi na mwanaye tulikuwa vipi.”
“Kwa hiyo hujui hali ya Hans?”
“Sijui chochote.”
Mara simu ya Mage iliita alipoangalia ilikuwa ikitoka kwa Colin, aliitazama na kukunja uso bila kuipokea. Brenda aliyekuwa akimtazama usoni alimuuliza.
“Simu ya nani?”
“Achana nayo,” alijibu kwa mkato.
“Mmh!”
Baada ya muda simu iliita tena, Brenda alishtuka kuona jina la Colin bila kupokelewa.
“Shoga mbona hupokei?”
“Achana naye.”
“Ha! Wewe si ulikuwa kwa Colin na umeondokaje?”
“Sijamuaga nimemuchana bado amelala.”
“Unajua unacho kifanya unaiweka ndoa yako njia panda.”
“Kwani asiponioa nitapungukiwa nini?” Mage alijibu huku akibinua midomo.
“Mage, usipoteze muda wa Colin, kuamini unampenda kumbe upo naye kivuli tu.”
“Brenda mwenye uamuzi wa kumpenda nani ninao mimi.”
“Kwa hiyo Colin si chaguo lako?”
“Brenda huu si wakati wa kuzungumzia Colin zaidi ya kujua hali ya Hans ndiye aliyetuleta hapa.”
“Mmh! Sawa.”

ITAENDELEA
 
SEHEMU: 09
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500..

ILIPOISHIA:
“Brenda mwenye uamuzi wa kumpenda nani ninao mimi.”
“Kwa hiyo Colin si chaguo lako?”
“Brenda huu si wakati wa kuzungumzia Colin zaidi ya kujua hali ya Hans ndiye aliyetuleta hapa.”
“Mmh! Sawa.”
SASA ENDELEA...
***
Colin baada ya kushtuka usingizini alijua mpenzi wake yupo msalani au bafuni, lakini muda ulikatika bila kuonekana. Alikwenda msalani kumtafuta huku akimwita bila kupata jibu. Alitoka hadi nje na kumuuliza mlinzi.
“John umemuona shemeji yako?”
“Ametoka asubuhi sana, hakukuaga?”
“Ameniacha nimelala.”
“Tena alionekana kama analia nilijua mmegombana.”
“Hata sielewi kitu.”
Colin alimpigia simu mchumba wake, lakini iliita bila kupokelewa. Alirudia zaidi ya mara tatu vilevile haikupokelewa. Alijiuliza Mage amepatwa na nini, wasiwasi wake labda kwao kumetokea tatizo. Aliingia ndani na kuvaa pensi na fulana chini alivaa ndala na kuingia kwenye gari kuelekea Kigamboni kwa kina Mage ili ajue amepatwa na nini.
Alikimbiliza gari, kutokana na foleni aliamua gari lake kulipaki Posta ya zamani na kuchukua bodaboda ili awahi kuifika. Baada ya kuvuka alichukua nyingine iliyo mpeleka nyumbani kwao Mage.
Alimlipa dereva na kuingia ndani ya geti, alipofika sebuleni alimkuta msichana wa kazi akifanya usafi.
“Habari Sofi?”
“Nzuri shemu, shikamoo.”
“Marahaba, vipi Mage yupo?”
“Sijamuona toka asubuhi.”
“Mama.”
“Yupo chumbani kwake.”
“Kaniitie.”
Colin alibakia sebuleni kumsubiri mama Mage, baada ya muda alitokea na kushangaa kumuona Colin katika hali ile.
“Vipi baba, kwema?”
“Kwema, sijui hapa.”
“Hapa hatujambo, mwenzio yupo wapi?”mama Mage alimuulizia mwanaye baada ya kumuona Colin peke yake.
“Nimeshtuka kitandani sikumkuta, nimempigia simu haipokelewi, nikawa na wasiwasi na kuamua kuja huku.”
“Hapa sijamuona, atakuwa amekwenda wapi? Mmh! Basi atakuwa kwa Brenda tu.”
Colin alipiga simu kwa mara nyingine lakini haikupokelewa, alirudia mara mbili vilevile haikupokelewa baadaye ikazimwa kabisa.
“Mama simu haipokelewi niliporudia imezimwa kabisa.”
“Mmh! Atakuwa wapi mtoto huyu la..”
Mama yake alinyamaza baada ya kumuona mwanaye akiingia, wote walipeleka macho kwake. Walishtuka kumuona macho yake yamevimba kuonesha alikuwa akilia.
Aliwapita bila kuwasemesha na kuelekea chumbani kwake kitu kilichomshtua mama Mage na kumuuliza Colin.
“Colin umemfanya nini mwanangu?”
“Mama sijamfanya kitu, si umuulize mbele yangu.”
Mama Mage alimfuata mwanaye chumbani na kumkuta amejilaza kwa kulilia tumbo.
“Mage.”
“Abee.”
“Kuna nini?”
“Hans ana hali mbaya asishangae kusikia amefariki.”
“Amefanya nini?”
“Amevamiwa na majambazi, mke wake na mwanaye wameuawa.”
“Mungu wangu! Ndipo unapotoka?”
“Ndiyo, mama.”
“Mbona hukumuaga mwenzio?”
“Ningemuaga nakwenda wapi?”
“Na mbona umempita bila kumsalimia.”
“Nitamweleza nini?”
“Kwa hiyo itakuwaje?”
“Mwambie aondoke siwezi kuzungumza naye chochote kwa sasa.”
“Magee, unajua Colin ni nani yako?”
“Mchumba wangu na mume wangu mtalajiwa, lakini kwa leo naomba aniache nitamtafuta mwenyewe.”
“Mage, unajua unanitafutia lawama, Colin atatuelewa kweli?”
“Mama tumia kila uwezavyo ili Colin aondoke nitamtafuta.”
“Unanitia kwenye ubaya, Mage unaibomoa ndoa yako kwa mikono yako, unapoteza uaminifu kabla ya ndoa.”
“Mama ndoa ni zawadi toka kwa Mungu, kama si riziki yangu siwezi kuilazimisha.”
“Mmh! Sawa wacha nikajaribu,” mama Mage alitoka chumbani na kumwacha mwanaye amejilaza huku akiwa na mtihani wa kumweleza Colin ili aondoke bila kuhoji kitu.
Colin alibakia sebuleni akiwaza kipi kimempata mchumba, alijiuliza alikwenda wapi asubuhi ile mchumba wake kama hakurudi nyumbani na kwa nini ameonekana analia kipi kimemsibu. Alibakia kusubiri kwa hamu kujua kipi kimemsibu mchumba wake, ambaye aliamini ndiye moyo wake yeye alibakia na mwili tu.
Mama Mage alirudi hadi sebuleni, Colin aliyekuwa ametazama juu akiwa mwingi wa mawazo kutokana na kilichotokea asubuhi ile. Aliposikia sauti ya miguu ikisogea alipokuwa amekaa aliyahamisha macho yake na kumuona mama Mage, alijikuta akinyanyuka kama anampokea mheshimiwa.
“ Vipi mama?”
“Mmh! Safi tu,” Mama Mage alijibu huku akijitahidi kutengeneza uso wa mbuzi ili aweze kutengeneza mambo hasa kutokana kuwa mzazi.
“Vipi Mage alikuwa wapi na amepatwa na nini?” Colin aliuliza akiwa amemkazia macho.
“Mmh! Si..si..au fanya hivi, baba wewe nenda nyumbani mpenzi wako kuna mambo yao ya kitoto si unajua baba mwenzio bado mdogo?”
“Ndiyo najua, lakini amepatwa na nini na alikwenda wapi bila kuniaga ikiwa hawa wewe hujui?”
“Mwanangu, wala hakuna jambo la kutisha, u..u..najua mwenzio, baba eeh, hebu kwanza hili tuliache jioni mwenyewe atakueleza kila kitu,” mama Mage alijitahidi kubadili mazungumzo.
“Sawa mama, lakini Mage ni mchumba wangu ninatakiwa kujua kila kitu chake, sasa hivi ni mke wangu, tumetenganishwa na ndoa tu ambayo haipo mbali. Hivi nirudi nyumbani namweleza mama nilichokikuta hapa kisha naulizwa kimetokana na nini nitajibu nini?” Colin alitetea hoja yake.
“Mwanangu ngoja nikutoe wasiwasi, mwenzio alikwenda kwa shoga yake sijui nini anamdai, basi wametibuana ndiyo maana yupo vile,” mama alitengeneza uongo.
“Sasa mama kama ni hivyo kwa nini hataki kuzungumza na mimi?”
“Colin mwanangu, mi mkubwa naomba uondoke ili jioni uzungumze vizuri na mwenzako. Atakachokuambia hata wewe utacheka.”
“Mmh! Sawa, basi mi’ naondoka.”
Colin alisema huku akinyanyuka kuelekea nje, alipofika nje alikodi bodaboda hadi Kivukoni ambako alivuka upande wa pili na kukodi bodaboda nyingine hadi kwenye gari lake na kuingia ndani.
Kabla ya kuondoka alitulia mikono aliweka juu usukani na macho aliangalia mbele, alikuwa kama anaona lakini alizama kwenye mawazo na kujiuliza Mage alikwenda wapi bila kuaga na kwa nini amerudi akilia kipi kimempata alipokwenda na mwisho alijiuliza kwa nini amekataa kuzungumza naye.
Baada ya kukosa majibu ya maswali yake aliondoa gari kuelekea nyumbani, alitembea mwendo wa kawaida huku akili yake ikiwa haijakaa sawa. Alipofika katika makutano ya barabara ya Kawawa na Morogoro macho yake yalishtuka kumuona msichana mmoja akiuza ndizi.
Sura yake haikuwa ngeni machoni mwake lakini mavazi yalifanya macho yapingane na akili yake. Sura ilikuwa ya Cecy lakini mavazi yake yalikuwa machakavu na mwili ulimvaa vumbi kwa ajili ya kutembea barabarani kwa miguu kuuza ndizi. Kwa vile alikuwa kwenye foleni alituliza macho yake kwa binti yule ambayo yalimwambia ni Cecy.
Wakati anataka kuondoa gari alisikia mtu akimwita.
“Cecy leta ndizi mbili.”
Kwa vile taa ziliruhusu aliliondoa gari na kwenda kulipaki kituo cha mafuta cha Magomeni, alilizima na kutoka nje, kwa vile Cecy alikuwa amevuka barabara kwenda kuuza ndizi maeneo ya Hospitali. Alimtuma kijana mmoja aliyekuwa akiuza miwa.
“Samahani mkubwa, naomba kwamwambia yule msichana alete ndizi kumi.”
Yule kijana alimfuata Cecy aliyekuwa ametua beseni lake chini akiuza ndizi, alipofika alimwambia.
“Dada peleka ndizi kumi kwenye lile gari.”
“Kumi hazitafika zitabaki sita.”
“Mpelekee zote.”
“Sawa, ngoja nichukue hela.”
Baada ya kuuza alibeba beseni lake na kuvuka barabara mpaka kwenye gari, kioo cha gari kilikuwa kimepandishwa kidogo hivyo hakumuona aliyekuwa kwenye gari. Aligonga kioo kidogo ili auze ndizi.
“Kaka.”
Colin aliteremsha kioo na kufanya Cecy amuone vizuri kitu kilichomfanya ashtuke.
“Ha! Colin?” mshtuko alioupata ulifanya adondoshe beseni la ndizi.
Hakuliokota alibakia amesimama mpaka Colin alipoteremka kwenye gari na kuokota ndizi zote kisha alimshika mkono Cecy.
“Cecy.”
“Abee,” Cecy aliitikia huku machozi yakimtoka na mwili kumtetemeka.
“Unalia nini mchumba?”
“Colin mimi si mchumba wako, mchumba wako Mage,” Cecy alijibu kwa ukali kidogo.
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Mama yako amechotufanya kwa ajili yako, Colin lini nilikutamkia nakupenda?”
“Hujawahi hata siku moja.”
“Kwa nini mama yako amefunga safari ya kuja kunituka kuwa naingilia ndoa yako na kutudhalilisha kwa ajili ya umaskini wetu. Colin maskini hapendi?”
“Anapenda.”
“Ni kweli Colin nakupenda zaidi ya kukupenda, nailaumu nafsi yangu kuchelewa kukueleza ukweli kuwa nakupenda. Najua haikuwa bahati yangu unayetaka kumuoa ndiye chaguo la moyo wako. Kipi kilichomtuma mama yako kuja kunitukana na kutudhalilisha bahati yake sikumkuta najua ningemfanya nini!” Cecy alisema kwa sauti ya hasira.
“Lini?”
Cecy alimtajia siku na kukumbuka siku ambayo Colin alikumbuka ndiyo siku aliyokamata picha kumbe alikwenda kumtukana Cecy bila kutaka kuujua ukweli.
“Cecy samahani sana, pia pole kwa kushindwa kuujua upendo wako.”
Alimweleza ukweli juu ya uchumba wake na Mage alivyotengenezwa na mama yake.
“Kwa hiyo Mage si chaguo lako ni la mama yako?”
“Hapana, mwanzo lilikuwa chaguo la mama baada ya kumuona nilikubaliana naye na ndiyo tulipanga kuoana.”
“Kwa hiyo siku ile uliniita kuja kunidhalilisha na kuumiza moyo wangu?”
“Hapana nilikualika kama wageni wengine, pia nina mpango mkubwa sana kwako ambao utakusaidia kimaisha.”
“Colin mpango ambao naukubali kwako labda niwe mkeo lakini zaidi ya hapo usijisumbue,” Cecy alisema kwa sauti ya kike kwa kujiamini.
Colin alijitahidi kumwelewesha sababu ya picha zake na kipi alichokipanga juu yake.
“Hivi leo hii nifanye kazi kwenye kampuni yetu mama yako atakubali anajua sisi ni wapenzi, kuna kazi?”
“Kwanza hebu nieleze sababu ya wewe kuwa kwenye hali hii?” Colin alimuuliza huku akiangalia mavazi na hali aliyokuwa nayo Cecy.
“Sina thamani haya ndiyo maisha niliyoyachagua ili mama yako akiniona asiwe na wasiwasi na ndoa yako.”
“Cecy nitakutafuta tuzungumze akili yako ikitulia.”
“Usijisumbue.”
“Lazima nijisumbue kwako kwa vile kuna kitu ndani yako nilichokiona.”
“Colin niache nirudi nyumbani.”
“Unakaa wapi nikupeleke.”
“Colin unataka mama yako aje kuchoka pagala letu, aliona picha ikawa vile vipi anione kwenye gari lako?”
“Hawezi, na ungeniambia alichokifanya ningempa ukweli, tabu ya kina mama wa kiswahili wazungu hawajali vitu vya kijingakijinga.”
“We nenda tu.”

Itaendelea
 
SEHEMU: 10
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500..

ILIPOISHIA:
“Cecy nitakutafuta tuzungumze akili yako ikitulia.”
“Usijisumbue.”
“Lazima nijisumbue kwako kwa vile kuna kitu ndani yako nilichokiona.”
“Colin niache nirudi nyumbani.”
“Unakaa wapi nikupeleke.”
“Colin unataka mama yako aje kuchoka pagala letu, aliona picha ikawa vile vipi anione kwenye gari lako?”
“Hawezi, na ungeniambia alichokifanya ningempa ukweli, tabu ya kina mama wa kiswahili wazungu hawajali vitu vya kijingakijinga.”
“We nenda tu.”
SASA ENDELEA...

Colin alimbembeleza sana Cecy, kwa vile naye alikuwa akimpenda akiingia kwenye gari na kurudishwa nyumbani kwao. Walipomfikisha Colin naye aliteremka na kuongozana hadi kwa kina Cecy ambako kulikuwa na nyumba ya vyumba viwili na sebule. Lakini nyumba ilikuwa ya hali ya chini bati zake zilikuwa na kutu na juu waliweka mawe ili kuzuia bati lisiezuliwe na upepo.
Cecy baada ya kufika eneo la kwao alishukuru na kuanza kuelekea nyumbani, lakini Colin alimsemesha.
“Cecy mbona unaniacha mgeni?”
“Colin nashukuru umenileta, lakini naomba usifike nyumbani.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Nimekueleza mara ngapi kuhusu mama yangu, unataka mama yako aje akitie moto kibanda chetu.”
“Cecy suala la kuhusu mama yangu niachenie mimi, naomba nimsalimie mama mara moja.”
“Mmh! Sawa.”
Waliongozana Cecy na Colin hadi nyumbani kwao ambako alitambulishwa kwa mama yake na kumfanya mama Cecy ashtuke.
“Ha! Wewe ndiye unayenyanyasa mwanangu?”
“Kumnyanyasa kivipi mama?”
Mama Cecy alimweleza mateso yote ya mwanaye juu yake na jinsi mama yake alivyokwenda kuwatukana huku akitishia maisha ya Cecy kama ataharibu ndoa yake na Mage. Colin baada ya kusikilia maneno yale aliyarudia maneno ya Cecy juu ya mapenzi yake kwake.
Ashangaa kuona penzi la Cecy kwake lilikuwa wazi kwa mama yake lakini mhusika mkuu alikuwa hajui kitu zaidi ya kumuona Cecy kama msichana mzuri lakini hakuwa na uwezo wa kumtamkia chochote kutokana na mama yake kumtafutia mwanamke aoe ambaye kwa upande wake aliungana na uchaguzi wa mama yake.
“Mzazi wangu, kwanza niwaombeni radhi kwa yote yaliyotokea kwa mama yangu kuja kuwatukana bila sababu. Naweza kusema labda makosa nimefanya mimi kwa kutomjulisha nini nilichotaka kukifanya na Cecy.
“Najua mama yangu alimpenda Cecy lakini si kuwa mke wa mwanaye bali msichana mzuri anayejiheshimu. Inawezekana kigezo cha elimu ndicho kilichomfanya mama yangu amtafute Mage, nina imani kama Cecy angekuwa na elimu kama ya Mage basi angekuwa chaguo la kwanza la mama.
“ Wasiwasi mkubwa wa mama ilianzia siku alipomuona Cecy kapendeza naweza kusema aliwashinda wote waliokuwa kwenye sherehe yangu. Kilichomshtua mama yangu kunikuta na picha ya Cecy aliyokuwa amependeza sana. Aliamini kabisa ni mpenzi wangu hivyo kujihami kabla mambo hayajaharibika kutokana na harusi yetu kuandaliwa kwa fedha nyingi sana.
“Lakini hakutakiwa kuchukua uamuzi aliochukua bila kuniuliza mimi japokuwa nilimweleza sababu ya kuwa na picha ile. Ila napenda kuwaeleza kitu kimoja kuwa sitauacha upendo wa Cecy upitee hivihivi najitolea kumsomesha ili aongeze elimu na ujuzi.
Baada ya elimu hiyo nitafanya naye kazi ndani na nje ya nchi ambayo naamini itamweka katika maisha mazuri na ramani ya dunia. Pia nitahakikisha naijenga nyumba yenu katika hadhi ya kisasa pia mama nitakufungulia mradi ili muendeshe maisha yenu,” Colin alieleza nia yake nzuri kwa Cecy na mama yake.
“Asante bab..”
“Mama nani kamwambia sisi tuna shida ya vitu hivyo? Kama kilichonitesa nimekikosa, sihitaji kitu kingine toka kwako,” Cecy alimkatisha mama yake na kumjia juu Colin kwa kauli yake.
“Cecy mimi na wewe nani mwenye kosa, ulilolisema leo ungelisema mapema situngefika huku,” Colin alijitetea.
“Muongo! Colin hata ningesema ingekuwa sawa na kazi bure kwa vile tayari mama yako aliisha kuchagulia mwanamke,” Cecy alisema kwa hisia kali.
“Kabla ya kutoa uamuzi ningechagua.”
“Mimi na Mage unampenda nani?”
“Nawapenda wote, ila kwa sasa Mage kwa vile ndiye tupo katika mipango ya ndoa.”
“Kwa kauli hiyo naomba tukomane kila mtu ashike hamsini zake ukinikuta njiani nipite kama nguzo ya umeme,” Cecy alisema kwa hasira.
“Cecy kuwa na adabu, heshimu anachokisema mwenzako...Baba kama una nia hiyo ifanye faida hataiona leo, lakini baadaye atakushukuru.”
“Sawa mama nimekuelewa, Cecy punguza hasira nina nia nzuri na wewe, uzuri wako nitaulinda na baadaye utakuingia fedha nyingi na kumsaidia mama. Utauza ndizi mpaka lini?”
Cecy hakujibu kitu aliinama chini, Colin alimsogelea na kumbembeleza kitu kilichomfanya Cecy aangue kilio na kusema:
“Colin nisamehe kwa yote, hujui kiasi gani penzi lako lilivyouathiri moyo wangu, najua nilikupenda bila kushauriana na moyo wangu. Mnaweza kuniona mdogo lakini nami nina hisia za mapenzi kama wengine,” Cecy alisema huku akimtazama Colin kwa macho yaliyojaa machozi.
“Najua Cecy, isingekuwa mipango ya harusi ningeza kufanya chochote ili ujue nauthamini upendo wako.”
“Sawa Colin nimekuelewa.”
Kwa vile muda ulikuwa umekwenda Colin aliaga kuwahi nyumbani baada ya kuondoka bila kuaga. Alikwenda kwenye gari na kuwaletea laki moja, walimshukuru naye aliondoka kuelekea nyumbani. Njiani alijikuta akimuwaza Cecy msichana mdogo lakini alikuwa jasiri kuzielezea hisia zake japo aliamini mama yake asingemkubali kutokana na uduni wa maisha na kukosa elimu.
Kwa upande mwingine aliamini kabisa kutokana na kasi ya mabadiliko duniani Mage ndiye mwanamke sahihi kwake. Kwani aliamini maisha ni zaidi ya mapenzi kwa vile maisha yakiwa vizuri kila kitu kinakwenda. Aliamini kwa umbile adimu la Cecy angeweza kuifanya kazi yake vizuri ya maonesho ya mavazi.
Kitu kikubwa aliamini Cecy kama atapata twisheni ya kingereza ataweza kuongeza uwezo wake hata kusafiri nchi za nje kufanya kazi ya maonesho ya mavazi pia kupata tenda ya kupamba majarida. Aliamini akimtumia vizuri Cecy kampuni yake itafika mbali na yeye kujitengezea kipato kikubwa.
Alipanga kuwekeza fedha nyingi kwa Cecy baadaye angevuna fedha nyingi kwa kuamini alikuwa na kitu cha ziada ambacho wasichana wengi hawakuwa nacho. Japokuwa alikuwa na wasiwasi na kikwazo cha mama yake, lakini kwa vile yupo kikazi alijua mama yake angemuelewa tu.
Alipanga ndani ya wiki mbili nyumba ya kisasa ya kina Cecy iwe imesimama huku akimtafutia twisheni nzuri ili kuijua lugha haraka. Alipanga kufungua duka mbele ya nyumba yao ambalo litawafanya waingize kipato kila siku. Kutokana na kuzama kwenye mawazo ya kumuwaza Cecy alijikuta akimsahau Mage mpaka alipofika kwao.
***
Alipoingia ndani alikutana na mama yake ambaye alishangaa kumuona mwanaye akiteremka kwenye gari.
“Colin unatoka wapi?”
Colin ilibidi amweleze mama yake kilichotokea, baada ya kumsikiliza alimuuliza:
“Colin mwanangu umemfanya nini mtoto wa watu?”
“Mama sijamfanya kitu chochote kama nilivyokueleza.”
“Mage si mjinga kulia tu na kukataa kuzungumza na wewe wakati mlikuwa pamoja?”
“Yaani sijui kitu labda uulize wewe utapata jibu.”
“Nitauliza, lakini Colin kuna kitu unanificha haiwezekani Mage aondoke bila kukuaga kisha akatae kuzungumza na wewe wakati usiku mmelala pamoja?”
“Mama piga simu uulize labda utagundua kitu.”
“Mmh! Sasa nimepata jibu,” mama Colin alisema huku akitikisa kichwa kama kakumbuka kitu.
“Jibu gani?”
“Colin lazima kuna kitu Mage amegundua kuhusu wewe na Cecy, nasema hivi ndoa ikivunjika Cecy atanitambua.”
“Mama unamuonea bure mtoto wa watu, toka siku ile ya sherehe sijaonana na Cecy,” Colin alidanganya.
“Muongo umemkataza asilete ndizi ili mkutane sehemu nyingine. Colin Mage akinieleza kuwa amegundua una uhusiano na msichana mwingine pagala lao nakwenda kulitia moto sasa hivi.”
“Mama kwa nini unanihukumu kwa kosa nisilofanya, nimekueleza piga simu uulize unaanza kutengeneza mawazo yako. Cecy amekukosea nini mpaka kumchukuia hivyo, ni wewe ndiye uliyekuwa naye karibu?”
Mama Colin hakusema kitu aliingia ndani kuchukua simu ili ampigie Mage kujua amepatwa na nini.
***
Baada ya Colin kuondoka mama Mage alimfuata mwanaye chumbani aliyekuwa amezama kwenye dimbwi la mawazo juu ya hali ya Hans na familia yake ilivyomtenga na kumuona kama kinyesi. Moyo ulimuuma na kujua hakukuwa na haja ya yeye kwenda hospitali pia kumuacha mchumba wake mumewe mtarajiwa akiwa amelala na kuondoka bila kumuaga.
Alijilaumu kwa kitendo chake cha kumpita Colin bila kumsemesha, alijiuliza atamfikiliaje. Alijiuliza ndoa yake ikivunjia na ijulikane sababu ya Hans mwanaume asiye na mapenzi naye ataiweka wapi sura yake. Lakini alijiuliza angesimama na kuzungumza na Colin angemwambia anatoka wapi na kwa nini hakumuaga?
Akiwa katika dimbwi la mawazo mama yake aliingia na kumkuta amezilaza chali huku ameukumbatia mto wake na wacho yake alikuwa akiangalia darini.
“Mage..Mage.”
“A..a..bee.”
“Mbona sikuelewi mwanangu?”
“Mama nahitaji msaada wako najua nimechanganya madawa.”
“Nikusaidie nini?”
“Sijui Colin atanielewaje maana nilichomfanyia si kitu kizuri.”
“Kwa kweli hatua tuliyofikia huku vikao vikienda vizuri halafu mwenzako abadili uamuzi sijui sura zetu tutaziweka wapi?”
“Hapo ndipo ninapochanganyikiwa, mama kitendo walionifanyia familia ya kina Hans sitawasahau.”
“Umeona eeh, nilikueleza toka zamani familia ile ilikuwa haikupendi kama ungeolewa na Hans ndoa yako isingedumu. Mungu amekuletea mwanaume wa maisha yako unamchanganya.”
“Mama nimeisha fanya kosa naomba msaada wako, nitamweleza nini Colin anielewe.”
“Wala usiwe na wasi kamwambie kuwa ulimtuma Brenda cheni ambayo ulipanga kumpatia kama surprise umekuta hajaitengeneza na kujikuta umekasirika na kuanza kulia.”
“Mmh! Atanielewa? Naona kama utetezi mwepesi.”
“Walaa, ye anajua ulikuwa kwa Brenda, nilimwambia kuna kitu mmeshindwa kuelewana ndiyo maana ulirudi katika hali ile.”
“Mmh! Basi ngoja nifanye hivyo.”
Wakiwa katikati ya mazungumzo simu ya iliita ilikuwa ikitoka kwa mama Colin.
“Mkweo,” mama Mage alisema.
“Mmh! Lazima ataulizia kilichotokea.”
“Ngoja nimsikilize,” alisema huku akibofya cha kupolelea na kuweka simu sauti ya nje.
“Haloo mama Colin.”
“Eeh! Dada kuna nini huko?”
“Kwani vipi?”
“Naona Colin ananichanyanyia maneno wala simuelewi.”
“Wala hakuna kitu cha kutisha bali mkweo aliudhiwa na shoga yake, lakini kwa sasa yupo sawa na wakati wowote atakuja huko.”
“Mmh! Afadhali maana nilikuwa na wasiwasi.”
“Wa nini?”
“Nilijua Colin kisha mtibua mkwe wangu.”
“Walaa, sema mkweo ana hasira za kitoto kitu kidogo analia kama kafiwa.”
“Basi nikuacheni muendelee na mambo mengine.”
Baada ya simu kukatwa mama Mage alimgeukia mwanaye na kumwambia.
“Unaona ulivyotaka kumsababishia matatizo mwenzako?”
“Mama lazima niende sasa hivi najua mpenzi wangu hayupo kwenye hali nzuri.”
“Fanya hivyo na...” mama Mage alinyamaza baada ya mlango kugongwa.
“Unasemaje?” aliuliza kwa sauti.
“Kuna wageni.”
“Nakuja,” mama Mage alitoka nje kwenda kumsikiliza mgeni.
Alitoka hadi getini na kukutana wa wanaume wawili na mwanamke mmoja, aliwatazama walikuwa wageni kwake.
“Karibuni.”
“Asante.”
Aliwakaribisha hadi sebuleni, baada ya kuketi mama Mage alitaka kujua wana shida gani.
“Ndiyo jamani mna shida gani?”
“Sisi ni maafisa wa polisi,” walitoa vitambulisho vyao.
“Ndiyo, mna shida gani?”
“Tuna imani hapa ndipo anaishi Magreth Chogo.”
“Ndiyo.”
“Yupo?”
“Mna shida gani?”
Kabla hajajibu Mage alitoka chumbani ili awaone wageni ni kina nani, askari mmoja baada ya kumuona alijua ni Mage alibahatisha kwa kumwita jina.
“Mage.”
“Abee.”
“Upo chini ya ulinzi,” alisema askari wa kike.
“He! Kwa kosa gani?” Mage alishtuka.
“Kutokana na tukio lililomtokea mpenzi wako wa zamani.”

ITAENDELEA
 
SEHEMU: 11
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500..

ILIPOISHIA:
Kabla hajajibu Mage alitoka chumbani ili awaone wageni ni kina nani, askari mmoja baada ya kumuona alijua ni Mage alibahatisha kwa kumwita jina.
“Mage.”
“Abee.”
“Upo chini ya ulinzi,” alisema askari wa kike.
“He! Kwa kosa gani?” Mage alishtuka.
“Kutokana na tukio lililomtokea mpenzi wako wa zamani.”
SASA ENDELEA...

“Sasa mimi nahusika kivipi?”
“Utajua yote kituoni.”
“Mi siendi,” Mage alitaka kugoma kwenda.
“We nenda wala usihofu, ila jamani chondechonde mwanangu asiguswe wala kulazimisha kusema uongo tutaelewana vibaya.”
“Hakuna tatizo, atakuwa salama baada ya mahojiano atarudi.”
Ilibidi Mage achukuliwe kupelekwa kituo cha kati cha polisi, mama yake alichukua simu na kumpigia mkuu wa polisi ambaye alikuwa rafiki mkubwa wa mzee Chogo baba yake Mage.
“Vipi shemeji?” ulipokewa upande wa pili.
“Mwanao Mage amekamatwa na vijana wako sasa hivi.”
“Kwa kosa gani?”
Alimwelezea kila kitu, baada ya kumsikiliza alimjibu.
“Basi hakuna tatizo shemeji nitalishughulikia mwenyewe, yupo kituo gani?”
“Cha kati.”
“Usiwe na wasi waache wamuhoji watamwachia tu.”
“Sawa shemeji kwa hiyo niende.”
“Hapana nitamfuta mwenyewe.”
“Asante shemeji.”
Mama Mage baada ya kukata simu alijikuta njia panda, alijifikiria kumpigia simu Colin lakini alijiuliza akimpigia atamwambia nini. Aliamua kukaa kimya ili kusubiri hatima yake ndipo ajue afanye nini.
***
Mage alipelekwa hadi kituoni na kuingizwa chumba cha mahojiano, Inspekta Koleta alikaa mbele ya meza aliyokuwa amekaa Mage na kalatasi ili kuandika mahojiano yale.
“Unaitwa nani?”
“Mage.”
“Nataka jina kamili.”
“Magreth Chogo,” Mage alijibu kwa sauti ya chini kidogo.
“Una umri gani?”
“Miaka 24.”
“Unamfahamu vipi Hans?”
“Namfahamu kama mpenzi wangu wa zamani.”
“Ulijuaje amepata matatizo?”
Mage alielezea jinsi alivyopigiwa simu na shoga yake Brenda ambaye alipigiwa simu rafiki yake Hans, Ndubukile.
“Wewe ulikuwa wapi?”
“Kwa mchumba wangu.”
“Anaitwa nani?”
“Colin.”
“Inasemekana mlikuwa ikipendana sana na Hans kwa nini hakukuoa akamuoa msichana mwingine?”
“Alichaguliwa na wazazi wake.”
“Unafikiri kwa sababu gani alichaguliwa msichana mwingine wakati wewe ndiye uliyekuwa mpenzi wake kila mtu alijua.”
“Kwa kweli kwa hiyo siwezi kujua.”
“Hans alipoona mwanamke mwingine wewe ulichukuliaje?”
“Sikuwa na jinsi ila roho ilinikuma sana.”
“Ulifikiria kufanya nini baada ya kuachwa na Hans?”
“Nilipanga kutojishughulisha na mapenzi tena.”
“Hukupanga kulipa kisasi?”
“Kisasi cha nini?”
“Kwa vile ndoto zako zilikuwa kuolewa na Hans.”
“Ni kweli ndoto zangu zilikuwa kuolewa na Hans lakini sikuwa chaguo la wazazi wake.”
“Unafikiria kwa nini unahusishwa na matukio ya mauaji na shambulizi la Hans?”
“Hata mimi nashangaa.”
“Kuna ukweli gani umelipa kisasi cha kuachwa kuolewa?”
“Hakuna ukweli wowote kwa vile sasa hivi nami nipo katika maandalizi ya ndoa yangu, kwanza nifanye vile kwa ajili gani kwa vile Hans sijagombana naye ameoa tukiwa tunapendana. Pia sikuwa na kinyongo na familia yake.”
“Unaweza kufikiria nani aliyefanya vile?”
“Mmh! Kwa kweli sijui kwa vile niliisha kata mawasiliano na Hans toka alipooa.”
“Kuna taarifa mlikuwa na penzi la siri na Hans?”
“Si kweli, mara nyingi Hans alinitafuta kuniomba msamaha nilimkatalia kwa vile yeye ni mume wa mtu sikutaka kuonekana naingilia ndoa yake hasa baada ya familia yake kutonihitaji.”
Wakiwa katika ya mazungumzo mkuu wa polisi aliingilia Mr Clarence, Inspekta Koleta alinyanyuka na kupiga saluti. Mage alipomuona alifurahi kwani siku zote alikuwa mtu wa karibu katika familia yao.
“Shikamoo baba.”
“Marahaba, kuna nini?”
“Mkuu kuna tukio la mauaji na mashambulizi ambayo inaonekana mshukiwa wa kwanza ni huyu binti,” alijibu Inspekta Koleta.
“Hebu nipe hiyo kalatasi ya maelezo.”
Mkuu wa Polisi Mr Clarence aliichukua na kuisoma kisha aliomba kuzungumza na Mage kidogo. Baada ya kupishwa alimuuliza mswali kuhusiana na tukio lile.
“Mage.”
“Abee baba.”
“Naomba uniambie ukweli ili nikusaidie hata kama umehusika niambie ili nijue jinsi ya kukusaidia,” Mr Clarence alimwambia kwa upole.
“Baba haki ya Mungu sijui chochote zaidi ya kupigiwa simu asubuhi nikiwa kwa mkweo, kwa vile Hans ndiye aliyekuwa chaguo la moyo wangu pia sikukosana naye bali penzi letu lilivunjwa kwa nguvu ya wazazi wake nilishtuka sana kupata habari ile. Huwezi kuamini taarifa ile ilisababisha nitoke hata bila kumuaga mkweo hivi ndiyo nilikuwa najiandaa kwenda kuzungumza na mkweo japo sikutaka ajue nimekuja kumuona mpenzi wangu wa zamani.”
“Una muda gani ujaonana na Hans?”
“Mmh! Sasa ni mwaka na nusu.”
“Kwa nini?”
“Baba, yeye kaoa na mimi Mungu kanipa wangu kuna umuhimu gani kuendeleza ukaribu?”
“Nimekuelewa, sasa nitawaambia utoke kazi yote niachie mimi.”
“Asante baba.”
Mkuu wa polisi alimwita Inspekta Koleta na kumweleza amwachie Mage na kumweleza waendelee na upelelezi kwa vile Mage ahusiki na matukio yake. Walikubaliana na Mage aliruhusiwa kutoka. Mkuu wa Polisi Mr Clarence alimchukua Mage na kumrudisha nyumbani.
Mama yake alifurahi kumuona mwanaye na Mr Mulisa.
“Asante shemeji.”
“Kawaida, nina imani Hans akipata nafuu kila kitu kitakuwa wazi.”
“Tena Mungu ampe afya ili kuwaumbua wenye roho mbaya wanataka kuiharibu harusi na mwanangu.”
“Usiwe na wasi kila kitu kitakwenda kilivyopangwa na aliyetenda unyama ule atajulikana mkono wa dola ni mrefu.”
Mkuu wa polisi aliaga na kumuacha Mage na mama yake, baada ya kuondoka Mage aliagungua kilio.
“Mama kosa langu nini? Mbona familia ya kina Hans wameniandama hivyo, jamani mimi nimuue mke wa Hans na mwanaye na kutaka kumuua Hans ili iweje?”
“Ndiyo dunia mwanangu, kwa vile baba yako yupo atakusimamia.”
“Unajua mama mi’ nilikuwa na wasiwasi labda aliyefanya vile ni Colin.”
“Wee! Temea chini tena usirudie kusema kitu kama hicho, Hans na Colin wapi na wapi?” Mama yake alikuwa mkali.
“Basi mama nisamehe ni mawazo tu.”
“Tena umeniudhi sana, wee kidogo ufe kwa presha kwa kusingiziwa unataka kumpaka shombo mtoto wa watu.”
“Basi mama nisamehe ulikuwa wasiwasi wangu.”
“Nataka uoge ubadili nguo uende kwa mwenzio ukamtoe hofu usimweleze ya kupelekwa polisi.”
“Sawa mama.”
Mage alikwenda kuoga na kubadili nguo alichukua gari na kwenda kwa Colin, akiwa njiani alijawa na mawazo juu ya familia ya Hans kumshukia yeye katika tukio lile.
Alijiuliza kipi hasa kilichofanya wamfikirie yeye kwanza.
Aliona jinsi gani familia ile jinsi ilivyokuwa ikimchukia na kuamini kauli ya mama yake kuwa hata kama angeolewa asingedumu kwenye ndoa yake kwa vile hakuwa chaguo lao.
Alijikuta taratibu mapenzi yake yote akiyahamishia kwa Colin na kuuapia moyo wake kumpenda kwa nguvu zake zote na kwa akili zake zote. Alipofika nyumbani kwao Colin baada ya kuteremka kwenye gari aliingia ndani huku akikimbia kama mtu aliyepagawa. Sebuleni alimkuta mama Colin, alishtuka kumuona katika hali ile.
“Vipi Mage?”
“Mama, mume wangu yupo wapi?” aliuliza akionesha kuchanganyiwa.
Wakati huo Colin alikuwa akitokea chumbani kwake kuja sebuleni, alipomuona alikimbilia na kumkumbatia.
“Jamani mume wanguu!”
“Vipi mbona hivyo?” Colin alishtuka uchangamfu wa Mage uliopitiliza.
“Najua nimekuudhi nisamehe sana, mama nimemuudhi sana mume wangu,” Mage alisema huku akilia.
“Hujamuudhi chochote,” mama Colin alisema.
“Najua nimemuudhi, Colin naomba twende chumbani.”
Walishikana mikono na kuelekea chumbani na kumuacha mama Colin akiwatazama na kuchekelea moyoni na kusema kwa sauti ya chini. “Kweli wanapendana.” Aliwatazama mpaka walipopotea machoni kwake.
Colin na Mage alikwenda hadi chumbani, alipofika ndani Mage alijifupa kifuani kwa mpenzi wake na kuanza kulia kitu kilichomshtua Colin na kuhoji.
“Vipi mpenzi?”
“Colin nisamehe sana mpenzi wangu.”
“Kwa lipi?”
“Najua leo nimekukosea kwa kuondoka bila kukuaga kitu kilichokufanya usumbuke kunitafuta, kibaya zaidi zijapokea simu zako na kukataa kuzungumza na wewe uliponifuata nyumbani.”
“Kumbe ni hayo? Achana nayo.”
“Hapana najua umenikubalia ili yaishe lakini umejenga picha mbaya juu yangu.”
“Walaa.”
“Colin nihukumu hukumu yoyote lakini elewa nakupenda sana mpenzi wangu, nilitaka kufanya surprise lakini ikaenda ndivyo sivyo. Nilishindwa nikueleze nini kwa vile sikuwa na lakukueleza kwa wakati ule hasa baada ya Brenda kunichanganya.”
“Yote mama alinieleza ndiyo maana nilikuelewa toka asubuhi.”
“Colin lakini si unajua nakupenda?” Mage alimuuliza kwa sauti ya kudeka.
“Najua, ndiyo maana upo hapa.”
“Nashukuru kulifahamu hilo.”
Siku ile Mage alishinda pale na kufanya kazi zote za nyumbani ikiwa pamoja na kupika chakula cha jioni. Colin aljikuta akisahau yote na kujiona kama tayari kaisha muoa Mage.
Siku ile muda wote walikuwa pamoja kama kumbikumbi kwa kufanya kazi kwa kusaidizana. Mama Colin muda wote alikuwa mtu wa tabasamu na kuona ndoa ya mwanaye jinsi itakavyojaa furaha na upendo.
Aliwaangalia walivyopendeza kwa kusaidizana kazi zote za jikoni mtu na mchumba wake. Alifumbata mikono yake na kuomba kwa sauti ya chini.
“Eeh! Mwenyezi Mungu baba nijalie ndoa ya wenetu iwe yenye matunda,” baada ya dua alipiga njia ya msalaba kumshukuru Mungu.
Siku ile ilikuwa ya furaha kwa wapenzi wawili kwa Mage ambaye alihamishia mapenzi yake yote kwa Colin baada ya kujua hata kama angempenda vipi Hans asingekuwa na nafasi ndani ya familia yake. Aliona jinsi gani sivyo mpenda mpaka kumzushia shutuma nzito za mauaji ya shambulio la kuua.
Kingine kilichomuweka njia panda kama Mungu atamsaidia Hans kupona atamchukuliaje, lazima naye atangeamini mhusika ni yeye. Lakini kwa upande wa Hans alijua ni vigumu kumshuku yeye kutokana na ukaribu wao ulivyokuwa.
Angekuwa na wasiwasi kama angekuwa akilipigania penzi la Hans. Kama tatizo lile lingemtokea baada ya kuoa lazima Hans angejua ni yeye, lakini baada ya mkewe kupata ujauzito na kujifungua penzi lake alilizika rasmi.
Aliamini ule ndiyo muda wa kulionesha penzi lake halisi kwa Colin, siku ile alilala tena na kuondoka siku ya pili huku kila mmoja akifurahia penzi la mwenzake.
****
Ukaribu wa Mage na Colin kwa kufuatana muda wote kama kumbikumbi, Ulifanya Colin ashindwe kutekeleza ahadi yake kwa kina Cecy. Baada ya kusubiri kwa wiki bila kuonekana dalili zozote za kutekelezwa ahadi. Cecy aliyekuwa amejilaza kitandani na kukosa usingizi.
Alijikuta akinyanyuka kitandani na kumfuata mama yake aliyeamini ameisha pitiwa usingizi ambaye alikuwa na matumaini ya kuyakimbia maisha ya kulala nyumba ya kuvuja na taa ya kibatari.
Alitoka chumbani kwake na kwenda hadi kwenye mlango wa mama yake na kugonga.
“Mama..mama.”
“Unasemaje Cecy,” alimuuliza bila kuamka kwa vile tayari alikuwa amepitiwa usingizi.
“Kuna jambo nataka tushauliane.”
“Jambo gani, kwani lazima tuzungumze usiku?”
“Ndiyo, asubuhi nikiamka nijue cha kufanya.”
“Mmh! Nakuja.”
Mama yake aliamka na kutoka sebuleni, alimkuta Cecy amesimama, mama yake aliketi kwenye kigoda na kumtazama mwanaye aliyekuwa bado amesimama.
“Unasemaje mama?”
“Mama siku zote japo mdogo lakini huwa nayaamini mawazo yangu japokuwa sina elimu kubwa, lakini busara haina elimu bali kipawa toka kwa Mungu.”
“Ni kweli.”
“Hivi mama tulipokuwa tukifanya biashara zetu tulipungukiwa nini?”
“Hatukupungukiwa kitu, kwani maisha ya mwanadamu Mungu ndiye anayetuongoza.”
“Kwa hiyo hatuwezi kumtegemea mtu?”
“Ndiyo, kwani amelaaniwa kila amtegemea mwanadamu.”
“Nimefurahi sana kulifahamu hilo.”
“Ulikuwa una maanisha nini?”
“Huoni kama tunamkosea Mungu kumtegemea mtu.”
“Tunamtegemea nani?”
“Tumeacha kufanya biashara zetu kwa ajili ya Colin aliyetugeuza watoto kutuahidi pipi, leo ni siku ya ngapi hatufanyi biashara kwa ajili ya kusubiri ahadi yake. Wiki inakatika hakuna cha tofari wala mchanga.”
“Cecy mwanangu Colin, naye binadamu huenda amepatwa na matatizo. Hivyo tulitakiwa kuvuta subira.”
“Mama niliyajua haya mapema, sikutaka kukukata kauli kwa vile wewe ni mtu mzima. Lakini nilijua hakuna kitu, Colin atujengee nyumba kwa kipi cha maana tulichompa?”
“Kwa hiyo ulikuwa unasemaje?”
“Kesho asubuhi nakwenda Mabibo kununua ndizi na kuendelea na kazi yangu inayoniweka mjini.”
“Mmh! Si wazo baya.”
Walikubaliana siku ya pili Cecy aendelee na biashara yake ya ndizi kama kawaida. Kila mmoja alirudi chumbani kwake na kupanda kitandani. Cecy alichelewa kulala huku moyo ukimuuma kwa kitendo cha Colin kuwadhalilisha kwa kuwaahidi kitu kisichowezekana.
Alijikuta akimchukia Colin na kuapa hata zungumza naye siku zote za maisha yake. Kutokana na hasira alijikuta akichelewa kulala.
Siku ya pili Cecy aliamka na mapema na kuwahi kununua ndizi, baadaye alirudi nyumbani na kuoga kisha aliingia chumbani na kuchagua nguo za kuiingia nazo mtaani. Alitafuta gauni lililochoka na upande wa khanga uliopauka na kuvaa.
Alitoka kuelekea nje, alipofika mlangoni alisita kidogo na kujiuliza swali.
“Hivi maisha yangu namtegemea nani? Jibu Mungu, kwa nini niishi maisha kwa ajili ya mtu fulani? Ina maana bila Colin sina maisha? Hapana..hapana,” Cecy alisema huku akirudi chumbani na kuvua nguo chakavu na kufungua sanduku lake na kutoa nguo nzuri na kuzivaa kisha alitoka na kuchukua beseni lake la ndizi na kumuaga mama yake aliingia mtaani kuuza ndizi.
Alishangaa siku ile alimaliza ndizi mapema tofauti na alivyobadili mfumo wa maisha baada ya kuumizwa na penzi la Colin na kuamua kuishi kwa kutojijali. Toka alipoamua kuishi maisha yale biashara yake haikuwa kama awali alijikuta akimaliza biashara zake kwa kutembea umbali mrefu pia kutumia muda mwingi.
Alijikuta akijilaumu kwa kupoteza muda wake mwingi kumuwaza Colin mwanaume asiye na mapenzi naye ambaye tayari alikuwa na mpenzi wake. Moyo wake aliutoa kifungoni na kuwa tayari kupokea penzi jipya ila la mtu atakaye mpenda naye ampende ambaye atakuwa sahihi kwa moyo wake.
Hakuwa tayari kumkubali mwanaume anayetumia umaskini wake kufanya naye ngono. Siku zote aliamini mwenye mapenzi ya kweli hawezi kutanguliza ngono mbele zaidi ya upendo kwanza.
Lakini kwa Colin alikuwa radhi kuupoteza usichana wake hata bila ndoa kwani aliamini penzi la Colin lilizidi furaha ya maisha yake. Baada ya matukio yote aliamini muda wa uvumilivu ulikuwa umepita hivyo alitakiwa kitengeneza mawazo mapya na kuwaza kitu kingine kabisa kigeni katika ubongo wake.
Kila usiku ulipoingia alitumia muda mwingi kuwaza maisha wanayoishi ya kuuza ndizi mwisho wake nini. Aliamini muda ule bado ana nguvu alitakiwa atafute njia mbadala itakayomsaidia kukabiliana na ukali wa maisha aweze kumsaidia mama yake. Wazo lilikuwa kila jioni baada ya kutoka kwenye biashara zake ambazo zilikuwa zikifanya vizuri japokuwa changamoto za wanaume zilikuwa kubwa ambazo alikabiliana nayo.
Wazo kubwa lilikuwa aanze kusoma masomo ya jioni kujifunza kingereza ambacho kingemsaidia kufafuta kazi ya kuajiliwa na kuachana na kazi ya kuzurula huku akila vumbi la barabarani.
Wazo lile alimwambia mama yake ambaye naye aliliafiki, jioni ilipofika alikwenda sehemu moja iliyokuwa ikifundisha twisheni na kuomba kusoma kingereza ambacho aliahidiwa kukijua baada ya miezi mitatu. Alilipa ada na kuanza kusoma siku ileile huku akiwa na ndoto za siku moja naye kuzungumza kingereza.

Itaendelea
 
SEHEMU: 12
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500..
ILIPOISHIA:
Wazo lile alimwambia mama yake ambaye naye aliliafiki, jioni ilipofika alikwenda sehemu moja iliyokuwa ikifundisha twisheni na kuomba kusoma kingereza ambacho aliahidiwa kukijua baada ya miezi mitatu. Alilipa ada na kuanza kusoma siku ileile huku akiwa na ndoto za siku moja naye kuzungumza kingereza.
SASA ENDELEA...
***
Mipango ya harusi ya Colin na Mage ilizidi kupamba moto huku kila familia ikijipanga kufanya sherehe ya kufuru. Nayo Hali ya Hans iliendelea vizuri iliyofanya atolewe hospitali na kurudishwa nyumbani. Baada ya kutulia kwa wiki moja aliitwa polisi kutoa maelezo kutokana na tukio lililomtokea lililopeleka kupoteza mke na mtoto.
“Pole sana,” Inspekta Koleta alianza kwa kumpa pole.
“Asante.”
“Unajisikiaje kwa sasa?”
“Namshukuru Mungu sijambo kabisa.”
“Unakumbuka tukio lilivyotokea?”
“Ndiyo, nilikuwa chumbani mke na mwanangu wakiwa sebuleni ghafla nikasikia sauti kama ya amri, mwanzo nilifikiri labda sauti inatoka kwenye tivii kwa vile alikuwa akiangalia tamthilia. Lakini sauti ya maumivu ya mke wangu ilinishtua na kunifanya nitoke chumbani. Nilishtuka kuona mke na mwanangu wamelala chini.
“Nilipotaka kwenda kuwasaidia nilipigwa na kitu kizito kichwani kilichonifanya nipoteze fahamu. Nilipozinduka nilijikuta nipo hospitali na kupewa taarifa za kushtusha za kifo cha mke wangu na mwanangu,” Hans alipofika hapo alianza kulia na kumfanya Inspekta Koleta kumbembeleza.
“Pole sana.”
“Asante, lakini inauma sana heri wangeniua mimi kuliko mke na mwanangu!”
“Najua inauma, unawafahamu waliofanya unyama ule?”
“Kwa kweli siwafahamu kutokana na kuziba nyuso zao na kofia za kuziba kichwa.”
“Unamjua Mage?”
“Mage yupi?”
“Wewe unamjua Mage yupi?”
“Mmh! Mmoja.”
“Yupi?”
“Aliyewahi kuwa mpenzi wangu.”
“Unamfahamu vipi?”
“Alikuwa mpenzi wangu, lakini bahati mbaya nilioa mwanamke mwingine badala yake.”
”Kwa sasabu gani ulioa mwingine na kumuacha mpenzi wako wa muda mrefu?”
“Wazazi wangu walikuwa hawamtaki.”
“Unafikiri kitendo cha wazazi wako kumkataa Mage na kumchukua mwanamke mwingine kilimpandisha Mage hasira na kuamua kukukomoa?”
“Walaa, yule msichana hausiki kabisa.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Sasa hivi yupo katika mipango ya harusi anategemewa kuwa mke wa mtu afanye vile ili iweje?”
“Kwa hiyo huna mtu yeyote unayemshuku?”
“Mmh! Hakuna,” Hans alikataa.
“Basi tukikuhitahi tutakuita.”
“Hakuna tatizo.”
Baada ya mahojiano yale Hans aliruhusiwa kuondoka, alirudi kupumzika nyumbani. Kila alipokaa peke yake moyo aliendelea kuumia bila kuonana na Mage na kumweleza neno lililo moyoni mwake kabla ya kuolewa.
Aliamini kwa vile ulikuwa umebakia mwezi mmoja na nusu harusi ifungwe ingekuwa vigumu kuonana ana kwa ana. Wasiwasi wake ulikuwa kutopata nafasi baada ya kupata taarifa kwenda kumuona hospitali na kufukuzwa kisha kufunguliwa shtaki la kuishambulia familia yake. Aliamini Mage hatakuwa tayari kumsikiliza.
Alijaribu kumpigia shoga yake Brenda ili amsaidie aweze kuzungumza naye hata kwa dakika mbili kisha moyo wake uwe radhi Mage kuolewa. Alichukua simu yake na kumpigia Brenda ambaye aliipokea upande wa pili.
“Haloo.”
“Haloo Brenda.”
“Abee, nani mwenzangu?”
“Hans.”
“Hans yupi?”
“Shemu kweli umenichoka yaani leo unaniuliza hivyo?”
“Ha! Kumbe wewe? Vipi unaendeleaje?”
“Nipo fiti kama chuma.”
“Wewee! Utani huo upo wapi?”
“Nyumbani, kwanza niwapeni pole kwa kitendo cha familia yangu kuwazuia kuniona kimeniuma sana kwa hiyo nakuombeni radhi sana.”
“Hans wewe siku zote huna kosa, familia yako ndiyo kikwazo katika maisha yako.”
“Hilo nalijua.”
“Hans mtoto bado ana mapenzi na wewe baada ya taarifa zile kachanganyikiwa mbio hospitali lakini walichomfanya familia yako hawezi kusahau kibaya zaidi wamempakazia tatizo lako.”
“Yaani wamenichanganya ile mbaya, Brenda naomba unikutanishe na Mage ili nimuombe msamaha.”
“Mmh! Sijui kama utampa kwa vile sasa hivi yupo katika maandalizi ya ndoa yake.”
“Sikiliza Brenda naomba nikupitie kwenu twende hadi nje ya nyumba yao Mage kisha uje naye nizungumze naye kwa dakika tano kisha nikurudishe nyumbani kwenu. Nakuahidi zawadi nzuri ukiniwezesha kumuona Mage kwa dakika hata mbili tu.”
“Mmh! Kwani sasa hivi upo wapi?”
“We nieleze nikufuate wapi?”
“Njoo home basi.”
“Fanya hivi chukua gari la kwenu tukutane Kivukoni.”
“Haina tatizo.”
Hans baada ya kuelezwa vile alitoka na kuingia kwenye gari aina ya Toyota Verosa na kuelekea Kigamboni kwa kina Mage. Alipofika Kivukoni hakukaa sana simu yake iliita ilikuwa ya Brenda, aliipokea.
“Haloo Brenda.”
“Hans nimefika, upo wapi?”
“Nami nimefika umekuja na gari gani?”
“Nissan Patrol nyeupe.”
“Basi tuvuke.”
Walikubaliana kuvuka upande wa pili, baada ya watu na baadhi ya magari kujaa ndani ya kivuko safari ya kuelekea Kigamboni ilianza. Kivuko kiliposimama upande wa Magogoni, watu waliteremka na kuelekea maeneo ya Kigamboni, Mji mwema mpaka Geza ulole na kwingineko.
Brenda alitangulia baadaye aliliona gari la Hans likija nyuma, hakusimama aliendelea na safari mpaka karibia na kwa kina Mage alisimamisha gari pembeni Hans naye alisimamisha pembeni yake na kuteremka.
Hans na Brenda walikumbatiana na kupeana pole upya huku Brenda akiwa haamini kama Hans amepona.
“Dah! Pole sana.”
“Asante.”
“Sasa inakuwaje?”
“Fanya hivi hili gari langu tuliache sehemu salama ili twende na lako tukifika utaingia ndani kwenda kumuita akija utamuingia kwenye gari lako najua atashangaa kuniona lakini nitatumia muda huo kuzungumza naye kisha atarudi ndani mwao na sisi tuondoke.”
“Hakuna tatizo.”
Hans alilipaki gari lake sehemu ya usalama na kuingia kwenye gari la Brenda hadi nyumbani kwao na Mage. Alipofika alilisimamisha gari pembeni ya geti hakutaka kuliingiza ndani na kuteremka. Mlinzi alishangaa kuliacha gari nje na kumuuliza.
“Da’ Brenda mbona huingizi gari ndani?”
“Hapana sikai sana,” Brenda alijibu huku akiingia ndani ya geti.
Alitembea kwa mwendo wa kukimbia hadi ndani, alimkuta msichana wa kazi akiondoa vyombo mezani na kumuuliza.
“Mage yupo wapi?”
“Chumbani kwake.”
Alikwenda hadi chumbani na kugonga.
“Ingia,” sauti ya Mage toka ndani ulisema.
Brenda alisukuma mlango na kuingia ndani Mage alishtuka kumuona shoga yake muda ule, kwa vile hawakuwa na miadi ya kukutana muda ule wakati mchana wa siku ile walikuwa pamoja na kuachana jioni.
“He! Vipi mbona huku muda huu?” Mage alimshangaa Brenda.
“Shoga hebu twende nje mara moja.”
“Kuna nini?”
“Utajua huko, we twende mara moja.”
Mage bila kuongeza neno alinyanyuka kitandani na kuongozana na Brenda hadi nje, alishangaa kuona wanatoka nje ya geti. Lakini hakuhoji alisubiri kuona Brenda kamuitia nini. Alipotoka nje ya geti aliliona gari la Brenda, kwa vile alikuwa akisubiri muda wa kwenda kwa Colin na alichelewa kwenda kutokana na mama yake kutoka alimwambia shoga yake.
“Brenda siwezi kufika mbali namsubiri mama ili niende kwa mume wangu.”
“Hata huendi popote twende ndani ya gari.”
“Kuna nini?”
“Hebu punguza maswali.”
Waliongozana wote hadi kwenye gari.
“Ingia mlango wa nyuma,” Brenda alimwambia Mage, naye hakubisha aliingia.
Ndani ya gari palikuwa giza, Brenda baada ya kuingia mbele aliwasha taa na kumfanya Mage ashtuke kumuona Hans.
“Ha! Hans?”
“Ndiyo mimi Mage samahani kwa kukushtukiza.”
“Bila samahani, kwanza unaendeleaje?”
“Namshukuru Mungu sijambo kabisa.”
“Pole na kufiwa mke na mtoto.”
“Asante, pole na wewe kutokana na ulichotendewa na familia yangu.”
“Hans achana na hayo yameisha pita, nina imani kuna kitu kimekuleta naomba tuzungumze kwa haraka nataka kwenda kwa mume wangu muda si mrefu.”
Hans alijikuta akitulia huku maneno yakigoma kutoka mdomoni, Mage alishangaa kuona mpenzi wa zamani akitokwa na machozi. Brenda alitoka nje ya gari na kuwaacha wapenzi ndani ya gari wazungumze yao.
“Jamani nipo nje.”
“Hakuna tatizo, usikae mbali natoka sasa hivi,” Mage alisema.
Baada ya kutoka Mage alimuuliza Hans aliyekuwa akitokwa machozi.
“Hans ameniita kuona machozi yako au kuna kitu kingine kama ni machozi nimeisha yaona, naomba niende zangu,” Mage alizungumza kwa sauti ya upole huku akimtazama usoni Hans.
“Ma..ma..ge,” Hans alisema kwa kigugumizi.
“Jina langu.”
“Kilichonileta si kuja kukuonesha machozi bali moyo wangu umejaa maumivu makali.”
“Najua inauma kupoteza mke na mtoto si kitu cha kawaida yataka moyo wa chuma kuyashinda maumivu yake lakini Mungu siku zote ni mfariji na kukufanya utayasahau yote kisha atakuletea mke mwingine.”
“Mage mimi na wewe tuliahidiana nini?”
“Kuoana kuwa mke na mume.”
“Baada ya matatizo ya familia yangu nilikueleza nini?”
“Ulisema huwezi kuzaa na yule mwanamke, baadaye utamuacha na kunioa mimi.”
“Kwa nini umekubali kuolewa na mwanaume mwingine?”
“Kwa sababu umevunja ahadi yetu.”
“Mage nina imani unajua jinsi gani ninavyokupenda?”
“Siyo unavyonipenda bali ulivyokuwa ukinipenda.”
“Mage moyo wangu hautachoka kukupenda, nilikueleza nini baada ya kulazimishwa kuoa mwanamke mwingine?”
“Ulisema wakikulazimisha kuoa utajiua.”
“Ulinishauri nini?”
“Nilikuwa radhi uoe lakini si kukupoteza maishani, ulichoniahidi ndicho kilinipa moyo na kuwa radhi kukusubiri hata miaka mia. Lakini wewe ndiye ulivunja mkataba na kuamini sina changu na kuamua nami kutafuta wangu japokuwa ilikuwa sawa na kunimezesha mfupa.”
“Ndiyo sababu ya mimi kuja kuzungumza na wewe, baada ya kunisikiliza uamuzi utakaoutoa hapa sitapingana nao hata kama utaniumiza.”
“Haya niambie hicho kilichokuleta.”
Hans alianza kuzungumza kwa sauti ya chini yenye kusikika huku machozi yakiweka michirizi kwenye mashavu. Mazungumzo yalikuwa (Of air) ambayo hayakutakiwa mtu yeyote kusikia zaidi ya watu wawili tu. Hans alimaliza kuzungumza huku machozi na kamasi zikimtoka chapachapa.
Muda wote Mage alijitahidi kumbembeleza Hans japokuwa naye alikuwa akilia.
“Hans nimekuelewa lakini hukutakiwa kufanya hivyo.”
“Sikuwa na jinsi, hukutaka kunisikiliza nilikuwa na wakati mgumu wa kuweza kunisikiliza. Kama ningekufa bila wewe kuujua ukweli wa moyo wangu ningekuwa nimekufa kibudu. Kama ningeshindwa kabisa ningekuja kujiua kwenye harusi yako ili ujue nilichokuahidi hakitabadilika moyoni mwangu kuwa kifo pekee ndicho kitanitenganisha na wewe.”
“Mmh! Mbona Hans unanipa mtihani mkubwa, japokuwa uamuzi ni wangu lakini dunia itanitenga.”
“Lakini Mage nilikueleza kila kitu juu yetu, wewe ndiye uliyeshikilia uhai wangu kwa mara nyingine wa kuniua au kuniacha hai ni wewe.”
“Hans hata siku moja kifo chako hakitatoka mikononi mwangu, naombani uniache kwa leo mengine tutazungumza kesho kichwa changu kimevurugika hata sielewi jifanye nini.”
“Ila kumbuka uhai wangu umeubeba wewe.”
“Naelewa Hans.”
“Kwa hiyo niondoke na jibu gani?’
“Niache kwa leo, nimekuelewa Hans.”
“Sawa lakini bado nipo njia panda.”
“Hans kuwa muelewa nimekueleza nimekuelewa unataka nini tena?”
“Basi nashukuru.”
“Nikutakie usiku mwema.”
“Na kwako pia.”
Mage aliteremka kwenye gari na kumuaga shoga yake huku akifuta machozi yaliyokosa kizuizi kisha alielekea ndani mwao. Brenda aliingia ndani ya gari na kushangaa kumkuta Hans akifuta machozi wakati Mage naye alitoka akifuta machozi.
“Vipi kuna usalama?”
“Kiasi.”
“Umeelewana?”
“Ndiyo.”
“Kwa hiyo tunaweza kwenda.”
“Ndiyo.”
Brenda aliwasha gari na kuliondoka kuelekea walipokuwa wameliacha gari la Hans, njiani alijaribu kudodosa kwani kila mmoja alionekana kulia.

Itaendelea
 
SEHEMU: 13
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500.

ILIPOISHIA:
Mage aliteremka kwenye gari na kumuaga shoga yake huku akifuta machozi yaliyokosa kizuizi kisha alielekea ndani mwao. Brenda aliingia ndani ya gari na kushangaa kumkuta Hans akifuta machozi wakati Mage naye alitoka akifuta machozi.
SASA ENDELEA...

“Vipi kuna usalama?”
“Kiasi.”
“Umeelewana?”
“Ndiyo.”
“Kwa hiyo tunaweza kwenda.”
“Ndiyo.”
Brenda aliwasha gari na kuliondoka kuelekea walipokuwa wameliacha gari la Hans, njiani alijaribu kudodosa kwani kila mmoja alionekana kulia.
“Hans, Mage anasemaje?”
“Hana la kusema bali nilitaka tu kumfikishia ujumbe, nashukuru amenisikiliza.”
“Kwa hiyo roho yako umetulia?”
“Nashukuru, tukifika kwenye gari nitakupa zawadi yako niliyokuahidi.”
“Nitashukuru.”
***
Muda ulizidi kukatika bila Mage kuonesha dalili zozote za kutoka kwenda kwa Colin, kitu kiliochomshtua mama yake ambaye aliwahi kurudi kwa ajili ya mwanaye kwenda kwa mchumba wake. Aliangalia saa ya ukutani ilimuonesha inakaribia saa nne usiku, alijiuliza labda mwanaye ametoka bila yeye kujua.
Ilibidi amuulize msichana wa kazi kama Mage ametoka yeye akiwa chumbani.
“Sofi Mage ametoka saa ngapi bila kuniaga?”
“Mmh! Mama sijamuona kutoka.”
“Una maanisha yupo chumbani kwake?”
“Sijajua ila sijamuona.”
Mama Mage alinyanyuka na kwenda chumbani kwa mwanaye, alikuta mlango umerudishwa alisukuma na kuingia bila hodi na kumkuta Mage amejilaza akiwa amekumbatia mtu huku machozi yakimwagika kama maji. Mama yake alishtuka na kutaka kujua kuliko mwanaye kuwa katika hali ile.
“Mage! Nini mwanangu?”
“Mamaa..maamaa,” Mage alishindwa kuzungumza aliangua kilio.
“Mage una nini?” mama yake alizidi kumshangaa.
“M..m..maa..ma,” Mage kila alipotaka kusema maneno yaligoma kutoka mdomoni.
“Mage mwanangu umepatwa na nini, hebu nieleze mimi ndiye mama yako nipo tayari kukusikiliza na kukusaidia.”
“Mama nipo kwenye wakati mgumu sana maishani mwangu.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Najua nitakuudhi wewe mama yangu lakini nina imani ndiyo tiba sahihi ya moyo wangu ambao umekuwa matesoni kwa muda mrefu.”
“Una maanisha nini?” mama yake alishtuka mpaka mapigo ya moyo yalianza kumwenda kasi.
“Mama nitakacho kisema najua kitakuwa sawa na kumng’oa mtu jino bila ganzi.”
“Una maanisha nini?”
“Mama sitaki kuolewa tena.”
“Niniii?” mama alishtuka.
“Mama sitaki kuolewa na Colin.”
“Kwa nini?”
“Si chaguo la moyo wangu.”
“Mwanangu unasema ukweli au unatania?”
“Nasema kweli kabisa.”
“Mmh! Na mipango ya ndoa?”
“Tunasitisha kwa vile muda bado.”
“Na watu tuliowachangisha fedha za send of.”
“Tutawarudishia fedha zao.”
“Wee mwana tutazupata wapi?”
“Mi najua pa kuzipata.”
“Hebu mwanangu nieleza tatizo nini, kama Colin amekukosea bado tuna nafasi ya kuzungumza tukalimaliza.”
“Mama, Colin hajawahi kunikosea toka tujuane, ila mimi ndiye nimekuwa nikimkosea muda wote. Najua ananipenda sana na uamuzi wangu utamchanganya, lakini ukweli utabakia palepale si chaguo la moyo wangu. Nimejilazimisha kumpenda lakini moyo umekataa hivyo sina budi kuusikiliza moyo wangu unachotaka.
“Siku zote moyo wa mtu huwa ndiyo muamuzi kwa jambo lolote kwa vile wenyewe ndiyo unaopokea furaha kwa jambo zuri au huzuri kwa jambo baya.”
“Kwa hiyo unasema hujakosana na Colin?”
“Walaa, najua Colin ananipenda sana na ataumizwa na uamuzi wangu lakini sina jinsi kila ndege hutua mtu aupendao.”
“Mage upo sawa mwanangu?”
“Nipo sawa mama.”
Kauli ile ilimfanya mama yake akae kwenye kitanda baada ya miguu kukosa nguvu.
“Mage mwanangu mbona sikuelewi, kipi kimekusibu mama?”
“Mama najua itakuwa vigumu kunielewa lakini utanielewa tu.”
Mara simu ya Mage iliita, aliichukua na kuitazama na kuirudisha bila kuipokea kitu kilichomfanya mama yake kuuliza.
“Mbona upokei kwani inatoka wapi?”
“Kwa Colin.”
“Sasa kwa nini hupokei?”
“Sasa nitazungumza naye nini?”
“Pokea mwambie leo huwezi kwenda hujisikii vizuri.”
“Siwezi kuzungumza naye kwa leo, nitajisikia vibaya.”
Simu iliita tena lakini haikupokelewa mpaka inakatika, baada ya muda msichana wa kazi alimwita mama Mage kuwa kuna simu yake inaita. Alitoka na kuichukua ilikuwa inatoka kwa mama Colin, aliipokea mara moja.
“Haloo dada.”
“Eeh! Kuna usalama huko?”
“Kiasi.”
“Kulikoni?”
“Mage kichwa kilimshika ghafla.”
“Jamani mkwe wangu! Vipi hali yake?”
“Kidogo hajambo amelala kwa sasa.”
“Basi tunakuja kumuona.”
“Usisumbuke, alitaka kuja nikamzuia hayupo serious sana.”
“Basi augue pole maana mwenzake alikuwa na wasiwasi baada ya kupiga simu isipokelewe.”
“Mwambie asiwe na wasiwasi ni kichwa tu lakini anaendelea vizuri kesho atakuwa hajambo.”
“Basi niwatakie usiku mwema.”
“Na ninyi pia.”
Mama Colin baada ya kumaliza kuzungumza alimgekia mwanaye aliyekuwa pembeni ya mama yake akifuatilia mazungumzo yale.
“Vipi mama?”
“Kumbe kichwa kilimshika ghafla amekunywa dawa kimetulia, alitaka kuja lakini mama yake kamwambia alale kwa leo atakuja kesho.”
“Duh! Afadhali, nilikuwa na wasiwasi sana.”
“Kapumzike, kesho mchumba wako atakuja.”
“Sawa mama.”
Colin alikwenda chumbani kwake, kabla ya kulala alichukua simu yake na kuangalia picha zote alizopiga na Mage na nyingine iliyopigwa siku ile mchana aliyotumiwa na Mage alipokuwa na shoga yake Brenda Mlimani City Samakisamaki. Aliibusu picha picha kubwa ya mpenzi wake aliyokuwa katika tabasamu la kufa mtu na kusema kwa sauti ya chini.
“Mage wewe ndiye mke wa maisha yangu,” aliikumbatia na kujilaza.
***
Mama Mage usingizi uligoma kabisa na kukiona kichwa kikitaka kupasuka kutokana na kuchanganywa na kauli ya mwanaye, alijiuliza kama mwanaye atasimamia uamuzi ule angeuweka wapi uso wake. Wasiwasi wake huenda amemfumania Colin na mwanamke mwingine na kuamua kuvunja uchumba.
Bado aliona kama ni hivyo linazungumzika kwa vile wote wamejuana wakiwa tayari wanayajua mapenzi. Alinyanyuka kitandani na kutoka kwenda kwa mwananaye kupata ukweli kwani alikuwa amechanganyikiwa sana. Alitoka taratibu taa ya sebuleni zilikuwa zimezimwa kulikuwa na hali ya ukimya kutokana na watu wote kuwa wamelala.
Hakutaka kuwasha taa ya sebuleni alitembea taratibu hadi chumba cha Mage alipotaka kuushika mlango alimsikia mwanaye akizungumza na simu alitulia ili asikilize anazungumza nini na nani. Alimsikia mwanaye akisema:
“Kama hivyo nimeisha litibua yote kwa ajili ya mapenzi yangu mazito kwako, kama umemejitoa muhanga kwa ajili yangu nami sina budi kujitoa kwa ajili yako. Najua uamuzi wangu utamchanganya mama na yule mchovu lakini wewe ni zaidi yao wote nakupenda sana zaidi ya kukupenda.
“ Nipo radhi vyote duniani viondoke ubakie peke yako, please mpenzi usinitende kosa lako ni mauti yangu, nashukuru kwa kujali mapenzi yangu kwako. Asante mpenzi wangu naomba ulale usingizi mororo huku ukiniota. I love you and i need you in all my life, mmmmwa.”
Mama Mage alijiuliza mwanaye anazungumza na nani, wazo lake lilipelekea labda ni Hans, lakini hakukubaliana nalo kutokana na maumivu aliyoyapata mwanaye kutoka kwa Hans na familia yake. Wazo lilielekea huenda kapata mpenzi mwingine ambaye kamzidi kete Colin.
Alishangaa mabadiliko yake ya ghafla kwani mpaka saa tatu kasoro usiku mwanaye alikuwa na kimuhemuhe cha kwenda kwa mchumba wake Colin na kumuhimiza kuwahi. Lakini aliporudi alikuwa mambo yamebadilika ghafla kama saa sita mchana ugeuke kiza totoro na watu wasionane.
Alipata wazo la kwenda chumbani kwa Sofia msichana wa kazi kumuuliza kuna kitu gani kilitokea kabla ya kurudi na kusababisha hali ile. Alikwenda kugonga chumba cha msichana wa kazi aliyeamka.
“Abee mama.”
Mama Mage aliingia chumbani bila kusema kitu kisha alirudisha mlango na kumuuliza kwa sauti ya chini.
“Sofi.”
“Abee mama.”
“Eti nilipotoka, Mage alitoka?”
“Hapana hajatoka,” Sofi alikataa huku akitikisa kichwa.
“Colin alikuja?”
“Hapana.”
“Nani alikuja.”
“Mmh! Da’ Brenda.”
“Brenda si alikuja mchana na kuondoka na Mage?”
“Hata usiku alikuja na kwenda chumbani kwa dada Mage kisha walitoka nje baadaye nilimuona dada Mage akirudi peke yake huku ameshikilia kitambaa mkononi kama anafuta machozi lakini sikumtilia maanani.”
“Mmh! Sasa nimeelewa,” mama Mage alisema huku akishika mikono kiunoni.
“Kuna nini mama?” Sofi alishtushwa na kauli ya mama Colin.
“Kawaida, ila nimeelewa,” alisema huku akitoka chumbani kwa Sofi na kurudi chumbani kwake.
Alipoingia chumbani alichukua simu na kumpigia Brenda ili amwambie alimpeleka wapi mwanaye mpaka kugeuka ghafla na kumtia gharama na fedheha kubwa. Baada ya kupiga simu ya Brenda ulipokelewa upande wa pili.
“Haloo mama.”
“Brenda za saizi?”
“Nzuri mama.”
“Eti Brenda kumetokea nini mama?”
“Kuhusu nini?”
“Ulimpekeka wapi Mage?”
“Sijampeleka popote nilitoka naye nje mara moja akarudi ndani kujiandaa kwenda kwa shemeji Colin.”
“Unajua wewe ndiye umevunja ndoa ya Mage?”
“Kivipi mama?” Brenda alishtuka.
“Umemwambia nini Mage mpaka akakataa kuolewa, gharama za harusi utazilipa wewe?”
“Mama kwa nini unasema hivyo?” Brenda alishtuka.
“Haiwezekani kuja wewe ghafla na Mage kubadili uamuzi wa kuolewa.”
“Mamaa! Hebu subiri,” Brenda alikata simu na kumpigia Mage.
Baada ya kuita kwa muda simu ilipokelewa.
“Haloo Brenda afadhali umenipigia.”
“Mage kuna nini?”
“Nimevunja uchumba na Colin.”
“Mungu wangu! Kwa nini tena?”
“Nimepata tiba ya moyo wangu.”
“Mage unajua lawama zote nabebeshwa mimi?”
“Brenda walaa hilo halikuhusu, kila kitu kitaeleweka, nitazungumza na mama muda si mrefu.”
“Mage ndugu yangu naomba usivunje ndoa yako utaniweka mahari pabaya,” Brenda alimbembeleza Mage.
“Nitaolewaje na mtu nisiyempenda?”
“Mage leo yamekuwa hayo? Si ni wewe ndiye ulinihakikishia Colin ndiye tiba ya moyo wako?”
“Hakuwa tiba bali dawa ya kupunguza maumivu lakini Hans ndiye tiba kamili, kama alijitoa kwa ajili yangu nami sina budi kujitoa kwa ajili yake.”
“Colin anajua?”
“Hajajua ila sitaki mtu yeyote amwambie nitamwambia mimi mwenyewe nina imani tutaelewana tu.”
“Mmh! Mbona najuta kiherehere cha kumleta Hans!” Brenda alijua yeye ndiye chanzo cha yote yaliyotokea.
Alijiuliza Hans alimweleza Mage kitu gani kilichomfanya abadili ghafla uamuzi wa kuolewa. Aliamua kumpigia simu Hans kutaka kujua aliwambia nini Mage mpaka kuamua kuvunja uchumba wakati kila kitu kilikuwa kipo katika hatia za mwisho. Lakini simu ya Hans haikuwa hewani, alijikuta akijiuliza atamwambia nini mama Mage mpaka amwelewe. Usiku ulikuwa mrefu kwa Brenda na kujuta kwa nini alimkubalia Hans kwenda kuonana na Mage.
***
Siku ya pili Mage aliamka asubuhi na kuoga na kujipamba kisha alitoka, alimkuta mama yake amekaa sebuleni ameshika tama.
“Mama vipi mbona hivyo?” alimuuliza huku akijilazimisha kujenga tabasamu.
“He! Safari ya wapi?”
“Naenda kwa Colin mama.”
“Kweli?” mama yake alishtuka.
“Ndiyo mama.”
“Haya wasalimie.”
“Sawa mama, ila sitakuwa hewani kwa siku mbili.”
“Kwa nini?”
“Utajua nikirudi.”
“Kwani mnakwenda wapi?”
“Itajua tu mama.”
“Haya mwanangu safari njema.”
“Asante mama.”
Mage kabla ya kutoka alimbusu mama yake na kuelekea nje na kumfanya mama yake kumsindikize kwa macho kisha alinyanyua mikono juu kumshukuru Mungu kwa kuweza kumbadili msimamo wake. Alijiuliza kama angesimamia msimamo wake kwake ingekuwa aibu na fedhea ya kuvunjika harusi aliyoiandaa kwa nguvu kubwa.
Ilikuwa toka aamke alikuwa hajaoga zaidi ya kukaa sebuleni kutafuta njia ya kuinusuru ndoa ya mwanaye ambayo aliamini ni muujiza pekee ndiyo wenye kuiponya kwa kuamini nguvu za kibinaadamu zisikingeweza. Alinyanyuka na kwenda kuoga ili apate kifungua kinywa.
Mage alikwenda kuchukua gari aina ya Prado nyeupe na kutoka kuelekea nyumbani kwa kina Colin. Aliendesha gari taratibu tofauti na siku zote aliendesha kwa fujo. Alirudisha kukumbuka ya muda mfupi ya picha ya mama yake aliyokuwa amekaa ameshika tama kuonesha kabisa uamuzi aliochukua umemchanganya sana na kumnyima raha.
Alipeleka macho yake kwenye simu yake iliyokuwa pembeni yake na kuichukua alitafuta namba ya Hans na kumpigia. Iliita kidogo na kupokelewa.
“Haloo ma adorable.”
“Vipi umeamka salama?” alimuuliza kwa sauti iliyopooza.
“Mmh! Naweza kusema nimezaliwa upya nimelala usingizi mtamu nilioukosa muda mrefu.”
“Nashukuru kama ni hivyo.”
“Mmh! Niambie moyo wangu?”
“Hans nilitaka kukujulisha kuwa sitakuwa hewani kwa siku mbili ila ya tatu nitarudi kama kawaida.”
“Kuna nini?”
“Utajua baadaye.”
“Upo wapi?”
“Nimetoka mara moja.”
“Sawa nimekuelewa mpenzi.”
“Basi nikutakie siku njema yenye furaha.”
“Na kwako pia.”
Mage alikata simu na kumpigia shoga yake Brenda, haikuchukua muda ilipokelewa upande wa pili.
“Vipi shoga?”
“Poa, za asubuhi?”
“Nzuri tu.”
“Nilitaka kukujulisha sitakuwa hewani kwa siku mbili.”
“Kwa nini shoga halafu mbona leo kama hujachangamka?”
“Aah! Nipo katika kipindi kigumu lakini nitakivuka tu japokuwa najua jasho la damu lazima litoke.”
“Bado unamsimamo uleule?”
“Utajua baada ya siku mbili.”
“Sasa upo wapi?”
“Nakwenda kwa Colin.”
“Loh! Afadhali shoga maana mimi mwenyewe nilikuwa sina amani moyoni mwangu.”
“Basi ndiyo hivyo tutawasiliana kesho kutwa.”
“Na kesho?”
“Sitakuwa hewani kwa siku mbili.”
“Mmh! Umeamua, safari njema msalimie sana shemu Colin mwambie nimemmisi.”
“Salamu zimefika.”
Baada ya Mage kukata simu shoga yake Brenda alitipa simu kwenye kochi na kushika kifua na kusema:
“Ooh! Afadhali Mage kabadili uamuzi sijui kama mama yake angenielewa.”
Mage baada ya kumaliza kuzungumza na Brenda aliweka simu pembeni na kuiweka mikono yote juu ya usukani na kukanyaka mafuta kuelekea nyumbani kwao Colin. Macho yake yalitulia kutazama mbele huku machozi yakijaa taratibu katika macho yake. Alijikuta akisema kwa sauti kama anazungumza na mtu.
“Mapenzi haya! Kwa nini Mungu uliumba mapenzi kwa nini yakuwa kila siku yanachukua furaha yangu badala ya kunifariji?”
Alichukua kitambaa pembeni yake alifuta machozi na kuendelea na safari. Alisimamisha gari mbele ya geti la nyumba ya kina Colin, geti lilifunguliwa na kuingia ndani. Aliliweka kwenye maegesho kabla ya kuteremka alivaa miwani ya jua ili kuficha macho yake na kuteremka

ITAENDELEA
 
SEHEMU: 14
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500.
ILIPOISHIA:
Alichukua kitambaa pembeni yake alifuta machozi na kuendelea na safari. Alisimamisha gari mbele ya geti la nyumba ya kina Colin, geti lilifunguliwa na kuingia ndani. Aliliweka kwenye maegesho kabla ya kuteremka alivaa miwani ya jua ili kuficha macho yake na kuteremka.
SASA ENDELEA...

Wa kwanza kuonana naye alikuwa mama Colin ambaye alimkimbilia na kumpokea Mage.
“Wawaooo mkwe wangu.”
“Waawoo mama, Shikamoo.”
“Marahaba.”
“ Colin yupo wapi?”
“Yupo chumbani kwake, aliniambia utakuja.”
“Ndiyo mama.”
“Vipi unaendeleaje?”
“Namshukuru Mungu nipo sawa.”
“Haya mwanangu kamuone mwenzio maana alikuwa na kimuhemuhe hasa baada ya kusikia unaumwa.”
“Sawa mama.”
Mage alielekea chumbani kwa Colin, mlango ulikuwa umerudishwa aliusukuma bila hodi na kuingia ndani alimkuta Colin akibadika picha kubwa ya rangi ukutani wakiwa ufukweni wamelaliana chini ya picha ule kulikuwa na maneno ya rangi nyekundu yaliyokuwa yanasomeka, kwa juu yaliandikwa: ASANTE MUNGU KWA KUNIPA MKE MWEMA na chini kuliandikwa MAGRETH NAKUPENDA ZAIDI YA KUPENDA .
Mage aliposoma yale maneno na kuiona ile picha moyo ulimuuma na kuangua kilio cha sauti, Colin alishtuka kusikia sauti ya mchumba wake, alipogeuka alimuona Mage amesimama akiwa ameshika kifua chake. Aliteremka haraka kitandani alipokuwa amepanda kubandika picha ile kubwa na kumfuata alipokuwa amesimama na kumkumbatia kwa kumlazia kifuani.
“Vipi mpenzi kipi kinakuliza?”
“Najua nina mtihani mzito moyoni mwangu lakini Mungu atanipa nguvu na nitashinda.”
“Kuna nini mbona unanitisha?”
“Kawaida tu, Colin naomba ujiandae tuna safari.”
“Ya wapi?”
“Surprise.”
“Waawoo!” Colin alisema huku akimkumbatia Mage.
Kwa vile alikuwa ametoka kuoga alibadili nguo na kumweleza Mage.
“Nipo kamili mpenzi.”
“Chukua na nguo nyepesi za kupumzikia.”
“Tunaenda wapi?”
“Utajua tu.”
Walichukua begi dogo na kuongozana hadi sebuleni, walimkuta mama Colin akimuelekeza jambo msichana wa kazi alipowaona aliacha na kuwageukia.
“Jamani wapendanao safari ya wapi?”
“Tunatoka kidogo,” alijibu Mage.
“Haya mwende salama.”
“Asante mama, ila hatutakuwa hewani kwa siku mbili.”
“Kwa nini?”
“Utajua tu,” Mage alijibu
“Kwa hiyo leo hamrudi?”
“Ndiyo mama tutarudi kesho kutwa.”
“Mmh! Haya wanangu nawatakieni safari njema,” mama Colin aliwakumbatia wote na kuwabusu kisha aliwasindikiza nje hakuondoka mpaka walipotoka nje ya geti ndipo aliporudi ndani.
***
Baada ya gari kuingia barabarani Mage alimgeukia Colin aliyekuwa ametulia na kumwambia.
“Colin zima simu yako.”
“Kwa nini?”
“Sitaki uwasiliane na mtu yeyote zaidi yangu.”
“Sawa mpenzi,” Colin alizima simu yake.
“Zima na yangu.”
Colin alichukua simu ya Mage ni kuizima, safari iliendelea, gari lilielekea barabara ya Kawawa mpaka Mwenge na kukata mtaa wa viwanda mpaka njia panda ya Kawe. Mage hakukunja alinyoosha na kutokea Afrikana alikata kulia kuelekea Tegeta. Colin hakuhoji gari lilivuka Tegeta likaingia Boko likavuka Bunju na kuitafuta Bagamoyo
Ndani ya gari muziki laini uliendelea kuunguruma kila mtu akiwa kimya kutokana na mwendo wa kasi aliokuwa akienda nao Mage.
Alisimamisha gari mbele ya hoteli ya Oceanic Bay, baada ya kusimamisha gari alimgeukia Colin aliyekuwa ametulia akiuangalia umahiri wake kuendesha gari.
“Nina imani tuna siku mbili ya kila mmoja kumaliza hamu zake kwa mwenzie.”
“Mage mpenzi siku zote kitamu hakiishi hamu, penzi lako kwangu siwezi kulikinai.”
Mage hakuongeza neno alimshika mkono na kuongozana naye mpaka mapokezi na kukodi chumba kizuri kwa siku tatu.
“Mage si umesema tunarudi kesho kutwa.”
“Tatizo nini hata tukikaa mwaka kuna mtu anatudai?”
“Hakuna.”
Baada ya kupata chumba walikwenda chumbani kwao, chumba kilikuwa kizuri sana.
“Colin unakionaje chumba hiki?”
“Kizuri sana, unaonaje fungate yetu tuje tuifanye huku.”
“Tutaangalia muda ukifika.”
Baada ya kuoga kwa vile muda ulikuwa umekwenda walivaa nguo nyepesi na kwenda hotelini kupata chakula cha mchana. Kisha walihamia ufukweni kupata upepo wa bahari, muda mwingi Colin alikuwa mtu mwenye furaha kuwa karibu na mpenzi wake mchumba wake mkewe mtalajiwa.
Lakini Mage alionekana kulazimisha furaha kutokana na siri nzito iliyokuwemo moyoni mwake. Baada ya kutosheka na upepo wa bahari walirudi ndani na kujilaza kitandani mkao wa mahaba huku wakiangalia video. Colin muda mwingi alijiuliza kwa nini wamezima simu ilibidi amuulize Mage.
“Mpenzi kwa nini tusiwashe simu hata kwa muda?”
“Colin hizi ni siku zetu ambazo ni muhimu kwetu sitaki kusikia chochote masikioni kwangu zaidi ya sauti yako.”
“Nimekuelewa mpenzi wangu.”
“Colin,” Mage alimwita.
“Naam mpenzi.”
“Hivi mfano uwe nyumbani kwenu mara mama yangu anakupigia siku kukueleza nimefariki utafanyaje?”
“Mage hayo ni maneno gani, umesema tupo kwenye furaha sasa maneno ya kifo yanafuata nini?”
“Najua hapa siyo sehemu yake lakini naomba unijibu.”
“Kwa kweli nitachanganyikiwa naweza hata kufa.”
“Hivi umpendaye akifa kuna sababu ya kuchanganyikiwa ikiwa baada ya mazishi yake kuna wengine wapo pengine zaidi ya yule aliyeondoka?”
“Ni kweli, lakini kinachomtesa mtu ni mazoea si uzuri wa sura wala umbile la mtu.”
“Kwa mfano mi nikisema sikupendi utafanyaje?”
“Nitafanyaje nawe umeamua.”
“Hutaumia?”
“Nitaumia lakini nitafanya nini, lakini naamini mimi na wewe tunapendana hakiwezi kutokea kitu kama hicho.”
Mage alibadili mazungumzo kwa kumshika mkono Colin na kuelekea naye bafu kuoga, waliingia kwenye jakuzi na kuoshana kisha walirudi kitandani kuburudisha mioyo yao. Mage alimpa penzi Colin penzi shatashata ambalo lilimrusha akili naye alijibu mashambulizi kitu kilichomfanya Mage aangue kilio na kumshtua mpenzi wake.
“Vipi mpenzi mbona unalia?”
“Colin sina jinsi lazima iwe.”
“Iwe nini?”
“Utajua tu.”
Mage alimvamia Colin na kuendelea kustarehe bila kuliweka wazi lililikuwa likimliza, alijitahidi kurudi katika hali yake ya kawaida ya uchangamfu na kumfanya Colin asahau kitendawili chake.
Walikaa kwenye hoteli ile kwa siku mbili huku wakiongozana kama kumbikumbi huku kila mmoja alijua watu wale wanapenda mapenzi ya dhati. Siku iliyofuata majira ya mchana baada ya kupata chakula walipumzika kwa muda kabla ya kurudi mjini. Mage akiwa amejilaza pembeni ya Colin alijinyanyua na kumgeukia mpenzi wake na kumwita.
“Colin.”
“Naam mpenzi.”
“Hivi unajua kwa nini toka juzi sijakuita mpenzi?”
“Sijajua.”
Mage alitulia kwa muda akimtazama Colin usoni mara machozi yalianza kumtoka, Colin alizidi kumshangaa mpenzi wake kwani toka wamefika Bagamoyo ameshindwa kumwelewa.
“Colin, “ alimwita tena.”
“Naam.”
“Najua unanipenda.”
“Sana.”
“Najua kabisa nitakachokueleza kitakushtua na kukumiza moyo wako sawa na kuupasua bila ganzi kwa kisu butu. Lakini ukweli utabakia palepale sina jinsi, nina imani penzi la kweli huwa alitengenezwi na mtu bali mhusika mwenyewe.”
“Ni kweli kabisa.”
“Unajua penzi letu halikuwa la sisi kupendana bali kutengenezwa na wazazi wetu?”
“Najua lakini tulipoonana kila mtu alimpenda mwenzake.”
“Unajua hiyari yashinda utumwa?”
“Najua.”
“Nina imani nilikueleza jinsi mapenzi yalivyoniumiza.”
“Ndiyo.”
“Na aliyesababisha nilikueleza.”
“Ndiyo.”
“Basi napenda kukueleza hili ambalo moyo wangu unavuja damu kwa maumivu kwa vile sikupenda liwe kwa vile hiyari yashindwa utumwa, lazima niseme ukweli wa moyo wangu kuwa Colin nilikupenda lakini Hans nilimpenda zaidi. Hans baada ya kufiwa na mkewe amerudi kwangu na yupo tayari kutimiza ndoto yetu tuliiweka muda mrefu,” Mage alimeza mate huku akiendelea kutokwa machozi kisha aliendelea kuzungumza kwa sauti ya chini yenye mchanganyiko na kilio.
“Najua kauli yangu itakumiza lakini ndiyo ukweli wenyewe, Colin nimeamua kwa hiyari na mapenzi yangu nikiwa na akili timamu kuuvunja uchumba wetu kwa hiyo harusi yetu haitakuwepo tena, Penzi tamu tulilopeana ndilo la mwisho tukitoka hapa kila mtu ashike hamsini zake.”
“Mage,” Colin alimwita kwa sauti ya chini.
“Abee.”
“Unasema kweli au unatania?”
“Nasema kweli,” Mage alijibu huku akikaza macho.
“Hapana acha utani Mage unaweza kuniua kwa presha.”
“Huwezi Colin, wewe ni mwanaume umeubwa kukabiliana na matatizo, kumbuka amenikuta tayari nimeishaanza uhusiano na mtu ambaye ndiye aliyenionjesha dunia ya mapenzi na aliniahidi kunioa. Toka niachane naye sikuwahi kuwa na mwanaume mwingine zaidi yako kilichotokea ni kutoelewana lakini sasa hivi tumeelewana na mipango yetu lazima itimie.”
“Mage japo Hans ndiye alikuonjesha dunia ya mahaba lakini alikutenda, Mage nimekukosea nini mpaka uchukue uamuzi mzito na wa kikatili kama huo?” Colin aliuliza huku machozi yakimtoka.
“Hujanikosea kitu, hata mimi nilikupenda sana, lakini siwezi kuishi na wewe kwa kujilazimisha au kukufanya kama bodi lakini injini awe Hans. Colin, Hans nampenda sana aliniudhi na kuumiza moyo wangu lakini siku aliponiomba msamaha moyo wangu aliyeyuka kama bonge la mafuta kwenye kikaango cha moto. Siwezi kuwa nawe kimwili wakati mawazo yangu yote yapo kwa mwanaume mwingine.
“Narudia naomba ukubaliane na uamuzi wangu wa kuvunja uchumba tukiwa na mioyo safi, kuachana kwetu kusijenge uadui tuendelee kuwa marafiki kwenye harusi yangu uje ya kwako nije.”
“Mage uamuzi uliochukua ni kuupasua moyo wangu bila ganzi, naomba urudishe moyo nyuma mpenzi wangu, bora ungeninyang'anya kila kitu katika mwili wangu na kuniachia moyo wako ni muhimu kuliko chochote duniani japo nipo nawe kwa muda mfupi lakini nimekuzoea sana.”
“Siwezi kuishi mapenzi ya kuigiza niache nimpende aliyechaguliwa na moyo wangu.”
"Mage siwezi kukubali kirahisi namna hiyo nasema sikubali, lolote na liwe nasema huondoki kama sio nitamwaga damu ya mtu," Colin alisema huku akisimama.
"Colin mapenzi si lazima usisababishe nikakasilika na kutoa maamuzi yatakayokuumiza mara mbili."
"Nasema sikubali...toa uamuzi wowote kumbuka nimekutoa kwenye mateso ya kutendwa , leo nikuache uondoke hivihivi sikubali," Colin alikuwa mkali.
"Colin nasema hivi kila usemalo ni kweli tupu na una haki yoyote ya kufanya lakini kumbuka penzi alilazimishwi nina imani umenielewa kuwa mstaarabu tuachane kwa usalama."
Mage alinyanyuka na kumsogelea Colin aliyekuwa ameinama akilia na kumpigapiga mgongoni.
"Sweet naomba usilie mwanaume kaumbwa kukabiliana na matatizo hili ni moja wapo.”
Colin alinyanyuka kama mbogo na kumsukuma Mage aliyeanguka chini huku akibwata.
"Muongo mkubwa mnafiki wewe unanipaka mafuta kwa mgongo wa chupa eti sweet!"
"Huwezi amini Colin nakupenda sana japo Hans nampenda zaidi, nipo yatari kulipa gharama zote za maandalizi ya harusi yetu, pia hata kulipa gharama zozote ili kuhakikisha nawe unakuwa na mke atakayeziba pengo langu."
Mage pamoja na kusukumwa hakukasirika akiamka pale chini alipoanguka Colin hakumjibu neno lolote zaidi ya kuinama huku akilia. Mage alimshika mkono na kunyanyua, alimtazama kwa macho yaliyojaa machozi na kusema kwa sauti ya chini.
“Colin nisamehe sana siwezi kuwa mnafiki mapenzi nayajua, nipe ruksa mpenzi wangu. Nilikuja huku ili tupate muda wa kulizumgumza hili, sikutaka tulizungumze juujuu. Nakupenda lakini sitaki nikutese kwa kukunyanyasa kimapenzi kwa vile mapenzi nayajua yanavyoumiza.”
Colin alitulia huku akimtazama Mage aliyekuwa akitia huruma, alijiona mjinga kulazimisha mapenzi. Alikohoa kidogo na kusema:
“Sawa nimekuelewa.”
“Nashukuru.”
“Kuna la zaidi?” Colin alimuuliza Mage.
“Hakuna.”
“Tunaweza kuondoka.”
Walichukua vitu vyao na kuelekea nje kwenye gari ili warudi mjini.
***
Cecy baada ya kutoka twisheni alisimama chini ya mti kuagana na shoga yake huku wakijikumbusha baadhi ya mada walizopewa wakasome nyumbani. Alikuwa amepiga hatua kubwa katika kusoma na kundika hata kuzungumza lugha ya kingereza baada ya kusoma kwa uchungu mkubwa.
Siku zote aliamini kumkosa Colin kulitokana na kukosa elimu, kwake umaskini hakuuona sababu kama ungekuwa na elimu yake ambayo hata mama Colin angeiheshimu. Toka aanze kusoma alionekana ndiye mwanafunzi aliyetaka kujua lugha kuisoma kuiandika na kuizungumza.
Japokuwa hakukijua sana lakini aliweza kumsikia mtu na kumwelewa hata kumjibu mawili matatu. Ile ilimpa kiburi cha kuzungumza muda wote hata alipokosea hakujisikia vibaya kwa vile alielekezwa. Baada ya kujadiliana na shoga yake alisogea mbele kuelekea njia ya kwao japo palikuwa mbali kidogo lakini hakujali umbali ule kutembea kwa miguu kwa vile alikuwa akitafuta kitu.
Siku zote aliingia darasa la mchana kwa vile asubuhi alikuwa akienda kwenye biashara zake. Ada ya mwanzo alitumia fedha aliyoachiwa na Colin siku aliyompeleka kwao na kuwaacha kwenye mataa kwa ahadi tamu ya kuyabadili maisha yao. Alikumbatia daftari lake na kutembea taratibu kukifuata kichochoro cha kuingilia njia ya mkato. Aliangalia saa yake ilimuonesha ni saa kumi na moja na nusu jioni.
Alishtushwa na sauti ya gari aina ya Prado jeupe new model lililosimama nyuma yake. Alipogeuka aliona msichana akiteremka kwenye gari huku akibwata kwa sauti kuonesha anazozana na mtu ndani ya gari. Alipomwangalia aligundua ni Mage mwanamke aliyezima ndoto zake za kuwa mke wa Colin. Alisimama nyuma ya mti kumwangalia, alimuona akisema kwa sauti:
“Wewe mtu gani unayelazimisha mapenzi nimekueleza ninaye ninayempenda hutaki kunielewa. Naomba uteremke kwenye gari langu, siwezi kutembea na mtu asiyeelewa. Sasa hiyo elimu uliyosoma inakusaidia nini ikiwa hutambui nini maana ya upendo?
Nasema teremka la sivyo nitakuachia gari niondoke zangu.”
Baada ya muda Cecy alishtuka umuona mwanaume aliyekuwa akiambiwa vile ni Colin, baada ya kuteremka kwenye gari kinyonge na alisogea pembeni na kusimama bila kujua nyuma yake yupo Cecy.
Cecy roho ilimuuma kuona mtu ampendaye akidhalilishwa vile, Colin alionekana machozi yakimtoka kitu kilichozidi kuumiza moyo wake na kushangaa watu ambao muda si mrefu walitegemea kufunga ndoa lakini ajabu mwanamke kutoa maneno makali kama yale ya kumdhalilisha mumewe mtalajiwa.
Alitulia aione sinema ile inaishaje kwa kujificha nyuma ya mti ili wasimjue, baada ya muda alisikia sauti ya Colin.
“Mage pamoja na hayo lakini kumbuka tumepanga nini mimi na wewe katika maisha yetu?”
“Hainihusu! Nimekwambia mapenzi siyo lazima, ninaye nimpendaye wewe nikuweke wapi?”
“Mage...Mage.”
“Jina langu, kwa heri.”
Mage alisema huku akielekea kwenye gari ili aondoke na kumuacha Colin aliyekuwa bado amesimama akilia. Kitendo kile kilimuumiza sana Cecy bila kujitambua alitoka nyuma ya mti na kwenda kumvamia Mage kwa nyuma na kuzivuta nywele zake na kuanza kumshushia kipigo.
Colin alishtuka kumuona Cecy eneo lile na kujiuliza ametokea wapi, ilibidi amuwahi kumtoa juu ya Mage aliyekuwa akipiga kelele za maumivu.
“Cecy muache.”
“Hawezi kukudhalilisha kiasi hicho kama umalaya wake apeleke mbele,” Cecy alisema huku akitweta kwa hasira akitaka kujitoa mikononi mwa Colin ili akamfunze adabu Mage.
“Colin have you sent this bastard to come and attack me?“ (Colin umemtuma chokoraa huyu aje anipige?) Mage alibadili lugha na kusema huku akisikilizia maumivu.
“No, baby, I’m also suprised as to where she came from.” (Hapana mpenzi hata mimi nashangaa sijui katokea wapi.) Colin alijitetea.
“Colin, what type of a man who forces to be loved, what’s wrong with you? Let her go!” (Colin wewe ni mwanaume gani unang’ang’aniza mapenzi una kasoro gani mwacha aende) Cecy safari hii naye alivunja yai na kufanya Colin abakie mdomo wazi.
“Colin thank you, stay with that bastard whom you sent to beat me.” (Colin asante, baki na huyo chokoraa uliyemtuma kunipiga) Mage alisema huku akielekea kwenye gari.
Colin aliyekuwa amemshika Cecy ili asiendelee kumuadhibu Mage, alimuachia na kumfuata Mage kumuomba msamaha.
“Please Maggie excuse me, do not be so cruel to me.” (Tafadhali Mage rudisha moyo nyuma usinifanyie ukatiri huo.)
Alipopiga hatua ili amfuate Mage kwenye gari, Cecy alimfuata na kumzuia kwenda kuomba msamaha.
“Colin...Colin... why do you cling to her, how good is her; do you love her for her riches or behaviour? (Colin... Colin... unamng’ang’ania ana sifa gani, unampendea utajiri au tabia?)
Colin alijitahidi kujitoa mikononi mwa Cecy lakini alikamatwa madhubuti, wakati huo Mage alikuwa ameingia kwenye gari na kutupa nje begi la Colin na kuondoa gari kwa kasi na kumuacha Colin akilisindikiza kwa macho. Baada ya gari kupotea machoni alitulia huku machozi yakiziba macho.
Cecy roho ilimuuma kuona mtu ampendaye akitokwa machozi kwa ajili ya kulilia penzi lisilokuwepo.
“Colin, mbegu ya penzi humea kwenye moyo wenye rutuba ya mapenzi, kwa nini unalazimisha kupanda mbegu yako kwenye mawe? Kwani nini unakuwa kenge asiyetaka kuelewa. Mshukuru Mungu msichana wa watu amekuwa mkweli mapema,” Cecy alisema kwa sauti ya kilio iliyomshtua Colin na kurudisha macho kwake.
Pamoja na yote yaliyomtokea alishangazwa na ujasiri wa Cecy msichana aliyeonesha kuumizwa na kitendo cha kudhalilishwa na Mage. Kingine na uwezo wa kuzungumza kingereza kwa ufasaha mkubwa pia kuonekana binti mwenye mvuto kutokana na mavazi na muonekano.
“Cecy,” alimwita kwa sauti ya upole.
“Abee.”
“Kwanza samahani.”
“Ya nini Colin?”

Itaendelea
 
SEHEMU: 15
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500.

ILIPOISHIA:
Pamoja na yote yaliyomtokea alishangazwa na ujasiri wa Cecy msichana aliyeonesha kuumizwa na kitendo cha kudhalilishwa na Mage. Kingine na uwezo wa kuzungumza kingereza kwa ufasaha mkubwa pia kuonekana binti mwenye mvuto kutokana na mavazi na muonekano.
“Cecy,” alimwita kwa sauti ya upole.
“Abee.”
“Kwanza samahani.”
“Ya nini Colin?”
SASA ENDELEA...

“Najua nimekudhalilisha kwa kitendo changu cha kumlilia Mage.”
“Colin siwezi kukulaumu kwa vile ile ni haki yako japo sijui sababu ya yeye kukudhalilisha kiasi kile ikiwa kila kitu kipo katika hatua za mwisho kilichobaki ni ndoa.”
“Mage amerudiana na bwana yake wa zamani na kuamua kuvunja uchumba wetu.”
“Kama amekueleza ukweli sasa unamng’anganiza wa nini?”
“Cecy ni ghafla sana heri kungekuwa na tatizo, kanifuata nyumbani juzi na kunipeleka Bagamoyo, niliamini ana mapenzi yake ya dhati kwangu lakini baada ya kukaa siku mbili za furaha siku ya tatu alinieleza kitu ambacho kimenichanganya sana.”
“Colin ulikuwa unampenda Mage mapenzi ya dhati au tamaa ya macho?” Cecy alimuuliza akiwa amemkazia macho.
“Mapenzi ya dhati.”
“Muongo! Umempenda kwa shinikizo la mama yako, kama amejitoa kwa hiyari yake huoni hii ni nafasi ya kuipanda mbegu yako sehemu sahihi ambayo utaotesha mti mwenye kivuli na matunda matamu?”
“Cecy kwanza unatoka wapi muda huu?”
“Shule.”
“Hongera.”
“Siwezi kusema asante.”
“Kwa nini?”
“Mpaka ufute machozi yangu.”
Colin alitoa kitambaa mfukoni ili amfute Cecy machozi, lakini alishikwa mkono na kumfanya aulize:
“Vipi Cecy mbona unanishika mkono?”
“Si machozi haya Colin.”
“Machozi gani Cecy?” Colin alishtuka.
“Ya moyoni, nimeumizwa sana pia nimedhalilishwa sana juu ya penzi lako, lakini Mungu si mnafiki leo amekudhihilishia mbele ya macho yangu kuwa mke uliyechaguliwa mara ya pili hakuwa mke sahihi bali lilikuwa penzi la kuingiza. Colin mimi ndiye mkeo uliyechaguliwa na Mungu. Nifute machozi yangu kwa kufunga ndoa na mimi si kwa kitambaa cha mkononi bali cha moyoni,” Cecy alisema kwa sauti iliyojaa hisia kali za mapenzi.
“Cecy nimekuelewa naomba unipe muda.”
“Muda wa nini wakati nafasi yangu imerudi tena nikiishuhudia si kwa kuhadithiwa na mtu.”
“Nimekuelewa, niache kwanza nifike nyumbani kwanza kumbuka toka juzi sipo nyumbani na ninarudi na taarifa hizo sijajua mama atazipokeaje?”
“Mmh! Sawa, ila pole kwa yote yaliyokukuta.”
“Nashukuru.”
“Colin naomba nikusindikize mpaka kwenu,” Cecy aimwambia Colin huku akiuchezea mkono wake.
“Hapana si unamjua mama atapata la kusema.”
”Nimekuelewa mpenzi.”
Colin alitoa hela mfukoni bila kuzihesabu na kumpatia Cecy, alizipokea na kushukuru kwa kupiga magoti kitu kilichomshtua Colin na kuona tofauti yake na Mage. Siku zote Cecy alikuwa msichana mtiifu ambaye mwanzo alikuwa chaguo la mama yake baadaye alimgeuka baada ya kumuona Mage. Waliagana kila mmoja kukodi gari mpaka kwao.
****
Mage baada ya kuachana Colin alijiendesha gari kwa kasi huku moyo ukimuuma kwa kitendo chake cha kikatili alichomfanyia mtu aliyeonesha mapenzi mazito kwake na aliyemkabidhi moyo wake mzimamzima kutokana na kumuamini. Aliyakumbuka maneno yaliyokuwa kwenye picha kubwa chumbani kwa Colin yaliyosema, moja lilisema: ASANTE MUNGU KWA KUNIPA MKE MWEMA na lingine MAGE NAKUPENZA ZAIDI YA KUPENDA.
Mage alijikuta akilia na kufanya machozi kuziba macho, alisimamisha gari pembeni ya kuendelea kulia kilio cha kwikwi. Aliisikia sauti ya Colin ikisema:
““Mage uamuzi uliochukua ni kuupasua moyo wangu bila ganzi, naomba urudishe moyo nyuma, mpenzi wangu bora ungeninyang'anya kila kitu katika mwili wangu na kuniachia moyo wako ni muhimu kuliko chochote duniani japo nipo nawe kwa muda mfupi lakini nimekuzoea sana.”
Sauti ile ilimfanya apaze sauti na kusema:
“Colin nisamehe sana, najua jinsi gani nilivyokuumiza najuayajua mapenzi yanavyo jeruhi moyo wa mtu. Colin nisamehe sina jinsi nilikupenda lakini Hans ni pumzi zangu siwezi kuiacha nafasi adimu aliyonirudishia.”
Mage aliongea kwa sauti kama anazungumza na Colin, alinamia usukani na kuendelea kulia. Uchungu ulimjaa moyoni kila alivyomfikilia Colin jinsi alivyokuwa akimbembeleza na kutokata tamaa ya kukubaliana na ukweli kwamba penzi limekwisha.
Aliamini asingeweza kuendesha gari kwa hali aliyokuwa nayo kwani hata nguvu zilikuwa zimemuisha kwa ajili ya uchungu uliomjaa moyoni. Aliwaza kumpigia Brenda ili aje amchukue. Wazo lile hakukubaliana nalo kwa vile siku ile alitaka kwanza kuonana na Hans ili amweleze kilichojili ndipo aende nyumbani.
Aliamua kumpigia Hans, alichukua simu ili ampigie ilibidi afute machozi kwanza kuziona ‘kiipadi’ .
Alitafuta jina la Hans na kupiga, hakuita mara mbili ilipokewa upande wa pili.
“Haloo.”
“Hans,” Mage aliita.
“Naam Mage vipi mpenzi?”
“Upo wapi?”
“Nipo Masaki.”
“Naomba uje haraka.”
“Nyumbani kwenu?”
“Hapana nipo njiani karibia na njia panda ya Masaki.”
“Mbona kama unalia?”
“Hans njoo kwanza.”
“Haya nakuja.”
“Kodi bodaboda.”
“Sawa.”
Baada ya kukata simu aliitupia kwenye kiti cha pili na kujilaza kwenye kiti baada ya kukiteremsha kwa nyuma ili kumsubiri Hans.
****
Cecy baada ya kuachana na alikwenda hadi nyumbani kwao, baada ya kusalimiana na mama yake aliingia chumbani kwake na kujifungia chumbani kwake. Baada ya kuvua nguo zote alijifunga upande wa kanga na kujilaza chali kitandani na kuweka mikono nyuma ya kichwa na kutazama kwenye dali. Alitulia kwa muda na kuanza kuyakumbuka matukio yalitokea muda mfupi.
Alijikuta akijilaumu kuingilia mambo yasiyo muhusu, kwani ule ulikuwa ugomvi wa wapendao, lakini kwa upande mwingine aliona kufanya vile ni kulipigania penzi lake. Aliamini ndoa ya Mage na Colin haitakupo na ile ndiyo ilikuwa nafasi yake kukipata alichokipoteza.
Alijiuliza kama ndoa ile itavunjika nani atakuwa mke wa Colin, kwake aliona ana nafasi ndogo hasa baada ya mama Colin kumdharau kutokana na umaskini wake lazima angemtafuta mwanamke mwingine kutoka familia yenye uwezo. Bado alitaka kujua sababu ya Mage kuuvunja uchumba ambao ulibakia siku chache kufunga ndoa kanisani
Moyoni alijiapiza kama ndoa ya Colin na Mage itavunjika basi ataipigania nafasi yake kwa nguvu zake zote. Mama yake alishangaa kumuona mwanaye yumo ndani muda mrefu, alipomfuata alikuta umefungwa. Aligonga mlango huku akiita.
“Cecy mbona umeingia ndani mwaka mzima kuna usalama?”
“Ndiyo mama.”
“Hebu toka basi.”
Cecy alitoka nje, mama yake macho yake hakucheza mbali na uso wa mwanaye na kugundua mabadiliko.
“Cecy upo sawa?”
“Ndiyo.”
“Hapana kuna kitu kimekutokea, si kawaida yako kuingia ndani moja kwa moja bila kunitania na kizungu chako cha kuombea maji.”
“Ni kweli mama kuna kitu kimenitoka kumenichanganya sana.”
“Kitu gani?”
Cecy alimweleza mama yake yote yaliyotokea wakati akitoka twisheni, mama yake alishtuka kusikia kampiga mchumba wa Colin.
“Cecy kwa nini unatafuta balaa, unakumbuka mama Colin alituambia nini?”
“Mama mimi sijavunja ndoa yao bali wenyewe mimi kiichoniudhi ni kashfa aliyokuwa akiitoa yule mwanamke.”
“Colin kasemaje?”
“Amesema amechanganyikiwa kwani maamuzi yalikuwa ya ghafla ila alisema atanitafuta.”
“Mmh! Sawa, basi kaoge ule.”
“Sawa mama.”
Cecy alipitia ndoo ya maji na kuelekea bafuni kuoga na kumuacha mama yake akimtazama mwanaye na kutikisa kichwa aliamini vita ya mapenzi ni nzito kuliko ya kumsaka gaidi mapangoni.
***
Colin baada ya kuachana na Cecy na kukodi gari lililompeleka hadi kwao, aliteremkia nje ya geti na kuingia ndani kwa miguu. Mama yake alikuwa wa kwanza kumuona akiingia sebuleni, lakini uso wa mwanaye haukuonesha furaha kitu kilichomshtua na kuhoji.
“Colin, baba vipi kwema utokapo?”
“Kwema si kwema.”
“Una maanisha nini?”
“Nitakwambia naomba kwa sasa niache nikapumzike kwanza.”
“Kuna nini? Mbona unanitisha?”
“Mama naomba uniache kwanza.”
“Mage yupo wapi?”
“Sijui.”
“Colin ni majibu gani hayo?” mama alishtuka majibu ya mwanaye.
“Mama yangu nipo chini ya miguu yako naomba uniache kwanza.”
“Mmh! Sawa.”
Mama Colin aliachana na mwanaye aliyeelekea chumbani kwake, moyo wake ulimsukasuka alichukua simu kumpigia mama Mage kutaka kujua kuna nini kimetokea. Baadaya simu kuita kwa muda ilipokelewa upande wa pili.
“Haloo dada.”
“Za saa hizi?”
“Nzuri, lete habari.”
“Mage yupo hapo?”
“Mmh! Toka atoke juzi sijamuona kwani vipi?”
“Nimemuona Colin akirudi peke yake huku uso wake ukionesha kuna kitu si cha kawaida, nimemuuliza kuhusu Mage amesema hajui.”
“Mmh! Lazima watakuwa wametibuana, sasa Mage yupo wapi?”
“Hapo ndipo pananichanganya, nilipotaka kumchimba sana Colin ameniomba nimuache kwanza apumzike.”
“Mmh! Lazima watakuwa wametibuana tu.”
“Kwa hiyo hajafika?”
“Bado, akifika atanieleza tatizo, nitakujuza kila kitu.”
“Sawa dada.”
Mama Colin alikata simu, alipogeuka alimuona mwanaye amebeba vitu akitoka navyo nje, hakujua amebeba nini. Alisubiri muda ili akaone mwanaye amechukua nini na anapeleka wapi. Colin baada ya kuachana na mama yake alikwenda chumbani kwake, baada ya kufungua mlango wa chumba chake macho yake yalikutana na picha kubwa aliyoibandika muda mfupi kabla ya kuelekea Bagamoyo akiwa na Mage katika pozi zito la mahaba.
Picha kubwa aliyoibandika ukutani ambayo mwanzo aliiona ni sehemu ya kuongeza furaha ya moyo wake. Lakini siku ile ilikuwa chukizo la moyo wake, alipanda kitandani bila kuvua viatu na kuibandua na kuitupa chini huku akiitemea mate. Alifungua kabati na kutoka picha zote alizopiga na baadhi ya nguo za Mage alizikusanya na kutoka nazo nje kwenda kujichoma moto.
Alipofika nje alizikusanya sehemu moja na kuzimwagia mafuta ya taa na kuzitia moto, mama yake alitokea kwa nyuma yake. Alipotupa jicho aliona moja ya picha ya Mage ikiteketea na moto pia nguo za mkwewe mtarajiwa.
“Colin! Unafanya nini?” alimuuliza kwa sauti mwanaye.
Colin hakujibu kitu aligeuka kumtazama mama yake aliyekuwa ameshangaa mkono kiunoni.
“Colin mwanangu una nini mbona unachoma picha na nguo za mchumba wako?”
“Mama uliponichagulia mchumba ulifanya uchunguzi kwanza.”
“Wa nini?”
“Kama ana mpenzi anayempenda kuliko mimi.”
“Mage hakuna na mpenzi, kwani nini unaniuliza hivyo?”
“Ndiyo maana nikakuuliza ulifanya uchunguzi kabla ya kumchagua kuwa mkweo?”
“Ndiyo, kwani vipi?”
“Tulitaka kujenga nyumba kwenye kiwanja cha watu.”
“Una maana gani?”
“Mage ni mchumba wa mtu.”
“Una maanisha nini kusema hivyo?” mama Colin alishtuka kusikia habari ile.
Colin alimweleza yote yaliyojili Bagamoyo walipokaa siku tatu mpaka kumteremsha njiani na kumtupia mfuko wake. Lakini hakumweleza jinsi Cecy alivyo ingilia ugomvi ule na kipondo alichompa Mage.
Mama yake alibakia macho yamemtoka kama kaona meli ikitembea barabarani. Alishusha pumzi nzito na kubakia akimuangalia mwanaye asipate la kusema.
***
Hans alifika na bodaboda sehemu aliloelekezwa na Mage, aliliona gari limepaki pembeni. Alimuomba dereva wa bodaboda amshushe, aliteremka na kumlipa hela yake na kuchepua mwendo hadi kwenye gari alilolikuta limefungwa vioo vyote. Aligonga kwenye kioo na kumfanya Mage anyanyue kichwa kuangalia, alimuona Hans alifungua mlango.
Hans alishangaa kumkuta Mage macho yamemuiva kwa kulia.
“Vipi mpenzi?” alishtuka kuiona hali ile.
“Hans mpenzi umekuja?”
“Ndiyo mpenzi wangu mbona unalia?”
“Hans nimekaza moyo ili niumeze mfupa nisikupoteze mpenzi wangu.”
“Una maanisha nini?”
“Hii si sehemu sahihi ya mazungumzo, endesha gari tuondoke,” Mage alisema huku akihama kwenye usukani kumpisha Hans.
“Mmh! Safari ya wapi, nyumbani?” alimuuliza huku akimtazama usoni.
“Nyumbani siendi sasa hivi mpaka tumalizane na wewe.”
“Sasa twende wapi?”
“Sea Cliff hoteli.”
“Hakuna tatizo.”
Hans aligeuza gari na kuelekea Masaki, muda wote Mage alikuwa amejilaza kwenye siti baada ya kuilaza kwa nyuma. Hans alisimamisha gari kwenye maegesho ya Sea Cliff hoteli.

ITAENDELEA
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom