Hadithi : Wakili Wa Moyo

Hadithi : Wakili Wa Moyo

SEHEMU: 16
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500.

ILIPOISHIA:
“Hakuna tatizo.”
Hans aligeuza gari na kuelekea Masaki, muda wote Mage alikuwa amejilaza kwenye siti baada ya kuilaza kwa nyuma. Hans alisimamisha gari kwenye maegesho ya Sea Cliff hoteli.
SASA ENDELEA...

“Bebi tumefika,” alimshtua Mage aliyekuwa amefumba macho.
“Kachukua chumba kabisa,” Mage alijibu bila kufumbua macho.
“Sawa.”
Hans aliteremka na kwenda kulipia chumba kisha alirudi kumweleza Mage.
“Tayari.”
Aliteremka na kufunga gari lao kisha waliongozana hadi ndani ya chumba walichokikodi. Mage alipofika alijilaza kitandani macho alitazama juu mikono alilalia kwa nyuma. Pembeni ya macho yake michirizi ya machozi iliendelea kuteremka na kulowesha shuka.
“Vipi bebi?” Hans alizidi alishtuka.
“Hans sijui nikueleze nini uelewe najua jamii itanitenga kwa ajili ya uamuzi wangu wa kuvunja uchumba, wapo watakao niona sina akili lakini anayejua mapenzi ataniunga mkono. Nimekubali kubeba lawama zote za wanadamu lakini niufurahishe moyo wako. Sijui nitakaporudi nyumbani mama atanipokeaje naweza kutengwa na familia kwa uamuzi wangu huu.”
“Kwani huyo jamaa umeisha mwambia ukweli?”
“Siku tatu zilizokuwa naye Bagamoyo nilizitenga mahususi kwa ajili ya kumweleza taratibu kuuvunja uchumba wetu rasmi. Ningeweza kumwambia tu, lakini naheshimu mapenzi yake kwangu.”
“Amepokeaje?”
“Ilikuwa kazi kwelikweli jamaa alichachamaa mpaka kutishia kutoa mtu roho, siyo siri alikuwa amekufa kaoza nina wasiwasi akawa mwendawazimu au kuchukua uamuzi wa kujinyonga.”
“Mi nafikiri mshale umerudi porini haujapotea, Mage nakuapia kwa Mungu kutoujutia uamuzi wako. Kama ulivyojitoa kwangu nami nitazishia mapenzi mara mia ya mwanzo. Nina amani ulikubali kuolewa kwa shinikizo, lakini moyo wako bado ulikuwa kwangu nami unaamini hivyo.
“Hii ni nafasi nyingine ya kuidhihilishia dunia kuwa mimi na wewe tulizaliwa ili tuwe mwili mmoja. Mage nashukuru kuuponya moyo wangu uliokuwa na maumivu ya muda mrefu kulishwa nisicho kitaka, lakini kwa sasa nakula ninachokitaka.”
“Hans naamini unanipenda zaidi ya kunipenda ndiyo sababu ya mimi kukubali kurudi kwako, wasiwasi wangu mkubwa ni familia yako. Hans nitakufa na mtu kila atakayetia mkono katika penzi letu sijali ni nani,” Mage alitoa mkwala mzito.
“Mage nitalipigania penzi letu nakuahidi hakuna atakayeingilia penzi letu, nakuahidi mapenzi ya peponi. Nitayafuta machozi yako kwa kitambaa cha upendo,” Hans alisema huku akimfuta machozi kwa kiganja cha mkono.
“Hans nimejilipua ukinitenda umenimaliza,” Mage alisema kwa sauti ya kilio huku akijitupia kifuani kwa Hans.
“Nakuhakikishi na harusi yetu haitachukua muda mrefu.”
“Kweli Hans?” alimuuliza huku akiyatoa macho yake yaliyojaa machozi kumtazama Hans.
“Toka uliponitamkia matumaini ya kurudi kwangu nilikwenda mbali zaidi ya maandalizi ya ndoa yetu. Nilikuwa nasubiri kauli yako ili nikueleze hili.”
“Wazazi wako je?”
“Niliwaeleza wakasema hawawezi kunichagulia tena.”
“Huoni kama ule wasiwasi wao juu ya kifo cha mkeo utazidi na mimi kuonekana ndiye muhusika?” Mage aliingiwa wasiwasi.
“Nilijua hilo litatokea lakini nimewaeleza mimi ndiye niliyekufuata japokuwa wewe haukuwa tayari kurudiana na mimi hasa baada ya kukutosa kukuoa pia familia yangu kukuingiza kwenye matatizo. Nashukuru walinielewa.”
“Mmh! Sawa, kwako umemaliza sijui kwangu mama atapokeaje.”
“Atakuelewa kwa vile anajua penzi letu lilivyokuwa naamini moyo wake utafurahi kumpata mkwe sahihi.”
“Mmh! Tutaona.”
Walikwenda kuoga kisha walipata vinywaji na kufurahisha nafsi zao walipanga kuondoka pale saa sita usiku.
****
Muda ulizidi kukatika bila Mage kuonekana kitu kilichozidi kumtia wasiwasi mama yake na kujiuliza atakuwa amepitia wapi. Mawazo yake yalimpeleka labda yupo kwa shoga yake Brenda. Lakini aliamini kama aliondoka nyumbani siku tatu zilizopita alitakiwa afike nyumbani kwanza ndipo aende kwa shoga yake.
Alipiga simu ya Mage haikuwa hewani kitu kilichofanya azidi kuingiwa wasiwasi, aliamua kumpigia simu Brenda. Simu iliita kwa muda mrefu bila kupokelewa na kushindwa kuelewa kuna nini ikiwa simu ya Mage haipatikani na simu ya shoga yake haipokelewi.
Akiwa katika ya mawazo simu iliita aliichukua haraka na kupokea ilikuwa inatoka kwa Brenda.
“Haloo mama.”
“Brenda, kwema?’
“Kwema mama, samahani simu ilikuwa mbali kidogo nimekuta umepiga, unasemaje mama?”
“Mage amefika huko?”
“Sijamuona, kwani amerudi?”
“Nasikia amerudi toka saa kumi na moja lakini mpaka sasa sijamuona na simu yake haipatikani.”
“Umemuulizia shemeji Colin si ndiye aliyekuwa naye?”
“Mmh! Ipo kazi.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Basi ngoja nimpigie Colin alinieleze Mage kaenda wapi.”
“Itakuwa vizuri.”
Baada ya kukata simu, alimpigia Colin nayo haikuwa hewani kitu kilichozidi kumweka njia panda asijue nini kinaendelea aliamua kumpigia mama Colin simu iliyopokelewa.
“Haloo shoga kuna habari gani maana mimi mwenyewe moyo hauna raha, toka Colin kafika kajifungua ndani kuna habari gani huko?” mama Colin alipokea na kuanza kumwaga maneno.
“Dada mbona umezungumza mengi, huku mpaka muda huu Mage sijamuona wala simu yake haipatikani. Nimemuulizia kwa shoga yake hajafika, simu ya Colin haipatikani kuna nini katikati mbona sielewi, Colin yupo?”
“Ndiyo.”
“Naomba kuzungumza naye.”
“Sawa.”
Mama Colin alimpelekea simu Colin aliyekuwa amejilaza akitafakari kilichotokea. Mpaka muda ule alikuwa akiona kama ndoto yenye ukweli. Alijiuliza maandalizi yote na matangazo ya sherehe ya kukata na shoka atafanya nini atawaeleza nini jamaa zake aliojitolea kusimamia sherehe ya harusi yao kwa gharama zao.
Rafiki zake wa nje ya nchi aliosoma nao Ulaya nao alijiuliza atawaambia nini ikiwa tayari walikuwa wameshona suti kwa ajili ya sherehe ile na walikuwa tayari kuja nchini ikiwa pamoja na kukodi vyumba kwenye hoteli za nyota tano na malipo yalikuwa tayari.
Kila alivyofikiria alikosa jibu, alitamani hata kumshawishi Mage akubali amuoe hata kwa mkataba wa mwezi mmoja ili jamaa zake wakiondoka waachane lakini wakiwa wamedhudhulia sherehe yake iliyopangwa kutekekeza mamilioni ya fedha. Pamoja na kuujua msimamo wa Mage bado aliamini kupitia wazazi wao anaweza kukubaliana nao.
Lakini wazo la kuendelea kumbembeleza aliona kama kujidhalilisha, alikumbuka kitu. Alinyanyuka kitandani na kwenda kwenye kabati, kabla hajashika mlango uligongwa alipaza sauti ukuuliza.
“Nani?”
“Mimi,” ilikuwa sauti ya mama yake.
“Naam mama, unasemaje?”
”Hebu fungua mlango.”
Alirudi hadi mlangoni na kufungua mlango, alionekana amechoka sana kitu kilichozidi kumuumiza mama yake.
“Mama Mage anataka kuzungumza na wewe.”
“Kuhusu nini?”
“Inasemekana toka ulipoachana naye hajarudi nyumbani na simu yake haipatikani, Colin mwanangu usiwe umemuacha wewe mtoto wa watu akaenda kujinyonga?”
“Mama mimi na wewe tunataniana hasa katika jambo zito kama hili? Inaonekana tukiwa ndani ya uchumba Mage alikuwa na mpenzi wake. Ni wazi lilikuwa shinikizo toka kwa mama yake ili nimuoe lakini ukweli umejidhihili maji hayachanganyikani na mafuta.”
“Hebu kwanza zungumza na mama Mage.”
“Mama nitaongea naye nini?”
“Ulichonieleza.”
Colin alichukua simu ya mama yake ambayo ilikuwa wakati huo imekata na kupiga, baada ya muda ilipokelewa upande wa pili.
“Haloo dada.”
“Hapana ni mimi Colin.”
“Ooh! Baba za siku mbili?”
“Nzuri, shikamoo.”
“Marahaba.”
“Naam mama.”
“Eti baba, mwenzio yupo wapi?”
“Sijui,” alijibu kwa mkato.
“Kwa nini unasema hujui wakati mlikuwa wote siku tatu.”
“Mama, nimeachana na Mage baada ya kunifukuza ndani ya gari lake kama mbwa.”
“Wee! Kwa sababu gani?” mama Mage alishtuka.
“Ana mtu ambaye ndiye aliyemuingiza dunia ya mapenzi na kwa kunitamkia kuwa amevunja uchumba wetu. Kumbembeleza kwangu kumekuwa kero kwake na kuamua kuniteremsha njiani kisha kunitupia mzigo wangu huku akinitolea maneno ya dharau kuwa yupo mwanaume wa ndoto yake.”
“Yupo wapi baba, yule mwanaume alimtenda.”
“Basi ameamua kurudi huko.”
“Sasa atakuwa amekwenda wapi?”
“Si kwa mpenzi wake,”Colin alijibu kwa kifupi.
“Lakini baba linazungumzika, mimi ndiye mzazi wake.”
“Ni kweli wewe ndiye mzazi wake lakini moyo wa uamuzi ampende nani unabakia kwa Mage.”
“Basi baba, niachie kazi hiyo.”
“Wala usisumbuke mwachie uamuzi wake, mapenzi hayalazimishwi japo kaniweka katika wakati mgumu maishani mwangu.”
“Baba…baba..naomba usifike huko nimekueleza niachie mimi naomba kuzungumza na mama yako.”
Colin alimpa simu mama yake aliyekuwa amesimama pembeni yake akiwa amepigwa na bumbuwazi kutokana na kauli za mwanaye.
“Haloo dada.”
“Dada kwanza nisamehe sana kama kweli asemayo Colin ni kweli, yaani nilidhania utani kumbe kweli. Dada naomba uniachie suala hilo.”
“Sawa, nikutakie usiku mwema.”
***
Majira ya saa sita usiku Mage aliingia ndani ya sebule ya nyumbani kwao, alishangaa kumkuta mama yake yupo kwenye sofa akiwa amepitiwa usingizi. Alimsogelea na kumbusu shavuni kitu kilichomfanya mama yake ashtuke. Mbele yake alikuwa amesimama mwanaye Mage.
Kabla ya kusema lolote aliangalia saa kubwa ya ukutani iliyomuonesha ni saa saba kasoro usiku. Hakuiamini aliangalia ya mkononi iliyokuwa sawa na ya ukutani, alimwangalia mwanaye kuanzia juu mpaka chini kama ndiyo siku yake ya kwanza kumuona kitu kilichomshtua Mage.
“Vipi mama?”
“Unatoka wapi?” mama yake alimuuliza kwa sauti kali huku akinyanyuka kwenye kochi.
“Kwani vipi?” Mage alijifanya kushangaa.
“Nijibu unatoka wapi muda huu?”
“Niliporudi nilipita kwa shoga yangu.”
“Nani?’
“Debora, humjui.”
“Kufanya nini?”
“Mama mbona maswali mengi?”
“Kwa nini unanitia aibu, Colin umemfanya nini?”
“Kama alivyokuambia kwa vile alichokueleza niliisha kueleza muda mrefu si kigeni kwako.”
“Kwa hiyo umerudiana na Hans?”
“Ndiyo mama ndiye chaguo la moyo wangu.”
“Wewe si ulikuwa unasema humpendi tena na mapenzi yako yote kwa Colin?”
“Mama ningempenda Colin kama Hans asingekuwepo, kama matatizo yangemtokea nimo ndani ya ndoa nisingeweza kutoka. Lakini amerudi kabla ya ndoa sina budi kumpokea, mama Hans nampenda zaidi ya kupenda nipo tayari kunioa bila mahari.”
“Mage mwanangu nitaweka wapi sura yangu?”
“Ukiwaogopa walimwengu huwezi kufanya jambo la kimaendeleo, watasema mwanzo lakini watanyamaza na kusahau.”
“Mage mwanangu naomba ukalale ili kesho tuzungumze vizuri.”
“Sawa mama.”
Mage alikwenda kulala na kumuacha mama yake akiwa bado yupo sebuleni.
***
Mama Colin usiku ulikuwa mkubwa kwake kila alivyojitahidi kulala usingizi ulikataa, aliamini kabisa Mage hana tatizo bali mwanaye ndiye aliyevunja uchumba na kusingizia Mage ana mwanaume mwingine anayempenda. Akili yake ilimpeleka kwa Cecy tu msichana aliyemuona ndiye tatizo kwa vile tokea awali aliona dalili mbaya.
Alipanga kesho asubuhi kwenda kwa kina Mage ili aweze kuzungumza naye na akimwambia Colin ndiye aliyevunja uchumba basi bleki yake ya kwanza kwa Cecy na kukitia moto kibanda chao na kumfanyia kitu kibaya ambacho hata kisahau mpaka kufa kwake.
Asubuhi alikuwa wa kwanza kufika mbele ya nyumba ya kina Mage na kipiga honi mbele ya geti. Baada ya kufunguliwa geti aliliingiza gari ndani na kwenda kupaki kwenye maegesho. Aliteremka na kuelekea ndani ambako ilionesha bado wamelala baada ya kumkuta msichana wa kazi akifanya usafi, alipomuona alimkaribisha:
“Karibu mama.”
“Asante, mama yupo wapi?”
“Bado yupo chumbani kwake.”
“Kamwite.”
Msichana wa kazi alikwenda kumuamsha mama Mage, baada ya muda alitokea na kushtuka kumuona mzazi mwenzie asubuhi ile.
“Karibu dada.”
“Asante, mmeamkaje?”
“Mmh! Tunamshukuru Mungu.”
“Mage yupo?”
“Yupo chumbani kwake.”
“Ndiye kanileta asubuhi yote hii.”
“Ngoja nikamwamshe.”
“Sawa.”
Mama Mage alikwenda chumbani kwa mwanaye na kumuamsha.
“Vipi mama mbona asubuhi sana?”
“Mama Colin anataka kuzungumza na wewe.”
“Ha! Mbona asubuhi sana?” Mage alishtuka.
“Kwani uliyofanya madogo?”
“Mmh! Haya twende nikamuone.”
Walitoka pamoja hadi sebuleni alipokuwa amekaa mama Colin.
“Shikamoo mama,” Mage alimsalimia mama Colin.
“Marahaba mwanangu, samahani kwa kukurupusha asubuhi.”
“Bila samahani mama.”
“Naomba tuzungumze kidogo.”
“Hakuna tatizo.”
“Na mimi niwepo?” mama Mage aliuliza.
“Kwanza naomba tuzungumze wawili kisha tutazungumza wote.”
Mama Mage aliondoka na kuwaacha mtu na mkwewe, baada ya kubaki wawili mama Colin alimuuliza Mage.
“Mage mwanangu, kuna tatizo gani kati yako na mwenzako?”
“Hakuna tatizo lolote.”
“Mbona anasema kuwa eti wewe umevunja ndoa yenu, ni kweli?”
“Ni kweli.”
“Kama ni hivyo sasa mbona unasema hakuna tatizo?”
“Ndiyo mama hakuna tatizo, ila ni kweli alichokisema Colin.”
“Wewe na yeye nani kavunja uchumba wenu?”
“Mimi.”
“Kwa nini?”
“Mama kabla ya kuwa na Colin nilikuwa na mchumba wangu ambaye kipindi hicho akuwa ameoa. Lakini kabla ya ndoa, alipata matatizo ya kufiwa na mkewe na kurudi kwangu. Kwa vile ndiye aliyekuwa chaguo la moyo wangu aliporudi kuniomba niwe naye wala sikuhitaji ushauri nilimkubalia na ndiye nategemea ufunga naye ndoa na si Colin,” Mage alisema kwa kujiamini.
“Mage, hebu kuwa mkweli naomba usinifiche, Colin amekufanya nini kilichopelekea kuchukua uamuzi huo?”
“Kwa haki ya Mungu hajanifanya lolote baya.”
“Hujamfumania na mwanamke?”
“Walaa.”
“Kwa nini unavunja ndoa yako? Mage nakuahidi kukupa chochote ukitakacho ili tu ukubali kufunga ndoa na Colin.”
“Mama naomba kuwa mkweli wa moyo wangu, japokuwa bado mdogo mapenzi nayajua kwa vile yalinijeruhi. Ningeweza kuolewa na Colin jina lakini mapenzi yangu yangekuwa kwa Hans. Lakini siwezi kufanya kitu kama hicho sitaki kumtesa Colin bila sababu.”
“Hans ndiye nani?”
“Mwanaume wa ndoto yangu.”
“Mmh! Nimekuelewa, basi Mage naomba ubadili uamuzi ili uolewe na Colin.”
“Siwezi kuulazimisha moyo wangu, najua nawavunjia heshima, lakini nayaogopa maumivu ya moyo, niliumia sana wakati Hans ameoa. Kurudi kwake kwangu ni kutibu majeraha ya moyo wangu siwezi…siwezi kubadilika kwa vile nampenda sana Hans,” Mage alisema kwa sauti ya hisia kali.
“Mmh!” mama Colin alishusha pumzi ndefu na kusema:
“Nimekuelewa.”
“Una la ziada?” Mage alimuuliza.
“Mpaka hapo sina, nikuache upumzike.”

Itaendelea
 
SEHEMU: 17
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500.

ILIPOISHIA:
“Mmh!” mama Colin alishusha pumzi ndefu na kusema:
“Nimekuelewa.”
“Una la ziada?” Mage alimuuliza.
“Mpaka hapo sina, nikuache upumzike.”
SASA ENDELEA...

“Sawa mama msalimie Colin, naendelea kumuombea naye apate mke mwenye mapenzi naye ya kweli.”
“Amen.”
Mama Colin alimwita mama Mage amuage, baada ya kuja alimweleza:
“Dada nikukimbie.”
“Jamani, mbona haraka mmeelewana na mwanao?”
“Tumeelewana na nimemuelewa vizuri sana.”
“Basi nikutoe.”
Waliongozana kutoka nje walipofika nje mama Mage alitaka kujua kama mwanaye amebadili uamuzi.
“Vipi amesemaje?”
“Amesimamia msimamo wake, nami naheshimu alichokisema kwa vile amekuwa mkweli. Japo inauma lakini ndiyo ukweli wenyewe.”
“Bado hatujakata tamaa nitazungumza naye.”
“Muache tu, kwa aliyo zungumza hata kwa mtutu wa bunduki habadili uamuzi wake.”
“Mmh! Sawa, lakini Mage ni mtoto bado nina nafasi kama mzazi,” mama Mage alisema kwa sauti ya kukata tamaa.
Waliagana na mama Colini aliingia kwenye gari lake kurudi kwake akipata uhakika wa ndoa ya mwanaye kuvunjika.
***
Siku ya pili Mage alimuamsha mama yake aliyekuwa bado amelala, baada ya kuamka alimuaga.
“Mama nasafiri kidogo.”
“Unakwenda wapi?”
“South.”
“Una maanisha Afrika ya kusini?”
“Ndiyo mama.”
“Na nani?”
“Na mchumba wangu.”
“Nani, Colin?’
“Hapana mama, ya Colin yameishafutika moyoni mwangu itabaki kama historia.”
“Unakwenda na Hans?”
“Mama kuna mwingine? huyo ndiye aliyeshikilia maisha yangu.”
“Mmh! Sawa.”
“Bai mama,” Mage alimsogelea mama yake na kumbusu shavuni.
“Mage mwanangu ndiyo umeamua kunivua nguo mbele za watu?” mama yake bado hakuamini.
“Mama nakuahidi nikitoka South barua ya posa inakuja na ndoa itakuwa ya haraka sana. Najua utasahau yote.”
“Mage mwanangu unamuamini vipi Hans mwanaume alikuacha katika wakati mbaya?”
“Lile lilikuwa shinikizo la wazazi wake si uamuzi wake najua kabisa Hans ananipenda sana hata mimi kama ningeolewa na Colin lilikuwa shinikizo letu.”
“Mage mwanangu nani alikulazimisha, si ulikubali kwa hiyari yako?”
“Nilikubali ili kufunika kombe mwanaharamu apite.”
“Mmh! Sawa, safari njema,” mama alisema kwa sauti ya unyonge ambayo haikumshitua Mage.
Mage alitoka hadi nje na kuchukua gari la nyumbani ambalo alikwenda kuliacha uwanja wa ndege. Aliungana na mpenzi wake kwenda Afrika ya kusini kupumzika kwa wiki moja kabla ya kurudi kwa ajili ya maandalizi ya harusi kabambe.
Wakati Mage na zilipendwa wake wakienda kutuliza mawazo Colin naye aliamini kuendelea kuwepo Tanzania kwa muda ule akili yake haitakuwa sawa.
Alipanga siku inayofuata aende Afrika ya Kusini kwa wiki moja ili arudi na mawazo mapya. Kwa vile ndege ilikuwa ikiondoka saa sita mchana Colin alipanga kuondoka saa nne asubuhi ili awahi saa moja kabla ndege haijaondoka baada ya taratibu zote alijiandaa kwa siku ya pili.
Siku ya pili Colin akiwa amejilaza kitandani alikumbuka kitu na kunyanyuka kwenda kwenye kabati na kutoa picha alizompiga Cecy siku ya birth day yake. Alizichukua na kuziweka juu ya kitanda, katika zile picha aliikuta picha moja ya Mage. Alipitia picha mojamoja, aliona kitu cha ajabu mbele ya macho yake Cecy alikuwa msichana mrembo kuliko Mage na kujiuliza kipi kinachomfanya amng’ng’anie Mage wakati kuna almasi juu ya mchanga.
Alitulia akiitazama picha ya Cecy na Mage, mara simu yake iliita, alipoangalia ilikuwa ya rafiki yake Lukonge.
“Niambie Musoti,” alimwita kwa jina alilokuwa akipenda kumtania kutokana na kufanana na umbile la mchezaji wa timu ya Simba, Donald Musoti raia wa Kenya.
“Mzee vipi?”
“Poa za siku?”
“Nzuri naona namba ya South, lini tena huko?”
“Na wiki sasa.”
“Naona mzee umenikumbuka?”
“Kawaida tu, Colin kuna kitu kinanitatiza sina uhakika nacho?”
“Kitu gani?”
“Ngoja nitume picha kwenye WhatsApp kisha utanipa jibu.”
“Poa tuma.”
Baada ya sekunde chache picha iliingia kwenye simu kupitia WhatsApp, aliifungua na kukutana na picha tofauti za Mage akiwa na mwanaume wakiwa katika mkao wa mahaba mazito. Alituliza macho na kushindwa kuelewa picha ile imepigwa lini na Mage yupo wapi. Baada ya muda Lukonge alipiga simu na kuuliza:
“Umeelewa?”
“Ndiyo, hii picha umetoa wapi?”
“Nimezipiga muda si mrefu, huyu si shemeji Mage?”
“Kwani wewe upo wapi kwa sasa?”
“Nipo Hilton hotel hapa Daban.”
“Musoti ni historia ndefu niache kwa muda nitakupigia.”
“Poa.”
Baada ya Lukonge kukata simu, Colin aliziangalia upya zile picha jinsi Mage alivyojiachia na mwanaume Afrika ya kusini. Akiwa katikati ya lindi la mawazo na kumuangalia Mage ambaye aliamini kabisa hakuwa na mapenzi naye na ukweli ilizidi kudhihirika. Mlango uligongwa, aliweka simu pembeni na kunyanyua uso wake kuangali mlangoni bila kusema kitu.
Alijua ni mama yake amerudi baada ya asubuhi kuondoka kwenda kwa mama Mage kutaka kutafuta muafaka. Aliamini picha zile ndizo zitapunguza presha ya mama yake aliyeng’ang’ania kuokoa ndoa yake na Mage ambayo iliisha kufa. Alikumbuka ameacha simu alirudi kitandani na kuichukua ili amuoneshe mama yake zile picha za Mage akiwa na mwanaume nchini Afrika ya kusini.
Baada ya kuichukua simu alirudi hadi mlangoni na kufungua, alishtuka kumuona mwanamke mgeni kwake akitabasamu aliyekuwa na miwani ndogo nyeupe. Aliwekewa kidole mdomoni na kumsukuma kumrudisha ndani, naye hakuwa mbishi alirudi hadi kitandani na kukalishwa. Msichana yule mrembo alifunga mlango na komeo na kugeuka huku akitoa miwani ndogo na kutabasamu.
Colin alikuwa kama anaota baada ya kumuona aliyekuwa amesimama mbele yake ni Cecy hakika alikuwa amependeza sana.
“Ha! Cecy?”
“Ndiyo mimi,” Cecy alijibu kwa madaha.
“Siamini…Siamini Cecy wewe ni mwanamke mzuri sana tena sana.”
“Simshindi Mage.”
“Cecy naomba uachane na kile kichefuchefu.”
“Colin leo unamuona Mage kichefuchefu kwa vile amekukataa?”
“Ilikuwa shinikizo la mama tu lakini ukweli sikuwa na mapenzi naye kama ninavyokupenda,” Colin alijitetea.
“Colin napita nilitaka kujua kama upo,” Cecy baada ya kusema vile aligeuka na kutoka nje.
“Cecy hebu nisikilize.”
“Ungekuwa na shida na mimi ungenifuata nyumbani kwetu.”
Colin aliamini kabisa Cecy alikuwa amechukizwa na kitendo cha kumterekeza na ahadi za uongo. Alitoka mbio kumuwahi Cecy nje, alimkuta amekaribia getini alimfuata na kumshika mkono asiondoke.
“Cecy najua nimekukosea naomba unisamehe.”
“Colin najua hunipendi bali mimi najipendekeza kwako, endelea na Mage wako.”
“Hapana Cecy nakuapia haki ya Mungu wewe ndiye moyo wangu,” Colin alipiga magoti mbele ya Cecy ambaye siku ile alionekana mrembo mara dufu.
“Colin wewe ndiyo wa unifanya hivi au kwa vile mimi ni maskini mbumbumbu sijui lolote, asante,” Cecy alisema kwa sauti ya kilio.
“Ha..ha..Si..si…” Colin alinyamaza baada ya kusikia honi lakini alishindwa kunyanyuka kwa vile alikuwa bado kamshika mkono Cecy akimuomba msamaha.
Geti lilifunguliwa na gari la mama Colin liliingia na kushangaa kumuona mwanaye amepiga magoti mbele ya binti mrembo.
Cecy alipomuona mama Colin akiteremka kwenye gari alimsukuma Colin na kutimua mbio kwenda nje.
“Cecy…Cecy rudi na..na..”
Cecy hakugeuka alitoka hadi nje ya geti, bahati nzuri aliona bajaj inapita aliisimamisha na kupanda kisha alimweleza dereva ampeleke nyumbani kwao. Colin alipotoka nje alikuta ameisha ondoka. Alirudi ndani mbio na kumwambia mlinzi afungue geti, alipanda kwenye gari alilokujanalo mama yake na kumfukuzia Cecy kwa kuamini hasira za Cecy hazikuhitaji kupewa muda zaidi ya kutulizwa haraka la sivyo atakosa bara na pwani.
Mama Colin toka afike alikuwa akijionea vihoja asijue kumetokea nini na yule binti mrembo ni Cecy gani. Alimsogelea mlinzi na kumuuliza.
“Eti yule msichana ni nani?”
“Hata sijui, alikuja na kukuuliza kama upo nikamwambia haupo, akaniuliza Colin nikamwambia yumo ndani. Basi aliingia ndani hata hajakaa niliona akitoka mara nikamuona Colin akimkimbilia na kumshika yule msichana akawa mkali. Nilishangaa kumuona akipiga magoti kumuomba msamaha.”
“Nimesikia anamwita Cecy, ni Cecy yupi?”
“Mmh! Ndiyo leo namuona.”
“Mmh! Sasa atakuwa amekwenda wapi?”
“Hata najua! Labda atakuwa amemfuata huyo msichana.”
Colin aliendesha gari kwa kasi kuitafuta bajaj ambayo ilikuwa imeishapotea kuonesha Cecy alimwambia dereva aikimbize. Aliakanyaga mafuta kuitafuta bajaj kuifuata njia ya kuelekea nyumbani kwao Cecy. Alipokaribia nyumbani kwao alimuona akiteremka kwenye bajaj na kuingia ndani.
Colin alisimamisha gari mbele ya nyumba ya kina Cecy na kuteremka, hakufunga mlango alikimbilia ndani, Cecy alishangaa kumuona Colin pale alimuuliza kwa sauti ya juu.
“Colin umefuata nini hapa kwa masikini?”
“Cecy mpenzi naomba unisikilize.”
“Nikusikilize nini, ni wazi nalazimisha mapenzi nenda kwa Mage mwanamke mwenye uwezo na elimu, niache mimi maskini nisiye na elimu.”
“Ukifanya hivyo utakuwa ukinifunga mikono na kunipiga sitaweza kujitetea, naomba unipe nafasi.”
“Umetudhalilisha vya kutosha kwa kutudanganya kuishi maisha ya peponi leo yapo wapi, najua una chaguo lako naomba uondoke utuache na umaskini wetu.”
“Cecy najua nimewakosea lakini nami ni mwanadamu ninayehitaji kusamehewa kwa vile si mkamilifu.”
Mama Cecy aliyekuwa nyumba ya pili akichota maji aliporudi alishangaa kumkuta Colin kampigia magoti Cecy.
“Kuna nini?” aliuliza kwa mshangao.
“Mama huyu si alikuja hapa kusema nini na alifanya nini?” Cecy aliuliza kwa sauti hasira.
“Mama najua sikuwa mkweli lakini mpango wangu upo palepale.”
“Baada ya kukataliwa na Mage eeh?” Cecy alimuuliza huku amemshikia kiuno.
“Hapana majukumu yalinibana, mama naahidi nikitoka hapa kila nilichoahidi nakitimiza nisipofanya hivyo chukue uamuzi wowote.”
“Tuchukue uamuzi gani ikiwa hatukudai ni hitari yako si lazima,” mama Cecy alisema.
“Mama nilikuwa katika kipindi kibaya ambacho naamini ningelezimisha ningeweza kuwatia kwenye matatizo.”
“Colin, maisha yetu ndiyo haya hatuhitaji msaada wako, hatujaja kwenu kuomba msaada, hata masikini ana nafasi kwa muumba,” Cecy alisema huku machozi ya uchungu yakimtoka.
“Cecy usifike huko, najua unanipenda,nakuhakikishia kulipa upendo mara mbili.”
“Sihitaji,” Cecy alijibu kwa nyodo japo moyo wake wote ulikuwa kwa Colin alitaka kutikisa kibiriti kuona kama kimejaa.
“Cecy najua nimekukosea lakini amini huu ni wakati wako wa kuponya maumivu ya moyo wako.”
“Cecy msamehe mwenzako,” mama Cecy aliingilia kati.
“Basi amka,” Cecy alinyanyua Colin ambaye alikuwa bado amepiga magoti kama muumini aliyekuwa akiungama kanisani.
Colin alinyanyuka na kukumbatiana na Cecy ambaye alijilaza kifuani kwa mpenzi wake, mama yake alikuwa pembeni alitabasamu huku akiomba dua Colin amuoe Cecy ili kutimiza ndoto ya mwanaye.
“Cecy nataka kukuhakikishia mbele ya Mungu, mama yako na mchana wa jua kuwa wewe ndiye mke wangu wa maisha.”
“Muongo Colin unanidanganya,” Cecy alisema kwa sauti ya kudeka.
“Unataka nifanye nini ili uamini ninayosema.”
“Nioe niwe mkeo.”
“Nakuhakikishia kukuoa uwe mke wangu na mimi niwe mumeo.”
“Asante.”
“Naomba sasa hivi twende nyumbani nikamueleze mama mbele yangu.”
“Akikataa?”
“Hawezi, hii ni nafasi yangu ambayo hakuna wa kuiingilia, naomba uniamini.”
“Mmh! Sawa wacha nikaoge ili tuondoke.”
Colin alipewa kiti ili amsubiri Cecy aliyekwenda ndani kubadili nguo, alitoka amejifunga upande wa khanga na kutoka kuelekea bafuni kuoga.
Colin alimsindikiza kwa macho baada ya kupata nafasi ya kuliona umbile la Cecy katika vazi la kanga rangi adimu ya isiyochanganywa madawa ya ngozi.
Aliamini chaguo la kwanza la mama yake lilikuwa sahihi, alijua ni wakati wa mama yake kuamini chaguo la pili halikuwa sahihi bali tamaa ya macho ndiyo iliyompoteza. Cecy baada ya kumaliza kuoga alirudi ndani na kubadili nguo kwa kujipamba kwa vazi la kitenge lililompendeza alionekana mwanamke wa Kiafrika hasa. Alisimama mbele ya Colin na kutabasamu.
“Colin tunaweza kwenda.”
“Duh!” Colin alisema akiwa haamini.
“Ndiye mimi Cecy, mwafrika asilimia ninayejivunia rangi yangu nyeusi.”
“Basi mama inatosha, “Colin alisema huku akinyanyuka na kumshika mkono.
“Mama tunaomba tukukimbie,” Colin alimuaga mama Cecy.
“Haya baba Mungu awatangulie mfike salama.”
“Amina.”
Walishikana mikono na kutoka nje kuelekea kwenye gari, mama Cecy aliwasindikiza kwa macho na kunyanyua mikono juu na kurudi kuomba dua yake ya Colin kumuoa mwanaye ili roho itulie. Hakuteremsha jicho mpaka gari lilipopotea machoni mwake.
Ndani ya gari Cecy moyo wake ulikuwa na furaha nusu kwa vile aliamini lazima Colin atumie nguvu nyingi bila hivyo hakuna mapenzi kwa vile mama yake aliishajenga uadui mapema. Alionekana mtu mwenye mawazo mengi kitu kilichomfanya Colin amshtue.
”Vipi mpenzi?”
“Colin bado moyo wangu una wasiwasi.”
“Wa nini?”
“Jinsi mama yako atakavyonipokea.”
“Ondoa wasi kila kitu niachie mimi.”
Colin alisimamisha gari mbele ya geti na kupiga honi, mlango ulifunguliwa na kuliingiza gari ndani. Alizunguka upande wa pili na kumfungulia Cecy na kumshika mkono kuteremka kwenye gari kwa heshima kisha alielekea naye ndani. Walitembea taratibu kama mtu na mkewe angetokea mtu na kuwaona angejua ni wapenzi wa muda mrefu wanaopendana sana.
Walipofika mlango wa kuingia sebuleni Colin alisema kwa sauti ya unyenyekevu:
“Karibu malkia wangu.”
“Asante mfalme wangu,” Cecy naye alijibu kwa unyenyekevu.
Sauti zile zilimfanya mama Colin aliyekuwa ameinama akisoma biblia kunyanyua macho na kumuona mwanaye na msichana mrembo ambaye aliamini ndiye aliyeondoka muda mfupi uliopita.
“Shikamoo mamkwe!” Cecy alimsalimia mama Colin kwa unyenyekevu huku akipiga magoti ya heshima.
“Marahaba mama, karibu.”
“Asante,” Cecy alijibu huku akinyanyuka na kumfuata Colin aliyekuwa amesimama pembeni yake na kumshika mkono.
Colin alimuongoza Cecy mpaka kwenye sofa na kumkaribisha tena:
“Karibu.”
“Asante,” Cecy alijibu huku akikaa.
“Unatumia kinywaji gani?”
“Chochote utakachonichagulia mfalme wangu.”
“Colin si ungemwita dada wa kazi awahudumie,” mama Colin aliingilia kati.
“Hapana huyu ni mgeni wangu, kila kitu chake nitafanya mimi.”
“Mmh! Haya.”
Muda wote mama Colin alikuwa bado hajaipata picha ya yule msichana mrembo, alituliza macho kwa wizi ndipo alipomgundua kuwa ni Cecy msichana muuza ndizi. Alikunja uso kwa hasira na kuamini kabisa lile si chaguo sahihi kwa mwanaye bali ni papara ya kuachwa na Mage.
Alinyanyuka na kuelekea chumbani kwake, alipotoka eneo la sebule alimwita Colin.
“Colin.”
“Naam mama.”
“Njoo mara moja.”
“Nakuja,” Colin alisema huku akimwekea juisi kwenye glasi na kunywa kidogo kisha alimkaribisha.
“Karibu malkia wangu.”
“Asante mfalme wangu.”
“Samahani namsikiliza mama mara moja.”
“Nenda mpenzi kamsikilize mama.”
Colin alimfuata mama yake kwenye korido alipokuwa amesimama, alimsogelea karibu na kumuuliza:
“Unasemaje maana umenitoka kama kuna kitu?”
“Yule nani?” aliuliza huku akinyoosha kidole sebuleni.
“Mke wangu mtarajiwa chaguo sahihi la moyo wangu.”
“Colin… Colin una tatizo gani wanawake wote wameisha mpaka umfuate huyu maskini mbumbumbu asiyejua kitu. Mwanangu tuna fedha tunaweza kumuona msichana yeyote mzuri mwenye elimu yake kwa fedha yoyote na popote duniani.”

Tukutane Jumatano
 
SEHEMU: 18
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500

ILIPOISHIA:
“Yule nani?” aliuliza huku akinyoosha kidole sebuleni.
“Mke wangu mtarajiwa chaguo sahihi la moyo wangu.”
“Colin… Colin una tatizo gani wanawake wote wameisha mpaka umfuate huyu maskini mbumbumbu asiyejua kitu. Mwanangu tuna fedha tunaweza kumuona msichana yeyote mzuri mwenye elimu yake kwa fedha yoyote na popote duniani.”
SASA ENDELEA...

“Mama naomba kwa hili usizungumze chochote uniache kabisa, umetafuta mwanamke ambaye leo katuvua nguo kwa vile ulimfuata msomi mwenye uwezo.”
“Lakini suala la Mage bado tulikuwa tunalishughulikia bado lilikuwa halijafika mwisho. Hivi leo Mage aje na mama yake wakikute kinyago hiki kuna ndoa kweli?”
“Penzi langu na Mage liliishia Bagamoyo, lilikufa tukalizika halitafufuka tena.”
“Lakini bado wazazi hatajabariki uamuzi wenu.”
“Mama si uamuzi wetu bali wa Mage, kasema ukweli ana mtu anayempenda tatizo lipo wapi?”
“Basi Cecy si chaguo langu.”
“Mama, mimi ni mwanao umenizaa na kunilea na kunifundisha kila kitu, lakini suala la nimpende nani ni matakwa ya moyo wangu. Nilikukubalia kwa Mage kwa vile ni mzazi wangu zoezi lako limefeli sasa huu ni muda wangu.”
“Lakini siyo kwa Cecy.”
“Mama Cecy ni zaidi ya mwanamke ndiye mwenye nafasi moyoni mwangu zaidi ya hapo sitakuwa na mwanamke mwingine.”
“Colin, Cecy umemjulia wapi kama siyo mimi?”
“Basi hili ndilo chaguo lako lililokuwa sahihi hujui tu.”
“Nilikuwa namtania tu lakini si kwa ajili ya kuwa mkeo.”
“Basi imekuwa hivyo bila kutegemea.”
“ Basi mimi simtaki.”
“Kwa hiyo unatafuta aibu nyingine?” Colin alisema huku akifungua simu upande wa picha na kumuonesha mama yake.
“Umeona unayempenda?”
Aliangalia picha za Mage na kuuliza:
“Hizi picha za nani?”
“Mage na mpenzi wake,” Colin alimjibu huku akimtazama usoni.
“Picha hii imepigwa lini?”
“Leo.”
“Wapi?”
“Wapo Afrika ya kusini wanakula raha katika hoteli ya Hilton jijini Durban, sasa naomba uniache na Cecy wangu.”
“Colin bado hujanieleza kitu, tafuta msichana mwingine lakini kwa Cecy sipo radhi kuingiza uchafu katika familia yangu.”
“Mama nakupenda na kukuheshimu sana naomba kuhusu Cecy usiniingilie kabisa zaidi ya hapo nitaondoka na kukuacha na fedha zako.”
“Colin mwanangu mbona umefika mbali,” mama alishtuka.
“Kwa sababu umeingilia haki ya moyo wangu, wewe ni mzazi gani usiye na huruma nimeumizwa badala ya kunihurumia bado unataka kuniongezea maumivu,” Colin alisema kwa uchungu.
“Lakini kumbuka wewe ni msomi unawezaje kuoa mwanamke mbumbumbu?”
“Mama mapenzi si cheo, elimu wala fedha, Cecy ni zaidi ya vyote hivyo kwangu.”
“Sawa, lakini utakuja kunikumbuka na uamuzi wako hata nikifa.”
“Ni kweli mama nitakukumbuka kwa kunitafutia mchumba aliye bora kuliko Mage. Cecy ni lulu iliyokuwa imejificha kwenye matope.”
“Nimekuelewa mwanangu, naomba unisamehe kwa kukukwaza.”
“Nilikusamehe kabla hujatenda.”
“Basi naomba ya huku yaache hukuhuku.”
“Sawa mama.”
Baada ya makubaliano Colin alirudi kwa Cecy na mama yake kwenda chumbani, alipofika alimpigia simu mama Mage kutaka kupata ukweli wa kauli ya mwanaye.
Baada ya simu kuita ilipokelewa upande wa pili:
“Haloo, dada vipi?”
“Mmh! Yaani bado nachanganyikiwa ulisema Mage kaenda wapi?”
“Nilikuambia amekwenda kwa shoga yake.”
“Wapi?”
“Aliniaga anakwenda Kibaha,” mama Mage alidanganya.
“Mmh! Mbona Colin anasema katumiwa picha za Mage akiwa na mwanaume Afrika ya kusini wakila raha kwenye ufukwe wa Hilton Hotel?”
“Mmh! Labda maana ametoka toka jana, dada wee hebu tuachane na Mage tufanye mambo zingine.”
“Sawa dada nimekuelewa.”
Baada ya kukata simu alitulia kwa muda akiwaza, alijikuta akimchukia Cecy na kuuapia moyo wake hatakuwa tayari kuona mwanaye akioa mwanamke asiye na hadhi. Alipanga kuhakikisha anauvunja uhusiano ule kwa hali na mali ili Colin aoe mwanamke mwingine mwenye elimu na kutoka familia yenye uwezo.
Alitoka chumbani na kujifanya kujichekeza kwa Cecy huku akimtania.
“Jamaniii mmependezaje wapenzi!”
“Asante mkwe,” alijibu Cecy kwa furaha huku Colin aliuona unafiki wa mama yake uliojificha moyoni ambao mpenzi wake hakuujua.
Kwa vile mama Colin hakupenda Cecy kuwa pale aliondoka na kwenda chumbani kwake na siri yake nzito moyoni.

JIJINI DURBAN AFRIKA KUSINI
Katika ufukwe wa hoteli ya Hiltoni wapenzi wa wawili walikuwa wakila raha, Mage alikuwa amelala kifuani kwa Hans huku akichezea kidevu chenye ndevu chache.
“Hans nikuambie kitu?”
“Niambie mpenzi.”
“Ningebugi vibaya kuolewa na mrugaruga kama yule(Colin).”
“Si haraka zako, nilikueleza piga ua lazima mke wangu utakuwa wewe pamoja na wazazi kunilazimisha kumuoa yule mwanamke.”
“Nilichanganyikiwa baada ya kuona umepata mtoto.”
“Ilikuwa lazima iwe vile ili wasijue nimepanga nini mbeleni.”
“Asante Hans kwa kuponya majeraha ya moyo wangu.”
“Nami nashukuru kukubali kurudi mikononi mwangu.”
“Kwa hiyo ndoa lini?”
“Tukirudi tu nyumbani mipango inaanza mara moja.”
“Nitafurahije mpenzi wangu.”
“Usijali nipo kwa ajili yako.”
“Basi naomba turudi nyumbani ili tukalisema hili mbele ya wazazi wetu wote.”
“Hakuna tatizo nakusikiliza wewe.”
“Nataka kesho jioni tuwe mbele ya wazazi wako ukiwaeleza kwa mdomo wako kuwa mimi ndiye mkeo baada ya hapo twende kwetu nikamweleze mama kuwa wewe ndiye mume wangu.”
“Hakuna tatizo mpenzi wangu.”
Walikubaliana kuondoa Afrika ya kusini siku ya pili mchana warudi Tanzania ili kwenda mbele ya wazazi wao kuthibitisha mapenzi yao ya dhati.
***

Colin na Cecy baada ya kutoka nyumbani walikwenda Bagamoyo katika hoteli ya Malaika ambako alipanga kukaa kwa siku moja. Majira ya jioni wakiwa wamejilaza mchangani huku wakipepewa na upepo mwanana wa bahari Colin aliyaangalia mawimbi ya bahari na mitumbwi ya wavuvi aliokuwa wakivua samaki.
Baada ya kugandisha macho baharini alijikuta akitokwa na machozi baada ya kukumbuka sehemu kama ile ndiyo iliyotumika kuvunja uchumba wake na Mage japokuwa ilikuwa hoteli tofauti lakini ni Bagamoyo ileile.
Machozi yalimdondoka bila kujua na kuangukia kwenye paji la uso la Cecy aliyekuwa amejilaza mapajani kwa mpenzi wake na kumfanya anyanyue macho kumwangalia. Alishtuka kumuona akibubujikwa machozi kitu kilichomfanya amuulize.
“Vipi mpenzi wangu mbona unalia?”
“Nimekumbuka kitu ambacho kimesababisha nitokwe machozi.”
“Kitu gani mpenzi wangu?” Cecy alimuuliza huku akimfuta machozi kwa upande wa mtandio aliojifunga.
“Ni juzi tu maeneo hayahaya yaliujerudi moyo wangu lakini, leo hii maeneo yaleyale yameujenga upya na kujiona kama nimezaliwa upya.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Juzi tulikuja huku na Mage kuvunja uchumba wetu ambao ulinishtua sana na kuumiza moyo wangu japokuwa haikuwa hoteli hii, lakini ni hukuhuku Bagamoyo. Lakini leo nimezaliwa upya kwa kulipata penzi la kweli ambalo naamini nilitaka kulipoteza haya ni machozi ya uchungu na furaha.”
“Nifurahi kusikia hivyo, lakini moyo wangu bado haujaamini kama tayari wewe ni wangu.”
“Kwa nini Cecy?”
“Naogopa Mage anaweza kurudi na wewe kunitosa, nitaumia mara mbili kwa vile nimeonja utamu wa mapenzi naweza kufa kwa presha kama utafanya hivyo,” Cecy alisema kwa sauti ya kulalamika.
“Cecy unataka kuamini vipi wakati penzi langu lilikuwa wazi mbele ya mama yangu.”
“Mama yako alikuitia nini pembeni?”
“Tulikuwa na yetu wala haikuhusiana na sisi,” Colin alitengeneza uongo ili kuendeleza furaha ya siku ile.
“Mmh! Nilikuwa na wasi labda chokoraa nilimeingia kwenye nyumba ya malkia,” Cecy alitania utani wenye ukweli.
“Hapana wewe ndiye malkia wangu.”
“Nashukuru kusikia hivyo,” Cecy alimkumbatia mpenzi wake kwa furaha bila kujua palichimbika mpaka yeye kuwa pamoja muda ule.
***
Mage na Hans waliwasili katika aridhi ya Tanzania katika jiji la Dar na ndege ya shirika la Afrika ya Kusini. Nje ya uwanja wa ndege walisubiriwa na gari la kifahari Land Cruiser V8 nyeusi. Baada ya ndege kutua waliteremka na kwenda moja kwa moja ndani ya gari lililokuwa likiwasubiri na kuingia.
Gari liliondoka kuelekea Mikocheni anapoishi Hans, njiani Mage alikuwa na furaha ya ajabu kurudi mikononi kwa mpenzi wake mwanaume wa maisha yake. Baada gari kuingizwa ndani na kusimama Hans alizunguka upande wa pili na kumfungulia Mage mlango na kumkaribisha.”
“Karibu utamu wangu.”
“Asante raha zangu.”
Walishikana mikono na kuingia ndani, mapokezi ya familia ya Hans yalikuwa tofauti na siku za nyuma waliufurahia ugeni wa Mage huku wadogo zake wakimwita wifi na shemeji na wazazi wakimwita mkwe. Ilikuwa ni faraja kubwa moyoni kwa Mage aliona sawa na ngamia kupita katika tundu la sindano kukubalika katika familia ile.
Moyoni alijilaumu kukubali kuolewa na Colin kumbe ahadi ya kuvumilia ili ndoto yao ya muda mrefu waliyoahidiana kutenganishwa na kifo ilikuwa njiani. Familia haikuwa na tatizo tena kuingilia uamuzi wa mtoto wao kwa vile chaguo lao Mungu alilichukua hawakuwa na jinsi.
Baada ya mapokezi mazuri katika familia ya mpenzi wake Mage na Hans walielekea Kigamboni nyumbani kwao Mage ili kujitambulisha rasmi kwa mzazi wake. Walipofika Kigamboni Mage alimkaribisha Hans nyumbani kwao.
“Karibu mume wangu.”
“Asante mke wangu.”
Walishikana mikono na kuingia ndani kwa mwendo wa mahaba, sebuleni walimkuta mama Mage. Mage alimuachia mkono Hans na kumkimbilia mama yake na kumkumbatia.
“Waaawoo mama.”
“Mage mwanangu karibu mama.”
“Asante mama.”
Mage alichukua nafasi ile kumtambulisha Hans.
“Mama leo nimemleta mume wangu chaguo la moyo wangu.”
“Nimemuona, karibu baba,” mama Mage alisema kwa sauti ya unyonge.
“Asante mama, shikamoo.”
“Marahaba.”
“Mama mbona mnyonge unaumwa?” Mage alimuuliza mama yake.
“Walaa, mwili umechoka tu.”
Mama Mage alinyanyuka na kuelekea chumbani kuwapisha alipoondoka eneo la sebule alimwita mwanaye.
“Mage mama njoo mara moja.”
“Nakuja mama,” kabla ya kuondoka alimuaga mpenzi wake.
“Mpenzi nakuja.”
“Hakuna tatizo msikilize mama.”
Mage alimbusu shavuni Hans na kuchepua mwendo kwenda kumsikiliza mama yake.
“Abee mama.”
“Njoo chumbani.”
Waliongozana hadi chumbani, walipofika mama yake alisimama na kumwambia Mage akae kwenye kochi, baada ya kukaa alimgeukia na kumwita.
“Mage.”
“Abee mama.”
“Hivi ndiyo umeamua kunivua nguo?”
“Kukuvua nguo! Kivipi mama.”
“Kwa hiyo hutaki kuolewa na Colin?”
“Mamaaa! Mbona hilo tuliisha limaliza, si nimekueleza ukweli wangu na Colin anajua kila kitu. Sasa swali kama hilo linatoka wapi?”
“Mage kwa nini unalamba matapishi yako?”
“Mama Hans si matapishi ni chakula kilichowekwa kwenye Hot port nimekipakuwa bado kina moto. Unajua jinsi gani nilivyoteseka baada ya Hans kulazimishwa kuona mwanamke mwingine. Ni wewe uliniambia niwe na subira sasa leo karudi mikononi mwangu unaniuliza hivyo?”
“Kama ungekuwa huna mchumba nisingekuuliza lakini wewe tayari umeishakuwa mchumba wa mtu tena upo kwenye hatua za mwisho za ndoa.”
“Mama wewe ndiye unayekuza mambo Colin tumeisha malizana na sasa hivi tunatoka nyumbani kwao Hans ambako sikuamini kama wangenipokea kama malkia. Yaani mama nimefurahi kukubalika katika familia ya mpenzi wangu.”
“Mwanangu siku zote mkataa pema pabaya panamwita.”
“Mamaa maombi gani hayo?”
“Nakuambia utamkumbuka Colin, ipo siku Hans atakukimbia na kurudi kwa Colin utambembeleza ukitembea kwa magoti, kibaya ukute ameoa mwanangu utakuja jutia uamuzi wako,” mama alitoa taadhali.
“Mama kuwa na Hans sitajuta katika maisha yangu ni chaguo sahihi la moyo wangu.”
“Mmh! Sawa.”
“Kuonesha Hans hataki kunichezea wiki ijayo barua inakuja na baada ya majibu maandalizi yanaanza mara moja. Kinachotakiwa vikao vya harusi visogezwe mbele ili michango ya harusi yangu na Colin iwe yangu na Hans. Hapo nina imani hakuna kitakacho haribika.”
“Sawa, siwezi kukuingilia kwa vile umeamua mwenyewe, ila kila aliyae ushika kichwa chake.”
“Mama hiyo misemo, ninacho shukuru nimepata tiba ya moyo wangu, kuna lingine?”
“Hakuna.”
“Basi mama yangu naomba unipe baraka zako kinyongo chake kinaweza kuvuruga ndoto zangu.”
“Siwezi kuna na kinyongo kwa vile nipo kwa ajili ya kuyaona maisha yako yanakuwa mazuri na salama.”
“Asante mama,” Mage alimshukuru mama yake kwa kumkumbatia.
Mage baada ya kuachana na mama yake alikwenda sebuleni alipokuwa amemuacha mpenzi wake.
Alirudi sebuleni na kumvamia Hans kwa mahaba motomoto bila kujali yupo sehemu gani. Mama yake hakutoka ndani alijikuta moyo ukimuuma na kuanza kulia peke yake huku akilaumu mapenzi ya mumewe kumuharibu mtoto.
****
Siku ya pili Colin na Cecy alirudi nyumbani, alimpitisha nyumbani kwa kisha yeye alirudi nyumbani kwa vile kulikuwa na mambo ya kufuatilia kuhusiana na shughuli zake alizoanza ikiwemo kupata kibari cha kuanzisha kampuni ya mitindo na mavazi ambayo alipanga kumtumia Cecy kwa ajili ya maonesha ya mitindo ya nguo.
Walipofika kabla ya kuondoka Colin alimwambia Cecy:
“Mpenzi pumzika ila jioni nitakufuata tutakuwa na mazungumzo marefu ila utarudi kulala nyumbani najua bi mkubwa amekumisi.”
“Hakuna tatizo msalimie mkwe.”
“Kuanzia wiki ijayo nategemea kutimiza ile ahadi.”
“Ahadi gani?”
“Ya ujenzi wa nyumba yenu, leo nitamtuma mtu awatafutie nyumba ili kesho muhame ili kupisha ujenzi.”
“Kama ni kweli tutashukuru.”
Colin alimwita mama Cecy na kumpa laki mbili.
“Mama utakunywa soda.”
“Asante baba.”
“Hakuna tatizo.”
Colin aliaga na kuondoka kuwahi nyumbani ili awahi mjini kwenye mipango yake na kumuacha Cecy akikumbatiana na mama yake kwa furaha. Kwa vile alikuwa na haraka alifika nyumbani hakukaa alibadili nguo na kuvaa suti ili kwenda kwenye miadi yake. Wakati anatoka alikutana na mama yake sebuleni.
“He! Baba umerudi saa ngapi?”
”Sasa hivi mama, Leo namiadi ya jamaa wale wa kampuni ya matangazo.”
“Na mwenzio yupo wapi?”
“Nimemuacha kwao.”
“Sawa baba baadaye.”
“Sawa mama baadaye.’
Colini aliagana na mama yake na kutoka nje ambako alichukua gari kuwahi Posta mpya katika Jengo la Benjamini Mkapa ghorofa ya kimi na nne. Baada Colin kuondoka mama yake aliamini ile ndiyo nafasi ya kwenda nyumbani kwao Cecy ili kuhakikisha ndoa na mwanaye haifungwi.
Alioga harakaharaka na kutoka kwenda nyumbani kwao Cecy, aliendesha gari kwa kasi kidogo ili kuwahi kabla mwanaye hajarudi. Aliamini kutumia fedha zake ataweza kuisambaratisha ile ndoa. Alisimamisha gari mbele ya nyumba ya kina Cecy na kuteremka.
Alimkuta mama Cecy amekaa kwenye kibalaza cha nyumba, alipomuona alimkaribisha kwa furaha na bashasha.
“Ooh! Karibu dada.”
“Asante, za hapa?”
“Nzuri, karibu japo maisha yetu ya kuungaunga.”
“Aah! Kawaida tu wala msijali.”
Alipotaka kumkaribisha ndani alikataa alisimama mbele ya nyumba, aliyatazama mazingira wanayoishi Cecy na mama yake moyo wake ulichefuka kwa kuona jinsi gani mwanaye alivyopotea maboya kutaka kumuona mwanamke fukara kama yule ambaye halingani na sifa na hadhi ya familia yao.

Itaendelea
 
SEHEMU: 19
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500

ILIPOISHIA:
Cecy alizipokea na kumfanya mama Colin kutabasamu kwa kuamini fedha ni sabuni ya roho. Alizitazama zile fedha kwa uchungu huku machozi yakimtoka na kuona jinsi gani umaskini wao ulivyotumiwa kama kisu butu cha kuupasua moyo wake bila ganzi. Alitulia akilia huku machozi yakidondokea kwenye zile fedha.
SASA ENDELEA...

Kwa hasira alizinyanyua na kumpiga nazo usoni mama Colin na kutoka ndani ya gari, kitu kilichomuacha mdomo wazi mama Colin. Mama yake alishangaa kumuona mwanaye akitoka ndani ya gari akilia.
“Cecy kuna nini?”
“Mama niache kwanza, huyu mama ni mchawi.”
“Mchawi! Kafanya nini?” mama yake alishtuka.
Wakati huo mama Colin kwa aibu aliwasha gari lake na kuondoka bila kuaga. Aliushangaa ujasiri wa Cecy msichana maskini lakini mwenye kujiamini kupita kiasi kwa kukataa fedha zile na ofa ya kuyabadili maisha yao. Hakuamini binti muuza ndizi kukataa fedha zile wakati maisha yao ya kubahatisha. Lakini alijiapiza kwa nguvu kwa hiyari kwa fedha kwa damu lazima Cecy ataachana na Colin.
Mama Cecy alimfuata mwanaye aliyeingia chumbani huku akilia na kushindwa kuelewa mazungumzo ya ndani ya gari yalikuwa ya nini. Alikumta akiendelea kulia kitu kilichomfanya ajiulize kipi kikubwa walichokizungumza ndani ya gari.
Alimkuta amelala kifudifudi akilia kwa sauti ya kwikwi, wasiwasi wake labda Colin amepata tatizo.
“Cecy mwanangu kuna tatizo gani tena?”
“Mama inaumiza sana.”
“Kuna nini mpenzi wako kapata tatizo?”
“Mama mtu anaweza kuununua moyo wangu hata kuuchukua bure nikiwa nimekufa, lakini nikiwa hai siuuzi kwa gharama yoyote kwa vile furaha ya mtu hainunuliwi dukani.”
“Una maana gani?” mama yake alikuwa bado njia panda.
Cecy alimweleza mama yote aliyozungumza na mama Colin, mama yake macho yalimtoka pima kusikia taarifa ile baada ya kuamini kila kitu kilikuwa vizuri kilichobakia ni ndoa ya mwanaye na Colin.
“Mmh! Mbona makubwa madogo yana nafuu,” mama Cecy alisema akiwa amechoka na maneno yale.
“Mama mimi na Colin basi,” Cecy alisema kwa hasira.
“Huo ni uamuzi wa hasira lazima umsikilize mwenzako si amesema atakupitia jioni basi msubiri umsikilize naye anasemaje kama lao moja na mama yake una haki ya uamuzi wako.”
“Mama kosa langu nini? Yaani anatumia fedha zake kuinunua furaha yangu?” Cecy alisema kwa uchungu.
“Mwanangu kama Colin si chaguo la Mungu basi hamtaoana lakini kama ni chaguo la Mungu hakuna kitakachozuia.”
“Yule mwanamke ni mnafikia akiwa na mwanaye ananichekea kicheko cha mamba lakini kumbe ananitamani kunimeza.”
“Wee yaache tusubiri jioni.”
“Sawa, lakini nina amini hakuna ndoa yangu na Colin labda mapenzi ya sisi wenyewe lakini mama yake hanipendi na yupo radhi kutumia njia yoyote kukwamisha mapenzi yetu.”
”Ngoja tumsubiri Colin anasemaje.”
“Namsubiri kwa ajili yako lakini ningekuwa peke yangu asingekanyaga hapa.”
****
Majira ya jioni Colin alimpitia Cecy kama alivyomweleza, aliposimamisha gari alishangaa kutomuona mpenzi wake kama kawaida, kwani aliisha mzoesha vibaya kumpokea kwa kumrukia kwa mahaba motomoto. Baada ya kusimamisha gari aliteremka na kwenda ndani huku akiita jina la Cecy mkononi alikuwa amebeba zawadi za mpenzi wake.
“Beeeebi.”
Hakuwa na jibu zaidi ya kusikia sauti ya kilio toka ndani kitu kilichomshtua na kufanya akimbilie ndani kwa kuamini mpenzi wake yupo kwenye matatizo. Alimkuta Cecy amelala kifudifudi akilia kilio cha sauti.
“Cecy mpenzi una nini?”
“Colin unaweza kununua kila kitu chini ya jua lakini si furaha ya mtu,” Cecy alisema bila kugeuka.
“Kuna nini mpenzi wangu?” Colin alishangaa.
“Umenikuta maskini hata siku moja sikuja kwenu kuomba pesa ya kula, nimeishi kwa kuuza ndizi nitaendelea kuuza ndizi lakini hamuwezi kuutumia umaskini wetu kama siraha ya kununua haki ya moyo wangu.”
“Cecy hebu geuka mpenzi wangu, kipi nimekukosea mpaka useme maneno makali hivyo?”
“Najua hunipenda lakini usitumie gharama kubwa kuniacha, tamko lako ni tosha kuliko gharama na nguvu mnayotaka kuitumia. Ni kweli nakupenda jambo ambalo lipo wazi mbele ya muumba. Lakini ni vigumu kulazimisha mapenzi ni sawa na kumvuta punda mtoni lakini huwezi kumlazimisha kunywa maji.”
“Cecy mpenzi wangu mbona toka jana tumekuwa na siku nzuri ambayo nilitegemea kuimalizia leo. Kipi nilichokufanyia ikiwa nimekuaga nimekwenda kwenye mipango ya maisha yetu ya mbeleni. Nimekuja na furaha ili kukujulisha nimekupatia chuo cha mambo ya urembo ambacho utasoma miezi sita na ukitoka hapo utakuta nimeisha kukufungulia kampuni yako ya urembo.
“Kwa nini wanawake mnapenda kuumiza moyo wangu, Cecy kabla hatujaanza mapenzi ulionesha kunijali lakini kuanza kwa ukaribu wetu hata mwezi bado unataka kuupasua moyo wangu bila ganzi. Cecy niliamini wewe ndiye tiba ya moyo wangu, lakini unataka kuongeza msumali wa moto kwenye kidonda. Naomba basi mnihurumie nami binadamu ninayehitaji upendo. Mapenzi yangu yamekuwa kama mtu anayemwaga maji baharini yasiyoonekana.
“Kwa nini hukuniambia mapema Cecy umeacha nijirushe juu ya ghorofa ya mapenzi nikiamini utanidaka, lakini najiona naangukia pabaya nawe umekataa kunidaka nitakufa kifo kibaya. Cecy utajiri wetu hauingiliani na mapenzi yetu, fedha inaweza kununua kila kitu lakini si penzi la kweli bali upendo wa dhati toka chini ya uvungu wa moyo wa mtu mwenye mapenzi ya kweli asiyeangalia kitu bali mtu mwenyewe alivyo.
“Ni kosa gani nililokufanyia mpaka kufikia kusema maneno mazito yaliyoushtua moyo wangu, kama moyo ungekuwa ukitoka nje naamini ungekuwa unavuja damu kutokana na mshtuko na maumivu ya kuona unatolewa sehemu salama na kutupwa kwenye miba.”
Maneno ya Colin ambaye alionekana hajui kilichokuwa kikiendelea kilimfanya Cecy aongeze sauti ya kilio na kujinyanyua alipokuwa amejilaza na kwenda kujitupa kifuani kwa Colin kitu kilichomshangaza mpenzi wake.
“Cecy mpenzi wangu hebu kuwa mkweli tatizo nini mpaka kusema maneno makali? Nipo radhi kujitoa muhanga ili kuliokoa penzi letu.”
“Colin najua unanipenda lakini mama yako hanipendi,” Cecy alisema kwa sauti ya kilio.
“Bebi, maneno gani hayo ikiwa jana uliona alivyokufurahi, yasahau yote yaliyopita.”
“Colin, mama yako mnafiki, ana tabia ya unafiki wa mamba anakuchekea machoni lakini moyo anakuchukia.”
“Kwa nini unasema hivyo?” Colin alishtuka kusikia vile.
“Mama yako hataki tuwe pamoja yupo radhi kutumia gharama yoyote kuhakikisha anatutenganisha.”
“Lakini mbona yaliisha.”
Cecy aliamua kumweleza ukweli, ujio wa mama yake na ahadi na fedha aliyotoa kwa ajili kulivunja penzi lao. Colin alibakia macho yamemtoka pima asiamini maneno ya Cecy.
“Cecy unayosema ni kweli?”
“Nimzulie uongo mama yako ambaye kama tungeoana angekuwa mama mkwe wangu.”
“Kama kafikia hatua hiyo naomba kwanza unisamehe sana, najua nitafanya nini. Ila nakuahidi kwa kuonesha msimamo umezisha upendo moyoni mwangu, pia hela aliyotaka kukupa nitakupa mara kumi yake na kutimiza ahadi yangu kwa kulijenga penzi letu.”
“Colin, narudi huwezi kuununua moyo wangu.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Sihitaji pesa zako kwa ajili yakuonesha kuwa unanipenda bali mapenzi ya dhati toka kwako. Pendo langu halina gharama japo ni ghali kwa vile nilikubali kukupenda kama ulivyo wala si kwa ajili ya gari, majumba au fedha zenu.”
“Asante kufahamu hivyo, basi naomba ukaoge ili twende nilipokueleza jana.”
“Sawa mpenzi wangu.”
“Pia, kesho mtahama ili kupisha ujenzi wa nyumba yenu kwa muda, nimewatafutie nyumba nzima ambayo nimelipia kwa mwaka mzima.”
“Kwani hiyo nyumba unachukua muda gani kujengwa?”
“Nitaka ijengwe vizuri hata miezi miwili au mitatu.”
“Basi si ungechukua miezi mitatu?”
“Msiwe na wasi, niliwaambia wakakataa wakataka mwaka mzima.”
“Ipo wapi?”
“Kimara Baruti.”
“Asante mpenzi wangu,” Cecy alimkumbatia Colin kwa furaha na kuyasahau maumivu yote.
Cecy alikwenda kuoga akimuacha Colin ambaye alihisi kichwa kinataka kupasuka kwa mawazo kutokana na alichokifanya mama yake aliyeamini ndiyo muongozo wake na kuitengeneza furaha lakini kwake ilikuwa kinyume. Alipanga akitoka pale kwenda na Cecy nyumbani kwao ili mama yake akayasema yale mbele yake.
Baada ya Cecy kumaliza kuoga na kubadili nguo ambazo zilizidi kumpandisha chati na kumfanya aonekane binti mrembo kuliko wanawake wote duniani mbele Colin. Walishikana mikono na kuelekea ndani ya gari na kuelekea moja kwa moja nyumbani kwao Colin.
“Colin unanipeleka wapi?” Cecy alishtuka.
“Usihofu naomba unifuate na mimi.”
“Mmh! Sawa.”
Gari lilipiga hodi na geti lilifunguliwa na Colin kuliingiza ndani, kama kawaida alizunguka na kumfungulia mlango kisha alimshika mkono na kuingia naye ndani. Sebuleni alikuwa mama Colin akizungumza na msichana wa kazi alipomuona Colin alinyanyua macho na kumuona ameongoza na hasimu wake.
Alijikuta akiponyokwa na glasi ya juisi aliyokuwa ameshikilia. Cecy alisogea hadi karibu na mama Colin na kumsalimia.
“Shikamoo ma mkwe,” kama kawaida alipiga goti la heshima mpaka chini.
Mama Colin alinyanyuka alipokuwa amekaa na kumfuata Cecy na kumnyanyua alipokuwa bado amepiga magoti na kumkumbatia kwa muda huku machozi yakimtoka.
Colin alishangazwa na mama yake kufanya vile aliamini alifanya vile kujitakasa mbele ya macho ya mwanaye lakini moyoni alikuwa na nia mbaya kuliko bomu la kutegwa. Alijiuliza mama yake atamwambia nini kwa kitendo cha kigaidi alichokifanya cha kusambalatisha penzi lake.
“Cecy,” alimwita huku akimshika mabegani na kumtazama usoni kwa macho yaliyojaa machozi.
“Abee ma’ mkwe,” Cecy aliitikia huku naye machozi yakimtoka.
“Najua siku ya leo huenda hutanielewa, unaweza kuwa msichana wa kwanza kunionesha kitu si cha kawaida. Lakini nilichokifanya leo ni mtihani wangu wa mwisho kwako, nakili kwa moyo wangu katika wasichana niliowapenda ulikuwa wewe namba moja.
“Lakini sikumaanisha kuwa utakuwa mke wa mwanangu kwa vile nilikuwa na Malengo makubwa kwa mwanangu baada ya kutumia kiasi kikubwa kumsomesha.
Niliamini mwanamke atakayemfaa ni mwenye elimu kama yake pia anayetoka katika familia yenye uwezo ambaye atakuwa na mapenzi ya kweli na hatafuata mali aliyonayo mwanaume.
“ Niliamini chaguo langu lilikuwa sahihi la kumchagua Mage kwa vile ni msomi tena anatoka katika familia yenye uwezo pia mama yake ni shoga yangu. Lakini kumbe siyo, nakiri toka moyoni mwangu mapenzi niliyokuwa nikimpenda Cecy yaligeuka na kumuona ni adui namba moja anayetaka kuvuruga ndoto zangu.
“Mwanzo nilidhani utani lakini siku ya birthday ya Colin nilivyokuona ulivyopendeza mpaka kukusahau na picha nilizomkuta nazo Colin niliona ndoa hakuna. Moyo wangu ulikosa amani mpaka mipango ya harusi kwenda vizuri huku nikiwa sisikii taarifa yako.
“Kwa kweli niliumia sana kwa kitendo cha Mage kuuvunja uchumba tukiwa katika hatua za mwisho. Siku zote nilikosa usingizi nimekuwa nikipungua siku hadi siku. Kitendo cha kuibuka wewe kwa kweli kilinichanganya sana, sikuamini kama una mapenzi ya kweli na mwanangu zaidi ya kufuata mali zetu.
“ Mtihani niliokupa leo umenipa sababu sahihi ya mwanangu kukuchagua wewe kuwa mkewe. Cecy kitendo cha leo kilifukua mapenzi yote ya nyuma na kukiri mapenzi si elimu wala mali bali upendo wa dhati toka moyoni mwa mtu. Umenionesha jinsi gani unavyo mpenda mwanangu mapenzi ya dhati si kwa ulichonacho.
“ Napenda kuwaomba radhi wote kwa kuwakwaza kwa namna moja ana nyingine.
Colin mwanangu nataka kukutamkia hili mbele ya mpenzi wako na Mungu shahidi yangu kama nitakwenda kinyume naomba anifanye kitu chochote kibaya. Kuanzia leo namtambua rasmi Cecy kama mkwe wangu na mipango ya harusi itaanza mara moja. “Cecy mkwe wangu kuna zawadi nitakupa kwa kuonesha msimamo na mapenzi ya dhati kwa mwanangu naamini wewe ndiye mke aliyechaguliwa na Mungu.”
Mama Colin alisema huku machozi yakimtoka, kila mmoja alitokwa na machozi, yalikuwa maneno yenye kuumiza moyo yaliyotaka moyo wa chuma kukufanya usidondoshe chozi.
Colin hakuwa na la kumuuliza mama yake baada ya kila kitu kuwekwa wazi. Mama yao aliwakusanya na kuwakumbatia wote kisha aliwaachia na kutaka kupiga magoti kuwaomba msamaha lakini walimuwahi mama yao kabla hajapiga.
“Hapana mama huna kosa, bali sisi ndiyo tulikwenda tofauti na mawazo yako, tunaomba utusamehe sana. Ombi letu utupe idhini toka moyoni mwako ili tufunge ndoa yenye baraka,” Colin alimwambia mama yake.
“Mungu ananisikia nimeibariki ndoa yenu duniani na mbinguni.”
“Ma’ mkwe, naomba usinipe zawadi yenye gharama kubwa bali kunipa mume wa ndoto yangu, inawezekana uliponiita mkwe na kunieleza nitaolewa na mwanao anayesoma Ulaya ulidhani utani. Na siku nilipomuona nilichanganyikiwa zaidi, moyoni niliamini nimeokota dhahabu katikati ya soko.
“Lakini niliumia siku nilipojua kumbe kuna chagua sahihi la Colin, kuanguka kwangu si ungonjwa bali presha ilipanda na kushindwa kujizua. Niliamua kujitoa na kukaa pembeni huku nikiwa nimejikatia tamaa. Niliumia zaidi siku Mage alipomshusha Colin kwenye gari na kumdhalilisha kwa kweli japo nilikuwa sipendwi niliingilia ugomvi kwa vile chenye thamani kwenye moyo wangu nikikiona kikidhalilishwa.
“Mpaka leo mama unasema maneno matamu kama haya si kwa urahisi bali nimetoka jasho la damu. Nashukuru mama mkwe, nakuahidi kuwa mke bora na kufurahia chaguo lako la awali.”
Ilikuwa furaha siku hiyo iliagizwa shampeni na kufurahi kutambulika rasmi kwa Cecy katika nyumba ya kina Colin.
****
Mipango ya harusi ya Hans na Mage ilikwenda vizuri, mama Mage hakuwa na haja ya kukusanya tena michango ya sherehe zaidi ya kugawa kadi za send of ya harusi ya mwanaye. Katika watu waliopelekewa kadi ya send of ya Mage ni familia ya mama Colin, tena Mage alisisitiza Colin ahudhulie send of yake.
Taarifa zilifika Colin alikubali kuhudhulia kwa kujua hataumia kwani Cecy alikuwepo.
Siku ya sherehe ya send of Colin na Cecy waliingia wakiwa watu wa mwisho, ilikuwa siku ambayo Cecy aliitafuta kwa udi na uvumba kuwaonesha walimwengu kuwa kila mguu hutulia kwenye kiatu saizi yake wala si kuvaa kikubwa kikakupwaya au kidogo kikakubana lakini kwake kilikuwa kimetulia.
Wakiwa wamependeza Colin katika vazi la shati refu la kitambaa cha maua laini na suruali nyeusi na viatu vyeusi vilivyo chongoka kidogo mbele. Cecy alivaa gauni refu jekundu la mikanda mabegani la kitambaa chepesi na viatu virefu vilivyoongeza mzuri wake.
Waliingia taratibu huku Cecy akiuweka mkono wa Colin kwapani kwake na kuushika kwa mbele. Waliingia taratibu na kufanya watu wote wageuze shingo kuwatazama wapenzi wawili walionekana kama ndiyo wamepata shahada ya mapenzi muda si mrefu.
Mage alishtuka kumwona Colin akiwa amependeza sana akiwa na msichana mrembo ambaye alimsahau kama ndiye aliyempa kipigo siku alipomdhalilisha Colin. Moyo ulimlipuka na kujikuta akiingia wivu, Colin alikuwa na tofauti kubwa na Hans kimuonekana alikuwa ana mvuto kwa mwanamke yoyote.
Lakini mapenzi yake Hans yakuwa makubwa kuliko kitu chochote chini ya jua. Colin pamoja na umbile na sura nzuri lakini kwake moyoni kwake alikuwa na nafasi ndogo.
Naye mke matarajiwa alipendeza katika gauni la kitenge alililoshonwa kwa ustadi mkubwa na kumwongezea urembo wake. Aliamini kabisa msichana aliyechukua nafasi yake alikuwa kama maji ya bahari na yeye, kuvunja uchumba na Colin ilikuwa sawa na kuchota maji kwa kikombe ndani yake na kufanya pengo lake lisionekane kabisa.
Sherehe ilienda vizuri kila mtu aliyekuwepo aliisifia jinsi ilivyofana kwa burudani iliyoandaliwa ilifanya wageni wasichoke kuwepo ukumbuni pale.Katika watu walikuwa na furaha siku ile alikuwa mama Colin baada ya kumwona mwanaye alivyopendeza akiwa na Cecy msichana aliyekuwa kama dhahabu iliyokuwa imechafuliwa na tope lakini mwanaye aliisafisha na thamani yake kuonekana mbele ya macho ya watu.

Itaendelea Jumatatu
 
SEHEMU: 19
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500
KIPANDE KILICHORUKWA
Alipotaka kumkaribisha ndani alikataa alisimama mbele ya nyumba, aliyatazama mazingira wanayoishi Cecy na mama yake moyo wake ulichefuka kwa kuona jinsi gani mwanaye alivyopotea maboya kutaka kumuona mwanamke fukara kama yule ambaye halingani na sifa na hadhi ya familia yao.
Lakini alijenga tabasamu la uongo ili kuonekana amefurahi kuonana naye.
“Dada karibu ndani.”
“Napita tu siku nyingine nitaingia, vipi mkwe wangu yupo?”
“Mmh! Amerudi muda si mrefu alikuwa na mwenzake muda si mrefu na kufikia kulala.”
“Naomba uniamshie.”
“Hakuna tatizo dada.”
Mama Cecy alikwenda kumuamsha mwanaye.
“Cecy mwanangu amka kuna ugeni mzito.”
“Nani tena mama?”
“Mama Colin.”
”Uongo!”
“Kweli, amekataa kuingia ndani ana shida na wewe mara moja.”
Cecy aliamka na kujifunga kanga na nyingine alijitanda mabegani na kutoka nje, alipofika nje na kumuona mama Colin aliteremka ngazi haraka na kwenda kumkumbatia kwa furaha.
“Waaawooo! Jamani mama mzaa chema.”
“Ndiye mimi.”
“Mama mbona umeishia nje si uingie ndani.”
“Hapana nina haraka kidogo naomba tuzungumze kwenye gari.”
“Hakuna tatizo.”
Cecy na mama Colin waliingia kwenye gari na kumwacha mama Cecy amekaa kwenye kibaraza huku akiamini ile ni dalili njema za ndoa ya mwanaye baada ya adui kugeuka rafiki.
Baada ya kuingia kwenye gari walifunga vioo vyote na kuwasha AC, Cecy alikuwa mtulivu ili kumsikiliza mama mkwe kipi kimemleta. Baada ya kimya kifupi Cecy alikuwa wa kwanza kuzungumza.
“Ndiyo mama, una habari gani?”
“Cecy nataka kukuliza kitu kimoja, umempenda mwanangu kwa ajili ya mapenzi au kufuata fedha?”
“Kimapenzi,” alimjibu kwa upole huku akimtazama usoni.
“Muongo, wewe mwanangu unampenda kwa ajili ya fedha hivyo nataka uniambie unahitaji kiasi gani ili umuache mwanangu?”
“Mmh! Haya yameenza lini mama na kipi nilichokiomba toka katika familia yenu kuonesha nahitaji fedha?”
“Sikiliza Cecy narudia tena, mwanangu huna mapenzi naye sitaki yatokee ya Mage hivyo naomba uachane naye. Sema unataka kiasi gani?”
“Kuachana na Colin wala sihitaji pesa yako mimi ni maskini niache na umaskini wangu. Unaweza kununua kila kitu lakini huwezi kununua moyo wa mtu.”
“Sikiliza Cecy nitayabadili maisha yenu kwa kuwajengea jumba la kisasa na kuwanunulia wewe na mama yako magari ya kutembelea pia kukufungulia duka kubwa la nguo na vipodozi katikati ya jiji ili tu uachane na Colin.”
“Nimeridhika na umaskini wangu wala usipoteze fedha na nguvu nyingi kuliua penzi letu.”
“Cecy nielewe si kuliua penzi lenu bali kumuokoa mwanangu na mateso, kingine sitaki nawe kuingia kwenye mkumbo huo kwa vile Colin bado anampenda Mage wakirudiana watakuumiza.”
“Sawa nimekuelewa unaweza kwenda,” Cecy alisema kwa mkato.
“Ila ukitoka hapa naomba hili libakie siri yetu.”
“Sawa, ila nami nakutuma kitu kimoja, ukitoka hapa kamkanye mwanao asije hapa la sivyo!”
“Utamfanya nini?”
“Siyo nimfanye nini asije hapa na wewe ukiondoka hapa usikanyage tena, nenda kwa matajili wenzio,” Cecy alisema kwa hasira.
“Cecy usifanye hasira hujui vitu gani vizuri nilivyovipanga kwako.”
Mama Colin alifungua mkoba na kutoka mabunda matano ya milioni mojamoja na kumpa Cecy huku akisema:
“Ukiachana na Colin utapata zaidi ya hizi.”
INAENDELEA HAPA...

ILIPOISHIA:
Cecy alizipokea na kumfanya mama Colin kutabasamu kwa kuamini fedha ni sabuni ya roho. Alizitazama zile fedha kwa uchungu huku machozi yakimtoka na kuona jinsi gani umaskini wao ulivyotumiwa kama kisu butu cha kuupasua moyo wake bila ganzi. Alitulia akilia huku machozi yakidondokea kwenye zile fedha.
SASA ENDELEA...

Kwa hasira alizinyanyua na kumpiga nazo usoni mama Colin na kutoka ndani ya gari, kitu kilichomuacha mdomo wazi mama Colin. Mama yake alishangaa kumuona mwanaye akitoka ndani ya gari akilia.
“Cecy kuna nini?”
“Mama niache kwanza, huyu mama ni mchawi.”
“Mchawi! Kafanya nini?” mama yake alishtuka.
Wakati huo mama Colin kwa aibu aliwasha gari lake na kuondoka bila kuaga. Aliushangaa ujasiri wa Cecy msichana maskini lakini mwenye kujiamini kupita kiasi kwa kukataa fedha zile na ofa ya kuyabadili maisha yao. Hakuamini binti muuza ndizi kukataa fedha zile wakati maisha yao ya kubahatisha. Lakini alijiapiza kwa nguvu kwa hiyari kwa fedha kwa damu lazima Cecy ataachana na Colin.
Mama Cecy alimfuata mwanaye aliyeingia chumbani huku akilia na kushindwa kuelewa mazungumzo ya ndani ya gari yalikuwa ya nini. Alikumta akiendelea kulia kitu kilichomfanya ajiulize kipi kikubwa walichokizungumza ndani ya gari.
Alimkuta amelala kifudifudi akilia kwa sauti ya kwikwi, wasiwasi wake labda Colin amepata tatizo.
“Cecy mwanangu kuna tatizo gani tena?”
“Mama inaumiza sana.”
“Kuna nini mpenzi wako kapata tatizo?”
“Mama mtu anaweza kuununua moyo wangu hata kuuchukua bure nikiwa nimekufa, lakini nikiwa hai siuuzi kwa gharama yoyote kwa vile furaha ya mtu hainunuliwi dukani.”
“Una maana gani?” mama yake alikuwa bado njia panda.
Cecy alimweleza mama yote aliyozungumza na mama Colin, mama yake macho yalimtoka pima kusikia taarifa ile baada ya kuamini kila kitu kilikuwa vizuri kilichobakia ni ndoa ya mwanaye na Colin.
“Mmh! Mbona makubwa madogo yana nafuu,” mama Cecy alisema akiwa amechoka na maneno yale.
“Mama mimi na Colin basi,” Cecy alisema kwa hasira.
“Huo ni uamuzi wa hasira lazima umsikilize mwenzako si amesema atakupitia jioni basi msubiri umsikilize naye anasemaje kama lao moja na mama yake una haki ya uamuzi wako.”
“Mama kosa langu nini? Yaani anatumia fedha zake kuinunua furaha yangu?” Cecy alisema kwa uchungu.
“Mwanangu kama Colin si chaguo la Mungu basi hamtaoana lakini kama ni chaguo la Mungu hakuna kitakachozuia.”
“Yule mwanamke ni mnafikia akiwa na mwanaye ananichekea kicheko cha mamba lakini kumbe ananitamani kunimeza.”
“Wee yaache tusubiri jioni.”
“Sawa, lakini nina amini hakuna ndoa yangu na Colin labda mapenzi ya sisi wenyewe lakini mama yake hanipendi na yupo radhi kutumia njia yoyote kukwamisha mapenzi yetu.”
”Ngoja tumsubiri Colin anasemaje.”
“Namsubiri kwa ajili yako lakini ningekuwa peke yangu asingekanyaga hapa.”
****
Majira ya jioni Colin alimpitia Cecy kama alivyomweleza, aliposimamisha gari alishangaa kutomuona mpenzi wake kama kawaida, kwani aliisha mzoesha vibaya kumpokea kwa kumrukia kwa mahaba motomoto. Baada ya kusimamisha gari aliteremka na kwenda ndani huku akiita jina la Cecy mkononi alikuwa amebeba zawadi za mpenzi wake.
“Beeeebi.”
Hakuwa na jibu zaidi ya kusikia sauti ya kilio toka ndani kitu kilichomshtua na kufanya akimbilie ndani kwa kuamini mpenzi wake yupo kwenye matatizo. Alimkuta Cecy amelala kifudifudi akilia kilio cha sauti.
“Cecy mpenzi una nini?”
“Colin unaweza kununua kila kitu chini ya jua lakini si furaha ya mtu,” Cecy alisema bila kugeuka.
“Kuna nini mpenzi wangu?” Colin alishangaa.
“Umenikuta maskini hata siku moja sikuja kwenu kuomba pesa ya kula, nimeishi kwa kuuza ndizi nitaendelea kuuza ndizi lakini hamuwezi kuutumia umaskini wetu kama siraha ya kununua haki ya moyo wangu.”
“Cecy hebu geuka mpenzi wangu, kipi nimekukosea mpaka useme maneno makali hivyo?”
“Najua hunipenda lakini usitumie gharama kubwa kuniacha, tamko lako ni tosha kuliko gharama na nguvu mnayotaka kuitumia. Ni kweli nakupenda jambo ambalo lipo wazi mbele ya muumba. Lakini ni vigumu kulazimisha mapenzi ni sawa na kumvuta punda mtoni lakini huwezi kumlazimisha kunywa maji.”
“Cecy mpenzi wangu mbona toka jana tumekuwa na siku nzuri ambayo nilitegemea kuimalizia leo. Kipi nilichokufanyia ikiwa nimekuaga nimekwenda kwenye mipango ya maisha yetu ya mbeleni. Nimekuja na furaha ili kukujulisha nimekupatia chuo cha mambo ya urembo ambacho utasoma miezi sita na ukitoka hapo utakuta nimeisha kukufungulia kampuni yako ya urembo.
“Kwa nini wanawake mnapenda kuumiza moyo wangu, Cecy kabla hatujaanza mapenzi ulionesha kunijali lakini kuanza kwa ukaribu wetu hata mwezi bado unataka kuupasua moyo wangu bila ganzi. Cecy niliamini wewe ndiye tiba ya moyo wangu, lakini unataka kuongeza msumali wa moto kwenye kidonda. Naomba basi mnihurumie nami binadamu ninayehitaji upendo. Mapenzi yangu yamekuwa kama mtu anayemwaga maji baharini yasiyoonekana.
“Kwa nini hukuniambia mapema Cecy umeacha nijirushe juu ya ghorofa ya mapenzi nikiamini utanidaka, lakini najiona naangukia pabaya nawe umekataa kunidaka nitakufa kifo kibaya. Cecy utajiri wetu hauingiliani na mapenzi yetu, fedha inaweza kununua kila kitu lakini si penzi la kweli bali upendo wa dhati toka chini ya uvungu wa moyo wa mtu mwenye mapenzi ya kweli asiyeangalia kitu bali mtu mwenyewe alivyo.
“Ni kosa gani nililokufanyia mpaka kufikia kusema maneno mazito yaliyoushtua moyo wangu, kama moyo ungekuwa ukitoka nje naamini ungekuwa unavuja damu kutokana na mshtuko na maumivu ya kuona unatolewa sehemu salama na kutupwa kwenye miba.”
Maneno ya Colin ambaye alionekana hajui kilichokuwa kikiendelea kilimfanya Cecy aongeze sauti ya kilio na kujinyanyua alipokuwa amejilaza na kwenda kujitupa kifuani kwa Colin kitu kilichomshangaza mpenzi wake.
“Cecy mpenzi wangu hebu kuwa mkweli tatizo nini mpaka kusema maneno makali? Nipo radhi kujitoa muhanga ili kuliokoa penzi letu.”
“Colin najua unanipenda lakini mama yako hanipendi,” Cecy alisema kwa sauti ya kilio.
“Bebi, maneno gani hayo ikiwa jana uliona alivyokufurahi, yasahau yote yaliyopita.”
“Colin, mama yako mnafiki, ana tabia ya unafiki wa mamba anakuchekea machoni lakini moyo anakuchukia.”
“Kwa nini unasema hivyo?” Colin alishtuka kusikia vile.
“Mama yako hataki tuwe pamoja yupo radhi kutumia gharama yoyote kuhakikisha anatutenganisha.”
“Lakini mbona yaliisha.”
Cecy aliamua kumweleza ukweli, ujio wa mama yake na ahadi na fedha aliyotoa kwa ajili kulivunja penzi lao. Colin alibakia macho yamemtoka pima asiamini maneno ya Cecy.
“Cecy unayosema ni kweli?”
“Nimzulie uongo mama yako ambaye kama tungeoana angekuwa mama mkwe wangu.”
“Kama kafikia hatua hiyo naomba kwanza unisamehe sana, najua nitafanya nini. Ila nakuahidi kwa kuonesha msimamo umezisha upendo moyoni mwangu, pia hela aliyotaka kukupa nitakupa mara kumi yake na kutimiza ahadi yangu kwa kulijenga penzi letu.”
“Colin, narudi huwezi kuununua moyo wangu.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Sihitaji pesa zako kwa ajili yakuonesha kuwa unanipenda bali mapenzi ya dhati toka kwako. Pendo langu halina gharama japo ni ghali kwa vile nilikubali kukupenda kama ulivyo wala si kwa ajili ya gari, majumba au fedha zenu.”
“Asante kufahamu hivyo, basi naomba ukaoge ili twende nilipokueleza jana.”
“Sawa mpenzi wangu.”
“Pia, kesho mtahama ili kupisha ujenzi wa nyumba yenu kwa muda, nimewatafutie nyumba nzima ambayo nimelipia kwa mwaka mzima.”
“Kwani hiyo nyumba unachukua muda gani kujengwa?”
“Nitaka ijengwe vizuri hata miezi miwili au mitatu.”
“Basi si ungechukua miezi mitatu?”
“Msiwe na wasi, niliwaambia wakakataa wakataka mwaka mzima.”
“Ipo wapi?”
“Kimara Baruti.”
“Asante mpenzi wangu,” Cecy alimkumbatia Colin kwa furaha na kuyasahau maumivu yote.
Cecy alikwenda kuoga akimuacha Colin ambaye alihisi kichwa kinataka kupasuka kwa mawazo kutokana na alichokifanya mama yake aliyeamini ndiyo muongozo wake na kuitengeneza furaha lakini kwake ilikuwa kinyume. Alipanga akitoka pale kwenda na Cecy nyumbani kwao ili mama yake akayasema yale mbele yake.
Baada ya Cecy kumaliza kuoga na kubadili nguo ambazo zilizidi kumpandisha chati na kumfanya aonekane binti mrembo kuliko wanawake wote duniani mbele Colin. Walishikana mikono na kuelekea ndani ya gari na kuelekea moja kwa moja nyumbani kwao Colin.
“Colin unanipeleka wapi?” Cecy alishtuka.
“Usihofu naomba unifuate na mimi.”
“Mmh! Sawa.”
Gari lilipiga hodi na geti lilifunguliwa na Colin kuliingiza ndani, kama kawaida alizunguka na kumfungulia mlango kisha alimshika mkono na kuingia naye ndani. Sebuleni alikuwa mama Colin akizungumza na msichana wa kazi alipomuona Colin alinyanyua macho na kumuona ameongoza na hasimu wake.
Alijikuta akiponyokwa na glasi ya juisi aliyokuwa ameshikilia. Cecy alisogea hadi karibu na mama Colin na kumsalimia.
“Shikamoo ma mkwe,” kama kawaida alipiga goti la heshima mpaka chini.
Mama Colin alinyanyuka alipokuwa amekaa na kumfuata Cecy na kumnyanyua alipokuwa bado amepiga magoti na kumkumbatia kwa muda huku machozi yakimtoka.
Colin alishangazwa na mama yake kufanya vile aliamini alifanya vile kujitakasa mbele ya macho ya mwanaye lakini moyoni alikuwa na nia mbaya kuliko bomu la kutegwa. Alijiuliza mama yake atamwambia nini kwa kitendo cha kigaidi alichokifanya cha kusambalatisha penzi lake.
“Cecy,” alimwita huku akimshika mabegani na kumtazama usoni kwa macho yaliyojaa machozi.
“Abee ma’ mkwe,” Cecy aliitikia huku naye machozi yakimtoka.
“Najua siku ya leo huenda hutanielewa, unaweza kuwa msichana wa kwanza kunionesha kitu si cha kawaida. Lakini nilichokifanya leo ni mtihani wangu wa mwisho kwako, nakili kwa moyo wangu katika wasichana niliowapenda ulikuwa wewe namba moja.
“Lakini sikumaanisha kuwa utakuwa mke wa mwanangu kwa vile nilikuwa na Malengo makubwa kwa mwanangu baada ya kutumia kiasi kikubwa kumsomesha.
Niliamini mwanamke atakayemfaa ni mwenye elimu kama yake pia anayetoka katika familia yenye uwezo ambaye atakuwa na mapenzi ya kweli na hatafuata mali aliyonayo mwanaume.
“ Niliamini chaguo langu lilikuwa sahihi la kumchagua Mage kwa vile ni msomi tena anatoka katika familia yenye uwezo pia mama yake ni shoga yangu. Lakini kumbe siyo, nakiri toka moyoni mwangu mapenzi niliyokuwa nikimpenda Cecy yaligeuka na kumuona ni adui namba moja anayetaka kuvuruga ndoto zangu.
“Mwanzo nilidhani utani lakini siku ya birthday ya Colin nilivyokuona ulivyopendeza mpaka kukusahau na picha nilizomkuta nazo Colin niliona ndoa hakuna. Moyo wangu ulikosa amani mpaka mipango ya harusi kwenda vizuri huku nikiwa sisikii taarifa yako.
“Kwa kweli niliumia sana kwa kitendo cha Mage kuuvunja uchumba tukiwa katika hatua za mwisho. Siku zote nilikosa usingizi nimekuwa nikipungua siku hadi siku. Kitendo cha kuibuka wewe kwa kweli kilinichanganya sana, sikuamini kama una mapenzi ya kweli na mwanangu zaidi ya kufuata mali zetu.
“ Mtihani niliokupa leo umenipa sababu sahihi ya mwanangu kukuchagua wewe kuwa mkewe. Cecy kitendo cha leo kilifukua mapenzi yote ya nyuma na kukiri mapenzi si elimu wala mali bali upendo wa dhati toka moyoni mwa mtu. Umenionesha jinsi gani unavyo mpenda mwanangu mapenzi ya dhati si kwa ulichonacho.
“ Napenda kuwaomba radhi wote kwa kuwakwaza kwa namna moja ana nyingine.
Colin mwanangu nataka kukutamkia hili mbele ya mpenzi wako na Mungu shahidi yangu kama nitakwenda kinyume naomba anifanye kitu chochote kibaya. Kuanzia leo namtambua rasmi Cecy kama mkwe wangu na mipango ya harusi itaanza mara moja. “Cecy mkwe wangu kuna zawadi nitakupa kwa kuonesha msimamo na mapenzi ya dhati kwa mwanangu naamini wewe ndiye mke aliyechaguliwa na Mungu.”
Mama Colin alisema huku machozi yakimtoka, kila mmoja alitokwa na machozi, yalikuwa maneno yenye kuumiza moyo yaliyotaka moyo wa chuma kukufanya usidondoshe chozi.
Colin hakuwa na la kumuuliza mama yake baada ya kila kitu kuwekwa wazi. Mama yao aliwakusanya na kuwakumbatia wote kisha aliwaachia na kutaka kupiga magoti kuwaomba msamaha lakini walimuwahi mama yao kabla hajapiga.
“Hapana mama huna kosa, bali sisi ndiyo tulikwenda tofauti na mawazo yako, tunaomba utusamehe sana. Ombi letu utupe idhini toka moyoni mwako ili tufunge ndoa yenye baraka,” Colin alimwambia mama yake.
“Mungu ananisikia nimeibariki ndoa yenu duniani na mbinguni.”
“Ma’ mkwe, naomba usinipe zawadi yenye gharama kubwa bali kunipa mume wa ndoto yangu, inawezekana uliponiita mkwe na kunieleza nitaolewa na mwanao anayesoma Ulaya ulidhani utani. Na siku nilipomuona nilichanganyikiwa zaidi, moyoni niliamini nimeokota dhahabu katikati ya soko.
“Lakini niliumia siku nilipojua kumbe kuna chagua sahihi la Colin, kuanguka kwangu si ungonjwa bali presha ilipanda na kushindwa kujizua. Niliamua kujitoa na kukaa pembeni huku nikiwa nimejikatia tamaa. Niliumia zaidi siku Mage alipomshusha Colin kwenye gari na kumdhalilisha kwa kweli japo nilikuwa sipendwi niliingilia ugomvi kwa vile chenye thamani kwenye moyo wangu nikikiona kikidhalilishwa.
“Mpaka leo mama unasema maneno matamu kama haya si kwa urahisi bali nimetoka jasho la damu. Nashukuru mama mkwe, nakuahidi kuwa mke bora na kufurahia chaguo lako la awali.”
Ilikuwa furaha siku hiyo iliagizwa shampeni na kufurahi kutambulika rasmi kwa Cecy katika nyumba ya kina Colin.
****
Mipango ya harusi ya Hans na Mage ilikwenda vizuri, mama Mage hakuwa na haja ya kukusanya tena michango ya sherehe zaidi ya kugawa kadi za send of ya harusi ya mwanaye. Katika watu waliopelekewa kadi ya send of ya Mage ni familia ya mama Colin, tena Mage alisisitiza Colin ahudhulie send of yake.
Taarifa zilifika Colin alikubali kuhudhulia kwa kujua hataumia kwani Cecy alikuwepo.
Siku ya sherehe ya send of Colin na Cecy waliingia wakiwa watu wa mwisho, ilikuwa siku ambayo Cecy aliitafuta kwa udi na uvumba kuwaonesha walimwengu kuwa kila mguu hutulia kwenye kiatu saizi yake wala si kuvaa kikubwa kikakupwaya au kidogo kikakubana lakini kwake kilikuwa kimetulia.
Wakiwa wamependeza Colin katika vazi la shati refu la kitambaa cha maua laini na suruali nyeusi na viatu vyeusi vilivyo chongoka kidogo mbele. Cecy alivaa gauni refu jekundu la mikanda mabegani la kitambaa chepesi na viatu virefu vilivyoongeza mzuri wake.
Waliingia taratibu huku Cecy akiuweka mkono wa Colin kwapani kwake na kuushika kwa mbele. Waliingia taratibu na kufanya watu wote wageuze shingo kuwatazama wapenzi wawili walionekana kama ndiyo wamepata shahada ya mapenzi muda si mrefu.
Mage alishtuka kumwona Colin akiwa amependeza sana akiwa na msichana mrembo ambaye alimsahau kama ndiye aliyempa kipigo siku alipomdhalilisha Colin. Moyo ulimlipuka na kujikuta akiingia wivu, Colin alikuwa na tofauti kubwa na Hans kimuonekana alikuwa ana mvuto kwa mwanamke yoyote.
Lakini mapenzi yake Hans yakuwa makubwa kuliko kitu chochote chini ya jua. Colin pamoja na umbile na sura nzuri lakini kwake moyoni kwake alikuwa na nafasi ndogo.
Naye mke matarajiwa alipendeza katika gauni la kitenge alililoshonwa kwa ustadi mkubwa na kumwongezea urembo wake. Aliamini kabisa msichana aliyechukua nafasi yake alikuwa kama maji ya bahari na yeye, kuvunja uchumba na Colin ilikuwa sawa na kuchota maji kwa kikombe ndani yake na kufanya pengo lake lisionekane kabisa.
Sherehe ilienda vizuri kila mtu aliyekuwepo aliisifia jinsi ilivyofana kwa burudani iliyoandaliwa ilifanya wageni wasichoke kuwepo ukumbuni pale.Katika watu walikuwa na furaha siku ile alikuwa mama Colin baada ya kumwona mwanaye alivyopendeza akiwa na Cecy msichana aliyekuwa kama dhahabu iliyokuwa imechafuliwa na tope lakini mwanaye aliisafisha na thamani yake kuonekana mbele ya macho ya watu.

Itaendelea Jumatatu
 
SEHEMU: 20
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500

ILIPOISHIA:
Katika watu walikuwa na furaha siku ile alikuwa mama Colin baada ya kumwona mwanaye alivyopendeza akiwa na Cecy msichana aliyekuwa kama dhahabu iliyokuwa imechafuliwa na tope lakini mwanaye aliisafisha na thamani yake kuonekana mbele ya macho ya watu.
SASA ENDELEA...

Katika kitu kilichomvutia siku ile ni jinsi Cecy alivyojiamini sana, kwake lilikuwa kama jibu ambalo alitamani siku moja Mage alipate baada ya kumuacha mwanaye. Kitendo cha kuonesha mapenzi mazito kwa mwanaye kilimpa faraja kubwa moyoni mwake na kujiapiza kumpa zawadi kubwa japokuwa alionesha Cecy haitaji zawadi ambayo aliitafsiri kama hongo.
Alipanga siku ya harusi ya mwanaye ampe Cecy zawadi ya nyumba ambayo ataanza kuijenga wakati wowote na zawadi ya gari la kifahari ili kurudisha shukurani kwake kumwokoa mwanaye aliyeachwa ghafla kama chuma cha moto kilichozimwa kwa kumwagiwa maji ya baridi lazima kipinde.
Aliamini kitendo Mage kumuacha ghafla lazima angekuwa kwenye hali mbaya lakini yeye alikuwa wokozi wake na kulipigania penzi la mwanaye mpaka mwisho kuibuka mshindi. Kila alipoyafikiria yale na kuangali mwanaye na Cecy walivyopendeza alimshukuru Mungu kutenda muujiza.
Sherehe iliendelea ilifika wakati wa Mage kwenda kumnyanyua mumewe matarajiwa alipokaa. Alinyanyuka alipokuwa na kuanza kumtafuta Hans aliyekuwa amekaa nyuma, alizunguka taratibu kwenye meza akimtafuta. Kwa vile toka Colin aingie na msichana mrembo alikuwa na hamu ya kutaka kuthibitisha uzuri aliouona kwa mbali ni kweli au cosmetic na vazi ndivyo vililompandisha chati.
Alitembea taratibu kwa kumtafuta kila meza iliyokuwa na mwanaume, alikwenda hadi kwenye meza aliyokuwa amekaa Colin na Cecy. Akitembea kwa mwendo wa taratibu alisogelea karibu macho yake yakiwa kwenye uso wa Cecy. Pamoja na kupata jibu lililokuwa akiusumbua moyo wake tangu Colin alipoingia akiwa ameongozana na msichana mrembo ambaye aliamini yule msichana ndiye mrembo kuliko wote waliokuwepo pale ukumbini.
Alishtuka kuiona sura ya Cecy, moyo ulimshtuka baada ya kumkumbuka ndiye aliyemshushia kipigo siku alipomteremsha Colin kwenye gari lake. Moyo ulimuuma kuona pamoja na kumpenda Colin kumbe alikuwa na msichana wa pembeni. Japokuwa sura ilikuwa yenyewe alitaka kujua jina lake kwa vile jina aliloitwa na Colin siku ile alikuwa akilikumbuka ili kupata uhakika asilimia mia.
“Mambo Colin?” Mage alisimama kidogo meza ya Colin na kumsemesha.
“Poa, hongera.”
“Asante, huyu ndiye wifi?”
“Si wifi ni mke mwenzio,” Cecy alijibu.
“Mmh! Anaitwa nani?”
“Cecy.”
“Si..si ndiye aliye ni…ni..”
“Shoga ndiye mimi, wee kamtafute mumeo mengine achana nayo,” Cecy alimpa makavu huku akibinua midomo ya dharau na kumpiga busu Colin.
Mage hakuwa na jibu aliondoka bila kuongeza neno akitamani kuomba Cecy aondolewe kwenye sherehe yake na kujilaumu kumwalika Colin kwani aliharibu furaha yake yote ya siku ile.
Baada ya kuzunguka meza kadhaa alifika alipokuwa Hans, alimshika mkono na kufanya ukumbi ulipuke kwa furaha. Aliongozana hadi meza iliyoandaliwa maalumu kwa ajili ya kukaa pamoja. Sherehe iliendelea huku zoezi la chakula likianza kwa kutangulia Mage na mumewe mtarajiwa.
Baada ya maharusi watarajiwa kuchukua chakula, wengine walifuata na kurudi kwenye nafasi zao. Wakiwa katika ya chakula aliingia mwanaume mmoja mtanashati lakini mwenye mwili mkakamavu hadi kwa MC na kuzungumza naye kitu na kuonesha meza aliyokaa bibi na bwana harusi watarajiwa.
Yule bwana alikwenda kwenye meza ya chakula alipokuwa amekaa bwana harusi na kumwomba wazungumze nje ya ukumbi. Hans alikitaka wazungumze pale ilibidi yule bwana amnong’oneze kitu. Ghafla Hans alikuwa mpole na kumwambia Mage.
“Samahani mpenzi nakuja.”
“Kuna nini?” Mage alishtuka.
“Nakuja sasa hivi.”
“Fanya haraka bwana.”
“Poa.”
Hans alijibu kwa mkato na kuongozana na yule mtu hadi nje ya ukumbi, alipofika nje alielekezwa gari la kuingia lilikuwa limesimama pembeni ya ukumbi. Alipofungua mlango na kukaa alikutana na pingu huku akiambiwa.
“Tuna imani kosa lako unalijua?”
Hans hakujibu alikaa kimya, baada ya kutojibu askari alimuuliza swali lingine.
“Unamjua huyu?”
Alioneshwa kijana mmoja aliyekuwa amemekaa pembeni yake ameinamisha kichwa. Alipomwangalia vizuri alimkumbuka na alishtuka na kujisema moyoni. “Nimekwisha.”
Hans alichukuliwa na kupelekwa kituo cha polisi kwa mahojiano zaidi. Alipofika aliingizwa chumba maalumu kwa ajili ya mahojiano. Kila aliloulizwa kuhusiana na kuhusika na njama za kuuawa mkewe na mwanaye alibakia bubu, baada ya kubana sana alikubali kuhusika kwa namna moja japo yeye hakuua.
Nyuma sherehe iliendelea huku Mage akiamini mchumba wake atarudi wakati wowote, baada ya muda bila kuonekana ilibidi aulize kuhusu mchumba wake.
Mara moja walianza kufuatilia, kwa kumuuliza rafiki kipenzi cha Hans, Ndubikile ambaye alikuwa amekaa bila kujua nini kinaendelea.
Hata yeye alishtuka sana na kuamua kupiga simu yake ambayo ilipokelewa na mtu mwingine.
“Haloo una shida gani?”
“Samahani nina imani napiga namba ya Hans?”
“Ndiyo.”
“Mwenye simu yupo wapi?”
“Yupo kituo cha polisi cha kati.”
“Ha! Amefanya nini?”
“Ukifika kituoni utajua kila kitu.”
“Sawa.”
Baada ya kukata simu aliwageukia waliokuwa wakitaka kujua kutoweka ghafla kwa Hans.
“Jamani waliomchukua hapa ni askari ambao wamempeleka kituoni cha kati.“
“He! Kwa kosa gani?” waliuliza wote kwa mshangao.
“Wamesema tufike kituoni tutajua kila kitu.”
Ilibidi watu watumie busara na kuficha kilichokuwa kikiendelea na kumdanganya Mage ili shughuli isivurugike kwa kumwambia Hans amekimbilia hospitali mdogo wake kapata ajali. Wakati sherehe ikiendelea familia ya Hans ilipewa taarifa zile nayo iliondoka kufuatilia kituoni.
Walipofika walielezwa kuwa Hans anashikiliwa na polisi kwa kosa la kupanga mauaji ya mkewe na mwanaye. Wote walishtuka na kutaka isibitisho wa habari zile, walielezwa jinsi walivyofuatilia mauaji yale taratibu mpaka kuwakamata wauaji ambao walijitetea kutumwa na Hans ili aweze kumuona mpenzi wake wa zamani.
Waliomba kukutana na Hans, walikutana naye na kutaka kujua habari zile zina ukweli wowote.
“Wazazi wangu hakuna ukweli wowote, haiingii akilini nimuue mke wangu na mwanangu kwa ajili ya mwanamke.”
“Basi mwanangu haki itapatikana, nina imani mpaka kunakucha utakuwa umetoka nje,” baba Hans alimpa moyo mwanaye ambaye moyoni alijua kila kitu kinachoendelea.
Kuondoka ghafla kwa familia ya Hans ilizidi kumshtua Mage na kujikuta akikata kususa sherehe. Ilibidi achukuliwe na kupelekwa pembeni na kuelezwa ukweli kuwa mpenzi wake kachukuliwa na polisi. Aliomba kupelekwa kituo cha polisi ili akamwone mpenzi wake kwa kuamini kupitia kwa rafiki wa baba yake mkuu wa polisi atatoka.
Alifikishwa kituo cha polisi na kupelekwa chumba alichokuwemo mpenzi wake na kuonana naye. Mage akiwa amechanganyikiwa macho yakiwa yamemvimba kwa ajili ya kumlilia mpenzi wake ambaye hakujua yupo pale kwa kosa gani.
“Vipi mpenzi kuna nini?”
“Mmh! Mambo magumu.”
“Kivipi?”
“Ile ishu imebumburuka.”
“Ishu gani?”
“Off air”
“Mungu wangu! Sasa itakuwaje?”
“Sijui, lakini naamini imekaa vibaya kwa vile kuna ushahidi mkubwa wa kunimaliza naamini siwezi kutoka.”
“Kwa nini?”
“Kila kitu kipo wazi lazima nitaozea gerezani.”
“Sasa harusi yetu itakuwaje?”
“Mmh! Itategemea muujiza wa ngamia kupita katika tundu la sindano.”
“Yupo ba’ mkubwa naamini utatoka tu,” Mage alimtia moyo mpenzi wake.
“Nami ndicho ninachokiomba.”
“Hebu subiri.”
Mage alichukua simu na kumpigia baba yake mkubwa mkuu wa polisi mzee Clarence. Baada ya kuita ilipokelewa upande wa pili.
“Haloo.”
“Haloo baba,” Mage alisema kwa sauti ya kulia.
“Vipi mama, mbona unalia?”
“Baba mchumba wangu amechukuliwa kwenye send of yangu na kuwekwa ndani.”
“Kwa kosa gani?”
“Hakuna kosa lolote zaidi ya uonevu.”
“Naomba kuzungumza na mkuu wa kituo.”
“Sawa baba.”
“Mpenzi nimeisha zungumza na baba utatoka sasa hivi ngoja nipeleke simu kwa mkuu wa kituo,” Mage alimueleza mpenzi wake huku akielekea kwa mkuu wa kituo.
“Hakuna tatizo.”
“Samahani kaka kuna simu kutoka kwa mkuu anataka kuzungumza na mkuu wa kituo,” alimwambia askari mmoja aliyekuwa kaunta.
“Mkuu gani?”
“Mkuu wa polisi wote.”
“Nenda chumba cha pili mkono wa kushoto.”
Mage alikwenda hadi mlangoni na kuingia bila hodi kitu kilicho mkasirisha mkuu wa kituo na kutaka kumfukuza.
“We binti toka nje unaingiaje kama msalani.”
“Kuna simu yako toka kwa mkuu wako unatakiwa kuzungumza naye.”
“Mkuu gani?”
“IGP.”
“He! Nipe,” mkuu wa kituo Aloyce Jacob alishtuka na kuichukua simu haraka aliweka sikioni na kusema kwa sauti ya juu.
“Samahani afande.”
“Bila samahani pole na majukumu.”
“Asante mkuu.”
“Kuna kijana mmemkamata usiku huu akiwa kwenye send of ya mchumba wake?”
“Ndiyo mkuu.”
“Kwa kosa gani?”
“Lile la mauaji tulilokuwa tukipeleleza.”
“Sasa yeye anahusika vipi?”
“Ndiye mtuhumiwa mkuu.”
“Una uhakika?”
“Kila kitu kipo wazi, kesho faili lake tunaifikisha mahakamani.”
“Nipe huyo binti.”
Simu alipewa Mage aliyekuwa akifuatilia mazungumzo ambayo yalimtisha na kuona tatizo la mpenzi wake lilivyo zito lakini aliamini kupitia wadhifa wa baba yake mkubwa lazima ataachiwa tu.
“Haloo baba.”
“Sasa mama suala la mpenzi wako lipo kisheria sana, hivyo nakuomba rudi nyumbani ili vyombo vya dola vifanye kazi yao.”
“Sasa baba harusi yangu itakuwaje?”
“Naomba urudi nyumbani kesho nitakuja.”
“Sawa baba.”
Mage alirudi kwa Hans kumweleza alipofikia, Hans aliamini hali ilivyo kulikuwa hakuna dhamana mpaka upelelezi ukamilike. Aliamini ukikamilika lazima utamtia hatiani na kufungwa.
Ilibidi Mage arudi nyumbani kwao akiwa amechanganyikiwa kutokana na tukio lile aliamini ndoa hakuna na atakuwa amepoteza mwana na maji ya moto. Kwa vile sherehe ilimalizwa alirudi nyumbani. Mama yake naye aliona sherehe ya mwanaye imeingia nuksi alitaka kujua kipi kilichompeleka mchumba wake polisi.
“Si lile tatizo lililoniweka ndani.”
“La kifo cha mke wa Hans?”
“Ndiyo.”
“Sasa yeye anahusika vipi?”
“Eti kahusika kumuua mkewe.”
“He! Ili iweje?” mama Mage alishtuka kusikia habari zile.
“Mimi sijui, eti mama mtu akishtakiwa kwa kosa la kupanga mauaji hukumu yake ipo vipi?”
“Kama hajatenda hawezi kufungwa lakini kama kweli amehusika hukumu yake ni miaka 30 au maisha.”
“Mungu wangu nimekwisha!” Mage alisema kwa sauti ya kukata tamaa.
“Mbona unasema hivyo?”
“Mashtaka ya Hans ni ya kupanga njama za kifo cha mkewe.”
“Sasa wasiwasi wako nini ikiwa haimuhusu, nitampigia simu baba yako mkubwa yataisha.”
“Mama nilizungumza na baba na kutaka kuzungumza na mkuu wa kituo baada ya mazungumzo aliniambia mashtaka yapo kisheria hivyo tuache vyombo vya dola vifanye kazi yake.”
“Mmh! Kama baba yako kasema hivyo itabidi tuwe watulivu.”
“Mama nina wasiwasi huenda harusi yangu haipo.”
“Kwa nini?”
“Nina wasiwasi mpenzi wangu atafungwa.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Hata sijui, mama hivi nikimfuata Colin atakubali kweli kunirudia?”
“Mage umefikiria nini tena mama! Kwa nini umefikia huko, mchumba wako yupo ndani na hana kosa asilotenda atatoka tu.”
“Sasa tutafanyaje?”
Mara simu ya Mage iliita ilikuwa ikitoka kwa mama Hans, alichukua na kuiweka sikioni.
“Haloo mama.”
“Nina imani sasa imefurahi.”
“Nifurahi nini mama?”
“Haya sasa mwanangu anafungwa kwa ajili yako, haya fanya sherehe kwa vile dhamira yako imetimia, imekuwa kama jini wa kutumwa humuachi mtu mpaka uone amefukiwa. ”
“Mama utanionea bure.”
“Tunashukuru ila Mungu yupo,” baada ya kusema vile alikata simu na kumuacha Mage kasimama kama sanamu kitu kilichomshtua mama yake.
“Nini tena?”
“Mama huu mkosi gani?” Mage alisema huku akilia.
“Kwani kuna nini tena mwanangu mbona unatakaa kuniuguza presha?” mama yake alitaharuki.
“Siamini maumivu ninayosikia juu ya mpenzi wangu kuwekwa ndani na kubambikiwa kesi nzito halafu familia yake inasema eti nimefurahi! Mimi Mage nifurahi kufungwa kwa mpenzi wangu?” Mage alimuuliza mama yake huku akibubujikwa na machozi ya uchungu.

Itaendelea
 
SEHEMU: 21
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500

ILIPOISHIA:
“Siamini maumivu ninayosikia juu ya mpenzi wangu kuwekwa ndani na kubambikiwa kesi nzito halafu familia yake inasema eti nimefurahi! Mimi Mage nifurahi kufungwa kwa mpenzi wangu?” Mage alimuuliza mama yake huku akibubujikwa na machozi ya uchungu.
SASA ENDELEA...

“Nani amekuambia hivyo?”
“Mama Hans.”
“Unaona mwanangu ile siyo familia badala ya kukuonea huruma ndiyo kwanza wanakulaumu, ufanye vile ili iweje ungeweza kuvuruga ndio yako kama mtu humpendi.”
“Mama nakuapia Hans akinioa sitaki kuwaona ndugu wa mume.”
“Mage mwanangu hayo siyo maneno, bado tunataka kuonesha upendo kwa wenzetu kipindi hiki kigumu.”
“Mama wakati Hans yupo ndani nataka kuzungumza na Colin naamini ananipenda sana.”
“Ukiisha zungumza naye?”
“Ili nikamate huku na huku kama Hans atafungwa basi niwe na Colin.”
“Na Hans akitoka gerezani na kukuta umeolewa?”
“Nitajua, nina imani Colin nammudu, nitamweleza ukweli kuwa kwake nilikuwa najiegesha na nimpendaye karudi. Mbona anajua kuwa kwa Hans nimekufa nimeoza.”
“Mage kumbuka ukianzisha uhusiano na Colin mpaka kufikia kufunga ndoa lazima watu watasema umehusika kumfunga mpenzi wako hapo ndipo utaongeza uhasama na familia ya kina Hans.”
“Nitafanya kwa siri.”
“Colin akitaka kukuoa?”
“Nitamvuta kwa muda ili kumsubiri Hans, kama anafungwa maisha sina jinsi kama miaka saba nitajishikiza kwa Colin.”
“Ulivyomuacha atakukubali kweli, ha..ha..lafu leo kaingia na msichana mrembo ni nani yake?”
“Mpenzi wa rafiki yake,” Mage aliongopa.
“Mmh! Ili kutengeneza mazingira mazuri unatakiwa kujipendekeza kwa mama Colin.”
“Nitafanya hivyo, najua yule mama ananipenda sana nikimfuata na kumweleza nimerudi kwa mwanaye nina imani atapiga vigelegele.”
“Mmh! Haya.”
Mage aliachana na mama yake na kwenda chumbani huku mawazo yake yote yakiwa kwa Colin kutokana na kuujua ukweli wa kesi ya Hans kwa kuamini kutoka kutakuwa muujiza. Alipanga kuanza kujipendekeza kwa familia ya kina Colin wakati akisubiri hukumu ya mpenzi wake.
****
Colin alimpeleka Cecy chuo cha urembo ambako alisoma kwa miezi mitatu, muda wote walikuwa kama kumbikumbi kila mmoja alionesha mahaba mazito. Taarifa ya kukamatwa mchumba wa Mage iliwafikia na kushagaa taarifa ya kukamatwa kwake kuwa alihusika na kifo cha mkewe na mwanaye ili tu amuoe Mage.
“Colin yaani naomba kama mama yako atasababisha tutengane usifanye kama mpenzi wa Mage alivyofanya. Heshimu uhai wa mtu, kama ipoipo tu, Mungu ana maajabu yake ameweza kutukutanisha pamoja bila sisi wenyewe kujua. Kwa hivyo ni makosa kulazimisha kitu.”
“Cecy kila dakika nakuwa mwanafunzi wako, wewe ni zaidi ya mwanamke pamoja na umri mdogo lakini Mungu amekupa busara na hekima.”
“Kama ni kweli mpenzi wa Mage anahusika kutenda unyama ule kwa ajili ya Mage atakuwa ametenda dhambi kubwa sana.”
“Mi’ siamini mtu anaweza kumuua mke na mwanaye kwa ajili ya mpenzi wake.”
“Kwa hiyo ungemuoa Mage, mimi ningekuwa na nafasi gani moyoni mwako?” Cecy alimuuliza swali la kizushi.
“Cecy tuachane na hayo, unakumbuka wiki ijayo ndiyo onesho lako la kwanza la mavazi, mazoezi yako yamenipa matumaini ya kuishtua dunia.”
“Mmh! Nitafunikaje maana nguo zote nilizojipima hadi mwenyewe najione wivu, si vibaya kujisifia mi’ mzuri bwana.”
”Siyo mzuri bali mrembo,” Colin alimrekebisha.
“Bwana eeh, urembo unatengenezwa lakini uzuri ni wa asili.”
“Sawa mama umeshinda.”
Wiki moja baadaye liliandaliwa onesho la kwanza la mavazi la kampuni ya Colin litakalo ongozwa na Cecy. Matangazo yalirushwa mwezi mzima katika vyombo vyote vya habari na kufanya watu wengi wavutike na kuapa kutolikosa. Miongoni mwa watu walipanga kwenda kwenye onesho hilo la kwanza la kimataifa alikuwa ni Mage na shoga yake Brenda.
Washiriki walikuwa wengi kutoka ndani na nje ya nchi na kufanya onesho lile lizidi kuvutia watu wengi. Siku ya onesho ilipowadia Mage na shoga yake Brenda walikuwa miongoni ma watu waliohudhulia onesho hilo lililojaza watu wengi. Muda ulipofika maonesho yalianza kwa kuanza kupita wageni ambao walionesha mavazi ya kigeni na kuwafanya watu walipuke mayowe.
Baada ya kumaliza wageni lilianza vazi la Kitanzania kuanzia vazi la vitenge, khanga na vikoi.Walianza kutangulia mabinti ambao nao walikuwa katika kampuni hiyo. Baada ya kupita wote ikafika kipindi akatokea Cecy katika vazi la kitenge chenye kilemba kirefu na kufanya ukumbi ulipuke mayowe.
Alipita na mavai zaidi ya kumi ya ubunifu na kuacha historia kwenye onesho lile.
“Mage huyu si yule msichana aliyeingia na Colin siku ya Send of yako?” Brenda aliuliza baada ya kumfananisha Cecy.
“Ndiye yeye.”
“Mage tuache utani msichana huyu mzuri tena ana uzuri wa asili,” Brenda alimsifia Cecy.
“Hana lolote uzuri upo wapi?” Mage aliponda.
”Wivu huo, kwenye ukweli uongo hujitenga, yule msichana mzuri.”
“Brenda tutakorofishana tumekuja kuangalia mavazi au kuja kumsifia mtu, kwanza mavazi aliyovaa ya kishamba nani sasa hivi anavaa mavazi ya khanga na kitenge. Angejua wala hakupendeza lolote,’ Mage alimbeza Cecy.
“Mageee! Siamini kama una nafasi katika moyo wa Colin, kitu kama hiki hata mimi nikimuona yupo na mpenzi wangu lazima nipate presha,” Brenda alizidi kumuumiza roho shoga yake.
“Brenda naona umetumwa kuja kuniumiza roho, kosa langu kuja na wewe pamoja?” Mage alikuja juu.
“Lakini Mage kwani nikimsifia yule mwanamke kuna ubaya gani ikiwa wewe ni mchumba wa mtu na Colin si mtu wako?”
“Unajuaje kama nitarudiana na Colin.”
“Mrudiane kivipi ikiwa wewe utaolewa na Hans na Colin anaweza kumuoa huyo msichana.”
Wakiwa katikati ya onesho Colin ambaye alifahamika kama mkurugenzi wa kampuni ile ya urembo na mavazi alifuatwa na watu wenye majarida ya urembo kumtaka Cecy kwa ajili ya kuyapamba majarida yao kwa sura yake kwa mkataba mnono. Pia makampuni mengine ya Afrika ya kusini na Ufaransa ambao walikuwa wageni waalikwa walivutiwa Cecy na kuomba kufanya naye kazi kwa mkataba mnono.
Nyota ya Cecy ilizidi kung’aa, Colin aliwakubalia lakini walitakiwa waonane kesho kwa ajili ya mazungumzo zaidi, walikubaliana. Siku ile pia ilikuwa maalumu kwa Colin. Wakati burudani ikiendelea Mc alisimamisha kwa ili mkurugenzi aseme neno.
Colin alichukua kipaza sauti na kuwasalimia wote kisha alisema:
“Ndugu zangu kwanza nashukuru kwa muitikio katika onesho la leo ambalo limekuwa na mafanikio makubwa tofauti na nilivyofikiria. Mpaka sasa tumepata naombi ya kumtaka Malkia Cecy kupamba majarida na pia kwenda kufanya maonesho Afrika ya kusini Marekani na Ufaransa,” kauli ile ilifanya ukumbi ulipuke kwa mayowe.
“Lakini hilo silo lililonifanya nimnyang’anye kipaza sauti Mc, nia yangu nilikuwa nimeweka ahadi moyoni mwangu siku ya leo nifanye kitu gani. Naomba nimwite malkia wa usiku wa leo Cecilia hapa mbele.”
Cecy alitoka chumba maalumu akiwa na gauni refu jekundu lililokuwa likiburuza kwa nyuma, lililokuwa limempendeza sana kama bi harusi.
“Ndugu zangu, wazazi wangu na wageni waalikwa katika onesho hili la kwanza la kimataifa. Leo ndiyo namtambulisha kwenu wakili wa moyo wangu binti mrembo Cecy kuwa ndiye mke wangu mtalajiwa,” ukumbi ulilipuka tena kwa mayowe.
Colin aliendelea kwa kujipapasa na kutoa mkebe mdogo na kusema:
“Cecy mpenzi fumba macho,” Cecy alifanya vile.
Colin alitoka pete ya tanzanite iliyochanganywa na almasi na kukishika kidole cha Cecy na kumvisha na kufanya ukumbi wote kulipuka kwa mayowe kila mtu akisema kuwa kila mmoja kampata mwenzake.
Lile lilikuwa pigo mujarabu kwa Mage aliyekuwa na ndoto za kurudi kwa Colin kama Hans atafungwa.
Mapigo ya moyo yalianza kumwenda mbio na jasho kumtoka kwa wingi, kizungumzungu kikali kilimshika na kiza kinene kilitanda mbele yake na kumfanya adondoke alipokuwa amekaa.
Alichukuliwa haraka kwenda kupewa huduma ya kwanza kwa vile pale ukumbuni kulikuwa na kila kitu.
Shughuli ilendelea kwa Mc kulitangaza vazi jipya la wachumba siku ya kuvishana pete lililompendeza vilivyo Cecy. Baada ya onesho yale Colin alijiandaa kuingia mkataba mnono wa Cecy na hayo makampuni.
***
Cecy aliingia mkataba wa mamilioni ya fedha ya miaka miwili kwa makampuni mawili ya majarida makubwa Marekani moja la Vibe na Ebony kwa ajili ya kupamba ukurasa wa mbele pia aliingia mkataba mnono wa kampuni ya maonesho ya mavazi ya Ufaransa ambayo yabadili maisha ya Cecy toka umaskini wa kutupa mpaka msichana bilionea.
Baada ya kuingia mkataba mnono uliomtaka aanze kazi hiyo mwezi mmoja baadaye kwa ajili ya mazoezi ya mwezi mmoja na kujifunza lugha vizuri kabla ya kuianza kazi hiyo mara moja. Cecy aliomba kuzungumza kwanza na familia yake pamoja na mpenzi wake Colin ili ajue ataanza lini kazi yake, walikubalia na kumpa siku mbili za kutoa jibu ili wakiondoka wajipange vipi.
Ilikuwa tofauti na mapokeo ya Cecy baada ya kulala maskini na kuamka tajiri mkubwa. Ndoto yake ilikuwa kuolewa na Colin na si kufanya kazi ya mabilioni, alijiuliza kukaa miaka mwili nje ya nchi lazima Colin atatafuta mwanamke mwingine na yeye kupoteza kitu muhimu maisha zaidi ya fedha atakazolipwa katika kazi yake.
Kwake alichokitafuta kilikuwa kuwa karibu na Colin na kufanikiwa kuwa naye karibu na kubakia kitu kimoja ndoa ambayo aliiota siku zote. Baada ya kuachana wa wenye makampuni toka nchini za nje. Cecy alionekana mtu mwenye mawazo tofauti na kitu alichokipata cha kugeuka bilionea kwa kufanya onesho lake moja na kuonekana.
Baada ya kufika nyumbani ilibidi amuulize:
“Vipi mpenzi wangu mbona kama hauna furaha wakati leo umeuaga umaskini?”
“Mi kwangu naona kama ndiyo unataka kuniongezea umaskini,” Cecy alijibu kinyonge.
“Kivipi?”
“Hivi nikiwa huko tutakuwa pamoja?”
“Hapana ila tutaonana mara chache kwa vile utakuwa bize na kazi yako ya kuizunguka dunia kufanya maonesho.”
“Uoni kama nitakuwa nimepata fedha zisizo na faida kwangu.”
“Kivipi?”
“Colin wewe ni kila kitu kwangu, niliapa kuwa mbali na wewe ni pale mmoja wetu akichukuliwa na umauti na si vinginevyo.”
“Hilo tu, nitakuwa naonana na wewe kila mara wala usihofu.”
“Colin nina wasiwasi nikiwa mbali kuna vipanga watu watakunyakuwa na mimi kuichukia dunia, kukupata nimetoka jasho la damu. Furaha yangu ni kuwa karibu yako na si kuingiza mamilio ya fedha.”
“Najua mpenzi unanipenda lakini hili dili ni zaidi ya mapenzi kwa vile litayabadilisha maisha yako sasa hivi una uwezo wa kujenga gharofa Masaki au Kunduchi.”
“Colin mimi huko siendi na hizo hela zao sizitaki.”
“Usifanye hivyo, ukilipoteza hutakuja kujuta maisha yako yote.”
“Moyo wangu naujua hauna shida ya mabilioni ya watu bali upendo toka kwako, pia naona umekwenda kinyume na makubaliano yetu.”
“Kivipi mpenzi?”
“Ulisema unataka kunifungulia kampuni ili niwe nafanya maonesho na si kwenda kufanya kazi nje ya nchi.”
“Mpenzi, yaani dili ulilopata fedha utakayoipata kwa miaka yote hiyo unaweza kukaa bila kufanya kazi na kuishi maisha ya juu.”
“Sina maana hiyo, uliniahidi baada ya kumaliza masomo unanioa sasa ahadi yetu ipo wapi? Au ndiyo unanitoa kijanja urudiane na Mage baada ya mpenzi wake kufungwa?” Cecy alilia wivu.
“Ahadi yetu ipo palepale, we fanya kazi mwaka mmoja kisha tunafunga ndoa ndipo nitajua nitafanya nini.”
“Cecy mpenzi hujui tu kiasi gani cha fedha utakacholipwa, ni wasichana wachache dunia wenye bahati hii. Tukitaka tufanye harusi itachukua muda wakati mwezi ujao unatakiwa Afrika ya Kusini kwa mazoezi ya wiki mbili kabla ya kwenda Ufaransa. Kutokana na makubaliano picha za jarida la Ebony watatumia za kwenye onesho na zile walizokupiga siku ile. Malipo yako ya kwanza yataingia mwezi ujao ya dola elfu mia mbili arobaini(408,000,000) kwa mwaka. Baada ya mwaka malipo yataongezeka na kuwa dola elfu mia tatu (510,000,000). Pia utapata bonas ya asilimia tano kutokana na mauzo huoni kwa miaka miwili utakuwa mbali mpenzi wangu kwa kutengeneza dola elfu mia tano arobaini (918,000,000).
Bado kampuni ya maonesho itakulipa dola elfu mia tatu (510,000,000) kwa mwaka na bonasi kila onesho la nchi kubwa barani Ulaya na Amerika. Unataka nini tena mpenzi wangu, kipindi hiki hebu ndoa iweke pembeni tupige pesa.”
“Colin nakuona kama unampigia mbuzi gitaa, nakueleza kwa mara ya mwisho pesa inaweza kununua kitu chochote chini ya jua lakini si furaha ya moyo wa mtu dawa ya mtu ni mtu si kitu.”
“Mmh! Sasa wewe ulikuiwa unatakaje?”
“Kwanza tuoane kisha tutajua kama kwenda au kufanyia kazi hapa lakini si kukaa mbali na wewe.”
Ulikuwa mtihani mzito kwa Colin kutokana na msimamno wa mpenzi na kuliona kama dili lile litapeperuka kwani walikuwa wapo wapo nchini wakisubiri kauli yao ataanza lini kufanya kazi. Lakini kwa Cecy alikuwa haelewi kitu bado ya kutetea ndoa yake pia kuwa karibu na mpenzi wake kwa kuogopa vibaka vya wapenzi wa watu.

Itaendelea
 
SEHEMU: 22
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500
ILIPOISHIA:
Ulikuwa mtihani mzito kwa Colin kutokana na msimamno wa mpenzi na kuliona kama dili lile litapeperuka kwani walikuwa wapo wapo nchini wakisubiri kauli yao ataanza lini kufanya kazi. Lakini kwa Cecy alikuwa haelewi kitu bado ya kutetea ndoa yake pia kuwa karibu na mpenzi wake kwa kuogopa vibaka vya wapenzi wa watu.
SASA ENDELEA...

Jioni ya siku ile Colin alikutana na mama Cecy na kumuelezea hatua waliyofikia na uamuzi wa Cecy.
“Mama nilikuwa naomba umweleze mwenzangu akubali kwanza kwenda kufanya kazi ndoa itafuata baadaye.”
“Mmh! Nitajaribu kumweleza, nina imani atanielewa.”
“Yaani nitashukuru sana, sijawahi kuona mwanamke mwenye msimamo kama Cecy.”
Kwa vile Cecy alikuwa amekwenda kuoga aliporudi alikaa pembeni ya mama yake na kumuacha Colin aliyekuwa amekaa kochi la peke yake. Baada ya ukimya mfupi mama Cecy aliuvunja ukimya ule.
“Cecy mama.”
“Abee mama.”
“Nina imani leo Mungu atuangazia maisha yetu?”
“Ni kweli mama, lakini maisha hayatakuwa na furaha bila kutimiza ndoto yangu.”
“Najua una hamu ya kutimiza ndoto yako, lakini kilichotokea ni muhimu kwa wakati huu ndoa yako ipo palepale.”
“Hilo nalijua, siku zote fimbo ya mbali haiuwi nyoka, kama nitaanza kazi naweza kukaa hata miezi mitatu bila kumuona Colin na wakati penzi langu limenitoa jasho la damu. Naweza kupata fedha lakini nikapata jeraha lisilopona mpaka nakufa na pengine likawa ndio sababu ya kifo changu.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Mama kama unavyojua mchumba wa Mage yupo ndani na kesi yake ni nzito, kwa habari za juujuu kweli anahusika katika vifo vya mkewe na mwanaye ili arudiane na Mage. Kwa hiyo uwezekano wa kutoka ni mdogo huoni muda huo nikiwa mbali na Colin penzi linaweza kuzaliwa upya na nafasi yangu kupotea.
“Kama nilijitoa kwa ajili ya Colin ifike wakati nimkose hizo fedha zitakuwa na faida gani kwangu. Nipo tayari kupoteza hata fedha zilizojaa bahari lakini si kumpoteza Colin, moyo wangu ndiyo unaojua thamani yake si yeyote. Mama hujui kiasi gani niliumia niliposikia Colin akioa lakini machozi yangu hayakwenda bure, Mungu alisikia kilio changu na kunirudishia mpenzi wangu mikononi mwangu na kuamini haki ya mtu huwa haipotei bali hucheleweshwa.”
“Sasa kama unafahamu hivyo kwa nini una wasiwasi na Mage?”
“Mama, Golden chance never came twise.”
“Hapo umeniacha feri una maanisha nini?”
“Kwangu hii ni nafasi ya dhahabu kamwe haijirudii mara mbili.”
“Cecy nakuahidi wewe ndiye mwanamke wa maisha yangu, nilivyofahamu thamani yako ndani ya moyo wangu upengo wangu uliongezeka mara dufu. Cecy wewe ndiye wakili wa moyo wangu uliyenitetea wakati wa matatizo hakuahidi sitamfungulia mwanamke mwingine moyo wangu nilipokufungia moyoni mwangu ufunguo niliutupa baharini,” Colin alimuhakikishia mapenzi yake ya dhati kwake.
“Colin ufunguo kuutupa baharini ni usemi tu lakini mnasahau ufunguo unaweza kumezwa na samaki na kuurudisha watu wakauokota na kuufunguo moyo wako na mimi ukanitoa moyoni mwako. Colin unanipenda?” Cecy alimuuliza Colin huku amemkazia macho.
“Zaidi ya sana na kama kuna kauli nyingine zaidi ya hiyo ungeijua ningeisema mbele yako.”
“Naomba unioe.”
“Nitakuoa kwa vile wewe ndiye mwanamke wa maisha yangu.”
“Si kwa wakati mnaotaka ninyi bali kabla ya kuanza kazi yangu nataka nikisimama sehemu nijulikane kama mrs Colin na si miss Cecy.”
“Muda tuliopewa ni mdogo sana wa maandalizi ya harusi, hivyo ungekwenda kufanya kwanza kazi kisha ukirudi tutafunga ndoa utakuta maandalizi tayari ukifika tunafunga ndoa na kuondoka.”
“Kwani kazi si naanza mwezi unaokuja huu muda hatuwezi kufunga ndoa?”
“Cecy wewe sasa si Cecy muuza ndizi bali wa kimataifa kwani wiki ijayo sura yako inaruka dunia nzima kwenye Jariba la Ebony harusi yako haitakiwi ya kulipua bali iendane na wewe mwenyewe.”
“Mimi Cecy hata niwe vipi bado nitabakia Cecy muuza ndizi, kwa hiyo kama mna nia nifanye kazi tufunge ndoa ya kawaida ila sherehe nikirudi zaidi ya hapo kazi yenyewe siitaki na msiambie kitu kinachohusu hiyo kazi. Fedha inatafutwa kwa njia yoyote lakini upendo kwa kweli ni adimu kama maji jangwani.
“Naweza kumsifu Mage kwa kuvunja uchumba wetu si kwanza nimepata nafasi bali amezieleza hisia zake za kweli toka moyoni kwake kuwa kuna mtu aliyekuwa akipenda kwa dhati. Kosa walilofanya kuua viumbe wasio na hatia lakini walikuwa wapo sahihi kabisa. Kama mliona Mage yupo radhi kulaaniwa na dunia kwa ajili ya mapenzi basi na mimi nipo tayari kufa maskini kwa ajili ya mapenzi,” Cecy alisema kwa sauti kavu isiyo na mzaha hata kidogo.
“Mmh! Mwanangu Colin mpaka hapo mimi sina neno siku zote mwenye kujua maumivu ya moyo ni mhusika, wengine ni washauri na mwisho wa siku ana uamuzi wa kukubali au kukataa anabakia nao mwenyewe na mwenzio amekataa,” mama Cecy hakuwa na kuongeza baada ya kauli ya mwanaye.
“Mama nimesikia yote nitayafanyia kazi, najua kabisa Cecy ananipenda na ameteseka juu yangu. Nimemuhakikishia yeye ndiye chaguo la moyo wangu na mwanamke wa maisha yangu kwa vile moyo wake imeingia wasiwasi basi nitafanya anavyotaka mpenzi wangu ili aamini mbegu yake ya upendo imemea kwangu na kuzaa matunda.”
“Hilo ndilo neno nililokuwa nikilisubiri usiku na mchana, najua hukupenda maamuzi yangu lakini utaamini siku moja kwa nini nimeharakisha harusi.”
Baada ya makubaliano ya kufunga ndoa kabla ya kwenda kuanza kazi, Colin alikwenda kwa mama yake kumweleza taarifa ya Cecy kupata mkataba mnono na kutakiwa kwenda kufanya kazi nje na alivyong’ang’ania kuolewa kuliko kufanya kazi. Alipofika nyumbani alimkuta mama yake amekaa sebuleni, alimsalimia na kukaa pembeni yake.
“Vipi baba, una jambo?” mama yake alimuuliza kwa vile alifahamu vizuri mwanaye.
“Ndiyo mama.”
“Ehe,” mama yake aliweka vitu vyake chini na kugeuka amsikilize vizuri mwanaye kwa vile kila kukicha alikuwa na jakamoyo. Hasa baada ya ndoa ya mwanaye na Mage kuvunjika katika hatua za mwisho.
Colin alimweleza mkataba alioingia Cecy na makampuni yote ambayo yalimuacha mama yake kinywa wazi kufikia hatua ya kusema.
“Yaani Cecy muuza ndizi alipwe mamilio ya fedha kwa kazi ya kupamba jarida na kuonesha mavazi huoni atakutana na watu wengi wenye fedha na wewe kumkuacha. Kwa nini umemtafutia kazi kama hiyo wakati shida yako ilikuwa awe mkeo kwa vile hatuna shida katika maisha yetu.”
“Mama, yote hayo tisa kuna kitu Cecy kanichanganya sana yaani mpaka kichwa kinaniuma,” Colin alisema kwa sauti ya unyonge.
“Kitu gani? Nilijua lazima uhusiano wenu utaingia dosari pesa atakazolipwa ni nyingi sana hasa akizingatiwa alikuwa hohehahe,” mama Colin alichangia bila kujua anataka kuambiwa nini.
“Sivyo unavyofikiria, mama Cecy anataka ndoa kabla ya kwenda kuanza kazi.”
“He! Si umesema mwezi ujao anatakiwa kuondoka?”
“Ndiyo, lakini yeye amesema bila ndoa na kazi hataki.”
“Mbona sikuelewi hataki kazi kwa ajili ya ndoa?”
“Ndiyo mama, anataka akiondoka hapa awe tayari mke wangu.”
“Kwa nini anafanya haraka hivyo, kwa nini asiende kwanza kisha arudi kufunga ndoa wakati huo maandalizi yatakuwa yamekamiliksa anaolewa na kuondoka.”
“Amekataa, amesema nikimlazimisha kwenda na kazi yenyewe hataki.”
“Kweli elimu ni muhimu. Yaani anataka kuyakataa mamilioni kwa ajili ya ndoa tu?” mama Colin alishangaa.
“Mama Cecy ni tofauti na wanawake wengi, mimi kwake ni kila kitu hasikii wala haoni anasema anaweza kuondoka huku nyuma Hans akafungwa hivyo naweza kurudiana na Mage na yeye kupoteza alichokitafuta muda mrefu. Yupo radhi kuendelea kuuza ndizi lakini si kunikosa mimi.”
“Mmh! Kazi ipo, sasa utafanyaje?”
“Nilikuwa naomba ushauri wako japo nilimkubalia kufunga naye ndoa kabla ya kuanza kazi.”
“Ninafikiri wazo lako zuri, japokuwa sikupenda harusi ya aina hiyo, lakini kwa vile naujua msimamo wa yule msichana sina budi kukubaliana nawe. Sijawahi kuona mwanamke msimamo mkali kama yule binti. Anajiamini katika kitu anachokitafuta hasa akiwa na haki nacho.”
Walikubaliana kufanya maandalizi ya harusi kwa kuandaa vikao vya wiki tatu, wiki ya nne inakuwa harusi.
***
Baada ya upelelezi wa kesi ya Hans kupanga njama za kifo cha mkewe na mwanaye kukamilika ilisomwa hukumu katika mahakama kuu. Siku hiyo walijaa watu pomoni kutaka kusikiliza nini kitakacho amuliwa juu ya tuhuma za Hans kumuua mkewe. Baada ya jaji kukaa kwenye kiti chake na watu wote kukaa chini alitulia kupanga kalatasi zake vizuri kisha alikohoa kidogo kuwafanya watu wote wakae tayari kumsikiliza wakiwemo Mage, mama yake shoga yake Brenda, familia nzima ya Hans pia alikuwepo mama Colin, Colin na mchumba wake Cecy.
Watu wote walitulia kumsikiliza jaji huku mioyo ikiwadunda wakiomba utokee muujiza utakao badili damu kuwa maji meupe. Kwa sauti yenye kusikika alisema:
Nina imani wote uliopo hapa mnajua tupo hapa kwa sababu gani, leo ndiyo siku tunayo hitimisha kesi inayomkabiri Hans Simgao ambaye anakabiriwa na kesi ya mauaji iliyochukua takribani mwezi mzima na leo ndiyo siku ya hukumu yake.
Kama kawaida kesi hii ilianza kusikiliza mahakama ya mwanzo ambayo haikuwa na uwezo wa kuhukumu na kuamuliwa kuletwa huku mahakama mkuu yenye uwezo wa kutoa hukumu kwa kesi yoyote nzito.
Baada ya hukumu kama mtuhumiwa hata ridhika na hukumu hii bado ana nafasi ya kwenda mbele zaidi kwenye mahakama ya rufaa.
Baada ya kusikiliza ushahidi wa pande zote za mashtaka na utetezi na mahakama kuridhika utetezi wa pande zote. Kutokana na maelezo upande mashtaka unaosema kuwa mtuhumiwa aliwatuma watu kumuua mkewe ili arudiane na mpenzi wake wa zamani ambaye wakati huo alikuwa kwenye maandalizi ya kuolewa na mwanaume mwingine.
Baada ya mashahidi wote waliopanda kizimbani akiwemo mchumba wa marehemu kutoa ushahidi wao ambao ulifanyiwa kazi na hatimaye kujiridhisha na ushahidi upande wa mashtaka ambao unatia hatiani moja kwa moja mtuhumiwa kwa hiyo mahakana inamuhukumu Hans Simgao kifungo cha maisha gerezani na kazi ngumu. Narudia tena kusema kuwa kama hamjalidhika na hukumu hii mna nafasi ya kukata rufaa mahakama ya rufaa,” hakimu alimaliza hukumu yake.
Hakimu baada ya kutoa hukumu ile iliamsha vilio mahakamani huku mama mzazi na Mage kuanguka chini na kupoteza fahamu. Ilibidi huduma ya kwanza ifanye kazi yake ya ziada kutoa huduma ya kwanza kutokana na watu wengi walipoteza fahamu baada ya hukumu nzito iliyompoteza Hans uraiani.
Baba yake hakukubaliana na huku ile na kuapa kukata rufaa kuhakikisha mwanaye anachiwa huku kwa vile makosa yalionekana ya kutengeneza lakini aliamini mwanaye hawezi kumuua mkewe kwa ajili ya mwanamke. Wakili aliyewekwa kutetea kesi ile aliomba nakala ya hukumu ili waweze kukata rufaa.
***
Mage alizinduka na kujikuta amelala kwenye kitanda cha hospitali akiongezwa maji, pembeni alikuwa mama yake na shoga yake Brenda. Alipowaona aliangua kilio upya huku akisema:
“Mama mkosi gani nimekosa Bara na Pwani, hivi nitaweka wapi uso wangu mbele ya jamii wakijua mimi ndiye niliyesababisha kifo cha mke wa Hans huku wengine wakiniona mimi ndiye sababu ya Hans kufungwa maisha.”
“Mage aliyoyafanya Hans hukumtuma kafanya kwa matakwa yake siamini kama angekushirikisha ungemkubalie afanye unyama kama ule. Ni heri angempa talaka kuliko alichokifanya,” alisema Brenda.
“Brenda naamini nuksi ndiyo nyota yangu haiwezekani Hans afungwe maisha Colin naye awe na mpenzi. Nina imani sina faida ya kuendelea kuishi.”
“Mage unataka kufanya nini?” Brenda alishtuka.
“Mwanangu hayo ni mawazo gani, Hans kufungwa si mwisho wa maisha bado una nafasi ya kuitafuta furaha,” mama yake alimtia moyo.
“Sasa mama hiyo furaha nitaipata wapi ikiwa hata aliyemweka kama spare tyre ana mwanamke mwingine ambaye ni mzuri kuliko mimi.”
“Brenda yote umeyataka mwenyewe ungenisikiliza sasa hivi ungekuwa kwa mumeo.”
“Mama sikubali nitalipiganie penzi la Colin kwa gharama yoyote.”
“Sasa Mage unataka kuchanganyikiwa, juzi tu Colin kamtangaza mchumba wake mbele za watu tena mtu maarufu utaanzia wapi?” Brenda alimuuliza.
“Kama mnataka niendelee kuishi naomba hili ninalotaka kuamua mniachie mimi mwenyewe zaidi ya hapo mtaokota mzoga wangu,” Mage alitoa vitisho.
“Lakini Mage wanaume wameisha? Mbona kuna wavulana wazuri kuliko huyo Colin na Hans?” Brenda alimuuliza.
“Ni kweli wapo wanaume wazuri lakini si kila mbegu humea kwenye udongo wowote. Mapenzi yangu kwa Hans na Colin ni kama mtende kwenye jangwa si rahisi mti mwingine kumea sehemu ile basi ndivyo mapenzi ya Hans na Colin walikuwa kama mapacha ndani ya moyo wangu.”
“Basi ndivyo hivyo mtaka pupa hadiliki kula tamu.”
“Jamani nimewaeleza naomba mniache ni uwamuzi wangu mtu atakayeingilia uamuzi wangu ajue ndiye atakayehusika na kifo changu.”
“Mmh! Fanya mchezo utakwenda kufunga ndoa na Hans gerezani,” mama Mage alitoa taadhari kwa mwanaye aliyetaka kuingilia mapenzi ya watu.
***
Kufungwa kwa Hans kuliongeza umakini kwa Cecy kuhakikisha kila kona aliyokuwepo Colin na yeye yupo huku moyo wake ukimpa tahadhari ya yeye kuwa mbali na Colin lazima kuna kitu kitatendeka. Wazo lake lilikuwa kuachana na kazi ya kufanya maonesho ya mavazi ili kumlinda mumewe na Mage msichana aliyebakia kama genda heka ambalo linaweza kuvamia mume wa mtu bila aibu.
Baada ya kutoka gym wakati wa kurudi nyumbani Cecy alionekana mtu mwenye mawazo mengi kitu kilichomfanya apoteze mchangamfu wake wa kawaida.
“Bebi.”
“Abee, Cecy alitikia huku akichukua chupa ya juisi.
“Vipi mazoezi ya leo yamekuchosha?” alimuuliza huku akimtazama.
“Hapana kawaida tu,” Cecy alimjibu bila kumtazama.
“Mbona huna uchangamfu wako wa kawaida.”
“Kuna kitu kinaniumiza kichwa nafikiria kubadili uamuzi.”
“He! Uamuzi tena mpenzi wangu?” Colin alishtuka kidogo agongane uso kwa uso na gari lililokuwa likija kwa mbele yao lakini alijitahidi kulirudisha sehemu yake.
“Ndiyo mpenzi kuna jinamizi linataka kuivamia furaha ya moyo wangu.”
“Jinamizi gani tena mpenzi wangu?” Colin aliipaki gari pembeni ya barabara ili amsikilize vizuri mpenzi wake.
“Colin naomba unisikilize vizuri.”
“Sawa mpenzi.”
“Nimeamua kuvunja mkataba wa kwenda kufanya maonyesho nje ya nchi.”
“He! Kwa nini jamani? Si nimekubali kufunga nawe ndoa ndipo uondoke,” Colin alishtuka.
“Hukumu ya Hans imeondoa kabisa amani ya moyo wangu.”
“Kivipi mpenzi?”
“Najua nikiondoka utarudiana na Mage.”
“Siwezi...siwezi mpenzi, yule ni matapishi sitayarudisha mdomoni mwangu.”
“Hapana Colin, yule mwanamke nikiondoka lazima atatumia hila za kike kukurudisha mikononi mwako na mimi kutoka kapa. Kwa hiyo mimi siendi popote wapigie simu waeleze nimevunja mkataba yote.”
“Mpenzi utafungwa, una hela za kuwalipa ili kuvunja mkataba?”
“Kwani kazi nimeanza?”
“Hakuna kitu kama hicho, ukitaka fanya hata mwaka mmoja ndipo uvunje.”
“Basi kama hivyo tutaondoka wote kwenda huko nitakapokuwa.”
“Sawa hakuna tatizo lakini usiache kazi.”
“Hapo tutaelewana kidogo na sitaki kumuona Mage kwenu wala kukupigia simu.”
“Yote yanatekelezeka mpenzi wangu.”
Kauli ya Colin ilirudisha furaha ya Cecy na kujikuta akitabasamu na kumnywesha juisi mpenzi wake aliyekuwa amezima gari kwa mshtuko. Aliwasha gari na safari ya kurudi nyumbani iliendelea. Wakiwa njiani simuya Colin iliita Cecy aliichukua na kuangalia na kukuta haina jina alimpa Colin.
“Mpenzi pokea simu.”
“Kapiga nani?”
“Haina jina.”
“Achana naye.”
“Hapana pokea hujui nani anakupigia.”
Colin aliichukua siku na kupokea:
“Haloo.”
“Ooh! Mpenzi wa maisha yangu, za toka jana mahakamani nina imani unajua kabisa sasa ndiyo nafasi yetu ya kufunga ndoa na kuwa mke na mume.”
“We! Nani?” Colin pamoja na kujua aliyepiga simu ni Mage alijifanya hamjui aliyepiga ili Cecy asijue kitu.
“Colin mpenzi kipi kilichokufanya usahau sauti ya malkia wa moyo wako au sababu ya hicho kinyago?”
“Jitambulishe au siyo nakata simu,” Colin alijifanya kuja juu.
Cecy alishtuka majibu ya mpenzi wake lakini alitulia amalize kuzungumza ndipo amuulize.
“Ni mimi Mage mwanamke pekee uliyeshushiwa na Mungu, amini kufungwa kwa Hans Mungu ametenda ili ile ndoa yetu ya ahadi itimie.”
“Umekosea namba,” Colin alisema huku akikata simu.
“Nani?” Cecy alimuuliza.
“Kuna mtu anaonekana amekosea namba.”
“Basi unakuta mtu anapiga simu na kuanza kutoa maagizo mengi bila kujua anazungumza na nani,” Cecy alimuunga mkono mpenzi wake.
“Umeona eeh, mpenzi nawe yamekukuta?”
“Mara chache.”
“Mara nyingi watu huwa wanachanganya namba badala ya sita wanaandika tisa basi akipiga inakwenda kwa mwingine,” Colin alizidi kuficha kilichopita.
Wakiwa katika ya mazungumzo ujumbe uliingia kwenye simu ya Colin, aliichukua simu haraka kwa kuamini unatoka kwa Mage. Kabla hajafungua upande wa ujumbe Cecy alidaka na kusema:
“Nipo kwa ajili yako nitasoma na kukueleza kimeandikwa nini.”
Colin alipoangalia namba ya ujumbe ule ilikuwa iliyopigwa muda mfupi na Mage, alijikuta njia panda kumuachia simu Cecy asome ujumbe ule ambao aliamini si mzuri kusomwa naye. Lakini hakuwa na jinsi huku akiomba usiwe ujumbe mbaya ambao utamchanganya mpenzi wake na kulizua jipya pengine kukataa hata kazi yenyewe..
Cecy alichukua simu na kufungua upande wa ujumbe na kuanza kusoma, ghafla macho yalimtoka pima na mapigo ya moyo yalianza kumwenda mbio huku jasho likitanda kwenye maji la uso.
Ujumbe ulikuwa umeandikwa:
Colin wewe ndiye mpenzi wangu wa maisha, kumbuka ahadi yetu tuliyoahidiana kuwa mume na mke ipo palepale. Huu ndiyo wakati wangu hicho kinyago chako hakina nafasi mimi na wewe tunajulikana kwa wazazi wetu na mbele ya Mungu. Colin nakupenda zaidi ya kupenda, kufungwa kwa Hans Mungu ametenda ili ahadi yetu itimie. Mimi ndiye mkeo uliyechangulia na Mungu. I love you my husband to be Colin forever and ever mmmmwaaa.
Colin aliyekuwa akifuatilia uso wa Cecy alishtuka kuona macho ya Cecy yakikodolewa pima kisha kuanza kutoka machozi, alijua kimenuka, kwa mchecheto bila kujielewa kama yupo barabarani gari lilihama njia na kwenda kujingonga kwenye nguzo ya umeme na kufanya utokee mlipuko mkubwa baada ya waya za umeme kugusana.

Itaendelea
 
SEHEMU: 23
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500

ILIPOISHIA:
Gari alilokuwa akiendesha Colin liliendelea kuteketea na hatimaye lilishika moto lote kutokana na kukosa msaada wa kuzimwa kutokana na miundo mbinu mibovu na kuteketeza kila kilichokuwepo pamoja na simu zote za Colin na Cecy.
SASA ENDELEA...

Msichana mmoja shoga wa Brenda rafiki wa Mage ambaye alikuwa akimfahamu Colin kutokana na kuwepo siku Colin alipomvisha pete Mage. Alikuwepo kwenye ajali ile kutokana na kutemka kwenye daladala na kukuta watu wakitolewa kwenye gari lililokuwa likiwaka moto.
Kwa vile hakuijua namba ya simu ya mama Colin aliamua kumpigia simu Brenda amweleze Mage ili ampigie mama Colin kumjulisha ajali ile. Baada ya kupigiwa simu Brenda alipokea upande wa pili:
“Haloo Loveness, niambie shoga!”
“Aisee kuna tatizo,” alisema kwa sauti iliyojaa wasiwasi.
“Mbona unanitisha kuna nini?” Brenda alishtuka.
“Colin kapata ajali mbaya sana.”
“Colin! Yupi?”
“Aliyekuwa mchumba wa Mage.”
“Wewe! Ajali ya nini tena Mungu wangu?”
“Gari alililokuwa akiendesha nimepata ajali mbaya barabara ya Sam Nujoma jirani na Mlimani City kwa kugonga nguzo ya umeme.”
“Mungu wangu, vipi hali yake?”
“Mmh! Kwa kweli kuna taarifa nyingi japo si rasmi.”
“Mungu wangu nisaidie mja wako, taarifa gani tena Love?”
“Wapo wanaosema wamekufa papohapo.”
“Jamaniii! Kwani alikuwa na nani?”
“Na msichana mmoja ambaye anaonekana alikuwa na nguo za mazoezi.”
“He! Yaani nimechoka, siamini kama Colin amekufa kirahisi namna hiyo.”
“Sasa shoga nina imani Mage ana namba ya mama yake, mpigie ili awajulishe nina imani hawana taarifa.”
“Poa, lakini siamini mpaka niuone mwili wa Colin kwenye jeneza.”
Brenda akiwa amechanganyikiwa alimpigia simu Mage aliyekuwa amekaa kwao huku akichezea simu yake. Baada ya kumtumia ujumbe Colin alipiga simu ambayo iliita bila kupokelewa na mwisho ilizimwa kabisa.
Baada ya kuzimwa alijikuta akijiapiza:
“Lazima nimpate Colin kwa hiyari kwa nguvu, nitahakikisha nampoteza kinyago wake ili niipate nafasi yangu bila hiyo sina maisha heri ninywe sumu.”
Akiwa katikati ya mawazo simu yake iliita, wazo lake alijua Colin alikuwa akitafuta sehemu nzuri ili ampigie. Alipoangalia alikuta inatoka kwa shoga yake Brenda, aliipokea.
“Niambie shoga.”
“Mage kuna taarifa siyo nzuri.”
“Taarifa gani?”
“Zinamhusu zilipendwa wako.”
“Nani, Hans?”
“Hapana, Colin.”
“He! Colin kakupigia simu?”
“Siyo kunipigia simu bali kapata ajali mbaya.”
“Acha utani, acha kunirusha roho unione kama nampenda, sio siri Colin ndiye aliyebeba uhai wangu.”
“Mage hebu tuliza akili unisilize.”
“Haya niambie mpenzi.”
“Colin amepata ajali mbaya barabara ya Sam Nujoma jirani na Mlimani City na haijulikani kama mzima au amekufa.”
“Brenda sipendi utani wa kujinga, nimetoka kuzungumza na Colin hata robo saa haijapita.”
“Sasa wewe fanya utani naomba umpigie simu mama yake sasa hivi, mweleze Colin amepata ajali na amekimbizwa Muhimbili. Naomba usiongeze lingine usije muua mama wa watu kwa mshtuko. Najua anampenda sana mwanaye ndiye kama mboni ya macho yake.”
“Japo siamini nitampigia tu.”
“Fanya haraka, unaambiwa hata gari alilokuwa akiendesha limeteketea lote.”
“Mungu wangu ! Brenda unasema kweli?” Mage aliuliza kwa sauti ya kilio.
“Kweli, siwezi kukutania kwa jambo zito kama hili.”
“Mungu wangu hii nuksi gani? Kama Colin akifa nitakuwa na faida gani ya kuendelea kuishi,” Mage alizungumza peke yake huku macho yamejaa machozi na mikono kumtetemeka wakati wa kutafuta namba ya mama Colin.
Kila alivyokuwa akilitafuta machozi yalizidi kuyafunika macho yake hata alipoyafuta kwa mkono yalijaa tena. Alitoka chumbani na simu mkononi hadi sebuleni na kumkuta mama yake.
“Mage nini?” mama yake alishtuka na hali ya mwanaye.
“Colin, mama,” alisema huku akilia na kumpa simu mama yake.
“Colin! Kafanya nini?”
“Ajali.”
“He! Lini?”
“Sasa hivi.”
“Taarifa umezitoa wapi?”
“Kanipigia Brenda sasa hivi?”
“Dah! Vipi hali yake.”
“Na..na..sikia a..a..meku..”
“Wewe mtoto ushia hapohapo,” mama Mage alimkata kauli mwanaye hakutaka kulisikia neno la mwisho kwa vile aliamini litamuumiza moyo wake.
“Mama mpigie simu mama yake hana habari.”
“Mmh!”
Mama Mage alichukua simu yake kutafuta namba ya mama Colin huku naye mikono ikimtetemeka. Baada ya kuipata alipiga simu ambayo ilipokelewa upande upande wa pili.
“Haloo dada vipi?”
“Kwema, una habari gani?”
“Za nini?”
“Kuhusu Colin.”
“Mmh! Sina habari zozote.”
“Kuna taarifa kapata ajali.”
“Ajali!?” mama Colin alishtuka.
“Eeh, ndiyo, kuna mtu kampigia simu Mage na kutaka tukujulishe kwa vile hakuwa na namba yako ya simu.”
“Mungu wangu wee, yupo katika hali gani?”
“Hebu subiri,” alisema na kuziba sehemu ya kuzungumzia na kumgeukia Mage.
“Eti Mage mwili wa Colin umepelekwa hospitali gani?”
“Mama sijasema amekufa ila watu wanafikiria hivyo,” Mage alimgeuka mama yake.
“Sasa kapelekwa wapi?”
“Mama mwambie amekimbizwa muhimbili, ila usimwambie yupo kwenye hali gani mengine atayajua hukohuko mwenyewe. ” Baada ya kuzungumza na mwanaye aliachia sehemu ya kuzungumzia na kuzungumza na mama Colin.
“Anasema baada ya ajali wasamalia wema wamewapeleka Muhimbili.”
“Wanasema hali yake ipo vipi?”
“Hawajajua kwa vile amebebwa na kuingizwa kwenye gari na kuwahishwa hospitali.”
“Na..na.. Cecy?”
“Sijajua hebu subiri...Eti Cecy alikuwepo? Alimuuliza mwanaye.
“Ndiyo.”
‘Ndiyo walikuwa pamoja.”
“Na..nashukuru dada.”
“Nami nakuja huko.”
“Sawa tutakutana.”
Baada ya kukata mama Mage alinyanyuka kuelekea chumbani kuchukua funguo ya gari, baada ya kuchukua alitoka nje na Mage alitoka kumfuata mama yake waliingia kwenye gari na kutoka kuelekea Muhimbili. Muda wote Mage alikuwa akilia kitu kilichomfanya mama yake kuingilia kati.
“Unasema hajafa unalia nini mbona unamchulia mwenzio.”
“Mama inauma Colin ndiye lilikuwa tumaini langu mwisho.”
“Muombee basi apone.”
“Yaani Mungu asikie dua langu, Colin apone lakini mchumba wake afe.”
“Wee mtoto roho gani hiyo?”
“Mama wakipona wote sina changu.”
“Hebu achana na mawazo hayo,” mama Mage alisema huku kanyaga mafuta kuwahi hospitali.
Mama Colin baada ya kuzipata taarifa zile alimpitia mama Cecy aliyekuwa hana taarifa zozote kwa kujua mwanaye alikwenda mazoezi asubuhi na mpenzi wake. Naye alishtuka lakini mama Colin alimpa moyo wafike hospitali ili wajue kipi kinaendelea japokuwa hakujua watoto wao wapo kwenye hali gani.
Walijikuta wakifika pamoja na Mage na mama yake, waliongozana wote mapokezi kuulizia taarifa za wagonjwa wao. Waliambiwa wote wamekimbizwa chumba cha wagonjwa mahututi kwa vile hali zao si nzuri. Walikwenda kuonana na mganga mkuu, aliwakaribisha ofisini kwake.
“Ndiyo wazazi wangu kwanza poleni sana.”
“Mmh! Hatujapoa kwani hatujui hali za watoto wetu,” alijibu mama Colin.
Dokta Bukos kwanza alitulia kama anasoma taarifa kwenye kalatasi kutafuta neno la kuwaeleza ili wasipagawe kutokana na hali za wagonjwa wao. Baada ya kutulia kwa muda alinyanyua uso wake na kusema kwa sauti ya upole.
“Wazazi wangu hali za wagonjwa si mbaya wala nzuri sana lakini bado tunapigania maisha yao.”
“Lakini baba mtu mpaka kuletwa chumba cha wagonjwa mahututi lazima hali yake ni mbaya sana?” aliuliza mama Colin.
“Ni kweli, chumba hicho ni kwa ajili ya uangalizi wa karibu kwa mgojwa.”
“Kwani hali zao zikoje?” aliuliza mama Cecy.
“Bado kwa vile wameletwa hawajitambui hivyo kwanza tunashughulika na suala la kurudisha ufahamu kisha tutajua tufanye kitu gani.”
“Mbona nilisikia wamekufa?” Mage aliropoka.
“Si kweli, kama wangekuwa wamekufa wodini tumewapeleka kufanya nini?” daktari alijibu kwa ukali kidogo.
“Wee Mage acha kuropoka,” mama yake alimkanya.
“Jamani naomba kuzungumza na wahusika wa wagonjwa wengine msubiri nje,” daktari alisema.
Mage na mama yake walitoka nje na kubakia mama Colin na Cecy, baada ya kubakia wawili dokta alitaka kujua uhusiano ya waliobakia na wagonjwa. Wote walijitambulisha.
“Basi wazazi wangu ajali waliyopata ilikuwa mbaya sana, majeraha si makubwa sana lakini inaonesha wamejigonga kwenye kitu kigumu wakati gari likipata ajali hivyo kusababisha mtikisiko wa ubongo uliopelekea kupoteza fahamu. Lakini tunahangaika ili kurudisha fahamu zao.”

Itaendelea
 
SEHEMU: 24
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500
...
ILIPOISHIA:
“Basi wazazi wangu ajali waliyopata ilikuwa mbaya sana, majeraha si makubwa sana lakini inaonesha wamejigonga kwenye kitu kigumu wakati gari likipata ajali hivyo kusababisha mtikisiko wa ubongo uliopelekea kupoteza fahamu. Lakini tunahangaika ili kurudisha fahamu zao.”
SASA ENDELEA...

“Zitachukua muda gani kurudi?” mama Cecy aliuliza.
“Hatuwezi kujua ubongo umecheza kiasi gani, lakini msiwe na wasiwasi hii ni hali ya kawaida kwenye ajali za namna hii,” dokta aliwapa moyo.
“Tunaweza kwenda kuwaona?” aliuliza mama Cecy.
“Kwa leo bado kuna baadhi ya mambo tunashughulika nayo kuanzia kesho mna nafasi ya kuja kuwaona.”
“Sawa.”
Mama Colin na mama Cecy walitoka ofisini kwa mganga mkuu na kukutana na Mage na mama yake wakiwasubiri, walipotoka waliwauliza.
“Vipi wanasemaje?” Mage alikuwa wa kwanza kuuliza.
“Bado wapo chini ya uangalizi maalumu,” alijibu mama Colin.
“Hatuwezi kuwaona?” mama Mage aliuliza.
“Kwa leo haiwezekani.”
“Mmh! Basi watakuwa wana hali mbaya sana,” Mage alisema.
“Anayejua ni dokta, sisi hatujui kwa vile hatujawaona,” alijibu mama Colin ambaye alionesha kuchoshwa na maswali ya Mage.
“Jamani hatuna cha kufanya maombi yetu yote yawe kwa watoto wetu ili Mungu awaepushe na matatizo yaliyo mbele yao,” alisema mama Mage.
“Ni kweli dada yangu,” alisema mama Cecy ambaye muda wote alikuwa kimya kutokana na mshtuko alioupaka kwa ajali ya watoto wao.
Walikubaliana kurudi nyumbani mpaka kesho ambayo wangerudi kuwaona, mama Mage aliwashauri wote waongozane nyumbani kwa mama Colin kufanya maombi ya pamoja ili Mungu awaepushe na matatizo yale. Waliongozana wote hadi nyumbani kwa mama Colin ambako walifanya maombi ya pamoja yaliyoongozwa na mama Mage.
Walipiga magoti na kushikana mikono kisha mama Mage alishusha maombi.
“Baba Mungu tumepiga magoti mbele yako tunajua hakuna chochote chini na juu ya jua kiwezacho kufanyika bali kwa idhini yako. Baba Mungu lisilowezekana kwa mwanadamu kwake linawezekana, lililo zito kwa mwadamu wako ni jepesi. Eeh, Baba tunaomba uwaepushe watoto wetu na matatizo mazito kama ulivyoweza kumuepusha mwanao mpendwa pale msalabani.
Kama ulivyoweza kumponya Ayubu na maradhi ya ajabu ambayo alipona kupitia kwa uweza wako. Baba Mungu unaweza kumponya aliye mahututi unaweza kumfufua aliyekufa kwako wewe hakuna kinachoshindikana baba waponye wenetu ambao hatujui hali zao ni wewe pekee mwenye kuugeuza usiku ukawa mchana basi yaondoe maradhi miilini mwao wape afya njema.
Baba vunja pepo wa maumivu vunja pepo wa mauti vunja pepo wa maradhi kwa jina la mwanao Yesu Kristo aliyehai Amen.”
“Ameni,” waliitikia pamoja.
Baada ya maombi walinyanyuka na kukaa kwenye makochi, kwa vile hawakuwa na la kuzungumza mpaka siku ya pili watakapokwenda kuwaona wagonjwa wao. Mama Mage na mwanaye waliaga na kuondoka kurudi nyumbani na kuwaacha mama Colin na Cecy wakiwa wamekaa kila mmoja akiwaza lake.
***
Siku ya pili alfajiri walikutana wote hospitali ya Muhimbili , kwa vile daktari alikuwa hajafika ilibidi wamsubiri mpaka saa moja asubuhi alipofika, alipowaona aliwaeleza wasubiri ili afike wodini kwanza. Dokta Bukos baada ya kuwazungukia wagonjwa wote na kuchukuwa taarifa kutoka kwa daktari wa zamu aliwafuata kwenda kuwaona wagonjwa wao.
Waliingia mmojammoja kutokana na taratibu za kuingia chumba cha wagonjwa mahututi (ICU). Colin alikuwa akipumulia mashine akiwa amelala bila kutikisika. Lakini dokta Bukos aliwaeleza kuwa kidogo ameanza kupata fahamu kwa misuli ya mwili kuanza kufanya kazi taratibu japo hakuonesha mabadiliko yoyote zaidi ya kulala vilevile walivyomkuta.
Katika chumba kingine Cecy naye alikuwa vilevile amejilaza akitumia mashine kupumua, yeye alionekana ufahamu bado kabisa japokuwa mapigo ya moyo dokta alisema yapo mbali sana. Lakini aliwaomba wazidishe kumuomba Mungu na si kulia.
WIKI MOJA BAADAYE
Baada ya wiki moja hali ya Colin ilimalika kidogo kwa kuweza kutambua watu japo bado alikuwa hawezi kuzungumza kwa haraka kwa kutafuta maneno. Cecy hali yake ilikuwa bado mbaya pamoja na mwili kuanza kurudisha hisia bado alikuwa akiendelea kutumia mashine za kumsaidia kupumua.
Walijikuta katika wakati mgumu baada ya hali ya Cecy kuonekana kuchelewa kuimalika. Mganga mkuu aliomba kama wana uwezo basi Cecy apelekwe India kwa ajili ya matubabu zaidi baada ya kuamini uwezo wa madaktari wa Tanzania uliishia pale kuweza kuuamsha mwili lakini hali ilikuwa bado tofauti na Colin ambaye aliweza kula hata kufanyishwa mazoezi japokuwa alikuwa akizungumza kwa shida.
Madaktari waliwahakikisha ndani ya wiki nyingine hali itaimalika zaidi na kuweza kuanza mazoezi ya peke yake. Fedha iliyokuwa ikitakiwa kwa ajili ya matibabu na nauri ya Cecy na msaidizi wake ilikuwa kubwa ambayo mama Cecy hakuwa nayo. Kwa hali ya mgonjwa ilivyokuwa ikionekana mama Colin aliamini kabisa Cecy hawezi kupona hivyo kutoa kiasi hicho cha fedha ni sawa na kuzitupa.
Mama Cecy alikuwa radhi kuuza nyumba ili tu mwanaye akatibiwe, lakini mama Colin alimshauri asisumbuke kwa vile wagonjwa wa aina ile huwa hawaponi heri asiipoteze nyumba kwani Cecy akifa atakuwa na sehemu ya kukaa.
Mama Cecy alikuwa radhi kulala nje lakini ajue hatima ya hali ya mwanaye, ili kujitoa kwenye lawama alichangia milioni tano katika milioni ishrini na tano zilizotakiwa. Mama Cecy alitafuta dalali wa kuiuza nyumba kwa bei ya kutupa ili tu mwanaye akatibiwe India kama kufa basi afe akijua alikuwa akipigania maisha yake.
Wiki ile ndiyo ilikuwa wiki ya malipo ya Cecy kutoka katika kampuni ya jarida la Ebony ambayo iliijngiza kwenye akaunti ya Cecy pia walifunga safari mpaka Tanzania kuonana na Cecy kwa ajili ya kumpiga picha zingine kwa ajili ya matoleo mengine. Jarida lililotoka na picha ya Cecy ilivunja rekodi ya mauzo ya kampuni ile toka ianzishwe.
Uongozi wa kampuni ile ulipanga kumpa mkataba mnono wa muda mrefu zaidi pia kumfunga asitumike kwenye majarida mengine. Walipofika walitaka kuonana na meneja wake ambaye ni mchumba wake Colin mmiliki wa kampuni ya Urembo. Taarifa walizopata ziliwashtuka kusikia Cecy na mchumba wake walipata ajali mbaya sana. Walikwenda mpaka hospitali na kuwaona wagonjwa.
Colin alionekana hajambo lakini Cecy bado hali yake ilikuwa tata, walionana na mganga mkuu na kutaka kujua nini hatma ya mgonjwa kwa siku alizokaa hospitali. Aliwaeleza hatua walizochukua tokea mwanzo kwa wagonjwa wote na kufanikiwa kwa mmoja na sehemu walipokwama na kuhitaji msaada wa matibabu zaidi nje ya nchi.
Waliulizia kama kuna uwezekana wa mgonjwa kupona, walijibu upo wa hamsini kwa hamsini. Waliuliza gharama ya matibabu yote walielezwa milioni ishirini na tano kwa awali kama itazidi watajulishwa kwa vile mgonjwa hakuwa wa kutoka mapema. Walikubali kugharamia matibabu ya Cecy mpaka hatua ya mwisho. Baada ya makubaliano zilifanywa taratibu zote za kumsafirisha mgonjwa na mtu wake wa karibu.
Siku ya tatu Cecy alisafirishwa pamoja na mama yake kwenda India kwa matibabu ambayo wengi waliamini madaktari wa Tanzania waliona aibu kusema ukweli kuwa Cecy ameisha kufa anachosubiri kupoa tu. Baada ya safari ya angani Cecy alitua katika jiji la Mumbay na kupelekwa katika hospitali ya Apolo.
Alipokelewa mara moja alianza kupatiwa matibabu kwa kuchukuliwa vipimo vyote ili kuangalia tatizo lipo wapi. Baada kurudi majibu ya vipimo ilionesha Cecy atapona lakini itachukua muda kurudi katika hali ya kawaida kutokana na kupoteza kumbukumbu na ubongo wake kucheza kidogo, lakini alikuwa na bahari nzuri ubongo haukuvia damu.
TANZANIA
Hali ya Colin iliendelea vizuri kwa kuimalika kwa kasi kubwa tofauti na walivyotegemea. Baada ya wiki aliweza kuzungumza vizuri na kuanza kumkumbuka mpenzi wake Cecy. Wakiwa wamekaa kitandani Colin alimuuliza mama yake.
“Mama mbona simuoni Cecy wala mama yake leo siku ya tatu?”
“Cecy alisafiri walifiwa na bibi yao kabla hujapata ajali.”
“Mama ina maana nilipata ajali peke yangu?”
Swali lile lilimchanganya sana mama yake aliyeamini mwanaye baada ya ajali alipoteza kumbukumbu na hakutaka kumshtua kutokana na hali na mchumba wake ambaye aliamini aliondoka mfu kwa asilimia tisini na tano.
“Kwani unakumbuka nini?”
“Unajua mama nakumbuka wakati napata ajali nilikuwa na Cecy tukitoka mazoezini na sababu ya ajali ni Mage.”
“Mage?” mama yake alishtuka.
“Ndiyo mama.”
“Mage kasababisha kivipi?”
Colin alimweleza tukio zima la ajali ilivyotokea mpaka kupata ajali, baada ya kumsikiliza aliguna na kusema:
“Kwani Mage aliandika ujumbe gani?”
“Kwa kweli sikuuona bali usomaji wa Cecy ulionesha ujumbe siyo mzuri.”
“Sasa wewe nini kilikupelekea kupata ajali.”
“Mama baada ya kumwangalia Cecy usoni moyo ulishtuka na kujua hakuna tena usalama kwa vile aliisha mshutumu Mage mapema baada ya hukumu ya mchumba wake kabla ya simu na kutishia kusitisha mkataba. Mage alinipigia simu na kuzungumza maneno ambayo ni uchokonozi kwa vile anajua kabisa nipo na nani.”
“Inaonekana alikuacha bado anakupenda ulikuwa una hiyari kukubali au kukataa au hata kumfanya spea taili.”
“Mama Cecy ni kila kitu kwangu ndiye mwanamke wa pekee moyoni mwangu sina nafasi nyingine.”
“Lakini ulitakiwa kujua ameandika ujumbe gani kabla ya kupagawa na kusababisha ajali mbaya.”
“Kwani gari limeharibika sana?”
“Limeungua lote na moto.”
“Mungu wangu na..na Cecy?”
“Naye alipata majeraha kama yako.”
“Yupo hapa hospitali?”
“Hapana yeye inaonekana alipata matatizo makubwa na kukimbizwa India.”
“Maskini mpenzi wangu,” Colin alishika kichwa kwa mshtuko.
“Lakini taarifa zinasema anaendelea vizuri,” mama yake alimpa moyo.
“Hospitali natoka lini?”
“Wiki hii lakini utatakiwa kuja kila siku asubuhi kufanya mazoezi ya viungo ili kuurudisha mwili katika hali ya kawaida.”
“Nikijisikia vizuri kidogo nakwenda India kumwona mpenzi wangu.”
“Hakuna tatizo tutakwenda wote,” mama Colin alimkubalia mwanaye kumpa moyo lakini aliamini kabisa Cecy hakuna kitu siku zake zilikuwa zikihesabika walichosubiri taarifa za msiba wake.

Itaendelea
 
SEHEMU: 25
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500

ILIPOISHIA:
“Wiki hii lakini utatakiwa kuja kila siku asubuhi kufanya mazoezi ya viungo ili kuurudisha mwili katika hali ya kawaida.”
“Nikijisikia vizuri kidogo nakwenda India kumwona mpenzi wangu.”
“Hakuna tatizo tutakwenda wote,” mama Colin alimkubalia mwanaye kumpa moyo lakini aliamini kabisa Cecy hakuna kitu siku zake zilikuwa zikihesabika walichosubiri taarifa za msiba wake.
SASA ENDELEA...
***
Mama Mage na mwanaye walikuwa wakizungumza kuhusiana na hali ya Colin na mchumba wake.
“Mama unafikiri mchumba wa Colin anaweza kupona?”
“Mmh! Kwa kweli ni Mungu tu mwenye uwezo wa kumponya, taarifa nilizopata kutoka kwenye hospitali aliyokuwa anatibiwa kupona ni asilimia ndogo na hata akipona bado hata kuwa sawa.”
“Kwa hiyo mama nina imani hii ni nafasi yangu ya kurudi kwa Colin?”
“Ni nafasi yako kama ukiifanyia kazi bila hivyo itakupita huku unaiona.”
“Sasa mama niifanyie kazi ipi au niende wa Karumanzila?”
“Si kwenda kwa Karumanzila bali kujipendekeza muda huu wa matatizo kuonesha unamjali sana Colin kwa kwenda asubuhi unarudi usiku ikiwezekana ulale hukohuko.”
“Mama tena naondoka muda huu.”
“Mwanangu kijua ndicho hiki lazima uuanike sasa, huenda Mungu alikuwa na kusudio lake la kuirudisha ndoa yetu iliyoyeyuka kwa kifungo cha Hans na kufa kwa Cecy.”
“Umeona eeh, mama utakuwa nabii kwa kuiona hilo, japo siwezi kufurahi kwa matatizo ya Cecy lakini kila kitu hupangwa na Mungu.”
“Halafu nimeambiwa Colin atatakiwa kila siku asubuhi apelekwe hospitali kwa mazoezi, nataka kazi hiyo uifanye wewe tena utachukua gari la kifahari la kumpelekea hospitali.”
“Mama hilo si la kusema mbona kikohozi kimepata mkohoaji nitahakikisha mahaba ninayo mpa anamsahau marehemu wake(Cecy).”
Baada ya mazungumzo Mage alimuaga mama yake kwenda kumwona Colin nyumbani kwao ili aurudishe ukaribu wao kutokana na matatizo ya mchumba wake Cecy. Mage maombi yake alitaka Cecy afie India, Tanzania urudi mwili tu usio na uhai, aliendesha gari hadi nyumbani.
Mama Colin alimpokea Mage aliyejionesha mwenye huzuni kutokana ugonjwa Colin.
“Karibu mkwe.”
“Asante mama, mume wangu anaendeleaje?”
“Mmh! Kiasi hajambo vipi nyumbani hamjambo.”
“Hatujambo kiasi.”
“Kuna anayeumwa?”
“Hapana ila huwezi kuamini toka Colin apate matatizo nimekuwa sili wala silali vizuri utafikiri naumwa mimi.”
“Pole, la muhimu kumuomba atapona tu.”
“Mama maombi yangu yote kila dakika ni kwa Colin.”
“Mama yako hajambo?”
“Hajambo, mume wangu yupo wapi?” Mage alijifanya ana shauku ya kumuona Colin.
“Yupo chumbani kwake amepumzika.”
Kwa vile chumba cha Colin alikuwa akikijua alikwenda moja kwa moja na kuingia ndani bila hodi. Alimkuta amesinzia aliinama na kumpiga busu la shavu lililomfanya Colin afumbue macho. Alishtuka kukutana na Mage aliyekuwa amemchanulia tabasamu pana amesimama pembeni ya kitanda.
“Colin mpenzi wangu pole sana,” Mage alisema huku akikaa kitandani, lakini Colin hakumjibu alikuwa kama anamshangaa.
“Vipi inaendeleaje mpenzi?” alimuuliza tena.
“Mage unatafuta nini hapa?” Colin alimuuliza akiwa amemkunjia uso.
“Colin mpenzi wangu maswali gani hayo wakati unajua wewe ni mgonjwa?”
“Hata kama mgonjwa sikukuita uje unione labda ungekuja kuona jeneza langu na si mwili wangu.”
“Kwa nini unasema hivyo mpenzi wangu?” majibu la Colin yalimshtua Mage.
“Kwanza naomba jina la mpenzi lifutike mdomoni na moyoni mpenzi wako, mpenzi wangu ni mmoja tu Cecy.”
“Kumbuka kabla ya Cecy nilikuwepo miye.”
“Kuna mtu aliye mpenzi wa moyo wako si mwingine bali Hans si Colin.”
“Colin, Hans amefungwa si mpenzi wangu mwenye nafasi hiyo ulibakia wewe peke yako.”
“Mimi ulinipenda lakini Hans ulimpenda zaidi kwa hiyo ndiye chaguo sahihi la moyo wako si mimi. Nami wewe nilikupenda lakini Cecy nilimpenda zaidi naye ndiye aliyenipenda kuliko kiumbe chochote kilichopo chini ya jua. Malaika sijawaona nina amini hata wao ningewaona wasingeuzidi uzuri wa Cecy.”
“Wewe Colin acha kukufuru Cecy ana uzuri gani kumshinda malaika?”
“Malaika uliisha muona?”
“Sijamuona lakini nasikia mzuri sana.”
“Basi uzuri wao haufiki kwa Cecy, kwa vile ulichokitaka kimefanikiwa naomba uachane na mimi.”
“Colin nimefanya nini?” Mage aliuliza huku akilia.
“Unajua umeniumiza mara ya kwanza hukutosheka umeniumiza kwa mara ya pili bado hujaridhika naona kimebakia roho yangu tu.”
“Colin usiseme hivyo unaniumiza?”
“Ulitaka tufe sote lakini nakuhakikishia Cecy atapona na atarudi tufunge ndoa hata kama Cecy atakufa nitafunga ndoa na maiti ya Cecy si mwanamke mwingine.”
“Colin usiseme hivyo, Cecy akifariki siyo mwisho wa dunia maisha yataendelea, nina imani hakutakuwa na mwanamke mwingine atakayechukua nafasi ya Cecy bali mimi.”
“Ninacho kisema hakitafutika moyoni mwangu Cecy ndiye mwanamke wangu wa maisha nawe msubiri Hans mfunge ndoa au nenda mkafungie ndoa gerezani.”
“Kwa nini Colin unanichukia hivyo?”
“Sitakusamehe mpaka nakufa naomba utoke nje,” Colin alisema kwa sauti ya juu.
“Colin ukikataa najiua.”
“Kajiue kwani ukifa mimi napungukiwa nini labda muuaji mwezio Hans.”
Maneno yale yaliuchoma moyo wa Mage ambaye alikuwa na matumaini ya kuchukua nafasi ya Cecy ambaye aliamini kupona kwake ni asilimia ndogo sana na hata kipona hataweza kuwa sawa. Kutokana na maelezo ya kidaktari aliyemfuata baada ya Cecy kupelekwa India.
Alimweleza kuwa kama atapona angeweza kuwa na tatizo la kusahau au kupoteza kumbukumbu ambacho huwa sawa na kichaa cha kipindi kama maji kupwa maji kujaa kuna wakati inakaa sawa kuna wakati inahama.
Baada ya kuumizwa na maneno ya Colin yaliyomkatisha tamaa alitoka nje akilia kilio cha kwikwi kitu kilichomshtua mama Colin aliyekuwa amekaa sebuleni akisoma Biblia.
“We, Mage unalia nini, Colin kazidiwa?”
“Ha..ha..pana mama, Colin kanifukuza eti hataki kunioa.”
“He! Kwa sababu gani?”
“Hata sijui, yaani anasema yupo radhi kufunga ndoa na maiti ya Cecy kuliko kunioa mimi. Eti mama, siombi ila kwa bahati mbaya Cecy amekufa mwanamke wa kuolewa na Colin kuna mwingine zaidi yangu?”
“Hakuna.”
“Sasa kwa nini ananidhalilisha kwa maneno makali?”
“Labda umemkuta leo hayupo vizuri.”
“Mama naomba kama Cecy atakufa basi nafasi yake nipewe mimi kwa vile tunajuana vizuri, inawezekana kufungwa kwa Hans na hii ajali ilikuwa mpango wa Mungu kuirudisha harusi yetu iliyofungwa mbinguni.”
“Mmh! Makubwa,” mama Colin aliguna maneno ya Mage.
“Mama naomba ukazungumze na Colin, si ulisema anatakiwa kupelekwa hospitali kila asubuhi, kazi hiyo nitaifanya mimi hata kumpikia chakula kumfulia kipindi chote nitafanya nini. Nipo tayari kuhamia hapa kuhakikisha Colin hapati tatizo lolote.”
“Basi tulia nitazungumza na Colin.”
Mama Colin alikwenda chumbani kwa Colin ili ajue kimetokea nini mpaka apishane kauli na mpenzi wake wa zamani. Alimkuta Colin amejilaza macho kaangalia juu, mlango ulipofunguliwa aligeuza shingo kuangalia nani anayeingia alimkuta ni mama yake.
“Vipi baba?” mama yake alimuuliza.
“Safi tu,” alijibu akiwa bado ameangalia juu.
“Upo sawa baba?”
“Sipo sawa,” alijibu akiwa bado macho yake yakiangalia darini.
“Kwa nini tena mwanangu?”
“Nani kampa ruhusa huyu shetani kuingia ndani?” aliuliza huku akigeuka kumtazama mama yake.
“Colin! Shetani nani?”
“Mage, sitaki kumuona machoni mwangu,” alisema kwa sauti ya juu kidogo.
“Kwa nini baba?”
“Aliyonifanyia madogo, leo ni Mungu tu nipo hai lakini kifo changu angechangia yeye hata mateso ya mpenzi wangu chanzo ni yeye. Kaniumiza mara ya kwanza hajafurahi karudia mara ya pili kaniumiza na mpenzi wangu bado tu ananifuata anataka nini kama siyo uhai wangu?”
“Lakini kwa nini unamhukumu bila kujua ujumbe alioandika umeandikwaje?”
“Mama, ulikuwa mbaya, Cecy hawezi kulia kwa ujumbe wa kawaida.”
“Colin bado hutakiwi kumhukumu kwa kitu usichojua, inawezekana ulikuwa wa kawaida lakini kwa vile mpenzi wako aliisha jenga chuki kwa Mage huenda hakufurahia ujumbe ule.”
“Lakini mama hata kama, ni haki mtu kutuma ujumbe au kupiga simu akijua kabisa mimi ni mchumba wa mtu na tupo katika hatua gani?”
“Hapo anaweza kuwa amefanya makosa lakini hakuna adui wa maisha, adui wa leo rafiki wa kesho, msamehe mwenzio nimemwacha analia kwa maneno yako makali.”
“Mama nitamsamehe Mage labda Cecy apone asipopona sitamsamehe mpaka nakufa.”
“Sikiliza mwanangu, ni wazi Mage anakupenda sana hujui tu, kama Mungu anapitisha uamuzi wake, Cecy anafariki Mage ndiye mwenye nafasi ya kuwa mkeo.”
“Mama kwa nini unakimbilia kufa mpenzi wangu, nataka nikuambie kitu. Cecy akifanya nitafunga naye ndoa kabla ya kuzikwa.”
“We’ Colin umerogwa yaani ufungwe ndoa na maiti ili iwe nini?”
“Kutimiza ahadi niliyomuahidi Cecy ambayo ndiyo ndoto yake kubwa kwangu ya kuwa mke na mume. Mama Cecy nampenda lakini yeye ni mwalimu wangu wa mapenzi ndiye wakili wa moyo wangu kanipigania wakati wote kuonesha ana mapenzi ya kweli kwangu Cecy hanipendei kitu bali mimi kama mimi.”
“Mmh! Na ukiisha muoa?”
“Nitaendelea kuwa muaminifu katika ndoa yangu mpaka mauti yatakaponichukua.”
“Kwa hiyo huoi tena?”
“Mama ndoa ipo moja tu dunia ikiisha fungwa duniani mpaka mbinguni haitafunguliwa.”
“Sasa kama amekufa si ndiyo mwisho wa ndoa yenu.”
“Kwangu itakuwa mwanzo kwa vile sijaitumikia ndoa yetu.”
“Colin mwanangu upo sawa?”
“Tena akili zangu zipo timamu.”
“Hebu pumzika naona kama haupo sawa.”
“Mama wala usisumbuke kufikiria unavyotaka kufikiria sina jibu zaidi hilo nililokupa.”
“Kwa mfano Cecy atarudi hayupo sawa na ugonjwa wake hauponi au amepooza utafanya nini?”
“Kama nitaweza kufunga ndoa na mwili wake usio na pumzi sitabadilika nitafunga ndoa na Cecy katika hali yoyote.”
”Mmh! Sawa.”
Mama Colin alitoka bila kuongeza neno huku akijiuliza Mage kamfanya nini Colin mpaka kufikia uamuzi mzito kama ule. Lakini aliamini zile ni hasira za kumwona Mage lakini baadaye zitashuka na kuelewana. Aliamini kabisa ugonjwa wa Cecy si wa kupona na kama akipona hata kuwa sawa hivyo mwanamke aliyeona anamfaa mwanaye ni Mage kwa vile tayari waliisha kuwa wapenzi kabla ya hapo.
Mage baada ya kutokeza mama Colin alikaa mkao wa kutaka kujua amezungumza nini na mwanaye.
“Vipi mama, Colin kasemaje?”
“Hii kazi niachie mimi, najua bado ana hasira zikipoa atanielewa tu.”
“Yaani mama siamini maneno anataka kuoa maiti ya Cecy kwani wanawake wamekwisha? Hata kama hanitaki mimi lakini bado wapo wazuri na wenye tabia nzuri kuliko Cecy.”
“Hilo lisikutie presha, nammudu kwa vile ni mwanangu na wala hataoa mwanamke mwingine zaidi yako. Ninyi mnafahamiana na vile mlikuwa mnapendana hivyo mtaendelea uliposimamia.”
“Umeona eeh mama, yaani Colin namshangaa kweli.”
“Sasa sikiliza kesho anatakiwa kupelekwa hospitali kwa mazoezi njoo asubuhi umpeleke.”
“Mamaa! Kwa hali hii atakubali?” Mage aliishangaa kauli ya mama Colin.
“Mage we njoo mimi nitajua nitafanya nini, nakuhakikishia lazima ataolewa na mwanangu.”
“Mmh! Mama nitafurahi, bado naona kama nipo ndotoni.”
“Wala si ndotoni, amini Colin wewe ndiye mkewe.”
“Nashukuru sana mama, basi nikuache niwahi nyumbani.”
“Hakuna tatizo msalimie mama yako.”
“Salamu zimefika.”
Mage aliagana na mama Colin na kurudi nyumbani kwao huku dua lake likiwa kwa Cecy asirudi hai ili aichukue nafasi ambayo aliamini ilikuwa yake hapo awali. Hakutaka kuyajutia maamuzi yake ya kuachana na Colin na kurudiana na Hans kwani kwake ulikuwa uamuzi sahihi ilitokea bahati mbaya ya kufungwa maisha.
Moyoni mwake alikuwa tayari kumsubiri Hans hata miaka kumi ili waoane lakini kifungo cha maisha kilimvunja nguvu na kuamini mtu sahihi kwake alikuwa Colin. Aliapa kumpigania Colin kwa nguvu zote kumrudisha mikononi mwake hata kwa kutoa uhai wa mtu. Alipofika nyumbani kwao alimweleza mama yake kilichotokea na kumshtua sana.

Itaendelea
 
SEHEMU: 26
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500

ILIPOISHIA:
Moyoni mwake alikuwa tayari kumsubiri Hans hata miaka kumi ili waoane lakini kifungo cha maisha kilimvunja nguvu na kuamini mtu sahihi kwake alikuwa Colin. Aliapa kumpigania Colin kwa nguvu zote kumrudisha mikononi mwake hata kwa kutoa uhai wa mtu. Alipofika nyumbani kwao alimweleza mama yake kilichotokea na kumshtua sana.
SASA ENDELEA...

“Mmh! Yamekuwa hayo unafikiri utafanyaje naona kila kitu kimevurugika.”
“Lakini mama Colin kasema kesho niende nikampeleke Colin hospitali.”
“Utampeleka vipi ikiwa hataki hata kukuona?”
“Mama yake kasema yeye anajua kila kitu kinachotakiwa kufanyika na ameniahidi lazima nitaolewa na mwanaye.”
“Mmh! Sawa kwa vile kasema mama yake lakini maneno ya Colin yamenitisha kusema, eti yupo tayari kufunga ndoa na maiti ya Cecy kuliko kuoa mwanamke mwingine.”
“Mama au akili ya Colin imepata tatizo baada ya kujigonga kwenye ajali?”
“Inawezekana maana ajali haikuwa ya kawaida.”
“Mmh! Inawezekana maana alivyonigeuka si kawaida yake, mama naamini Colin ananipenda.”
“Au yule mtoto alimwendea Colin kwa Karumanzila?”
“Inawezekana kabisa si bure ana urembo gani wa kumfanya Colin atake kufunga ndoa na maiti yake.”
“Hata mimi naona, lazima nasi tuhangaike ili kuhakikisha nafasi hiyo unaipata wewe.”
“Yaani huwezi kuamini sara zangu zote namuomba Ziraili amtokee Cecy na kummaliza kabisa tufikirie mambo mengine.”
“Duh! Kweli wewe kiboko, wenzio dua zao wanaomba amani wewe shari.”
“Siku zote adui yako muombee matatizo.”
“Mmh! Haya.”

MUMBAY INDIA
Katika hospitali ya Apolo katika mji wa Mumbay nchini India madaktari waliendelea kuumiza kichwa kutokana na ugonjwa wa Cecy ambao uliwachanganya akili baada ya kuweza kufumbua macho lakini mwili bado haukuwa na mawasiliano kwa asilimia zote.
Waliufanyia vipimo vyote na kukaa jopo la madaktari mabingwa kuchunguza Cecy ana tatizo gani lililopelekea kuwa katika hali ile. Hali iliyojitokeza ilikuwa tofauti na maelezo ya ajali yake, walijikuta wakifikia uamuzi wa kumrudisha Tanzania kwani waliamini hakutaka na mabadiliko yoyote kwa muda mfupi.
Matumaini ya kupata nafuu yalikuwa asilimia ndogo sana kuliko kupoteza maisha. Uhai wake waliamini hautachukua muda mrefu kwa vile mawasiliano hayakuwepo zaidi ya mapigo ya moyo yalienda kawaida pia hata mapafu yalifanya kazi vizuri.
Kilichowashangaza kuweza kupita kwa chakula laini na kufanyiwa kazi na kutoka kinyesi chepesi ambacho alisaidia bila habari. Mama yake alikuwa na kazi ya kumgeuza na kumsafisha anapojisaidia pia kumbadili ubavu ili kutoweka vidonda kwa kulalia upande mmoja kwa muda mrefu.
Mama Cecy naye alikata tamaa ya mwanaye kupona kutokana na kutotokea mabadiliko yoyote makubwa zaidi ya kuweza kutazama na kula kitu kilichokuwa kikitia matumaini kidogo.
Baada ya jopo la madaktari kukubaliana kumrudisha Tanzania, kwa kuamini kwa kuwa Tanzania ataweza kupata vitu viwili, moja kulikava taratibu akiwa nyumbani hivyo kupunguza gharama. Pili hata akifa wasipate gharama za kuusafirisha mwili wa marehemu.
Walimwita mama Cecy kumpa taarifa zile walizokubaliana kuhusu mwanaye kurudishwa Tanzania. Baada ya kuingia kwenye ofisi ya madaktari bingwa alikaa kitini huku akiwa na mkalimani daktari aliyeongozana naye.
“Mama Cecy, tumekuita hapa ili kukujulisha hatua tuliyofikia, inaonesha ugonjwa wa mwanao utachukua muda mrefu kupona. Hivyo tumeamua kumrudisha Tanzania ili uweze kumhudumia nyumbani pia kupata msaada wa matibabu ya kusaidia kuusisimua mwili.”
“Mmh! Sasa itakuwaje ikiwa hospitali inayotegemewa mmeshindwa, mwanangu si ndiyo anakwenda kufa?”
“Hapana si kufa bali huduma za muhimu tumejitahidi kadri ya uwezo wetu, hatuwezi kuendelea kumweka hospitali na kuongeza gharama wakati huduma zingine anaweza kuzipata akiwa hukohuko Tanzania. Sisi kazi yetu kubwa tumemaliza kilichobakia na kazi ya Mungu.”
“Mmh! Sawa.”
Mama Cecy alikubali kwa sauti ya kukata tamaa kwani siku zote watu waliokwenda India hurudi wamepona na ikishindikana basi mtu huyo huwa wa kumzika. Aliamini ile ilikuwa kauli ya kumpa moyo lakini siku za kuishi mwanaye zilikuwa zinahesabika.
Iliandaliwa mipango yote ikiwa pamoja na tiketi ya kurudi Tanzania na kupangiwa siku ya kurudi. Habari zile zilikuwa pigo mujarabu moyoni kwa mama Cecy mwanaye mmoja kama mboni ya jicho lake alimuona akitoweka katika sura ya dunia. Lakini yote alimuachi Mungu kwa vile muweza wa kila kitu.
Taarifa za kurudishwa Tanzania Cecy baada ya ugonjwa wake kuonekana utachukua muda mrefu kupata nafuu. Zilimfikia mama Colin na kuamini ile ndiyo nafasi ya pekee kwa Mage kuichukua nafasi ile baada ya kupata uhakika hali ile inaweza kuchukua muda mrefu kupata nafuu au maisha yake yote yawe ya kitandani alijua ilikuwa kuwapa moyo lakini Cecy alikuwa maiti mtalajiwa.
Kwa taarifa ile aliamini mwanaye pamoja na msimamo lazima atabadilika na kukubali kumuoa Mage huku akijitolea kumsaidia Cecy kwa kumwekea mtu wa kumhudumia na kumlipa kwa maisha yake yote ili tu kumfurahisha mwanaye.
Alitamani siku moja aitwe bibi na hakuwa na mtoto mwingine zaidi ya Colin ambaye ndiye aliyemtegemea kumleta mjukuu. Ugonjwa wa Cecy ulionesha hakukuwa na dalili zozote kuweza kubeba ujauzito na yeye kupata mjukuu. Moyoni alijikuta akipata mawazo mabaya ya kumuua Cecy kama mwanaye atasimamia msimamo wake wa kutotaka kuoa mwanamke mwingine.
Lakini kuna kitu kilimtisha baada ya kukumbuka kauli ya mwanaye kufunga ndoa hata na maiti ya Cecy. Hiyo ilimpa wakati mgumu. Lakini alipanga kumtumia Mage kuyabadili mawazo yake na kukubali kumuoa. Siku ya pili Mage alifika kama alivyoelekezwa na mama Colin lakini hakutakiwa kuonana na Colin mpaka mpango wake autekeleze.
Baada ya Mage kufika alifikia chumba cha msichana wa kazi na mama Colin alikwenda chumbani kwa Colin kumwamsha ili ajiandae kwenda hospitali.
“Jiandae basi ukafanye mazoezi.”
“Sawa mama.”
Colin aliingia bafuni kuoga baada ya kuoga alibadili nguo na kutoka chumbani kwake na kwenda kukaa sebuleni kumsubiri mama yake ili waende kwenye mazoezi ya viungo (Physiotherapy). Mama Colin alitoka chumbani kwake akiwa tayari kwa safari begi lake begani. Colin alipomuona mama yake alinyanyuka ili waondoke.
Lakini ghafla alishtuka kumwona mama yake akiweka mkono kichwani katika paji la uso huku amekunja uso.
“Nini mama?” Colin alishtuka.
“Kichwa,” mama alisema kwa sauti ya kujilazimisha.
“Mungu wangu! Kimefanya nini tena mama yangu?” Colin alishtuka na kujitahidi kumfuata mama yake ili amshike.
“Hapana baba , niache nitakaa mwenyewe,” mama Colin alisema huku akisogea kwenye kochi na kukaa.
“Nipe maji,” alisema akiwa ameinama mkono kichwani.
Colin alipotaka kwenda kumchukulia maji alimkataza na kutaka amwambie msichana wa kazi. Baada ya kuitwa alileta maji kwenye glasi na kumpa mama Colin aliyeyanywa yote na kupumua pumzi nyingi kisha alisema.
“Duh! Afadhali kidogo.”
“Sasa itakuwaje maana kwa hali hiyo huwezi kuendesha gari?”
“Na kweli siwezi kuendesha gari, nimekumbuka Mage alisema atakuja kukuona asubuhi.”
“Mage gani?”
“Si aliyekuwa mchumba wako.”
“Mama niseme mara ngapi kuwa sitaki kumuona yule shetani wa kike,” Colin alisema kwa hasira kidogo.
“Mwanangu wewe ndiye uliyekuwa ukinieleza siku zote nisikae na jambo baya moyoni muda mrefu naweza kupata matatizo. Kwa nini unamchukia hivyo Mage? Hata kama alifanya kosa lililosababisha ajali bado alitakiwa kusamehewa. Humtaki kuwa mpenzi wako lakini bado ni mwanadamu anayetakiwa kusamehewa na kumwona rafiki, hujui adui wa leo ni rafiki wa kesho.”
“Ni kweli mama, najitahidi kumsamehe lakini moyo wangu umekuwa mzito.”
“Huyo ni pepo mchafu tunatakiwa kumkemea.”
“Sawa mama nitajitahidi.”
“Kwa vile siwezi kuendesha gari leo basi naomba Mage atatupeleka hospitali.”
“Sawa mama,” Colin hakutaka kukataa kwani angemuudhi mama yake.
“Ngoja nimpigie simu.”
Mama Colin alijifanya kipiga simu na kujizungumzisha peke yake:
“Eeh! Umekaribia... tena umefanya vizuri... wahi basi utupeleke hospitali...haya tunakusubiri... Umekaribia... sawa... hakuna tatizo tupo tayari,” mama Colin alijifanya kukata simu.
“Kwani kafika wapi?” Colin aliuliza.
“Yupo nje ya geti.”
“Sawa.”
Mama Colin alijifanya kuelekea upande wa vyumbani na kwenda chumba cha msichana wa kazi na kwenda kuzungumza Mage.
“Mambo yamekwenda vizuri japokuwa imenibidi nilazimishe kwa cheo cha umama, sasa pitia mlango wa nyuma kisha ingilia mlango wa mbele kujifanya ndiyo unaingia.”
“Sawa mama.”
Mage alitokea mlango wa nyuma na kwenda kulichua gari alilokuwa amelipaki nje na kuingia nalo. Aliteremka kwenye gari na kuingia ndani.
“Karibu mama.”
“Asante, za hapa?”
“Nzuri.”
Mage alisogea kwa Colin na kumsalimia:
“Umeamkaje?”
“Namshukuru Mungu.”
“Nina imani hali yako itatengemaa muda si mrefu ili urudi katika majukumu yako, sara zangu zote hukutanguliza mbele nina imani Mungu ataipokea.”
“Amina.”
“Mage tunaweza kwenda.”
Mage alimshika mkono Colin na kunyanyua, alitoka naye hadi nje na kuingia kwenye gari la Mage ambalo aliomba walitumie kwa siku ile. Colin muda wote alikuwa kimya hakutaka kutia neno kwa kuhofia kumuudhi mama yake ambaye muda huo aliamini kabisa hali yake siyo nzuri hakutaka kuharibu kote kwani bado hali ya mpenzi wake Cecy ilibakia kitandawili.
Walikwenda mpaka kwenye kitengo cha mazoezi ya viungo (Physiotherapy), walipofika mama Colin alikaa pembeni na Mage alimsaidia Colin kufanya mazoezi kwa kumshikilia sehemu zingine ambazo alihitaji msaada. Kila dakika Mage alikuwa akitokwa na machozi kitu kilichomshtua Colin.
“Mage unalia nini?”
“Sijui moyoni mwako una hasira kiasi gani juu yangu.”
“Sina hasira yoyote.”
“Hapana Colin una kitu kizito juu yangu kutokana na yaliyotokea, ile ni mipango ya Mungu tu, naomba Colin unisamehe najutia kilichotokea ni mapenzi ndiyo yaliyonisukuma kufanya vile. Hata kama hutaki kuwa na mimi naomba unione rafiki na si adui.”
“Mage ningekuwa sijakusamehe tusingekuwa karibu hivi na kuweza kukusikiliza.”
“Nashukuru Colin kwa kunisamehe, naamini wewe ni mume mwema hakika Cecy kapata lulu kwenye chaza.”
“Nashukuru.”
“Vipi hali ya Cecy?”
“Kwa kweli mpaka sasa sijajua, mama amekuwa akinificha japo walinieleza inaendelea vizuri.”
“Mungu atamsaidi siku moja atasimama na kufanikisha mlichokipanga,” Mage alimpa moyo kinafiki.
“Amina.”
“Colin.”
“Naam.”
“Baada ya Cecy moyoni mwako yupo nani?”
“Bado sijamuona labda mwenetu atakaye zaliwa.”
“Basi naomba baada ya mwenenu nafasi inayofuata nipe mimi, naomba usiniweke mbali na mawazo yako.”
“Hakuna tatizo.”
“Naomba niwasiliane na wewe wakati Cecy yupo mbali.”
“Mage, suala la mawasiliano naomba tuliweke pembeni kwanza.”
“Kwa nini Colin, kukujulia hali tu.”
“Ukitaka kuwasiliana na mimi tumia simu ya mama lakini kwa sasa sitatumia simu kwa vile ndiyo iliyoleta yote haya.”
“Colin basi hujanisamehe.”
“Kukusamehe si kunilazimisha kufanya vitu nisivyo vitaka, nimekueleza sitaki kutumia simu unanilazimisha kwa kisingizio cha kutokusame. Kumbuka ubishi huo ndiyo uliosababisha yote haya.”
“Nimekuelewa Colin, nisamehe sana, nitajitahidi kukuelewa ili tusije kosana tena.”
“Itakuwa vizuri.”
“Colin nashukuru kunisamehe moyo wangu sasa mwepesi nilikuwa kama nimebeba mawe.”
“Kawaida katika maisha kuna kukosana na kupatana.”
“Nashukuru sana.”
Mama Colin aliyekuwa mbali kidogo mazungumzo yale yalimtia moyo na kuamini mpango wake umeweza kufanikiwa kwa kuamini Mage ndiye chaguo lake la awali kabla Cecy kuingilia penzi lile. Taarifa ya kurudishwa Cecy kutoka India hakutaka kumweleza haraka mwanaye mpaka akapotua nchini kwani kwa taarifa siku inayofuata ndiyo aliyokuwa akiwasilia nchini.

ITAENDELEA
 
SEHEMU: 27
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500
ILIPOISHIA:
Mama Colin aliyekuwa mbali kidogo mazungumzo yale yalimtia moyo na kuamini mpango wake umeweza kufanikiwa kwa kuamini Mage ndiye chaguo lake la awali kabla Cecy kuingilia penzi lile. Taarifa ya kurudishwa Cecy kutoka India hakutaka kumweleza haraka mwanaye mpaka akapotua nchini kwani kwa taarifa siku inayofuata ndiyo aliyokuwa akiwasilia nchini.
SASA ENDELEA...

Alipanga kuonesha ushirikiano mkubwa lakini alibakia na siri yake juu ya Cecy na ugonjwa wake ambao kama ulishindikana India basi Tanzania ilikuwa ni kusubiri kifo. Kumweka Mage karibu na Colin kungemsaidia kumweka karibu kimapenzi hata akifa Cecy basi Mage achukue nafasi ile.
Baada ya mazoezi walirudi nyumbani huku kila mmoja akiwa na furaha moyoni mwake japokuwa furaha ya Colin ilikuwa usoni na mdomoni lakini moyoni bado halikosa raha kushindwa kupata mawasiliano ya kujua hali ya mpenzi wake Cecy. Lakini aliamini baada ya muda hali yake itatengemaa na yeye mwenyewe kwenda India kumuona Cecy.
Siku ile Mage alishinda pale na kufanya kila kitu kwa ajili ya Colin, kuanzia usafi wa chumba chakula cha mchana vyote alifanya yeye na muda mwingi alikuwa karibu yake ili kuhakikisha anairudisha nafasi iliyoipoteza kupitia matatizo ya Cecy. Kitu kile kilimfurahisha sana mama Colin na kuuona mpango wake taratibu utafanikiwa.
Siku ile taarifa ilifika kwa Cecy anawasili toka India, mama Colin hakutaka kumwambia mwanaye ila saa sita usiku alikwenda kuwapokea pekle yake. Baada ya ndege tukutua abiria waliteremka na kutoka nje.
Alisimama macho yakiwa ndani huku akijiuliza Cecy atarudi katika hali gani, akiwa mapokezi alikiona kitanda kikisukumwa nyuma yake alikuwepo daktari aliyeondoka naye na nyuma ya daktari alikuwepo mama Cecy ambaye alionekana amepururuka mwili kutokana na matatizo ya mwanaye.
Mama Colin alijitokeza kuwapokea kwa kumkumbatia mama Cecy.
“Jamani dada karibuni, poleni na safari.”
“Mungu ni mwema.”
“Karibuni,” alikwenda kitandani kumwangalia Cecy ambaye muda huo alikuwa amepitiwa usingizi.
“Vipi anaendeleaje?”
“Tutazungumza nyumbani, vipi Colin naye anaendeleaje?”
“Kweli Mungu ni mwema anaendelea vizuri.”
Kwa vile alikuwa amekuja na gari aina ya Toyota Noah aliyeelezwa ndiyo inayotakiwa kumpokelea mgonjwa, walimweka kwenye gari na kuelekea nyumbani kwa mama Cecy ambako siku ile kulifanyika usafi na kuiweka nyumba katika hali nzuri. Hivyo walikuta nyumba ipo vizuri pamoja na msichana wa kazi aliyeachwa kwa ajili ya kuangali nyumba kwa muda wote ambao hakuwepo.
Baada ya kufikishwa nyumbani aliingizwa chumbani na kulazwa kitandani, muda wote mama Colin alimfuatilia Cecy na kuonesha hakuwa na dalili zozote za kupona. Pamoja na huruma kumjia lakini bado aliamini kama Cecy atakufa basi Mage ndiye mbadala wake.
Baada ya kumlaza kitandani daktari aliyekwenda na Cecy India alikaa na wazazi wawili na kuwaeleza:
“Jamani nina imani maelezo tulipewa India unayakumbuka, lakini kwa kuongezea ninataka kuwaeleza, mgonjwa hali yake bado japo kuna mabadiliko makubwa sana tofauti na alivyokwenda. Ugonjwa wa Cecy umekuwa tofauti na ugonjwa mwingine ambao madaktari bingwa wamekutana nayo huu kidogo umewala akili.
“Inaonekana mwili wa Cecy anajenga mawasiliano taratibu sana inaweza chukua muda mrefu sana kunyanyuka kitandani. Hivyo anatakiwa uangalizi wa karibu sana, kama kuna uwezekano aajiliwe mtu kwa kazi hii ili kumpumzisha mama yangu hapa kwani namhurumia amefanya kazi kubwa usiku na mchana kwa ajili ya kumwangalia mwanaye japo nilimsaidia bado muda wote alikuwa halali.
“Mgonjwa ataendelea kupata huduma ya kuchuliwa kila siku mwili mzima ili kusisimua misuli ya mwili. Nina imani kwa uwezo wa Mungu anaweza kupata nafuu upesi kwa vile mwisho wa akili ya mwanadamu ndipo uwezo wa Mungu huchukua nafasi yake,” dakta Mariamu Shaka aliwapa moyo kwa maneno ya hekima.
“Nina imani mpaka leo yupo hivi lazima turudishe shukrani zangu kwa Mungu wetu,”mama Colin alisema.
“Kingine mama, huoni maajabu pamoja na mwili kukosa mawasiliano lakini vitu vyote vya ndani vinafanya kazi hata kuweza kula japo chakula laini kitu ambacho kimewashangaza hata madaktari bingwa.”
“Ni kweli tuna kila sababu ya kumshukuru alichotupa si haba, kama leo katupa kidogo na kurudisha shukurani kwake basi hatasita kutupa kikubwa nina imani mwanangu siku moja atasimama,” alisema mama Cecy kwa hisia kali.
“Amina, Mungu wetu ni msikivu,” alijibu dokta Mariamu.
Kwa vile muda ulikuwa umekwenda mama Colin aliaga kurudi nyumbani na kumwacha mama Cecy mgonjwa na daktari ambaye alilala pale ili kesho yake baada ya kumpatia mgonjwa huduma arudi nyumbani kwake.
Kutokana na hali aliyomuona nayo Cecy hakutaka kumweleza mwanaye kwa kujua atamshtua hata kukosa raha na kumuongezea matatizo kwa vile alimpenda sana mchumba wake. Lakini alijiuliza mwanaye akijua lazima atamweleza vibaya, alipanga kumwambia baadaye kuwa Cecy amerudi.
Aliamua kukaa kimya huku wiki ilikatika bila kumweleza kitu chochote mwanaye juu ya Cecy kurudi toka India. Siku zote alitoka peke yake kwenda kumwona Cecy na kuonesha kugushwa na hali ile huku akimlipa daktari aliyekwenda naye India pesa nyingi ili kumpatia huduma ya kumchua na kumwangalia kila siku baada ya kazi.
Wema wake ulikuwa wa mamba wa kutoka machozi lakini alikuwa na siri moyoni mwake kujionesha anamjali mgonjwa. Lakini aliamini kupona kwa Cecy ni ndoto, kila alipoulizwa na mama Cecy kuhusu hali ya Colin alisema hajambo kiasi.
“Hawezi kutembea?”
“Mmh! Kwa sasa amekatazwa kutembea.”
“Kwa nini basi usimlete aje amwone mchumba wake?”
“Atakuja hali yake ikitulia.”
“Kwa hiyo hali yake inaonekana bado.”
“Ni kweli.”
“Mmh! Mpe pole isingekuwa hali ya Cecy ningekuja kumwona mkwe wangu.”
“Mungu atawapa afya na kuweza kunyanyuka.”
“Mungu atasikia dua zetu, kila jambo la heri Mungu ulishika mkono nina imani Cecy na Colin watasimama na siku moja kusherehekea harusi yao.”
“Amen,” mama Colin aliitikia huku moyoni akijisemea “Labda harusi aliyosema mwanaye ya kufunga ndoa na maiti ya Cecy, lakini harusi ya sherehe ukumbuni itakuwa muujiza.”
Mama Cecy aliamini hali ya Colin ni mbaya ila mama yake anampa moyo, alipanga siku akipata nafasi afike kumwona kwani haikuwa vizuri mzazi mwenzie kuja kumuona mwanaye na yeye kutokwenda kumuona Colin. Kwa vile hali ya mwanaye alijua alipanga siku moja baada ya kumpatia chakula akilala atoke mara moja kwenda kumwona Colin na kuwahi kurudi.
Siku ya tatu ambayo mama Colin alipiga simu kuwa hatakwenda kwa vile kuna sehemu ambapo angerudi usiku. Siku hiyo mama Cecy aliitumia kumwandaa Cecy ambaye alishangaa kuona mabadiliko madogo baadhi ya sehemu kupata joto kama miguuni ambako kulikuwa na ubalidi kwa muda mrefu.
Baada ya kumpatia chakula chepesi na dawa alimwacha apumzike na yeye kukodi gari mpaka kwa mama Colin kumjulia hali mgonjwa. Wakati huo Mage alikuwa akiendelea kuwa karibu na Colin ili kujivuta karibu kwa kuamini baada ya kifo cha Cecy basi nafasi ile ni yake.
“Colin nina imani sasa hivi afya yako ni nzuri unaweza hata kuendesha gari.”
“Namshukuru Mungu, pia nashukuru kwa msaada wako kwangu kwa muda wote wa kuniangalia.”
”Usijali nipo kwa ajili yako, nitapigania afya yako hata kwa gharama yoyote.”
“Usiwe na wasi nina imani sasa hivi sijambo na wiki ijayo nitakwenda India kumwangalia Cecy.”
“Lakini hali yako si bado kwa nini usisubiri upone kabisa.”
“Mage, mimi sijambo sasa hivi naweza kufanya lolote, lakini afya ya mpenzi wangu siijui. Mpaka leo bado yupo hospitali huenda yupo kwenye hali mbaya lazima niende nikajue hali yake.”
“Mmh! Sawa,” Mage aliogopa kutia neno kwa kuhofia kukorofishana na Colin ambaye alionekana bado ana mapenzi mazito na Cecy. Alijua msimamo wake ni kwa vile hajamwona lakini akimwona hali yake aliamini lazima angebadili mawazo na nafasi ile kumpa yeye.
Wakiwa katika ya mazungumzo walishtuliwa na hodi, waliponyanyua macho Colin hakuamini kumwona mama Cecy aliyejua yupo India na mpenzi wake, lakini afya yake ilioneka imedhoofu sana.
“Ha! Mama ni wewe?” Colin alisema huku akinyanyuka na kwenda kumpokea mama mkwe.
“Ni mimi mwanangu, unaendeleaje na wewe?”
“Namshukuru Mungu, hali yangu sijambo. Sasa hivi nilikuwa nasema wiki ijayo nakuja India kumwona mchumba wangu. Ha..ha..lafu mbona uko huku Cecy umemwacha na nani hospitali?”
“Kwani mama yako hajakwambia?”
“Kuhusu nini?”
“Kurudi kwetu, nimemuulizia ameniambia hali yako bado si nzuri, hivyo nikaona nije nikujulie hali baba yangu na kumwacha mchumba wako na msichana wa kazi.”
“Mama unataka kuniambia Cecy yupo Tanzania?” Colin alishtuka huku macho yamemtoka pima.
“Colin unauliza ukweli au unatania?”
“Mama mimi na wewe hutujawahi kutaniana, hata muulize Mage muda si mrefu nilikuwa namwambia lazima nije India kumjulia mchumba wangu hali yake baada ya mimi kuamini nimepona.”
“Siamini unachokisema najua unaumwa hivyo hukuwa na uwezo wa kuja kumpokea mchumba wako, lakini sikubali kauli yako kuwa huna taarifa yoyote kuwa mimi na Cecy tupo nchini kwa wiki sasa.”
“Wiki!?” Colin alishtuka.
“Colin hebu acha kujitoa akili, ina maana mama yako hajakwambia?”
“Hajaniambia, ina maana mama anajua?”
“Mbona ndiye aliyetupokea na kila siku lazima afike kumuona mgonjwa kasoro leo.”
“Mmh! Una maanisha mama yangu, mama Colin?”
“Ndiye huyohuyo, ina maana hajakwambia?”
“Haki ya Mungu sijui kitu, sikuwa ugonjwa wa kushindwa kuja kumpokea mpenzi wangu, kwa nini mama kanificha hivi, Cecy mpenzi wangu atanielewa vipi?” Colin alisema kwa uchungu.
“Sijui, labda muda wake wa kukueleza bado, lakini namshukuru sana amejitolea kwa hali na mali ili kuhakikisha afya ya mpenzi wako inatengemaa.”
“Vipi hali ya mpenzi wangu?”
“Bado, lakini ana afadhali kwa mbali sana.”
Colin alinyanyuka na kumwomba mama Cecy aende akamwone mpenzi wake.
“Mama naomba nikamwone mpenzi wangu.”
“Colin pumzika kwanza hujapona vizuri, nilikuja kukuona tu.”
“Hapana...kama Cecy ana wiki hapa mama kanitendea unyama mkubwa sana,” Colin alisema huku akionekana kuchanganywa na taarifa zile ambazo hakutegemea kusikia kwa kuamini Cecy bado yupo India.
Colin hakusema kitu alikwenda ndani na kuchukua ufunguo wa gari na kutoka.
“Mama naomba twende,” Colin alipagawa na kusahau muda mfupi alikuwa na Mage alitoka bila hata kumuaga na kumfanya Mage aumie moyoni kuona ana kazi kubwa ya kuubadili moyo wa Colin. Lakini aliamini kifo cha Cecy ndiyo tiketi yake ya kuwa na Colin, aliendeleza dua za kuomba kifo cha Cecy.
Colin japo alikuwa hajaruhusiwa kuendesha gari alikwenda kuchukua gari na kumwomba mama Cecy waondoke. Waliongozana hadi kwenye gari na kuondoka kuelekea kwa Cecy. Wakiwa ndani ya gari Colin alimdodosa mama Cecy.
“Mama kwanza vipi hali ya mchumba wangu?”
“Hajambo, lakini bado.”
“Bado nini kinamsubua?”
“Siwezi kukueleza kwa vile unakwenda mwenyewe kila kitu utakiona.”
“Mmh! Sawa.”
Colin aliendesha gari huku akiwa na mawazo mengi juu ya mama yake kukaa kimya huku kila siku anakwenda kumwona mgonjwa bila kumwambia aljiuliza alikuwa na maana gani na mchumba wake angemwelewa vipi kama amerudi bila kwenda kumwona.
Walipofika walikwenda hadi ndani, Colin alionekana mwenye kimuhemuhe cha kumwona mpenzi wake. Kwa vile alikuwa akikijua chumba cha Cecy aliingia moja kwa moja. Lakini chumbani kwake hakuwemo alitoka na kukutana na mama Cecy.
“Mama mpenzi wangu yupo wapi?” Colin aliuliza macho yamemtoka pima na presha juu.

Itaendelea Ijumaa
 
SEHEMU: 28
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500

ILIPOISHIA:
Walipofika walikwenda hadi ndani, Colin alionekana mwenye kimuhemuhe cha kumwona mpenzi wake. Kwa vile alikuwa akikijua chumba cha Cecy aliingia moja kwa moja. Lakini chumbani kwake hakuwemo alitoka na kukutana na mama Cecy.
“Mama mpenzi wangu yupo wapi?” Colin aliuliza macho yamemtoka pima na presha juu.
SASA ENDELEA...

“Colin taratibu umefika utamuona, subiri,” mama Colin alisema huku akielekea chumba alicholazwa Cecy.
Alipakaribia alipogusa mlango alishtuka kusikia Cecy akimwita sauti ambayo ilipotea toka alipopata ajali iliyokuwa ikimwita.
“Ma..a..ma...ma..a..ma.”
Alisogea haraka kitandani na kuitikia.
“Abee mwanangu.”
“Nigeuze nimechoka kulala hivi?”
Mama Cecy aliona ule ni muujiza mkubwa kwake kwa vile siku zote mgonjwa alikuwa wa kulala bila kujitikisa wala kusema neno zaidi ya kutumbua macho tu bila kuyapepesa. Alimgeuza na kumlaza vizuri.
“Niwekee mto chini.”
Mama yake haraka alichukua mtu na kumwekea mwanaye.
“Mama ulikuwa wapi?”
“Nilikuwepo nje.”
“Mbona dada alisema ulitoka?”
“Nilifika dukani.”
“Mume wangu Colin yupo wapi?”
“Yupo sebuleni.”
“Ana fanya nini?”
“Ndiyo amefika sasa hivi.”
“Alikuwa wapi?”
“Kwao.”
Cecy kusikia Colin yupo sebuleni alitaka kunyanyuka na kuishia kukaa kitako na kurudi tena chini. Kitendo cha kujinyanyua peke yake yalikuwa maajabu mengine kwa mama Cecy ambaye alipiga ishara ya msalaba na kumsukuru Mungu kwa kile alichokionesha muda ule mbele yake.
“Asante Mungu... Asante baba... Asante kwa kila akifanyacho mbele ya macho yangu.”
“Mama,” Cecy alimwita mama yake.
“Abee.”
“Naomba niende kwa Colin.”
“Subiri.”
Mama Colin alitoka hadi sebuleni ambapo Colin alikuwa akizungumza na dada wa kazi juu ya hali ya Cecy. Alimdodosa na kuelezwa yote toka akipofika na hali aliyokuwa nayo na maajabu ya siku ile alipokuwa akimtengeneza kitandani na kushtuka kumsikilia akiiita jina la Colini na baadaye aliita mama yake.
Dada wa kazi alimweleza ametoka, ndipo alipoanza kumuuliza maswali ambayo alimjibu kwa vile mambo mengi alikuwa akiyaelewa. Baada ya mazungumzo na dakika ishirini Cecy aliomba kugeuzwa tofauti na siku za nyuma alikuwa wa kulala tu na kugeuzwa kwa kipindi.
“Kwa hiyo toka apate ajali ndiyo kazungumza leo?”
“Ndiyo najua hata mama ataona muujiza.”
“Mmh!” Colin aliguna na kujiuliza nini hatima ya mpenzi wake ikiwa sehemu inayotegemewa na watu wote imeshindwa. Ile kwake ilikuwa picha mbaya sana kwake na kukiona kifo cha Cecy kipo mbele. Aliamini yote aliyasababisha yeye alijikuta akitokwa na machozi ya uchungu.
“Colin baba,” Colin alishtuliwa na mama Cecy.
“Naam mama,” Colin aliitikia huku akinyanyua kichwa.
“Ha! Unalia nini tena?” mama Cecy alishtushwa na machozi ya Colin.
“Inauma.”
“Cecy anakuita.”
Colin bila kujibu alinyanyuka na kuelekea chumbani ambako alimkuta Cecy amelala kitandani mwili ukiwa umepururuka kwa ugonjwa.
“Cecy,” aliita kwa sauti huku akisogea kitandani na kumkumbatia mpenzi wake.
“Colin mume wangu,” Cecy alisema huku akijitahidi kumkumbatia mpenzi wake.
Ilikuwa ajabu nyingine Cecy kuweza kumkumbatia Colin kwa mwili uliobakia mifupa mitupu.
“Ni mimi Cecy mke wa maisha yangu.”
“Colin nifurahi kukuona mpenzi wangu japokuwa nina muda mrefu nilikuwa siwezi kuzungumza wala kujigeuza. Lakini kuja kwako kumekuwa dawa ya kupona kwangu. Hata nikifa sasa hivi moyo wangu utakuwa na furaha kwa vile nimekuona chakula cha nafsi yangu,” Cecy alisema kwa sauti ya chini.
“Ni kweli naamini Mungu alituumba kwa ajili yetu, siamini niliyoyasikia na niliyo kutana nayo leo,” Colin bado alikuwa kama yupo ndotoni.
“Ni Mungu tu mpenzi wangu.”
Siku ile Colin alishinda pale mpaka jioni pembeni ya Cecy, pamoja na yeye hali yake kuwa katika uangalizi lakini hali aliyomkuta nayo mpenzi wake aliamini amepona kabisa. Jioni daktari aliyempeleka India alipopitia kuangalia hali mgonjwa wake alishikwa na mshangao baada ya kukuta hali ya Cecy ina mabadiko makubwa.
“Mungu mkubwa siamini ninachokiona leo,” mama Cecy alisema huku akifuta machozi kwa kiganja cha mkono.
“Ni kweli Mungu katenda muujiza wake,”Colin alisema huku naye akifuta machozi.
“Jamani msinililie tena, kama nilikuwa nusu mfu kwa muda mrefu na leo nipo hivi, basi aminini nimepona,” Cecy alisema kwa kujiamini.
Siku ile kazi ya masaji aliifanya Colin huku akimpa moyo mpenzi wake kuwa atapona.
“Kweli nitaweza kutembea? Maana kwa hali ya kulala kitandani kama nyoka nimechoka.”
“Utapona tena na kusimama, nakuahidi baada ya kupona nakufanyia bonge la surprise.”
“Colin nawe kwa kunipa moyo, je nisipopona?”
“Ugonjwa utakuwa wetu sote.”
“Hutafuti mwanamke mwingine?”
“Cecy baada ya kukufungia moyoini mwangu ufunguo niliutupia baharini, mimi ni kipofu mbele yako. Wewe ndiye uliyekuwa mwanamke wa mwisho kuonwa na macho yangu. Siamini kama nitapenda tena katika maisha yangu kama tutatengana. “Nakupenda Cecy zaidi ya kupenda. Amini usiamini muda si mrefu utasimama na kutimiza ndoto yetu ya kuwa mke na mume.”
“Colin sikuwahi kumwamini mtu katika maisha yangu lakini wewe kwangu sina la kuongeza nakuamini mpenzi wangu. Mungu ana maajabu yake amani kila litendekalo lina makusudio yake.”
“Cecy Mungu waajabu wewe ni yule wa jana leo na kesho, Mungu alikupa azina ya busara na hekima ni mtaji mkubwa katika maisha yetu.”
“Asante kwa kulitambua hilo.”
Pamoja na Cecy kuwa mgonjwa aliweza kuzungumza mengi mpenzi wake mpaka ulipofika muda wa kumwacha apumzike. Colin hakutoka alilala pembeni ya mpenzi wake. Daktari Mariam alishangazwa na hali aliyomkuta nayo Cecy ulikuwa muujiza mkubwa maishani mwake.
“Kweli Mungu mkubwa hutenda pasipo mtu kutegemea, siamini... siamini kuna kila sababu ya kumshukuru Mungu wetu,” dokta Mariam Shaka alichanganyiwa na hali aliyomkuta nayo Cecy.
Dokta Mariam alisema baada ya kumwona Cecy akijigeuza kitandani na kumwita mpenzi wake.
“Colin.”
“Naam mpenzi.”
“Nataka kwenda msalani.”
Colin alimnyanyua na kumkalisha kisha aliomba chombo cha kujisaidia na kupewa, kazi yote ya kumhudumia mpenzi wake alifanya mwenyewe. Baada ya kumwogesha alimrudisha kitandani. Baada ya huduma zote dokta Mariam alimchunguza ilionesha kila kiungo kimepata ufahamu.
Kila alipomminywa kwa nguvu alipiga kelele, ile ilikuwa dalili nzuri kuonesha mwili mzima umeisharudisha mawasiliano. Baada ya kufanyiwa uchunguzi alikalishwa kitako na kuelezwa aliyekuwepo mbele yake ni dokta Mariam Shaka dokta aliyekwenda naye India kwa siku zote alizokuwa naye huko katika kukuchua mwili.
“Asante dada yangu Mungu atakulipa,” Cecy alisema huku machozi yakimtoka.
“Usijali, Mungu mkubwa naamini muda si mrefu utasimama tena, hatua ya leo ni kubwa kweli kila lililo zito kwa mwanadamu kwa Mungu ni jepesi.”
“Hakika,” alisema mama Cecy.
Colin alikuwa karibu muda wote kuonesha jinsi gani anavyomjali mpenzi wake ambaye aliamini ni mwanamke wa maisha yake. Siku hiyo kila kitu Colin aliomba amfanyie mpenzi wake. Ilikuwa faraja kubwa kwa Cecy ambaye pamoja na kuwa bado mgonjwa lakini ukaribu wa kipenzi chake uliongeza faraja moyoni mwake.
***
Upande wa pili baada ya Colin kuondoka na mama Cecy, Mage hakuondoka alibakia kumsubiri Colin kwa kuamini kutokana na maelezo ya mama yake Cecy alikuwa nusu mfu mtu wa kulala tu. Hivyo asingekaa muda mrefu angerudi mapema na kumkuta, alitumia muda mwingi kuangalia mikanda ya video.
Mama Colin alirudi saa mbili kasoro usiku na kumkuta Mage peke yake amejaa tele sebuleni. Mage alipomwona mama mkwe zilipendwa alinyanyuka na kumpokea.
“Wawooo, karibu mama.”
“Asante mwangu, za kushinda?”
“Mmh! Nzuri.”
“Mbona kwanza umeguna kabla ya kujibu.”
“Hamna mama.”
“Mwenzio yupo wapi?”
“Ametoka.”
“Ametoka! Kaenda wapi?”
“Kumwona mgonjwa.”
“Mgonjwa! Mgongwa gani?”
“Cecy.”
“Cecy! Nani kamwambia kama Cecy yupo?” mama Colin alishtuka kusikia habari zile.

Itaendelea
 
SEHEMU: 29
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500

ILIPOISHIA:
Walikwenda kwa mama Cecy ambako kulikuwa na nyumba ya kisasa iliyojengwa na Colin kwa ajili ya mpenzi wake. Walipofika Mage hakushuka kwenye gari na mama Colin aliingia ndani, sebuleni kulikuwa na mama Cecy aliyekuwa ametulia macho yake yakiwa kwenye runinga.
SASA ENDELEA...

Alipomuona anaingia alihamisha macho kwenye runinga na kumtazama mlangoni alikuta ni mama Colin. Alinyanyuka alipokuwa amekaa na kwenda kumpokea.
“Karibu dada.”
“Asante,” mama Colin alijibu kwa sauti ya chini huku akificha hasira zake juu ya kitendo cha mzazi mwenzie kwenda kwake na kufanya mwanaye amchukie kwa kumficha kuwemo kwa mpenzi wake nchini.
“Karibu, Vipi hujafika nyumbani?” Mama Cecy alimshangaa usiku ule wakati alisema siku ile hawataonana.
“Colin yupo wapi?” mama Colin aliuliza kwa sauti kali kidogo.
“Dada hata salamu unakimbilia kumuulizia Colin?”
“Salamu si muhimu kama kujua hali ya mwanangu.”
“Mwanao hajambo.”
“Sitaki kusikia hajambo bali kumwona yupo au ameondoka?”
“Yupo chumbani na mchumba wake.”
“Chumbani? Anafanya nini?”
“Mama Colin ni swali gani hilo, ina maana chumbani kwangu kuna mzoga?” mama Cecy alijibu kwa hasira.
“Siyo hivyo dada, si unajua Colin bado mgonjwa mpaka sasa sijui yupo wapi.”
“Colin na Cecy nani mgonjwa na ugonjwa mwanangu kautoa wapi, mbona tumekwenda vizuri tunataka kuharibu mwisho?”
“Basi samahani dada najua Cecy anaumwa, lakini sijui Colin yupo wapi maana nilimwacha nyumbani amesikia amekuja kumwona mchumba wake.”
“Nimekujibu nini?”
“Sawa ngoja nikamwone.”
Mama Colin alielekea chumbani kwa mgonjwa akiamini atamkuta mwanaye pembeni ya kitanda huku akiumizwa na hali ya mpenzi wake aliye katika hali unusu mfu. Alipofika alipigwa na butwaa kumkuta Colin akimlisha Cecy matunda.
“Ha!” mama Colin alijikuta akipiga ukelele wa mshtuko.
“Aah! Mama karibu, Mungu mkubwa kuja leo mpenzi wangu kanyanyuka kama ningekuja mapema sasa hivi angekuwa hajambo kabisa,” japo yalionekana maneno ya kawaida lakini yalikuwa kama mkuki moyoni mwa mama Colin.
“Ha! Kweli Mungu mkubwa Cecy umenyanyuka mama!” mama Colin hakuamini alichokiona mbele yake.
“Karibu mama mkwe, sina cha kukulipa ina namuomba Mungu anipe afya niweze kukulea mama yangu katika maisha yangu yote. Umeweza kupigania maisha yangu kwa hali na mali. Naamini kabisa kwa Mungu hakuna kinachoshindikana, karibu mkwe,” Cecy alisema huku akijiweka vizuri.
“Asante mkwe wangu, Mungu ni muujiza ninachokiona mbele yangu ni kazi ya Bwana aliyotenda.”
Mama Colin alikwenda kumkumbatia Cecy ambaye alikuwa amepururuka na kubaki mifupa mitupu. Mama Cecy naye alikuwa amefika hakutia neno zaidi ya kukaa kimya akimwangalia mzazi mwenzie.
“Jamani leo ni katika siku ambazo nimepata furaha ya ajabu, nakuahidi kuipigania afya ya Cecy kwa gharama yoyote ili kuhakikisha anarudi katika hali yake ya zamani,” alisema mama Colin.
“Asante mkwe sina cha kukulipa bali kukuonesha mapenzi ya dhati yasiyo na chembe ya unafiki.”
“Asante mkwe wangu,” mama Colin alijikuta akitokwa na machozi kwa maneno mazito ya Cecy ambaye alipoteza kauli na viungo vya mwili kufanya kazi kwa zaidi ya miezi sita.
“Jamani nina imani Mungu ni mkubwa ameweza kutusimamia kwa hiyo tumshukuru kwa pamoja kwa kuweza kutenda juu yangu,” Cecy alisema huku akitaka kuteremka kitandani.
“Baki kitandani tutaomba ukiwa hapahapa kitandani,” Colin alimzuia mpenzi wake.
“Naomba niteremke ili nipige magoti pia kwa kauli yangu kufunguka naomba niongoze maombi kumshukuru Mungu.”
Baada ya wote kupiga magoti na kufumba macho Cecy alianza kuomba:
“Asante baba Mungu kwa wema na utukufu wako, umekuwa nami muda wote wa maradhi na mateso yangu mazito ambayo kila mwanadamu alikata tamaa lakini baba ulikuwa nami muda wote.
“Baba sina cha kukulipa zaidi ya kukuabudu kwa kufuata yote unayotaka tuyafanye na kuyaacha yote uliotukataza. Baba rudisha furaha mioyoni mwa wote waliopoteza matumaini na kuwafanyia wasiyo yategemea rudisha furaha kati nyumba yetu iliyopotea kwa muda mrefu tupe afya njema.
“Baba kila aliyetokwa na machozi kwa mayeso yetu mfute na umpe furaha kama kuna aliyefurahia matatizo yetu baba msamehe kwa vile hajui atendalo. Umetuumba wanadamu kwa udongo ulio safi basi tupe mioyo yetu upendo tupendani tuoneane huruma na kuombeana mazuri.
“Asante Baba kwa kuninyanyua leo, asante kwa kurudisha furaha iliyitoweka kwa muda mrefu katika familia zetu.Walipe mara mia wote waliotoa kwa ajili ya matatizo yetu. Baba yaliyotokea ni majaribu tupe imani ya kusimama upande wako na usimpe nafasi adui shetani kutupotosha.
“Baba timiza ndoto yetu ya mimi kuwa mke halali wa Colin, Baba Mungu nashukuru kwa kunichagulia mume mwema mwenye mapenzi ya dhati, nami namwahidi kuwa mke mwema katika siku za pumzi zangu. Simamia ndoa yetu ondoa kila jicho la hasada roho chafu za chuki, uongo na uadui kwa jina la mwanao Yesu Kristo aliye hai, Ameni.”
“Ameni,” waliitikia pamoja huku kila mmoja akifuta machozi kutokana na maombi mazito aliyoporomoshwa na Cecy.
“Naombeni maji,” Cecy aliomba maji baada ya kuomba kwa muda mrefu na kuvunjwa jasho kama maji, kutokwa na jasho jingi ulikuwa muujiza mwingine kwa mama Cecy baada ya kutotoka jasho jingi kwa zaidi ya miezi sita.
Alipatiwa maji na kuomba kupumzika, Colin alimpandisha kitandani na kumfunika shuka.
“Colin mpenzi napumzika kidogo ila usiondoke wewe ndiyo furaha yangu.”
“Sawa mpenzi.”
Walimwacha Cecy amelala na kutoka nje kwa ajili ya mazungumzo.
“Jamani kuna nini kimefanyika ambacho mimi sikijui?” mama Colin aliuliza.
“Hakuna kilichofanyika na muujiza wa Mungu, wakati narudi nilisikia Cecy ananiita nilipoingia nilishtuka kumwona akiniita. Nilipomsogelea sikiamini kumwona mwanangu katika hali ile kwani niliisha kata tamaa.”
“Kweli nimeamini muujiza wa Mungu upo,” alisema mama Colin.
“Ni kweli.”
“Sasa kwa vile nilikuwa nimekuja ghafla wacha nikapumzike pia tumwache mgonjwa apumzike ili kesho tujue tutafanya nini.”
“Dokta Mariam amesema lazima tumpeleke hospitali akafanyiwe vipimo.”
“Hakuna tatizo, Colin baba,” alimgeukia mwanaye.
“Naam mama”
”Itaidi tuondoke ili ukapumzike kwa vile nawe hali yako haijatengemaa vizuri.”
“Mama mimi nimepona kabisa mgonjwa ni Cecy na nipo hapa kwa ajili ya kuhudumia kwa kila kitu.”
“Sawa, lakini twende nyumbani tutakuja kesho.”
“Mama naomba unisamehe, leo siondoki nitalala na mpenzi wangu.”
“Mmh! Sawa.”
“Nikutakie usiku mwema.”
Mama Colin alimkumbatia mwanaye kisha alimuaga kuelekea alipopaki gari. Alimkuta Mage amesinzia baada ya kumsibiri kwa muda mrefu, alipofika alimwamsha.
“Mage pole kwa kukuweka.”
“Isijali mama mkwe, vipi mbona umechelewa Colin ameisha ondoka?”
“Yupo.”
“Mbona umemwacha?”
Mama Colin alimweleza Mage yote aliyoyakuta na kumfanya asindwe kuamini na kujikuta akiuliza:
“Mama unayosema ni kweli?” Mage hakuamini.
“Kweli kabisa, yaani nilichokiona mbele yangu ni muujiza Cecy amenyanyuka tena anaonekana kama mtu aliyepata nafuu wiki nzima.”
“Mmh! Nimekwisha!” Mage alisema kwa sauti ya kukata tamaa.
“Kwa nini unasema hivyo?” mama Colin alishtuka.
“Mama kweli Colin atanioa?”
“Sikudanganyi, Colin anampenda sana Cecy, hakuna kiumbe kitakacho mbadili mawazo, yaani nimemkuta kama mwenda wazimu sijui Cecy angekufa mwanangu angekuwaje.”
“Mmh! Sawa,” Mage alisema huku nguvu zikimwisha na kujikuta akijilaza kwenye usukani badala ya kuondoa gari.
“Vipi mbona hivyo?”
“Mama kupona kwa Cecy ni pigo zito moyoni mwangu, hapa nilipo sina hata nguvu za kuendesha gari. Naomba mama yangu uendeshe naweza kugonga.”

Itaendelea
 
SEHEMU: 30
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500
ILIPOISHIA:
“Mmh! Sawa,” Mage alisema huku nguvu zikimwisha na kujikuta akijilaza kwenye usukani badala ya kuondoa gari.
“Vipi mbona hivyo?”
“Mama kupona kwa Cecy ni pigo zito moyoni mwangu, hapa nilipo sina hata nguvu za kuendesha gari. Naomba mama yangu uendeshe naweza kugonga.”
SASA ENDELEA...

“Hakuna tatizo.”
Mama Colin alizunguka upande wa pili ili kuendesha gari baada ya Mage kupatwa na mshtuko kutokana na Cecy kupona. Mama Colin alishangazwa na hali ya Mage kubadilika ghafla baada ya kupata taarifa ya kupata nafuu kwa Cecy.
“Mbona umekuwa hivyo?”
“Mama basi tena.”
“Lakini Mage hukutakiwa kununua pilipili kwa shughuli ya mwenzio ile ilikuwa pata potea. Nafasi uliichezea mwenyewe huna wa kumlaumu.”
“Mmh! Sawa.”
Kutokana na kutokuwa kwenye hali nzuri Mage alilala palepale ili kuitafuta siku ya pili, mama Colin naye alikuwa na maswali yasiyo na majibu juu ya hali ya Cecy kubadilika kabisa wakati alikuwa nusu mfu. Lakini upande mwingine alimshukuru Cecy kupona kama angekufa mwanaye angekuwa chzi kwa jinsi alivyopagawa kwa mpenzi wake kupona.
***
Siku ya pili Cecy alichukuliwa na kupelekwa hospitali kwa ajili ya uchunguzi zaidi wa afya yake, majibu yalionesha kila kitu kimo sawa. Majibu yale yalikuwa faraja tele kwa Colin na kwa mama Cecy ambao ndiyo walioteseka kipindi chote cha ugonjwa wa Cecy.
Alitakiwa kufanya mazoezi kutokana na viungo kukaa muda mrefu bila kufanya kazi, afya ya Colin ilikuwa imetengemaa aliomba kwenda kupumzika na mchumba wake Afrika ya kusini kwa miezi miwili.
Wazazi hawakuwa na jinsi walikubali watoto wao waende Afrika ya kusini kupumzika na kuendelea kupata huduma za kiafya. Baada ya siku mbili Colin na Cecy walielekea Afrika ya kusini katika mji Port Elizabeth katika hotel ya The Beach Hotel kwa ajili ya mapumziko baada ya mateso ya muda mrefu.
Colin alichukua muda ule kuhakikisha anafuta machungu yote aliyoyapata mpenzi wake kutokana na ajali mbaya iliyowapata ili kurudisha imani kwake kwa vile Mage alionekana bado yupo karibu na familia yao hasa mama yake hivyo kutia doa upendo wake.
Muda mwingi walitumia kukaa wawili chumbani kila asububi na jioni walifanya mazoezi madogo madogo katika Gim iliyowa katika hoteli waliyofika na majira ya saa moja walitembeatembea pembezoni mwa ufukwe. Lilikuwa penzi lililozaliwa upya kwa wapendao baada ya kupoteana kwa kipindi kirefu.
Baada ya wiki mbili Cecy naye kimwili kilianza kurudi wakiwa wamejipumzisha chumbani kwao, Cecy alimuuliza mpenzi wake ambaye aliamini alikuwa na ufahamu tofauti na yeye alikuwa nusu mfu.
“Colin nina imani wakati naumwa ulikuwa karibu na Mage.”
“Si kweli, huwezi kuamini toka ile ajali sina ukaribu na mtu nilikuwa sitoki ndani hata simu kuanzia siku ile situmii. Najua Cecy huniamini lakini nakuhakikishia niliapa mbele ya mama yangu na mama Mage walipokuja kuniona hospitali kuwa sitaoa mwanamke mwingine kama wewe ungekufa.
“Niliwaeleza kama utakufa nitatimiza ahadi niliyokuahidi kwa kufunga ndoa na maiti yako na nisingeoa tena mpaka nakufa.”
“He! Kwa nini ufanye hivyo, ningekufa mimi si ingekuwa nafasi ya mwingine. Heri tungekuwa tumezaa ulikuwa na sababu ya kufanya hivyo.”
“Cecy kuoa mwanamke mwingine wakati ajali nimesababisha mimi ningekuwa nimeshiriki kwenye kifo chako. Wewe ndiye wakili wa moyo wangu umenitetea wakati wote wa matatizo yangu. Bila wewe kitendo alichonifanyia Mage ningeweza kuwa chizi.”
“Asante kwa kunipenda kwa kipindi chote cha mateso yangu, Colin nimeamini wewe ni mume wa maisha yangu naomba Mungu adumishe penzi letu ufe nikuzike nife unizike.”
“Asante mpenzi wangu nitakupenda siku zote za maisha yangu.”
“Hata mimi, Colin,” Cecy alimwita mpenzi wake akimtazama usoni.
“Naam.”
“Siku ya kuondoka ulikataa kubeba simu sasa tutawasiliana vipi na nyumbani?”
“Nimeapa sitatumia tena simu katika maisha yangu kwani ndiyo sababu yakutaka kuyachukua maisha yetu. Pia wazazi nimewajulisha tupo hoteli gani wakitutaka watupata tukiwataka tutawapata kwa njia ya simu ya hotelini.”
“Colin, naweza kusema wivu wangu wa kijinga umetufikisha hapa, sikutakiwa kukosa imani kiasi kile cha kutaka kila kitu katika simu yako nikione. Naweza kusema nilijitakia mwenyewe. Nimejifunza kitu sikutakiwa kukubana kiasi kile kwa vile mapenzi ya kweli yako moyoni na wala si kwenye simu.
“Colin nilikupenda kupitiliza na kujikuta nakuwa kichaa wa mapenzi kwa ajili yako, lakini umenidhilishia kwa vitendo kuwa unanipenda mapenzi ya dhati kwa vile hukuyumba wakati wa matatizo yangu. Angekuwa mwanaume mwingine angekwisha kuwa na mchumba mwingine au ameisha funga ndoa.
“Colin mpenzi wangu nakuomba kuanzia leo hii tumia simu, mimi si limbukeni tena wa simu. Upendo na uaminifu wako ameufanya moyo wangu uwe huru na kukuamini kwa asilimika mia. Colin najivunia kuwa na mwanaume kama wewe nimekutafuta kwa udi na uvumba japo mama yako alifanya utani kuniita mkwe lakini niliamini nami nina haki ya kuwa na mwanaume nimtakaye aliye katika hali yoyote.
“Asante Colin kugeuza mazoea ya maskini hana haki ya kupenda, nipende Colin nikupende, Colin unajua wewe ndiye mwanaume wangu wa mwanzo na wa mwisho. Nakupenda Colin zaidi ya kupenda.”
“Cecy najua thamani yako moyoni mwangu ni zaidi ya madini yote unayoyajua na usiyo yajua. Niliapa moyoni mwangu sitakupoteza mtetezi wa moyo wangu. Cecy mpenzi wewe ni zaidi ya mwanamke ni malaika wangu.”
“Asante mpenzi, ila hujanihakikishia utatumia simu?”
“Cecy nilitaka kuacha kutumia simu kwa ajili yako, lakini kwa vile umeniruhusu nitatumia.”
“Colin.”
“Naam.”
“Nina ombi moja naomba ukikubalie kwani toka nimefika hapa kuna kitu kimekuwa kikinisumbua jibu lako ni faraja ya moyo wangu.”
“Cecy malkia wangu, sema chochote nitakitekeleza.”
“Kuna kitu nimejifunza kwako kila unapotaka kufunga ndoa kuna tokea matatizo umeisha lingudua hilo?”
“Dah! Kweli kabisa mpenzi hilo jambo hutokea.”
“Sasa nitaka tufanye kitu tofauti katika safari yetu hii.”
“Kitu gani?”
“Tufunge ndoa kabisa hukuhuku tukurudi tuwe mke na mume.”
“Mmh! Lakini ndoa yenye baraka lazima wazazi wawepo.”
“Wazazi tutawaita huku tukirudi Tanzania tunafanya sherehe tu.”
“Sawa hakuna tatizo.”
Walikumbatiana kwa furaha walizima taa ya mwanga mkali na kuwasha ya mwanga hafifu kila mmoja aliyasikia mapigo ya moyo wa mwenzake.
***
Mage alionekana kuchanganyikiwa kutokana na taarifa za kupona kwa Cecy mwanamke aliyejua ni wa kufa siku yoyote. Kilichomchanganya zaidi ni kugeuka kwa mama Colin kusimama upande wa Cecy wakati mwanzo alimpa moyo wa kumpata mwanaye.
Akiwa bado hajajua atafanya nini alipata taarifa iliyomkata maini ya Colin kwenda Afrika ya Kusini na mchumba wake kwa ajili ya mapumziko ya muda mrefu. Lakini hakutaka kukata tamaa alianini njia ya kumpata Colin ni ni kumuua Cecy au kumtia kilema ambacho kitamfanya asiolewe na Colin.
Wazo la kuua aliliweka kando kwa muda kwa kuamini lile lingekuwa la mwisho kabisa baada ya mipango ya awali kuferi. Aliamini anaweza kutumia njia nyingi kuhakikisha Cecy aolewi na Colin. Mpango ulikuwa kumwagia tindi kali au kutuma vijana kubaka na picha zake kusambazwa kitu ambacho aliamini Colin na familia yake wasingekivumilia lazima angempiga chini Cecy.
Mpango wake alipanga kuupanga kabla ya Colin na mpenzi wake kurudi kutoka Afrika ya kusini. Alijua ndoa ingechukua muda ili kusubiri afya ya Cecy iimalike naye angetumia nafasi ile kumtia doa Cecy na yeye kuichukua nafasi aliyokuwa akiitafuta usiku na mchana kama wokovu baada ya mwenyewe kuichezea shilingi kwenye tundu la choo.
Aliapa kutumia kiasi chochote cha fedha kuhakikisha anampoteza Cecy na kulimiliki penzi la Colin. Walijipanga kutafuta watu ambao angewalipa kiasi cha pesa watakachokubaliana ili wamfanyie kazi yake kwa uhakika bila mtu yeyote kujua kitu.
Wakati akiwaza hayo taarifa ya kuitwa Afrika ya kusini iliwafikia wazazi wa Colin na Cecy kuwa wanatakiwa mara moja. Japokuwa hawakujua wanaitiwa nini, walikubaliana kuondoka kwenda kuwasikiliza watoto wao wana lipi. Baada ya siku nne Colin na Cecy waliwapokea uwanja wa ndege wa Port Elizabeth na kuwapeleka katika hoteli ya The Beach waliyofikia wao.
Wote walifarijika kukuta afya ya Cecy imeimalika haraka na nuru yake ya awali ikianza kuonekana kwa mbali. Ilikuwa furaha kwa familia kukutana wote wakiwa katika hali ya furaha. Usiku wa siku ile baada ya chakula walikaa pamoja kwa ajili ya mazungumzo.
Mzungumzaji mkuu alikuwa Cecy ambaye ndiye aliyemuomba Colin aseme yeye.
“Wazazi wetu najua mmeshtuka na wito wetu wa ghafla, lakini wito huu una maana kubwa katika maisha yetu watoto wenu. Wito huu ni kwa ajili ya kuja kusimamia harusi ya watoto wenu.”
“Watoto wetu kina nani?” mama Colin aliuliza.
“Ya mimi na mume wangu Colin ambayo tumepanga kuifunga wiki ijayo.”
“He! Mbona haraka sana kwa nini mnataka kufungia huku?” aliuliza mama Cecy.
“Mama kuna kitu kiliniijia haraka akilini mwangu ambacho nilikiamini kabisa na nilipomwambia mwenzangu ambaye alikubaliana na nilichokiona na kukubaliana kufunga ndoa huku.”
“Kitu gani?” mama Colin aliendelea kuuliza.
“Nilifuatilia hatua zote za harusi za mpenzi wangu ambazo huvurugika mwishoni, mfano wa kwanza muda mfupi kabla ya kumuoa Mage lilitokea tatizo lililomjeruhi moyo mpenzi wangu. Mfano wa pili muda mfupi kabla ya ndoa yetu likatokea la kutokea, hivyo imeonesha kuna tatizo.
“Nilichokiwaza mimi ni kuhusiana matukio yote hivyo naamini huku tutafunga ndoa isiyo na starehe ambayo itakuwa na baraka ya wazazi wa pande zote. Kwa hiyo wazazi wetu tunaomba mkubali ombi letu ili tukirudi Tanzani tuwe tayari mke na mume. Kuhusu sherehe tutaifanya tukijipanga.”
“Mmh! Colin we ulikuwa unasemaje?” mama Colin alimuuliza mwanaye.
“Mi namuunga mkono mpenzi wangu amekuwa na jicho la tatu ambalo wote tulikuwa hatuna.”

Je, harusi utafungwa?
 
SEHEMU: 31
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500

ILIPOISHIA:
“Nilichokiwaza mimi ni kuhusiana matukio yote hivyo naamini huku tutafunga ndoa isiyo na starehe ambayo itakuwa na baraka ya wazazi wa pande zote. Kwa hiyo wazazi wetu tunaomba mkubali ombi letu ili tukirudi Tanzani tuwe tayari mke na mume. Kuhusu sherehe tutaifanya tukijipanga.”
“Mmh! Colin we ulikuwa unasemaje?” mama Colin alimuuliza mwanaye.
“Mi namuunga mkono mpenzi wangu amekuwa na jicho la tatu ambalo wote tulikuwa hatuna.”
SASA ENDELEA...

“Mipango ya harusi mmeisha andikisha kanisani?”
“Tumeisha kamilisha kila kitu mlikuwa mkisubiliwa ninyi tu.”
“Basi hakuna tatizo kwa vile jambo ni la heri tutakuwa pamoja, sijui dada unasemaje?” mama Colin alimuuliza mama Cecy.
“Hata mimi naungana na wewe.”
Wazazi hawakuwa na pingamizi lolote walikubaliana kusimamia ndoa ya watoto wao ili wakirudi nyumbani Tanzania wajipange kwa sherehe.
***
Baada ya taratibu zote kufuatwa Colin na Cecy alifunga ndoa katika kanisa la Roman Cathotic la Mtakatifu Augustine jijini Port Elizabeth Afrika ya Kusini. Ndoa iliyokuwa na watu wachache lakini ilikuwa ni furaha isiyo kifani moyoni mwa Cecy pale alikupoulizwa kama anakubali kuwa mke halali wa Colin katika shida na raha pia Colin kukubali kuwa Cecy ni mkewe katika shida na raha na kifo ndicho kitakacho watenganisha.
Baada ya kufunga ndoa waliondoka na kurudi kwenye hoteli waliyofikia na jioni ya siku ile ilifanyika sherehe ndogo katika ufukwe wa hoteli ya The Beach na baadhi ya jamaa zao walikuwa katika mji wa Port Elizabeth.
Japo ilikuwa sherehe ndogo iliyoanzia ufukweni na kuishi kwenye ukumbi wa hoteli ile. Ilikuwa sherehe yenye kufana kila aliyekuwepo alifurahia sherehe ile ambayo watu walikunywa na kusaza. Baada ya shehere maharusi waliingia ndani ya chumba cha VIP ambacho walikichukua mahususi kwa ajili ya fungate.
Siku ya tatu mama Colin na Cecy walirudi Tanzania na kuwaacha watoto wao wakila fungate. Wakiwa ndani ya ndege kila mtu alimshukuru Mungu kwa kutenda ambalo lililoonekana kwa akili ya kibinadamu limeshindikana.
“Yaani unajua dada mpaka muda huu siamini kama nimeweza kuiona harusi ya Cecy na Colin,” alisema mama Cecy.
“Si wewe yaani mpaka sasa naamini Mungu akiamua kitenda hutenda jambo.”
“Kwangu naona kama muujiza siamini... siamini kama kuna siku nitamuona mwanangu akitabasamu lazima nimshukuru Mungu asante Mungu kwa kila unitendealo.”
“Kweli naamini Colin na Cecy wanapendana mapenzi ya dhati.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Mwanzo niliamini labda Cecy anampenda mwanangu kwa ajili ya utajiri wake lakini alinionesha hamuhitaji kwa ajili ya mali zake bali mapenzi ya dhati, Pia Colin alinihakikishia hataoa mwanamke mwingine zaidi ya Cecy na alikuwa radhi kuioa maiti na Cecy kama angekufa.”
“Ni jambo la kushukuru watoto wetu kupendana ni mwanzo wa kutengeneza familia yenye upendo.”
Wazazi wakiwa wanabadilisha mawazo ndani ya ndege jijini Port Elizabeth ndani ya chumba cha VIP katika hoteli ya The Beach, Cecy alikuwa akimuangalia Colin kwa muda mrefu na kuanza kutokwa na machozi kitu kilichomshtua Colin na kuhoji.
“Vipi mpenzi wangu mbona unalia?”
Cecy hakujibu machozi yaliendelea kumtoka kama maji na kuzidi kumweka mumewe kwenye wakati mgumu.
“Mke wangu kuna nini tena? Leo ni siku ya furaha baada ya kufika nusu ya safari yetu kutokana na mitihani mingi. Badala ya kufurahi mke wangu unalia, kipi kimekusibu mpenzi wangu au kama kuna nilichokukosea nipo radhi kwa adhabu yoyote,” Colin alisema huku akisogeza mbele ya Cecy kumpigia magoti.
Kabla hajapiga magoti Cecy alikurupuka alipokuwa amekaa na kumuwahi mpenzi na kumvamia na kuwafanya wote waanguke mweleka.
“Colin machozi haya si maumivu bali furaha iliyopitiza nashindwa... nashindwa mume kuvumilia. Siamini kama ndoto niliyoota mchana imekuwa kweli, leo hii mimi ni mke wa Colin, asante Mungu asante kwa kila jambo sitaacha kukushukuru usiku na mchana siku zote za pumzi zangu.”
“Cecy mpenzi wangu nilikupenda toka siku ya kwanza nilipokuona lakini nilikuta chaguo lingine la mama yangu. Lakini amini uliingia moyoni mwangu toka siku ya kwanza jicho langu lilipokuona. Naamini kabisa jicho la mwanzo lilikuwa sahihi kuliko mtu niliyechaguliwa.
“Umekuwa kiumbe wa ajabu ambaye siwezi kumfananisha na kiumbe wa kawaida, umewaze kunipigania japo katika hali yako ya umaskini, lakini ulikuwa radhi ukose kitu chochote chini ya jua ili unipate mimi. Nakuahidi lile jicho lililokuona mara ya kwanza na kukufungulia mlango moyoni mwangu ndilo hilohilo linalokuona ua zuri lililochanua mbele yangu.
“Wewe ni mwanamke niliyepewa zawadi na Mungu, nimeamini bundi hawezi kukaa kundi moja na njiwa.”
“Una maanisha nini?”
“Mage hakuwa njiwa katika safari ya maisha yangu, naamini mbeleni lazima angenitenda, Mungu alilijua hilo ndiyo maana alikuleta wewe wakili wa moyo wangu bila wewe nina wasiwasi ningekuwa nimeisha kufa kwa vile aliuhukumu moyo wangu kifo, lakini umeweza kuutoa moyo wangu kwenye adhabu nzito niliyopewa na Mage sijui usingekuwepo ingekuwaje?”
“Colin niliyafuatilia maisha yako kila hatua ni moyo wa upendo ulinisukuma, niliamini kabisa wewe ndiye mume wangu. Nilikupenda sitachoka kukupenda kwa vile kila siku unakuwa kiumbe kipya moyoni mwangu.”
“Hata mimi mke wangu.”
Walikumbatiana kwa furaha kuifurahi fungate yao iliyokuwa na raha ya aina yake baada ya safari ndefu yenye misukosuko.
****
Nchini Tanzani taarifa za mama Colin kwenda afrika ya kusini zilimshtua sana Mage, alijikuta akiwaza huenda Cecy amezidiwa na hivyo amekwenda kuangalia hali yake inavyoendelea. Aliomba kama ni hivyo basi akute Cecy amediziwa na kufariki dunia, lakini bado alibakia na akiba ya mpango wake wa kumfanyia kitu kibaya Cecy kama atakuwa hai ili kuhakikisha ndoa haifungwi.
Aliwaandaa watu kwa ajili ya kufanya utekaji na kumfanyia vitendo vichafu, walikubalia kuifanya kazi baada ya Cecy kurudi nchini kutoka Afrika ya kusini. Vijana walimuahidi kumfanyia kazi vizuri kwa vile walikuwa na uzoefu wa kazi zile. Aliwahidi kuwaongeza mara mbili ya malipo waliyokubaliana kama watafanikisha kazi ile.
“Sister mbona utakubali kazi yetu, hata ungetaka kichwa chake tungekuletea,” alijisifia wakora.
“Sasa damu yenye virusi tutaipata wapi?”
“Hilo dogo mbona kuna mshkaji wetu mmoja ameumia tutachukua damu yake kidogo na kumdunga mtu wako.”
“Nawaamini msiniangushe.”
“Hatujawahi kuharibu kazi hata siku moja, hata kama kuna kazi nyingine we tupe tukufanyie tena tutakupunguzia kwa vile wewe mtu wetu.”
“Picha nimewapa?”
“Ndiyo sister, tumemcheki vizuri mbona huyu amekwisha.”
Baada ya mipango yake kwenda sawa Mage alijipanga kuhakikisha Colin hamuoi Cecy, alipanga baada ya tukio hilo la kumteka Cecy na kumduga damu yenye virusi atumie laini mpya ya simu na kumtumia picha za Cecy akibakwa na ujumbe kuwa ameathirika.
Baada kuwaza yote yale alitabasamu na kuamini kila kitu kipo vizuri anachosubiri utekelezaji tu. Akiwa amejipumzisha alipata taarifa toka kwa mama yake kuwa mama Colin amerudi toka Afrika ya kusini.
“He! Mbona hajakaa sana, karudi na Colin?”
“Hapana karudi peke yake.”
“Mbona karudi peke yake kwani alikwenda kufanya nini?”
“Kwa kweli sikumuuza.”
Mage hakutaka kuuliza swali lingine alinyanyuka na kutoka kuelekea kwa mama Colin kutaka kujua sababu ya safari yake ya Afrika ya kusini na kwa sababu gani hakurudi na Colin. Alitoka hadi kwenye gari na kuchukua aina ya Toyota Harrie na kuelekea kwa mama Colin, aliendesha kwa kasi ili kuwahi kupata taarifa.
Alipofika alipaki gari kwenye maegesho, kwa shauku ya kuyajua ya Afrika ya kusini hakufunga hata mlango wa gari. Alitembea mwendo wa haraka hadi mlangoni wa kuiingia ndani. Alibisha hodi na kukaribishwa na mama Colin aliyekuwa amekaa na mama Cecy wakiangalia mkanda wa video huku wakinywa vinywaji.
“Karibu ma mkwe,” mama Colin alisema.
“A..a..sa..”
Alishindwa kumalizia sentesi ambayo ilikatikia njiani baada ya jicho lake kutua kwenye kioo cha runinga alichokiona mbele yake. Ilikuwa vigumu kuamini kama ni kweli au alikuwa akiangalia ni maigizo. Alimuona Cecy katika vazi la harusi akiwa na Colin katika suti ya gharama, alikaza macho kama yanataka kudondoka.
“Maa..a..ma.”
“Vipi mkwe?”
“Huyu si Colin?” alisema huku akinyoosha kidole.
“Ndiyo.”
“Na..na..huyu si Cecy?”
“Ndiyo.”
“Hii si..si..harusi?”
“Ndiyo.”
“Wameoana lini?”
“Leo ni siku ya nne toka waoane na sisi tumerudi jana usiku kutoka huko.”
“Mmh! Si kweli, haya ni maigizo tu ili kuniumiza roho.”
“Kukuimiza roho ili iweje? Na picha zao hizi hapa.”
Mage alizichukua albam akiwa haamini anachoambiwa, aliifungua na kuanza kuangalia picha mojamoja huku mapigo ya moyo yakimwenda mbio. Kila ukurasa alioufunua uliupasua moyo wake alijikuta machozi yamefunika macho na kushindwa kuona picha.
Alihisi mapigo ya moyo yakiongeza kasi pumzi zikamjaa na kutoka kwa shida, kiza kizito kilitanda mbele yake kilichoendelea hakukijua. Mage alianguka kama mzigo akiwa amepoteza fahamu, kitendo kile kiliwashtua sana. Walijikuta wakitaharuki ilibidi wamchukue na kumkimbiza hospitali kisha kumjulisha mama yake.

ITAENDELEA
 
HADITHI: WAKILI WA MOYO
SEHEMU: MWISHO
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500

ILIP{OISHIA:
Alihisi mapigo ya moyo yakiongeza kasi pumzi zikamjaa na kutoka kwa shida, kiza kizito kilitanda mbele yake kilichoendelea hakukijua. Mage alianguka kama mzigo akiwa amepoteza fahamu, kitendo kile kiliwashtua sana. Walijikuta wakitaharuki ilibidi wamchukue na kumkimbiza hospitali kisha kumjulisha mama yake.
SASA ENDELEA...

Mama Colin alijua kilichokuwa kikiendelea aliamini Mage alipatwa na mshtuko baada ya kuona Colin amemuoa Cecy. Mama yake alifika mara moja hospitali na kukuta tayari mwanaye kaingizwa kwenye chumba cha wagonjwa mahututi. Baada ya vipimo ilionesha alipatwa na mshtuko na kusababisha mishipa ya damu kupasuka na kusababisha apooze upande mmoja.
Kwa vile huduma ile haikuwepo alitakiwa kupelekwa Afrika ya kusini haraka kwani walisema ugonjwa ule ikiwa kupata matibabu ya haraka anaweza kupona. Siku ya pili alipelekwa Afrika ya kusini kwa ajili ya matibabu ya haraka katika hospitali ya Mil park.
***
Mage alisafiri na mama yake mpaka Afrika ya kusini katika hospitali ya Milpark iliyopo katika jiji la Johannesburg. Alipokelewa na kuanzishiwa matibabu mara moja, madaktari walifanikiwa kufanya upasuaji uliochukua saa tatu kuondoa damu zilizovuja baada ya mshipa kupasuka.
Baada ya upasuaji kwenda vizuri alirudishwa kwenye chumba maalumu chini ya uangalizi ya madaktari bingwa. Taarifa za Mage kuumwa zilimfikia Colin aliyekuwa katika mji wa Port Elizabeth.
“Mpenzi nasikia Mage anaumwa ameletwa hospitali ya Milpark, Johannesburg,” Colin alimwambia Cecy aliyekuwa akicheza game kwenye Ipad.
“Maskini mke mwenzangu nini kimemsibu?”
“Nasikia kapata mshtuko baada ya kuona video na picha zetu za harusi.”
“Maskini, Mage alikuwa kama fisi aliyeamini siku moja mwanadamu atadondosha mkono.”
“Namshangaa kutaka kufa wakati anajua mimi ni wa nani.”
“Wa Cecy.”
“Najiuliza bila Cecy, Colin leo ningekuwa wapi?”
“Anajua Mungu si sisi wanadamu ambao hupokea matokeo.”
“Asante mpenzi wangu kwa kuyaokoa maisha yangu, huwezi kuamini baada ya kuachwa ghafla na Mage nilijaa mawazo mengi na kujiona nina mapungufu.”
“Asante niseme mimi uliyoyapa majibu mswali yangu kama kuna siku maji yatapanda mlima.”
“Nina imani huu ni muda muafaka wa ku-renew mkataba wako na makapuni yote ya mavazi ya majarida. Waliniuliza afya yako nikawaambia hujambo kabisa hivyo wameomba tupange siku ya wao kuja ili uendelee na kazi yako.”
“Mpenzi moyoni mwangu nimepanga kwanza nikae na mume wangu kwa mwaka mzima ndipo nifanye kazi nyingine.”
“Cecy si tumeishafinga ndoa wasiwasi wako nini?”
“Sijaifaidi raha ya ndoa kazi ipo tu, kama wameweza kunisubiri muda wote waendelee kusubiri.”
“Makubaliano ya awali ni kwamba tutakuwa tupo pamoja katika kazi zako zote kwa vile mimi ndiye meneja wako.”
“Mmh! Kama hivyo sawa.”
“Mmh! Bado tu una wasiwasi wa kuibiwa?” Colin alimtania.
“Si umesikia mtu kataka kufa baada ya kusikia umeoa, vipi niwe mbali nawe? Nikisikia upo na Mage ningekufa mimi.”
***
Baada ya kuwajulisha siku ya kuonana kampuni ya Ebony walifika katika hoteli ya The Beach na kuingia mkataba mpya wa miaka miwili. Pia kampuni ya maonesho ya mavazi na urembo nayo iliingia mkataba mpya na makubaliano ya kuanza kazi baada ya miezi mitatu.
Mage naye alitoka hospitali akiwa na afya njema, mama yake alipotaka kujua sababu ya mshtuko ule, alimweleza ukweli kuwa baada ya kuona harusi ya Colin na Cecy alipata mshtuko wa ajabu kilichoendelea hakujua mpaka alipozindukia Hospitali Muhimbili akiwa amepooza upande mmoja.
“Unasema nani kaoa? Sijakuelewa vizuri,” mama Mage alishtuka kusikia Colin kaoa.
“Colin, mama.”
“Muongo! Hiyo harusi imefanyika lini mbona sina habari?”
“Ilikuwa ya siri imefanyikiwa Afrika ya kusini.”
“Kama ni kweli basi mwanangu achana na mawazo ya Colin, Mungu atakupa mume wa kweli.”
“Mama hata mimi nimejifirikia hivyo lakini Colin nilimpenda sana.”
“Si kweli, ulimpenda Hans, Colin anapendwa na Cecy kwa hiyo waache na ndoa yao.”
“Ndiyo mama, japo nilikuwa na nia mbaya kwa Cecy, lakini kuanzia sasa sitashughulika na Colin wala Cecy nami nasubiri ndoa yangu.”
“Hilo ndilo neno la kujasiri mwanangu.”
Baada ya Cecy kumaliza mapumziko alianza kazi rasmi, mwaka mmoja baadaye alishika ujauzito na kusubiri muda wa kujifungua. Mage naye alipata mchumba na mambo yalikwenda kama yalivyopangwa. Siku ya harusi akiwa anajiandaa kwenda kanisani anapata habari zilizo mshtua moyo na kufanya apoteze fahamu kuwa mpenzi wake Hans yupo huru baada ya kushinda rufaa yake.
MWISHO
 
HADITHI: WAKILI WA MOYO
SEHEMU: MWISHO
MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
SIMU: 0713 646500

ILIP{OISHIA:
Alihisi mapigo ya moyo yakiongeza kasi pumzi zikamjaa na kutoka kwa shida, kiza kizito kilitanda mbele yake kilichoendelea hakukijua. Mage alianguka kama mzigo akiwa amepoteza fahamu, kitendo kile kiliwashtua sana. Walijikuta wakitaharuki ilibidi wamchukue na kumkimbiza hospitali kisha kumjulisha mama yake.
SASA ENDELEA...

Mama Colin alijua kilichokuwa kikiendelea aliamini Mage alipatwa na mshtuko baada ya kuona Colin amemuoa Cecy. Mama yake alifika mara moja hospitali na kukuta tayari mwanaye kaingizwa kwenye chumba cha wagonjwa mahututi. Baada ya vipimo ilionesha alipatwa na mshtuko na kusababisha mishipa ya damu kupasuka na kusababisha apooze upande mmoja.
Kwa vile huduma ile haikuwepo alitakiwa kupelekwa Afrika ya kusini haraka kwani walisema ugonjwa ule ikiwa kupata matibabu ya haraka anaweza kupona. Siku ya pili alipelekwa Afrika ya kusini kwa ajili ya matibabu ya haraka katika hospitali ya Mil park.
***
Mage alisafiri na mama yake mpaka Afrika ya kusini katika hospitali ya Milpark iliyopo katika jiji la Johannesburg. Alipokelewa na kuanzishiwa matibabu mara moja, madaktari walifanikiwa kufanya upasuaji uliochukua saa tatu kuondoa damu zilizovuja baada ya mshipa kupasuka.
Baada ya upasuaji kwenda vizuri alirudishwa kwenye chumba maalumu chini ya uangalizi ya madaktari bingwa. Taarifa za Mage kuumwa zilimfikia Colin aliyekuwa katika mji wa Port Elizabeth.
“Mpenzi nasikia Mage anaumwa ameletwa hospitali ya Milpark, Johannesburg,” Colin alimwambia Cecy aliyekuwa akicheza game kwenye Ipad.
“Maskini mke mwenzangu nini kimemsibu?”
“Nasikia kapata mshtuko baada ya kuona video na picha zetu za harusi.”
“Maskini, Mage alikuwa kama fisi aliyeamini siku moja mwanadamu atadondosha mkono.”
“Namshangaa kutaka kufa wakati anajua mimi ni wa nani.”
“Wa Cecy.”
“Najiuliza bila Cecy, Colin leo ningekuwa wapi?”
“Anajua Mungu si sisi wanadamu ambao hupokea matokeo.”
“Asante mpenzi wangu kwa kuyaokoa maisha yangu, huwezi kuamini baada ya kuachwa ghafla na Mage nilijaa mawazo mengi na kujiona nina mapungufu.”
“Asante niseme mimi uliyoyapa majibu mswali yangu kama kuna siku maji yatapanda mlima.”
“Nina imani huu ni muda muafaka wa ku-renew mkataba wako na makapuni yote ya mavazi ya majarida. Waliniuliza afya yako nikawaambia hujambo kabisa hivyo wameomba tupange siku ya wao kuja ili uendelee na kazi yako.”
“Mpenzi moyoni mwangu nimepanga kwanza nikae na mume wangu kwa mwaka mzima ndipo nifanye kazi nyingine.”
“Cecy si tumeishafinga ndoa wasiwasi wako nini?”
“Sijaifaidi raha ya ndoa kazi ipo tu, kama wameweza kunisubiri muda wote waendelee kusubiri.”
“Makubaliano ya awali ni kwamba tutakuwa tupo pamoja katika kazi zako zote kwa vile mimi ndiye meneja wako.”
“Mmh! Kama hivyo sawa.”
“Mmh! Bado tu una wasiwasi wa kuibiwa?” Colin alimtania.
“Si umesikia mtu kataka kufa baada ya kusikia umeoa, vipi niwe mbali nawe? Nikisikia upo na Mage ningekufa mimi.”
***
Baada ya kuwajulisha siku ya kuonana kampuni ya Ebony walifika katika hoteli ya The Beach na kuingia mkataba mpya wa miaka miwili. Pia kampuni ya maonesho ya mavazi na urembo nayo iliingia mkataba mpya na makubaliano ya kuanza kazi baada ya miezi mitatu.
Mage naye alitoka hospitali akiwa na afya njema, mama yake alipotaka kujua sababu ya mshtuko ule, alimweleza ukweli kuwa baada ya kuona harusi ya Colin na Cecy alipata mshtuko wa ajabu kilichoendelea hakujua mpaka alipozindukia Hospitali Muhimbili akiwa amepooza upande mmoja.
“Unasema nani kaoa? Sijakuelewa vizuri,” mama Mage alishtuka kusikia Colin kaoa.
“Colin, mama.”
“Muongo! Hiyo harusi imefanyika lini mbona sina habari?”
“Ilikuwa ya siri imefanyikiwa Afrika ya kusini.”
“Kama ni kweli basi mwanangu achana na mawazo ya Colin, Mungu atakupa mume wa kweli.”
“Mama hata mimi nimejifirikia hivyo lakini Colin nilimpenda sana.”
“Si kweli, ulimpenda Hans, Colin anapendwa na Cecy kwa hiyo waache na ndoa yao.”
“Ndiyo mama, japo nilikuwa na nia mbaya kwa Cecy, lakini kuanzia sasa sitashughulika na Colin wala Cecy nami nasubiri ndoa yangu.”
“Hilo ndilo neno la kujasiri mwanangu.”
Baada ya Cecy kumaliza mapumziko alianza kazi rasmi, mwaka mmoja baadaye alishika ujauzito na kusubiri muda wa kujifungua. Mage naye alipata mchumba na mambo yalikwenda kama yalivyopangwa. Siku ya harusi akiwa anajiandaa kwenda kanisani anapata habari zilizo mshtua moyo na kufanya apoteze fahamu kuwa mpenzi wake Hans yupo huru baada ya kushinda rufaa yake.
MWISHO

Safi sana...

Mage ni sikio la kufa halisiki dawa, na ni mfa maji... mataka vingi vyote vimeponyoka, sasa Hans kaachiwa sijui ataghairi kuolewa...

Kila anayekua nae lazima amsababishie matatizo...

Hongera kwa Cecy na collins...


Chapter Closed...


Cc: mahondaw
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom