Lycaon pictus
JF-Expert Member
- Jan 31, 2021
- 7,067
- 12,439
JANGA
Eeh uliye kwenye mawingu, uliye mkubwa kuliko wote, tunaomba utusalimu kwa mwanga wako ili tujue iwapo u-hai. Eeeh Ingatambo mungu wa nchi yetu, tusaidie. Hiyo ilikuwa ni sala iliyotoka kwa mtindo wa kilio ikitolewa na wakazi wa Serengeti wakiongozwa na waganga wao na machifu.
Ni karibia mwaka wa tatu tangu mvua inyeshe kwa mara ya mwisho kwenye tambarare za Serengeti. Nchi yote ilikuwa imegeuka rangi na kuwa ya kaki kwa ukame. Vumbi lilikuwa limetimka na kujaa angani hadi kuna wakati ilikuwa ni vigumu kuonana. Sehemu nyingine vumbi lilikuwa jeupe kama unga na sehemu nyingine lilikuwa jekundu kama damu. Kuna sehemu nyingine inasemekana vumbi lilikuwa na kina kirefu hadi liliwafika twiga magotini! Kulikuwa hakuna majani hata kwenye mti mmoja.
Hali ilikuwa mbaya hadi miti iliyokuwa kando ya mito na mabwawa ilikuwa imepukutisha majani. Miti yote ilikuwa imebaki na matawi ya juu tu na haikuwa na magome. Baada ya wanyama kula nyasi zote, wakaanza kula majani ya miti na kisha wakaanza kula magome. Urefu na uzoefu wa twiga wa kula majani ya miti haukuwasaidia kitu. Kwanza miti karibu yote ilipukutisha majani na ile iliyobaki na majani iligombaniwa na wanyama wa kila aina. Wanyama walibuni mbinu mbalimbali za kujipatia chakula kutoka kwenye miti. Ilikuwa kitu cha kawaida kukuta wanyama wa aina tofautitofauti, wakubwa kwa wadogo wakishirikiana kuangusha mikwaju, mipogoro na miti mingine mikubwa. Tembo walikuwa wakibandua magome ya mibuyu na kufyonza maji yake. Kila mnyama alibuni mbinu za kujipatia chakula na maji.
Watoto waliozaliwa hawakuwa wakijua chochote kuhusu nyasi. Wengi walijenga picha kuwa nyasi ni nyekundu, nyeupe au kaki, kulingana na rangi ya vumbi kwenye eneo lao. Wengine walifikiri nyasi ni mipogoro midogomidogo, milaini, isiyo na miiba. Wanyama wakubwa nao walikuwa wanajiuliza, iwapo mvua ikija tena, je, nyasi zinaweza kuota kutoka kwenye lile vumbi? walijiuliza iwapo kwenye lile vumbi laini kama unga bado kuna mbegu.
Kwenye mwaka wa kwanza wa ukame, nchi ilikuwa imejaa miiba mitupu. Hii ni sababu miti mingi ya miiba ilikuwa imeangushwa na kutawanywa huku na kule. Ilikuwa kitu cha kawaida kukuta wanyama wakubwa kwa wadogo wakichechemea. Kuna hadithi kuwa hadi nyoka waliacha kutambaa sababu ya miiba! Baada ya mwaka na nusu, miiba hiyo ilikuwa imepigwa na jua kiasi kwamba hata ikikanyagwa inageuka kuwa unga. Wanyama wengi walikuwa wanaugua magonjwa ya upumuaji na macho, ilisadikika ni sababu ya vumbi lenye sumu iliyotoka kwenye miiba iliyosagika.
Kipindi hicho, si tu kwamba mvua haikunyesha, bali hata jua lilionekana kama limeongezwa ukali kuliko kawaida. Pamoja na kuwa kabla ya ukame mvua nyingi sana ilikuwa imenyesha lakini madimbwi, hata yale yanayotegemewa kipindi cha kiangazi yalikauka miezi michache baada ya mvua kuisha. Mito na madimbwi vilikauka kwa kasi ya ajabu. Kulikuwa na upungufu wa maji kila kona. Mwanzoni wanyama walikusanyika kando ya mito na vidimbwi lakini vilikauka baada ya muda mfupi, walianza kuchimbachimba kwenye matope na mchanga hadi kulipokuwa hakuna maji tena. Kutoka hapo wakahamia kwenye magome ya miti, miti yote yenye maji kama mibuyu ililiwa magome yote na kubaki myeupe pee.
Samaki, mamba na viboko walikuwa na hali ngumu zaidi. Samaki walikuwa wanakufa kwa mamia, ndiyo walikuwa wanyama wa kwanzakwanza kufa kwa wingi. Kuna dimbwi moja baada ya samaki kufa sana kutokana na upungufu wa maji na kubaki tope, mamba na viboko wakakaa kikao. Mkuu wa mamba kwenye eneo lile bwana Kinyang akaanza kwa kusema.
"Ndugu zangu, nimewaita hapa tujadili mustakabali wa uhai wetu. Baada ya kujadiliana na kiongozi wa viboko bwana Sapuki, tumefikia muafaka kwamba makao ni muhimu kama tu chakula na maji vilivyo muhimu. Mnyama anaweza kufa kwa kukosa makao kama tu anavyoweza kufa kwa kukosa chakula au maji. Tena inawezekana makao ni muhimu zaidi. Tuchukulie mfano Simba, makao yao ni nchi kavu, je nchi yote hii tukijaza maji, wanaweza ishi kwa muda gani? Sisi makazi yetu ni kwenye maji, hatuwezi ishi muda mrefu bila maji, ili tuwinde tunahitaji maji ya kutuficha, au nyie mmewahi kuona mamba anazunguka zunguka nyikani mchana akikimbiza swala na nyumbu na usiku analala chini ya mbuyu? Kwa jua hili kali, viboko wanaweza kuishi kwa muda gani bila maji? Samaki wanaweza kupumua bila maji? Makazi yetu ni kwenye maji na uhai wetu unategemea maji."
"Ndugu zetu samaki wamekufa kwa mamia sababu hawawezi pumua bila maji, walau sisi tunaweza. Kwa kweli ndugu zetu wamekufa vibaya sana, ni kama kifo cha kukabwa koo la hewa." Akasema Kinyang kwa sauti ya kusikitika huku machozi yakimlengalenga, kisha akaendelea. "Sasa tumefikia muafaka kuwa, dimbwi hili ni muhimu kwa uhai wetu, hivyo hatutamruhusu mnyama, ndege au mdudu yeyote kunywa maji kwenye hili dimbwi. Ingatambo shahidi yetu. "Ni kweli kabisa, na iwe hivyo" ilisikika sauti kubwa ya viboko na mamba. Mamba mmoja kwa jina Ol kinos akanyoosha mkono na kuuliza; "sasa kama tutawakataza kuja kunywa maji, sisi mamba tutapata wapi chakula?" ''tutakula wakaidi," akajibu Kinyang kwa ufupi. Kuanzia siku hiyo, walimfukuza kiumbe yeyote aliyekuja kunywa maji dimbwini, iwe mchana au usiku.
Eeh uliye kwenye mawingu, uliye mkubwa kuliko wote, tunaomba utusalimu kwa mwanga wako ili tujue iwapo u-hai. Eeeh Ingatambo mungu wa nchi yetu, tusaidie. Hiyo ilikuwa ni sala iliyotoka kwa mtindo wa kilio ikitolewa na wakazi wa Serengeti wakiongozwa na waganga wao na machifu.
Ni karibia mwaka wa tatu tangu mvua inyeshe kwa mara ya mwisho kwenye tambarare za Serengeti. Nchi yote ilikuwa imegeuka rangi na kuwa ya kaki kwa ukame. Vumbi lilikuwa limetimka na kujaa angani hadi kuna wakati ilikuwa ni vigumu kuonana. Sehemu nyingine vumbi lilikuwa jeupe kama unga na sehemu nyingine lilikuwa jekundu kama damu. Kuna sehemu nyingine inasemekana vumbi lilikuwa na kina kirefu hadi liliwafika twiga magotini! Kulikuwa hakuna majani hata kwenye mti mmoja.
Hali ilikuwa mbaya hadi miti iliyokuwa kando ya mito na mabwawa ilikuwa imepukutisha majani. Miti yote ilikuwa imebaki na matawi ya juu tu na haikuwa na magome. Baada ya wanyama kula nyasi zote, wakaanza kula majani ya miti na kisha wakaanza kula magome. Urefu na uzoefu wa twiga wa kula majani ya miti haukuwasaidia kitu. Kwanza miti karibu yote ilipukutisha majani na ile iliyobaki na majani iligombaniwa na wanyama wa kila aina. Wanyama walibuni mbinu mbalimbali za kujipatia chakula kutoka kwenye miti. Ilikuwa kitu cha kawaida kukuta wanyama wa aina tofautitofauti, wakubwa kwa wadogo wakishirikiana kuangusha mikwaju, mipogoro na miti mingine mikubwa. Tembo walikuwa wakibandua magome ya mibuyu na kufyonza maji yake. Kila mnyama alibuni mbinu za kujipatia chakula na maji.
Watoto waliozaliwa hawakuwa wakijua chochote kuhusu nyasi. Wengi walijenga picha kuwa nyasi ni nyekundu, nyeupe au kaki, kulingana na rangi ya vumbi kwenye eneo lao. Wengine walifikiri nyasi ni mipogoro midogomidogo, milaini, isiyo na miiba. Wanyama wakubwa nao walikuwa wanajiuliza, iwapo mvua ikija tena, je, nyasi zinaweza kuota kutoka kwenye lile vumbi? walijiuliza iwapo kwenye lile vumbi laini kama unga bado kuna mbegu.
Kwenye mwaka wa kwanza wa ukame, nchi ilikuwa imejaa miiba mitupu. Hii ni sababu miti mingi ya miiba ilikuwa imeangushwa na kutawanywa huku na kule. Ilikuwa kitu cha kawaida kukuta wanyama wakubwa kwa wadogo wakichechemea. Kuna hadithi kuwa hadi nyoka waliacha kutambaa sababu ya miiba! Baada ya mwaka na nusu, miiba hiyo ilikuwa imepigwa na jua kiasi kwamba hata ikikanyagwa inageuka kuwa unga. Wanyama wengi walikuwa wanaugua magonjwa ya upumuaji na macho, ilisadikika ni sababu ya vumbi lenye sumu iliyotoka kwenye miiba iliyosagika.
Kipindi hicho, si tu kwamba mvua haikunyesha, bali hata jua lilionekana kama limeongezwa ukali kuliko kawaida. Pamoja na kuwa kabla ya ukame mvua nyingi sana ilikuwa imenyesha lakini madimbwi, hata yale yanayotegemewa kipindi cha kiangazi yalikauka miezi michache baada ya mvua kuisha. Mito na madimbwi vilikauka kwa kasi ya ajabu. Kulikuwa na upungufu wa maji kila kona. Mwanzoni wanyama walikusanyika kando ya mito na vidimbwi lakini vilikauka baada ya muda mfupi, walianza kuchimbachimba kwenye matope na mchanga hadi kulipokuwa hakuna maji tena. Kutoka hapo wakahamia kwenye magome ya miti, miti yote yenye maji kama mibuyu ililiwa magome yote na kubaki myeupe pee.
Samaki, mamba na viboko walikuwa na hali ngumu zaidi. Samaki walikuwa wanakufa kwa mamia, ndiyo walikuwa wanyama wa kwanzakwanza kufa kwa wingi. Kuna dimbwi moja baada ya samaki kufa sana kutokana na upungufu wa maji na kubaki tope, mamba na viboko wakakaa kikao. Mkuu wa mamba kwenye eneo lile bwana Kinyang akaanza kwa kusema.
"Ndugu zangu, nimewaita hapa tujadili mustakabali wa uhai wetu. Baada ya kujadiliana na kiongozi wa viboko bwana Sapuki, tumefikia muafaka kwamba makao ni muhimu kama tu chakula na maji vilivyo muhimu. Mnyama anaweza kufa kwa kukosa makao kama tu anavyoweza kufa kwa kukosa chakula au maji. Tena inawezekana makao ni muhimu zaidi. Tuchukulie mfano Simba, makao yao ni nchi kavu, je nchi yote hii tukijaza maji, wanaweza ishi kwa muda gani? Sisi makazi yetu ni kwenye maji, hatuwezi ishi muda mrefu bila maji, ili tuwinde tunahitaji maji ya kutuficha, au nyie mmewahi kuona mamba anazunguka zunguka nyikani mchana akikimbiza swala na nyumbu na usiku analala chini ya mbuyu? Kwa jua hili kali, viboko wanaweza kuishi kwa muda gani bila maji? Samaki wanaweza kupumua bila maji? Makazi yetu ni kwenye maji na uhai wetu unategemea maji."
"Ndugu zetu samaki wamekufa kwa mamia sababu hawawezi pumua bila maji, walau sisi tunaweza. Kwa kweli ndugu zetu wamekufa vibaya sana, ni kama kifo cha kukabwa koo la hewa." Akasema Kinyang kwa sauti ya kusikitika huku machozi yakimlengalenga, kisha akaendelea. "Sasa tumefikia muafaka kuwa, dimbwi hili ni muhimu kwa uhai wetu, hivyo hatutamruhusu mnyama, ndege au mdudu yeyote kunywa maji kwenye hili dimbwi. Ingatambo shahidi yetu. "Ni kweli kabisa, na iwe hivyo" ilisikika sauti kubwa ya viboko na mamba. Mamba mmoja kwa jina Ol kinos akanyoosha mkono na kuuliza; "sasa kama tutawakataza kuja kunywa maji, sisi mamba tutapata wapi chakula?" ''tutakula wakaidi," akajibu Kinyang kwa ufupi. Kuanzia siku hiyo, walimfukuza kiumbe yeyote aliyekuja kunywa maji dimbwini, iwe mchana au usiku.