BRUNO THA FISHERMAN
Mtunzi.Nyemo
Episode 10
Mzee Todd alikuwa ndani ya ndege akipelekwa nchini Marekani. Taarifa za kukamatwa kwake zilikuwa ni za kimyakimya na hakutakiwa mtu yeyote afahamu kama mwanaume huyo alikuwa amekamatwa kwa kuogopa kuvamiwa na wauzaji wa madawa ya kulevya.
Humo ndani ya ndege, hakuwa na raha hata kidogo, alijua kwamba kila kitu kilichokuwa kimefanyika kilikuwa ni mchezo ambao ulichezwa na Maxwell kwa ajili ya kumpoteza.
Hakuona kama angeweza kutoka katika kesi hiyo kubwa. Mbele yake kulikuwa na ugumu lakini watu pekee ambao aliamini kwamba wangeweza kumsaidia kutoa ushahidi walikuwa wawili tu, Innocent na Bruno.
Alikuwa akisafirishwa kuelekea nchini Marekani huku matumaini yake yakiwa kwa watu hao wawili tu. Hakuzungumza kitu chochote kile, alikuwa kimya na kichwa chake kilikuwa kikifikiria ni kwa jinsi gani angeweza kupambana na kesi hiyo ambayo dunia nzima iliamini kwamba kweli madawa ya kulevya yalikutwa chumbani kwake na kulikuwa na uwezekano mkubwa kwamba alihusika katika kuiteketeza familia yake.
Baada ya saa zaidi ya ishirini, hatimaye ndege ikaingia nchini Marekani. Hapo, alikuwa akisubiriwa na maofisa wa CIA ambao walimchukua, wakampakiza ndani ya gari na kuondoka naye.
Walipoona kwamba amefika salama ndiyo taarifa zikaanza kutolewa kwa waandishi wa habari ambao wote hawakuamini kile walichokuwa wamekisikia.
Mwanaume huyo aliwasumbua kwa miezi sita, hawakuwa wamempata japokuwa walimtafuta kila kona, kukamatwa kwake ikawa shangwe, watu kwenye mitandao ya kijamii wakaandika sana kuhusu mwanaume huyo na kila mmoja alikuwa akimuhukumu kwa nafasi yake kama mtuhumiwa ambaye alitakiwa kunyongwa mpaka kufa.
Kwenye vyombo vya habari, ni picha zake tu ndizo zilikuwa zikitawala. Wamarekani walijua kucheza na akili za watu, walijisifia kwamba hakukuwa na mtu yeyote ambaye angethubutu kuichezea nchi hiyo na kutafutwa asipatikane.
Walihitaji watu wao warudishe matumaini kwao kwa mara nyingine kwani kulikuwa na watu wengi ambao walikuwa wakitafutwa na maofisa wa CIA lakini cha ajabu kabisa hawakuwa wakipatikana.
Kitendo cha kumkamata mzee Todd kikawahakikishia kwamba wangesifiwa kila kona kwani wangeonekana mashujaa ambao hawakulala usiku mzima kwa ajili ya mtu huyo.
Mzee Todd akawekwa ndani ya chumba cha mahojiano na kuanza kuulizwa maswali kadhaa. Hakufumbua mdomo wake kujibu swali lolote lile, kila kitu alichoulizwa, aliwaambia kwamba asingeweza kuongea lolote lile mpaka mwanasheria wake kuwa mahali hapo.
Hilo halikuwa tatizo hata kidogo, haraka sana mwanasheria wake, Harry Donny akapigiwa simu na ndani ya dakika chache alikuwa ndani ya chumba hicho na mzee Todd kuanza kujibu kila swali alilokuwa akiulizwa.
Aliulizwa zaidi ya maswali hamsini ambayo yote aliyajibu kwa ufasaha na hivyo kesi hiyo kutakiwa kufika mahakamani haraka sana.
Wakati huo kila kona duniani walikuwa wakimzungumzia mzee huyo, kesi yake hiyo nzito ilizua mambo makubwa mno, kila kona, watu wote walitaka kuisikiliza na kuona hatima ya mzee huyo ingekuwa nini.
Asilimia kubwa ya watu walitaka kushuhudia mzee huyo akifungwa kifungo cha miaka mingi gerezani kwani kwa miaka hiyo kulikuwa na idadi kubwa ya vijana waliokuwa wakipotea kutokana na matumizi mabaya ya madawa ya kulevya.
Waandishi wa habari walikuwa wakimiminika mahali hapo huku wakiwa na hamu ya kutaka kuzungumza na mzee huyo au hata kupata picha zake kwani picha nyingi ambazo zilikuwa zikitumika kipindi hicho zilikuwa ni picha za zamani tu.
Hakukuwa na mtu aliyepata nafasi hiyo, waliambiwa kwamba suala la picha walitakiwa kusubiri mpaka siku ambayo angepandishwa mahakamani.
Mwanasheria wake ambaye ndiye huyohuyo angekuwa wakili wake akaanza kumuuliza maswali mengi juu ya kilichokuwa kimetokea. Hakutaka kumficha, alimwambia ukweli kuhusu kila kitu kwamba hakuwa ameweka madawa ya kulevya ndani ya nyumba yake bali kulikuwa na mwanaume aliyeitwa Maxwell ambaye ndiye alikuwa nyuma ya mchezo wote.
Yeye ndiye aliyeratibu kila kitu na hata alipokwenda Afrika, yeye ndiye aliyepanga mipango ya kuuawa lakini ilishindikana baada ya kukutana na kijana aliyejitambulisha kwa jina la Bruno.
“Alisuka mipnago ya kunimaliza, nikasaidiwa kwani nilichukuliwa kwenye meli yake na kupelekwa sehemu kwa lengo la kuuawa ila tukatoroka bandarini,” alisema mzee Todd.
“Na huyo kijana kuna uwezekano wa kupatikana?”
“Ndiyo! Kuna uwezekano, yeye atatoa ushahidi wa kila kitu kilichotokea,” alisema mzee Todd huku akiwa na uhakika wa kumpata Bruno.
“Sawa. Haina shida!”
Walizungumza mambo mengi na baada ya kukamilisha kila kitu, tarehe ya mahakama ikapangwa tayari kwa kuanza kusikilizwa kwa kesi hiyo.
Mzee Todd alikuwa mtu mwenye huzuni tu, kila alipokuwa selo kichwa chake kilikuwa kikiifikiria familia yake tu, hakuamini kama aliipoteza kwa tamaa za mwanaume mmoja tu aliyetaka afutike ndani ya dunia hii.
Alihuzunika mno lakini alijiahidi kwamba kamwe asingelipa kisasi kwa kuwa aliamini kwamba kulikuwa na Mungu ambaye alisema kwenye maandiko yake kwamba visasi vyote vilikuwa juu yake.
Siku ziliendelea kukatika, baada ya siku kadhaa, hatimaye siku iliyokuwa ikisubiriwa kwa hamu ikawadia. Zaidi ya watu elfu tatu walikusanyika katika viunga vya mahakama kwa lengo la kusikiliza kesi hiyo. Hapo, kulikuwa na waandishi wa habari ambao kazi yao kubwa ilikuwa ni kupiga picha kila kitu kilichokuwa kikiendelea mahali hapo.
Mashirika makubwa ya habari duniani, CNN, BBC, Sky News na mengi yalikuwa bize kuonyesha moja kwa moja kila kitu kilichokuwa kikiendelea katika viunga vya mahakama huku wakijaribu kufanya mahojiano na baadhi ya watu waliokuwa mahali hapo.
“Namkumbuka mpenzi wangu, Jericho, alikuwa mtu mwema kabisa lakini baada ya kuanza kutumia madawa ya kulevya, nikampoteza, moyo wangu uliniuma sana, ninapomuona huyo mzee, ninatamani hata nimuue kwa mkono wangu,” alisema msichana mmoja huku akionekana kuwa na hasira mno.
“Nilimpoteza kijana wangu baada ya kuingia kwenye matumizi ya madawa ya kulevya. Nilimpa kila kitu, hakutaka kusoma, alichanganyikiwa kabisa na madawa. Halafu leo mniambie kwamba huyu mzee aachiwe huru, nadhani nitamuua hata mtaani,” alisema mwanaume mmoja, kwa kumwangalia tu isingekuwa vigumu kuamini kwamba angefanya kile alichokuwa akikisema.
Kila mtu aliyekuwa akihojiwa alimshutumu mzee huyo moja kwa moja, hakukuwa na mtu aliyetaka kumuona mwanaume huyo akiachiwa huru, kila mmoja alitamani kuona akihukumiwa jela kwa kosa alilokuwa amelifanya.
Baada ya saa moja, gari moja lililokuwa likiongozwa na baadhi ya magari ya CIA lilikuwa likiingia mahakamani hapo. Haraka sana waandishi wa habari wakasogea kule lilipokuwa na kuanza kulipiga picha.
Kila mtu aliamini kwamba huyo alikuwa mzee Todd, walipiga picha nyingi mpaka mlango ulipofunguliwa na mwanaume huyo kuteremshwa huku akiwa na pingu mikononi mwake.
Hakuuficha uso wake, alikuwa na uhakika wa kushinda kesi hiyo, alikuwa akiangalia huku na kule, hakutabasamu, alikuwa kwenye hali ya kawaida, alizungukwa na maofisa wa CIA mpaka alipoingizwa ndani ya jengo la mahakama.
Humo ndani, kulikuwa na watu zaidi ya mia saba waliokuwa wamekaa na wengine kusimama, kila mmoja alitaka kujua kile kilichokuwa kikiendelea, siku hiyo ilikuwa ni ya kusikiliza kesi lakini hakukuwa na mtu yeyote yule aliyetaka kukosa kesi hiyo.
Baada ya dakika kadhaa, mzee Todd akapelekwa kizimbani na hakimu kuingia. Kwa heshima kila mtu akasimama, alipokaa tu kwenye kiti chake, akagonga kinyundo na watu wote kukaa.
Kesi ikaanza mara moja. Siku hiyo haikuwa ya kusikiliza mashahidi, haikuwa siku ya kusikilizwa utetezi wake, ilikuwa ni siku ya kusomewa mashtaka, makosa aliyoyafanya na baada ya hapo kesi kuahirishwa mpaka baada ya wiki moja na nusu.
“Ninaiahirisha kesi hii mpaka tarehe 10/08,” alisema hakimu na kugonga kinyundo chake, akasimama na kuondoka mahali hapo.
Watu wakatoka nje lakini hawakutaka kuondoka mahakamani hapo, walitaka kumuona mzee Todd akiondolewa na kupandishwa ndani ya gari lake.
Polisi mmoja akamfuata pale kizimbani, akamchukua na kuanza kuelekea naye nje huku akiwa amemfunga pingu. Kila kona mahali hapo kulikuwa na ulinzi mkali, walijua kwamba mwanaume huyo alikuwa na watu wengi hatari ambao wangeweza kufanya kila liwezekanalo mpaka kuhakikisha wanamtoa mahali hapo.
Walichokuwa wakikifikiria kilikuwa tofauti kabisa, mzee Todd hakuwa na kundi lolote lile, alikuwa yeye kama yeye na hakukuwa na kitu ambacho aliamini kama mashahidi ambao wangeeleza kila kitu kilichokuwa kimetokea na hivyo kushinda kesi hiyo.
Alipotolewa nje, watu wakachukua simu zao na kuanza kumpiga picha, waandishi wa habari walikuwa wakihangaika, hawakutulia, kila mmoja alihakikisha anapata picha ambayo ingeyafanya magazeti yao na tovuti zao kutembelewa na watu wengi.
Mzee huyo hakuuficha uso wake kama watu wengine, hakuona kama alikuwa na hatia na muda wote alikuwa kimya tu, akachukuliwa na kupakizwa ndani ya gari na kuanza kuondolewa mahali hapo.
Wakati akiondolewa, wakili wake, Harry alikuwa akimwangalia, moyo wake ulimuuma mno, alimuonea huruma mteja wake lakini alikuwa na uhakika kwamba hao mashahidi ambao alimtajia basi wangeweza kumsaidia kutoka katika mikono ya kifungo kilichokuwa kikimkabiri.
Baada ya gari lile kuondoka, akalifuata gari lake na kuondoka mahali hapo. Wakati gari likiwa limefika katika Barabara ya Brooklyn, akaangalia kwenye kioo, kwa nyuma kulikuwa na gari lililokuwa likimfuata.
Alikuwa na wasiwasi nalo kwani kila alipokuwa akijaribu kwenda huku na kule, gari lile lilikuwa likimfuata kitu kilichomfanya kuhisi kuwa watu waliokuwa humo walikuwa wabaya ambao wangeweza kumfanya lolote lile.
Akaanza kuliendesha gari kwa mwendo wa kasi, hilo halikuweza kumsaidia kwani gari lake halikuwa na kasi kubwa kama gari lililokuwa likimfukuza kwa nyuma.
Aliendesha lakini hakuweza kuliacha, gari hilo likamfikia na kuanza kuendesha ubavuni mwake. Mwanaume mmoja akatokeza na kumnyooshea bastola na kumtaka asimamishe gari vinginevyo angeanza kumshambulia kwa risasi.
Harry akaogopa, hakutaka kuona akifa, mule ndani ya gari alipokuwa akaanza kutetemeka kwa hofu, akaanza kupunguza mwendo na kusimama.
Gari lile likasimama, wanaume wawili wakateremka na kumfuata huku wakiwa na bastola mikononi mwao, baada ya kulifikia, wakafungua mlango na kumteremsha na kumpeleka ndani ya gari lao.
“Don’t dare to open your fucking mouth,” (usithubutu kufungua wako) alisema mwanaume mmoja huku akimgongagonga na bastola kichwani. Harry akanyamaza, kijasho chembamba kikaanza kumtoka na kuhisi kwamba huo ungekuwa mwisho wake.
Je, nini kitaendelea?
Tukutane kesho