Bruno The Fishman
Mtunzi.Nyemo
Episode 7
Safari ya kuelekea katika kituo kikuu cha polisi ilikuwa ikiendelea kama kawaida. Ndani ya gari lile polisi wote walionekana kuwa na furaha kupita kawaida, kwao, kumpata mzee Todd iliwafurahisha na kujiona wakipata pesa ambazo ziliahidiwa kwa yeyote ambaye angefanikisha kupatikana kwa mtu huyo.
Bunduki zilikuwa mikononi mwao, walimpa ulinzi wa kutosha kwani walichokijua ni kwamba mwanaume huyo alikuwa hatari sana, kama wasingemlinda kama walivyofanya basi hali ingekuwa ya hatari mno. Mzee huyo alikuwa na Bruno humo, walimwangalia kijana yule, hawakumjua alikuwa ni nani kwa yule mzee lakini kitu walichohisi ni kwamba alikuwa kijana wa mzee Todd ambaye alikuwa akishirikiana naye kuuza madawa ya kulevya barani Afrika.
Wakati wakiwa wamekwishafika katika eneo maarufu kwa kuuza vitanda, Vasco Da Gama wakashtukia wakianza kumiminiwa risasi mfululizo. Hawakujua watu hao walikuwa wakina nani, walipigwa risasi lakini hawakuwaona watu waliokuwa wakiwashambulia.
Mpaka wanainama na kujificha, polisi wanne walikuwa chini, damu zilikuwa zikiwatoka. Watu waliokuwa karibu na eneo hilo, hawakutaka kubaki mahali hapo, wakaanza kukimbia kuyaokoa maisha yao. Vijana ambao waliwashambulia polisi hao, wakatoka walipokuwa wamejificha, walikuwa vijana saba wenye silaha kali aina ya AK 47, walitembea kwa mwendo wa kujiamini huku wakiendelea kulifuata gari lile.
Walipolifikia, wakalizunguka na mwanaume mmoja kuwatangazia polisi waliokuwa humo kwamba walitakiwa kutupa bunduki zao vinginevyo wangelilipua gari hilo. Polisi walivyosikia hivyo wakaogopa na kufanya kama walichoambiwa.
Walifanya hivyo kwa sababu mbili. Moja ni kwamba walihisi kwamba wangelipuliwa kweli lakini kubwa zaidi ni kwamba hawakuwa wakifahamu watu hao walikuwa wangapi.
Walipozitupa tu, wanaume hao wakalisogelea gari hilo, wakawaangalia polisi wote, walikuwa wamelala huku wakiwa na mzee Todd na Bruno ambao nao walikuwa kimya. Vijana hao hawakutaka kupoteza muda, walichokifanya ni kuwamiminia risasi polisi wote.
“Na hawa tuwafanye nini?” aliuliza mwanaume mmoja.
“Nao wamalize,” alisema mwingine, wakakoki bunduki zao tayari kwa kuwamaliza mzee Todd na Bruno.
***
Milio ya risasi ilikuwa ikiendelea kusikika kama kawaida. Baada ya mzee Todd na Bruno kukimbia kwa kuruka ukuta, Onyango akabaki ndani ya jumba lile na wenzake. Alijua kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wake, hakujua ni wakina nani walikuwa wakipiga risasi hizo, alichanganyikiwa ndani ya jumba lile kiasi kwamba wakati mwingine alitamani hata ardhi ipasuke atumbukie ndani.
Alitamani kwenda kupambana lakini kwa jinsi risasi zile zilivyokuwa zikirushwa, alijua kabisa kwamba watu hao walikuwa hatari, kwani risasi zilipigwa kwa malengo na nyingi ziliwapata wenzake.
Hakutaka kuona akifa, alitakiwa kupambana mpaka anashinda, njia pekee ya kuyaokoa maisha yake ilikuwa ni kuingia katika dari ndani ya nyumba hiyo. Hilo ndilo alilolifanya, haraka sana akaufungua mlango wa dari na kuingia ndani kujificha.
Huko juu, kulikuwa na harufu chafu, joto lakini alitakiwa kuvumilia kwa sababu tu alitakiwa kuupambania uhai wake. Baada ya dakika chache, mlango ukafunguliwa na wanaume kuingia ndani ya jumba hilo. Aliwasikia vilivyo, wanaume hao wakaanza kuongea ndani ya jumba hilo kwamba watu wote walikuwa wamekufa.
Kwa jinsi Kiingereza chao walivyoongea, alijua kabisa walikuwa Wamarekani, hawakuwa Wazungu wa Afrika Kusini, hakujua sababu za watu hao kuwa mahali hapo na kuwashambulia kiasi hicho. Baada ya dakika moja tu, wanaume hao wakaondoka baada ya kuhakikisha kwamba kila mtu aliyekuwa ndani ya nyumba ile alikuwa amekufa.
Huku akijiandaa kuteremka, akasikia mlango ukifunguliwa tena, muda huo alikuwa Bruno ambaye alifuata kadi ya ATM. Hakumuona, alichokijua ni kwamba alikuwa mmoja wa Wazungu wale hivyo akajificha kama kawaida. Baada ya sekunde kadhaa, mlango ukafungwa na mwanaume huyo kuondoka.
Baada ya nusu saa, Onyango akateremka kutoka ndani ya dari, kile alichokiona kilimsikitisha kupita kawaida, hakuamini kama marafiki zake wote walikuwa wamekufa ndani ya nyumba hiyo.
Hali iliyokuwa ndani ndiyo iliyokuwa na nje pia, kila kona kulitapakaa miili ya marafiki zake. Siku hiyo hapo Soweto kulikuwa na msiba mzito, watu walilia sana na kuwachukua Wazungu kupita kawaida.
Siku iliyofuata, Onyango akawatafuta watu wengine wa kuunda kundi jingine. Alikuwa na hasira mno na hakutaka kabisa kuona wakiendelea kushambuliwa na Wazungu, ilikuwa ni lazima wahakikishe wanapambana vilivyo.
Kundi jingine likaundwa, ingawa alikuwa Mkenya lakini kila Msauzi alikuwa akimpenda, alikuwa mkorofi sana, alijua kupambana na hata kuwalaghai watu wengine waungane naye.
Kuunda kundi kubwa tena haikuchukua siku moja, ilichukua wiki mbili, vijana ishirini wakajikusanya na kuunda kundi jingine kubwa la wahuni. Walichokuwa wakikihitaji zaidi kilikuwa ni silaha tu.
Walizokuwa nazo, hazikutosha, walitakiwa kujipanga na kutafuta nyingine. Baada ya kundi kutimiza mwezi, wakaamua kuondoka hapo na kwenda nchini Msumbiji.
Walichokuwa wakikihitaji kilikuwa ni bunduki tu. Waliogopa kufanya uhalifu Afrika Kusini kwa kuwa walihofia maisha yao na kutafutwa. Hawakutaka kuharibu huko, walitakiwa kuharibu sehemu nyingine kabisa, hivyo wakaenda huko.
Watu waliokuwa na bunduki walikuwa polisi hivyo kuanza kuchunguza na kugundua kwamba kulikuwa na gari la polisi lililokuwa likitoka katika Mbuga ya Limpopo na kuelekea mjini huku wakiwa na bunduki ndani ya gari hilo.
Hiyo ikawa nafasi yao, wakaelekea mjini na kutafuta sehemu kujificha. Hakukuwa na mtu aliyeonekana kuwa na hofu nao, walivaa kiheshima na walikuwa wakirandaranda mpaka kipindi ambacho gari la polisi lilipoanza kuonekana.
Hawakutaka kuchelewa, walichokifanya ni kuanza kulishambulia, watu waliokuwa mahali hapo wakakimbia kwani walijua kabisa kwamba watu hao walikuwa hatari. Kwa kuwa mule kulikuwa na polisi nane, waliamini kwamba kungekuwa na bunduki za idadi hiyo ambazo zingewafanya kuwa na idadi kubwa ya bunduki na hivyo kuendelea kufanya uhalifu.
“Na hawa tuwafanye nini?” aliuliza mwanaume mmoja.
“Nao wamalize,” alisema mwingine, wakakoki bunduki zao tayari kwa kuwamaliza mzee Todd na Bruno.
Huku kijana yule akijiandaa kuwafyatulia risasi watu hao, Onyango akaamuru waache kwani alitaka kuwaona kwanza. Hilo halikuwa tatizo, kijana huyo akaacha, Onyango akasogea mpaka kule, watu aliowaona, yeye mwenyewe akashtuka.
“Bruno!” aliita huku akionekana kushtuka.
“Onyango!”
“Vipi tena? Mbona sielewi?” aliuliza Onyango huku akiwaangalia kwa mshangao mkubwa.
Bruno hakujibu kitu, kitendo cha kumuona Onyango tu kilimaanisha kwamba maisha yao yangekuwa salama. Hilo lilikuwa eneo la tukio, hawakutakiwa kukaa sana mahali hapo, walichokifanya ni kuchukua bunduki walizokuwa wakizitaka na kuondoka mahali hapo.
Wakaingia ndani ya gari na kuanza kuelekea nchini Afrika Kusini kupitia katika Mbuga ya Wanyama ya Limpopo. Walijua njia za panya, walijua njia ambazo hakukuwa na kamera.
Asubuhi ya siku iliyofuata wakafika huko, wakaelekea mpaka Soweto na kupumzika. Huko ndipo Bruno akaanza kuwaambia kile kilichokuwa kimetokea, kwamba walikuwa na mpango wa kwenda Kenya lakini wakajikuta wakikamatwa.
“Mnataka kurudi Kenya?” aliuliza Onyango.
“Ndiyo!”
“Basi subiri nifanye mpango! Endeleeni kukaa hapa.”
Hawakuwa na jinsi, waliambiwa kwamba walitakiwa kusubiri na hivyo kufanya hivyo. Waliendelea kubaki mahali hapo huku siku zikiendelea kukatika. Alichokuwa akikifanya Onyango ni kuwatafutia watu ambao aliwaamini ambao wangewachukua watu hao mpaka nchini Kenya.
Bruno alikuwa na mawazo tele, kwake, siku moja ilionekana kuwa na saa arobaini na nane kwani alikuwa akisubiri sana lakini hakukuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea.
Wakati mwingine Bruno alikuwa akimuuliza kuhusu namba za simu za watu aliokuwa akiwafahamu nchini Kenya. Kwa Onyango, hilo halikuwa tatizo, aliwafahamu watu hao kwani kulikuwa na Wakenya wengi kutoka katika Kijiji cha Guolduvai.
Onyango akawa na kazi mbili, kwanza kuwatafuta vijana ambao wangefanikisha wao kufika nchini Kenya lakini pia vijana ambao walitoka katika kijiji hicho.
Baada ya mwezi kukatika ndipo akafanikiwa na hivyo kuwasiliana na Onyango na kumwambia kwamba kila kitu kilikuwa tayari.
Hata kabla Onyango hakumpelekea namba ya simu ya Alfred, mwanaume ambaye alimpata Afrika Kusini, akaamua kumpigia simu yeye mwenyewe na kuanza kuzungumza naye.
Alimwambia kwamba Bruno, mwanaume ambaye bila shaka alisadikiwa kufariki dunia nchini Kenya alikuwa hai nchini Afrika Kusini, ila mbali na hilo, alimwambia kwamba inawezekana Bruno akaja kuwa bilionea mkubwa kwa kuwa alikuwa na bilionea mkubwa ambaye alimsaidia kwa kila kitu.
“Bruno namkumbuka! Kijiji kizima kinajua kwamba amekufa,” alisema Alfred.
“Hajafa! Tupo naye huku!”
“Wapi?”
“Afrika Kusini!”
“Inawezekana vipi?”
“Ndiyo hivyo, ni stori ndefu, nafikiri akija huko atakwambia nini kilitokea,” alisema Onyango.
“Kwa hiyo nifanyeje?”
“Amesema mtafute rafiki yake anayeitwa Abdul, umwambie kwamba yupo hai!”
“Na nimwambie kuhusu ubilionea wake?”
“Hilo juu yako sasa!” alisema Onyango na kukata simu.
Baada ya hapo, akarudi nyumbani na kumwambia Bruno kwamba kila kitu kilikuwa tayari hivyo walichotakiwa ni kuanza safari siku inayofuata. Hilo halikuwa tatizo, wakajiandaa, ilikuwa ni lazima waondoke nchini humo kwani walikuwa wamekaa mno huku wakinusurika vifo na vifungo.
Bruno hakutaka kuridhika, alihitaji kuzungumza na huyo mwanaume kutoka nchini Kenya, hilo halikuwa tatizo, akapewa namba ya simu na kumpigia lakini kwa bahati mbaya, siku ya Alfred haikuwa ikipatikana.
Mpaka kesho yake inafika na kuondoka, bado simu ya mwanaume huyo haikuwa hewani. Vijana wanne walikuwa wakiondoka nao kuelekea nchini Kenya, hawakutakiwa kufika huko, walitakiwa kuishia njiani lakini pia hawakutakiwa kupitia Msumbiji, walitakiwa kupitia Botswana, Zambia, Tanzania na kuingia nchini Kenya.
Waliiona hiyo kuwa safari ndefu lakini walikuwa na uhakika kwamba watu hao wangeweza kufika huko salama kabisa. Baada ya kujiandaa kwa kila kitu, wakaanza safari hiyo kwa siri kubwa sana kuelekea nchini Kenya.
Wakati huo, tayari Bruno alikwishachukua kiasi cha dola laki moja benki ambapo dola elfu ishirini alimgawia Onyango kama shukrani huku akimuahidi kumtumia kiasi kingine cha pesa baada ya kufika nchini Kenya.
Safari ikaanza, ilikuwa ni ndefu na yenye kuchosha sana. Waliondoka kwa kujifichaficha sana mpaka wakatoka nje ya Afrika Kusini na kuingia Botswana.
Huko, njiani kote ni pesa tu ndiyo iliyokuwa ikitumika. Walipokuwa wakiona mambo magumu, walitoa kiasi cha pesa na kuwahonga polisi hivyo kuruhusiwa kupita katika sehemu ambazo hawakutakiwa kufika.
Walipoingia huko nchini Botswana, kitu cha kwanza kilikuwa ni kuchukua hoteli ya kawaida na kutulia. Bruno aliendelea kumpigia simu Alfred lakini hakuwa akipatikana, hilo lilimchanganya, alichokuwa akihitaji ni kuzungumza na mwanaume huyo na kumwambia kuhusu kwenda kule alipokuwa akiishi na kumwambia Abdul kwamba alikuwa hai.
Safari hiyo ilichukua wiki tatu mfululizo na ndipo wakafanikiwa kufika Tunduma nchini Tanzania. Hapo, wakachukua basi Mbeya Mjini ambapo huo ndiyo ungekuwa mwanzo wa kuelekea nchini Kenya.
Njiani, walichoka mno, walitamani hata Tanzania uwe mwisho wao, hawakutaka kuendelea zaidi lakini hawakuwa na jinsi. Walikuwa na pesa za kutosha, walipofika Mbeya Mjini, wakaelekea katika duka la kubadilisha pesa na kuchukua pesa za Kitanzania kiasi cha shilingi milioni sita na kuendelea na safari yao.
Kidogo kuwepo nchini Tanzania kuliwapa amani. Watu wa huko hawakuwa wakiangalia televisheni sana, walizipata taarifa kuhusu mzee Todd lakini hakukuwa na yeyote yule aliyeonekana kujali kuhusu mzee huyo.
Hapo Mbeya Mjini, walikaa kwa usiku mmoja na asubuhi wakapanda basi na kuanza safari ya kuelekea jijini Tanga. Safari yao ilichukua saa kumi na mbili wakafika jiji humo ambapo wakatulia katika nyumba ya wageni huku wakijiandaa safari ya kuelekea Mombasa.
“Tunaingia Kenya kesho, ila pia tutatakiwa kuingia kwa njia za panya kama tulivyofanya huko nyuma,” alisema Bruno.
“Ila Kenya si kwenu?”
“Ndiyo! Sina hati ya kusafiria, nahisi litakuwa tatizo!”
“Sawa. Basi tutatumia pesa kama kawaida,” alisema mzee Todd.
Hilo ndilo la msingi lililotakiwa kufanywa. Walichokifanya siku iliyofuata ni kuanza safari kwa njia ya basi kuelekea nchini Kenya. Njiani, hawakuonekana kuwa na hofu, waliamini kwamba wangefika nchini humo salama kabisa.
Basi lilitembea kwa mwendo wa kasi kuelekea mpakani mwa Tanzania na Kenya. Japokuwa huko kulikuwa na ulinzi mkubwa lakini walikuwa na uhakika wa kupita pasipo tatizo lolote lile. Ndani ya basi walikuwa wakizungumza mambo mengi, mzee Todd alimshukuru mno Bruno kwa kuwa alimsaidia sana mpaka kipindi hicho kuwa hai.
Hakuwa na familia yake lakini kitendo cha kuwa hai kipindi hicho kilimpa uhakika wa kuendelea kuishi na kujipanga kwa ajili ya maisha yake ya mbele.
Kulikuwa na kesi ya kuuza madawa ya kulevya, hakutaka kufikiria hilo sana kwani alikuwa na uhakika wa kulishinda, kitu pekee na cha umuhimu kabisa kilikuwa ni kuelekea nchini Marekani na kuendelea na maisha yake.
“Nakushukuru sana Bruno, bila wewe nadhani sasa hivi ningekuwa marehemu,” alisema mzee huyo huku akimwangalia Bruno.
“Tumesaidiana! Hata mimi nakushukuru sana! Naamini kila kitu kilitokea kwa mpango wa Mungu!” alisema Bruno huku uso wake ukiwa na tabasamu pana.
“Unahitaji nini nikufanyie?” aliuliza mzee huyo.
“Unifanyie?”
“Ndiyo!”
“Mimi ni masikini sana, mkwe hanitaki kwa kuwa mimi ni masikini!” alisema Bruno.
“Hilo si tatizo! Kuna jingine ambalo unataka nikufanyie?” aliuliza mzee Todd.
“Labda kukitengeneza Kijiji cha Guolduvai ninapoishi, hakuna zaidi,” alijibu Bruno.
Walikaa na kuzungumza mengi, wakati huo safari ilikuwa ikiendelea kama kawaida. Baada ya saa kadhaa, wakakaribia katika mpaka wa Tanzana na Kenya kwa upande wa Tanga ulioitwa Horohoro.
Siku hiyo ilionekana kuwa tofauti na siku nyingine, kulikuwa na idadi kubwa ya magari yaliyokuwa yakisubiri kuingia nchini Kenya. Mbali na magari hayo, pia kulikuwa na watu wengi waliokuwa wakitaka kuingia na kutoka.
Kila basi, abiria walitakiwa kuteremka na kuangaliwa hati zao za kusafiria. Kwao, hawakuwa na kitu chochote kile, walichokuwa wakikitegemea kilikuwa ni pesa tu walizokuwanazo.