Gharama Halisi ya Ufisadi hulipwa na Maskini!

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,476
39,995
MAHALI popote duniani ambapo ufisadi umeshamiri, basi, gharama yake halisi hulipwa na maskini na matajiri waadilifu.

Kwa kiasi kikubwa jamii ikikubali kuishi katika mfumo wa utawala wa kifisadi, ni vigumu kuweza kuona gharama hiyo; kwani imejipenyeza katika gharama za kawaida na hivyo kuonekana kama ni gharama "ya kawaida".

Kwa vile gharama hii hulipwa kwa kiasi kikubwa na maskini, basi, maskini wanafika mahali wanashindwa kuendelea kulipa gharama hiyo na matokeo yake hugoma, huasi, au husimama kukataa kuilipa. Gharama ya ufisadi kamwe haiwezi kulipwa milele!

Gharama hii ni vigumu kuiona kama mtu hatachukua muda kufikiria uwepo wake. Tuchukulie mfano wa kwanza ambapo mtumishi serikalini ambaye anafanya dili zake na watu wengine na mwisho wa siku anajikusanyia Shilingi milioni 300 ambazo ni "zake" na anaziweka benki.

Hizi ni fedha "zake" lakini hazikutokana na jasho lake; bali zimetokana na ‘kuchezea kalamu', mbinu na makubaliano na watu wengine ambao nao bila ya shaka watakuwa wamepata "makato yao".Mtumishi huyo anapopata shilingi hizo milioni 300 anaamua kwenda kutafuta kiwanja ili ajenge; anaenda mahali ambapo mtu mmoja anamhakikishia kuna kiwanja kizuri tu cha Shilingi milioni 30. Wanapoenda kwa mwenye kiwanja, yule dalali kumbe alishampa taarifa mwenye kiwanja kuwa adai Shilingi milioni 50 (halafu amkatie milioni 10).


Wanapoenda kukutana na mwenye kiwanja, anaonyeshwa kiwanja kizuri, kimekaa eneo zuri na pembeni kimezungukwa na viwanja vya maskini wengine na vijumba vya nyasi hapa na pale. Mtumishi wetu anakipenda kiwanja, na kwa kweli anakitamani.


Mwenye shamba anasema hawezi kukiuza kwa Shilingi milioni 30; kwani tayari ameshakataa ofa kama hiyo kutoka kwa mtu mwingine na hawezi kukiuza chini ya Shilingi milioni 55!

Wanajadiliana na mwisho mtumishi wetu anakubali kununua kiwanja hicho kwa Shilingi milioni 50! Akitoka hapo anamlipa yule dalali Shilingi milioni 5 (walizokubaliana), na mwenye kiwanja anamlipa dalali milioni 10 walizokubaliana, na dalali na mwenye kiwanja wanatengeneza fedha zaidi ya walizotarajia!

Mtumishi anaondoka na mwenye furaha na akimaliza mchakato mzima wa kubadilishana hati za umiliki anajikuta amefikia zaidi ya Shilingi milioni 65! Mtumishi wetu hana wasiwasi anazimudu gharama hizo; kwani anazo fedha za kutosha ambazo amezitengeneza.


Yule bwana anakuja na kuanza kujenga kwenye eneo hilo huku akiendelea kufanya dili zake ofisini na kwa washirika mbalimbali, na anaweza ndani ya mwaka mmoja tu kujenga jumba la kisasa la zaidi ya Shilingi milioni 200 na kufanya thamani ya nyumba na kiwanja kufika zaidi ya Shilingi milioni 300 baada ya kuongeza miundo mbinu nk.

Lakini wakati huo huo kuna mtumishi mwingine mwadilifu ambaye amekuwa akitafuta kiwanja ambacho angeweza kukimudu. Katika utafiti wake anapelekwa kwenye kiwanja cha jamaa ambapo anaambiwa angeweza kupata kiwanja kizuri tu kwa Shilingi milioni 5 kutoka kwa mkulima mmoja na kama akitaka pamoja na shamba, basi, angeweza kupata kwa Shilingi milioni 15; hakuna dalali kuhusishwa.


Anapoenda kufanya majadiliano anajikuta kuwa mkulima kabadilisha mawazo; kwani sasa kiwanja kimepanda thamani; sasa ni Shilingi milioni 25. Anauliza kisa nini anaambiwa jirani hapo kauza kiwanja chake kwa mtumishi "kama yeye" kwa Shilingi milioni 50!


Akiwa anashangaa shangaa, viwanja vingine vyote pale navyo vinapandishwa thamani na hakuna tena kiwanja kinachopatikana hapo chini ya Shilingi milioni 30! Yule mtumishi mwadilifu anajikuta anaamua kutonunua kiwanja bali bora kuendelea kupanga kwa mama "mwenye nyumba".

Kwa haraka haraka mtu atasema kuwa "soko limeamua". Lakini ukweli ni kuwa mtumishi fisadi ndiyo ameamua gharama ya kiwanja; kwani kwake yeye hakulipa gharama ya jasho lake kununua kiwanja na hakuona uchungu wa kufanya hivyo kwani fedha alizotumia hazikuwa zake lakini ameweza kuwaathiri watu wengine kununua viwanja eneo hilo.


Matokeo yake eneo zima sasa litaanza kuvutia watu wenye kipato cha juu na muda si mrefu wamiliki wa asili wa viwanja hivyo wakajikuta wanaachiwa vimaeneo vidogo vya kujenga vibanda vyao pembezoni mwa majumba yanayoibuka ya wakubwa.

Gharama ya ufisadi inalipwa na maskini
lakini pia hulipwa na matajiri waadilifu. Fikiria mtu kafanya kazi zake, biashara kwa uadilifu, akijinyima na kuinyima familia yake hadi ameweza kujikita na kuanza kula faida. Na katika hiyo faida ameamua sasa angalau ajipatie nyumba nzuri zaidi na kubwa na gari jingine la kisasa.

Vyote hivyo anataka kuvipata kwa kutumia hela yake halali ambayo ameitolea jasho. Anapokwenda kutafuta kiwanja anakutana na hali ile ile kama ya mtumishi maskini; kwani bei ya viwanja haiangalii umepataje fedha zako wewe mnunuzi. Japo anauwezo wa kulipa Shilingi milioni 30 au 40 kwa kiwanja lakini kinamuuma!

Kinamuuma kwa sababu hii ni fedha yake aliyoitolea jasho na anajua kama yule fisadi asingenunua ardhi kwa bei ya juu hivyo angeweza kupata kiwanja kile kile kwa nusu ya bei yake ya sasa. Kwa vile kila anakogusa anakuta mafisadi wameshapandisha bei, basi, anajikuta analazimika kununua kiwanja kwa milioni 40 ambacho kingemgharimu labda shilingi milioni 20 tu. Analipia gharama ya ufisadi.

Akitaka gari hali ni hiyo hiyo. Ameagiza gari na anapoenda bandarani anazungushwa na analipishwa Shilingi milioni 15 zaidi katika ada mbalimbali na mikato mbalimbali ili hatimaye gari yake ije ikiwa salama salmini. Anafanya hivyo kwa sababu mafisadi tayari wana watu wao ambao wanapitisha magari kwa urahisi na hawajali gharama yake!

Hili nalo ni kweli hata kwenye huduma za hospitali. Wakati mafisadi wanaweza kabisa kumudu gharama za afya kwa muda mrefu, maskini na matajiri waadilifu wanajikuta wanalipia huduma ya afya kwa kiwango cha juu kwa sababu hakuna hospitali ambayo itakuwa tayari kutoza fedha ya chini wakati wapo watu wanaoweza kuimudu bila kusikia uchungu.

Hili nalo unaweza kuliona kwenye elimu vile vile ambapo mafisadi wanaweza kumudu kupeleka watoto wao mahali popote na kwa elimu ya kiasi chochote; kwani kwao gharama hiyo hawailipi wao hasa. Na hivyo utaona wanapandisha gharama ya shule hizi kwa watu wa kawaida ambao wangeweza kujinyima ili waweze kupeleka watoto wao huko.

Na wanaathiri matajiri waadilifu kwa sababu wao wanalipia zaidi kutoka katika faida yao ili waweze kuwapeleka watoto wao kwenye shule hizo. Wale mafisadi wao hawajali sana kwa sababu wanajua wakifanya hivi au vile wanaweza bado kuchota fedha ya kutosha kutoka katika hazina ya taifa na kumudu mahitaji yao.

Kwa mifano hiyo michache unaweza kuona kabisa kuwa maskini na matajiri waadilifu ndio hulipia zaidi gharama halisi ya ufisadi. Mafisadi hawana uchungu kutumia fedha isiyokuwa ya kwao na kwa kiasi chochote kile. Wanaweza kabisa kubadilisha gharama ya vitu mbalimbali na huduma mbalimbali kwa sababu wao hawalipi kutoka katika jasho lao.

Matokeo yake ni kwamba kadri mafisadi wanavyozidi kupandisha gharama ya vitu hivyo, ndivyo pia maskini inampasa kujitutumua zaidi au na yeye katika ngazi ya chini aliko kumpasa kutumia mbinu mbalimbali za kifisadi ili aweze kuyamudu maisha. Matokeo yake utaona ufisadi unakuja na pande mbili kubwa.

Wapo mafisadi wakubwa ambao ndio wanasimamia uchumi; na wapo mafisadi wadogo ambao wanalazimishwa kushiriki ufisadi kwa sababu mafisadi wakubwa ndio wanasimamia uchumi. Hawa maskini mafisadi ni watu ambao kwa kweli kabisa wangeweza kutojihusisha na vitendo vya kifisadi endapo wangejua kuwa tabaka la mafisadi wa juu wanadhibitiwa.


Juzi, Rais Kikwete akifungua ukanda wa uwekezaji uliopewa jina la "Rais Mwekezaji nambari moja", Benjamini Mkapa, alijaribu kulizungumzia hili la ardhi na madalali. Lakini ukweli ni kuwa udalali wa ardhi ni kazi halali kabisa na si haki kuwazuia watu kujihusisha nayo.

Tatizo la msingi ni mafisadi!

Mahali pote duniani madalali wa ardhi wanatengeneza fedha vizuri tu endapo watapata wanunuzi na wauzaji wanaokubaliana. Si kosa la dalali kuweza kuuza ardhi na kujipatia kamisheni yake. Tatizo ni kuwa wapo watu wanaolipa bei hiyo.

Rafiki yangu mmoja amekuja akitokea Marekani ili aweze kuanzisha shughuli ya kibiashara na yuko mbioni kutafuta sehemu ya makazi (apartment). Mwenyewe katika bajeti yake alitaka nyumba ambayo ina kila kitu na nzuri kwa gharama ya kama dola 2,000 kwa mwezi.

Kwa Marekani pango la dola 2,000 ni zuri kabisa na unaweza kupata nyumba nzuri tu na ya kisasa tena "furnished". Dalali mmoja aliposikia bajeti yake hiyo alimcheka. Alimuambia Dar huwezi kupata nyumba ya kisasa kwa namna hiyo, na hasa kwa vile yeye ni Mmarekani.

Akaambiwa lolote analotaka anahitaji si chini ya dola 4,000! Sasa hiyo yawezekana isiwe kweli kwa kila mahali lakini ina ukweli ndani yake.

Hali hii haiwezi kamwe kudumishwa kwa muda mrefu. Endapo maskini wengi wataendelea kujikuta wanasukimizwa nje ya ukingo wa mafanikio, kuna wakati watafika mahali wataweka mguu chini na kusema hawasukumizwi tena.

Tayari wameshaanza na msemo kuwa "hatudanganyiki tena". Huko tunakokwenda watasimama na kusema "hatuendi tena"; kwani hata punda akibebeshwa mzigo sana kuna wakati hugoma.

Katika Tanzania yetu hii, maskini na matajiri waadilifu hulipia gharama kubwa ya vitendo vya kifisadi. Hawana uwezo wa kuzuia lakini kwa kadri siku zinavyokwenda, na kwa kadri mzigo huu wa ufisadi unavyozidi kuongezewa kwenye migongo iliyokwisha pinda ya hawa maskini, kuna wakati watataka kutua mzigo huo kwa njia yoyote ile.

Ipo siku Watanzania wataamua mzigo wa ufisadi utoke migongoni mwao. Itakuwa ni siku ya kujikomboa; kwani ufisadi ulivyo hauwezi kudumishwa na hauwezi kuwa endelevu.


(RAIA MWEMA)
 
Na mara baada ya matumbo kujaa kwa kufakamia kwa kasi,ni wananchi hao hao watawalipia na mazoezi ya vitambi ka P.Diddy anavyodai,yani vituko tu!
Back to the real point nashangazwa sana kama hakuna sheria zinazogovern real estate vile?Hapo naona mafisadi ndio wenye kutoa maamuzinchi inaendeshwa ka genge,hayo maelezo yamethibitisha hilo.
 
Mkjj article yote hiyo kitaalam inaweza kuwa na maana moja tu, nayo ni "HYPERINFLATION" au "GALLOPING INFLATION"

Inapotokei watu wanakuwa na hela nyingi ambazo hawajazitolei jasho na kuamua kuzitumia bila kuwa na uchungu nazo, ni wazi hizi pesa zinakuwa na thamani ndogo (low real value) kwao ukilinganisha na mchimba mchanga anayejaza lory kwa shs 20,000. Matokeo yake ni kusababisha bei kuongezeka kwa more than 100% in a short time of period. Ingekuwa kila mtu anazo basi hapo tungeshuhudia watu wanaenda nunua mkate kwa gunia la noti, ila kwa kuwa ni wachache wanazo, matumizi yao yanaleta "domino effect" ya bei kwa watanzania wote.

Tatizo kubwa lipo pale BOT wanaotakiwa kudhibiti hii hali, kama wao wanaweza ku-overstate price ya nyumba ya gavana basi inakuwa kama wanakuwa wameseti standard. Pia kuchekea mafisadi, wakati wa JKN ilikuwa mtu ukinunua kitu kilicho juu ya kipato chako unamulikwa na kufilisiwa, hivyo ilikuwa inawafanya japo waogope ku-over spend, ila kwa sasa wakikuona wanakuletea na Kadi ya mchango wa kampeni za uchaguzi kama mfadhili wa CCM.
 
Mzee Manakijiji,

Watanzania ni wavivu kufikiria na kamwe hawatakuelewa kwa maana wamesharidhika na mfumo mbovu na kuuona ni wa kawaida! Angalieni Bangkok, moto mkali unasambaa kwa kasi!
 
Mzee Manakijiji,

Watanzania ni wavivu kufikiria na kamwe hawatakuelewa kwa maana wamesharidhika na mfumo mbovu na kuuona ni wa kawaida! Angalieni Bangkok, moto mkali unasambaa kwa kasi!

Halafu Thailand ndio ilikuwa inakuja kwa kasi.. one of those mini-asian tigers!... ooh well! huwezi kuwasukuma maskini pembezoni mwa mafanikio ukasalimika.
 
Think Tank wetu hawaoni tatizo lililopo mbele ya safari kutokana na umasikini. Wao kwao ni serikali ya CCM na wachangiaji wake! Wakiwa na mapesa basi nchi imesalimika. Kweli asiyejuaa maana huwa haambiwi maana.
Kuna msomi mmoja(Alexzander Ushakov, In the gun sight of KGB) enzi zile za USSR aliandika paper ikiwa na title "why USSR and Communism will fail", akaitwa traitor akakimbilia USA. Lakini hakukurupuka kutoa maoni yake bila kukusanya facts. Leo Mwanakijiji unatukumbusha kama yule jamaa alivyowakumbusha USSR, na pengine tutakuita hivyo hivyo. Ila unachokisema ni ukweli mtupu. Time will tell and sometimes in the most difficult circumstances.
 
Ukiangalia siku za karibuni wananchi wameanza kuwa very assertive linapokuja suala la haki zao. Kwa kadiri ya kwamba wanazidi kuhisi wanasukimizwa pembezoni mwa mafanikio huku wachache wakizidi kuletwa karibu ndivyo hivyo hivyo wao nao wanazidi kujikuta wanalazimisha. Matokeo yake ni kuongezeka kwa vitendo vya ujambazi na uporaji.
 
Ukiangalia siku za karibuni wananchi wameanza kuwa very assertive linapokuja suala la haki zao. Kwa kadiri ya kwamba wanazidi kuhisi wanasukimizwa pembezoni mwa mafanikio huku wachache wakizidi kuletwa karibu ndivyo hivyo hivyo wao nao wanazidi kujikuta wanalazimisha. Matokeo yake ni kuongezeka kwa vitendo vya ujambazi na uporaji.

Mzee Mwanakijiji, Serikali yetu kwa Makusudi kabisa imeamua kufanya Wananchi wake kuwa Makondoo, watu wa Yes Mzee, watu wasio jua kwamba kuna watu wanawajibika (Siyo khiari) kuhakikisha kwamba wanapata haki zao za Msingi. Na Serikali inatambua Udhaifu wa wananchi wake kwamba hata siku moja hawawezi kunyanyuka wakadai haki zao kwa maana wamekuzwa wakiamnishwa kwamba haki ni Jambo la hisani tu ambalo hata kama watanyimwa au wakipewa kidogo wanaishukuru Serikali. Mfano ni suala la Usajili wa CCJ katika nchi nyingine sasa hv Msajili angekuwa hana haki lakini leo Mwanakijiji ukiamua uanzishe Maandamano ya kudai haki kuna wengine watafanya Counter Maandamano ya kukulaani wewe na unaweza kushangaa hao wengine wakapata kibali cha kufanya hayo maandamano lakini wewe ukapigwa dana dana. Mfano hai ni Suala la TUCTA
 
Nimesoma makala kwa Unakini mkubwa sasa naweza kusema yafuatayo

Gharama za Ufisadi ni

1: Mishahara midogo kwa Wafanyakazi wengi wa Serikalini
2: Huduma Mbovu za Afya
3: Huduma zisizo sawa za Elimu ( Wengine wanasoma darasa la makuti wengine wanasoma Madarasa yenye viyoyozi, wengine wanatembea zaidi ya kilomita 10 kuifuata shule wengine wanafuatwa na magari mpaka milangoni halafu mwisho wa siku wanapimwa kwa Mtihani mmoja
4: Miundo Mbinu mibovu kuanzia Barabara, Usafiri wa anga, mifumo ya Maji taka na maji safi isiyokidhi mahitaji ya Miji yetu matokeo yake ni Magonjwa ya Milipuko kama Kipindupindu ambapo wahanga wengi ni maskini ( Hivi mafisadi huwa wanakufaga na Kipindupindu?)
5: Gharama za maisha kupanda kama Usafiri nk


Tanzania iliyokombolewa itawezekana tu kama kila mmoja wetu atafahamu Gharama za Ufisadi, pale kila mmoja wetu atakapofahamu namna anavyolipa gharama za Ufisadi, Kila mtu atakapofahamu kwamba Haki zake za Msingi kuna mtu ana Wajibu kuzitekeleza hata ikiwa kwa Mikwaju ya bakora
 
Nimesoma makala kwa Unakini mkubwa sasa naweza kusema yafuatayo

Gharama za Ufisadi ni

1: Mishahara midogo kwa Wafanyakazi wengi wa Serikalini
2: Huduma Mbovu za Afya
3: Huduma zisizo sawa za Elimu ( Wengine wanasoma darasa la makuti wengine wanasoma Madarasa yenye viyoyozi, wengine wanatembea zaidi ya kilomita 10 kuifuata shule wengine wanafuatwa na magari mpaka milangoni halafu mwisho wa siku wanapimwa kwa Mtihani mmoja
4: Miundo Mbinu mibovu kuanzia Barabara, Usafiri wa anga, mifumo ya Maji taka na maji safi isiyokidhi mahitaji ya Miji yetu matokeo yake ni Magonjwa ya Milipuko kama Kipindupindu ambapo wahanga wengi ni maskini ( Hivi mafisadi huwa wanakufaga na Kipindupindu?)
5: Gharama za maisha kupanda kama Usafiri nk


Tanzania iliyokombolewa itawezekana tu kama kila mmoja wetu atafahamu Gharama za Ufisadi, pale kila mmoja wetu atakapofahamu namna anavyolipa gharama za Ufisadi, Kila mtu atakapofahamu kwamba Haki zake za Msingi kuna mtu ana Wajibu kuzitekeleza hata ikiwa kwa Mikwaju ya bakora

Ujumbe huu unatakiwa usambazwe kwa kila mtanzania, na kwa kadri watakavyoelewa ndiyo harakati za ukombozi zitakavyopamba moto.

KAZI KUBWA ILIYO MBELE YETU NI KUWAKOMBOA WATANZANIA WALIO WENGI KIFIKRA, MENGINE YATAPATIKANA HUMO HUMO!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom