EWURA yatangaza ahueni kwa Watanzania

singidadodoma

JF-Expert Member
Nov 11, 2013
4,394
1,531
MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), imetangaza bei mpya za kikomo kwa bidhaa za mafuta na petroli nchini kuanzia Februari 3, 2016 huku ikizidi kuwapa ahueni Watanzania kwa kushusha bei kwa wastani wa sh. 55 kwa lita ya petroli huku dizeli ikivunja rekodi kwa kushuka kwa sh. 147 kwa lita tofauti na kiwango kichotangazwa Januari 6, mwaka huu.

Kutokana na bei hizo mpya zinazoanza kutumika leo (Februari 3), lita moja ya petroli kwa Mkoa wa Dar es Salaam itakuwa sh. 1,842 huku dizeli ikivunja rekodi kwa kushuka hadi sh. 1600.

Kutokana na bei hizo elekezi ni wazi kuwa Tanzania sasa ni nchi inayoongoza kwa bei za chini za bidhaa hiyo muhimu katika maisha ya kila siku ikilinganishwa na nchi jirani za Kenya na Uganda.

Kwa upande wa Uganda, bei ya lita moja ya petroli ni sh. 3,610 sawa na sh. 2,272 za Kitanzania huku dizeli ikiwa ni sh. 3,056 sawa na sh. 1,924 za Kitanzania. Kwa upande wa Kenya bei ya lita moja ya petroli ni sh.90.6 sawa na sh. 1,948 za Tanzania huku Dizeli ikiuzwa sh. 78. 85 sawa na sh. 1695.

Kwa mujibu wa taarifa ya Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Felix Ngalamgosi, wafanyabiashara wanaruhusiwa kushindana kwa kuuza bei ya chini ili kuweka ushindani katika soko huria lakini hawaruhusiwi kuuza kwa bei ya juu ya kikomo kwa kuwa kufanya hivyo ni kosa kisheria na mamlaka itatoa adhabu kali.

Licha ya bei ya mafuta kuwa na ahueni katika soko la dunia, lakini pia EWURA imezidi kuonesha uwezo wake katika usimamizi na ufuatiliaji wa karibu kuhakikisha Watanzania wananufaika na kupata unafuu wa maisha bila kuacha mwanya kwa wafanyabiashara wasio na uzalendo kupandisha bei ya bidhaa hizo za mafuta.

Kushuka kwa bei ya mafuta ya petroli kutoka wastani wa sh. 2250 hadi sh. 1842 na dizeli kwa takriban sh. 2150 hadi 1600 takriban miezi mitatu tu iliyopita ni dalili njema kwa uchumi wa Tanzania lakini mbaya kwa uchumi wan chi kama Nigeria mbazo uchumi wake unategemea bidhaa hiyo.

Kwa muda mrefu, Watanzania wamekuwa wakihoji uhalali wa bei ya mafuta kuwa juu zaidi kuliko hata nchi za Kenya na Uganda jambo ambalo limekuwa likihusishwa na ulaghai wa wafanyabiashara wakubwa kutumia mwanya huo kuzidi kuneemeka huku maisha ya walio wengi ikizidi kuwa ngumu.

Kwa mujibu wa EWURA, bei kikomo ya jumla kwa bidhaa ya mafuta kwa mkoa wa Dar es Salaam ni sh. 1,737.38 kwa petroli na sh. 1,494.85 kwa dizeli huku mafuta ya taa ikiwa ni sh. 1,594.04.
 
Back
Top Bottom