Mafisadi wa EPA hakuna wa kupona
Mwandishi Wetu
Novemba 5, 2008
DPP asema sheria itawabana wahalifu
Wamejichimbia Mbezi Beach kupitia mafaili
SIKU chache baada ya Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) kukabidhiwa majalada ya watuhumiwa wa wizi wa fedha katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT), imefahamika kwamba waliolipa fedha hawatakwepa mkono wa sheria ikibainika kuwapo jinai wakati wa kuchota fedha hizo.
Habari za uhakika kutoka ndani ya Serikali ambazo Raia Mwema imezipata zimeeleza kwamba hakuna mhalifu atakayesalimika ikiwa kutakuwapo ushahidi wa kuweza kufungua mashitaka; licha ya kuwapo mgawanyiko mkubwa kuhusiana na baadhi ya watuhumiwa kuendelea kutaka kukingiwa kifua na watendaji wa ndani ya serikali na wengine kutolewa kafara.
Kwa mujibu wa habari hizo, kauli ya Rais Jakaya Kikwete kuhusiana na wasiolipa ndio watakaochukuliwa hatua, imekuwa ikitumika na sasa imeibua mgawanyiko kwa wahusika wa ndani na nje ya Serikali; huku kila upande ukiitumia kwa mtazamo tofauti na kwa nia ya kulinda ama kupigania maslahi maalumu.
DPP, Elieza Feleshi, aliliambia Raia Mwema, jana Jumanne, kwamba ofisi yake ni asasi huru inayoendesha shughuli zake kwa kuzingatia sheria, na kwamba hakuna nguvu yoyote itakayoweza kuwafanya wafanye jambo kinyume cha sheria.
Alipoulizwa kuhusu kufikishwa au kutofikishwa mahakamani kwa baadhi ya watuhumiwa waliolipa mabilioni ya fedha za EPA, Feleshi alisema, "hatujajua kwa sasa, kwani ndio kwanza tuko kazini," na alipoulizwa kuhusiana na kusamehewa kwa wezi, alisema, "ofisi yangu inaendeshwa kwa kufuata sheria zilizopo na hatuwezi kufanya jambo lolote nje ya sheria."
Kuhusiana na uhuru wa ofisi yake kufanya maamuzi, Feleshi alisema, "Ofisi hii (DPP) iko huru tokea tunapata uhuru kwa kuwa iliwekwa wazi katika katiba yetu ya kwanza na hadi katiba ya sasa iko hivyo, hiki ni chombo huru."
Maelezo ya Feleshi na watendaji wengine serikalini yanaonyesha uwezekano wa serikali kubadili mwelekeo kwa kuepuka kuwalinda watuhumiwa waliobainika kushiriki vitendo vya jinai wakati wa mchakato wa kuchukua fedha za EPA, jambo ambalo limeelezwa ni kutokana na msukumo mkubwa nje ya mfumo rasmi serikalini.
"Unajua hata Rais Kikwete kama kiongozi anayeongoza kwa kufuata sheria hawezi kusema lolote kuhusiana na watu watakaochukuliwa hatua kwani kazi hiyo inahusu vyombo vya kisheria ambavyo ni lazima akwepe kuwapa nafasi ya kuweza kujitetea watakapofikishwa mahakamani kwamba walishahukumiwa," anasema mtu aliyekaribu sana na serikali.
Habari za uhakika zinaeleza kwamba kuanzia Jumatatu wiki hii, wanasheria wa Serikali wamejichimbia katika hoteli moja ya ufukweni, maeneo ya Mbezi Beach, jijini Dar es Salaam, wakipitia majalada yaliyowasilishwa ofisi ya DPP kutoka katika kikosi kazi (task force) kilichokuwa kikichunguza watuhumiwa wa EPA.
"Wameongeza nguvu kwa kuleta wanasheria makini baadhi kutoka nje ya Dar es Salaam kwa ajili ya kazi hiyo na wamepewa wiki mbili tu wawe wamemaliza kazi na hivi tunavyozungumza wako Mbezi wakifanya hiyo kazi kwa makini kuweza kukamilisha kabla ya kwisha kwa muda waliopewa," kinasema chanzo chetu chenye mahusiano ya kikazi na wanaofuatilia sakata hilo serikalini.
Kwa mujibu wa chanzo hicho, kwa sasa kumeibuka kwa hali ya wasiwasi miongoni mwa baadhi ya watu waliohusika kwa namna moja au nyingine na sakata la EPA, hata wale ambao walikuwa wanaamini kuwa wamejificha nyuma ya watu wengine katika kampuni zilizohusika na wizi huo.
" Nakuhakikishia hakuna atakayepona pamoja na kuwa wale mnaowataka mmoja anaweza kufikishwa mahakamani lakini wengine bado kazi kubwa inafanyika kupata ushahidi usio na shaka kutokana na nguvu kubwa waliyonayo watuhumiwa hao. Nakwambia hakuna atakayepona na wasidhani kuna msamaha kwa wahalifu. Msamaha unaweza kuwapo kwa waliochukua fedha bila kutenda kosa la jinai," kinaeleza chanzo hicho.
Siku tatu za mwisho kabla ya Oktoba 31, 2008 ziku ambayo Rais Kikwete alitoa kuwa mwisho wa waliochukua fedha za EPA kuzirudisha, baadhi ya wafanyabiashara walipeleka benki mabilioni ya fedha, sehemu ikiwa ni fedha taslimu.
"Hivi nchi hii kweli kuna sheria zinafanya kazi! Haiwezekani mtu anaweza kuwa na fedha taslimu kwa mabilioni na anawezaje kuzipeleka kwa mara moja benki. Waliziweka wapi, au ndio zile zinazodaiwa kuchapishwa?" alisema.
Baadhi ya wafanyabiashara walikimbilia kulipa fedha kupitia benki mbalimbali jijini Dar es Salaam, baadhi wakipeleka fedha taslimu katika maboksi na mabegi wakiwa na imani ya kupata msamaha, imani ambayo imeelezwa kuweza kuwagharimu.
Zaidi ya Sh bilioni 69 zumekusanywa kutoka kwa waliochota fedha za EPA,kiasi ambacho kilitangazwa na Rais Kikwete alipohutubia taifa mwisho wa mwezi uliopita.
Kumekuwapo na mjadala mzito kuhusiana na kauli za Serikali kuhusiana na malipo ya fedha za EPA kuwa kinga ya kufunguliwa kwa mashitaka ya kijinai kwa wahusika.
Wanasheria, wanasiasa na wananchi wengine wamekuwa wakisisitiza kwamba baadhi ya watuhumiwa wa wizi wa fedha za EPA walighushi nyaraka na hivyo wanapaswa kushtakiwa.
Hata hivyo, bado ni kitendawili kuhusiana na nani hasa atakayefikishwa mahakamani huku kukiwa bado na hofu ya kulindwa kwa baadhi ya watu 'wazito' walioko nyuma ya kampuni 13 zilizochota sehemu kubwa ya Sh. bilioni 90 ambazo zimethibitishwa kuchotwa kwa njia ya kihalifu.
Ripoti ya Wakaguzi wa Kampuni ya Ernst and Young waliofanya kazi kwa niaba ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ilionyesha kwamba kiasi cha Shilingi 90,359,078,804.00 zililipwa kwa kampuni 13 ambazo zilitumia kumbukumbu, nyaraka na hati zilizo batili na za kugushi na kwamba kampuni hizo zilifanya uhalifu na hazikustahili kulipwa chochote.
Wakaguzi hao na Ikulu kupitia taarifa iliyotolewa na Luhanjo, Januari 9, 2008, walipendekeza wahusika wa kampuni hizo 13 wachukuliwe hatua za kisheria ndani yake ikiwamo Kagoda Agricultural Limited na kampuni tisa za mfanyabiashara mwenye asili ya Kiasia, Jeetu Patel.
Kampuni ambazo Jeetu Patel anahusika nazo ni Navycut Tobacco (T) Limited, Ndovu Soaps Limited, Bina Resorts Limited, Bencon International Limited, Maltan Mining Company Limited, Bora Hotels & Apartments Limited, Venus Hotels Limited, and B.V. Holdings Limited.
Nyaraka za serikali zinaonyesha Kagoda Agriculture Limited inamilikiwa na John Kyomuhendo mwenye hisa 40 na Francis William anayemiliki hisa 60 katika kampuni hiyo, huku kukiwa na nyaraka nyingine muhimu zinazotaja wahusika zaidi ambao wanaelezwa kuwa na nguvu kubwa ndani ya mfumo wa.utawala.
Kampuni nyingine ni V.B & Associeties Company inazomilikiwa na Devendra Patel na Jantkumar Chandubhai Patel na Changanyikeni Residential Complex Limited inayomilikiwa na Jose Van de Merwe, Samson Mapunda na Charles Mabina ikiwa na makao yake, Sinza, Kumekucha, Dar es Salaam.
Katika orodha ya kampuni 13 zilizoghushi nyaraka zimo kampuni nyingine za Money Planners & Consultants inayomilikiwa na Paul Nyingo na Fundi Kitungi na kampuni ya Njake Hotel & Tours Limited inayomilikiwa Japhet Lema, Anna Lema, Abel Lema, Derick Lema na Benard Lema wa Arusha.
Miongoni mwa wanaotajwa kushirikiana na Jeetu Patel kupitia kampuni ya Ndovu Soap Limited ni Jayantulal Chandubhai Patel na Sidik Yacoubu.
Kampuni ya Bora Hotels and Apartments wamiliki wake wamo Jayantkumar Chandubhai Patel na Devandra Patel wakati Bina Resort Limited iliyosajiliwa Machi 31, 2005, wamo Jayantikumar Chandubhai Patel na Devendra Patel.
Kampuni ya Maltan Mining Company iliyosajiliwa Machi 8, 1993 inamilikiwa na Jantkumar Chandubhai Patel na Hariharier Radhakrishna wakati Navy Cut Tobacco iliyosajiliwa Oktoba 12, mwaka 1995 inamilikiwa na Jantkumar Chandubhai Patel na Radakrishna.
Kampuni nyingine ni Bencon Limited, B.V Holdings, Venus Hotels na V.B & Associeties Company zinazomilikiwa na Devendra Patel na Jantkumar Chandubhai Patel, ambazo zote zilisajiliwa Aprili 4, 2005.
Katika orodha ya BRELA imo pia kampuni ya Excellent Service Limited inayomilikiwa na Emil Samanya, Peter Sabas na Elisifa Ngowi. Kampuni hiyo ilisajiliwa Mei 13, 1992 na kupewa namba 26959.
Ngowi anahusishwa pia katika kampuni nyingine ya Clyton Marketing iliyosajiliwa Juni 6, 2005 akiwa na mwenzake Edwin Mtoi.
Wamiliki wengine waliofahamika ni Rajabu Maranda na Thabit Katunda ambao wanatajwa kumiliki kampuni ya Liqiud Service Limited ambayo usajili wake ulifanyika Desemba 12, 2004 na kupewa namba 15007.
Wamo pia Johnson Lukaza na Mwesigwa Rutakyamilwa Lukaza ambao wao wanamiliki kampuni ya Karnel Meals Holdings Ltd, Mibale Farm ambayo inamilikiwa na Kizza Selemani na Farijala Hussein na Malegesi Law Chambers inayomilikiwa na Beredy Malegesi.
Wamiliki wengine ni Paul Nyingo na Fundi Kitungi, wanaomiliki Kampuni ya Money Planners & Consultants iliyosajiliwa Machi 22, 2005 na Kiloloma & Bros Enterprises inayomilikiwa na Charies Kissa, ambayo ilisajiliwa Aprili 8, 2005.