DUNIA HAINA USAWA
Kila mtu aliyekuwa ndani ya chumba kile ikulu akapigwa na mshtuko, hawakuamini kile walichokuwa wakikiona, rais wao alikuwa chini, alianguka baada ya kupata presha mara tu alipoona pesa zote alizokuwa nazo kwenye akaunti zilikuwa zimehamishwa kwenda katika hospitali moja nchini Marekani.
Wote wakamsogelea na kumbeba, vijana wanne kutoka humohumo ikulu wakafika, wakamnyanyua na kumpeleka katika chumba maalumu ambacho kilikuwa kikitumika kama hospitali ndogo humo ndani.
Presha yake ilipanda kutoka 120/80 mmHg mpaka kufika 230/130 mmHg. Kila mmoja alishtuka, walijua kabisa kwamba kama wasingefanya kazi ya ziada basi huo ingewezekana kuwa mwisho wa rais huyo.
Alitulia kitandani, hakutingishika kiasi kwamba ilikuwa ni rahisi kusema kwamba alikuwa amefariki dunia. Macho yake yaliziba, kwa jinsi alivyoonekana ilionyesha kama tayari system ya mwili wake haikuwa ikifanya kazi kabisa.
Mkewe alichanganyikiwa, akatoka chumbani na kwenda mpaka katika chumba kile cha matibabu, alipomwangalia mume wake kitandani pale, alibaki akilia kwani hali ilionyesha kwamba tayari mume wake huyo alikuwa marehemu.
“Imekuwaje jamani! Imekuwaje mume wangu kupatwa na tatizo hili?” aliuliza Bi Estelita huku akimwangalia mume wake kitandani pale.
“Mumeo alianguka na kuonekana presha kupanda kwa ghafla sana,” alisema daktari wa ikulu ambaye muda wote alikuwa humo kuhakikisha kila kitu kinakwenda salama.
“Ataamka tena?”
“Hatujui! Ndiyo tunaendelea kupambana! Vuta subira na umuombe Mungu! Natumaini kila kitu kitakuwa salama,” alisema daktari huyo ambaye alionekana kuwa bize kupita kawaida.
***
Hali ilikuwa imechafuka katika Benki ya Geneva nchini Uswisi, mkurugenzi wa benki hiyo aliitisha kikao cha haraka sana kwa ajili ya kujadili kitu kilichokuwa kikiendelea katika ‘system’ yao ambayo ilionyesha kulikuwa na muamala ilifanyika pasipo hata mwenye akaunti kuthibitisha muamala huo ufanyike.
Lilikuwa kosa kubwa, kiasi cha dola za Kimarekani milioni mia moja zilikuwa zimehamishwa kwenda katika akaunti nyingine nchini Marekani na mbaya zaidi hata kuzizuia walishindwa kwani pesa hizo zilipelekwa huku zikiwa na ulinzi mkubwa wa kiteknolojia.
Hawakujua mtu aliyefanya jambo hilo, vichwa vyao vilichanganyikiwa na wakati mwingine kuhisi kwamba kulikuwa na wafanyakazi ambao waliihujumu benki hiyo kitu ambacho kila mmoja alikana kufanya tukio hilo.
Lilikuwa tatizo kubwa, walitakiwa kupambana nalo kwa haraka sana hata kabla watu wengine hawakujua kilichokuwa kimetokea. Katika chumba kile kidogo kilichokuwa kikifanyika mkutano, mkurugenzi wa benki hiyo, Bwana Edward Peterson alivimba, kila kitu kilichokuwa kimetokea, kilimtia hasira.
“What the hell wrong?” (kuna tatizo gani?) aliwauliza viongozi wa benki hiyo akiwemo meneja mkuu, Bwana Linderfock.
Hakukuwa na mtu aliyejua kilichokuwa kikiendelea, walichokifanya ni kuwasiliana na watu wa IT hapohapo benki na kuanza kuzungumza nao. Wao wenyewe hawakujua kitu kilichokuwa kikiendelea, kulikuwa na mtu alikuwa ameingia kwenye database yao na kubana kila kitu, mafaili ya wateja wote yalifichwa kwa saa kadhaa na yalipokuja kuachiwa, tayari muamala ulikuwa umefanyika.
“Kweli hamuwezi kumgundua mtu aliyefanya hivyo?” aliuliza Bwana Peterson huku akiwaangalia.
“Tunahisi tutaweza kufanya hivyo! Cha kwanza tuzizuie pesa hizo kutoka kwenye akaunti ya hiyo hospitali,” alishauri jamaa mmoja.
Hilo ndilo lililofanyika, wakafanya mawasiliano na Bank of America na kuwaambia kilichokuwa kimetokea kwamba pesa zilizokuwa zimeingia katika akaunti yenye namba 08637621905 zilitakiwa kuzuiwa haraka iwezekanavyo kwani zilikuwa zimechukuliwa kiwizi kwenye benki kuu nchini Uswisi.
“Hakuna shida! Ila kwa jinsi zilivyo, nadhani hakuna mtu ambaye atakuwa na uwezo wa kuzitoa zaidi ya mhusuka tu, sisi tunazuia, ila hata mkisema tuzirudishe, tutashindwa kwa kuwa hata zilivyoingia tu, hatujui zimeingiaje,” alisema meneja wa Bank of America.
Hawakutaka kukubali, wakawasiliana nna watalaamu wa mambo ya IT na kuwaambia kilichokuwa kimetokea, kila mtu aliamini kwamba kazi hiyo ilikuwa ni rahisi sana kwani kama kulikuwa na virusi vilivyokuwa vimefanya figisu kisha kuhamisha pesa hizo basi vingewezwa kuangamizwa na kila kitu kurudishwa kama kilivyokuwa.
Vijana kumi na mbili kutoka nchini China wakafika nchin Uswisi kwa ajili ya kuifanya kazi hiyo. Walikuwa wataalamu waliobobea, waliokuwa akifanya kazi chini ya serikali, walipofika hapo, wakafanya kila linalowezekana kuweka mambo sawa lakini hakukuwa na kitu walichofanikiwa.
“Imekuwaje?” aliuliza Bwana Peterson.
“Bado tunapambana! Ila tunaweza kufanikiwa,” alisema kijana mmoja aliyeitwa Shu Yang ambaye alikuwa mtaalamu wa kucheza na system lakini kazi aliyokutana nayo hapo, kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka.
****
Kuanguka kwa Rais Bokasa haikuwa siri tena, watu wengi wakafahamu kile kilichokuwa kimetokea huku sababu kubwa ya jambo hilo likiwa limefichwa kabisa. Watu walishangaa, hawakujua kitu gani kilikuwa kimetokea mpaka rais huyo kuanguka na kuwa kwenye hali mbaya.
Si kila mtu aliyekuwa akihuzunika, asilimia kubwa ya Watanzania walikuwa wakifurahia, hawakuamini kilichotokea, wakapiga magoti na kumuomba Mungu kwamba kama ingewezekana rais huyo asifumbue macho yake, afe hapohapo kitandani kwani kwa maisha yaliyokuwa yakiendelea, kila mtu alikuwa akiyachukia.
Taarifa tofautitofauti zilikuwa zikiendelea kutolewa kutoka ikulu kwamba rais huyo alikuwa akiendelea vizuri. Taarifa hizo ziliwauma watu wengi kwani kusudio lao kubwa lilikuwa ni kumuona akifa kitandani pale kwani waliamini kwamba kama angekufa basi ingekuwa rahisi sana kwa maisha ya Watanzania wengi kubadilika.
Madaktari hawakutulia, kila daktari bingwa akaitwa kwa ajili ya kumtibu rais huyo, kila mmoja alikuwa akitaka kupewa sifa kwamba yeye ndiye aliyefanikisha mpaka rais huyo kupona ugonjwa huo.
Matibabu yaliendelea lakini hakuna aliyefanikiwa na hatimaye kusafirishwa kuelekea nchini India katika Hospitali ya Ganga kwa ajili ya kupatiwa matibabu zaidi.
Mpaka muda huo, hakukuwa na aliyekuwa na uhakika kwamba rais huyo angeweza kusimama tena, tangu alipoanguka na kupoteza fahamu hakuwa ameyafumbua macho yake japokuwa mapigo yake ya moyo yalikuwa yakiendelea kudunda kama kawaida.
Mitaani kulikuwa na stori nyingi juu ya tukio hilo. Kuna wengine walisema kwamba alipigwa na mkewe, wengine wakasema kwamba rais huyo alianguka akiwa bafuni, wengine walisema kwamba alitembea na mke wa mtu hivyo mwenye mume kuamua kumroga.
Hakukuwa na mtu aliyejua ukweli ila waliamini kwamba kila kitu kingewekwa wazi katika Akaunti ya Mabadiliko ya Kweli kwani mtu huyo alionekana kama ofisa wa usalama wa taifa kwa jinsi alivyokuwa akipata taarifa nyingi tena kwa wakati.
Baada ya siku mbili tangu rais aanguke na kupoteza fahamu ndipo Godwin akaandika katika akaunti ile kila kitu kilichokuwa kimetokea kwamba yeye ndiye aliyesababisha rais huyo aanguke na kuumiza vibaya baada ya kuhamisha pesa zake alizowaibia wananchi kuwapelekea wagonjwa waliokuwa katika Hospitali ya St. Lucas nchini Marekani.
“Niliamua kuhamisha pesa zake zote katika akaunti yake iliyokuwa katika Benki ya Geneva, pesa zote hizo niliamua kuzipeleka katika Hospitali ya St. Lucas iliyokuwa nchini Marekani, sababu ya kufanya hivyo ni kwamba pesa si zake, ni pesa zangu, zako, zetu wote, tunalipa kodi, yeye ndiye ambaye aliamua kuzichukua kwa manufaa yake, sasa nimeamua kuziondoa kutoka kwake,” aliandika Godwin.
Hakukuwa na mtu aliyehuzunika, kila mmoja alifurahi kwani kwa kilichokuwa kimetokea, wote waliona kwamba rais huyo alistahili kufanyiwa kile alichofanyiwa.
Wananchi walikuwa wakiumia, kodi zilikuwa juu, ziliwaumiza kupita kawaida kiasi kwamba wengine hawakuona matunda ya kazi waliyokuwa wakiifanya ila kwa kuwa pesa zile walizokuwa wameibiwa kwa miaka mingi ziliondolewa kutoka kwa mbaya wao, walibaki wakimsifu Godwin kwa kile kilichotokea.
Viongozi wengine waliokuwa wameficha pesa zao huko wakashikwa na hofu na kuona kwamba kama wasingefanya kila liwezekanalo kuhamisha pesa hizo basi hata nao pesa zao zingechukuliwa na kupelekwa sehemu nyingine.
Walikuwa mawaziri watano, wakapigiana simu na kujadiliana ni kitu gani walitakiwa kufanya ili kuhakikisha pesa zao zinabaki salama katika mikono yao. Wakakubaliana kwamba ilikuwa ni lazima kuzihamisha pesa hizo kisiri kwenda kwenye benki nyingine nchini Tunisia ambapo zingewekwa kwa mtindo wa kuanzishwa taasisi ndogo ya Kiislamu ambayo iliweka kambi huko kwa ajili ya kusambaza misaada kwa watoto yatima na wanawake wagonjwa.
Wakati wakipanga mipango yao, hawakujua kama simu zao zilikuwa zikidukuliwa na Godwin ambaye alikuwa akifuatilia kila kitu, alipogundua kwamba viongozi hao walikuwa na mpango huo wa kuhamisha pesa zao na kupeleka katika moja ya benki nchini Tunisia, akaanza kucheza nazo kwa ajili ya kuzificha kama alivyomfanyia Rais Bokasa.
“Niwaambie tu kwamba viongozi watano waliokuwa wakiwasiliana jana kwamba watahamisha pesa zao kwenda kwenye moja ya benki nchini Tunisia, mpango wenu umekwamba kwani mpaka inafika asubuhi, hamtoweza kuziona pesa zenu,” aliandika Godwin katika akaunti yake kitu kilichowafanya watu wote kushangaa kwamba jamaa alikuwa akinasa vipi mawasiliano ya viongozi hao kiasi cha kuwatia hofu.
Alichokisema ndicho kilichofanyika, siku hiyohiyo akazizuia pesa za viongozi hao. Walipokuwa wakiingia, waliziona lakini walipotaka kufanya miamala, pesa hazikuwa zikionekana.
Haraka sana wakawasiliana na Mkurugenzi Peterson na kumwambia kilichokuwa kikiendelea. Hakuamini, alichanganyikiwa kwani Wachina aliokuwa amewaita kufanya kazi, walikuwa wakihakikisha Rais Bokasa anarudishiwa pesa zake, sasa kabla kazi hiyo haijafanyika na kukamilika, tayari kulikuwa na kesi nyingine, haikuwa kwa mtu mmoja, kwa wateja wao watano kiasi kwamba yeye mwenyewe hakujua afanye nini.
“Hebu subiri kwanza. Mnanichanganya,” alisema Bwana Peterson.
“Tunajua! Ila kwa nini pesa zetu hazitoki!”
“Kuna mtu amedukua akaunti zenu!”
“Inawezekanaje?”
“Naomba mnipigie baadaye. Sijui hali imekuwaje! Naomba mnipigie baadaye, tunashughulikia tatizo lenu,” alisema Bwana Peterson huku akionekana kuchanganyikiwa kupita kawaida.
Simu ikakatawa, kila kitu kilikwenda ndivyo sivyo, kilichokuwa kikiwashangaza ni namna ambavyo mtu huyo alivyoweza kupata mawasiliano yao, hawakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea.
Walisikilizia simu kutoka nchini Uswisi, hawakupigiwa, dakika zilisonga, saa likakatika, saa mbili nazo zikaenda, mpaka saa tano, bado hawakupigiwa hali iliyowapa majibu kwamba watu hao walikuwa wakiendelea kuhangaika kuhakikisha kile kilichokuwa kimetokea kinapatiwa ufumbuzi haraka sana.
“Wakati tunasikilizia huko, waambie usalama wa taifa wamtafute huyo Godwin!” alisema Waziri wa Kilimo, Abraham Ojuku.
“Wanafanya kazi hiyo mkuu. Tatizo picha zake!”
“Hakuna picha zake?”
“Ndiyo! Kwenye mitandao zipo zile za utotoni!”
“Ukubwani hakuwahi kupiga picha?”
“Hapana!”
“Hebu waambie wafuatilie, aliposhuka na ndege alitoka wapi, alikuwa anafanya nini huko. Hakikisha wanafuatilia, na kama alikuwa akisoma chuo, alisoma chuo gani, tukipata yote hayo, tutafanikiwa kwani cha msingi tupate picha yake ya ukubwani, ya utotoni hatutofanikiwa kumpata kwani anaweza akawa na ndevu nyingi kama Osama,” alisema Waziri Ojuku huku akionekana kuchanganyikiwa.
“Tunafuatilia mkuu!”
***
Usalama wa Taifa hawakutaka kutulia, waliambiwa kwamba walitakiwa kufuatilia kuhusu Godwin na siku hiyohiyo kituo cha kwanza kabisa cha kuanza upelelezi wao kilikuwa ni uwanja wa ndege kulipokuwa na ofisi ya Shirika la Ndege la Orange.
Wakafika katika ofisi hizo na kitu pekee walichokuwa wakikihitaji ni taarifa juu ya msafiri ambaye alisafiri kwa ndege yao siku ya Jumamosi na hivyo kuwapa orodha ya majina ya watu waliosafiri kwa ndege hiyo.
Haraka sana wakaanza kupitia majina ya abiria hao, wala hawakuchukua muda mrefu wakaliona jina la Godwin Mapoto ambaye alikuwa amesafiri huku pembeni yake kukiwa na msichana mwingine aliyeitwa kwa jina la Manka.
Ilionyesha kabisa kwamba Godwin alitokea Dubai katika ndege iliyotokea nchini Japan ambapo huko hawakujua alikwenda kufanya nini kwani kutokana na Waafrika wengi kwenye katika nchini za Mashariki ya Kati, iliwafanya kutokundua kama alikwenda kibiashara au kusoma.
“Ni lazima tusafiri kwenda huko, inawezekana tukapata taarifa zaidi,” alisema Boniphace Ngumije, mmoja wa wanausalama walioambiwa wafuatilie kila kitu kuhusu Godwin na ikiwezekana waweze kupata picha zake.
Wakatoa taarifa kwa mkuu wao na kumwambia kwamba walikamilisha theluthi ya upelelezi wao na kugundua kwamba mtu waliyekuwa wakimtafuta alikuwa ametokea nchini Japan lakini hawakujua dhumuni hasa la mtu huyo kuwa nchini humo.
“Nendeni mpaka huko, hakikisheni mnafanya kila linalowezekana kupata picha zake,” alisema mkuu wao.
Wakasafiri na kuelekea huko, njiani, walikuwa na mawazo tele, walikuwa wakimtafuta mtu ambaye waliamini kwamba alikuwa nchini Tanzania. Walikuwa wakijadiliana juu ya kitu gani kilitakiwa kufanyika mpaka kuhakikisha wanapata picha za mtu huyo na kurudi nazo nchini Tanzania.
Walichukua saa zaidi ya ishirini mpaka kufika Japan ambapo wakachukua chumba, wakalala na siku iliyofuata ilikuwa ni kufuatilia katika ofisi za Shirika la Ndege la Orange ili kupata kila kitu kilichokuwa kikiendelea.
Kama ilivyokuwa kule Tanzania, napo wakapewa jina la mtu huyo, namba ya tiketi yake lakini kuhusu kila kitu kilichokuwa kikiendelea, kupata picha yake ilikuwa ni lazima kuwasiliana na ubalozi wa Japan nchini Tanzania kuwaambia kuhusu mtu huyo.
“Taarifa hazionyeshi kitu chochote kile, huwa tunazihifadhi katika kompyuta zetu, cha ajabu taarifa za mtu huyo hazipo. Mna uhakika alikuwa Japan?” aliuliza balozi wa Japan nchini Tanzania ambaye alikuwa akitumiwa taarifa zote.
“Ndiyo! Au alizifuta?”
“Haiwezekani! Hakuna mtu anayeweza kuingia kwenye kompyuta zetu,” alisema balozi huyo pasipo kujua kwamba taarifa zote kuhusu Godwin, mwanaume huyo alizifuta.
Hawakutaka kukata tamaa, vijana waliokuwa Japan wakapewa taarifa kuanza kufuatilia katika vyuo nchini humo kuona kama kulikuwa na mwanafunzi aliyekuwa na jina hilo ambaye alimaliza chuo siku chache zilizopita.
Walizunguka kwenye kila chuo, jina walilokuwa wakiliangalia lilikuwa ni Godwin tu. Waliwapata vijana wengi lakini hawakuwa mtu waliyekuwa wakimtafuta kwa nguvu zote lakini baada ya kwenda katika Chuo Kikuu cha Waseda kilichokuwa Tokyo, wakaambiwa kwamba kulikuwa na mwanafunzi aliyekuwa na jina hilo, aliitwa Godwin Mapoto.
“Ndiye huyohuyo! Hebu tunaomba data zake zote,” alisema Boniphace huku akionyesha tabasamu, walikaa siku tatu nchini humo na hawakupata chochote kile, kitendo cha siku hiyo kupata mwanga, kiliwafurahisha.
“Alikuwa mwanafunzi wa mwisho mweusi kusoma katika chuo hiki. Alichukua PhD yake siku chache zilizopita. Alikuwa raia wa Tanzania. Data zake hizi hapa,” alisema mkuu wa chuo hicho huku akiwaonyeshea mwanaume huyo.
“Safi sana.”
“Ni mtu makini sana. Ana akili nyingi mno, inasadikiwa ndiye mtu mwenye akili kubwa na kucheza na kompyuta, mambo yote kuhusu programming, networking, huyo ndiye alikuwa balaa,” alisema mkuu wa chuo, hakuishia hapo akaanza kuwapa simulizi kuhusu Godwin ambayo iliwasumbua wataalamu wengi, hasa baada ya kuficha mafaili ya chuo.
Hawakuamini kama kungekuwa na Mtanzania ambaye angekuwa na akili kiasi hicho. Walibaki wakiangaliana na kukiri kwamba mtu waliyekuwa wakidili naye hakuwa mtu wa kawaida hata kidogo na ndiyo maana hata ile akaunti yake ilikuwa ni vigumu sana kufutwa na watu wengine.
“Sawa. Tunashukuru sana. Naomba kuuliza swali!” alisema Martin, kijana aliyeongozana na Boniphace.
“Uliza.”
“Mbona kwenye taarifa zake hakuna picha yake?” aliuliza Martin.
“Picha yake? Picha yake ilikuwepo hapa. Sijui imekwenda wapi lakini ilikuwepo hapa,” alisema mkuu wa chuo huku akishangaa, taarifa zote za wanafunzi zilikuwa zikiwekwa na picha ila cha kushangaza kwenye faili la Godwin hakukuwa na picha.
“Una uhakika picha zilikuwepo?”
“Ndiyo! Ni juzi tu zilikuwepo.”
“Tunaweza kuzipata?”
“Haina shida.”
Kuzipata picha za Godwin hakukuwa na tatizo lolote lile kwani kulikuwa na picha nyingi ambazo zilikuwa katika tovuti ya chuo watu walikuwa wamepiga. Mkuu huyo wa chuo alifungua tovuti hiyo na kuangalia picha zote, kitu cha ajabu kabisa ambacho kilimchanganya, kote huko zile picha zote ambazo mwanaume huyo alitokea, hazikuwepo kitu kilichowachanganya.
Boniphace na mwenzake hawakutaka kubaki Japan, walimwambia mkuu wao kwamba kule walipokuwa wamekwenda hawakufanikiwa kupata kile walichokuwa wakikihitaji ila kwa taarifa tu ambazo walizipata kutoka kwa mkuu wa chuo zilieleza kwamba mtu waliyekuwa wakimtafuta alikuwa hatari sana katika kutumia kompyuta.
Hilo likawafanya kukata tamaa kupata picha zake, walichokifanya ni kuchukua picha zilezile alizokuwa mtoto mdogo na kuzisambaza katika vituo mbalimbali vya polisi ili kama wangemuona mtu aliyekuwa akifanana na mtoto huyo wamchukue na kumpeleka kituoni mara moja.
“Mmh! Hivi tunaweza kufanikiwa kweli? Sidhani ila haina jinsi, ni lazima tutii kile tulichoambiwa!” alisema mkuu wa Kituo cha Polisi cha Mkwajuni.
****
Godwin hakuwa na hofu hata kidogo, kwa kila kitu kilichokuwa kikiendelea kwake kulikuwa na amani tele. Alikuwa akiichanganya serikali, kila siku alikuwa akiwapa taarifa watu kuhusu madudu mengi yaliyokuwa yakitokea nchini Tanzania.
Watu walimshukuru ingawa kwa upande wa pili serikali ilikuwa ikichomwa na mbaya zaidi hakukuwa na mtu aliyekuwa akijua mahali mwanaume huyo alipokuwa kwani kila walipojaribu kuidukua simu yake kujua alipokuwa, iliwaonyesha kwamba ilikuwa Urusi na wakati mwingine kuwaonyesha ilikuwa Dubai.
Walichanganyikiwa, walituma maofisa wa usalama wa taifa, waliamini kwamba mwanaume huyo alikuwa katika mtaa mmoja wa kitajiri akila maisha hivyo kuwatuma watu wengi huko. Ni kama Godwin alijua kwani mara baada ya kutoka hotelini, akaondoka na kuanza maisha katika Mtaa wa Tandale kwa Mtogole, akapanga katika chumba kimoja chakavu, akanunua nguo za mtumba Tandale Sokoni na kila siku kazi yake ilikuwa ni kuendeleza harakati zake katika akaunti yake ya Mabadiliko ya Kweli.
“I want to know who killed my parents and sister,” (nataka kumjua aliyewaua wazazi wangu na dada yangu) aliandika Godwin kwenye akaunti yake kitu kilichozua maneno mengi na wengine kugundua kwamba inawezekana Godwin alikuwa akifanya hayo yote kwa kuwa kulikuwa na watu waliokuwa wameiteketeza familia yake.
Maoni yalikuwa mengi, wengi walikuwa wakiuliza kilichokuwa kikiendelea mpaka kuandika maneno hayo ambayo yaliwasisimua watu wengi. Kila swali alilokuwa akiulizwa, alilijibu pasipo tatizo lolote lile kitu kilichowafanya watu kugundua maovu makubwa yaliyokuwa yakifanywa na serikali iliyokuwa madarakani.
“Nilijua tu! Hii serikali magumashi sana. Inawezeje kuiangamiza familia nzima. Kwanza huyu jamaa ni mtoto wa familia ipi? Baba yake alikwishawahi kuwa kiongozi yeyote yule?” alihoji jamaa mmoja kwenye Mtandao wa Facebook huku akiwa ameipiga picha ile posti aliyoiandika Godwin.
Posti hiyo ikaibua mambo mengi, kila mtu mitaani alikuwa akizungumza lake. Kwa Godwin hakutaka kuzungumzia kitu chochote kwa undani ila alichokifanya ni kutafuta vifaa vyote vya kuchorea tatuu na kujichora tatuu kifuani iliyokuwa na maneno hayo aliyoandika kwenye akaunti yake.
“Hii ni vita ya kisasi na kamwe haitomuacha mtu salama,” aliandika Godwin na kuongezea maneno mengine mengi yaliyosomeka:
“Huu utakuwa mwezi wa viongozi wengi kujiua. Sitowaua mimi, ila ninatarajia viongozi wengi watakwenda kujiua. Kuna data nilikuwa nazikamilisha, zipo poa. Ninawahakikishieni kwamba viongozi wengi watajiua, si kwamba ninapenda kuwaua, hapana, watajiua wao wenyewe kwani kashfa zitakawatafuna, hakika hawatoona thamani ya kuishi.
“Kama mlikuwa hamjui, kuna msichana aliitwa Vanessa Fabian, msichana mrembo ambaye ndiye atasababisha viongozi hao kujiua. Unajua kwa nini? Nitakuandikia Jumatatu kila kitu kilichotokea kwa msichana huyu, wengi mtahuzunika ila mwisho wa siku mtatabasamu, itakuwa historia yenye kumgusa kila mtu. Unataka kuifahamu historia ya msichana huyo, nitawaandikia Jumatatu mahali haphapa,” ilisomeka posti hiyo ndefu.
Kila mtu akawa na hamu, wengi walitaka kumjua huyo Vanessa, alikuwa nani na alibeba historia gani yenye kuhuzunisha ambayo ingewafanya viongozi wengi wa serikali kujiua?
Maoni yakawa mengi mno na kila mmoja alionekana kuguswa kwa kile kilichokuwa kimeandikwa hivyo watu wengi kuwa na hamu ya kutaka kufahamu. Ni mambo gani yalitokea ambayo yangepelekea viongozi wengi kujiua? Kila mmoja alitaka kujua.
***
Godwin hakuwa mtu wa kutoka sana nje, alikuwa mtu wa kukaa ndani kila wakati. Japokuwa akaunti yake ilikuwa maarufu sana lakini hakukuwa na mtu aliyekuwa akijua kwamba yule mwanaume aliyepanga kwenye nyumba ile mbovumbovu ndiye yuleyule aliyekuwa akiinyima furaha Serikali ya Tanzania.
Kazi yake kubwa ilikuwa ni kudukua mawasiliano yote yaliyokuwa yakifanyika nchini Tanzania hasa kwa viongozi wa nchi hiyo. Alijua siri nyingi, mikataba ya siri iliyokuwa imesaniwa ambayo iliruhusu madini kuondoka, pesa za mitambo ya umeme, kila aina ya uchafu uliokuwa ukifanyika data zake alikuwa nazo.
Alitaka kuandika historia kuhusu msichana Vanessa, hakuwahi kukutana na msichana huyo ila historia yake alikutana nayo katika barua pepe ya Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Bwana Samson Mwinyimkuu.
Ilikuwa ni historia ya msichana Vanessa, msichana aliyekuwa mrembo mno ambaye aliamua kuiandika historia ya maisha yake na kumtumia waziri huyo ambaye aliiweka katika barua pepe yake na kuifanya siri nzito.
Godwin aliipata barua hiyo, ilikuwa ni ndefu mno lakini hakuwa na jinsi, ilikuwa ni lazima kuiandika kwa ufasaha na kuiweka katika akaunti ile.
Watu walikuwa wakisubiri kwa hamu kubwa, kuanzia siku ya Jumamosi mpaka Jumatatu ilionekana kuwa kama mwezi mzima. Kila mmoja alitaka kujua kile kilichokuwa kimetokea kwa msichana huyo mrembo, hawakujua alikuwa Vanessa yupi kwani kwa kipindi hicho kulikuwa na wasichana wengi wenye jina hilo waliokuwa maarufu sana.
Mara baada ya Waziri Mwinyimkuu kuona posti hiyo, haraka sana akaingia katika barua pepe yake ili kuangalia kama ilikuwepo, aliiona ila hofu yake kubwa ilikuwa ni juu ya msichana huyo ambaye kwa kipindi hicho alikuwa marehemu, je, alimtumia Godwin barua hiyo hata kabla hajafa?
Wakati akiwaza hayo, kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka, alikuwa na presha kubwa, alikuwa akiheshima na kila alipokuwa akipita watu walimpigia makofi, alikuwa mchapakazi ambaye kila siku viongozi wengi wa serikali waliambiwa waige utendaji kazi wake mkubwa.
Hakujua ni kitu gani kingetokea mara baada ya uovu wake aliomfanyia Vanessa kwa kushirikiana na viongozi wengine kuwekwa wazi. Alitetemeka, mapigo ya moyo wake yalidunda kupita kawaida.
Watanzania wengi waliona Jumatatu kuwa mbali lakini ni yeye tu ndiye aliyeiona siku hiyo kuwa karibu sana. Mishale ya saa yake ilikimbia kwa kasi ya ajabu, alijiona akiwa nje, kwenye umati mkubwa huku watu wakimwangalia, walimcheka na kumdhihaki na watu wengi kutamani kuona mwanaume huyo akifa kutokana na uovu aliokuwa ameufanya.
“Ngriiiii...ngriii...” alishtushwa na mlio wa simu, haraka sana akaichukua na kuipeleka sikioni, kwa jinsi alivyokuwa amechanganyikiwa, hata kuangalia jina la mpigaji hakuangalia.
“Mwinyimkuu! Upo wapi?” aliuliza mwanaume wa upande wa pili.
“Ny..um..ban..i..” alijibu Mwinyimkuu huku akitetemeka.
“Umeona kilichopostiwa? Ile barua pepe uliifuta kweli au uliihifadhi kama jumba la makumbusho?” aliuliza mwanaume wa upande wa pili, kama alivyochanganyikiwa waziri huyo hata na yeye alikuwa amechanganyikiwa.
“Sikuifuta!”
“Hukuifuta? Kwa nini? Isije kuwa huyu mtu anataka kuiandika ile historia ya yule binti!” alisema jamaa huyo.
“Sidhani! Hawezi! Atakuwa anatutisha tu!”
“Mh! Ya kweli hayo? Sasa amejuaje kuhusu Vanessa?” aliuliza.
“Sijajua kabisa. Ni bora kama yule msichana angekuwa hai tungemuuliza. Ibra, naomba unipigie baadaye,” alisema Mwinyimkuu na kukata simu.
Hakuishia kupokea simu ya Ibra tu bali alipokea simu za viongozi watatu ambao wote hao walimuuliza kuhusu kile kilichokuwa kimeandikwa, kila mmoja alikuwa na hofu kubwa na kuona kabisa kwamba uovu wote waliokuwa wamemfanyia msichana huyo sasa ulikuwa ukienda kujulikana na kila mtu.
“We are finished,” (tumekwisha) aliandika mwanaume mmoja ambaye naye alishirikiana na Mwinyimkuu katika kila kitu kuhusu msichana Vanessa.
Jumatatu asubuhi tayari watu walikuwa mbele ya kompyuta zao huku wengine wakiwa katika simu zao. Walitaka kushuhudia ni kitu gani kilikuwa njiani kuandikwa. Kazini, kila mfanyakazi alikuwa na simu yake, hakutaka kuiweka chini, walitaka kusoma kuhusu msichana huyo mwenye historia ya kusikitisha mno.
Saa 3:00 asubuhi Godwin akaposti sehemu ya kwanza kuhusu msichana huyo. Alianza kusimulia historia ya maisha yake, jinsi alivyokuwa kwenye maisha ya kimasikini mpaka pale alipoamua kumfuata Mwanyimkuu kwa ajili ya kumsaidia.
Mwanaume huyo alipofuatwa na msichana huyo, aliahidi kumsaidia kwa moyo mmoja lakini badala ya kufanya hivyo, akaanza kwa kumuomba penzi. Kilikuwa ni kitu ambacho Vanessa alimkatalia kwa nguvu zote kwani hakuwahi kufanya mapenzi na mwanaume yeyote, alichokuwa akikihitaji kilikuwa ni msaada tu kwa kuwa aliamini mwanaume huyo alisaidia watu hivyo hata yeye angemsaidia.
“Bila penzi hakuna msaada.”
“Ila mama anaumwa sana. Naomba unisaidie, umasikini unatutesa, bila pesa, mama yangu atakufa, bila pesa, wadogo zangu watakufa kwa njaa, hatuna kitu, maisha yetu ni masikini, naomba utusaidie,” ilisema sehemu ya posti ile alipokuwa akizungumza msichana Vanessa.
“Bila penzi, mama yako atakufa, na bila penzi wadogo zako watakufa pia,” alisema mzee huyo.
Vanessa hakutaka kuona mama yake akifa, alipenda kuona akiendelea kuishi miaka yote na hivyo kumpa penzi mzee huyo. Alisikia maumivu makali kwa kuwa ilikuwa ni siku yake ya kwanza. Kiasi cha pesa alichokuwa akikihitaji hakukipata kutoka kwa mzee huyo zaidi ya kupewa asilimia ishirini ya kile alichokiomba.
Mzee Mwinyimkuu akatumia pesa na madaraka kumchezea msichana huyo, alimtumikisha kingono na alipoona kwamba ameridhika, akawaambia wengine matatizo ya msichana huyo na hivyo nao kumfanyia mchezo huo msichana huyo mdogo. Wanaume hao wengine watatu walikuwa ni Waziri Mamboleo, Kijuku na Mburu.
Msichana wa miaka kumi na sita akatumikishwa kingono na wanaume wanne, hawakuwa na huruma, waliendelea kumchezea pasipo kumsaidia na wakati alipokuwa akiwatisha kwamba ataenda polisi kushtaki, walimwambia kwamba wangemuua na hivyo kuogopa.
Ni maisha yaliyoogepesha na kusisimua mno. Mmoja kati ya wanaume hao alikuwa ameathirika ugonjwa wa Ukimwi, akamuambukiza Vanessa na kuwaambukiza wanaume hao wote.
Ilikuwa ni historia ndefu ambayo Godwin aliiandika kimafungumafungu, hakutaka kuishia hapo, alihakikisha anaweka kila kitu wazi, hawakujua majibu ya vipimo vya Ukimwi alivitoa wapi, aliweka karatasi za majibu ya damu zao baada ya kupima damu hospitalini.
“Mungu wangu! Kumbe wameathirika! Wamemuambukiza na mtoto yule jamani!” alisema jamaa mmoja.
Wanawake waliokuwa wakisoma historia ndefu ya msichana huyo hawakuvumilia, walikuwa wakilia kwa maumivu makali mioyoni mwake, walisisimka, hawakuamini kama kungekuwa na watu waliokuwa na hali ya kinyama kama viongozi hao.
“Hatuwezi kukubali! Tutaandamana kuwataka wajiuzulu,” alisema jamaa mmoja.
Vijana wenye msimamo, walioumizwa hawakutaka kubaki nyumbani kwao. Ilikuwa kashfa kubwa iliyolitetemesha taifa kwa ujumla, viongozi ambao kila siku walikuwa wakiheshimiwa kila walipopitwa kumbe walikuwa na maisha ya kinyama, kwa kutumia pesa na nguvu zao waliamua kumdhalilisha Vanessa kingono.
Msichana huyo alikufa miaka miwili iliyopita kwa ugonjwa huo ambao watu hawakujua aliupata wapi na mbaya zaidi, viongozi hao nao walikwenda kuhudhuria msiba huku wakijifanya kuwa na huzuni mno.
“Siwezi kuishi! Siwezi kuivumilia aibu hii,” alisema mwinyi mkuu, historia ndefu aliyokuwa ameambiwa na Vanessa ndiyo ambayo ilikuwa ikionekana katika akaunti ya Mabadiliko ya Kweli.
Hakujua mahali mtu huyo alipoipata kwani mara baada ya Vanessa kuiandika, akamtumia na alikuwa na uhakika kwamba hakutumiwa mtu mwingine kwa kuogopa kuuawa, sasa ilikuwaje mpaka mtu mwenye akaunti hiyo kuipata?
Aliumia, alijutia kila kitu alichokifanya maishani mwake. Hakujua Tanzania ingemuangaliaje, hakujua familia, ndugu, jamaa na marafiki wangemuangaliaje, uamuzi alioufanya ulikuwa ni mmoja tu, kujiua kwa kujipiga risasi.
“Mwinyimkuu amejiua!” alisema jamaa mmoja.
“Kweli?”
“Ndiyo! Hiyo ni breaking news wameiandika Global. Cheki braza,” alisema jamaa huyo huku akimuonyeshea simu mwenzake.
Huo ulikuwa ni kama mwanzo, ilikuwa ni fedhea, wahusika wote waliumia, hakukuwa na hata aliyebaki, ili kuogopa aibu kubwa mbele yao, wakaamua kujiua kwa vifo tofauti, yule alijipiga risasi, mwingine akajinyonga, mwingine akanywa sumu na mwingine akaamua kujichinja.
“Yapo mengi tu! Nilipowaambia nimekuja Tanzania kufanya kazi namaanisha nimekuja kufanya kazi. Nitaweka wazi mambo mengi sana! Nyie subirini, kuna vitu vingine havielezeki, nitawaelezea mpaka wachungaji ambao wanashirikiana na viongozi serikalini kuwaibia wananchi. Unajua wanawaibia vipi na wachungaji hao ni wakina nani? Nitawaandikia kesho mahali hapa. Lengo ni kuisafisha nchi, hilo tu,” aliandika Godwin, kwa kipindi hicho, kila kitu alichokuwa akikiandika kwenye akaunti ile alikuwa na uthibitisho nacho
Kwa kile kilichokuwa kimetokea, kila kona ikawa gumzo. Akaunti ile iliwasumbua watu wengi, katika nchi nyingine Afrika Mashariki kila mmoja alikuwa akizungumza lake, wengi walilaumu kwa kilichokuwa kimetokea, Tanzania ikaingia doa, kila kona ilizungumziwa vibaya lakini pamoja na hayo yote, watu wote walikuwa wakimsifu mtu aliyekuwa akiweka wazi madudu yote yaliyokuwa yakitokea nchini humo.
Je, nini kitaendelea?