Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, imethibitisha kuwa ndiyo iliyotoa agizo la kusitishwa kwa maandamano na operesheni Sangara ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) mpaka pale zoezi la sensa ya watu na makazi litakapokamilika.
Msaidizi wa Msajili wa Vyama vya Siasa, Piencia Etanga, alisema kuwa ofisi yake kama mlezi wa vyama ilitoa taarifa za maandishi kwa vyama vya siasa kuvitaka kusitisha mikutano na maandamano yote ili kupisha zoezi la sensa lililoanza Agosti 26, mwaka huu.
Mikutano na maandamano yanavuta watu wengi, jambo ambalo lingevuruga zoezi la sensa, kwa hiyo ofisi ya Msajili kama mlezi wa vyama vyote, ilichukua jukumu lake kwa kuviandikia vyama kuviomba kusitisha mikutano na maandamano ili zoezi la sensa lifanyike vizuri kwa sababu lina umuhimu mkubwa, na vyama vilituelewa kwa taarifa hiyo, alisema Etanga.
Wafuasi wa Chadema mjini Iringa juzi walilalamikia kufutiwa maandamano yao huku Jeshi la Polisi mkoani humo likidai kuwa wanatimiza agizo kutoka kwa Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, John Tendwa.