Elections 2010 Dkt Shein Kitanzini!

Buchanan

JF-Expert Member
May 19, 2009
13,199
1,969
• WAPINZANI WAKE WAMKAMIA KUMG'OA DODOMA

na Mwandishi wetu

KINYANG’ANYIRO cha uteuzi wa urais Zanzibar, kimeingia katika hatua mpya baada ya kuwapo mkakati wa kutaka kumwengua Dk. Ali Mohamed Shein kwa madai kuwa hana sifa.
Mkakati huo ambao Tanzania Daima Jumatano imeunasa, unaandaliwa na kundi la wapinzani wake kisiasa katika kuwania kiti hicho ambapo harakati zake wiki hii zimehamia mjini Dodoma kutakakofanyika vikao vya uteuzi.

Tayari wapambe na mashabiki wa wagombea 11 wanaowania uteuzi wa kiti cha urais visiwani Zanzibar kinachoshikiliwa na Rais Aman Abeid Karume, wamewasili mjini Dodoma kuwapigia debe wagombea wao mbele ya wajumbe wa Kamati Kuu (CC) na Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (NEC).

Duru za siasa kutoka mjini Zanzibar na Dodoma kwa nyakati tofauti, zimethibitisha kwamba wapinzani wa Dk. Shein anayepewa nafasi kubwa kutokana na kuungwa mkono na vigogo wa serikali, wamekamia kutumia sheria ya Katiba ya Zanzibar kumuengua kwenye kinyang’anyiro hicho.

Vyanzo vyetu vya habari vilisisitiza kuwa Katiba ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ya mwaka 1984, ndiyo itakayotumika kumbana Makamu huyu wa Rais wa Muungano.

Kwa mujibu wa Katiba hiyo toleo la mwaka 2003, iliyopitishwa Julai 17, sura ya 15, kifungu cha pili kinataja sifa za mtu anayefaa kuwa Rais wa Zanzibar.

Kifungu hicho chenye sehemu (a) hadi (d), kinataja sifa za mtu anayefaa kuwa rais wa Zanziabr kuwa ni pamoja na kuwa Mzanzibari wa kuzaliwa, awe ameshatimiza umri wa miaka 40.

Sifa nyingine ni kwamba awe na sifa za kumuwezesha kuchaguliwa kuwa Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi na sifa ya mwisho inamtaka awe mwanachama na mgombea aliyependekezwa na chama cha siasa kilichosajiliwa rasmi kwa mujibu wa sheria ya vyama vya siasa 1992.

“Katika kifungu cha 2(C), kinachosema awe na sifa za kumwezesha kuchaguliwa kuwa mjumbe wa Baraza la Wawakilishi, ndicho kitakachotumika kumbana Dk. Shein maana hana sifa hiyo,” alisema mmoja wa makada wa CCM.

Kwa mujibu wa kifungu hicho, sifa za mtu anayefaa kuchaguliwa kuwa mjumbe wa Baraza la Wawakilishi ni pamoja na kwamba awe Mzanzibari aliyetimiza umri wa miaka 21.

Sifa nyingine ambayo wapinzani wa Dk. Shein wamejipanga kumnyuka nayo ni ile ya kifungu cha 68(b) ambacho kinasema awe amejiandikisha au ana sifa za kujiandikisha katika jimbo la uchaguzi kama mpiga kura katika uchaguzi wa Baraza la Wawakilishi.

Kifungo hicho kinadaiwa kinaweza kuwa kitanzi kwa Dk. Shein kwani hakujiandikisha katika jimbo lake la uchaguzi kama mpiga kura katika uchaguzi wa Baraza la Wawakilishi.

“Kwa hiyo, Dk. Shein ana mtihani mzito wa kuteuliwa maana hakujiandikisha katika jimbo lake kama mpiga kura. Amekiweka chama na yeye mwenyewe kwenye wakati mgumu sana wa kufanya maamuzi,” alisema mmoja wa wajumbe wa NEC ya CCM.

Hata hivyo kifungu hicho cha Katiba kimewagawa baadhi ya wana-CCM hasa wanaomwunga mkono Dk. Shein kwamba hawezi kubanwa nacho.

Mmoja wa watetezi wa Dk. Shein ambaye ni mjumbe wa NEC, aliliambia Tanzania Daima Jumatano kuwa Dk. Shein hawezi kubanwa na kifungu hicho na wanaopanga kumwekea pingamizi, wameshindwa kukisoma na kukielewa vizuri.

“Waambie wasome vizuri kifungu hicho na hata nyie waandishi wasaidieni. Hicho kifungu kinasema awe amejiandikisha au na sifa ya kujiandikisha katika jimbo la uchaguzi kama mpiga kura katika uchaguzi wa Baraza la Wawakilishi.

“Kwa hiyo, kama hakujiandikisha kupiga kura katika jimbo lake, haina maana kwamba hana sifa maana kifungu kinasema awe amejiandikisha au awe na sifa ya kujiandikisha. Sifa za mtu kujiandikisha zipo na Dk. Shein anazo, hivyo hakuna kibano hapa ila watu hawajui kukitafsiri kifungu hicho cha Katiba,” alisema kada huyo.

Wakati wapinzani wake wakijipanga kumnyuka kwa kutumia kifungu hicho cha sheria, Dk. Shein tayari alishaeleza mara mbili juu ya kifungu hicho ambapo mara ya mwisho alijieleza kwenye kikao cha Kamati Maalum ya CCM, Zanzibar.

Tatizo la Dk. Shein linafanana na lile lililowahi kumkuta Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, ambapo mwaka 2007 alizuiliwa na sheha kujiandikisha katika jimbo la uchaguzi kama mpiga kura kwa madai kuwa alikuwa hana makazi maalum.

Endapo Maalim Seif angeshindwa kujiandisha, wapinzani wake kisiasa walipanga kutumia Katiba ya Zanzibar kumuengua kwenye kuwania kiti cha urais. Hata hivyo Maalim aliruhusiwa kujiandikisha.

Katika harua nyingine, wapambe wa waliomba uteuzi kuwania urais Zanzibar, wako mjini Dodoma kwa ajili ya vikao vya juu vya maamuzi vinavyotarajiwa kuanza mwishoni mwa wiki hii, mjini Dodoma.

Kama ilivyo ada ya mkutano mkuu wa CCM, mji wa Dodoma umefurika wapambe wa wagombea ambao wamekuwa wakikesha kupiga kampeni.

Tayari makada watano kati ya 11, walioomba kuteuliwa kuwania nafasi ya urais Zanzibar, wamependekezwa kwa kupewa alama za juu na kikao cha Kamati Maalum ya Halmashauri Kuu (NEC) ya Chama cha Mapinduzi (CCM).

Waliopendekezwa ni pamoja na Waziri Kiongozi Mstaafu Dk. Mohammed Gharib Bilal, Makamu wa Rais Dk. Ali Mohammed Shein, Naibu Waziri Kiongozi Shamsi Vuai Nahodha, Naibu Waziri Kiongozi Ali Juma Shamuhuna na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Haroun Ali Suleiman.

Wagombea wengine ni Balozi Ali Karume, Hamad Mshindo, Mohammed Yusuf Mshamba, Mohammed Aboud, Mohamed Raza na Mussa Omar Sheha


Source: Tanzania Daima.
 
Headline ya gazeti ina nia ya kuuza gazeti, huu ndio uandishi njaa. Nimesoma maelezo yote hakuna kitanzi hata kimoja wala sehemu ambayo inaonyesha kwamba Shein anaweza kubanwa.
 
wajinga hao.

"Katika kifungu cha 2(C), kinachosema awe na sifa za kumwezesha kuchaguliwa kuwa mjumbe wa Baraza la Wawakilishi, ndicho kitakachotumika kumbana Dk. Shein maana hana sifa hiyo," alisema mmoja wa makada wa CCM.

Kwa mujibu wa kifungu hicho, sifa za mtu anayefaa kuchaguliwa kuwa mjumbe wa Baraza la Wawakilishi ni pamoja na kwamba awe Mzanzibari aliyetimiza umri wa miaka 21.

Sifa nyingine ambayo wapinzani wa Dk. Shein wamejipanga kumnyuka nayo ni ile ya kifungu cha 68(b) ambacho kinasema awe amejiandikisha au ana sifa za kujiandikisha katika jimbo la uchaguzi kama mpiga kura katika uchaguzi wa Baraza la Wawakilishi.

Wanashindwa kuelewa hata maana ya mtu kuwa na sifa za kutimiza jambo fulani.
 
hata iweje shein hafai kalegea sana bana..kapoooza utadhani omondi/zezeta
 
Hao NEC gani hata wanashindwa kutafsiri kifungu chepesi kama hicho? Dr. Shein ana sifa zote za kuchaguliwa kuwa mjumbe wa baraza la Wawakilishi. Yeye muda wote kwasasa anaishi Dar, angeenda kujiandikisha Zanzibar ili iweje?

Watafute kifungu kingine cha kumbana lakini sio hicho wanachotumia sasa.
 
Hapa sijaona Kitanzi kwa shein labda wapinzani wa shein. Washabiki wa Dr.Bilal wanasahau kitu kimoja kuwa mtu anayeumwa na nyoka basi akiona kichaka tu anakimbia. Jamaa NEC hawasahau upinzani Komandoo aliouonyesha waziwazi dhidi ya CCM NEC sasa jamaa wanauliza mara nyingi Bilal mpambe wake Salmin atakuwa tofauti jibu wanapata no!!! Basi wanamuengua maskini. subirini mtasikia jamaa ameshinda na Shein kuteuliwa mgombea rasmi wa zanzibar
 
Mtizamo wangu kwa hicho kipengele cha kujiandikisha kinamnyima sifa za kuwa rais wa zanzibar. Itakuwa je rais apigiwe kura na watu wakati yeye hawezi piga kura maana hakuna alikojiandikisha. Ama anafikiri kwa kuwa anakaa dar atakuwa amejiandikisha huko? Sidhani kama inawezekana kupiga kura Dar ya urais wa zanzibar. Inaonekana shein hakuwahi kufikiri kugombea Smz ila ameshtukizwa na watu wachache wanaotaka kumweka pale, na hicho ndicho kitu Shein anachoweza. Ni mzuri sana wa kutumwa lakini Shein hana uwezo wa kimaamuzi yeye mwenyewe. Umefika wakati wa wazanzibar kupewa mtu wanaemtaka sio kulazimishiwa mtu na viongozi wa bara. Safari hii huko dodoma wakiwalazimishia mtu nawashauri wazanzibar kuhamia CUF na kumbwaga huyo mjumbe wa vigogo wachache.
 
Kitu kimoja tu ambacho kinaweza kumwangusha Dr.Shein - Mpemba.
Kama alivyoangushwa Salim A. Salim sioni sababu nyingine ya msingi ambayo inaweza kutolewa hasa baada ya Muafaka baina ya Karume na Seif - Dr.Shein to be President, makamu wa rais awe Karume na waziri kiongozi Seif Sharrif Hamad.. mmmmmh!..Wapemba wawili kuwepo ktk ngazi ya juu ya Uongozi wa Zanzibar ndio tatizo, kwa sababu Waunguja wanamfahamu Seif na hawawezi kukubali apewe nafasi hiyo akishirikiana na Mpemba mwenzake - President has to be Muunguja!
 
Nafikiri mwanzilishi wa topic hii alitaka kumaanisha kuw DK Shein hana sifa za ukaazi Z,bar ambazo zingewezesha kuwa kujiandikisha kuwa mpiga kura, if that is the case then hana sifa za kuwa mpiga kura Zbar. Hebu tutazame tutaon mengi mwaka huu
 
Mtizamo wangu kwa hicho kipengele cha kujiandikisha kinamnyima sifa za kuwa rais wa zanzibar. Itakuwa je rais apigiwe kura na watu wakati yeye hawezi piga kura maana hakuna alikojiandikisha. Ama anafikiri kwa kuwa anakaa dar atakuwa amejiandikisha huko? Sidhani kama inawezekana kupiga kura Dar ya urais wa zanzibar. Inaonekana shein hakuwahi kufikiri kugombea Smz ila ameshtukizwa na watu wachache wanaotaka kumweka pale, na hicho ndicho kitu Shein anachoweza. Ni mzuri sana wa kutumwa lakini Shein hana uwezo wa kimaamuzi yeye mwenyewe. Umefika wakati wa wazanzibar kupewa mtu wanaemtaka sio kulazimishiwa mtu na viongozi wa bara. Safari hii huko dodoma wakiwalazimishia mtu nawashauri wazanzibar kuhamia CUF na kumbwaga huyo mjumbe wa vigogo wachache.

Kipengele hakisemi inabidi awe amejiandikisha " ..... au ana sifa za kujiandikisha" wamekosa habari za kuandika hawa.
 
Yote watapiga kelele ila Dodoma ndo jibu yote ya matatizo ya chaguzi za CCM Zanzibar.Twendeni Dodoma,sasa kumekucha!!!!!!!!!
 
Kipengele hakisemi inabidi awe amejiandikisha " ..... au ana sifa za kujiandikisha" wamekosa habari za kuandika hawa.

Vipeperushi vyamwagwa kumchafua Dk Shein

Wednesday, 07 July 2010 15:09
Waandishi Wetu Zanzibar, Dar
Dr. Shein
HARAKATI za kumpata mgombea urais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) zimechukua sura mpya katika siku mbili zilizopita baada ya kundi la watu wasiojulikana kuanza kampeni chafu dhidi ya Makamu wa Rais, Dk Ali Mohamed Shein.

Katika kile kinachoonekana kukumbusha historia ya siasa za kukashifiana na kutukanana zilizokuwa zimepamba moto katika miaka ya 90, juzi na jana makaratasi ya aina mbili yalimwagwa katika mitaa mbalimbali ya mji wa Zanzibar kumchafua Dk Shein.

Makaratasi hayo yalionekana kumwagwa katika Soko Kuu la Mjini Zanzibar na pia katika maeneo ya Michenzani, karibu na eneo la Kisonge ambako wiki iliyopita Waziri Kiongozi Mstaafu Dk Mohamed Gharib Bilal ambaye pia ni mgombea katika kinayang'anyiro hicho, alifanya mkutano wakati wa kuchukua na kurejesha fomu zake.

Makaratasi ya kwanza ambayo yalitawanywa alfajiri ya Jumapili yalilenga kumshambulia Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Mohamed Seif Khatib yakimtuhumu kumuunga mkono Dk Shein.

Alfajiri ya jana makaratasi mengine yalimwagwa yakielekeza mashambulizi kwa Rais wa Zanzibar na Makamu Mwenyekiti wa CCM (Zanzibar) Dk Amani Karume na Dk. Shein mwenyewe.

Waandishi wa makaratasi hayo wanaonekana kulenga kutumia kete ya muungano kwa kumwonyesha Dk Shein kama kibaraka wa Tanzania Bara ambaye hatojali maslahi ya Zanzibar.

Sehemu ya ujumbe uliobebwa katika makaratasi yaliyomwagwa jana inasema "Dk Shein sio Mzanzibari, mzaliwa wa Bagamoyo, atatuvuruga kwa manufaa ya Tanganyika".

Maeneo mengine karatasi hizo yanasema "Karume kweli umeishiwa kumpigia kura Shein ambaye anafahamika udhaifu wake ambao hauna tofauti na wako, hapa umechemsha!"

Katika hali ya kutokuficha ni mgombea yupi waandishi wa makaratasi hayo wanamuunga mkono, wanaeleza, "Karume wacha kumchukia Dk Bilal, siku zako zimekwisha, umeongoza nchi kwa kibri na majungu, kwa ushauri wa mama na mashemeji."

Takriban wagombea wengine kadhaa waliojitokeza nao wametajwa kwa kutumia lugha ya dharau na kejeli wote wakitajwa kama ni watu wanaoungwa mkono na Rais Karume.

Wagombea wengine wanaoonekana kuguswa ni Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali wa Zanzibar, Haroun Ali Suleiman ambaye ametajwa kwa kabila lake akiitwa ni "Kumbaro" pamoja na Mohamed Aboud Mohamed, Naibu Waziri wa Afrika Mashariki katika Serikali ya Muungano.

"Ulianza kwa Jaji Mkuu ambaye hana analolijua. Ukamfuata Kumbaro ambaye hana historia, amechukua alivyochukua kama wewe, mbaya zaidi umemuachia kukifunga Chuo Cha Kiislamu na fedha mmegawana ambazo amepewa na Marekani. Ukamfuata Moh'd Aboud ambae ni mzigo usiobebeka, hata CUF ilishindwa kuubeba", inasomeka sehemu nyingine ya karatasi hizo.

Hata hivyo, shabaha hasa inaonekana kuelekezwa kwa Dk Shein ambaye katika sehemu nyingine anatajwa kama "mwenye roho dhaifu kama yako amemuacha kaka yake kuuza genge la nyanya".

Haikuweza kufahamika mara moja ni kwa nini makaratasi hayo yanaonekana kumlenga zaidi Dk Shein ambaye kwa hulka yake ni mtu mstaarabu na mkimya na ambaye anaelezwa kutopendelea siasa za makundi.

Baadhi ya wananchi wa Zanzibar wamezieleza kampeni hizo kuwa ni chafu na ambazo zimeonekana kuendeshwa na mojawapo ya makundi ya wagombea wengine wa nafasi hiyo wanaotishwa na hatua ya Dk Shein kuwania nafasi hiyo.

Hatua hii mpya ya kuchafuana imekuja siku chache tu baada ya Kamati Maalum ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM kukutana mjini Zanzibar kuyapitia majina ya wagombea 11 waliojitokeza na ambapo Dk Shein alitajwa kwamba alionekana kuungwa mkono na wajumbe wengi.

Mbali na Dk Shein, Dk Bilal, Haroun na Mohamed Aboud, wagombea wengine waliojitokeza ni Waziri Kiongozi Shamsi Vuai Nahodha, Naibu Waziri Kiongozi Ali Juma Shamuhuna, Ali Karume, Hamad Bakari Mshindo, Omar Sheha Mussa, Mohamed Yusuf Mshamba na Mohamed Raza Dharamsi.

Hata hivyo, mgombea urais wa Zanzibar kupitia CCM atajulikana keshokutwa Ijumaa baada ya Halmashauri Kuu ya chama hicho (Nec) kuwapigia kura wagombea watatu kati ya 11 walioomba kupewa ridhaa hiyo.

Kikao hicho cha Nec kinakaa siku moja baada ya Kamati Kuu (CC), kuyapitia na kuyachuja majina hayo na kubakia matatu.

Tayari Kamati Maalum ya Halmashauri Kuu ya chama hicho Zanzibar imependekeza majina matano ya wagombea wa urais wa Zanzibar kati ya 11 ambayo yatajadiliwa katika kikao hicho cha CC.

Kamati hiyo Maalum ilijadili majina ya wagombea hao 11 waliojitokeza na kuchukua fomu kuwania kuteuliwa na CCM kuwa mgombea urais wa saba wa Visiwa vya Zanzibar vilivyo na ushindani mkali kisiasa.


Wakati huohuo, mgombea anayetaka kuteuliwa na CCM kuwania Urais Visiwani Zanzibar katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu Ali Karume ameibuka na kusema moja kati ya sifa 13 zilizowekwa na chama hicho kumpata mgombea wa kiti hicho imekiukwa kwa kubadilishwa kinyemela.

Kauli ya Karume ambaye ni Balozi wa Tanzania nchini Italia, inakuja wakati keshokutwa mjini Dodoma, Halmashauri Kuu ya CCM (Nec) inapiga kura kumchagua mgombea wa urais wa Zanzibar.


Akizungumza jana kupitia idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Ujerumani, Karume alisema sifa ya elimu inayotumiwa hivi sasa kwa wagombea inapingana na ile ambayo ipo katika katiba ya CCM.

"Kinachonishangaza sasa ni kuwa pamoja na mambo mengine, sifa ya elimu anayotakiwa awe nayo mgombea wa kiti cha urais iliyoanishwa katika Katiba ya CCM inatofautiana na inayotumika sasa katika kuteua mgombea," alisema Karume

Habari hii imeandaliwa na Salma Said Zanzibar, Sadick Mtulya na Exuper Kachenje Dar
 
Hizi sarakasi na maneno ya wanaCCM tumeshayazoea "mwaka huu patachimbika Dodoma" lakini kila nikienda Dodoma sijawahi ona hata shimo moja, wanamaliza rim za karatasi bure kupeperusha vipeperushi, tunawajua viongozi wa CCM wakiwa na mtu wao huwa hawasikilizi kitu wanaweka pamba masikioni, tusubiri Ijumaa sio mbali wapambe wa Bilal hawataamini macho yao.
 
Hivyo vipeperushi ndivyo vitakavyomfanya Dr. Shein apite kwenye mchujo. Kikwete na wajumbe wa NEC wa Tanzania bara hawako tayari kuona Muungano unakufa. Wagombea wengine karibu wote wameishaweka bayana kwamba Muungano una kero na unatakiwa kujadiliwa ili kumaliza hizo kero. Hapo ndipo inapokuja hoja ya Zanzibar ni nchi au siyo nchi? Hili limewavuruga sana na ndiyo maana Seif Mohammedi Khatib hakuchukua fomu kwa kuwa yeye alishaonyesha wazi kwamba yuko pro-Muungano na waZanzibari wenzake walimshambulia kwamba kama ana nia ya kugombea wao hawatamchagua kwa kuwa yuko upande wa Bara. Pia kuna swala la mafuta ambalo limeongelewa sana kwenye vikao vya Baraza la Wawakilishi, hili nalo linagusa Muungano.

Kwa kuwa NEC ina wajumbe wengi kutoka Tanzania Bara, na kwa kuwa majority ya wagombea wanaona Muungano una kasoro, wajumbe wa NEC wote watampa kura Dr. Shein na hapo ndipo inapokuja ile hoja ya mwaka 2000, kwamba Karume hakuwa chaguo la waZanzibari, bali alipitishwa na bara na yuko pale kwa maslahi ya bara.

Iwapo Dr. Shein atapita kama mgombea wa CCM, hii inampa Maalim Seif Shariff Hamad nafasi nzuri ya kushinda kwa kuwa itabidi CCM walazimike kuiba kura nyingi sana (kura za maruhani) ili kuhakikisha Dr. Shein anashinda. Waunguja walio wengi kuanzia serikalini mpaka kwenye Wajumbe wa Baraza, wamechoka na habari za kuburuzwa na Bara kwenye maswala ya Muungano. Hii inakwenda mpaka kwa wananchi wa kawaida ambao wanaweza kupiga kura ya chuki ama wanaweza kumpa uongozi Maalim ili akiwa Rais wa Zanzibar akomalie hoja ya kwamba Zanzibar ni nchi na pia waruhusiwe kujiunga na OIC na pia mafuta yaondolewe kwenye Muungano. Dr. Shein hana ubavu wa kukomalia hizo hoja kwa kuwa Ofisi yake kwa miaka karibu 10 imekuwa ikishughulikia hoja za kero za Muungano na waZanzibari hawajaona kama amefanya lolote la maana.

Kwa kifupi, kama uchaguzi wa Zenji utakuwa huru na wa haki, basi Maalim yuko njiani kuelekea Ikulu ya Unguja. CCM wameshikwa pabaya sana kwa kuwa wagombea wengi wanataka Zanzibar itambulike kama nchi na iwe huru kufanya maamuzi ya associations kwenye jumuiya za kimataifa. Je, wajumbe wa CCM wataenda kumuuza Dr. Shein huko Unguja?
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom