CHADEMA
JF-Expert Member
- Apr 13, 2013
- 488
- 2,468
Katibu Mkuu Dk. Slaa ameendelea na ziara yake ya kuimarisha na kukagua uhai wa chama mkoani Tabora ambapo ametoa kauli juu ya masuala yanayoendelea bungeni akisema Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali anapaswa kufanya ukaguzi maalum haraka kwa Ofisi ya Bunge kutokana harufu ya ufisadi kwenye matumizi ya taasisi hiyo.
Amesema kuwa amenasa nyaraka za siri, zikiwemo barua za Katibu wa Bunge kwenda hazina zikiomba mabilioni ya fedha ambayo matumizi yake, hususan yale yaliyofichwa kwenye kichaka cha 'safari za ndani na nje' yananuka uvundo wa ufisadi unaofanywa na taasisi hiyo kisha kuuhalalisha kwa vitu visivyolingana na thamani ya rasilimali iliyotumika wala havina tija kwa wananchi.
Katibu Mkuu ameyasema hayo leo mkoani Tabora, Wilaya ya Uyui, alipokuwa akizungumza kwenye mkutano wa hadhara katika maeneo ya Tura na Kigwe, jimboni Igalula, akiendelea na ziara yake ya kutembelea mikoa minne, Shinyanga, Kigoma, Tabora na Singida.
"Ndugu zangu wananchi wa Kigwe naomba kutumia nafasi hii kuzungumza masuala kadhaa ya kitaifa kabla sijazungumza masuala mahususi ya hapa kwenu kijijini, jimboni, wilayani na mkoani kwenu. Bila shaka mtakuwa mmesikia mambo yanayoendelea huko bungeni.
"Kwa muda sasa kumekuwepo na hoja inayohusu posho...posho za safari abazo wabunge wanatuhumiwa kuchukua kisha hawakwenda hizo safari. Imefikia mahali Spika Makinda ametoa maagizo...sasa mimi nasema hatuna tatizo kabisa na wabunge kuchunguzwa au kukaguliwa.
"Wakaguliwe wote kabisa...waliofanya safari za ndani na nje ya nchi. Wote...nasema hivyo kwa sababu ninawajua wabunge, wapo wanaoghushi hata risiti ili wapate malipo. Wapo wabunge badala ya kuwa watetezi wa mali za umma wamegeuka kuwa mstari wa mbele kuhujumu wananchi wao," amesema Dk. Slaa.
Amesema kuwa amenasa barua mbili za siri zilizoandikwa mwaka huu na Katibu wa Bunge kwenda hazina zikiomba jumla ya bilioni 52 ambazo zimetumika ndani ya miezi sita, huku matumizi yake yakiacha shaka kubwa hivyo akasema kama bunge linataka kuonekana 'relevant' kwa wananchi, ni lazima fedha hizo zikaguliwe.
"Barua ya kwanza inaomba jumla ya bilioni 23 kwa ajili ya matumizi ya Julai-Oktoba mwaka huu. Kwa wasiojua fedha hizi zinaweza kujenga takriban madarasa 300 yaliyokamilika yenye kila kitu bila kumchangisa mwananchi wangu hapa hata senti moja.
"Bunge limeomba fedha hizi kwa ajili ya posho ya jimbo, kwa ajili ya gharama za mkutano wa 14 gharama zenyewe hazijaoneshwa hapa, pia wameomba kwa ajili ya Kamati za Bunge, zingine ni kwa ajili ya kamati teule, kamati ya uchunguzi, pia wameomba bilioni 1 kwa ajili ya ziara za nje ya nchi za kamati.
"Kwa ajili ya ziara za kikazi ndani na nje ya nchi wameomba milioni 300 ambazo ni sawa na kituo kimoja cha afya kilichokamilika bila kuwachangisha wananchi. Pia wameomba kwa ajili ya matibabu ndani na nje ya nchi jumla ya shilingi milioni 130, ambazo wangeweza kuzitumia kujenga hospitali nzuri hapa nchini kila mtu anaweza kutibiwa, kwa ajili ya uendeshaji ofisi na mikataba gani sijui wameomba bilioni 1," amesema Dk. Slaa akinukuu barua hiyo.
Katika barua ya pili, Dk. Slaa amedai kuwa bunge limeomba jumla ya bilioni 29 kwa ajili ya Oktoba hadi Desemba, huku akisema fedha fedha hizo zingeweza kutumika vizuri kwa manufaa na maslahi ya Watanzania ambao bado wanahangaika kupata huduma za msingi ndani ya nchi yao.
"Hivi hizi fedha zingeweza kulipa madeni na mishahara ya walimu wangapi, zingejenga barabara za vijijini ngapi, zingehudumia wananchi kiasi gani katika elimu, afya au maji bila kuwachangisha michango ya ajabu ajabu. Hivi kuna mtu anaweza kuniambia thamani ya fedha za posho ya jimbo endapo hata wabunge hawaji majimboni kama huyu wa kwenu.
"Nani anaweza kuniambia hapa tija aliyopata au kama amesikia Kamati ya Bunge imemsemea mkulima wa tumbaku wa Tabora au hapa Igalula, nani anaweza kusema amepata tija kwa safari hizi za ndani au nje ya nchi za kamati za bunge au za ofisi. Ndiyo maana nasema, naunga mkono kabisa wabunge wakaguliwe, lakini tunataka ukaguzi maalum...performance audit ya ofisi ya bunge," amesema Dk. Slaa huku akishangiliwa na wananchi hao.
Amesema kuwa chombo hicho muhimu kwa ajili ya kuwasemea na kuwawakilisha wananchi kimeanza kupoteza maana kwa wabunge wakisaidiwa na kiti, kuanza kujikita katika masuala yasiyokuwa na umuhimu wowote kwa Watanzania wanaotaka kuwasikia wakijadili maslahi ya watu waliowatuma bungeni.
"Bunge limeacha kazi ya kutetea, kusemea na kuwakilisha wananchi, badala yake, wanageuza bunge sehemu ya majungu, vijembe, umbea wakisaidiwa na spika au naibu spika kulinda mambo hayo ya ajabu. Tunataka bunge lifanye kazi yake. Nimenyamza kwa muda mrefu. Nimekaa kimya muda mrefu juu ya bunge...
"CAG afanye huo ukaguzi maalum, tunataka kujua thamani ya fedha za walipa kodi Watanzania hawa. Wanapanga ufisadi mkubwa kama huu kisha wanatafuta namna ya kuuhalalisha kwa kupanga safari zinazoitwa za kazi au mafunzo...wakati hazina mpango wowote wala manufaa kwa Mtanzania," amesema Dk. Slaa.
Kesho Dk. Slaa ataendelea na ziara yake ya kutembelea maeneo mbalimbali ya majimbo ya Mkoa wa Tabora, akiwa amebakiza majimbo ya Bukene, Nzega na Igunga, kisha ataingia Mkoa wa Singida.
Katibu Mkuu, Dk. Slaa akihutubia Kijiji cha Tura