SOMA JAHAZI JPILI,katika Gazeti la Tzn Daima YA LEO.
By P Karugendo
CCM WANAPOJIFUNGA GOLI LAWAMA ZIMWENDEE NANI.?
CCM wanapojifunga goli lawama zimwendee nani?
Prudence Karugendo
JUMA lililopita nilionyesha jinsi kanuni mojawapo, katika mpira wa miguu, inavyoweza kutumika vilevile kwenye ushindani wa kisiasa na kuleta manufaa yale yale yanayokuwa yamelengwa na kanuni hiyo katika mchezo wa mpira wa miguu.
Kanuni hiyo ni ya mtego wa kuotea "off side trick" ambayo chama kikuu cha upinzani nchini, Chadema, kimejinufaisha nayo kinapoitumia dhidi ya chama tawala, CCM.
Katika makala hiyo nilikuwa nimejaribu kuangalia mashambulizi ya chama tawala dhidi ya upinzani, hasa yanayoelekezwa kwa chama kinachoonekana kuwa ni tishio zaidi kwa sasa katika mustakabali wa CCM, Chama cha Demokrasia na Maendeleo.
Kwa jinsi mashambulizi hayo yanavyofanyika kwa papara na bila mpangilio maalumu, kutokana na sababu nitakazozieleza baadaye kwenye makala hii, na hivyo CCM kushindwa kuelewa au kuzisoma mbinu za mpinzani wake.
Papara hizo ndizo zinazokifanya chama hicho kikongwe kuingizwa kirahisi kwenye mtego wa kuotea, kwa maana ya chama hicho kujikuta kikifanyishwa kazi ya kukijenga na kukipamba chama pinzani kwa imani kuwa kinaubomoa upinzani.
Kufuatia makala hiyo baadhi ya wasomaji wameniomba niangalie pia na upande wa ngome ya CCM ili kuleta uwiano wa mfumo wa timu.
Kwahiyo katika makala hii nataka niangalie jinsi CCM ilivyoiweka ngome yake dhidi ya mashambulizi ya upinzani hasa yale makombora yanayofyatuliwa na washambuliaji wa Chadema.
Je, CCM imefanikiwa kuiimarisha ngome yake dhidi ya mashambulizi hayo? Baada ya kuwaona washambuliaji wake kuwa hawauelewi mtego wa kuotea, je, ngome ya CCM imekaa sawa kuyadhibiti mashambulizi ya Chadema?
Ngome hiyo ya CCM inazo mbinu kama walizo nazo walinzi wa Chadema za kutumia nguvu kidogo kuzuia mashambulizi yenye nguvu za ziada lakini yasiyo na mpangilio maalumu?
Ngome ya CCM ikitazamwa si tu kwamba inaonekana inapwaya bali pia iliyo tayari kujifunga mabao yenyewe baada ya kutiwa msukosuko kidogo tu na washambuliaji wa upinzani.
Mara kadhaa tumeishuhudia CCM ikijifunga mabao yenyewe na kushindwa kuyarudisha kutokana na kukosa safu iliyo imara ya ushambuliaji.
Mwaka 1995 CCM walijifunga bao wenyewe, bao ambalo bado wanalijutia mpaka leo, pale walipolipoteza kiuzembe jimbo la Karatu. Bila mizengwe ya CCM si ajabu jimbo lile lingekuwa bado ni mali yake mpaka leo, kama chama hicho kingekuwa kinayasikiliza na kuyaheshimu matakwa ya wanachama wake.
Ikumbukwe wana CCM wa jimbo la Karatu walikuwa na chaguo lao, mtu waliyemtaka awe mgombea wa jimbo hilo katika nafasi ya ubunge kwa tiketi ya chama chao, naye si mwingine bali Dk. Willbrod Slaa.
Lakini chama chao, kwa mtindo wake maarufu wa huyu si mwenzetu, kikaamua kuyapuuza matakwa ya wanachama wake katika jimbo lile. Kikamwengua Dk. Slaa ambaye wanachama wachache wa chama hicho katika ngazi ya kitaifa walimuona kuwa si mwenzao.
Pamoja na ukweli kwamba alikuwa mwanachama hai na zaidi ya hapo kipenzi cha wanachama ngazi ya jimbo. Badala yake CCM ikamuweka mtu (to impose) aliyekuwa hakubaliki jimboni, Patrick Qorro.
Wana CCM wa Karatu kuona vile, wenyewe, wakamuonyesha Slaa njia ya kutokea na mahali pa kuelekea, ndipo Dk. Slaa akatua Chadema. CCM ikawa imejifunga goli yenyewe na kuipa Chadema ushindi bila jasho. Tangu wakati huo CCM wanapigana kufa na kupona kulirudisha jimbo lile bila mafanikio.
Ni wazi kwamba CCM wameishatumia gharama kubwa sana katika jitihada za kulirudisha jimbo lile kwenye ngome yake. Na sidhani kama gharama inayotumika kuusafisha uzembe uliofanywa na ngome ya chama hicho inatokana na michango pekee ya wanachama wake.
Nina imani kwamba gharama zinazosababishwa na uzembe wa ngome ya CCM, inayojifunga magoli badala ya kuyazuia, zinatugusa Watanzania wote walio ndani ya CCM na walio nje yake. Sote ni waathirika wa uzembe wa ngome ya chama tawala.
Pesa ambayo ingetumika kufanyia mambo ya maana kwa ajili ya ustawi wa wananchi inabidi itumike kuusaka kwa mabavu ushindi wa chama tawala baada ya chama hicho kuwaweka kwa mizengwe kwenye ushindani baadhi ya wanachama wake wasio na uwezo wa kushindana.
Ni kwa nini chama hicho kinachukua maamuzi hayo yanayogeuka mzigo kwa wanachama na wasiokuwa wanachama? Hilo ni swali ambalo sina hakika kama kuna kada yeyote wa chama hicho aliye tayari kulitolea maelezo ya kina.
Ipo mifano zaidi ya jinsi ngome ya CCM inavyojifunga magoli yenyewe kwa faida ya wapinzani wake. Mkoani Shinyanga, katika Uchaguzi Mkuu uliopita, Jimbo la Maswa Magharibi lililazimishwa kwenda Chadema kwa mtindo uleule wa CCM kujifunga goli yenyewe.
Kwingine ni Kawe, Iringa Mjini, Nyamagana, Ilemela na kwingineko. Pia yapo majimbo mengine ambayo CCM imeyatetea kwa kutumia mtutu wa bunduki baada ya kila njia kuwa imeshindikana.
Anayelitilia shaka hilo awaulize wapiga kura wa Jimbo la Karagwe, mkoani Kagera, njia iliyotumika kumtangaza mgombea wa CCM kuwa ndiye mshindi.
Pia awaulize wapiga kura wa Jimbo la Segerea namna alivyopatikana mshindi wa kiti cha ubunge wa jimbo hilo kitu ambacho mpaka sasa bado kimewaacha midomo wazi.
Hizo zote ni gharama ambazo chama tawala kinalazimika kuziingia ili kujiepushia aibu inayosababishwa na udhaifu wa ngome yake inayolazimishwa na wapinzani kujifunga magoli badala ya kuyazuia.
Timu yoyote inayokuwa na ngome yenye wachezaji wanaojifunga magoli badala ya kuyazuia magoli yasiingie upande wake ni wazi kwamba inakuwa na kasoro katika muundo wake.
Inawezekana kwamba wachezaji ambao wangepaswa kuwekwa kwenye nafasi za ushambuliaji ili wakafunge magoli na kuipatia timu ushindi ndio wanaowekwa nyuma kwenye nafasi za ulinzi wakati walio na uwezo wa ulinzi wakiwekwa mbele ili wakashambulie.
Matokeo yake wale walio mbele wanaishia kuotea kwenye "off side trick" wakati walinzi wake wakipachika mabao kwenye goli lao. Hivyo ndivyo CCM ilivyo kwa wakati huu. Sijui ni nani anayepaswa kubeba lawama za muonekano huo wa timu iliyojichanganya kimfumo namna hiyo?
Na kwa vile hiki ni chama tawala tusije tukajidanganya kwamba kasoro hizo za kichama zitaishia tu katika chama. Ni lazima kasoro hizo zijitokeze katika ngazi ya utawala wa nchi.
Ni lazima nchi nayo ionekane pia inajifunga magoli wakati safu yake ya ushambuliaji ikiwa butu. Mifano tunayo mingi inayolishadidia jambo hilo bila pingamizi.
Tuangalie mikataba tunayoingia na watu wanaoitwa wawekezaji. Wengi wa watu hao wanakuja kuzoa tu rasilimali za nchi yetu wakiwa hawajawekeza lolote.
Tujiulize, mtu anayekuja kuzoa tu madini yetu na kupeleka kwao anakuwa amewekeza nini? Ardhi yetu, madini yetu, watumishi wetu, na wakati mwingine mitaji tunawapa sisi, lakini wao eti ni wawekezaji, wanaondoka na kila kitu na kutuachia makorongo yaliyojaa vumbi!
Wawekezaji wengine kama IPTL, Richmond, Dowans na wengine wa aina hiyo wanakuja kutuuzia huduma wakiwa wametusainisha mikataba sawa na ile ya kina Karl Peters, mikataba ya kwamba hata kama huduma zao hatuzihitaji ni lazima tuzinunue, tukazifanyie nini? Hilo sio tatizo lao kujua, wao wanachokitaka ni pesa yetu basi.
Kwa kukubali kuingia katika mikataba ya aina hiyo ni nani atabisha kwamba hatujifungi mabao sisi wenyewe kwa faida ya hao wageni ambao kwa hapa naweza kuwaita wakora?
Tatizo linaloanzia kwenye mfumo wa chama tawala linageuka kuwa tatizo la nchi. Nchi inalazimika kuugua ugonjwa unaokisumbua chama tawala.
Lakini tatizo hilo linaanzia wapi? Au niulize tatizo hilo ni lini na kwa nini limekipata chama tawala?
Wakati nchi yetu ikiendeshwa kimaadili, miaka ya nyuma kidogo, siasa nayo ilikuwa ni taaluma inayojitegemea. Ilikuwa si rahisi kama ilivyo sasa kwa kila mtu kuivamia siasa.
Si kila mfanyabiashara, kwa mfano, angeamua kuingia kwenye siasa jinsi anavyotaka yeye. Hata wanazuoni si wote walikuwa wanajiona wanaiweza siasa. Kwa maana hiyo maprofesa walibaki vyuoni kufundisha.
Madaktari nao walibaki mahospitalini kuwatibu wananchi, wafanya biashara walibaki kwenye biashara zao nakadhalika. Siasa ilibaki kwa wanasiasa.
Walioitamani siasa, hata kama walikuwa wanazuoni, iliwabidi waende shule kwanza. Vilikuwepo vyuo vya siasa, mfano kile cha Kigamboni. Tena wakati huo chama cha siasa kikiwa kimoja tu lakini kikiwa na itikadi ambayo ilikuwa lazima mtu aisomee kwanza ndipo aweze kujitambulisha kama mwanasiasa.
Tuseme kilikuwepo kitu ambacho ilimbidi mtu kukisomea na kukielewa vizuri kabla ya kujitambulisha kama mwanasiasa.
Lakini baada ya utaratibu huo kuondolewa katika mpango wa soko huria ndipo siasa ikabaki haina mwenyewe. Kila mmoja akajiona anaiweza siasa. Hiyo ikawa fursa ya wafanyabiashara wakubwa kwa wadogo kuwekeza kwenye siasa baada ya kuona kuwa inalipa.
Matokeo yake ndiyo haya, tuna watu wanaofanya siasa wakiwa si wanasiasa kwa vile chama tawala kimeiondoa siasa katika taaluma na kuifanya ni shughuli inayoweza kufanywa na kila mtu.
Ni kwa maana hiyo chama tawala kimewawezesha hata wacheza tunguli kuingia bungeni wakiwa tayari ni wanasiasa.
Kwa vyovyote vile hawa hawawezi kukisaidia chama hicho kisiasa, kwa vile kiuhakika hawa siyo wanasiasa, bora tuwaite wawekezaji tu waliogundua kuwa siasa inalipa na kuamua kujibana mle kwa vile ni mfumo wa soko huria.
Hilo linaweza likatuonyesha ni jnsi gani Chama Cha Mapinduzi kinavyoelemewa na mzigo kiliojitwisha bila kuelewa kinaupeleka wapi.
Chama cha siasa kinaposheheni wawekezaji wakijiita wanasiasa tujue kuwa huo ni mzigo mkubwa kwa chama na inapotokea chama hicho kikawa chama tawala basi huo ni mzigo wa nchi. Na ieleweke kwamba ni vigumu kuwapambanisha wawekezaji hao katika siasa na wanasiasa machachari waliodhamiria kufanya siasa.
Tofauti na CCM ambamo kwa sasa watu wanaingia kama wawekezaji, chama kikuu cha upinzani nchini, Chadema, kina wanasiasa waliodhamiria kufanya siasa.
Hawa wamelazimika kuingia kwenye siasa baada ya kuiona siasa ya nchi yao ikienda mrama, wamelenga kuinusuru nchi yao kisiasa. Siwezi kuwaita hawa kuwa nao ni wawekezaji, hapana, hiyo ni kwa sababu Chadema bado ni kama pori, waliomo wameingia ili wakalime. Ni tofauti na CCM ambalo ni shamba linalotoa mavuno, kwahiyo wanaoingia mle wanakuwa wamevutiwa na matunda na si kitu kingine. Kwa jinsi hali ilivyo ni kwamba CCM wanajifunga mabao wenyewe kutokana na chama hicho kuwachezesha watu wasioelewa mbinu za mchezo. Kwahiyo kwa tatizo hilo hawapaswi kumtafuta mchawi nje ya kikosi chao.