Historia ya Chuchu Sound Band
Mwanamuziki mwanzilishi wa bendi ya Chuchu Sound,
Omari Mkali, anabainisha kuwa ujio wa
Yusuph Chuchu aliyekuwa akiishi Marekani ndiko ikapelekea wazo la kuanzishwa bendi ya
Chuchu Sound. Mahala ilikuwa Zanzibar na Kabla hata hatujakubali au kukataa alishasema jina la bendi kuwa itaitwa Chuchu Sound kwa kulipa heshima jina la familia yake, tukakubali na kuja Dar es Salaam , kuasisi Chuchu Band.
Anasema walipofika Dar -es-Salaam aliwapangishia nyumba nzima maeneo ya Mwananyamala Komakoma na kuanza kupiga kazi ambapo mnamo Februari mwaka 2000, wakaanza kazi rasmi.
Anaeleza kuwa walianza kazi wakiwa chini ya usimamizi wa
King Jovanii ambaye pia ndiye alikuwa mpiga solo akishirikiana naye katika uongozi.
Anawataja wanamuziki walioanzisha bendi hiyo kuwa ni
Abuu Mwanazanzibaa aliyekuwa anapiga (Kii bodi),
Mbwana Mponda (Base gitaa), George Choka (Rythm gitaa), Mohamed Kachumbari (tumba).
Anawataja wapiga Drums kuwa ni
Gabi Katanga (marehamu), aliyekuwa mwanzilishi na baadye wakamuongeza mpigaji mwingine ambaye naye ni
Mudi Termineta (marehemu).
Omari Mkali anaendelea kueleza kuwa safu ya waimbaji ilikamatwa vyema na yeye akishirikiana na
Jonical Flower, Ledslaus Manyama, ambaye kwa sasa ni marehemu, huku Mao Santiago akiwa mshereheshaji rapa.
Anautaja ukumbi wao wa kujidai ulikuwa ni Vatican City Sinza,Dar-es-Salaam ambapo wakipiga mwishoni mwa wiki kiingilio kilikuwa ni Sh2,500 na siku za kawaida kilikuwa Sh2,000.
Tukiwa na Chuchu Sound band tulitoa jumla ya albamu tatu ambazo ni
- Kusema sema,
- Hodi Hodi Wana Chuchu na
- Mkataa pema,
Albamu hizi zilikuwa na nyimbo kali na za kusisimua kama Sitishiki, Usione vyaelea, Marafiki na nyingine nyingi kali, alisema Mkali.
Anaitaja bendi hiyo kuwa ndiyo iliyoasisi mduara dansi hadi kuwa maarufu kila kona ya Tanzania. alitaja sababu kubwa iliyowafanya wapate umaarufu ni kuimba kwa kujibizana kwa sauti mbili nene na laini kwa maana ya mwanamke na mwanaume, kitu ambacho hadi sasa watu wakipiga muziki wa aina hiyo wanakiiga wao ndiyo waliokianzisha.
Source:
Mwananchi: Makala - Gazeti la habari za kiswahili la kila siku Tanzania, linaongoza