Kili Stars yajisahihisha
Tuesday, 30 November 2010 19:40 newsroom
* Yaipiga Somalia 3-0
* Maelfu waipiga tafu
NA ABDALLAH MWERI
TIMU ya taifa ya Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars, imefufua matumaini ya kusonga mbele katika michuano ya Kombe la Chalenji,
baada ya jana kupata ushindi wa mabao 3-0 ilipovaana na Somalia, mchezo uliochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Maelfu ya mashabiki wa soka waliitikia mwito wa waandaji wa michuano hiyo Baraza la Vyama vya Soka Afrika na Kati (CECAFA), walipojitokeza kwa wingi kuishangilia Kilimanjaro Stars, iliyocheza soka ya kiwango bora tofauti na mchezo wa kwanza ilipochapwa bao 1-0 na Zambia kwenye uwanja huo. CECAFA juzi ilitoa tamko la kuruhusu mashabiki kuingia bure uwanjani kushuhudia mechi za michuano hiyo hadi keshokutwa, baada ya mashabiki wachache kujitokeza siku ya ufunguzi Jumamosi iliyopita. Tofauti na mchezo wa Zambia, Chipolopolo, mashabiki waliishangilia kwa nguvu Kilimanjaro Stars dakika zote 90 za mchezo.
Kilimanjaro Stars ilianza kufanya vitu vyake dakika ya sita ya mchezo baada ya Mrisho Ngasa kupiga mpira wa krosi uliokosa mchezaji wa kuunganisha, kabla ya dakika moja baadae, kiungo Mohamed Banka kufumua shuti kali akiwa ndani ya eneo la hatari lakini shuti lake lilipanguliwa na kipa Aden Hussein.
Timu hiyo iliendelea kuliandama lango la Somalia na kumpa kazi ya ziada kipa huyo aliyecheza kwa ustadi kipindi cha kwanza, kwa kuokoa mashuti ya wachezaji wa Kilimanjaro Stars. Kiungo wa kushoto aliyecheza badala ya Idrissa Rajabu, Salum Machaku nusura afunge bao baada ya kufumua shuti ndani ya eneo la hatari liliokolewa na Hussein.
Dakika 20 za mwanzo lango la Somalia lilikuwa katika hali ngumu baada ya Kilimanjaro Stars kulishambulia kama nyuki, ambapo Ngasa alikuwa mwiba mkali kwa mabeki wa timu hiyo. Dakika za 25 na 27, Ngassa na Banka walikosa mabao kwa kupiga nje licha ya kuingia na mipira ndani ya eneo la penalti.
Nahodha wa zamani wa timu ya taifa, Taifa Stars, Henry Joseph, alianza kuwainua vitini mashabiki wa soka baada ya kufunga bao la kwanza dakika 42 kwa mkwaju wa penalti kufuatia beki wa Somalia, Mohamed Hassan kushika mpira katika harakati za kuokoa. Penalti hiyo ililalamikiwa kwa muda na wachezaji wa Somalia kabla ya kukubali.
Kuingia kwa bao hilo kuliamsha hasira za wachezaji wa Somalia ambao walitulia na kupanga mashambulizi langoni mwa Kiliamanjaro Stars na dakika 44 Isse Abshir alikosa bao baada ya kuitoka ngome ya wapinzani wao iliyokuwa chini ya Juma Said 'Nyoso' na Kelvin Yondani.
Mchezaji chipukizi aliyeanza badala ya Gaudence Mwaikimba, Thomas Ulimwengu, nusura afunge bao dakika 51 baada ya kupiga shuti liliokolewa na kipa. Dakika 57, Banka alikosa bao kutokana na mpira wake kupaa juu ya lango. Mshambuliaji aliyetokea benchi akichukua nafasi ya Ulimwengu, John Bocco alifunga bao la pili dakika 76 kwa shuti hafifu baada ya kuuwahi mpira uliotemwa na Hussein.
Kilimanjaro Stars iliendelea kuichachafya ngome ya Somalia na kupata bao la tatu kupitia kwa Nurdin Bakari aliyeingia kuchukua nafasi ya Machaku akiunganisha kwa kichwa mpira wa krosi uliopigwa upande wa kushoto na Ngassa aliyewatoka mabeki wa Somalia kwa chenga za maudhi.
Kilimanjaro Stars imefikisha pointi nne katika mechi mbili ilizocheza na itamaliza mchezo wa kundi A kwa kuvaana na Burundi Desemba 4.
Baada ya mchezo huo, kocha wa Kilimanjaro Stars, Jan Poulsen alisema timu yake ilicheza soka ya kiwango bora kulinganisha na mechi dhidi ya Zambia. Kwa upande wake kocha wa Somalia, Yousuf Adam aliisifu timu yake kwa mchezo mzuri licha ya kufungwa.
Kiliamanjaro Stars: Juma Kaseja, Shedrack Nsajigwa, Juma Jabu, Juma Nyoso, Kevin Yondani, Henry Joseph, Shaaban Nditi, Mohamed Banka/Jabir Aziz, Mrisho Ngassa, Thomas Ulimwengu/John Bocco na Machaku Salum/Nurdin Bakari.
Somalia: Aden Hussein, Khalid Ali, Mohamed Hassan, Yassin Mohamed/Jabril Hassan, Mohamed Haji, Ilyasi Abdi, Abdulah Osman, Abdulkadir Ali/Mohamed Ahmed, Isse Abshir, Anwar Sadad na Sa'ad Salah.
Katika mchezo wa awali, Zambia ilitoka suluhu na Burundi kwenye uwanja huo. Michuano hiyo inaendelea leo kwenye uwanja huo ambapo timu za Sudan na Rwanda zilizopangwa kundi B zitamenyana katika mchezo wa kwanza, kabla ya Ivory Coast kupepetana na Zanzibar.
Source; Uhuru
Hapo kwenye bold. Hivi timu mwenyeji huwa inaanza na point za bure?