elivina shambuni
JF-Expert Member
- May 31, 2018
- 461
- 295
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Dodoma kimepita bila kupingwa katika vijiji, mitaa na vitongoji 3,905 kati ya 4,032 vilivyopo sawa na asilimia 96.85. Akizungumza na Habari- LEO Katibu wa CCM Mkoa wa Dodoma, Jamila Yusuph alisema ushindi huo ni taswira nzuri katika kuelekea Uchaguzi Mkuu mwaka 2020.
Alisema ushindi huo walioupata hadi sasa unatokana na wana CCM mkoa huo kuwa na utaratibu wa kufanya tathmini kila baada ya uchaguzi, ili kujikosoa walipokosea na kujisahihisha. Katibu wa CCM alisema hiyo ndiyo siri ya ushindi mkubwa katika mkoa huo kupata viti vingi vya vitongoji, mitaa na vijiji. “Kati ya vijiji 564 vilivyopo, CCM imepita bila kupingwa katika vijiji 533 sawa na asilimia 94, kati ya mitaa 258 iliyopo CCM imepita bila kupingwa mitaa 255 sawa na asilimia 98 na huo ni ushindi mkubwa katika mkoa wa Dodoma,” alisema.
Jamila alitoa rai kwa wanachama wa CCM kutopumzika kwa kuwa wameshapata ushindi bali wanatakiwa kuendelea kutafuta kura katika maeneo yaliyobaki. Alisema hata mahali ambapo CCM imepita bila kupingwa, wanachama wa chama hicho wanatakiwa kwenda kuwashukuru wananchi na kuwaelezea mipango ya serikali katika kuwapatia maendeleo wananchi wanyonge.