nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Aprili 6, 2011
KIKAO cha Halmashauri Kuu (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinachotarajiwa kufanyika mjini Dodoma wiki hii kitakuwa na ajenda nzito zitakazoamua kukigawa ama kukipa uhai mpya chama hicho kikongwe nchini, huku Katibu Mkuu wake, Yussuf Makamba akielezwa ya kuwa atang'atuka rasmi.
Taarifa za ndani ya chama hicho zinaeleza kwamba, miongoni mwa ajenda zinazotarajiwa kuibua mjadala mzito na huenda kuwagawa wajumbe katika makundi ni ile ya 'kujivua gamba,' hoja ambayo ni sehemu ya ahadi ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, aliyoitoa katika maadhimisho ya miaka 34 ya kuzaliwa kwa CCM, Februari mwaka huu.
Imeelezwa kwamba ajenda hiyo itawagawa wajumbe katika makundi mawili makubwa, lile linalojipambua kupiga vita ufisadi ambalo Kikwete sasa anaelezwa kuliunga mkono na lile linalokejeli vita hiyo ama kutajwa kuhusika na ufisadi.
Taarifa zinabainisha kuwa ajenda hiyo ina nguvu kubwa ndani ya CCM kwa sasa baada ya kubainika wazi kwamba ilikiponza chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana (2010) na chama hicho kuporomoka na kutoa mwanya kwa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuimarika kwa kuongeza idadi ya wabunge hasa katika majimbo ya miji mikuu.
CHADEMA kilishinda ubunge katika majimbo ya Nyamagana na Ilemela mjini Mwanza, Musoma Mjini, Mbeya Mjini, Moshi mjini, Arusha mjini, Iringa mjini na sehemu ya kigoma mjini. Inadaiwa kuliibuka mpasuko mkubwa ndani ya CCM unaodaiwa msingi wake ni nguvu ya fedha kutumika kuteua wagombea ubunge kwa tiketi ya CCM, badala ya nguvu ya kisiasa.
Imefahamka kwamba wajumbe kutoka ukanda mmoja wa Jamhuri ya Muungano wamejipanga ‘kulitolea uvivu' suala hilo kwa kutamka bayana kwamba wanaohusika, hata kama ni kutajwa tu, katika ufisadi watoswe.
"Wale jamaa wamepania kutaja hata majina ya watu ambao wanaona ni mzigo kwa CCM. Huko moto utakua mkali maana na wao wahusika wamejipanga kuwashughulikia wabaya wao na ikibidi hata Mwenyekiti Rais Kikwete ili kupoza joto," anasema mjumbe mmoja wa NEC.
Imeelezwa tayari nukuu mbalimbali za nyaraka za CCM ikiwamo Katiba, Mwongozo na vitabu vya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere zimeanza kukusanywa ili kushadidia hoja zitakazowasilishwa katika kukosoana na hatimaye kujisahihisha ndani ya CCM.
Ajenda nyingine inaelezwa kuwa ni malumbano yanayoendelea kati ya UVCCM na viongozi waandamizi wa zamani serikalini, jambo ambalo linatajwa kuibua mjadala hasa baada ya wazee kuamini kwamba vijana wametumwa kabla ya Rais Kikwete kugusia suala hilo hivi karibuni.
Pamoja na kulitolea tamko, bado wazee hao wameelezwa kwamba wanataka kusikia kauli ya Kikwete ndani ya NEC kutokana na kauli hiyo kutolewa na UVCCM Mkoa wa Pwani anakotokea, huku mwanawe, Ridhiwani Kikwete, akiwa mjumbe mwenye nguvu za kisiasa katika UVCCM mkoani humo.
"Wazee watataka Rais atoe tamko ndani ya NEC kuwakemea vijana hao, lakini kuna wazee wengine wanawaunga mkono vijana na wataweka wazi kwamba ni lazima viongozi wa zamani wamsaidie Rais wa CCM amalize kipindi chake salama kama na wao wanataka kuwania urais na washinde," anasema mjumbe huyo.
Hivi karibuni visiwani Zanzibar, Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Iddi, alitamka hadharani kuunga mkono kauli ya vijana kuhusu viongozi wa zamani wanaotoa matamko hadharani na alikemea vijana wanaotumika kufanikisha malengo ya baadhi ya viongozi wa kisiasa.
Imeelezwa katika kikao hicho, Katibu Mkuu, Yusuf Makamba anaweza kutangazwa kuwa anastaafu, ikiwa ni baada ya kipindi kirefu cha mashinikizo ya kumtaka ang'atuke kutoka kwa vijana, na sasa hata wazee wenzake ambao baadhi wamemuandikia hadi barua na yeye akawakejeli.
Taarifa zaidi za kiuchunguzi zinabainisha kuwa kati ya wazee waliomwandikia barua Makamba kumtaka aachie ngazi ni pamoja na aliyekuwa Mbunge wa Kwela, Dk. Chrisant Mzindakaya.
Mzindakaya ambaye naye alistaafu kuwania ubunge mwaka jana, anatajwa kumuandikia Makamba barua ya kutaka aachie ngazi na kuainisha sababu kadhaa, ikiwamo ya kutomudu changamoto za sasa za kisiasa.
Inaelezwa kuwa Mzindakaya, mbali na kumwandikia Makamba barua hiyo, nakala amezisambaza kwa baadhi ya viongozi wengine wakuu wa CCM Makao Makuu.
"Mzee Makamba atatangazwa kustaafu kwa heshima na anatarajiwa kufanyiwa sherehe ya kumuaga rasmi," anaeleza mtoa habari wetu.
Mkutano wa sasa wa NEC unafanyika katika wakati ambao tayari UVCCM wameonyesha kuingia katika mvutano wa wenyewe kwa wenyewe, na pia mvutano kati ya baadhi ya viongozi wa umoja huo na viongozi wastaafu serikalini ambao pia kwa sasa baadhi ni wajumbe wa NEC-Taifa.
Mbali na kadhia hiyo, CCM imekuwa katika mvutano wa makundi kwa muda mrefu kiasi cha kulazimika kuundwa kwa Kamati Maalumu ya kufuta mpasuko huo, hasa uliotajwa kuwagusa zaidi wabunge wa Bunge la tisa kutoka CCM.
Kamati hiyo maalumu iliyoongozwa na Rais mstaafu, Ali Hassan Mwinyi, akisaidiwa na Makamu Mwenyekiti wa CCM, Pius Msekwa na kada mwenzao, Abdulrahman Kinana, imeelezwa kama kamati iliyoshindwa kufanya kazi yake, na haikuwahi kutoa ripoti yake hadharani na dalili za kuendelezwa kwa makundi hayo zimekuwa zikijitokeza wazi wazi.
Hayo yakiendelea, baadhi ya wajumbe wa NEC waliozungumza na Raia Mwema hawana matumaini ya kuwapo maamuzi yoyote ya maana yatakayoweza kukisaidia chama hicho.
Kukata tamaa kwa baadhi ya wajumbe kunaelezwa kuchangiwa zaidi na hulka ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, ambaye wanamwelezea kuwa ni kiongozi asiyeeleweka, hivyo kuwawia vigumu hata kumsaidia pale inapolazimu.
"Hakuna jipya, kwa Bwana Mkubwa wetu hatutarajii jipya lolote," anasema Mjumbe mmoja wa NEC alipohojiwa na Raia Mwema kupata undani wa kikao hicho.
Taarifa za ndani kutoka kwa baadhi ya wajumbe hao wa NEC zinabainisha kuwapo kwa makundi mawili makuu, moja likisimamia maslahi ya taifa na jingine likisimamia maslahi binafsi, na ni kundi hili lenye kusimamia maslahi ya taifa linaloonekana kukatishwa tamaa na hulka ya Mwenyekiti wao ya kutoweka msimamo wake wazi kuhusu kundi la pili linaloundwa na marafiki zake wa karibu.
"Si rahisi kuwa na maamuzi mazito; tatizo la bwana mkubwa haeleweki. Tunashindwa kumsaidia. Tazama kama suala la Dowans, utadhani hakuna serikali, Waziri mzima (Ngeleja) anaitisha press conference anasema walipwe, Mwanasheria Mkuu wa Serikali naye anasema walipwe, Rais kakaa kimya, Kamati Kuu nayo inakaa inasema ni suala la kisheria, halikwepeki, walipwe, badala ya kufanya siasa nao wanashabikia Dowans kulipwa, sasa unajiuliza bwana mkubwa kasimamia wapi katika suala hili, huwezi kumuelewa," anasema mjumbe mwingine.