Mchambuzi, nimeisoma makala yako kwa umakini mkubwa, na nakiri kuwa kuna mambo nimejifunza, ingawa hayakuwa mageni sana lakini yameniongezea maarifa.
Ndani ya chama chetu CCM, kwanza kabisa hatujabadili mfumo wa siasa, hii ina maana siasa zetu ni zile za chama kimoja kikiwa mamba na vyama vingine vikiwa dagaa.
Lakini kumbe ukweli ni kuwa, siasa ya hapa nchini imebadilika, inataka kuona ahadi zikitekelezwa na sio ahadi zikibadilishwa tarehe, kwa mfumo huu wa siasa ni changamoto kwa viongozi wanaounda serikali.
Kikubwa ninacho kiona kuhusu viongozi wanaounda serikali ni udhati wa kutumikia taifa, hapa nakiri kuwa viongozi wengi wa CCM wanaounda serikali hii ya Kikwete wengi ni weupe, nikimaanisha ni wachovu kiutendaji. Kama tungekuwa na baraza la mawaziri lililo sheheni watu kama dr. Mwakyembe, dr. Kagasheki and the like, hali ingekuwa si haba katika kutekeleza ilani ya chama.
Katika kasi ambayo CHADEMA wanalipeleka taifa, katika hali ya kuwaaminisha wananchi kuwa serikali ya CCM inapaswa kuwapa zaidi ya inachokitoa kwa jamii, na ukweli ni kwamba, CHADEMA wana hoja za kuthibitisha kauli zao hizi, hoja zenyewe ni kama ufisadi, misamaha ya kodi, matumizi makubwa ya fedha kwenye shughuli za kawaida n.k, basi serikali yangu kwa kipindi hiki kifupi ijitahidi kuendana na kasi ambayo CHADEMA wanaaminisha watu, jambo ambalo lipo ndani ya uwezo wa serikali.
Hapa naona kabisa serikali yangu inalazimishwa kukata viuno kwenye ngoma wanayoipiga CHADEMA, kama vijana wameyapokea mapambano na kuungana na jitihada za CHADEMA katika kuleta mabadiliko, hii hiwe changamoto ndani ya serikali ili kukinusuru chama chetu kwenye uchaguzi mkuu wa 2015.