BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,825
- 287,847
Buriani CCM, salamu nyingi kwa KANU, UNIP
Samson Mwigamba
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
TULIFUNDISHWA katika somo la Kiswahili tulipokuwa darasa la tatu wakati huo, kwamba kuna maneno ya aina tatu yanayotumika tunapoagana.
Tukiagana usiku tunapokwenda kulala tunasema, ‘alamsiki'. Ikiwa kuna mmoja au baadhi yetu wanakwenda safari ya kawaida tu isiyo ya hatari sana, tulifundishwa kuagana kwa kusema, ‘kwaheri ya kuonana'. Na kama ni safari ya hatari ambayo haina uhakika wa kurudi mfano kwenda vitani, tunaagana kwa kusema ‘buriani'.
Mwaka 1978, Mzee Mtwale wa Kijiji cha Namhura jimboni Mwibara wilayani Bunda, hakupata nafasi ya kuagana na kijana wake Mugeta aliyekwenda kulipigania taifa lake dhidi ya nduli Idi Amin Dada mpakani mwa Tanzania na Uganda.
Kijana wake alikuwa amehitimu darasa la 14 la wakati huo na wakati vita inatangazwa alikuwa katika Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
Vijana hawa wasomi wa wakati huo, walichukuliwa kwenda kulipigania taifa lao. Alitokea JKT na kwenda vitani bila ya kupata nafasi ya kuagana na baba yake na kusema buriani.
Siku chache baada ya vita, asubuhi moja majira ya saa tano, gari la Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) liliingia nyumbani kwake.
Mzee Mtwale alikuwa akikamua ng'ombe wake asubuhi ile alipoulizwa na askari walioshuka kwenye lile gari ikiwa hapo palikuwa ndipo nyumbani kwa Mzee Mtwale.
Alipojibu ndiyo, bila ya kumung'unya maneno wala kufumba fumba, askari wale wa JWTZ walimweleza kwamba walikuwa wameleta mwili wa marehemu mtoto wake aliyefia vitani.
Mzee aliruka na kuanguka kule wakati kikontena cha maziwa kikianguka huko. Kilikuwa ni kilio kikubwa kwake kumpoteza kijana wake tegemeo.
Nadhani shida kubwa zaidi ni kwamba hakupata nafasi ya kusema ‘buriani' wakati kijana wake akienda vitani. Angeagana naye hivyo, angelitegemea lolote na hata kifo cha mwanawe kingekuwa ni jambo lililotegemewa na yumkini asingepatwa na mshtuko mkubwa kiasi hicho.
Nisingependa wanaCCM yawakute yaliyomkuta mzee huyu. Mwaka 2005 walipoingia vitani hawakujua kwamba safari yao ilikuwa ni ya vita na kwamba uwezekano wa kufia vitani ulikuwa mkubwa na hivyo walitakiwa waage kwa kusema buriani. Walidhani safari yao ilikuwa ya kawaida tu.
CCM walidhani mambo ni yaleyale. Walifikiri safari ni ile ile ya kuwadanganya Watanzania kwa kauli hewa za "maisha bora kwa kila Mtanzania", "Tanzania yenye neema inawezekana", "Ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya" kisha ndani ya safari yao ya miaka mitano ikawa "maisha bora zaidi kwa kila fisadi", "Tanzania maskini zaidi inawezekana", "ufisadi mpya kwa staili mpya na viwango vikubwa zaidi". Na baada ya miaka mitano wanakuja na kauli hewa nyingine na kuzoa kura kwa kishindo. Walikuwa wamekosea.
Mwaka 2005 wakati kampeni zikielekea mwishoni mwishoni, tukiwa nyumbani tunajadili na mke wangu majaliwa ya baadaye ya taifa letu, aliniuliza kwamba ni nini hasa kilichowafanya Watanzania wengi kumshabikia Kikwete (mgombea urais kupitia CCM wakati huo), yule yule aliyetoka CCM ile ile iliyoshindwa kuleta maendeleo yale yale kwa miaka 44 ya uhuru?
Na je, Mungu hawaonei Watanzania huruma na kuamua kufanya kitu ili wachaguliwe viongozi wapya wenye mtazamo mpya na wenye nia na uchungu wa dhati wa kuwatoa Watanzania kwenye lindi kubwa la umaskini? Majibu yangu yalikuwa hivi:
"Mungu anawaonea huruma sana Watanzania. Lakini hawezi kulazimisha kuzigeuza nia zao kwa uwezo alio nao. Anaweza tu kuwafunulia wazi hali halisi na kuwaacha wafanye uchaguzi. Wala hatafanya kazi kwa miujiza kama ile aliyoifanya kwa vizazi vya kale ili waamini. Sitegemei kama kuna siku atashusha roho mtakatifu kama alivyofanya siku ya Pentekoste.
Kwamba itokee ghafla siku moja kabla ya kupiga kura na bila kuwapo kwa jambo lolote, viongozi wa vyama vya upinzani wajazwe roho mtakatifu na kuanza kuzungumza kwa lugha ngeni, lakini kila Mtanzania akisikia kwa lugha yake mwenyewe? Kwanba ghafla Freeman Mbowe, Ibrahim Lipumba, Dk. Willibrod Slaa, Hamad Rashid Mohamed, Augustine Mrema, John Cheyo, Zitto Kabwe, Wilfred Lwakatare, James Mbatia, Dk. Sengodo Mvungi, Anna Komu na wengineo wengi wanazungumza kwa lugha ngeni, lakini Wajita wanawasikia wakiongea kwa Kijita, Wasukuma wanasikia wakiongea Kisukuma, Wachaga wanasikia ni Kichaga kinaongewa, Wazaramo nao wanasikia Kizaramo, vivyo hivyo kwa Waha, Wanyakyusa, Wagogo, Wamasai na Waarusha, Wadengereko, Wasambaa, Wangoni, na makabila yote ya Tanzania.
Wote wasikie kwa lugha yao viongozi hawa wa upinzani wakizungumzia uchafu wa chama tawala halafu eti kwa mwujiza huo ndipo sasa wakubali na kuing'oa CCM siku ya uchaguzi. La Hasha! Lakini binafsi naona kitu kimoja ambacho Mungu amekiruhusu kwa kusudi la kuwasaidia Watanzania. Amewaacha waleweshwe na mvinyo ulioandaliwa na wanamtandao, yakiwemo baadhi ya magazeti na kufikia kuamini kwamba Kikwete ni chaguo la Mungu.
Watanzania wamejenga matumaini makubwa juu ya ‘malaika' huyu na hakika hawataamini macho, masikio na fikira zao pale ‘kiumbe' huyu anayeonekana kama kashushwa kutoka juu atakaposimikwa kuwa kiongozi wa taifa hili.
Na ni baada ya yeye kuvurunda, ndipo Watanzania wataamka na kugundua kwamba hakuna ‘chema' kilichosalia ndani ya kapu hili liitwalo CCM.
Na hapo ndipo kifo chake kitakapokuwa kimewadia. Kwangu mimi CCM inapoelekea kushika madaraka ya nchi hii tena, nawaaga kwa kusema ‘buriani' Ni maneno niliyoyasema mwaka 2005 ambayo bado naamini yatatimia. Ni wakati huo kwa mara ya kwanza nilitamka neno ‘buriani' kwa Chama Cha Mapinduzi.
Leo natumia kalamu hii kuwakumbusha wanaCCM wote kwamba walisahau kuaga buriani. Nachelea kusema tusipowakumbusha sasa wataanguka na kuzimia pale chama chao tegemeo kitakapokufa.
Wataruka na kuanguka kule wakati ‘vijikontena' walivyotunza ‘vijisenti' walivyovikamua kwenye EPA, Richmond, Dowans, IPTL na kwingineko vikianguka huko.
WanaCCM, chama chenu kiko taabani. Kinaelekea kule kule ilikokwenda KANU ya Daniel arap Moi, Malawi National Congress ya Kamzu Banda, UNIP (United National Independency Party) ya Kenneth Kaunda, na vinginevyo.
Vipimo vinaonyesha wazi kwamba virusi vya UKIU (Ukosefu wa Kinga ya Ufisadi), vimeenea mwili mzima wa chama kuanzia kichwani (Makao Makuu) hadi nyayoni (kwenye mashina). Napenda niwakumbushe kwamba hapo chama kilipofikia hakuna kinga wala tiba tena labda mjaribu kubadilisha kabisa damu (total blood transfusion) ambapo unaondoa damu yote mwilini yenye virusi na kuweka damu safi.
Hii itamaanisha kuondoa uongozi wote wa chama kuanzia juu hadi chini na kuweka viongozi wapya wanaotoka katika jamii ya kawaida ya wakulima na wafanyakazi ambao hawajaathirika kwa vyovyote na virusi vya ufisadi. Kwa bahati mbaya sana, hii oparesheni haijawahi na haiwezi kufanyika hapa nchini kwa sasa.
CCM ikiwa vitani askari wake wameanza kunyoosheana mitutu ya bunduki na panga zikatazo kuwili. Wamekuwa kama Wafilisti niliowahi kuwazungumzia huko nyuma wakiwa ndani ya kambi yao usiku wakijiandaa na vita dhidi ya Waisrael.
Ghafla wanasikia sauti kubwa ya matarumbeta yapigwayo na Waisrael (wapinzani, wanahabari na wanaharakati mbalimbali) na kushtushwa na miale mikali ya mienge yao ndani ya kambi.
Wafilisti wanadhani Waisrael wameshaingia ndani ya kambi yao na kila mmoja wao anaponyanyuka anadhani yule aliye jirani naye ni Muisrael. Hivyo ananyoosha upanga na kukata kumbe akikata Mfilisti mwenzake hadi wakamalizana.
WanaCCM wanamalizana. Kila anayeshtuka mambo yake yakiwa yameanikwa, anadhani mpinzani ni mwanaCCM mwenzake. Anajibu mapigo kwa kuanika mambo ya yule anayemhisi na hata kupambana naye kwa njia nyingine.
Watashtuka ifikapo asubuhi na kujikuta wamemalizana huku wanamapinduzi wa leo tukitangaza ushindi na kusherehekea kifo cha ‘joka mla watu'.
Hivi sasa wanarusha makombora hata bila kujua wanayaelekeza wapi. Mwulize Anna Abdallah kwamba alikuwa akimwelekezea nani mashambulizi wakati akichangia mjadala wa bajeti bungeni? Mzee Malecela naye juzi aliibuka na kudai kwamba eti kashfa za EPA ziliibuliwa na Dk. Raphael Chegeni, yule Mbunge wa Busega (CCM).
Mara hapo hapo anadai anayestahili sifa ni Rais Kikwete aliyemtimua kazi Gavana aliyekwisha kujiuzulu na kwenda kumficha yeye na hata kifo chake huko Marekani. Rais ambaye hadi leo hataki kuitoa ripoti yote ya wakaguzi wa Ernst & Young kuhusu mabilioni ya EPA, hataki kuwatimua Mwanasheria Mkuu na Mkuu wa TAKUKURU kama alivyoagizwa na Bunge, hataki mafisadi walioiba mabilioni ya EPA watajwe na kukamatwa, hataki ‘mabest' wake waliohusika na kashfa ya Richmond waguswe. Tumsifu kwa lipi? Kwa maoni yangu, hayo yote yalinenwa na wahenga kwamba "mfa maji haachi kutapatapa". Waacheni CCM watapetape, lakini kifo chao ni hakika. Ujumbe kwetu ni mmoja tu, kwamba tuzidishe mashambulizi maana ushindi unakaribia.
Wakati umewadia ambako tutaishuhudia CCM ikiwa ndani ya jeneza lililopakwa rangi ya kijani kibichi. Siku hiyo inakuja mbio na wenye macho msisubiri kuambiwa mtazame. Ila kwa wanaCCM wenyewe hili bado ni fumbo. Hawana habari, wanaendelea kukamua ng'ombe wao madini, misitu, mikataba mibovu, utawala mbovu, ufisadi wa kutisha, na wengineo. Maziwa yanaendelea kuingia vyomboni mwao chururu chururu, si ndo ndo ndo.
Makamanda tunaolibeba jeneza la CCM tusichoke. Twende nalo huko huko Mtera (2010) bila kuchoka. Na tutakapofika wala hatuhitaji lugha ya mafumbo mafumbo (ya kuwanyima wabunge wengi na kuwapa urais) la! Tutawaambia ‘live' kama wale wanajeshi kwamba tumeleta mwili wa marehemu CCM (kuwanyima udiwani, ubunge na urais) aliyefia kwenye vita dhidi ya maisha bora kwa kila Mtanzania.
Hatutajali jinsi mafisadi walioshikilia chuchu za ng'ombe wao akina EPA, Richmond, IPTL na wengine watakavyoruka na kuanguka anguko kuu kuliko lile la Mzee Mtwale. Tutawasaidia kuchimba kaburi na kuizika CCM.
Najua huu utakuwa ujumbe mchungu zaidi kuwahi kutolewa kwa chama hiki kikongwe na wenyewe wakisoma watatamani ‘waikolimbe' kalamu hii isiandike tena. Lakini kalamu hii haiwezi kuuficha ukweli huu. Kiapo chake ni kusema ukweli, tena ‘ukweli uchi' (naked truth) siku zote.
Na wakati mkiwa mmekunja nyuso zenu kwa hasira dhidi ya kalamu hii, yenyewe inawaaga : "Buriani CCM, salamu nyingi kwa KANU, UNIP na wengineo huko mwendako."
smwigamba@yahoo.com
0713 953761
Samson Mwigamba
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
TULIFUNDISHWA katika somo la Kiswahili tulipokuwa darasa la tatu wakati huo, kwamba kuna maneno ya aina tatu yanayotumika tunapoagana.
Tukiagana usiku tunapokwenda kulala tunasema, ‘alamsiki'. Ikiwa kuna mmoja au baadhi yetu wanakwenda safari ya kawaida tu isiyo ya hatari sana, tulifundishwa kuagana kwa kusema, ‘kwaheri ya kuonana'. Na kama ni safari ya hatari ambayo haina uhakika wa kurudi mfano kwenda vitani, tunaagana kwa kusema ‘buriani'.
Mwaka 1978, Mzee Mtwale wa Kijiji cha Namhura jimboni Mwibara wilayani Bunda, hakupata nafasi ya kuagana na kijana wake Mugeta aliyekwenda kulipigania taifa lake dhidi ya nduli Idi Amin Dada mpakani mwa Tanzania na Uganda.
Kijana wake alikuwa amehitimu darasa la 14 la wakati huo na wakati vita inatangazwa alikuwa katika Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
Vijana hawa wasomi wa wakati huo, walichukuliwa kwenda kulipigania taifa lao. Alitokea JKT na kwenda vitani bila ya kupata nafasi ya kuagana na baba yake na kusema buriani.
Siku chache baada ya vita, asubuhi moja majira ya saa tano, gari la Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) liliingia nyumbani kwake.
Mzee Mtwale alikuwa akikamua ng'ombe wake asubuhi ile alipoulizwa na askari walioshuka kwenye lile gari ikiwa hapo palikuwa ndipo nyumbani kwa Mzee Mtwale.
Alipojibu ndiyo, bila ya kumung'unya maneno wala kufumba fumba, askari wale wa JWTZ walimweleza kwamba walikuwa wameleta mwili wa marehemu mtoto wake aliyefia vitani.
Mzee aliruka na kuanguka kule wakati kikontena cha maziwa kikianguka huko. Kilikuwa ni kilio kikubwa kwake kumpoteza kijana wake tegemeo.
Nadhani shida kubwa zaidi ni kwamba hakupata nafasi ya kusema ‘buriani' wakati kijana wake akienda vitani. Angeagana naye hivyo, angelitegemea lolote na hata kifo cha mwanawe kingekuwa ni jambo lililotegemewa na yumkini asingepatwa na mshtuko mkubwa kiasi hicho.
Nisingependa wanaCCM yawakute yaliyomkuta mzee huyu. Mwaka 2005 walipoingia vitani hawakujua kwamba safari yao ilikuwa ni ya vita na kwamba uwezekano wa kufia vitani ulikuwa mkubwa na hivyo walitakiwa waage kwa kusema buriani. Walidhani safari yao ilikuwa ya kawaida tu.
CCM walidhani mambo ni yaleyale. Walifikiri safari ni ile ile ya kuwadanganya Watanzania kwa kauli hewa za "maisha bora kwa kila Mtanzania", "Tanzania yenye neema inawezekana", "Ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya" kisha ndani ya safari yao ya miaka mitano ikawa "maisha bora zaidi kwa kila fisadi", "Tanzania maskini zaidi inawezekana", "ufisadi mpya kwa staili mpya na viwango vikubwa zaidi". Na baada ya miaka mitano wanakuja na kauli hewa nyingine na kuzoa kura kwa kishindo. Walikuwa wamekosea.
Mwaka 2005 wakati kampeni zikielekea mwishoni mwishoni, tukiwa nyumbani tunajadili na mke wangu majaliwa ya baadaye ya taifa letu, aliniuliza kwamba ni nini hasa kilichowafanya Watanzania wengi kumshabikia Kikwete (mgombea urais kupitia CCM wakati huo), yule yule aliyetoka CCM ile ile iliyoshindwa kuleta maendeleo yale yale kwa miaka 44 ya uhuru?
Na je, Mungu hawaonei Watanzania huruma na kuamua kufanya kitu ili wachaguliwe viongozi wapya wenye mtazamo mpya na wenye nia na uchungu wa dhati wa kuwatoa Watanzania kwenye lindi kubwa la umaskini? Majibu yangu yalikuwa hivi:
"Mungu anawaonea huruma sana Watanzania. Lakini hawezi kulazimisha kuzigeuza nia zao kwa uwezo alio nao. Anaweza tu kuwafunulia wazi hali halisi na kuwaacha wafanye uchaguzi. Wala hatafanya kazi kwa miujiza kama ile aliyoifanya kwa vizazi vya kale ili waamini. Sitegemei kama kuna siku atashusha roho mtakatifu kama alivyofanya siku ya Pentekoste.
Kwamba itokee ghafla siku moja kabla ya kupiga kura na bila kuwapo kwa jambo lolote, viongozi wa vyama vya upinzani wajazwe roho mtakatifu na kuanza kuzungumza kwa lugha ngeni, lakini kila Mtanzania akisikia kwa lugha yake mwenyewe? Kwanba ghafla Freeman Mbowe, Ibrahim Lipumba, Dk. Willibrod Slaa, Hamad Rashid Mohamed, Augustine Mrema, John Cheyo, Zitto Kabwe, Wilfred Lwakatare, James Mbatia, Dk. Sengodo Mvungi, Anna Komu na wengineo wengi wanazungumza kwa lugha ngeni, lakini Wajita wanawasikia wakiongea kwa Kijita, Wasukuma wanasikia wakiongea Kisukuma, Wachaga wanasikia ni Kichaga kinaongewa, Wazaramo nao wanasikia Kizaramo, vivyo hivyo kwa Waha, Wanyakyusa, Wagogo, Wamasai na Waarusha, Wadengereko, Wasambaa, Wangoni, na makabila yote ya Tanzania.
Wote wasikie kwa lugha yao viongozi hawa wa upinzani wakizungumzia uchafu wa chama tawala halafu eti kwa mwujiza huo ndipo sasa wakubali na kuing'oa CCM siku ya uchaguzi. La Hasha! Lakini binafsi naona kitu kimoja ambacho Mungu amekiruhusu kwa kusudi la kuwasaidia Watanzania. Amewaacha waleweshwe na mvinyo ulioandaliwa na wanamtandao, yakiwemo baadhi ya magazeti na kufikia kuamini kwamba Kikwete ni chaguo la Mungu.
Watanzania wamejenga matumaini makubwa juu ya ‘malaika' huyu na hakika hawataamini macho, masikio na fikira zao pale ‘kiumbe' huyu anayeonekana kama kashushwa kutoka juu atakaposimikwa kuwa kiongozi wa taifa hili.
Na ni baada ya yeye kuvurunda, ndipo Watanzania wataamka na kugundua kwamba hakuna ‘chema' kilichosalia ndani ya kapu hili liitwalo CCM.
Na hapo ndipo kifo chake kitakapokuwa kimewadia. Kwangu mimi CCM inapoelekea kushika madaraka ya nchi hii tena, nawaaga kwa kusema ‘buriani' Ni maneno niliyoyasema mwaka 2005 ambayo bado naamini yatatimia. Ni wakati huo kwa mara ya kwanza nilitamka neno ‘buriani' kwa Chama Cha Mapinduzi.
Leo natumia kalamu hii kuwakumbusha wanaCCM wote kwamba walisahau kuaga buriani. Nachelea kusema tusipowakumbusha sasa wataanguka na kuzimia pale chama chao tegemeo kitakapokufa.
Wataruka na kuanguka kule wakati ‘vijikontena' walivyotunza ‘vijisenti' walivyovikamua kwenye EPA, Richmond, Dowans, IPTL na kwingineko vikianguka huko.
WanaCCM, chama chenu kiko taabani. Kinaelekea kule kule ilikokwenda KANU ya Daniel arap Moi, Malawi National Congress ya Kamzu Banda, UNIP (United National Independency Party) ya Kenneth Kaunda, na vinginevyo.
Vipimo vinaonyesha wazi kwamba virusi vya UKIU (Ukosefu wa Kinga ya Ufisadi), vimeenea mwili mzima wa chama kuanzia kichwani (Makao Makuu) hadi nyayoni (kwenye mashina). Napenda niwakumbushe kwamba hapo chama kilipofikia hakuna kinga wala tiba tena labda mjaribu kubadilisha kabisa damu (total blood transfusion) ambapo unaondoa damu yote mwilini yenye virusi na kuweka damu safi.
Hii itamaanisha kuondoa uongozi wote wa chama kuanzia juu hadi chini na kuweka viongozi wapya wanaotoka katika jamii ya kawaida ya wakulima na wafanyakazi ambao hawajaathirika kwa vyovyote na virusi vya ufisadi. Kwa bahati mbaya sana, hii oparesheni haijawahi na haiwezi kufanyika hapa nchini kwa sasa.
CCM ikiwa vitani askari wake wameanza kunyoosheana mitutu ya bunduki na panga zikatazo kuwili. Wamekuwa kama Wafilisti niliowahi kuwazungumzia huko nyuma wakiwa ndani ya kambi yao usiku wakijiandaa na vita dhidi ya Waisrael.
Ghafla wanasikia sauti kubwa ya matarumbeta yapigwayo na Waisrael (wapinzani, wanahabari na wanaharakati mbalimbali) na kushtushwa na miale mikali ya mienge yao ndani ya kambi.
Wafilisti wanadhani Waisrael wameshaingia ndani ya kambi yao na kila mmoja wao anaponyanyuka anadhani yule aliye jirani naye ni Muisrael. Hivyo ananyoosha upanga na kukata kumbe akikata Mfilisti mwenzake hadi wakamalizana.
WanaCCM wanamalizana. Kila anayeshtuka mambo yake yakiwa yameanikwa, anadhani mpinzani ni mwanaCCM mwenzake. Anajibu mapigo kwa kuanika mambo ya yule anayemhisi na hata kupambana naye kwa njia nyingine.
Watashtuka ifikapo asubuhi na kujikuta wamemalizana huku wanamapinduzi wa leo tukitangaza ushindi na kusherehekea kifo cha ‘joka mla watu'.
Hivi sasa wanarusha makombora hata bila kujua wanayaelekeza wapi. Mwulize Anna Abdallah kwamba alikuwa akimwelekezea nani mashambulizi wakati akichangia mjadala wa bajeti bungeni? Mzee Malecela naye juzi aliibuka na kudai kwamba eti kashfa za EPA ziliibuliwa na Dk. Raphael Chegeni, yule Mbunge wa Busega (CCM).
Mara hapo hapo anadai anayestahili sifa ni Rais Kikwete aliyemtimua kazi Gavana aliyekwisha kujiuzulu na kwenda kumficha yeye na hata kifo chake huko Marekani. Rais ambaye hadi leo hataki kuitoa ripoti yote ya wakaguzi wa Ernst & Young kuhusu mabilioni ya EPA, hataki kuwatimua Mwanasheria Mkuu na Mkuu wa TAKUKURU kama alivyoagizwa na Bunge, hataki mafisadi walioiba mabilioni ya EPA watajwe na kukamatwa, hataki ‘mabest' wake waliohusika na kashfa ya Richmond waguswe. Tumsifu kwa lipi? Kwa maoni yangu, hayo yote yalinenwa na wahenga kwamba "mfa maji haachi kutapatapa". Waacheni CCM watapetape, lakini kifo chao ni hakika. Ujumbe kwetu ni mmoja tu, kwamba tuzidishe mashambulizi maana ushindi unakaribia.
Wakati umewadia ambako tutaishuhudia CCM ikiwa ndani ya jeneza lililopakwa rangi ya kijani kibichi. Siku hiyo inakuja mbio na wenye macho msisubiri kuambiwa mtazame. Ila kwa wanaCCM wenyewe hili bado ni fumbo. Hawana habari, wanaendelea kukamua ng'ombe wao madini, misitu, mikataba mibovu, utawala mbovu, ufisadi wa kutisha, na wengineo. Maziwa yanaendelea kuingia vyomboni mwao chururu chururu, si ndo ndo ndo.
Makamanda tunaolibeba jeneza la CCM tusichoke. Twende nalo huko huko Mtera (2010) bila kuchoka. Na tutakapofika wala hatuhitaji lugha ya mafumbo mafumbo (ya kuwanyima wabunge wengi na kuwapa urais) la! Tutawaambia ‘live' kama wale wanajeshi kwamba tumeleta mwili wa marehemu CCM (kuwanyima udiwani, ubunge na urais) aliyefia kwenye vita dhidi ya maisha bora kwa kila Mtanzania.
Hatutajali jinsi mafisadi walioshikilia chuchu za ng'ombe wao akina EPA, Richmond, IPTL na wengine watakavyoruka na kuanguka anguko kuu kuliko lile la Mzee Mtwale. Tutawasaidia kuchimba kaburi na kuizika CCM.
Najua huu utakuwa ujumbe mchungu zaidi kuwahi kutolewa kwa chama hiki kikongwe na wenyewe wakisoma watatamani ‘waikolimbe' kalamu hii isiandike tena. Lakini kalamu hii haiwezi kuuficha ukweli huu. Kiapo chake ni kusema ukweli, tena ‘ukweli uchi' (naked truth) siku zote.
Na wakati mkiwa mmekunja nyuso zenu kwa hasira dhidi ya kalamu hii, yenyewe inawaaga : "Buriani CCM, salamu nyingi kwa KANU, UNIP na wengineo huko mwendako."
smwigamba@yahoo.com
0713 953761