Return Of Undertaker
JF-Expert Member
- Jun 12, 2012
- 4,572
- 26,868
TAARIFA KWA UMMA
USIMAMIZI KWA WATOA HUDUMA NDOGO ZA FEDHA
USIMAMIZI KWA WATOA HUDUMA NDOGO ZA FEDHA
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilipitisha Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2018 mnamo tarehe 16 Novemba 2018, ili kutekeleza matakwa ya Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2017. Ibara ya 12 ya Sheria hiyo imeipa mamlaka Benki Kuu ya Tanzania Kusajili, Kusimamia na Kudhibiti biashara ya huduma ndogo za Fedha Tanzania Bara.
Vile vile, Sheria hiyo imetoa tafsiri ya “huduma ndogo za fedha” kuwa ni; biashara inayojumuisha kupokea fedha, kama amana au riba kutokana na amana au mkopo na kuikopesha kwa wanachama au wateja; kupokea amana na kutoa mikopo au huduma ya mikopo kwa wajasiriamali wadogo, kaya au mtu mmoja mmoja; kutoa huduma za mikopo midogo, akiba ndogo, bima ndogo, huduma ndogo za karadha, pensheni ndogo na mikopo midogo ya nyumba; huduma za kutuma fedha na malipo, ikijumuisha huduma ndogo za fedha kwa njia ya mtandao; kutoa elimu ya fedha; na huduma nyingine zinazofanana na hizi kama zitakavyoainishwa kwenye Kanuni za Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2018.
Benki Kuu ya Tanzania imeandaa Kanuni za Udhibiti na Usimamizi wa Huduma Ndogo za Fedha kulingana na madaraja tofauti yaliyoainishwa kwenye Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2018. Pamoja na mambo mengine, kanuni hizi zinagusia vigezo vya utoaji wa leseni, mitaji na utawala wa taasisi ndogo za fedha. Kanuni hizi zimechapishwa kwenye Gazeti la Serikali mnamo tarehe 13 Septemba 2019 pamoja na kwenye tovuti ya Benki Kuu ya Tanzania.
Kwa mujibu wa Kifungu cha 57 cha Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha, watoa huduma wote katika sekta ya huduma ndogo za fedha wanatakiwa kuwasilisha maombi ya leseni au usajili Benki Kuu ya Tanzania au kwenye Mamlaka zilizokasimishwa katika kipindi cha miezi 12 baada ya Sheria kuanza kutumika, yaani tarehe 1 Novemba 2019. Watoa huduma watapaswa pia kukidhi matakwa mengine ya Kanuni za Udhibiti na Usimamizi wa Huduma Ndogo za Fedha katika kipindi tajwa. Aidha, watoa huduma wapya wanaweza kuomba leseni wakati wowote.
Kwa mujibu wa Kifungu cha 14 cha Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha, Benki Kuu ya Tanzania imekasimisha jukumu la usimamizi wa watoa huduma ndogo za fedha waliopo katika Daraja la 3 na 4 kwa Kamisheni ya Maendeleo ya Ushirika na Serikali za Mitaa, mtawalia.
Hivyo basi, watoa huduma ndogo za fedha wanahimizwa kuwasilisha maombi ya leseni ya Benki Kuu katika kipindi kilichotolewa na Sheria kama ifuatavyo:
Watoa huduma ndogo za fedha walio katika Daraja la 2 wawasilishe maombi yao ya leseni Benki Kuu ya Tanzania Makao Makuu au katika matawi yaliyopo Arusha, Mwanza, Zanzibar, Mbeya, Mtwara na Dodoma, kulingana na ukaribu.
Watoa huduma ndogo za fedha walio katika Daraja la 3 wawasilishe maombi yao ya leseni kwenye Ofisi ya Ushirika ya Wilaya au Mrajisi wa Vyama vya Ushirika wa Mkoa, kulingana na ukaribu.
Watoa huduma ndogo za fedha walio katika Daraja la 4 wawasilishe maombi ya kuandikishwa katika Ofisi ya Serikali ya Mtaa iliyokaribu.
Maombi ya leseni au kuandikishwa yanapaswa kuzingatia na kuwa na taarifa zote zilizoainishwa katika Kanuni za watoa huduma wa daraja la 2, 3 na 4, ili yaweze kufanyiwa kazi na leseni husika kutolewa.
Benki Kuu inapenda kusisitiza kuwa kwa mujibu wa Kifungu cha 16 cha Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2018, ni marufuku kwa mtu au taasisi yoyote kufanya biashara ya kutoa huduma ndogo za fedha bila kuwa na leseni au usajili uliotolewa na Benki Kuu ya Tanzania au Mamlaka zilizokasimishwa. Adhabu kali itatolewa kwa mtu au taasisi yoyote itakayokiuka Sheria hii.
Kwa ufafanuzi zaidi kuhusu taarifa hii, tafadhali wasiliana na Mkurugenzi wa Usimamizi wa Sekta ya Fedha, Benki Kuu ya Tanzania-Makao Makuu, Ghorofa ya 6 Mnara wa kaskazini, S.L.P. 2939, Dar es Salaam au wasilisha barua pepe kwa vctarimu@bot.go.tz; nfmongateko@bot.go.tz; na dasasya@bot.go.tz