Richard
Platinum Member
- Oct 23, 2006
- 16,825
- 26,228
Raisi Robert Mugabe wa Zimbabwe leo aliamuru ndege iliyokuwa ikimpeleka nchini Indonesia siku ya Ijumaa igeuzie Dubai na kurudi Harare mara moja.
Mzee Jongwe ambae ana umri wa miaka 92 ndiye raisi mzee kuliko maraisi wote wa barani Afrika, alikuwa akielekea nchini Singapore ambako mara nyingi huwa anakwenda kwa ajili ya kupata matibabu.
Raisi Mugabe aliondoka mapema nchini Swaziland siku ya jumanne na kuacha kikao cha SADC kikiendelea ambapo alianza safari yake ya barani Asia lakini ndege yake ikasimama kwa muda mjini Harare kabla ya kuruka kuelekea mjini Dubai nchini Saudi Arabia.
Maofisa wa raisi Mugabe wamekuwa wagumu kutoa sababu za kiongozi huyo kughairi safari yake ya Asia na kusimama mjini Dubai na baadae leo asubuhi kurudi mjini Harare.
Msemaji wa raisi bwana George Charamba alikanusha madai ya vyombo vya habari kwamba kiongozi huyo ana hali mbaya na kudai kwamba ikiwa hivyo serikali ingesema lakini hizo ni safari ambazo yeye raisi Mugabe alizipanga hapo kabla.
Baada ya kurejea jumamosi asubuhi mzee Jongwe aliwatania waandishi wa habari waliokuwa wakimsubiri kwa hamu kwa kuwaambia kwa kiingereza kwamba, "Yes, I was dead, its true I was dead. I resurrected as I always do. Once I get into my country I real", alisema mzee Jongwe mbele ya waandishi wa habari.
Kiongozi huyo alisema alikwenda Dubai kwa masuala ya kifamilia na alikwenda kumwona mmoja wa watoto wake ambae anamhofia, alisema bila kufafanua zaidi.
Raisi Mugabe hivi sasa serikali yake anayoiongoza inakabiliwa na upinzani wa wananchi ambao wamechoshwa na hali mbaya ya uchumi wa nchi hiyo na vitendo vya rushwa na ufisadi ambavyo vimekithiri katika kila idara ya serikali.
Kumekuwepo na maandamano ambayo yamepangwa na umoja wa vyama vya upinzani nchini humo na polisi walizuia maandamano siku ya Alhamisi iliyopita kwa wiki mbili.
Raisi Robert Mugabe ameitawala Zimbabwe tangu nchi hiyo ipate uhuru mwaka 1980 na wazimbawe hawajawahi kumwona raisi mwingine zaidi ya Mugabe ambae amepanga kugombea kiti hicho tena katika uchaguzi wa raisi mwaka 2018.
Mke wa raisi Mugabe Grace Mugabe amesema muwe wake ataongoza nchi hiyo kutokea kaburini.
Akihutubia mkutano wa hadhara leo jioni ambao uliandaliwa na umoja wa vijana wa ZANU-PF, raisi Mugabe amesisitiza kuwa serikali yake haitavumilia maandamano yanayofanywa na vyama vya siasa na kwamba chini ya utawala wake jambo hilo halitafanikiwa.
Mzee Mugabe aliendelea kuvituhumu baadhi ya vyombo vya nchi za magharibi na khasa Marekani kwamba ndivyo vilivyo nyuma ya maandamano na migomo mbalimbali nchini humo na kudai kuwa wanatumia pesa kuvirubuni vyama hivyo ili kuleta mitafaruku nchini humo na kuzorotesha hali ya kisiasa na kiuchumi kupitia vikwazo kadhaa vya kiuchumi.
Zimbabwe imekuwa katika matatizo ya kiuchumi kwa miongo kadhaa na pia kuwa nchi yenye asilimia 90 ya watu waso na ajira.
Serikali ya Zimbabwe kwa sasa haina hata uwezo wa kulipa mishahara watumishi wake wakiwemo polisi, na hata benki karibu zote nchini humo zinakabiliwa na uhaba wa fedha.
Ndani ya chama tawala tayari kuna mgawanyiko ambapo kuna kambi mbili zinazopimana ubavu kati ya kambi ya Emmerson Mnangagwa ambae ni makamu wa raisi na kambi ya Grace Mugabe mke wa raisi Mugabe.
Leo jioni mjini Harare kumekuwa na utulivu huku wananchi wakitafakari na kusikilizia habari yoyote ile inayosomwa katika redio na televisheni nchini humo na hali ya usalama ipo kama kawaida huku askari kanzu wa CID na wale wa ujasusi wa CIO wakiwa kama kawaida yao wamechanganyika na wananchi wakipiga story za hapa na pale na pia kushiriki maandamano.
Chanzo cha habari: vyombo mbalimbali vya habari duniani.
Nakumbuka wimbo wa Mlimani Park Orchestra na sauti ya mwimbaji Hassan Rehani Bichuka akisema , "Sura ya Zimbabwe inajionyesha Siasa za Mugabe zinazidi kung'ara"
Lakini hadi sasa Zimbambwe ina shida na Mugabe siasa zake zimeshindwa.
Je ikiwa Mugabe anaaga dunia ZANU-PF itaweza kuhimili nguvu ya wapinzani nchini humo au itatawala kwa nguvu?
Je kwa Mugabe kujitangaza kuwania tena uraisi mwaka 2018 anataka kumwachia kiti hicho mke wake au bwana Mnangagwa?
Je wapinzani wana nafasi yoyote ya kushinda uchaguzi wa mwaka 2018?