Magazetini
JF-Expert Member
- Aug 16, 2014
- 588
- 1,698
KIONGOZI wa Chama cha ACT-Wazalendo, Kabwe Zitto anatarajia kuanza ziara ya siku moja mkoani hapa ikiwa ni sehemu ya ziara yake kwa mikoa 10 nchini.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini hapa, Katibu wa ACT-Wazalendo wa Mkoa, Denis Nyandwi alisema lengo la ziara hiyo ni kutambulisha rasmi chama hicho kwa wakazi wa Mkoa wa Dodoma.
"Pia ziara yake hiyo ina lengo la kuwahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi ili wajiandikishe kwenye Daftari la Kudumu la Wapigakura ili waweze kushiriki katika Uchaguzi Mkuu ujao."
Alisema uongozi wa chama wa mkoa ukiongozana na vikundi mbalimbali vya ngoma utampokea rasmi kiongozi huyo katika eneo la Gairo, kesho na atapitiliza moja kwa moja kwenda wilayani Bahi.
"Akishapokewa na uongozi wa mkoa ataelekea moja kwa moja wilayani Bahi katika Kijiji cha Chiduo ambacho chama chetu kilishinda katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambapo atapata fursa ya kuzungumza na wananchi ambapo atavikwa uchifu wa kigogo na baadaye atarudi Dodoma Mjini na kuhutubia wananchi kwenye mkutano wa hadhara utakaofanyika katika Uwanja wa Mashujaa," alifafanua.
Alisema kiongozi huyo wa chama atashiriki katika chakula cha jioni sanjari na kushiriki kwenye mkutano wa ndani wa kuchangia ziara yake kutoka kwa mashabiki, wapenzi na watu wenye mapenzi mema na chama hicho.
Mwenyekiti wa Mkoa wa ACT -Wazalendo, Eva Kaka alisema wanajivunia ushindi wa kishindo ilioupata wakati wa uchaguzi wa serikali za mitaa, ambapo kilishinda na kutwaa uongozi wa Serikali katika kijiji cha Chiduo na kuwataka Watanzania watarajie ushindi katika Uchaguzi Mkuu ujao.
"Tuna uwezekano mkubwa wa kushinda viti katika ubunge na madiwani zaidi ya 30 kwa Mkoa wetu wa Dodoma, hii itawezekana kwa sababu tumejipanga kutoa elimu ya upigaji kura na ile ya uraia kwa wakazi wa Mkoa wa Dodoma," alisema Kaka.
Mratibu wa ziara hiyo kwa Mkoa wa Dodoma, Steven Shekulukai alisema maandalizi kwa ajili ya ziara hiyo yamekamilika. Aliomba vyombo vya habari nchini kushiriki kikamilifu kukitangaza chama kifahamike zaidi kwa wananchi.
CHANZO: Habari Leo