abdulahsaf
JF-Expert Member
- Aug 31, 2010
- 858
- 130
[h=1][/h]
Na Joster Mwangulumbi - Imechapwa 13 June 2012
Tuseme Ukweli
KAMPENI za wakazi wa visiwa vya Unguja na Pemba kutaka muungano huu wa Tanganyika na Zanzibar upitiwe upya au hata kutaka uvunjwe si mpya, lakini zinazidi kupata nguvu.
Hiari ya Wazanzibari kuingia kwenye muungano kwa mazingira ya wakati ule imegeuka utumwa wa kudumu; watake wasitake watabaki kwenye muungano.
Canada imekuwa ikiteswa na jimbo la Québec kutaka kujiamulia mambo yake huku na Hispania ikisumbuliwa na jimbo la Basque kutaka kujitenga.
Québec imo ndani ya Canada na Basque ni sehemu ya Hispania. Tofauti na majimbo hayo, Zanzibar ni nchi huru inayokataliwa kukaa na wenzao wa Tanganyika kuupitia muungano wao.
Nchini Hispania, wanafunzi wa jimbo la Basque, baada ya kuona wanasiasa wanashindwa kushinikiza jimbo hilo kujitenga, mwaka 1959 waliunda kikundi ambacho baadaye kilikuja kujulikana kama Euskadi Ta Askatasuna (ETA). Hiki ndicho hadi leo kinapanga na kufanya mashambulizi kuihujumu serikali ili iridhia eneo hilo kujitenga.
Nchini Canada, wanasiasa wa jimbo la Québec, kwa miaka mingi wamekuwa wakiendesha kampeni kutaka kuwa taifa huru.
Msuguano huo una historia ndefu. Wakijiona kwamba asilimia 80 ya wakazi wake wanazungumza Kifaransa, Québec waliiandama serikali ya Canada kutaka jimbo hilo lipewe uhuru wa kujitawala.
Kampeni zilikuwa kubwa, serikali ikaingiwa hofu kuwa ikiwa ingeitishwa kura ya maoni huenda wanaosema ndiyo yaani wanaotaka kujitenga wangeshinda. Lakini ili kupata ufumbuzi wa kudumu watawala wa Canada waliondoa woga wakaitisha kura ya maoni MARA MBILI.
Kwanza kura ya maoni ilipigwa mwaka 1980, matokeo yakaonyesha waliosema hapana yaani waliopinga pendekezo la Québec kujitenga walishinda; na mara ya pili mwaka 1995 hapana walishinda japo kwa tofauti ndogo sana.
Canada ikapumua, lakini mwaka 2006, Bunge la House of Commons lilipitisha muswada wa ishara kutambua Québec kama taifa ndani ya Canada. Tangu wakati huo kelele zimeisha.
Mfano mwingine mzuri ni wa Jamhuri ya Watu wa China, ambayo wakati wa kampeni za kuyakomboa majimbo yake mawili ya Macau na Hong Kong kutoka kwa wakoloni Wareno na Waingereza, haikupaparika kuunganisha majimbo hayo kwa kila kitu.
Pamoja na kwamba ni sehemu ya China, Hong Kong ambayo sarafu yake ya dola ni ya 10 kwa umadhubuti duniani, inayofuata uchumi huria, maisha ya hali ya juu na uchumi mzuri ilikombolewa kutoka kwa Waingereza mwaka 1997.
Miaka miwili baadaye yaani 1999 ikawa zamu ya Macau kujiondoa kwenye makucha ya Wareno. Uchumi wa Macau unategemea kamari, utalii na uzalishaji nguo.
Hong Kong na Macau zilirejeshwa China chini ya sera ya nchi moja, mifumo miwili tofauti. Kutokana na sera hiyo, serikali kuu ya China inasimamia masuala ya ulinzi na mambo ya nje, lakini masuala mengine yote usalama wa ndani (polisi), usimamizi wa fedha (benki kuu), sera za ushuru wa forodha na uhamiaji ziko chini ya mamlaka za Macau na Hong Kong.
Macau na Hong Kong zinashiriki mikutano mbalimbali ya kimataifa isiyohitaji utambulisho wa kitaifa, kama nchi huru. Hii ina maana Macau na Hong Kong ni nchi huru ndani ya China.
Busara na hekima hii ya China kwa majimbo ya Hong Kong na Macau inaweza kuazimwa na watawala wa Tanganyika na Zanzibar kuondoa ukakasi katika muungano. Rai ya Wazanzibari ni kuwa na muungano unaotoa fursa na utambulisho kwa nchi zote mbili ndani na nje.
Kama Macau na Hong Kong zina mamlaka kamili juu ya usalama wa ndani (polisi), usimamizi wa fedha (benki kuu), sera za ushuru wa forodha, uhamiaji nk kwa nini Zanzibar ikose uhuru kama huu ibaki inategemea kila kitu kutoka serikali ya muungano?
Waumini wa muungano huu watueleze hizo articles of union hazina kifungu kinachoruhusu upande mmoja kuomba mkataba huo kupitiwa upya?
Je, articles of union ni msahafu usiorekebishwa na yeyote hadi Mwalimu Julius Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume watakapofufuka?
Maana sera hii ambayo Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinalazimisha ionekane kuwa inafaa, wengi hawaitaki sasa kama ilivyokataliwa sera ya muungano wa serikali moja. Makubaliano ya kupitia upya muungano huo sasa ni muhimu kwa mustakbali wa taifa.
Wakati wa mfumo wa chama kimoja, CCM ilikuwa na uhakika wa kuzima hoja zote na hata kutumia mabavu kukandamiza uhuru wa maoni. Tangu uliporejeshwa mfumo wa vyama vingi mwaka mwaka 1992, CCM, japo imeshinda chaguzi za 1995, 2000, 2005 na 2010 hakina uhakika wa kutawala milele.
Hii ndiyo sababu mwaka 1994 walibadili katiba ili rais wa Zanzibar asipate tiketi ya moja kwa moja ya kuwa makamu wa rais wa Jamhuri ya Muungano.
Mwaka huo ndio waliongeza kero, wakaingiza suala la mgombea mwenza rais wa Zanzibar anabaki kama waziri au msikilizaji tu. Huyu makamu wa rais mpya, naye hana lolote katika serikali ya Zanzibar isipokuwa kuongeza gharama za uendeshaji wa serikali ya muungano.
Aliyehofiwa mwaka 1994 ni Maalim Seif Sharrif Hamad wa Chama cha Wananchi (CUF) ambaye alitikisa siasa za Zanzibar na inadaiwa alishinda uchaguzi mkuu wa 1995.
Kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2000, ndani ya CCM ukaanza mjadala kuhusu elimu. Wakapendekeza mgombea urais awe na digrii. Aliyelengwa wakati ule alikuwa Augutine Lyatonga Mrema wa Tanzania Labour Party (TLP) ambaye akiwa na NCCR-Mageuzi aliitesa CCM ambayo ilivuruga matokeo ya uchaguzi katika mkoa wa Dar es Salaam.
Baada ya kuona mgombea wao upande wa Zanzibar hakuwa na nondo za Mlimani wakafifisha hoja ya elimu. Kwa hiyo, marekebisho ya katiba yanashikiliwa na CCM, na sasa, kwa kutumia muhuri wa bunge lenye wabunge wengi wa CCM, wameapa muungano huu uliolalamikiwa tangu 26 Aprili 1964, ubaki kama ulivyo.
Wazanzibari waliingia katika muungano kwa hiari yao hivyo wanapotaka upitiwe upya wasikilizwe, hiari yao isigeuzwe utumwa wa milele.
Watawala wana hiari ya kutumia busara ya Canada au China. Muungano hulindwa na watu wenye imani na amani moyoni, hauwezi kulindwa kwa bunduki. Soviet iliyokuwa na majeshi kila mahali Ulaya Mashariki na kuunganisha nchi nyingi, ilisambaratika.
Matukio ya baadhi ya vijana kufanya vurugu kubwa Zanzibar hadi kuchoma makanisa yawaamshe watawala wa serikali zote mbili ya Zanzibar na Muungano. Leo mnawaita majambazi, kesho mtawaita al-Qaeda, lakini keshokutwa yakitokea madhara makubwa ndipo mtapata busara kukaa nao mezani.
Gazeti toleo lenye makala hii
Chanzo Mwanahalisi
Na Joster Mwangulumbi - Imechapwa 13 June 2012
Tuseme Ukweli
KAMPENI za wakazi wa visiwa vya Unguja na Pemba kutaka muungano huu wa Tanganyika na Zanzibar upitiwe upya au hata kutaka uvunjwe si mpya, lakini zinazidi kupata nguvu.
Hiari ya Wazanzibari kuingia kwenye muungano kwa mazingira ya wakati ule imegeuka utumwa wa kudumu; watake wasitake watabaki kwenye muungano.
Canada imekuwa ikiteswa na jimbo la Québec kutaka kujiamulia mambo yake huku na Hispania ikisumbuliwa na jimbo la Basque kutaka kujitenga.
Québec imo ndani ya Canada na Basque ni sehemu ya Hispania. Tofauti na majimbo hayo, Zanzibar ni nchi huru inayokataliwa kukaa na wenzao wa Tanganyika kuupitia muungano wao.
Nchini Hispania, wanafunzi wa jimbo la Basque, baada ya kuona wanasiasa wanashindwa kushinikiza jimbo hilo kujitenga, mwaka 1959 waliunda kikundi ambacho baadaye kilikuja kujulikana kama Euskadi Ta Askatasuna (ETA). Hiki ndicho hadi leo kinapanga na kufanya mashambulizi kuihujumu serikali ili iridhia eneo hilo kujitenga.
Nchini Canada, wanasiasa wa jimbo la Québec, kwa miaka mingi wamekuwa wakiendesha kampeni kutaka kuwa taifa huru.
Msuguano huo una historia ndefu. Wakijiona kwamba asilimia 80 ya wakazi wake wanazungumza Kifaransa, Québec waliiandama serikali ya Canada kutaka jimbo hilo lipewe uhuru wa kujitawala.
Kampeni zilikuwa kubwa, serikali ikaingiwa hofu kuwa ikiwa ingeitishwa kura ya maoni huenda wanaosema ndiyo yaani wanaotaka kujitenga wangeshinda. Lakini ili kupata ufumbuzi wa kudumu watawala wa Canada waliondoa woga wakaitisha kura ya maoni MARA MBILI.
Kwanza kura ya maoni ilipigwa mwaka 1980, matokeo yakaonyesha waliosema hapana yaani waliopinga pendekezo la Québec kujitenga walishinda; na mara ya pili mwaka 1995 hapana walishinda japo kwa tofauti ndogo sana.
Canada ikapumua, lakini mwaka 2006, Bunge la House of Commons lilipitisha muswada wa ishara kutambua Québec kama taifa ndani ya Canada. Tangu wakati huo kelele zimeisha.
Mfano mwingine mzuri ni wa Jamhuri ya Watu wa China, ambayo wakati wa kampeni za kuyakomboa majimbo yake mawili ya Macau na Hong Kong kutoka kwa wakoloni Wareno na Waingereza, haikupaparika kuunganisha majimbo hayo kwa kila kitu.
Pamoja na kwamba ni sehemu ya China, Hong Kong ambayo sarafu yake ya dola ni ya 10 kwa umadhubuti duniani, inayofuata uchumi huria, maisha ya hali ya juu na uchumi mzuri ilikombolewa kutoka kwa Waingereza mwaka 1997.
Miaka miwili baadaye yaani 1999 ikawa zamu ya Macau kujiondoa kwenye makucha ya Wareno. Uchumi wa Macau unategemea kamari, utalii na uzalishaji nguo.
Hong Kong na Macau zilirejeshwa China chini ya sera ya nchi moja, mifumo miwili tofauti. Kutokana na sera hiyo, serikali kuu ya China inasimamia masuala ya ulinzi na mambo ya nje, lakini masuala mengine yote usalama wa ndani (polisi), usimamizi wa fedha (benki kuu), sera za ushuru wa forodha na uhamiaji ziko chini ya mamlaka za Macau na Hong Kong.
Macau na Hong Kong zinashiriki mikutano mbalimbali ya kimataifa isiyohitaji utambulisho wa kitaifa, kama nchi huru. Hii ina maana Macau na Hong Kong ni nchi huru ndani ya China.
Busara na hekima hii ya China kwa majimbo ya Hong Kong na Macau inaweza kuazimwa na watawala wa Tanganyika na Zanzibar kuondoa ukakasi katika muungano. Rai ya Wazanzibari ni kuwa na muungano unaotoa fursa na utambulisho kwa nchi zote mbili ndani na nje.
Kama Macau na Hong Kong zina mamlaka kamili juu ya usalama wa ndani (polisi), usimamizi wa fedha (benki kuu), sera za ushuru wa forodha, uhamiaji nk kwa nini Zanzibar ikose uhuru kama huu ibaki inategemea kila kitu kutoka serikali ya muungano?
Waumini wa muungano huu watueleze hizo articles of union hazina kifungu kinachoruhusu upande mmoja kuomba mkataba huo kupitiwa upya?
Je, articles of union ni msahafu usiorekebishwa na yeyote hadi Mwalimu Julius Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume watakapofufuka?
Maana sera hii ambayo Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinalazimisha ionekane kuwa inafaa, wengi hawaitaki sasa kama ilivyokataliwa sera ya muungano wa serikali moja. Makubaliano ya kupitia upya muungano huo sasa ni muhimu kwa mustakbali wa taifa.
Wakati wa mfumo wa chama kimoja, CCM ilikuwa na uhakika wa kuzima hoja zote na hata kutumia mabavu kukandamiza uhuru wa maoni. Tangu uliporejeshwa mfumo wa vyama vingi mwaka mwaka 1992, CCM, japo imeshinda chaguzi za 1995, 2000, 2005 na 2010 hakina uhakika wa kutawala milele.
Hii ndiyo sababu mwaka 1994 walibadili katiba ili rais wa Zanzibar asipate tiketi ya moja kwa moja ya kuwa makamu wa rais wa Jamhuri ya Muungano.
Mwaka huo ndio waliongeza kero, wakaingiza suala la mgombea mwenza rais wa Zanzibar anabaki kama waziri au msikilizaji tu. Huyu makamu wa rais mpya, naye hana lolote katika serikali ya Zanzibar isipokuwa kuongeza gharama za uendeshaji wa serikali ya muungano.
Aliyehofiwa mwaka 1994 ni Maalim Seif Sharrif Hamad wa Chama cha Wananchi (CUF) ambaye alitikisa siasa za Zanzibar na inadaiwa alishinda uchaguzi mkuu wa 1995.
Kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2000, ndani ya CCM ukaanza mjadala kuhusu elimu. Wakapendekeza mgombea urais awe na digrii. Aliyelengwa wakati ule alikuwa Augutine Lyatonga Mrema wa Tanzania Labour Party (TLP) ambaye akiwa na NCCR-Mageuzi aliitesa CCM ambayo ilivuruga matokeo ya uchaguzi katika mkoa wa Dar es Salaam.
Baada ya kuona mgombea wao upande wa Zanzibar hakuwa na nondo za Mlimani wakafifisha hoja ya elimu. Kwa hiyo, marekebisho ya katiba yanashikiliwa na CCM, na sasa, kwa kutumia muhuri wa bunge lenye wabunge wengi wa CCM, wameapa muungano huu uliolalamikiwa tangu 26 Aprili 1964, ubaki kama ulivyo.
Wazanzibari waliingia katika muungano kwa hiari yao hivyo wanapotaka upitiwe upya wasikilizwe, hiari yao isigeuzwe utumwa wa milele.
Watawala wana hiari ya kutumia busara ya Canada au China. Muungano hulindwa na watu wenye imani na amani moyoni, hauwezi kulindwa kwa bunduki. Soviet iliyokuwa na majeshi kila mahali Ulaya Mashariki na kuunganisha nchi nyingi, ilisambaratika.
Matukio ya baadhi ya vijana kufanya vurugu kubwa Zanzibar hadi kuchoma makanisa yawaamshe watawala wa serikali zote mbili ya Zanzibar na Muungano. Leo mnawaita majambazi, kesho mtawaita al-Qaeda, lakini keshokutwa yakitokea madhara makubwa ndipo mtapata busara kukaa nao mezani.
Gazeti toleo lenye makala hii
Chanzo Mwanahalisi