Ya San Suu Kyi na Anna Makinda wetu!

Ustaadh

JF-Expert Member
Oct 25, 2009
413
19
MWISHONI mwa wiki kulitokea matukio mawili ya kihistoria yanayohusu wanawake ambayo yaliigusa nafsi yangu. Moja lilitokea huko Burma na la pili lilitokea hapa nyumbani. La huko Burma lilihusu kuachiliwa huru kwa mpambanaji maarufu wa demokrasia duniani, Aung San Suu Kyi, na la hapa nyumbani lilihusu kuchaguliwa kwa spika wa kwanza mwanamke, Anna Makinda.

Japo matukio hayo hayafanani, na japo Burma na Tanzania ni mbali mno, napenda kuyazungumzia kidogo na kueleza ni kwanini yaliigusa nafsi yangu. Nikianzia na la Burma ambalo lilikuwa ni habari kubwa katika tevisheni zote za kimataifa – CNN, BBC, Sky News, Aljazeera nk, kuachiliwa kwa mpambanaji huyo mwanamke kulipokewa kwa furaha kote duniani. Maelfu kwa maelfu ya wa-Burma waliovalia fulana zilizoandikwa We love you San Suu Kyi (tunakupenda San Suu Kyi) waliizunguka nyumba ya shujaa wao huyo, mjini Rangoon, wakiimba kwa furaha kumkaribisha nyumbani. Ni tukio lililogusa hisia za wengi duniani walioliangalia kupitia televisheni. Kwa kigezo chochote kile, Aung San Suu Kyi, ni mwanamke ambaye ameweka historia ya upambanaji wa kutetea haki za binadamu sawa na iliyowekwa na kina Nelson Mandela (Madiba) na Mahatma Gandhi. Licha ya kuweka maisha yake na ya familia yake katika hatari kubwa, Aung San Suu Kyi alipambana na majenerali wa kijeshi wa tawala tofauti za Burma kwa zaidi ya miaka 21; huku miaka karibu 15 kati ya hiyo akiwa anatumikia vifungo vya ndani (house arrest).

Majenerali hao wa tawala dhalimu za Burma walitumia kila mbinu kujaribu kumlainisha mama huyo ikiwa ni pamoja na vitisho vya kumuua, kumhonga vyeo au hata kujaribu kumpa mapesa mengi; lakini vyote havikumyumbisha. Alisimama imara kutetea haki na kuililia demokrasia, na alikuwa tayari kufia kizuizini.
Ni ujasiri huo uliomfanya afahamike na kuheshimika duniani kote kama championi wa demokrasia au kama alivyosema Rais Obama wa Marekani; "alama ya dunia ya ujasiri na matumaini" (global champion of courage and hope). Mama huyo ataendelea kukumbukwa na dunia hata baada ya kifo chake (Mungu aepushe mbali); maana alijitolea maisha yake yote kutetea wanyonge wa nchi yake ya Burma. Kwa hakika, waliomtunuku tuzo ya amani ya Nobel akiwa bado kizuizini, hawakukosea hata kidogo.

Tukirejea ya hapa nyumbani ya Anna Makinda, si lengo langu kujaribu kufananisha ujasiri wa spika wetu huyo mpya mwanamke na wa Aung San Suu Kyi; maana kufanya hivyo ni kujaribu kulinganisha mlima na kichuguu! Lakini ninachojaribu kueleza ni kwamba changamoto za kidemokrasia zinazoikabili nchi yetu, kwa sasa, zitamhitaji Anna Makinda kuonyesha japo robo tu ya ujasiri wa Aung San Suu Kyi, na hiyo ni kama ana matamanio ya kuacha legacy ya maana kwa vizazi vijavyo vya hapa nchini kama ambavyo mama huyo wa shoka wa Burma ataiacha nchini mwake. Changamoto kubwa ya kidemokrasia ambayo Anna Makinda anayo, ni kuhakikisha Tanzania inapata Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano, na inapata Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi ndani ya kipindi cha miaka mitano ya uspika wake. Nasisitiza kwamba hiyo ndiyo changamoto kubwa kushinda nyingine zote zinazomkabili mama huyo; maana kama yaliyotokea katika uchaguzi mkuu uliopita (Oktoba 31) yametufunza lolote, basi, ni dhahiri ghasia na umwagaji damu hautaepukika kama tutaingia katika uchaguzi wa mwaka 2015 tukiwa na katiba hii hii na tume hii hii ya uchaguzi.

Ni jambo lisilofurahisha kulisema, lakini hatuna budi kulisema; kwamba kama si kuchachamaa kwa wanachama wa CHADEMA katika majimbo ya Arusha Mjini, Ubungo, Mbeya Mjini na huko Mwanza, wagombea wa CCM wangetangazwa washindi kinyume na matokeo ya kura, na hapo ghasia na umwagaji damu visingeepukika.
Kwa hiyo, sasa wagombea watarajiwa wa Upinzani kwa uchaguzi wa mwaka 2015 wanajua fika kwamba kama wanataka kura zao zisichakachuliwe na CCM, basi, wafuasi wao hawana budi kuchachamaa na kulala karibu na yalipo masanduku ya kuru ikibidi hata kwa wiki nzima, na wawe tayari kwa lolote. Katika hali hiyo, umwagaji damu utaepukika? Kwa maneno mengine, uchakachuaji wa kura tulioushuhudia katika uchaguzi wa Oktoba 31 unaweza kufanywa tu na CCM chini ya mazingira hovyo ya Katiba yetu ya sasa ya Jamhuri ya Muungano, na chini ya mazingira hovyo ya Tume Taifa ya Uchaguzi ya sasa.
Kwa hiyo, vilio vya kutaka tuwe na Katiba mpya na tuwe na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi si vilio vya kutaka tu kuiondosha CCM madarakani. La hasha. Ni vilio vya kutaka kuwepo mazingira ya haki sawa kwa wote katika uchaguzi wetu mkuu wa kuwapata rais, wabunge na madiwani – mazingira ambayo, kwa hakika, ndiyo yatakayotuokoa kwenye umwagaji damu unaoinyemelea kwa kasi nchi yetu.

Kwingineko Afrika (mfano Zimbabwe au Kenya) waliziba masikio ili wasivisikie vilio hivyo, na kilichotokea huko sote tunakijua. Ni majuzi tu Kenya imezinduka na kuandika Katiba mpya, na sasa iko mbioni kuunda Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi. Lakini ilichukua hatua hizo baada ya damu kuwa imeshamwagika. Je, hivyo ndivyo nasi tutakavyo? Bila shaka jibu ni hapa. Sasa natambua kilio hicho kitatolewa kwa nguvu mwakani ndani ya Bunge letu si tu na wabunge wa kambi ya Upinzani; bali pia wachache kutoka chama tawala cha CCM wanaoipenda nchi yao kwa dhati. Kilio hicho kitamkuta Anna Makinda amekalia kiti cha uspika. Je, ataonyesha japo robo tu ya ujasiri wa Aung San Suu Kyi na kukisikiliza na kukishughulikia au ataziba masikio yake; kama ambavyo wahafidhina ndani ya CCM na Serikali yake wangependa afanye?
Anna Makinda ana chaguo la njia moja tu ya kufuata kati ya mbili zilizopo. Anaweza kuzizima kikatili hoja binafsi zitakazowasilishwa ndani ya bunge kudai Katiba mpya na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, na kwa hiyo kwa kufanya hivyo akakaribisha umwagaji damu katika chaguzi zetu zijazo, au anaweza kuvisikiliza vilio hivyo, na hivyo kuusimamia vyema bungeni mchakato utakaotuwezesha kuwa na vitu hivyo. Kama ataongozwa na maslahi yake binafsi na maslahi ya chama chake CCM, na hivyo akaichagua njia ya kwanza, ni dhahiri hataacha legacy yoyote nchini, na jina lake litasahaulika haraka mno atakapokiacha kiti cha uspika. Lakini kama ataichagua njia ya pili, ni dhahiri legacy yake italifanya jina lake lishabikiwe nchini kama ambavyo jina la mwanamke mwenzake, Aung San Suu Kyi, litakavyoendelea kushabikiwa nchini Burma miaka mingi tu baada ya kifo chake. Vyovyote vile; nimkumbushe tu Anna Makinda wetu kwamba Watanzania kamwe hawatamsamehe kama atashusha viwango vya Bunge hilo kutoka katika vile vilivyowekwa na Spika aliyemtangulia, Samwel Sitta.

Maana, umpende Sitta au usimpende, ukweli unabaki pale pale; nao ni kwamba aliikomesha tabia ya miaka mingi ya Bunge letu kuwa ni muhuri tu wa Serikali. Kwa maneno mengine, uspika wa Sitta uliosababisha hata Waziri Mkuu, Edward Lowassa kujiuzulu, utakumbukwa nchini kwa miaka mingi ijayo kuliko uspika wa Pius Msekwa. Licha ya mazingira magumu na kupigwa vita na wahafidhina ndani ya chama chake cha CCM (hasa mafisadi,) Sitta (against all odds) alipambana na kufanikiwa kuleta mageuzi ndani ya Bunge hilo kwa kuboresha mfumo na kanuni zake ili ziendane na wakati tuliopo. Ni nani asiyejua kwamba hata utaratibu ule wa ndani ya Bunge wa Waziri Mkuu kupigwa maswali ya papo kwa papo na wabunge, ni matunda ya juhudi za Sitta za kujenga demokrasia ya kweli ndani ya Bunge?

Kwa hiyo, ujumbe wangu kwa Anna Makinda ni kwamba Samwel Sitta alishamsafishia njia, na anachopaswa yeye kufanya ni kuifuata tu njia hiyo ya kuelekea kwenye demokrasia ya kweli. Hataitendea haki nchi hii kama katika kipindi cha uspika wake atalirejesha Bunge letu huko lilikotokea badala ya kulifanya lisonge mbele zaidi katika kuisaka demokrasia ya kweli nchini mwetu. Nihitimishe kwa kumkumbusha tena Anna Makinda wetu kwamba mwenzake, Aung San Suu Kyi, atakumbukwa daima katika Burma si kwa sababu tu ni mwanamke; bali kwa sababu alikuwa championi wa kweli wa demokrasia na mpambanaji jasiri.
Vivyo hivyo Anna Makinda wetu hatakumbukwa nchini kwa sababu tu eti alikuwa spika wa kwanza mwanamke; bali anaweza kukumbukwa kama mpambanaji jasiri aliyepigania bungeni kuwepo kwa Katiba mpya na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, na kwa kufanya hivyo aliliepusha taifa lake na umwagaji damu uliokuwa ukilinyemelea.
Tafakari.

Source: http://www.raiamwema.co.tz/news.php?d=2744
 
Umenena vema, lakini huyu Anna Makinda ni nani?
Ni mwanaharakati? Mzawa? Kiongozi aliye committed? Mhafidhina wa CCM? Au zao pandikizi la mafisadi?
Mi nadhani Makinda ni zao pandikizi la mafisadi (you shall prove what im saying some days ahead)
Kwanza Makinda amesema hatambui kama CCM kuna mafisadi. Hizi ni dalili za kwanza za kuonesha kushindwa. Either ndo ameanza kazi ya waliomweka kwenye kiti (mafisadi) au ameonesha udhaifu wa kiutenda (kukosa trend).
Lolote kati ya haya litamfanya Makinda ashindwe kuongoza bunge, maana kama yuko kwa maslahi ya mafisadi ni hatari, lakini kama nyuma ya kivuli cha woga ni hatari zaidi.
 
Too much expectations..

Labda niwe devil's advocate hapo...katiba mpya na tume huru ya uchaguzi ni vitu ambavyo vinatakiwa viwe demand-driven..It can't happen out of blue, spika alete hizo motions ndani ya bunge out of nowhere.
 
Back
Top Bottom