WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), George Simbachawene ametangaza kuifuta Bodi inayosimamia jengo la Machinga Complex, Dar es Salaam Aidha Waziri amemsimamisha kazi Meneja anayesimamia jengo hilo na kumtaka kwenda katika ofisi za jiji kwa ajili ya kumpangia kazi nyingine.
Simbachawene aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na Jumuiya ya wafanyabiashara nchi nzima. Jengo hilo kwa sasa limekabidhiwa kwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kwa ajili ya kuandaa mpango wa kuwaingiza wafanyabiashara bila masharti huku ukiangaliwa utaratibu mpya kwa wafanyabiashara hao.
Alisema jengo hilo limekuwa likitumiwa kinyume na lengo ambalo walitakiwa wafanyabiashara kulitumia kwa gharama kidogo lakini limekuwa likitumiwa na watu wengine tofauti na wafanyabiashara jambo ambalo limesababisha kushindwa kulipa deni linalodaiwa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF).
“Jengo hili limejengwa kwa gharama kubwa sana lakini kwa matumizi hayo kumesababisha kushindwa kumaliza deni ambalo tunadaiwa na tumelipa Sh milioni 50 pekee,” alisema Simbachawene.
Aidha waziri huyo pia ameziagiza halmashauri zote nchini kutotoa leseni kwa wafanyabiashara wa nje hadi tamko kutoka katika Wizara yake lengo likiwa ni kuongeza nafasi kwa wafanyabiashara wa nyumbani na endapo watatoa leseni hizo lazima zipitie katika wizara yake.
Pia amewaagiza wakuu wa mikoa wote nchini kuwa walezi wa vyama vya jumuiya katika mikoa yao na wakuu wa wilaya wawe wasimamizi wa jumuiya hizo katika wilaya zao kwani utaratibu huo utasaidia kuwaleta karibu wafanyabiashara.