Waziri atolewa jasho

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,299
33,080
headline_bullet.jpg
Ni kwa maswali magumu ya wananchi
headline_bullet.jpg
Ajibu baadhi, mengine asema hana ubavu
headline_bullet.jpg
Aagiza wasibughudhiwe, ni demokrasia



Nagu%2818%29.jpg

Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Dk. Mary Nagu.



Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko, Dk. Mary Nagu, jana alikuwa katika wakati mgumu, baada ya kuulizwa maswali 'magumu' juu ya serikali yake na utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambayo baadhi yake alishindwa kuyatolea majibu.
Kutokana na ugumu wa maswali hayo, Dk. Nagu alijikuta akitamka wazi kuwa yeye kama kiongozi, hawezi kusema chochote, isipokuwa amesikia maelezo ya wananchi na hivyo mawazo na kero zao, ataziwasilisha serikalini ili zifanyiwe kazi haraka.
“Nimesikia kero zenu, lakini hapa sifanyi uamuzi isipokuwa nazipeleka serikalini kwa ajili ya utekelezaji wa haraka,” alisema Dk. Nagu.
Miongoni mwa maswali yaliyomtoa jasho Dk. Nagu yaliulizwa na wanachama wa CCM, huku wapinzani nao wakipigilia msumari wa moto kwa kumuuliza maswali mazito.
Aliyekuwa wa kwanza kumbana Waziri Nagu ni Mwalimu Lastwell Siyame, aliyetaka kujua sababu za serikali kuwazuia wakulima kuuza mazao yao nchi jirani ya Zambia wakati ikiwa haitoi msaada wowote kwa mkulima kufanikisha kilimo.
Mwalimu Siyame alisema wakulima wadogo ambao hawapati msaada wa serikali tangu wanapoandaa mashamba yao hadi kuvuna, wanapopata mavuno yao badala ya kusaidiwa kupata soko la uhakika, wanazuiwa kulifikia soko lililo jirani nao ambalo ni nchi jirani, wakati wakiwa hawana uwezo wa kulifikia soko la ndani ambalo liko mbali nao.
"Tunaomba utueleze, inakuwaje njaa ya Moshi, ambayo sisi kama wakulima wadogo hatuna uwezo wa kufikisha huko mazao yetu inasababisha tuzuiwe kuuza mazao Zambia ambako tunaweza kufika kwa urahisi na tukapata faida sababu kuna bei nzuri?” alihoji Mwalimu Siyame.
Diwani John Mshana kutoka wilayani Ileje naye alimuuliza Waziri Nagu aeleze kuhusu viwanda vya sukari vya Tanzania vinafanya nini na lini sukari hiyo ambayo inauzwa ghali itafika wilayani Ileje.
Augustino Mtega, ambaye ni mkazi wa Tunduma, alimbana Waziri akimtaka aeleze kwa nini mabati yanayotengenezwa na viwanda vya Tanzania hayana ubora, ni mepesi kiasi cha kutobolewa na gunzi linaporushwa juu ya paa.
Alisema mabati kutoka nje ingawa yanauzwa bei ghali ni magumu, imara kuliko ya Tanzania ambayo nayo yanauzwa bei mbaya.
Swali kama hilo pia liliulizwa na mkazi mwingine wa Tunduma aliyejitambulisha kwa jina moja la Nicodemu, ambaye pia alilalamikia ubora wa saruji, akidai kuwa nyumba zinazojengwa kwa saruji ya siku hizi zinabomoka haraka kuliko zile zilizojengwa kwa saruji ya zamani, hali ambayo inaonyesha kuwa ubora wa saruji nao umeporomoka.
Alfred Sanga, mkazi wa mjini Tunduma, alimuuliza Waziri Nagu kuwa kwa nini serikali haijaweka duka angalau moja mjini Tunduma linalouza bidhaa za Tanzania bila ushuru ili kuwavutia wateja kutoka nje ya nchi.
Kwa upande wake, Fred Siwale, mkazi wa eneo la Mpemba, nje kidogo ya mji wa Tunduma, alisema benki za Tanzania kwa sasa hazina msaada kwa wakulima na wafanyabiashara wadogo, kwa sababu hata zikiwakopesha fedha huanza kuwadai baada ya mwezi mmoja.
“Benki za Tanzania, zikitukopesha mwezi huu, mwezi ujao zinataka tuanze kurejesha fedha zao, kwa mtindo huu benki hizi zinakuwa hazina msaada kwa wafanyabiashara wadogo, sasa waziri utatusaidia vipi?” alihoji Siwale.
Naye Paulo Songa, aliyejitambulisha kuwa ni mwanachama wa CCM, alimuuliza Dk. Nagu kuwa inakuwaje mbolea ya ruzuku inayotolewa na serikali wanaiona ikipita kwenda Zambia huku wao wakiikosa.
“Katika hili la mbolea, sisi wakulima wadogo tunanyonywa na wafanyabiashara, kama sio kuna hila ndani ya serikali,” alisema Songa.
Mwalimu Elija Msuya ambaye alijitambulisha kuwa ni mwanachama NCCR-Mageuzi, alisema anatamani kila mwaka uwe wa uchaguzi, kwa sababu kila uchaguzi unapokaribia wananchi huambiwa maneno matamu yenye kutia matumaini na viongozi wao. Alisema uzoefu unaonyesha kuwa kila uchaguzi unapokaribia bei za bidhaa mbalimbali hushuka kidogo na baada ya uchaguzi zinapaa na kusababisha maisha ya wananchi kuwa magumu kupita kiasi.
Alisema Tunduma ina viwanda viwili tu, kimoja cha kusindika nafaka na kingine ambacho hakina wataalamu ni cha kusindika taka, hivyo akamtaka Waziri aeleze lini kiwanda hicho cha taka kitapata wataalamu ili kiweze kufanya kazi.
Bilgrahamu Kusiluka, alimweleza Waziri Nagu kuwa serikali ya awamu ya nne imekuwa legelege katika kudhibiti huduma za afya, ambapo hivi sasa mjini Tunduma na maeneo mengine watoto wa madaktari ndiyo wanauza kwenye maduka ya dawa licha ya kuwa hawana utaalamu wowote.
Alisema pia dawa nyingi ni feki, ambazo baadhi ya makopo ya dawa hayana lebo, hali ambayo inawakosesha imani kama dawa wanazonunua ni sahihi.
Mkazi mwingine wa Tunduma aliyemtolea uvivu Waziri Nagu ni Joseph Kibona, ambaye alimweleza kuwa kama kuna wizara iliyochoka katika Serikali ya awamu ya nne ni ya Viwanda, Biashara na Masoko, anayoiongoza yeye Waziri Dk. Nagu.
Alisema viwanda vingi vimekufa na hakuna mazingira mazuri yaliyoandaliwa na serikali kwa ajili ya kuvifufua wala kujenga vipya.
“Serikali kwenye viwanda imechoka kabisa, vingi vimekufa, havifufuliwi wala havijengwi vipya, hivi sasa wananchi tunaishi kwa kutumia bidhaa feki ambazo ndiyo nyingi madukani na hata hapa Tunduma zimejaa tele,” alisema Kibona huku akishangiliwa.
Mkazi wa mwisho kuuliza swali alikuwa Gasto Sinka, ambaye alimuuliza Dk. Nagu kuwa ni lini maji ya bomba yatafika Tunduma kama ambavyo waliahidiwa na CCM wakati wa kampeni zake mwaka 2005.
Pia Sinka aliulalamikia uongozi wa Halmashauri ya Mji Mdogo wa Tunduma kwa kupiga marufuku baiskeli kuegeshwa mjini Tunduma kwa madai kuwa ni uchafu.
“Mheshimiwa Waziri, leo naomba utueleze kama baiskeli ambazo tunazinunua kwa taabu ili zitusaidie sisi wananchi wa kipato kidogo ni uchafu, kwa nini viwanda bado vinazitengeneza,” alihoji Sinka.
Alipoinuka kujibu mwaswali hayo ya wananchi, Waziri Nagu alisema baadhi ya maswali yako nje ya uwezo wake kwa vile yanashughulikiwa na wizara nyingine, lakini kwa vile serikali ni moja, amesikia na atafikisha kero zao.
Hata hivyo, Waziri Nagu ambaye awali alihutubia akiwa amepanda jukwaani, baada ya maswali ya wananchi alishindwa kurejea jukwani na badala yake kujibu baadhi ya maswali hayo akiwa chini ya jukwaa.
Akizungumzia suala la sukari, Dk. Nagu alisema Tanzania ina viwanda vichache vya sukari ambavyo vipo Kilombero, Morogoro; Arusha Chini, Kilimanjaro na Kagera huko Bukoba.
Alisema viwanda hivyo ni vichache kwa sababu kila vinapotakiwa kujengwa lazima kuwepo na miwa ambayo ndiyo malighafi pekee inayotumika kutengeneza sukari. Alisema ili kutatua tatizo la uhaba wa sukari, atawasiliana na Bodi ya Sukari ili itoe vibali kwa wafanyabiashara wadogo waingize sukari kutoka nchi za jirani, badala ya kuagizwa kutoka India.
Kuhusu bidhaa za Tanzania kutokuwa na ubora, hasa mabati na saruji, Waziri Nagu alisema amelipokea na kuwa atawasiliana na Shirika la Viwango (TBS) walishughulikie kwa kina. Waziri Nagu alisema suala la duka lisilokuwa na ushuru (duty free) amelisikia na atazungumza na wadau ili kuwepo na duka moja kubwa litakalouza bidhaa za Tanzania pekee ambazo hazitalipiwa ushuru katika mpaka wa Tunduma.
Kuhusu mbolea ya ruzuku kupelekwa Zambia, maduka ya dawa kuuzwa na watu wasiokuwa na sifa, benki kutosaidia wakulima, baiskeli kuitwa uchafu na vibali vya kusafiria, Waziri Nagu alisema hayo yako nje ya uwezo wake na kuwa ameyachukua na atayafikisha katika sehemu husika.
Akihitimisha ziara yake, wakati wa chakula cha mchana kwenye ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mbozi, mjini Vwawa, Waziri Nagu aliwashukuru maofisa wa Serikali kwa maandalizi mazuri ya ziara yake na kuwaeleza kuwa maswali yaliyoulizwa na wananchi mjini Tunduma yawazindue na kuwaonyesha udhaifu wao ulipo.
Aliwaagiza kutowasumbua wote waliouliza maswali, kwa sababu wakifanya hivyo watakuwa wanaibana demokrasia na siku nyingine watashindwa kusikia kero za wananchi, ambazo kwa kiasi fulani zinasaidia kuwaonyesha mahali penye udhaifu.
Waziri Nagu alihitimisha ziara yake ya kiserikali ya siku mbili mkoani Mbeya na kurejea jijini Dar es Salaam.
Wakati huo huo, viongozi wa Vyama vya Wafanyakazi mkoani Mbeya, juzi waligoma kushiriki mkutano wa Waziri Nagu, kwa madai kwamba kushiriki mkutano huo ingekuwa wanajipendekeza kwa serikali ambayo wana mgogoro nayo kutokana na kushindwa kuyapatia ufumbuzi madai yao.
Waziri Dk. Nagu, juzi aliitisha mkutano kuzungumza na wananchi wa Mkoa wa Mbeya kuelezea utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambapo ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya ilitoa mwaliko pia kwa viongozi wa vyama vya wafanyakazi ambao waligoma kuhudhuria. Mkutano huo uliofanyika ukumbi wa Chuo cha Uhasibu Mbeya, ulihudhuriwa na wakuu wa wilaya, wakurugenzi wa halmashauri, wenyeviti wa halmashauri, viongozi wa vyama vya siasa na wawakilishi wa taasisi mbalimbali za serikali na binafsi zilizopo mkoani humu.
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Mkoa wa Mbeya, Kibwana Njaa, akizungumza na Nipashe jana alisema ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya iliwapelekea barua za mwaliko wa kuhudhuria mkutano wa Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko.
Imeandaliwa na Emmanuel Lengwa na Thobias Mwanakatwe, Mbeya.



CHANZO: NIPASHE
 
Waziri Dk. Nagu, juzi aliitisha mkutano kuzungumza na wananchi wa Mkoa wa Mbeya kuelezea utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambapo ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya ilitoa mwaliko pia kwa viongozi wa vyama vya wafanyakazi ambao waligoma kuhudhuria. Mkutano huo uliofanyika ukumbi wa Chuo cha Uhasibu Mbeya,

Kumbe zile ziara za kijinga zimeanza! Hivi haya mambo mimi mtizamo wangu ni Kampeni kwa fedha zetu walipa kodi. Hiyo Ilani si wanayo na wanatakiwa kufanya evaluation ili waweze kuandaa ilani ya uchaguzi ujao sasa hawa wanafanya nini? Naona CCM bado haipati dira wala mwelekeo hivi kwa nini hawa watu wenye mawazo finyu wasipumzike waache nchi kwa watu wenye uwezo?
 
Back
Top Bottom