Waziri ageuzia kibao wenzake

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Waandishi Wetu


230_nundu_img_0.png



WAZIRI wa Uchukuzi, Omar Nundu


WAZIRI wa Uchukuzi, Omar Nundu, amekuwa akipambana na wenzake wizarani akitaka mradi wa upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam uliokwisha kupitishwa, sasa usitishwe, badala yake, uanzishwe upya na usimamiwe na kampuni ya chaguo lake, imefahamika.

Ameiambia Raia Mwema wiki hii kwamba baadhi ya viongozi wenzake wanataka kujinufaisha na mradi huo wa karibu shilingi bilioni 600, ambao tayari ulikwisha kupata kibali serikalini kupitia Wizara ya Fedha iliyotoa idhini kwa Benki ya Exim ya China kuugharimia.

Maelezo hayo ya Waziri Nundu yanatokana na madai ya kuwapo kwa mipango ya ufisadi katika mradi wa upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam, ambao katika moja ya matoleo yaliyopita ya gazeti hili, tuliripoti kuwa waziri huyo ni kati ya viongozi wanaotajwa kuingilia mradi huo kinyume cha taratibu za uendeshaji wa mradi wenyewe.


"Ipo kampuni inayoshinikizwa na watu ili ichukue mradi huo (wakati) haina fedha bali inategemea wizara ikope Exim Bank kuendesha mradi huo. Fanyeni utafiti mtagundua ni kina nani wanashinikiza… Utaratibu wa kutoa na kupokea rushwa ndiyo napingana nao na hiyo ni moja ya sababu inayosababisha kuzushiwa mambo ya uongo," alisema Nundu akikanusha kuhusishwa katika tuhuma za ufisadi unaohusu mradi huo wa upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam.


Katika mahojiano maalumu na Raia Mwema, Nundu amekwepa kuzungumzia kuhusu kuwapo kwa mawasiliano kati ya Serikali ya Tanzania na China pamoja na Benki ya Exim ya China, inayotoa fedha hizo na badala yake amebeza mpango wa kukopa kutoka benki hiyo huku yeye akiendelea kutafuta mwekezaji mpya.


Amekiri kufanya mazungumzo na kuingia makubaliano na kampuni nyingine nje ya nchi kuhusiana na mradi huo huo wa upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam eneo la gati namba 13 na gati namba 14, ingawa inafahamika kwamba kuna zuio maalumu la Serikali linalowataka mawaziri, ambao kimsingi ni wanasiasa tu,( si watendaji), kuingia mikataba nje ya nchi.


Akikwepa kuzungumzia mchakato uliopo kati ya Serikali ya Tanzania na China wa kuikopesha Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) ili kupanua eneo la gati namba 13 na namba 14, Waziri Nundu anaupigia debe mchakato wake mpya akisema kwamba kampuni zote zinazotaka kushiriki mradi huo zitashindanishwa upya.


Maelezo ya Nundu yanazungumzia kampuni zitakazokuja nchini kujenga na kuendesha eneo hilo nyeti la bandari japo taarifa za awali zinasema mradi anaoupinga unalenga kuiwezesha TPA kuwa ndiyo inaendesha shughuli nzima katika gati hizo baada ya ujenzi kukamilika. Imefahamika pia kwamba katika mpango wake, Nundu analenga ujenzi huo wa Bandari ya Dar es Salaam uhusishe pia ujenzi wa Bandari ya Mwambani, Tanga lilipo jimbo lake. (Nundu ni Mbunge wa Tanga Mjini).


Awali Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Fedha, ilihitimisha mchakato wa mradi huo ulioanzishwa na Wizara ya Uchukuzi kwa kuandika barua Januari 24, kwenda benki ya Exim ya China kuhusiana na mkopo huo, barua yenye kumbukumbu namba TYC/E/450/2/02, na mradi huo umepangwa kuanza Julai, mwaka huu.


Uchunguzi wa Raia Mwema umebaini kwamba, katika kikao cha Baraza la Mawaziri cha hivi karibuni, Nundu alitaka kuwasilisha mapendekezo mapya juu ya mradi huo, kabla ya Rais Jakaya Kikwete, kumshauri kuboresha mambo aliyoyakuta yameanzishwa na mtangulizi wake, Dk. Shukuru Kawambwa.


Pamoja na kukiri kuwa amekwenda China na Dubai kutafuta wawekezaji wapya, Nundu alisema; "Hili la mimi kuleta mkandarasi kutoka China lilitoka huko kwenu; sikuleta mkandarasi kutoka China na hao mnaofanya nao kazi sijui mnafanya kazi na kina nani wanaojaribu kuchafua jina langu".


Akizitaja kampuni alizoingia nazo makubaliano, Nundu alisema moja ni kampuni kutoka Dubai ambayo ilikuwa tayari kujenga mradi huo kwa fedha zao wenyewe kwa gharama ya dola za Marekani bilioni 250, na nyingine kutoka China iliyokubali kujenga mradi huo pamoja na ule wa Bandari ya Mwambani, Tanga, na akadai kwamba hajakwamisha mradi huo bali uko katika "mchakato".


Akikanusha kufanya uamuzi wa masuala mbalimbali bila kufuata ushauri wa wataalamu, Nundu anasema kwamba katika safari zake za nje ya nchi, amekuwa akifuatana na maofisa wa wizara yake na wale wa mashirika husika wakiwamo wa TPA na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA).


Akidhihirisha kuwapo kwa uhusiano mbaya kati yake na watendaji aliowakuta wizarani, Nundu anazungumzia kwa mara ya pili hadharani kuhusu kumuondoa mmoja wa maofisa wake wa ngazi ya juu walioazimwa kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, anasema;


"Kumbuka nilimuondoa mkurugenzi (Dk. William Nshama) kutokana na kasi ya utendaji wake kutoridhisha. Nikasema miaka mitano nitajenga miundombinu kwa kasi hii ambayo watu wanaleta proposal (mapendekezo) hawajibiwi? Nikaona vema mkurugenzi akae pembeni. Mwaka mzima nimekaa hapa nafikiria nitafanya kazi gani (kama) watu wanajitokeza lakini naambiwa maombi yao hawajibiwi."


Taarifa zisizo rasmi ambazo zimelifikia Raia Mwema zinasema Dk. Nshama ambaye ni mhandisi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam aliombwa na aliyekuwa waziri kabla ya Nundu, Dk. Shukuru Kawambwa, kwenda kuongeza nguvu wizarani kwa kuwa ni mbobezi katika masuala ya usafirishaji.


Sasa baada ya kutemwa na Nundu, Dk. Nshama amechukuliwa na Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, kwa kazi zile zile alizokuwa akifanya kwa Waziri Nundu.


Mradi huo wa upanuzi wa gati namba 13 na gati namba 14, uliorodheshwa katika miradi muhimu ya TPA mwaka 2008 ukiwa na gharama za dola za Marekani milioni 525, ambazo zitawezesha kupanuliwa kwa Bandari ya Dar es Salaam pamoja na kina chake ili kuweza kushindana na Bandari ya Mombasa, nchini Kenya na bandari mpya inayojengwa eneo la Lamu.


Kumekuwa na madai kutoka kwa wadau mbalimbali wa sekta ya uchukuzi wakiwamo wamiliki wa kampuni za meli, mawakala na hata watumishi wa umma kwamba matatizo makubwa katika sekta ya bandari yanatokana na ukiritimba uliopo kwa Kitengo cha Makontena ambacho kinaendeshwa na Kampuni binafsi ya Tanzania International Container Terminal Services Limited (TICTS).


Ni madai hayo pamoja na mengine ndiyo yameisukuma Serikali kuanza mradi wa upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam ambayo inategemewa na nchi kadhaa kupokea mizigo yao, zikiwamo nchi za Rwanda, Burundi na Kongo (DRC), Malawi na Zambia.


TICTS ambayo iliingia nchini katika mazingira tata, imekuwa katika migogoro ya mara kwa mara na wadau na hasa wafanyakazi wake kutokana na kile kinachoelezwa ya kwamba kuna imkono wa "wanasiasa wachafu", ambao wamekuwa wakiendelea kuyumbisha sekta ya uchukuzi nchini.


Katika eneo hili la Afrika Mashariki, taarifa zinasema, ni Tanzania pekee, katika hatua inayotafsiriwa kuwa ya kujinyima mapato, ndiyo imekabidhi uendeshaji wa biashara kubwa ya kupakia na kupakua mizigo bandarini kwa kampuni binafsi.

Nchini Kenya mradi mkubwa umezinduliwa Pwani ya Lamu ambao utaziunganisha nchi za Kenya, Ethiopia na Sudan Kusini. Ujenzi wa mradi huo mkubwa wa bandari unatarajiwa kugharimu dola za Marekani bilioni 23, na utakuwa Kusini Mashariki mwa pwani ya nchi ya Kenya kwenye Mji wa Lamu mpakani mwa Somalia.

Mradi huo utajumuisha pia ujenzi wa bomba la mafuta, reli na barabara kuunganisha Mji wa Lamu na Sudan Kusini pamoja na Ethiopia. Nchi iliyopata uhuru wake hivi karibuni ya Sudan Kusini ina mipango ya kutumia Lamu kama njia kuu ya kusafirishia mafuta yake.








 
  • Thanks
Reactions: GIB
Hii Mikataba ya Ajabu, Dr. Shukuru Kwawabwa alisaini sasa Nundu anakuja anataka avuruge mikataba yote na yeye asaini Mipya eti kuwa Ufisadi.

Hatutaendelea Nchi yetu, na Kenya na big Lamu project
 
Tatizo maslahi binafsi..Siku tukiwa wazalendo Tanzania itakuwa kama Malaysia in just 2 years.
 
Maslahi binafsi. Kama umemfukuza mkurugenzi kwa madai kuwa hafanyi kazi vizuri wakati huo huo jembe kama Magufuli amemchukua ujue asilimia kubwa wewe nundu una matatizo. Niliwahi kumuona Magufuli akiwakoromea wakurugenzi wazembe katika wizara fulani na wengi wao walinyooka wakawa wanachapa kazi. Kama kweli huyo mkurugenzi ana tatizo naamini Magufuli asingemchukua, hivyo basi namalizia kwa kusema Nundu una lako jambo hapo, acha lisije likakutokea puani.
 
haiwezeka mradi wa wizara yake akose ten pasent..huo ndo mwiko kwa serikali ya jk hapo atang'ang'ania na yeye lazima apate.!
 
Akizitaja kampuni alizoingia nazo makubaliano, Nundu alisema moja ni kampuni kutoka Dubai ambayo ilikuwa tayari kujenga mradi huo kwa fedha zao wenyewe kwa gharama ya dola za Marekani bilioni 250, na nyingine kutoka China iliyokubali kujenga mradi huo pamoja na ule wa Bandari ya Mwambani, Tanga, na akadai kwamba hajakwamisha mradi huo bali uko katika "mchakato".


Hapo Kwenye red $250 bilion ?
MR Nundu give me a break kama hizo pesa ni zao hivi Tajiri wa kwanza ana kiasi gani vile
Kama kukudanganya ali kudanganya wewe kwa suti sio Watanzania
 
mi nafikiri kwa sasa hii nchi tungesimamisha shughuli zote za miradi,sijui uwekezaji na utalii.. tusubiri nchi itakaporudi mikononi mwa wananchi chini ya cdm ndio tuanze upya hayo mambo..au mnaonaje bandugu..!!!!
 
Back
Top Bottom