Watoto wa mbwa watishia amani

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
HOFU imetanda kwa wakazi wa Mtaa wa Matokeo Kata ya Mabibo baada ya kuzuka kundi la vijana wa kihuni wanaojiita ‘Watoto wa Mbwa’ wanaofanya uhalifu katika eneo hilo.Akizungumza na gazeti hili, Mwenyekiti wa Mtaa wa Matokeo, Dustan Ernest, amesema kundi hilo limesababisha uvunjifu wa amani kwa wakazi wa eneo hilo na kuwafanya waishi kwa mashaka.

“Wakazi wa eneo hili kwa sasa wanaishi kwa mashaka wakiliogopa kundi hili, nimeshapokea kesi mbalimbali za matukio ya uhalifu yaliyofanywa na vijana wa kundi hili,” amesema Ernest

Amesema katika kuweka mambo sawa aliwaita wazazi wa watoto hao na kuwataka wawaonye vijana wao kwa kuwa vitendo wanavyovifanya ni vibaya katika jamii.

Wazazi hao waliahidi kulitekeleza hilo lakini vijana hao bado wanaendelea na vitendo viovu.

“Baada ya kuzungumza na wazazi pia niliwaita vijana hao kwa kuwa tunaishi nao hapa mtaani na wanafahamika, nikawaeleza waache kufanya uhalifu nao wakanikubalia lakini walivyotoka pale wakaenda kumbaka binti wa watu na kumuibia mali zake,” amesema Ernest

Ameongeza kuwa aliamua kuandika barua na kuipeleka kituo kidogo cha Polisi cha Luhanga tangu Aprili 8, 2010, akiomba apatiwe Polisi watakaoshirikiana na kamati yake katika kupambana na wahuni hao lakini hakujibiwa ndipo alipoandika barua nyingine na kuipeleka kwa Mkuu wa Kituo cha Urafiki.

“Nimepeleka kilio changu kwa Mkuu wa Kituo cha Urafiki naamini atanipa askari tutakaofanya nao kazi ya kuwasaka wahuni hao walikojificha na ikiwezekana kuingia nyumba kwa nyumba kwa kuwa tunafahamu wanakoishi,” amesema.

Mwenyekiti huyo ameliomba jeshi la Polisi kulishughulikia tatizo hilo haraka kwani wanapozidi kuchelewa wananchi wanazidi kuumia na wanapochoshwa uamua kuchukua sheria mikononi kwa kuwaua wahalifu.
 
Back
Top Bottom