Elections 2015 Wanawake wanaweza, Dr. Asha-Rose Migiro lini uliweza?

KennedyMmari

JF-Expert Member
Dec 12, 2012
979
183
Na Charles William
Dr. Asha-Rose Mtengeti Migiro ni moja kati ya majina ya watanzania wachache wenye rekodi za kushika nafasi kubwa na za heshima kubwa duniani, akiwa amewahi kuteuliwa kushika nafasi ya unaibu katibu mkuu wa umoja wa mtaifa(UN) kwa miaka mitano tokea mwaka 2007 mpaka mwaka 2012 akiwa ndiye msaidizi wa mtendaji mkuu wa wa UN Ban Ki moon katika kipindi hicho chote.

Itakumbukwa kuwa hapo awali Dr. Migiro alikuwa mhadhiri wa chuo kikuu cha Dar es Salaam kitivo cha sheria kwa zaidi ya miaka 19 tokea mwaka 1981 mpaka mwaka 2000 alipopata uteuzi wa ubunge na kisha uwaziri katika wizara ya maendeleo ya jamii, wanawake na watoto nafasi ambayo aliitumikia kwa miaka mitano mpaka mwaka 2005 ambapo Rais Benjamini Mkapa alimaliza uongozi wake na kisha Rais Jakaya Mrisho Kikwete kuingia madarakani kama Rais wa awamu ya nne.

Ni katika kipindi hiki cha awamu ya nne ndipo ambapo mwanamama huyu msomi na mzaliwa wa wilaya ya Songea mkoa wa Ruvuma alipopata umaarufu zaidi mara baada ya kuteuliwa kuwa mbunge na kisha kuteuliwa kuwa waziri akishikilia wizara ya mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa, nafasi ambayo Rais Kikwete alikuwa akiishika kabla ya kuwa Rais huku Dr. Migiro akipewa Benard Membe kama naibu waziri wake na yeye binafsi akiweka rekodi ya kuwa mwanamke wa kwanza kushika wadhifa huo tangu nchi hii kupata uhuru mnamo Desemba 1961!

Mwaka mmoja baada ya Dr. Migiro kuikwaa nafasi hiyo nyeti tokea January 2006 mpaka Februari 2007 taarifa zilizofurahisha watanzania wengi zilisambaa ya kwamba mwanamama huyu ameteuliwa na katibu ,mkuu wa umoja wa mataifa UN bwana Ban Kimoon kuwa naibu katibu mkuu wa umoja huo huku akiweka rekodi nyingine ya kuwa mtanzania wa kwanza kushika wadhifa wa juu zaidi katika umoja wa mataifa lakini pia akiingia kwenye rekodi kama naibu katibu mkuu wa tatu wa umoja huo tangu kuanzishwa kwa nafasi hiyo mwaka 1997.

Baada ya uteuzi huyo gazeti kongwe la Marekani yalipo makao makuu ya umoja huo linalojulikana kwa jina la New York times liliripoti kuwa uteuzi wa Dr. Migiro ulikuwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi ya Ban Ki-moon aliyoitoa wakati wa kuomba kuungwa mkono katika nafasi hiyo ambapo aliahidi kuteua mwanamke kutoka katika nchi za dunia ya tatu kushika wadhifa huo, gazeti hilo lilibainisha pia kuwa uteuzi huo ulitokana na urafiki na ukaribu baina ya Dr. Migiro na Ban Ki-moon kwani walikuwa wakifanya kazi pamoja kama mawaziri wa mambo ya nje ya nchi zao, huku Ban akiiwakilisha Korea Kusini.

Baada ya utumishi wa miaka mitano katika umoja wa mataifa hatimaye ilibainika kuwa bwana Ban Ki moon hakuwa tayari kumteua tena Dr. Migiro kuendelea kushika wadhifa huo na hivyo kurejea Tanzania ambapo Chama cha mapinduzi kilimteua kuwa kuwa katibu wa siasa na mahusiano ya kimataifa wa chama hicho na baada ya muda kidogo mwaka 2013 Rais Kikwete alimteua kuwa mkuu wa chuo kikuu huria cha Tanzania lakini kabla hata ya mwaka mmoja kutimia tangu uteuzi huo Rais Kikwete kwa mara nyingine tena alimteua kuwa mbunge na kisha kumteua kuwa waziri wa katiba na sheria mara baada ya mabadiliko ya baraza la mawaziri.

Nimeamua kueleza kwa kina kuhusu historia na rekodi za mwanasiasa, msomi na wakili huyu ambazo nadhani ni miongoni mwa vitu vilivyomsukuma yeye binafsi au kusukumwa na watu wake wa karibu kuwania Urais wa Tanzania kupitia CCM huku akiwa ni miongoni mwa wanawake wanne waliojitokeza kuwania nafasi hiyo lakini pia miongoni mwa wanasiasa zaidi ya 40 waliojitokeza kuiwania nafasi hiyo ya juu zaidi katika uongozi wa taifa hili.

Pamoja na rekodi zote hizi za za kuteuliwa kitaifa na za kimataifa lakini hakuna mahali popote ambapo nimejiridhisha kuwa Dr. Asha Rose Migiro alifanya makubwa katika nafasi aliyokabidhiwa kuanzia ile ya kuwa waziri wa maendeleo ya jamii jinsia na makundi maalum, waziri wa mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa, Naibu katibu mkuu wa umoja wa mataifa (UN) na hata sasa katika uwaziri wa katiba na sheria. Ukweli huu unanifanya niamue kusema wanawake wanaweza lakini Migiro hajawahi kuweza kufanya lolote la kufanya sasa tumfikirie kushika urais wa Tanzania!!

Namuona Dr. Migiro kama msomi mzuri, mwanadiplomasia, wakili na mwanasiasa mwanamke aliyewahi kupata nafasi ya kushika nafasi nyeti na za juu ndani nan je ya nchi lakini pia namuona kama mwanasiasa ‘laini laini' ambaye amekuwa na bahati ya kuonwa na kuteuliwa mara kwa mara pengine kwa bahati au kwa mazingira na mahusiano mazuri ya kikazi baina yake na wakuu wake wa kazi. Namuona laini na mwepesi katika medani ya siasa za kupambana, kukabili changamoto na kushinda kwa bila kubebwa ndani na nje ya chama.

Mtazamo huu hauna maana kuwa miongoni mwa wanaume zaidi ya 40 waliojitokeza kuna ambao wana uwezo mkubwa sana au wamefanya makubwa kuliko mwanazuoni huyu, la hasha! Wapo ambao uwezo wao unafaa kuhojiwa hata kwenye uongozi wa ngazi ya udiwani lakini nimeamua nimzungumzie huyu kidogo katika kipindi hiki ambacho CCM inaelekea kutuletea mgombea mmoja na katika harakati za kuua makundi, uhasama na misuguano uamuzi wowote unaweza kuchukuliwa.

Katika harakati za kuua makundi na kupunguza misuguano ndani ya CCM uamuzi wa dharura unaweza kuchukuliwa ukiwemo kama ule uliochukuliwa mnamo mwaka 2010 ambapo wagombea uspika Andrew Chenge, Samuel Sitta na wengine ambao ni wa jinsia ‘me' walionekana kuwa wangeweza kukipasua na kukisababishia nyufa chama hicho katika mchakato huo na kisha wote wakawekwa kando na pambano likabaki kuwa la kina mama pekee na hatimaye Anna Semamba Makinda akawaangusha akina Anna Abdallah.

Ni kweli kwamba miongoni mwa wanawake wanne waliojitokeza Dr. Asha Rose Migiro ndiye mwanasiasa mwenye uzoefu wa kushikilia uongozi katika nafasi nyingi zaidi za juu ndani nan je ya nchi lakini hili halitufanyi tusimchunguze ‘samaki' huyu kinaga ubaga na kumuangalia kila upande kujua ubora na uzima wake kabla ya kumfanya kuwa kitoweo chetu. Kipi kikubwa alichowahi kukifanya katika nyadhifa alizopewa? Jee amewahi kuonyesha uthubutu wa kwenda mbele za wananchi na kuomba kupewa majukumu yoyote ya utumishi zaidi ya kupewa uteuzi tu? Kwanini mumlete mtu ambaye hajawahi kuiomba dhamana yoyote ya kuwaongoza wananchi popote zaidi ya kuteuliwa ilihali yupo kwenye uwanja wa siasa?

Wengi mtaniuliza jee kwa kigezo hicho nimemuondoa (disqualify) na jaji Augustino Ramadhani katika kinyang'anyiro hiki? Jee kwa mtazamo huu nimewang'oa na wagombea wengine kama balozi Amina Salum Ally, Dr. Mwele Malecela pia na wanasiasa wengine bila kujali jinsia zao ambao hawajawahi kuwa wanasiasa wa majukwaani na kuwania nafasi zozote za uwakilishi wa moja kwa moja wa wananchi? Mimi nasema hapana, sijawaengua katika kinyang'anyiro hiki lakini angalau basi kama hawawezi kusema kubwa linalofanania au kukaribiana na Urais watuambie waliwahi kuaminika na kupewa majukumu yoyote na wananchi? Kama hawajawahi kwanini wanautaka Urais? NIKATEKELEZE ILANI YA CHAMA!!!

Ni kweli Dr. Migiro ni msomi, ni kweli amewahi kupewa majukumu makubwa ndani na nje ya nchi, ni kweli pia hajawahi kufanya lolote kubwa katika nyadhifa alizoaminika linalofaa kufanya tumfikirie na kumpa nafasi ya Urais, ni kweli pia kuwa hajawahi kuwa na uthubutu wa kupambana kwa nguvu zake mwenyewe kisiasa na kujituma katika kutaka kuwawakilisha wananchi moja kwa moja, pengine akiamini kwa elimu yake, hadhi yake chama cha mapinduzi kinaweza kumteua tu katika nafasi za viti maalum au Rais anaweza kumteua katika nafasi zake 10 za kuteua wabunge au labda hajawahi kuwa na muda wa kufanya hivyo. Jee, ameiva na kufaa kukabidhiwa majukumu makubwa ya Urais?

Wapo wanaosema Urais ni taasisi na inahitaji msimamizi tu wala sio mtu binafsi au mtu mmoja(an individual) kuiendesha lakini kwanini tumpe mtu laini laini na asiye na rekodi za kuomba dhamana kwa wananchi? Jee katika medani ya siasa za uthubutu na mapambano, ukomavu na uwakilishi wa wananchi anaweza kuwekwa chungu kimoja na wanawake wengine walioacha viti maalumu na kutongoja uteuzi wa Rais wakaenda kupambana majimboni dhidi ya wanaume ndani na nje ya vyama na wakashinda? Mathalani bi Anne Kilango Malecela kule Same?
Miongoni mwa wanawake wanne waliochukua fomu za Urais ndani ya CCM ambao ni balozi Amina Salum Alli, Dr. Mwele Malecela, Dr. Migiro na bi Monica Mbega , Dr. Migiro ndiye mwenye jina kubwa kisiasa kuliko wenzake kutokana na kuwahi kuteuliwa katika nyadhifa kubwa zaidi lakini katika siasa za uthubutu na mapambano katikati ya mfumo wa ndani nan je ya chama anaachwa mbali sana na bi. Monica Mbega. Anaachwa mbali na wanawake wengine wengi tu ambao hawajachukua fomu hiyo kama Dr. Mary Nagu ambaye ni waziri na mbunge wa Hanang, anaachwa mbali pia na mbunge aliyepambana ndani ya chama na anayepambana na kero za wananchi jimboni kama Beatrice Shelukindo(Kilindi Tanga).

Bi Monica Mbega ukiacha elimu nzuri aliyonayo(elimu ni jambo muhimu) lakini angalau amewahi kuonyesha uthubutu wa kupambana na changamoto za moja kwa moja za wananchi wa Iringa mjini katika vipindi tofauti akiwa kama mbunge tangu mwaka 1995, ana uzoefu mkubwa wa kuwa ndani ya serikali pia kwani amewahi kuhudumu kama naibu waziri kisha waziri katika serikali na pia kushika nafasi za ukuu wa mkoa na zinginezo, amepambana ndani na nje ya chama na kushinda lakini pia kushindwa nje ya chama kama alivyodondoshwa katika ubunge wa jimbo hilo mwaka 2010.

Dr. Mary Nagu yeye pia ukiachilia mbali elimu kubwa aliyonayo (sawa na Dr. Migiro) lakini pia ana uzoefu wa siasa za kitanzania kwa kupambana ndani na nje ya mbeleko ya chama na kushinda, mwanamama huyu alianzia ubunge wa viti maalum ndani ya CCM kwa miaka 10 tokea mwaka 1995 mpka 2005 na kisha kugombea ubunge wa jimbo la Hanang na kushinda katika vipindi viwili mfululizo 2005 na kisha 2010 lakini pia ameshika nafasi za uwaziri katika wizara zaidi ya tatu katika nyakati tofauti jambo linalompa uzoefu wa siasa za kitanzania, uzoefu serikalini na uthubutu wa mapambano ya kisiasa kuliko Dr. Migiro.

Pamoja na rekodi hizo za kina mama wengine ndani ya CCM kuonyesha uthubutu, ukomavu na uzoefu wa siasa za hapa nchini kuliko Naibu katibu mkuu huyu wa zamani wa umoja wa mataifa lakini bado nguvu ya wapambe na hata vyombo vya habari(publicity) inamuweka juu zaidi na hata kumtabiria kuwa anaweza kupitishwa na kamati kuu ya chama hicho kuwa miongoni mwa wana CCM watano ambao majina yao yatapelekwa halmashauri kuu(NEC) ya chama hicho ili kupigiwa kura huku jina lake likilenga kuwaridhisha na kuwafurahisha wanawake kuwa wanaweza na wamefikia mpaka hatua ya mwisho ya mchato huo!!

Naam, hilo linaweza kufanyika na hakika wanawake wataambiwa wanaweza na wamefikia hatua kubwa na wakijaribu tena wanaweza kufanya vizuri zaidi! Ni kweli wanawake wanaweza hasa kwa kutazama wagombea wanaume waliojitokeza kuwania nafasi ya Urais kupitia CCM, historia zao, elimu zao na rekodi zao za kazi katika majukumu waliyowahi kupewa zinalingana kabisa na zile za wanawake wengi waliopo ndani ya CCM lakini chonde chonde Dr. Asha Rose Mtengeti Migiro sio miongoni mwa wanasiasa wanawake wenye uzito wa kutosha kuweza kukabili changamoto na mapambano katika kipindi cha hali tete kwa taifa letu kama hiki.


Hatujawahi kumuona akiweza bila kuwezeshwa kwa jicho la uteuzi wa mezani. Akiwa Rais nani atamuwezesha kuongoza taifa? Ni kweli takuwa na wasaidizi wa kazi zake lakini yeye ndiye atakuwa muamuzi wa mwisho wa mambo mengi yanayohusu hatima ya taifa hili, atamudu? Hata hivyo siku nikipata mtoto wa kike sitaacha kumsihi asome sana na kumtia moyo kwamba anaweza kushika wadhifa mkubwa duniani kama ilivyowahi kutokea kwa Dr. Asha-Rose Mtengeti Migiro, Hakika umekuwa mfano wa kutamaniwa na wanawake wengi Tanzania.


Makala hii imetoka leo tarehe 9th, June 2015 katika gazeti la Mawio
 
Huyu mama na spika makinda wametia aibu kubwa wanawake wa Tanzania, sidhani kama itatokea mwanamke kutoka nchi hii akapewa wadhifa wowote duniani, tutabaki kuteuana tu ndani ya chama, wameonyesha udhaifu mkubwa ambao haujawahi fanywa na mwanamke yoyote duniani.
 
Tatizo hawezi kuwa na maamuzi, kama sasa tu ana nafasi ya uwaziri tu tunaona madudu, je akiwa huko juu zaidi si ndiyo shughuli, kil la kheri katika mchakato
 
katika vitu ambayo watanzania ni mabigwa ni kujipendeza hata wasomi wakubwa nchini wameingia katika mfumo huu wa kujipendeza kwa mabosi au viongozi ndo maana watu wengi na viongozi wengi wamepata vyeo c kwa uwezo na ujuzi wao bali ni kwaajili ya kujipendeza kwa viongozi wao bt ni tofauti kwa wenzetu walioendelea Mr ban k-moon alijua kuwa Tanzania ni kama kwao mtu anapata cheo kwa uwezo na ufahamu wake kumbe c kweli vyeo huku ni kujipendeza au kuwa mwanamtandao alipomchukua akamweka katika office ya watu waliokwenda shule kiukweli c ujanja ujanja akajikuta kazi zote anafanya yeye

kwa wale ambao wamepata kufanya kazi na wazungu mfano akikuajili myb kuwa mtu wa masoko bt kila mda unakuja kumuuliza uliza juu ya kazi aliyokupa mwishoni atakuuliza je tulifanya makosa kukuajili wewe mbona kazi zako nakufanyia mimi? mshahara wako tutagawana?

lakini kwa bongo ukiwa unafanya kazi bila kwenda kumuuliza uliza boss juu ya kazi atajua madili yote unamaliza peke yako atakufanyia fitina utoke.

hilo ndo likamfanya mama yetu aonekane mzigo wakaona wampumzishe .
 
Huyu mama na spika makinda wametia aibu kubwa wanawake wa Tanzania, sidhani kama itatokea mwanamke kutoka nchi hii akapewa wadhifa wowote duniani, tutabaki kuteuana tu ndani ya chama, wameonyesha udhaifu mkubwa ambao haujawahi fanywa na mwanamke yoyote duniani.

Wenyewe wanasema WAKIWEZESHWA,wana weza
 
Kwa muda mrefu sana nimekua nawaangalia wasomi wengi walioko ccm (mf. presa Jumanne Magembe, Shukuru Kawambwa, Benson Banna n.k) including huyu mama; nimejiridhisha hivi, ili tusiendelee kupoteza vipaji vyao ni bora wabaki shule (chuo kikuu) na kuendelea kufundisha tu, hao niliwataja kiukweli walifauru vizuri sana darasana, kwa wengine msiojua, chuo kikuu cha Dar hakiwezi kumbakisha mtu kwa ajili ya degree ya 2 ili baadae aje kua miongoni mwa walimu wa pale kama umefauru kwa kutoa chochote (sijui kwa mfumo wa sasa hivi, but zamani that is how they were doing),Kwa msiofahamu, huyu mama kawafundisha wanasheria nguli sana hapa nchini akiwepo Dr. Tundu Antipas Lissu. Kitu ambacho hadi leo hua sikielewi kwa hawa wasomi wa ccm ni hiki, kwanini hua hawawezi kuzifanya zile theories walizonazo kichwani kwa vitendo ili tupate maendeleo? Nakubaliana kabisa na mwandishi wa hu uzi, Dr. Migiro hana uwezo hata wa kua waziri mkuu sio uraisi tu, tena huko ni mbali sana. Labda tu nijaribu kusema ninacho kifikiria, ukiona wakubwa hawa wanataka kumpa uongozi mkubwa mwanamke ujue lengo lao sio hiyo inayoitwa gender balance, issue hapo wanataka kumuongoza kwa remote, yaani yeye ataonekana ndio kiongozi but in fact somebody from somewhere ndio atakae kua anafanya maamuzi yote, mfano tumeuona kwa spika mama Anna Makinda, JK pia kamsifia jana, angalia pale wizara ya fedha, is like everything kinafanywa na Mwigulu. Narudia, napendekeza hao wasomi wa ccm wengi wao, watadumu sana kwenye ubora wao kama wakirudi chuo kufundisha kuliko kua viongozi wetu.
 
Wanawake wa Tanzania wengi wao hawajawa tayari kuwa viongozi,mfano ni spika wa bunge, Anne Makinda, ovyo kabisa na hata huyu Migiro hakuna kitu. Nahisi kwenye tano bora ya CCM Migiro ataingia ili kubalansi gender lakini atabwaga tu maana hana uwezo wa kuwa rais. N aikitokea tukawa na rais mwanamke Tanzania basi hali itakuwa mbaya zaidi kuliko hata hii awamu ya nne ya Jk. Ufisadi utatamalaki maana hakuna mtu wa kuwanyooshea vidole mafisadi.
 
Kwa muda mrefu sana nimekua nawaangalia wasomi wengi walioko ccm (mf. presa Jumanne Magembe, Shukuru Kawambwa, Benson Banna n.k) including huyu mama; nimejiridhisha hivi, ili tusiendelee kupoteza vipaji vyao ni bora wabaki shule (chuo kikuu) na kuendelea kufundisha tu, hao niliwataja kiukweli walifauru vizuri sana darasana, kwa wengine msiojua, chuo kikuu cha Dar hakiwezi kumbakisha mtu kwa ajili ya degree ya 2 ili baadae aje kua miongoni mwa walimu wa pale kama umefauru kwa kutoa chochote (sijui kwa mfumo wa sasa hivi, but zamani that is how they were doing),Kwa msiofahamu, huyu mama kawafundisha wanasheria nguli sana hapa nchini akiwepo Dr. Tundu Antipas Lissu. Kitu ambacho hadi leo hua sikielewi kwa hawa wasomi wa ccm ni hiki, kwanini hua hawawezi kuzifanya zile theories walizonazo kichwani kwa vitendo ili tupate maendeleo? Nakubaliana kabisa na mwandishi wa hu uzi, Dr. Migiro hana uwezo hata wa kua waziri mkuu sio uraisi tu, tena huko ni mbali sana. Labda tu nijaribu kusema ninacho kifikiria, ukiona wakubwa hawa wanataka kumpa uongozi mkubwa mwanamke ujue lengo lao sio hiyo inayoitwa gender balance, issue hapo wanataka kumuongoza kwa remote, yaani yeye ataonekana ndio kiongozi but in fact somebody from somewhere ndio atakae kua anafanya maamuzi yote, mfano tumeuona kwa spika mama Anna Makinda, JK pia kamsifia jana, angalia pale wizara ya fedha, is like everything kinafanywa na Mwigulu. Narudia, napendekeza hao wasomi wa ccm wengi wao, watadumu sana kwenye ubora wao kama wakirudi chuo kufundisha kuliko kua viongozi wetu.
Umeongea bonge la point naikubali naturally wanawake wameumbwa ili kutawaliwa kwa mbaaaali nayaona majamaa idirectly yanataka kutawala miaka mingi ijayo. ........!
 
Huyu mama na spika makinda wametia aibu kubwa wanawake wa Tanzania, sidhani kama itatokea mwanamke kutoka nchi hii akapewa wadhifa wowote duniani, tutabaki kuteuana tu ndani ya chama, wameonyesha udhaifu mkubwa ambao haujawahi fanywa na mwanamke yoyote duniani.

Usimsahau Getrude Mongella aliyeiba hela za bunge la AU.
 
Back
Top Bottom