Mtambuzi
Platinum Member
- Oct 29, 2008
- 8,809
- 15,438
Wanasaikolojia sasa wamebaini kwamba, mwanamke ana uwezo mkubwa wa kuvumilia kwenye hali ngumu kuliko mwanaume. Kwa hiyo, anaweza kuanzia chini sana, kwa kuuza muhogo wa kukaanga hadi akafika juu na kumiliki biashara kubwa. Lakini wanawake walio wengi wamefundishwa kwamba, wao hawawezi, hawana nafasi bali ni hadi waume zao wapende au wawasaidie mtaji. Mimi ninawajua wake wa watu wenye uwezo kifedha ambao, mmoja alikuwa akipika maandazi na kuyasambaza kwenye mighahawa kadhaa. Hivi sasa huyu mama anamiliki mghahawa mzuri na maarufu huko mkoani Arusha.
Mwingine alikuwa anatengeneza na kudarizi vitambaa vya mezani kwa miaka tisa, wakati mumewe angeweza kumpa mtaji mkubwa zaidi, kwani alikuwa na uwezo. Lakini hakukaa kusubiri mumewe ampe, aliamua kufanya kwa kutumia akili na mwili wake. Huyu mama hivi sasa anamiliki duka kubwa la nguo za kike na watoto hapa jijini Dar. Kwa nini waliamua kufanya wenyewe, tena kwa kuanzia chini, bila kusubiri waume zao? Kwa sababu wao ni binadamu kamili ambao wanaweza sawa na wengine. Waliamua kuweza siyo kusubiri kuwezeshwa. Kwani hata wanaume ambao wanapata fedha au mali si wameanzia mahali fulani! Mtu anasubiri kupewa hajishughulishi, halafu anatarajia atendewe haki! Utatendewa vipi haki nawe ni ombaomba ambaye unaamini kwamba, kuomba ndiyo haki yako?
Kuna wanawake ambao ukiwatazama, utagundua kwamba, wanaamini kuwa waliletwa hapa duniani kuwasubiri wanaume wayafinyange maisha yao kama wanavyotaka. Kwa hiyo, badala ya kutenda, badala ya kuanza kujitafuta, wanasubiri waume zao wawape mitaji. Wengine wanapewa kweli hiyo mitaji, lakini wanalipia puani fadhila hio. Naita fadhila kwa sababu hakuna mahali ilipoandikwa kwamba, mwanaume au mume anapaswa kumpa mkewe mtaji au kumtafutia kazi. Ninachojua mimi ni kwamba kila mtu ameletwa hapa duniani kuja kuishi kama yeye. Kwenye zile ndoa ambazo wanawake hawako tayari kuthubutu, hawana ubunifu wowote na wanasubiri waume zao wawafanyie kila kitu, hata kuwaambia wafanye nini, hakuna amani. Hakuwezi kuwa na amani kwa sababu wanawake kama hawa wana utegemezi kwenye kila kitu, ni wavivu wa kufikiri na kutenda. Unaweza kushangaa hata kulea watoto kunawashinda.
Mwanamke hana ajira, hana shughuli yoyote ya kumwingizia anayofanya, lakini anashindwa hata kuwasaidia watoto wake kufanya homework jioni. Kazi yake ni kuzurura na kutafuta umbea au kutafuta kusifiwa kwa kuvaa dhahabu kochokocho na nguo za fasheni. Na ndio maana wanawake wengi waume zao wanapokufa hawalii kwa sababu wamepoteza wenza, wamepoteza watu waliokuwa wamezoeana nao , hapana. Wanalia kwa sababu hawajui waanzie wapi, waguse na kupapasa wapi. Wanalilia nafsi zao, siyo za marehemu wao. Kwao kufiwa na mume ni sawa na kufa wenyewe. Wengine husema kabisa, umeniachia watoto, sasa nitawalea vipi?
Unataka kusema wewe ulikaa tu, hukuwa na mchango wowote kwenye kulea watoto wenu! Na ni kwa nini usiwe na mchango mkubwa kuliko wa mumeo katika kuwalea? Ni kwa sababu uliamua kujifanya nusu-mtu! Kila binadamu anaweza kufanya lolote, kila binadamu anaweza kuyakabili maisha kwa namna anavyotaka na kumudu. Lakini wanawake wengi hawakulelewa na kufanywa kuamini hivyo. Wanaamini kwamba, wanaume ndiyo wanaoweza na wao wamezaliwa ili kuwa wategemezi. Hiyo si kweli, ingawa kwa wanawake hao inaonekana kuwa ndiyo ukweli.
Ni kweli kwamba, wanawake wamenyimwa nafasi nyingi na wamefanywa raia wa daraja la pili na mfumo-dume. Lakini kwa leo kuendelea kujikunyata na kusubiri waume zenu wawafanyie kila kitu ni dhambi kubwa. Kuna idadi kubwa ya wasomi ambao mama zao waliwasomesha kwa kuuza maandazi na vitumbua. Kuna mama namjua ambaye mumewe alikuwa hajui kama kuna kitu kinaitwa kutunza familia. Huyu mama aliweza kwa mwili na akili yake kuhangaika hadi watoto wake wawili kati ya sita wakafika chuo kikuu. Hakuwa mwanamke msomi wala hakuwa na ajira. Alikuwa na moyo mkuu wa kutumia nafasi za kutafuta maisha alizoziona na kuzibuni. Unaweza kushangaa, mume anakufa mwanamke anaachiwa mali. Kwa sababu hajui chochote, hakuwahi kuhangaika kujua namna ya kutafuta, anatafuta mwanaume au mume mwingine ili amsaidie kusimamia mali. Mwanaume huyo anamtapeli mali zote na kumwacha akijikunguta.
Mwanamke, simama mwenyewe, anza leo kujituma hata kwa kuuza maji.