Wabunge 40 hatarini kunyang'anywa uheshimiwa............

Rutashubanyuma

JF-Expert Member
Sep 24, 2010
219,470
911,174
Wabunge 40 hatarini

Imeandikwa na Mwandishi Wetu; Tarehe: 10th December 2010 @ 23:59

LICHA ya kuapishwa na kuanza kuwatumikia wananchi, nafasi za wabunge 39 kati ya 239 walioibuka washindi katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31 mwaka huu ziko shakani kutokana na ushindi wao kupingwa mahakamani.

Habari ambazo gazeti hili inazo na pia zimethibitishwa na Msajili wa Mahakama ya Rufaa, Francis Mtungi zinasema kwamba, kesi hizo za uchaguzi tayari zimeshaifikia ofisi yake.

Akithibitisha jana, Mtungi alisema: "Nimepewa taarifa kuwa zimefika 39, lakini kazi ya kuzungumzia hili nimemuachia Msajili wa Mahakama Kuu."

Hata hivyo, HABARILEO ilipokwenda kwenye ofisi ya Msajili Msaidizi wa Mahakama Kuu, Eva Nkya, alisema: " Bado kuna kazi ya kuziorodhesha na kupata taarifa kutoka mikoani, Jumatatu nitakuwa kwenye nafasi nzuri ya kulizungumzia hili."

Ingawa majina hayako wazi, lakini tayari kuna taarifa za kupingwa kwa wabunge wengi katika Mahakama. Miongoni mwa wabunge waliopingwa mahakamani ni Naibu Waziri wa Ajira na Vijana, Makongoro Mahanga (Segerea), ambaye amefunguliwa kesi na aliyekuwa mgombea wa Chadema katika jimbo hilo, Fred Mpendazoe; Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe (Mtama), ambaye amefunguliwa kesi na aliyekuwa mgombea wa NCCR-Mageuzi, Worfam Ndaka.

Wengine ni Mbunge wa Newala, George Mkuchika ambaye ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), ambaye Chama cha CUF kimefungua kesi kupinga ushindi wake; pamoja na Waziri wa Uchukuzi, Omari Nundu, ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Tanga Mjini naye amepingwa.

Mwingine anayepingwa ushindi wake ni Christopher Chiza, Mbunge wa Buyungu Naibu Waziri wa Kilimo, ambaye Chama cha NCCR-Mageuzi kimeapa kwenda mahakamani kupinga ushindi wake, Naibu Waziri wa Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Godluck Ole Medeye ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi, matokeo ya ushindi nayo yanapingwa na mgombea wa Chadema, Matias Ole Kisambo.

Wabunge wengine ambao ushindi wao unapingwa mahakamani ni pamoja na Mbunge wa Mwibara wilayani Bunda, Kangi Lugola kupitia CCM, ambaye ushindi wake umepingwa na mgombea wa ubunge katika jimbo hilo kupitia Chadema, Chiriko David.

Kesi hiyo ya rufaa namba 7/2010 imefunguliwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza ambapo mgombea huyo anadai kuwa uchaguzi jimboni humo haukuwa huru na wa haki. Matokeo ya ubunge katika Jimbo la Busega yaliyomtangaza mgombea wa CCM, Dk. Titus Kamani pia yamepingwa baada ya mgombea, Jacktas Katinde (Chadema), naye kufungua kesi katika Mahakama Kuu ya Mwanza yenye namba 9/2010.

Jimbo la Magu Mjini, Julius Ngongoseke wa UDP kufungua kesi No 8/2010 akilalamikia kuporwa ushindi wake, na kwamba anaiomba Mahakama itengue mara moja ushindi wa Dk. Festus Limbu.

Wabunge wengine ambao ushindi wao unapingwa ni pamoja na Murji Mohamed wa Jimbo la Mtwara Mjini kupitia CCM, Juma Njwayo wa Jimbo la Tandahimba, kupitia CCM; Zubeir Mtemvu (CCM) Mbunge wa Temeke, Esmail Abdulkarim wa Mafia na Richard Ndassa wa Sumve, ambapo Chama cha Wananchi CUF kimesema tayari kimeanza mchakato wa kupinga matokeo katika majimbo hayo.

Kwa upande wa NCCR-Mageuzi, wao wametajwa kuwa kinapinga matokeo katika majimbo matatu ya Kawe, Babati Vijijini na Moshi Mjini. Halima Mdee wa Chadema aliibuka kidedea dhidi ya mgombea wao, James Mbatia katika Jimbo la Kawe ambaye hata hivyo aliachwa mbali na Angela Kizigha wa CCM aliyemfuatia Mdee, wakati Babati Vijijini, Jitu Soni alishinda.

Mgombea ubunge Moshi Mjini kwa tiketi ya chama hicho, Faustine Sungura amefungua kesi Mahakama Kuu dhidi ya Mbunge wa Jimbo hilo, Philemon Ndesamburo akidai ushindi wa mbunge huyo ulikuwa batili.

Majimbo mengine ambayo wabunge wake ushindi wao unapingwa mahakamani ni Mbunge wa Kigoma Mjini, Peter Serukamba, ambaye amefunguliwa kesi na Ally Alfan Mlee katika Mahakama Kuu ya Tabora na Stevene Masele wa Jimbo la Shinyanga Mjini na aliyekuwa mgombea wa Chadema, Philipo Shelembi.

Katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31, CCM ilivuna wabunge 186, ikiwa ni pungufu ya wabunge 19 ikilinganishwa na idadi ya wabunge 205 waliotinga bungeni kwa tiketi ya chama hicho tawala mwaka 2005.

Chadema ambayo mwaka huu imejiwekea rekodi ya kutwaa viti vingi vya ubunge kwenye majimbo ya Bara, imejipatia wabunge 23 kutoka watano wa mwaka 2005 huku CUF iliyokuwa na wabunge 19, mwaka huu ina wabunge 23.

UDP imebaki na Mbunge mmoja ambaye ni Mwenyekiti wake wa ngazi ya Taifa, John Cheyo wa Jimbo la Bariadi Magharibi, NCCR Mageuzi imepata wabunge wanne ambao wote wanatoka mkoani Kigoma.

Katika Bunge hilo ambalo Spika wake ni Anne Makinda, mwanamke wa kwanza nchini kushika wadhifa huo, TLP ina Mbunge mmoja, ambaye ni Mwenyekiti wake, Augustine Mrema.

Kwa upande wake CCM kupitia kwa aliyekuwa Meneja wa Kampeni za CCM Abdulrahman Kinana na Katibu Mkuu wa chama hicho, Yusuf Makamba, imetoa mwito kwa waliokuwa wagombea ubunge kupitia chama hicho na kuanguka, kukata rufaa mahakamani endapo kama kuanguka kwao kulisababishwa na kasoro kwenye uchaguzi.

Wakati Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ikiendelea kutangaza matokeo ya ubunge na urais katika majimbo mbalimbali nchini, Kinana alikutana na waandishi wa habari na kutoa tathmini iliyofanywa na chama hicho kupitia kwa mawakala wake na kutangaza CCM kushinda katika majimbo hayo 186.

Kinana alisema CCM itakuwa tayari kuwalipia gharama za mawakili wagombea wake walioanguka watakaofungua kesi mahakamani endapo watakusanya vielelezo kuhusiana na kasoro zilizosababisha kuanguka kwao.
 
Back
Top Bottom